Historia ya Mashahidi wa Yehova Katika Nyakati za Kisasa
—United States ya Amerika
MIAKA yote ambayo makolpota waaminifu na Wanafunzi wa Biblia wengine walipozitangaza habari njema kwa juhudi, Shetani Ibilisi hakulegeza mkono wake na kuacha kujitahidi kuwaharibu. Angaliweza kufanya hivyo isingalikuwa ni kwa sababu ya kulindwa na Mungu. (1 Pet. 5:8, 9; Ebr. 2:14) Wao walikubali ukweli wa ahadi ya Mungu kwa watu wake ya nyakati za kale: “Kila silaha itakayofanyika juu yako haitafanikiwa, na kila ulimi utakaoinuka juu yako katika hukumu utauhukumu kuwa mkosa.”—Isa. 54:17.
Yesu Kristo aliteswa, na wafuasi wake wanaweza kutazamia kutendewa namna iyo hiyo na wenye kuzoea dini ya uongo na ulimwengu kwa ujumla. (Yohana 15:20) Walakini, nyakati nyingine shambulio la Shetani limekuwa la kutokea ndani, likianza na watu wenye tabia mbaya ndani ya tengenezo la Kikristo, likitokana na visa vilivyohusu watu ambao kweli ‘si wa kwetu.’—1 Yohana 2:19.
Kwa kuwa Charles Taze Russell alifundisha kweli kutokana na Neno la Mungu, alichukiwa na kusingiziwa, sana sana na viongozi wa dini. Lakini, Wakristo wa kisasa wanatazamia kutendewa hivyo, kwa maana ndivyo Yesu na mitume wake walivyotendewa na wapinzani wa kidini.—Luka 7:34.
MATARAJA MAKUU
Wakati huo zilikuwako pia sababu za kufurahi. Kwa miaka mingi watu wa Mungu walikuwa wameonyesha mwaka wa 1914 kuwa mwaka ambao ungekuwa mwisho wa Majira ya Mataifa. Mataraja yao hayakuwa ya kufisha moyo. Julai 28, 1914, Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ilifyatuka, nayo Oktoba 1 ilipokaribia mataifa na milki zaidi na zaidi zikaingia vitani. Kama vile mashahidi wa Yehova wa Kikristo wajuavyo kwa kujifunza Biblia, kipindi cha utawala usiokatizwa wa ulimwengu wa Mataifa kilikoma 1914, ufalme wa kimbinguni wa Mungu ulipozaliwa Yesu Kristo akiwa mfalme. (Ufu. 12:1-5) Lakini kulikuwa na mataraja mengine pia kuhusu mwaka wa 1914. Juu ya hayo, Ndugu A. H. Macmillan aliandika hivi katika kitabu chake Faith on the March: “Agosti 23, 1914, kama ninavyokumbuka vizuri, Pasta Russell alifunga safari kwenda magharibi ya Kaskazini, kushuka katika pwani ya Pacific na kupanda kuingia katika mikoa ya Kusini, kisha akaimalizia katika Saratoga Springs, New York, ambako tulikuwa na kusanyiko Septemba 27-30. Huo ulikuwa wakati wa kupendeza sana kwa sababu baadhi yetu tulifikiri kabisa kwamba juma ya kwanza ya mwezi huo wa Oktoba tungekwenda mbinguni.”
Wazo la kwenda mbinguni mwaka wa 1914 lilikuwa lenye nguvu kati ya wengine wa Wanafunzi wa Biblia. C. T. Russell mwenyewe alikuwa ameonya juu ya kufikiri-fikiri kwa watu kusiko na msingi mzuri. Kwa mfano, alizungumza mwisho wa Majira ya Mataifa kisha akasema hivi katika The Watch Tower la Desemba 1, 1912: “Mwishowe, na tukumbuke kwamba hatukujiweka wakf ama mpaka Oktoba, 1914, wala mpaka Oktoba, 1915, wala mpaka tarehe yo yote nyingine, bali ‘mpaka kufa.’ Ikiwa kwa sababu yo yote Bwana ameruhusu tukosee hesabu ya unabii, ishara za nyakati zatuhakikishia kwamba makosa ya hesabu hayawezi kuwa makubwa sana. Nayo neema ya Bwana na amani yake ikiwa pamoja nasi wakati ujao kama ilivyokuwa zamani, kulingana na ahadi Yake, tutafurahi kwenda au kubaki wakati wo wote, na kuwa katika utumishi Wake, ama upande huu wa kisetiri au upande ule mwingine [duniani au mbinguni], lo lote ambalo Bwana wetu ataona linafaa zaidi.”
C. J. Woodworth asema, “Lakini Oktoba 1, 1914 ilifika na kupita—na miaka chungu nzima ikapita—na bado watiwa mafuta walikuwa duniani hapa. Wengine waliona uchungu wakaiacha kweli.”
Katika gazeti The World, ambalo ndilo gazeti kubwa zaidi la mji wa New York, kulikuwa na makala yenye kusema “Mwisho wa Falme Zote mwaka wa 1914,” katika sehemu yake ya Jumapili ya tarehe ya Agosti 30, 1914. Humo ilisemwa hivi, kwa ufupi:
“Kutokea kwa vita yenye kuogofya katika Ulaya kumetimiza unabii usio wa kawaida sana. Kwa robo karne iliyopita, kupitia kwa wahubiri na magazeti, ‘Wanafunzi wa Biblia wa Mataifa Yote,’ wanaojulikana vizuri zaidi kama ‘Millennial Dawners,’ wamekuwa wakitangazia ulimwengu kwamba Siku ya Ghadhabu iliyotajwa kwa unabii katika Biblia ingepambauka mwaka wa 1914. ‘Jihadharini na mwaka wa 1914!’ ndivyo mamia ya wainjilisti wenye kusafiri huku na huko nchini wamekuwa wakipaza sauti, wakiwakilisha imani hii ngeni, kwamba ‘Ufalme wa Mungu u karibu.’ . . . ”
—Kutoka 1975 Yearbook of Jehovah’s Witnesses.