Historia ya Mashahidi wa Yehova katika Nyakati za Kisasa
—United States ya Amerika
HOTUBA za Biblia zilitoa nafasi ya kueleza kweli za Maandiko, naye C. T. Russell alihutubia wasikilizaji wengi mara nyingi. Kwa mfano, mwaka wa 1905 mpaka 1907 alisafiri United States na Canada kwa gari-moshi la pekee au motokaa akaongoza mfululizo wa makusanyiko ya siku moja. Wakati huo hotuba yake ya watu wote ilikuwa ikisema “Kwenda Hell na Kurudi.” Hotuba hiyo ilikuwa yenye kuchekesha ikitoa maelezo juu ya safari ya kuwazia ya kwenda hell na kurudi, nayo ilitolewa nyumba zikiwa zimejaa pomoni katika karibu kila jiji katika nchi zote mbili.
Hotuba za Biblia zilitolewa pia wakati wa safari za C. T. Russell za kwenda ng’ambo. Mwaka wa 1903 alikuwa amefunga safari ya pili kwenda Ulaya, akahutubia wasikilizaji katika miji mbali-mbali. Halafu, kuanzia Desemba 1911 mpaka Machi 1912, Russell alifunga safari ya kuzunguka ulimwengu akiwa ndiye mwenyekiti wa halmashauri ya watu saba, akaenda Hawaii, Japan, China, kupita kusini ya Asia mpaka Afrika, kisha akaenda Ulaya na kurudi New York. Walipitia katika njia walizopitia wajumbe wa Jumuiya ya Wakristo (Kristendomu) kwenda katika nchi za ugenini nao wakatoa hotuba nyingi kwa njia hiyo wakaeneza mbegu za kweli ambazo baadaye zilitokeza vikundi vikundi vyenye bidii vya Wakristo watiwa mafuta katika maeneo yaliyotawanyika ya dunia. Walakini, zaidi ya safari hii ya ulimwenguni pote C. T. Russell alisafiri Ulaya kwa kawaida na kusafiri sana katika Amerika ya Kaskazini yote akiwa katika magari-moshi ya pekee ya “safari ya makusanyiko” akifuatana na wafanya kazi wenzake wengi
NJIA MPYA YA KUTANGAZIA HABARI NJEMA
Wanafunzi wa Biblia waliukumbuka sana unabii wa Yesu Kristo: “Habari njema ya ufalme itahubiriwa katika ulimwengu wote, kuwa ushuhuda kwa mataifa yote; hapo ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mt. 24:14) Kwa hiyo, mwaka huo wenye maana wa 1914 ulipokuwa ukikaribia zaidi, watu wa Mungu walianza shughuli kubwa sana ya ulimwenguni pote isiyopata kuwa na kifani kufikia hapo, ya kuelimisha na kuonya. Walitumia njia mpya ya kijasiri ya kutangazia habari njema.
Tuseme sasa ni mwaka wa 1914. Wazia kwamba umeketi kati ya mamia ya watu katika jumba la sinema lenye giza. Mbele yako kiko kitambaa kikubwa cha sinema. Unashangaa kuona mwanamume mwenye mvi aliyevaa kanzu akitokea, naye aanza kusema bila kuwa na karatasi yenye mambo anayosema. Naam, umepata kwenda sinema. Lakini hii ni tofauti. Mwanamume huyo asema nawe wayasikia maneno yake. Hii si sinema ya kikawaida tu isiyo na sauti. Ni kitu cha pekee kwa kutengenezwa kwa ufundi nao ujumbe wake pia ni wa pekee, nawe unavutiwa. Mwanamume huyo ni nani? Yeye ndiye Charles Taze Russell. Nayo sinema hiyo ni ipi? Ndiyo “Photo-Drama of Creation.” Ilikuwa sinema ya saa nane ya picha ndogo za kusimama (slides) na nyingine yenye picha zenye kuonyesha vitu vikitembea na kupita, si kusimama mahali pamoja tu, ikiwa na rangi na sauti. Sinema hiyo iliyokusudiwa kuonyeshwa kwa sehemu nne ilionyesha uumbaji na historia ya kibinadamu hata upeo wa kusudi la Mungu kwa dunia na wanadamu mwishoni mwa utawala wa miaka elfu wa Yesu Kristo. Vipande vya picha ndogo ndogo (slides) na zile zenye kupita vilipangwa kwa njia ambayo rekodi za hotuba na muziki zilifanya kazi wakati ule ule sinema ilipokuwa ikiendelea. Yalikuwa yamefanywa majaribio mengi ya kuwa na sinema za rangi na sauti, lakini miaka mingi ilipita bila ya wenye kujaribu kufanikiwa kibiashara. Ni mwaka wa 1922 sinema ya rangi kamili ilipotokea, yenye kuonyesha umbo lote la kitu, badala ya kuonyesha nusu tu. Mwaka wa 1927 ndipo watu walipoweza kuona sinema ya pesa yenye maongezi ya watu wawili na muziki. Hata hivyo, sinema ya Photo-Drama of Creation ilikuwa na rangi, na maneno na muziki. Ilikuwa imeonyeshwa kwa maneno na muziki kabla sinema za namna hiyo hazijatokea, na mamilioni ya watu yaliiona bila malipo!
Kwa hiyo, Demetrius Papageorge, ambaye alikuwa mshiriki wa muda mrefu wa wafanya kazi wa makao makuu ya Sosaiti, hakusema hivi bure: ‘Photo-Drama ilikuwa kazi ya ufundi mwingi, tunapofikiria hesabu ndogo ya Wanafunzi wa Biblia na pesa chache zilizokuwako. Kweli ilikuwa ikitegemezwa na roho ya Yehova!
MAKOLPOTA ‘WAPASHWA MOTO KWA ROHO’
Kwa miaka mingi kabla ya 1914 makolpota wenye juhudi, wanaume na wanawake wa Kikristo ‘waliopashwa moto kwa roho,’ walikuwa wamekuwa wakieneza habari njema kote kote. (Rum. 12:11, NW) Utumishi wa ukolpota ulianza mwaka wa 1881, wakati Zion’s Watch Tower ilipokuwa na makala yenye kusema “Watakiwa Wahubiri 1,000.” Watu ambao hawakuwa na jamaa za kuwategemea na ambao wangeweza kutoa fungu moja la wakati wao kwa kazi ya Bwana walipewa shauri la mpango fulani. Ulikuwa mpango wa kwenda katika majiji na miji wakiwa makolpota au waeneza injili. Kwa kusudi gani? Watch Tower lilisema hivi: “Tafuteni kila mahali Wakristo wenye bidii . . . jaribuni kuwajulisha utajiri wa neema ya Baba Yetu, na mazuri ya neno Lake.” Watu hao walipaswa kuachiwa vitabu vya habari za Biblia, na makolpota waliruhusiwa kulipa gharama zao wenyewe kwa pesa zilizopokewa kutokana na maangusho ya vitabu na maandikisho ya Watch Tower yaliyopatikana.
Zion’s Watch Tower la Mei 1887 lilitolea makolpota mashauri mazuri juu ya watakayosema milangoni. Lilisema hivi pia: “Iweni na moyo wa ushujaa uliojawa na upendo kwa Mungu na kwa wale mnaotaka kuelekeza nuruni, uliojawa na imani katika Mungu na tumaini katika ahadi zake, na uliojawa na tumaini kwamba Mungu atapendezwa kuwatumieni kwa utukufu wake sasa na kuendelea vilevile.”
Wakiwa na makusudi yasiyo ya kichoyo, makolpota waaminifu walifanya kazi kwa bidii, wakimtegemea Yehova. Nazo jitihada zao zilithawabishwa. Nyakati nyingine makundi yalianza kwa sababu ya utendaji wa makolpota. Waliridhika sana na kupata thawabu za kiroho. Naam, walichoka, lakini Edythe anasema hivi kwa niaba ya makolpota waaminifu wote wa zamani: “Sisi tulikuwa vijana na wenye furaha katika utumishi, tukipendezwa kutumia nguvu zetu tumtumikie Yah.”
—Kutoka 1975 Yearbook of Jehovah’s Witnesses.