Historia ya Mashahidi wa Yehova Katika Nyakati za Kisasa
—Ujeremani (Inaendelea)
“AZIMIO la mashahidi wa Yehova 230 wa mataifa sita, waliokusanyika katika msitu karibu na Schwerin katika Mecklenburg.
“Sisi mashahidi wa Yehova tuliokusanyika hapa, tunatuma salamu za moyoni kwa watu waaminifu wa agano la Yehova na wenzi wao ulimwenguni mwote kwa maneno ya Zaburi 33:1-4 na 37:9. Na ijulikane kwamba Mungu wetu mkuu, ambaye jina lake ni Yehova, ametimiza ahadi yake kwa watu wake, hasa katika eneo la Mfalme wa Kaskazini. Tumetoka katika kipindi kirefu chenye magumu na majaribu na wale ambao wamehifadhiwa, twaweza kusema walinyakuliwa katika tanuru la moto, hata hawana harufu ya moto. (Tazameni Danieli 3:27.) . . .
“Sisi, mashahidi wa Yehova, twatangaza tena kwamba tunamwamini Yehova na kwamba tumejiweka wakf kabisa kwa Theokrasi yake. . . .
“Tunamalizia azimio letu kwa maneno ya Zaburi 48 tukisadiki kwa furaha kwamba tutaungana mapema.
“Watumishi wenzenu kwa ajili ya jina takatifu la Yehova.”
KUMBUKUMBU YA UAMINIFU
Ripoti hii imejaribu kueleza sehemu ya maana katika historia ya kisasa ya watu wa Yehova. Lakini ni sehemu ndogo tu ya mambo yenye kupendeza yaliyowapata ndugu na dada Ujeremani ambayo yameweza kusimuliwa. Vitabu vingi sana vingehitajiwa ili kuripoti kila jambo lililotukia kwa sababu Mashahidi walishikamana sana na ibada ya kweli wakaliunga mkono jina la Yehova. Mambo yaliyoonwa yakasimuliwa moja moja na yawakilishe mengi ambayo yangalipaswa kutajwa pia ili Yehova, si wanadamu, asifiwe na kuheshimiwa kwayo. Yeye ndiye aliyechukua hatua katika wakati unaofaa akomboe watu wake wakiwa kikundi, ingawa aliruhusu wengi wafe kwa ajili ya jina lake takatifu.
Ye yote aliyezungumza na wale waliokombolewa na uonezi mwaka wa 1945 anakumbuka namna wote pamoja walivyokuwa wakimsifu Yehova mara nyingi kwa kutumia maneno ya Zaburi 124. Walifikiria makala nzuri sana za Mnara wa Mlinzi zilizokuwa zimetokea mateso yalipoanza, naye Yehova alikuwa amewatayarisha wapambane na wakati huo wenye magumu kwa kuzitumia. Sasa walielewa Yesu alimaanisha nini aliposema wasiwaogope wawezao kuuharibu mwili. Walijua kilichomaanishwa na kutupwa ndani ya tanuru la moto au ndani ya pango la simba, kama Danieli. Lakini walifahamu pia kwamba Yehova ni mwenye nguvu zaidi, akiwashupaza zaidi kuliko maadui.
Ingawa hali zilikuwa zenye magumu, wenye kumwabudu Yehova walishangilia kweli kweli! Walikuwa wamepewa pendeleo la kuhakikisha ukamilifu wao kwa Mtawala Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wote. Wakati wa utawala wa Hitler 1,687 kati yao walikuwa wamepoteza kazi zao, 284 biashara zao, 735 nyumba zao na 457 hawakuruhusiwa kuendesha biashara zao. 129 walikuwa wamenyang’anywa mali zao, 826 wenye kupokea mishahara ya uzeeni walikuwa wamenyimwa wasiipate na 329 wengine walikuwa wamepata hasara za kipekee. Walikuwako watoto 860 waliokuwa wametenganishwa na wazazi wao. Ndoa 30 zilikuwa zimevunjwa kwa sababu ya mikazo ya wakuu wa kisiasa, na talaka 108 zilikuwa zimetolewa wakati wenzi wenye kupinga kweli walipoomba iwe hivyo. Jumla ya ndugu 6,019 walikuwa wamekamatwa, wengi wao wakiwa wamekamatwa mara mbili, mara tatu au hata zaidi, hata ikaandikwa jumla ya visa 8,917 vya wenye kukamatwa. Wote pamoja walikuwa wamehukumiwa kutumikia kifungo cha miaka 13,924 na miezi miwili, kipindi hicho kikiwa ni mara mbili na robo za urefu wa kipindi cha tangu kuumbwa kwa Adamu. Jumla ya ndugu na dada 2,000 walikuwa wametiwa katika kambi za mateso, ambako walikaa miaka 8,078 na miezi sita, wastani ikiwa ni miaka minne kwa kila mmoja wao. Jumla ya ndugu na dada 635 walikuwa wamefia kifungoni, 253 wakahukumiwa kufa na 203 kati ya hao wakauawa hasa. Looo! kumbukumbu la ukamilifu hilo!
KAZI YAANZA KUTAYARISHWA UPYA
Mara baada ya vita, ndugu katika Betheli ya Switzerland peke yao ndio waliopashana habari na ndugu Wajeremani. Baada ya kupata habari juu ya maelekeo fulani mabaya yaliyokuwa katika makundi mengi hata baada ya kufunguliwa kwa akina ndugu katika zile kambi, walituma barua hii kwa makundi yote.
“Kwa watumishi wenzetu wapenzi wote katika Ujeremani. Ndugu Wapenzi katika Kristo,
“Mwishowe mko huru na nira ya Nazi!—Wengine wenu mmetaabika miaka mingi, ama gerezani ama katika kambi za mateso au kwa kuteswa kwa njia nyingine. . . .
Walakini, hakuna ye yote aliyehesabiwa anastahili kutaabika sana kwa ajili ya jina la Bwana atakayekuwa mwenye kichwa kikubwa akijitukuza juu ya wengine wasiokuwa gerezani wala katika kambi za mateso. Hakuna anayepaswa kujivuna-vuna kwa wanadamu wenzake juu ya taabu zake. Msisahau kwamba wengi wa akina ndugu waliobaki nyumbani walikuwa na magumu mengi pia nao walikuwa chini ya mikazo mikali sana. Mkristo hawezi kujichagulia taabu zake. Bwana ndiye huzichagua ama kuziruhusu.
“Kwa hiyo, akina ndugu, tusiwe wenye kupendelea huyu wala yule wala kulaumu mtu ye yote tunayedhani kulingana na kuwaza kwetu amekubaliana au amekuwa na nia ya kukubaliana na wenye kumwagiza avunje ukamilifu wake. Bwana ndiye anayehukumu mioyo. Tukiwa mbele zake sisi ni kama kitabu kilichofunguliwa. . . .
“Ndugu Erich Frost wa Leipzig amepewa mamlaka ya kuchukua uangalizi wa mambo ya eneo lenu. Walakini, mpango huo ni wa muda tu, kulingana na maagizo ya msimamizi. Kama itakavyowezekana, Ndugu Frost atatoa ripoti kwa msimamizi juu ya maendeleo ya kazi ya uchapaji.
“Kazi ya kuhubiri ikiwa chini ya uongozi wa msimamizi mpya wa Sosaiti, Ndugu Nathan Homer Knorr, imetayarishwa vizuri kupita wakati mwingine wo wote nayo inafanya maendeleo makuu! . . .
“Jamaa ya Nyumba ya Biblia katika Bern katiwa sahihi Fr. Zurcher”
Mara tu baada kufunguliwa kwao, Ndugu Frost, Schwafert, Wauer, Seliger, Heinicke na wengine, walianza kujaribu kupata tena mali ya Sosaiti wakikusudia kuanza kuongoza kazi tena kutoka huko.
KUSANYIKO KATIKA NURNBERG
Akina ndugu walipokuwa wakijaribu sana kutengeneza makundi tena na kuyapa chakula cha kiroho ijapokuwa karatasi zilikuwa chache, tamaa yao ya kuwa na kusanyiko kubwa ilikua. Hamu kati ya akina ndugu ikaongezeka hata zaidi ilipotangazwa kwamba serikali ya kijeshi mwishowe ilikuwa imekubali kutuacha tutumie Zeppelinwiese katika Nurnberg.
Wakati huo kesi ya waliokuwa ‘wavunja sheria wakati wa vita’ ilikuwa inaendelea katika Nurnberg nao walipaswa kuhukumiwa Septemba 23. Tarehe hiyo ilikuwa imewekwa juma nyingi mapema, nao ulimwengu ulikuwa umekwisha julishwa.
Ilipowezekana kufanya kusanyiko katika Nurnberg, akina ndugu waliamua kwa ghafula kuliongezea siku moja limalizike Jumatatu, Septemba 30. Baada ya kutayarisha upya magari-moshi ya pekee na kufanya mipango mingine yote kwa ajili ya siku hiyo ya tatu ya kusanyiko, radio na magazeti yakatangazia ulimwengu kwa ghafula kwamba hukumu zilizotolewa katika kesi ya uvunjaji wa sheria uliofanywa wakati wa vita katika Nurnberg zisingejulishwa kwa watu wote mpaka Septemba 30. Hii ilitokeza magumu, kwa sababu serikali ya kijeshi ya Amerika iliogopa kwamba huenda maonyesho yenye fujo yakatokea katika Nurnberg na kwa hiyo ikaagiza watu wazuiwe wasiondoke nyumbani kwao. Hiyo ilikuwa na maana ya kwamba hakuna mtu wa mjini angeweza kuhudhuria hotuba ya watu wote Jumatatu. Kwa hiyo ikapangwa upya iwe Jumapili jioni saa 1:30, Ndugu Frost akiwa ndiye mwenye kusema juu ya habari “Wakristo Wajaribiwa Vikali.” Ndugu 6,000 waliokuwako walishangilia isivyoelezeka waliposikia kwamba watu 3,000 zaidi wa kutoka Nurnberg walikuwapo kusikia hotuba hiyo.
Ingawa kwanza wakuu wa serikali ya kijeshi ya Amerika walijaribu kukomesha kukusanyika kwetu siku ya tatu kwa sababu ya kutolewa kwa hukumu ya wavunja sheria wa wakati wa vita siku hiyo, akina ndugu walifaulu. Baada ya kufanya mapatano yaliyochukua muda mrefu wakuu wa kijeshi walifuta agizo walilokuwa wametoa. Waliona haifai kukataza mashahidi wa Yehova kumaliza kusanyiko lao kwa amani na bila kusumbuliwa, kwa maana wao walikuwa wamewapinga waliokuwa kesini sasa kwa miaka mingi sana.
Hivyo Jumatatu asubuhi akina ndugu waliokuwa katika kusanyiko lenye kichwa “Wenye Ujasiri kwa ajili ya Kipindi cha Baada ya Vita,” walisikia hotuba nyingine kuu yenye kichwa “Wajasiri Kujapokuwa na Hila ya Ulimwengu.”
Ndugu 6,000 waliokusanyika walifurahi sana walipojua namna Yehova alivyosimamia mambo kwa busara. Ebu wazia, baada ya kuanguka kwa serikali ya Nazi, mashahidi wa Yehova ambao ndio wenye ujumbe wa kweli wa amani kwa wanadamu, ndio waliokuwa wa kwanza kuruhusiwa kukusanyika pamoja katika uwanja huo ambao wakati mmoja ulikuwa mahali pa magwaride ya Hitler. Na je! tunaweza kuwazia walivyoona wakati wa kufikiria kwamba siku iyo hiyo ya tatu ya kusanyiko hukumu za kifo zilitangazwa juu ya wale waliokuwa wauaji wenye kujaribu kufutilia mbali mashahidi wa Yehova? Mwenyekiti katika kusanyiko alisema hivi: “Kupata kuona siku hii kulifaa miaka tisa katika kambi ya mateso, ambayo ni maono ya mbele tu ya ushindi wa watu wa Mungu juu ya adui zao penye Har–Magedoni.” Maneno hayo yaliandikwa magazetini (yaani, ya ulimwengu) yakapelekwa kila mahali ulimwenguni.
WASONGA MBELE KUJAPOKUWA NA MAGUMU YA BAADA YA VITA
Kwa sababu watu wa Yehova walikuwa na nia ya kuweka faida za kiroho kwanza walipata amani, umoja na ongezeko. Wakati wa mwezi wa kusanyiko wa Julai, wahubiri 33,741 waliripoti utumishi, nayo hesabu hiyo ikaongezeka mwaka uo huo wa 1948 katika mwezi wa Agosti, hata wahubiri wakawa 36,526. Mwaka wa utumishi ulikwisha kukiwa na ongezeko la 83 kwa mia. Makundi yaliongezeka, na katika Oktoba 15 mizunguko ikagawanywa tena, na sasa kuna mizunguko 70.
Mwanzoni mwa mwaka wa 1949 kiwanda cha uchapaji cha Wiesbaden kilipanuliwa; mashine nane za kuchapia zikawa zikifanya kazi, mbili kati yazo zikifanya hivyo mchana na usiku. Baadaye mwaka huo karibu vitabu milioni moja na nusu vilitumwa kutoka Brooklyn, navyo vilipoenezwa kukawa na msingi mkubwa zaidi wa kufanya ziara mpya za kurudia na mafunzo ya Biblia. Hesabu ya wahubiri iliongezeka kila mwezi, na Agosti 1949 walikuwako 43,820 wenye kuripoti. Mwaka huo wa utumishi lilipatikana ongezeko la 33 kwa mia katika wahubiri.
UPINZANI KATIKA UJEREMANI YA MASHARIKI YENYE KUTAWALIWA NA WAKOMUNISTI
Maendeleo ya kazi yalikuwa tofauti sana katika Ujeremani ya Mashariki na katika sehemu ya Mashariki ya mji wa Berlin, nazo sehemu hizo zilikuwa zinakaliwa na Warusi zikisimamiwa na utawala wa kijeshi wa Warusi mwishoni mwa Vita ya Ulimwengu ya Pili. Wengi wa wakuu wake wa kijeshi hawakuwajua mashahidi wa Yehova sana, isipokuwa walijua kwamba walikuwa wamevumilia mateso ya ukatili ya Wanazi. Hapo kwanza hawakusumbuliwa sana, lakini makundi yalipoanza kusitawi na watu wengi wakaanza kuonyesha wanapendezwa na ujumbe wa Ufalme, utawala wa kijeshi wa Warusi ukaanza kuwa na mashaka juu ya kazi yetu, kwa maana ilionekana hawawezi kuizuia. Mara nyingi kulikuwa na watu wengi zaidi katika mikutano yetu ya watu wote kuliko waliokuwako katika mikutano ya kisiasa ya chama cha Wakomunisti hao, iliyosaidiwa na serikali ya kijeshi.
Katika mwaka wa 1949 mwezi wa Juni, hesabu ya wahubiri katika Ujeremani ya Mashariki wenye kuangaliwa na afisi ya tawi ya Magdeburg ilifikia 16,960. Watu wengi walitaka kweli za Biblia. Waangalizi wenye kusafiri waliripoti kwamba mara nyingi walikuwako watu zaidi ya 100 hata 150 katika mikutano ya watu wote katika makundi ya wahubiri 30 hata 40 tu. Katika miji mikubwa hotuba zilihudhuriwa mara nyingi na zaidi ya watu elfu moja. Mafunzo mengi ya Biblia yalianzwa; katika kundi moja wastani ya mafunzo ilikuwa 3.8 kwa kila mhubiri. Waangalizi wenye kusafiri hawakuwa na kazi nyepesi sikuzote. Wengine wao walisafiri kwa kutumia baiskeli kuu-kuu za kuazima, na nyingine kati yazo hazikuwa na mipira ya magurudumu, bali zilikuwa na vyuma vya magurudumu tu. Walisafiri sana. Halafu tena, kulikuwa na ugumu wa kupata kadi za serikali za kuruhusiwa kupata chakula. Mwangalizi wa mzunguko mmoja asema kwamba muda wa hati aliyopewa na afisi ya wafanya kazi yenye kumtambulisha kama “mhubiri” haukurefushwa, na kwa hiyo hakuwa na kadi ya kuruhusiwa kupata chakula.
Mwangalizi wa mzunguko mwingine asema hivi: “Wapelelezi walihudhuria kila hotuba. Wakati mmoja akina ndugu walikuwa na mashaka juu ya mtu mmoja aliyekuwa amevaa mavazi ya kiraia. Kabla ya hotuba kuanza nikamkaribia nikamwuliza hivi: ‘Samahani, afisa, waweza kuniambia ni saa ngapi hasa?’ Akaniambia, na kwa sababu hakuonekana kushangaa kwa vile nilivyomwita tukajua yeye ni polisi aliyevaa mavazi ya kiraia.”
Uadui wa wakuu wa Urusi na wa Ujeremani ya Wakomunisti ulizidi kuongezeka. Shughuli iliendelea kupangwa kwa nguvu zaidi kwa kupinga mashahidi wa Yehova. Uhuru wa kuabudu ulipunguzwa zaidi na zaidi. Uongozaji wa mafunzo ya Biblia ulipigwa marufuku, mapolisi wakakatiza ibada, ndugu wakafutwa kazi zao kwa sababu ya dini. Serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Ujeremani ilipewa ombi la kuhakikisha kwamba kuna uhuru wa kweli wa kidini katika Februari 18, 1950. Kwa sababu hiyo ibada zikawa zinakatizwa kwa namna isiyolingana na katiba ya nchi, vitabu vikachukuliwa kwa nguvu na wahudumu kadha wenye kuongoza wakakamatwa. Juni 27, 1950, mashahidi wa Yehova walitumia serikali katika Ujeremani ya Mashariki ombi jingine, likiwa limeandikwa kwa Mhudumu Rais Otto Grotewohl. Ndipo mkono wenye ukatili wa Wakomunisti ulipopiga kwa nguvu.
Asubuhi na mapema ya Agosti 30, 1950, majeshi ya mapolisi Wakomunisti yalimiminika katika Betheli yetu ya Magdeburg kwa amri ya wakuu wawili Warusi. Wakakamata ndugu wote isipokuwa mmoja, ambaye walimweka awe “mwangalizi.” Barua iliyotoka kwa Wizara ya Mashauri ya Ndani ikijulisha Watch Tower Society katika Magdeburg juu ya marufuku ilikuwa ya tarehe ya Agosti 31. Lakini mapolisi walimpa ndugu aliye peke yake aliyeachwa nyuma akiwa “mwangalizi” barua hiyo Septemba 3.
Mambo yaliyoshuhudiwa kwa macho yanayotoka kwa akina dada wa Betheli yanaeleza lililotukia asubuhi hiyo ya Agosti 30: “Karibu na saa 11:00 asubuhi kengele ililia. Nikavalia upesi. . . . Nilipofungua mlango nikimbie kuelekea orofa ya chini, nilikutana na mapolisi wawili wakaniagiza nibaki chumbani mwangu. Kisha mmoja wa wakuu hao akaingia akaniambia nifungue kabati la nguo. Nikakataa mpaka aliponionyesha kitambulisho chake. Wakatupa-tupa kila kitu huku na huko. . . . ” Mapolisi hao waliingiaje katika makao ya Betheli? Dada mwingine anatuambia hivi: “Nilitazama nje dirishani katika chumba Na. 23 nikamwona polisi akiruka juu katika mlango wa ua. Wengine walikuwa wamekwisha ingia. Mlinzi wa usiku alikuwa amekataa kuwafungulia. Nakadiri kwamba walikuwako mapolisi wasiopungua 25 mpaka 30 katika kikundi hicho, na hakuna ye yote kati yao aliyekuwa na mavazi ya kipolisi.”
Dada Bender, aliyekuwa akitumikia katika Betheli ya Magdeburg wakati huo na ambaye hata sasa anatumikia kwa uaminifu katika Betheli ya Wiesbaden, anasimulia aliyoona: “Agosti 30, 1950, kati ya saa 10 na saa 11 asubuhi mapolisi wa Ujeremani ya Mashariki walikuja kwenye makao ya Betheli. Kila mtu alilazimishwa akae chumbani mwake, lakini karibu na saa 4 asubuhi mimi niliponyoka nikatoka Betheli bila kuonekana na polisi kwa kushuka katika ngazi inayotumiwa wakati wa hatari ya moto ya orofa ya kwanza na kuruka juu ya ua wa kati ya jumba letu na la jirani yetu. Ingawa niliwaona mapolisi barabarani, nikatoka katika uwanja wa jirani huyo kama mtu asiyejua neno nikaenda kwenye nyumba ya ndugu mmoja ambako baadhi ya hati za Sosaiti ziliwekwa. Nikazichukua na ndugu mmoja akanipeleka Berlin kwa gari.” Kwa njia hiyo iliwezekana kuokoa baadhi ya hati hizo.
Vitabu vyote vilichukuliwa kwa nguvu pamoja na lori la Sosaiti. Vyakula vilivyokuwa jikoni vilichukuliwa pia. Akina dada peke yao ndio walioruhusiwa kubaki na kadi zao za kuruhusiwa kupata chakula cha serikali. Mtu aliyeshuhudia kwa macho asema hivi: “Kwa sasa walikuwa wamechuka ndugu wawili wawili kwa kimya.
Mateso yalikuwa yamechacha. Polisi walipokuja kukamata ndugu mmoja, yeye alikwenda kukutana nao amevaa mavazi yenye milia aliyokuwa amelazimishwa kuvaa katika kambi ya mateso ya Nazi! Kesi za upuzi zilifanywa halafu kwa mara nyingine kazi ya mashahidi wa Yehova ikaanza kuendeshwa chinichini.
Lothar Wagner alikuwa mmoja wa ndugu waliohukumiwa kifungo kirefu mwaka wa 1950. Anaeleza waziwazi namna alivyoweza kuendeleza ukamilifu wake wakati wa miaka saba ya kuwa katika kifungo cha kutengwa na watu wengine wote:
“Agosti 30, 1950, nilikamatwa Plau, Mecklenburg, na Oktoba 4, 1950, nikahukumiwa kifungo cha miaka kumi na mitano katika gereza ya kufunzia adabu na baraza kuu ya DDR katika Berlin. Kwa sababu ya msukosuko uliokuwa Hungary mwaka wa 1956 kifungo changu kilipunguzwa kikawa miaka kumi.
“Nilikaa katika gereza ya kufunzia adabu katika Brandenburg-Gorden miaka hiyo kumi (na juma sita za kuwekwa kizuizini ili wafanye uchunguzi, nazo juma hizo hazikupunguzwa katika kifungo changu). Nilifunguliwa huko Oktoba 3, 1960.
“Wakati huo nilitumia miaka saba katika kifungo cha kutengwa na watu wengine wote. Miaka ya kwanza mitatu nilipata barua moja tu, nayo ilikuwa nusu-karatasi ya kuchapia, yenye mistari kumi na mitano, nami niliruhusiwa kuandika kadiri ya mistari hiyo na kuipokea kadiri iyo hiyo kila mwezi—ikitegemea kama yaliyokuwamo yalikubaliwa na polisi au sivyo. Kazi ilionwa kama pendeleo mpaka mwaka wa 1958—kwa hiyo sikuruhusiwa kufanya kazi. Kutoka mwaka wa 1958 kazi ilionwa kama adhabu—sasa nililazimika kufanya kazi.
“Mtu anapokuwa katika kifungo cha kutengwa na watu wengine wote kwa miaka mingi hivyo kunakuwa na adui mmoja mkuu kati ya vitu vingi vyenye kusumbua, naye amepaswa apambane na adui huyo, yaani, wakati. Lazima utafute njia za kumaliza wakati.
“Mimi nilitatua ugumu huu wa wakati kwa njia ifuatayo: Umoja unatia nguvu, na ndivyo ilivyo na wakati. Kipindi chote cha kufungwa cha jumla ya miaka kumi na mitano kikifikiriwa kama kitu kimoja, mtu anakaribia kupondeka kwa huzuni kwa sababu ya wakati huo mwingi, kwa sababu tu kwa kukiwazia tunakiona kuwa wakati mwingi mno. Imempasa mtu ajikaze autiishe wakati. Wakati watawala wa ulimwengu huu wanapojaribu kutawala idadi kubwa ya watu wasioweza kutiisha, mara nyingi wanafuata kanuni hii: gawanya utawale!
“Kwa habari ya wakati mimi nilitumia kanuni hiyo; niliugawanya wakati huo. Sikuuhesabu kwa kutumia miaka wala miezi, hata sikutumia juma wala siku, bali nilitumia saa. Asubuhi kama saa 1:00 sikujiuliza hivi: Nifanye nini leo? bali, Nitafanya nini mpaka saa 3:00?
“Kwa ghafula kila kitu kikaonekana tofauti. Saa moja au mbili hazikuwa zenye kuogofya, ningeweza kuvumilia wakati huo. Lakini bado kulikuwa na ugumu mmoja: Nitaujaza wakati huo na nini? Haikuwezekana kupata karatasi wala kalamu. Kazi halisi ya pekee ilikuwa kusafisha kijumba cha gereza na kula. Hata nilipofanya mambo hayo kwa uangalifu sana na polepole kama ilivyowezekana bado sikuweza kumaliza siku nzima nikiyafanya. Niliwaza karibu pande zote za utumishi wa Kitheokrasi, nikawaza kwanza juu ya funzo la kipekee halafu makusanyiko ya mataifa yote, kisha utumishi wa nyumba kwa nyumba hata hotuba za watu wote. Ijapokuwa nilijitahidi sana mara nyingi nilikuwa na saa moja au mbili siku hiyo nisizokuwa na la kufanya, nazo saa hizo ndizo zilizokuwa hatari zaidi kwa maana mtu angeweza kwa vyepesi kubomoa kila kitu alichokuwa amejenga siku yote kwa jasho, kwa sababu ya uzembe, kufa moyo au kuhuzunika.
“Siku moja nikagundua ‘saa’ iliyonisaidia kwa miaka mingi katika kutumia kwa mafaa wakati huo wenye hatari nisiokuwa na jambo la kufanya. Nikagundua kwamba zilikuwa zimebaki saa mbili ndiyo wakati wa chakula cha mchana ufike. Nikatembea-tembea hapa na pale katika kijumba changu, mbele nikatembea hatua tano na nyuma hatua tano huku nikiimba nyimbo za Ufalme. Nilipomaliza wimbo wa 30 mlango ukafunguliwa nikapewa chakula cha mchana. Nilikuwa nimekaza fikira zangu juu ya maneno ya nyimbo zenyewe hata sikujua kwamba wakati umefika. Hilo ni jambo nililogundua likaniondolea uchovu na huzuni kwa miaka mingi. Kwa juma kadha nilikaza fikira juu ya kumaliza kuweka akiba ya nyimbo za Ufalme. Nisipojua maneno yenyewe hasa nilikuwa nikijitungia beti moja au mbili. Nilikuwa nikitumia sauti za nyimbo za kilimwengu nilizopenda ili nitunge nyimbo za Ufalme kwa kufikiria maneno ya kitheokrasi. Kwa njia hiyo mwishowe nilikusanya nyimbo 100 za Ufalme nilizoweza kuimba, na zote zilikuwa na namba. Wimbo mmoja ulichukua dakika nne barabara, kwa hiyo ningeweza kuwaza ningeimba nyimbo ngapi ndiyo nimalize kiasi fulani cha wakati. Miaka yote hiyo niliimba angaa saa mbili kila siku, ndiyo kusema nilikuwa nikiimba nyimbo 30 za Ufalme kwa siku. Kwa njia hiyo wakati mmoja niliweza kuimba kutoka asubuhi hata jioni nilipojisikia kutotaka kufanya jambo jingine. Jamani! nyimbo zetu za Ufalme zina mawazo mengi sana yenye kutia moyo na kujenga. Mtu akitumia maneno ya kila wimbo kama muhtasari anaweza kwa vyepesi kutayarisha hotuba kutokana na kila wimbo, nayo hiyo ni njia nyingine ya kujaza wakati na jambo la kufanya bila kupata hasara ya kiroho. Tunaweza kusema kwa kweli kwamba nyimbo zetu za Ufalme ni chakula kwa wakati wake.
“Namshukuru Yehova sana kwamba kwa msaada wa roho yake niliweza kuendelea kuwa mwenye nguvu za kiroho miaka hiyo kumi ya kutenganishwa kabisa na tengenezo lake. Ningependa kutia kila mtu moyo athamini inavyofaa chakula chote cha kiroho tunachopewa kwa maana hatujui namna kitakavyotufaa wakati fulani. Tukila chakula cha kiroho cha wakati wake kwa kawaida, kitatusaidia tukiwa katika nyakati zenye magumu makubwa na tukiwa peke yetu, ili tumtumainie Yehova na kuvumilia tukiwa thabiti upande wake.”
Kutoka Septemba 1, 1955, mpaka Agosti 31, 1961, Sosaiti ilikuwa na afisi ya tawi ya kupendeza katika Berlin ya Magharibi, ikawezesha hali za pekee ziangaliwe vizuri zaidi katika mji huo wenye migawanyiko. Ilifaa sana pia kuwa na ushirikiano wa kitengenezo kati ya Berlin ya Magharibi na Ujeremani ya Mashariki.
Kutoka mwanzo wa mateso mwaka wa 1950 mpaka “Ukuta wa Berlin” ulipojengwa mwaka wa 1961, wakuu wa Ujeremani ya Mashariki walikamata mashahidi wa Yehova 2,897; kati yao ndugu 2,202 kutia na dada 674, walipelekwa barazani wakahukumiwa kifungo cha jumla ya miaka 12,013 au wastani ya miaka mitano na nusu kila mmoja. Walipokuwa wamefungwa ndugu 37 na dada kumi na watatu walikufa kwa kutendewa vibaya, kwa sababu ya ugonjwa, kwa sababu ya kukosa chakula cha kujenga mwili na uzee. Hapo kwanza ndugu kumi na wawili walikuwa wamehukumiwa kifungo cha maisha, lakini baadaye kikapunguzwa kikawa miaka kumi na mitano.
Upesi ndugu wa Ujeremani ya Mashariki walizoea hali mpya iliyoletwa na kujengwa kwa “Ukuta wa Berlin.” Njia nyingine zilitumiwa kuwapa chakula cha kiroho kilicho cha lazima nao waliendeleza huduma yao ya Kikristo kwa juhudi nyingi. Kwa wazi wakuu wa Kikomunisti hawakutazamia kwamba ndugu wangefanya hivyo. Walijaribu kuchangamanisha tengenezo na wapelelezi waliotembelea mashahidi wa Yehova wakadai wao ni ndugu waliotumwa na Sosaiti kusaidia kutengeneza kazi ilingane na hali mpya. Lakini akina ndugu walikuwa wamezoezwa sana; upesi waligundua watu hao kuwa wapelelezi.
Miaka ilipoendelea kupita hesabu ya ndugu wenye kukamatwa na kuhukumiwa ilipungua sana. Watu wengine kumi na watano tu ndio waliokamatwa kati ya mashahidi wa Yehova mwaka wa 1963 na tisa katika mwaka wa 1964, na hali miaka iyo hiyo miwili ndugu 96 na wengine 48 walifunguliwa. Katika kiangazi cha mwaka wa 1964 ndugu wanne waliokuwa wamefungwa kwa miaka mingi waligutuka. Hapo kwanza walikuwa wamehukumiwa kifungo cha maisha, kisha kwa ghafula wakafunguliwa na kupelekwa Ujeremani ya Magharibi. Walifika karibu tu na wakati wa kusanyiko. Wakadhani wanaota. Siku chache tu kabla ya hapo, walikuwa wamekuwa ndani ya gereza za kufunzia adabu za Ujeremani ya Mashariki bila tumaini la kukusanyika pamoja na akina ndugu kwa uhuru. Na sasa walikuwa wanaona kutimizwa kwa ghafula kwa tamaa iliyokuwa mioyoni mwao. Wawili wa ndugu hao, Friedrich Adler na Wilhelm Engel, walikuwa washiriki wa jamaa ya Betheli katika Magdeburg. Friedrich Adler alikamatwa akafungwa mwaka wa 1950, miezi miwili kabla ya kazi kupigwa marufuku, lakini Wilheim Engel alikuwa mmoja wa waliokamatwa Betheli iliposhikwa Agosti 30, 1950. Ndugu Engel alipelekwa kwa watu wa Msalaba Mwekundu katika mpaka wa Berlin kwa sababu ya kuwa na afya mbaya. Upesi alipelekwa hospitalini alikofia juma chache baadaye. Ndugu hao walikuwa wamekwisha kaa miaka tisa kifungoni wakiwa chini ya serikali ya Hitler na hivyo wote pamoja walikuwa wamevumilia kifungo cha miaka 23 kwa sababu ya imani yao. Friedrich Adler alichukua utumishi wa Betheli tena, sasa katika Wiesbaden. Akaweza kutazama nyuma na kuona namna alivyokuwa na maisha marefu yenye matukio katika utumishi wa wakati wote, akiwa amekwisha tumikia kama ndugu mhaji huko nyuma katika miaka ya 1920. Kwa kuwa alikuwa amedhoofishwa na kifungo chake kirefu, alimaliza mwendo wake wa kidunia Desemba 1970.
Mwaka wa 1965 ndugu zetu walichunguzwa na kusumbuliwa sana na wapelelezi na makachero wa wizara ya usalama wa nchi. Nyumba nyingi zilipekuliwa, ndugu wakasimamishwa barabarani wakaulizwa maulizo. Vinasa-sauti vilifichwa katika motokaa na nyumba, hata katika vyumba vya kulala vya akina ndugu. Wakuu walijaribu kuonyesha akina ndugu kwamba mambo yote waliyofanya yalijulikana. ”
Bila shaka, wakuu waliweza kupata habari nyingi kwa “kusikiliza” mazungumzo yasiyo na hatia ya akina ndugu. Kesi zilipofanywa makachero walijaribu kufanya ionekane kwamba walikuwa wamepata habari zinazohusu kazi katika nchi za nje, kwa njia hiyo wakaonyesha ndugu wa huko walikuwa wazembe. Walikuwa wakijaribu kutufanya tutilie mashaka Baraza Inayoongoza na akina ndugu waliokuwa katika afisi za Sosaiti. Lakini akina ndugu hawakujiacha wahangaishwe na jambo hilo, kwa hiyo baadaye walifahamu vizuri zaidi kwamba walikuwa wamekazwa sana na uchunguzi wa wapelelezi hao.
Walifahamu hivyo hasa wakati nyumba za akina ndugu katika nchi yote zilipoingiliwa na vikundi vikundi vya wakuu wanane zikapekuliwa kwa saa kadha, katika asubuhi moja ya mwaka wa 1965. Ndugu kumi na watano waliodhaniwa kuwa ‘viongozi’ walikamatwa wakawekwa jela kati ya miezi tisa na kumi na mitatu mpaka waliposhtakiwa na kujaribiwa. Mwaka wa 1966 walipata hukumu za kufikia miaka kumi na miwili, wastani ikiwa ni zaidi ya miaka saba.
Wakati ndugu hawa walipokuwa wakitendewa kama wahalifu wa kupindukia, makachero walikuwa wakiwinda wengine waliokuwa wamekuwa wakihubiri habari njema na kukusanyika wamwabudu Yehova vikundi vikundi kama vile ndugu waliohukumiwa walivyokuwa wamekuwa wakifanya. Waliwaambia wangeweza kuendelea kukutana vikundi vikundi na kubaki na vitabu vyao vya kujifunzia Biblia na kuandikiana na ndugu wa nchi nyingine wakitoa ripoti juu ya utendaji wao na kutoa majina ya wenye kushiriki hudumani, ili kuhifadhi usalama wa nchi. Lakini akina ndugu walilikataa toleo hilo la uongo la wakuu. Mmoja wa wakuu kasema hivi kwa huzuni: “Tulidhani tumechukua viongozi wenu, kumbe hata hatujui mnavyoendesha kazi yenu.”
Tangu kazi katika Ujeremani ya Mashariki ilipozuiwa isiwe na uhusiano na nchi nyingine wakati “Ukuta wa Berlin” ulipojengwa katika mwaka wa 1961, maelfu wamesikia habari njema, wakajifunza kweli, wakajiweka wakf wakabatizwa. Wao wanahakikisha kabisa kwamba roho ya Yehova haizuiliwi, hata na kuta na maboma yaliyojengwa na wanadamu. Hivyo mashahidi wa Yehova katika Ujeremani ya Mashariki ambao wamekuwa wakifanya kazi na kuishi chini ya marufuku na magumu kwa zaidi ya miaka 23 sasa wanaweza kusema hivi pamoja na Mfalme Daudi: “Kwa msaada wa Mungu wangu naruka ukuta.”—Zab. 18:29.
—Kutoka 1974 Yearbook of Jehovah’s Witnesses.