Historia ya Mashahidi wa Yehova Katika Nyakati za Kisasa
—United States ya Amerika
Yesu Kristo alisema kwamba wafuasi wake wote ni “ndugu” na kwamba ‘aliye mkubwa zaidi kati yao lazima awe mhudumu wao.’ (Mt. 23:8-12) Kwa hiyo, hakuna Mkristo ye yote wa kweli anayempa mwamini mwenzake heshima isiyomstahili. Lakini, Biblia inafunua tabia za watumishi mbalimbali wa Mungu. Kwa mfano, Musa alijulikana sana kwa upole wake; Yakobo na Yohana, wana wa Zebedayo walijulikana kwa bidii yao kali kali. (Hes. 12:3; Marko 3:17; Luka 9:54) Kwa kuwa Joseph F. Rutherford alikabidhiwa madaraka mengi katika tengenezo la Mungu la kidunia, inapendeza kuangalia tabia na sifa zake.
“Sikuzote Rutherford alikuwa ameonyesha upendo mwingi sana wa Kikristo kwa washirika wenzake,” kasema A. H. Macmillan, “naye alikuwa mwenye moyo wa upole sana; lakini kwa asili hakuwa na hali ya upole na utulivu kama Russell. Yeye alisema mambo waziwazi wala hakuficha mawazo yake ya ndani. Kusema kwake mambo waziwazi, hata kulipofanywa kwa upole, nyakati nyingine kulieleweka vibaya. Lakini baada ya muda mfupi tu wa kuwa msimamizi ilionekana kwamba Bwana alikuwa amechagua mtu anayefaa kazi hiyo.”
“MSIONE KUWA NI AJABU ULE MSIBA ULIO KATI YENU, UNAOWAPATA KAMA MOTO”
Walakini, si watu wote waliokuwamo katika tengenezo waliofurahi J. F. Rutherford alipochaguliwa kuwa msimamizi. Kwa kweli, kuanzia mapema mwaka wa 1917, watu kadha walijaribu kusimamia Sosaiti kwa kujitakia makuu. Wakawa wasio na ushirikiano na wengine, na hivyo kipindi cha majaribu kama moto kikaanza. Bila shaka, Wakristo wanatazamia kupingwa na kuteswa na adui wa kilimwengu. Lakini majaribu yanayoanza ndani ya tengenezo la Kikristo lenyewe mara nyingi hayatazamiwi nayo ndiyo magumu zaidi kuvumilia.
C. T. Russell alikuwa ameona uhitaji wa kutuma mtu fulani Uingereza kutoka makao makuu akawatie nguvu Wanafunzi wa Biblia waliokuwa huko baada ya kutokea kwa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza. Alikusudia kumtuma Paul S. L. Johnson, Myahudi aliyeacha dini ya Kiyahudi akawa mhudumu Mlutheri kabla hajapata maarifa ya kweli ya Mungu. Johnson alikuwa ametumikia kama mmoja wa wasemaji wa Sosaiti wenye kusafiri naye alijulikana sana kuwa mtu mwenye uwezo. Kwa sababu ya kuheshimu vile Russell alivyotaka, halmashauri yenye amri iliyotumikia muda mfupi kabla Rutherford hajachaguliwa kuwa msimamizi ilituma Johnson Uingereza, ikampa karatasi fulani za kumwezesha kuingia nchi hiyo. Walakini, kupokewa kwake Uingereza wakati wa Novemba 1916 kulielekea kupotoa uamuzi wake na mwishowe kuwaza kwake, “mpaka,” kama alivyosema A. H. Macmillan, “akafikia azimio la upuzi kwamba yeye alikuwa ndiye ‘wakili’ wa mfano wa Yesu wa dinari. Baadaye alidhani yeye ndiye kuhani mkuu wa ulimwengu.” Katika hotuba alizotolea Wanafunzi wa Biblia katika Uingereza yote, Johnson alijiita mrithi wa Russell, akikazia kwamba vazi la Pasta Russell lilimwangukia yeye kama vile joho la Eliya (“vazi rasmi,” NW) lilivyomwangukia Elisha.—2 Fal. 2:11-14.
Alipokuwa Uingereza Johnson alijaribu kusimamia mambo yote ya utendaji wa Uingereza, hata akajaribu bila ruhusa kuondoa wafanya kazi fulani wa makao makuu ya London. Johnson alijipa hakika ya kwamba yeye mwenyewe amepaswa awe ndiye msimamizi wa Sosaiti. Alijaribu kusadikisha baraza ya wasimamizi. Kwa kufanya ionekane kwamba Ndugu Rutherford hakufaa kuwa msimamizi, Johnson alisihi wanne wa washiriki saba wa baraza hiyo wajiunge naye. Watu hao wanne walimpinga msimamizi wa Sosaiti, msimamizi-mdogo na mweka hazina, nao wasimamizi hao wapinzani wakajaribu kumnyang’anya msimamizi uongozi wake. Walakini, nia yao ilionyesha kwamba hawakustahili kuwa wasimamizi. Kwa kufaa Rutherford aliwaondoa akaweka washiriki wapya wanne wa baraza nako; kuwekwa kwao kungethibitishwa katika mkutano mkubwa ambao ungefuata wa shirika, mapema mwaka wa 1918.
Ndugu Rutherford hakuondoa haraka haraka wale wasimamizi wa zamani katika tengenezo la Kikristo. Bali, aliwapa vyeo vya kuwa wahaji, Walikataa, wao wenyewe wakatoka Betheli wakaanza kueneza upinzani wao kwa kuhutubu sana na kuandika barua katika United States yote, Canada na Ulaya. Kwa hiyo, baada ya kiangazi cha mwaka wa 1917, makundi mengi ya Wanafunzi wa Biblia yalikuwa yamegawanyika katika vikundi viwili—cha wale walioshikamana na tengenezo la Yehova na wengine waliopata kusinzia kiroho wakadanganywa kwa maneno ya werevu ya wapinzani.