Maswali Kutoka Kwa Wasomaji
● Je! Mathayo 27:52, 53 inamaanisha kwamba wakati wa kufa kwa Yesu watu fulani walifufuliwa kaburini?
Wafafanuzi wengi wa Biblia wanadhani hiyo ndiyo maana ya mistari hiyo. Lakini wanafunzi wanakubali kwamba maana na tafsiri inayofaa ya mistari hiyo ni ngumu sana. Kwa kweli, ziko sababu za kuamini kwamba mistari hiyo inamaanisha kwamba Yesu alipokufa tetemeko la nchi lililofuata lilifungua makaburi wazi karibu na Yerusalemu na kutoa maiti nje hata zikaonekana na wapita njiani.
Mathayo 27:52, 53 inasema kwamba “makaburi pia yalifunguliwa, na miili mingi ya watakatifu waliokuwa wamelala usingizi ikainuliwa, nao wakiisha kutoka makaburini baada ya ufufuo wake wakaingia katika mji mtakatifu wakaonekana na wengi.”—Common Bible.
Lakini ikiwa ufufuo ulitokea wakati Yesu alipokufa, kama vile tafsiri hii na nyingine zinavyoonyesha, je! waliofufuliwa wangalingoja mpaka Yesu mwenyewe afufuliwe, siku ya tatu baada ya kufufuliwa kwao, kabla hawajaondoka katika makaburi yao? Mungu alikuwa na sababu gani ya kufufua “watakatifu” hao wakati huo, kwa maana Yesu ndiye aliyepaswa kuwa “mzaliwa wa kwanza katika wafu”? (Kol. 1:18; 1 Kor. 15:20) Pia, Wakristo waliotiwa mafuta au “watakatifu” wangeshiriki katika ufufuo wa kwanza Kristo akiisha kuwapo wakati ujao.—1 The. 3:13; 4:14-17; Ufu. 20:5, 6.
Angalia kwamba, masimulizi hayasemi kamwe kamwe kwamba “miili” hiyo ilihuika (ilipata uhai). Yanasema kwamba iliinuliwa au ikatupwa nje ya makaburi na tetemeko la nchi. Jambo kama hilo lilitukia katika mji wa Sonson katika Colombia mwaka wa 1962. Gazeti El Tiempo (Julai 31, 1962) lilitoa habari hizi: “Maiti mia mbili zilitupwa kutoka makaburi yao na tetemeko la nchi lenye nguvu nyingi.” Watu wenye kupita karibu au katika makaburi hayo waliiona mizoga, na kwa hiyo ikawapasa watu wengi katika Sonson waende wakazike tena watu wa ukoo wao.
Bila ya kupotoa sarufi ya Kigiriki, mtafsiri anaweza kutafsiri Mathayo 27:52, 53 kuonyesha kwamba ni kwa njia iyo hiyo maiti zilivyotolewa nje na tetemeko la nchi lililotokea wakati wa kufa kwa Yesu. Hivyo tafsiri ya Johannes Greber (1937) inatafsiri mistari hiyo hivi: “Makaburi yakafunguliwa wazi, na miili mingi ya wale waliozikwa ikarushwa ikiwa wima. Ilitoka katika makaburi ikiwa hivyo ikaonekana na wengi waliopita karibu na mahali hapo wakirudi mjini.”—Linganisha New World Translation.
Tetemeko hilo la nchi lenye nguvu lililotoa nje maiti zilizoonekana karibuni na wasafiri waliopeleka habari Yerusalemu, pamoja na kupasuka kwa pazia la hekalu lililotenganisha Patakatifu na Patakatifu Zaidi Sana, lilikuwa uhakikisho zaidi kwamba Yesu hakuwa mvunja sheria wa ivi hivi aliyeuawa kwa kufanya kosa. Yeye alikuwa ndiye Masihi ambaye karibuni angekuwa mzaliwa wa kwanza kutoka kwa wafu na kuamuliwa kupata uzima wa kimbinguni.