Historia ya Mashahidi wa Yehova Katika Nyakati za Kisasa
—United States ya Amerika
WATU wa Mungu waliambiwa waendelee kuwa thabiti ‘wakazidi sana kutenda kazi ya Bwana.’ (1 Kor. 15:58) Kisa kilichosimuliwa na A. H. Macmillan miaka mingi baadaye kilionyesha kwamba Ndugu Russell alisadiki kwamba kulikuwa na kazi kubwa mbele ya kufanywa na watumishi wa Yehova. Sikuzote C. T. Russell alitumia nyakati zake za asubuhi, kutoka saa 2:00 asubuhi mpaka adhuhuri, akitayarisha makala za Watch Tower na kuandika mambo mengine na kuchunguza Biblia. Macmillan aliandika hivi: “Hakuna mtu aliyekwenda karibu na chumba cha uchunguzi saa hizo asipokuwa ameitwa au akiwa na jambo la maana sana. Karibu dakika tano baada ya saa mbili, stenografa (mwandikaji wa maneno ya mkato) mmoja alishuka akikimbia ngazini akaniambia: ‘Ndugu Russell anataka akuone katika chumba cha uchunguzi.’ Nikawaza, ‘Kwani nimefanya nini?’ Kuitwa kwenye chumba cha uchunguzi asubuhi kulimaanisha kulikuwa na jambo la maana.” Sikiliza masimulizi zaidi ya Ndugu Macmillan:
“Nilikwenda kwenye chumba cha uchunguzi naye akasema: ‘Ingia, ndugu. Tafadhali ingia katika chumba cha uchoraji.’ Hicho kilikuwa chumba kilichoongezwa kupanua chumba cha uchunguzi. Akasema: ‘Ndugu, je! unapendezwa sana na kweli kama ulivyokuwa ulipoanza?’ Nilishangaa. Akasema: ‘Usishangae. Hilo lilikuwa ulizo la kukudokezea mambo tu.’ Kisha akanieleza hali yake ya kimwili, nami nilijua vya kutosha kwamba kulingana na dalili zake za kimwili asingekuwa hai miezi mingi zaidi isipokuwa akipata nafuu. Akasema: ‘Haya, sasa ndugu, mimi nilitaka kukuambia hivi. Siwezi kuendeleza kazi tena, na hali kuna kazi kubwa ya kufanywa. . . . ’
“Nikasema, ‘Ndugu Russell, mimi sielewi unavyosema.’
“‘Wamaanisha nini, ndugu?’ akauliza.
“‘Ufe kisha kazi hii iendelee?’ nikajibu. ‘Utakapokufa sote tutakunja mikono yetu kwa kuridhika na kungojea kwenda mbinguni pamoja nawe. Wakati huo tutaacha kufanya kazi.’
“‘Ndugu,’ akasema, ‘ikiwa hilo ndilo wazo lako, wewe huelewi ilivyo. Hii si kazi ya mwanadamu. Mimi si wa maana kwa kazi hii. Nuru inazidi kung’aa. Kuna kazi kubwa mbele.’ . . .
“Baada ya kueleza kazi iliyokuwa mbele, Ndugu Russell akasema: ‘Sasa, mimi nataka mtu atakayeingia humu na kuchukua daraka langu. Mimi bado ndimi nitaongoza kazi, lakini siwezi kuifanya kama zamani.’ Kwa hiyo tukazungumza juu ya watu mbalimbali. Mwishowe, nilipoondoka nikapitia katika mlango wa kusukuma na kuendea kijia cha kuondokea humo, akasema: ‘Ngoja kidogo. Nenda chumbani mwako ukaseme na Bwana juu ya jambo hili kisha uje uniambie kama Ndugu Macmillan ataikubali kazi hii.’ Alifunga mlango mimi nikiwa kimya kabisa. Nilisimama hapo nimeduwaa. Ningeweza kufanya nini nimsaidie Ndugu Russell katika kazi hii? Ilitaka mtu mwenye kujua habari za biashara zilizomhusu yeye, nami nilijua kuhubiri dini tu. Walakini, nikawaza tena nikarudi baadaye nikamwambia: ‘Ndugu, nitafanya lo lote nitakaloweza. Mimi sijali utakaponiweka.’”
C. T. Russell aliwaambia washirika wake wa karibu wajitayarishe kuongezeka katika idadi, akisadiki kwamba kulikuwa na kazi nyingi sana mbele ya watu wa Mungu. Akafanya mabadiliko fulani ambayo yangeunganisha tengenezo, akapendekeza mabadiliko ya wakati ujao asipoweza kuyafanya mwenyewe. A. H. Macmillan akakabidhiwa uangalizi wa afisi na makao ya Betheli. Kisha, Russell akafunga safari ya kutoa hotuba aliyokuwa ameipanga zamani, ijapokuwa afya yake ilikuwa ikiharibika zaidi na zaidi naye akipatwa na masumbufu mengi ya kimwili kufikia vuli ya mwaka wa 1916.
SAFARI YA MWISHO
Ndugu Russell na mwenzake waliondoka New York Oktoba 16, 1916. Walifika Los Angeles Jumapili, Oktoba 29, na ndiko C. T. Russell alikotolea hotuba yake ya mwisho kwa kundi jioni hiyo. Wakati huo alikuwa amenyong’onyea sana asiweze kusimama akitoa hotuba. “Nasikitika siwezi kusema kwa nguvu,” kasema Russell. Kisha akampungia mkono mwenyekiti aondoe kinara na kuleta kiti, akasema hivi alipokuwa akiketi, “Tafadhalini mnisamehe kwa kuketi.” Akahutubu kwa karibu dakika 45, kisha akajibu maulizo kwa muda mfupi. Dwight T. Kenyon anasema hivi juu ya wakati huo: “Mimi nilikuwa na pendeleo la kuhudhuria hotuba ya mwisho ya Ndugu Russell katika Los Angeles Oktoba 29, 1916. Alikuwa mgonjwa sana naye aliendelea kuketi wakati wa hotuba yake juu ya Zekaria 13:7-9. Andiko lake la kwa heri la Hesabu 6:24-26 lilinivutia weeee!”
Akijua kwamba hali yake mbaya sana isingemwezesha kusonga mbele, Russell aliamua kuacha kusafiri akahutubu apate kurudia makao ya Betheli haraka katika Brooklyn. Jumanne, Oktoba 31, C. T. Russell alikuwa akielekea kufa. Katika Panhandle, Texas, daktari aliyekuwa ameitwa kwa simu alipanda gari-moshi kwa muda akachunguza hali ya Russell, akaona dalili za hatari. Kisha gari-moshi likaendelea na mwendo wake. Muda mfupi baadaye, alasiri mapema Jumanne, Oktoba 31, 1916, Charles Taze Russell mwenye umri wa miaka 64 alifia Pampa, Texas.
Watumishi wa Yehova walikuwa ndio kwanza wapite katika wakati wenye kujaribu, lakini miaka ya hatari ilikuwa mbele yao. C. T. Russell alipokufa Oktoba 31, 1916, Watch Tower Society ilikosa msimamizi (president). Halmashauri yenye amri ndiyo iliyosimamia mambo ya Sosaiti mpaka mkutano wake wa kila mwaka Januari 6, 1917. Bila shaka, wakati huo ulizo lilitokea juu ya ni nani angekuwa msimamizi wa pili. Siku moja Ndugu Van Amburgh alimwuliza A. H. Macmillan: “Ndugu, wewe waonaje juu ya jambo hili?” “Yuko mtu mmoja tu, upende usipende,” alijibu Macmillan. “Yuko mtu mmoja tu anayeweza kuangalia kazi hii sasa, naye ndiye Ndugu Rutherford.” Akimshika Macmillan mkononi, Ndugu Van Amburgh akasema: “Nakubaliana nawe.” J. F. Rutherford hakuwa na habari juu ya jambo hilo wala hakugombea uchaguzi. Lakini katika mkutano wa kila mwaka wa Sosaiti Januari 6, 1917, alitajwa na kuchaguliwa kuwa msimamizi wa Watch Tower Society.
Alipokuwa akichukua daraka lake jipya kwa unyenyekevu, Ndugu Rutherford alihutubu kifupi juu ya wakati huo, akaomba waamini wenzake watoe “sala za umoja, wawe na huruma nyingi na kushirikiana kabisa.” “Yeye ambaye ametuongoza kufikia hapo ataendelea kutuongoza. Na tuwe na mioyo mijasiri, akili zenye utayari na mikono yenye nia, sikuzote tukimtumaini Bwana kabisa, tukimtegemea kwa uongozi. Yeye atatuongoza kwenye ushindi kamili. Tunapothibitisha upya Agano letu pamoja Naye leo, tukiwa tumeungana katika vifungo vitakatifu vya upendo wa Kikristo, na tuondoke tukautangazie ulimwengu, ‘Ufalme wa Mbinguni umekaribia.’”
MSINGI WA MAISHA YA RUTHERFORD
Rutherford mwenyewe alikuwa mpiganiaji shujaa wa kweli. Alizaliwa na wazazi Wabaptist katika Morgan County, Missouri, Novemba 8, 1869. Kutoka kwa Dada Ross, dada mkubwa wa damu wa Joseph Franklin Rutherford, A. D. Schroeder alipata habari hizi: “Baba yao alikuwa Mbaptist imara katika Missouri ambako jamaa iliishi. Ndugu yake (Ross) mdogo Joseph hakutaka kamwe kukubali fundisho la Kibaptist la moto wa mateso. Hiyo ilitokeza ubishi mkali sana mara nyingi katika jamaa hata kabla hawajasikia habari za kweli. Sikuzote ndugu yake alikuwa mwenye kusadikisha sana na kutaka sana kuona mambo yakifanywa kwa njia ya haki. Tangu ujana wake alitaka kuwa wakili na hakimu. Baba yao alitaka akae shambani badala ya kwenda chuo kikuu akajifunze sheria. Joseph alilazimika kutafuta rafiki wa kumkopesha pesa, si za kuajiri tu mtu wa kukaa badala yake katika shamba la baba yake, bali pia za kumwezesha kuendelea na masomo yake ya sheria.”