Historia ya Mashahidi wa Yehova Katika Nyakati za Kisasa
MUDA mfupi baada ya Betheli kufunguliwa tena, watu wa Yehova kwa ujumla walifurahia kuungana tena. Muda mfupi baada ya Ndugu Rutherford kufaulu kufanya mikutano ya watu wote katika Los Angeles Mei wa 1919, aliamua kufanya kusanyiko kubwa. Mwishowe Cedar Point, Ohio, ndipo mahali palipochaguliwa pa kufanyia kusanyiko hilo. Kusanyiko hilo la Septemba 1-8, 1919, likawa lenye faida nyingi sana za kiroho.
Wajumbe wenye furaha waliendelea kuja. Hudhurio liliongezeka kutoka karibu 3,000 jioni ya siku ya kwanza kufikia 6,000 siku ya Ijumaa. Katika hotuba ya watu wote ya Jumapili karibu watu 7,000 walihudhuria. Katika kusanyiko hilo lenye furaha zaidi ya watu 200 walionyesha wakf wao kwa Mungu kwa kubatizwa katika maji.
Kusanyiko la mwaka wa 1919 lililofanyiwa Cedar Point lilijulisha sana kadiri kubwa ya kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote ambayo ingefanywa na watu wa Yehova. Kama alivyosema A. H. Macmillan: “Kwa hiyo wazo hilo likaanza kuthibitika kwamba, ‘Sasa tunalo jambo la kufanya.’ Sasa tusingekaa-kaa tu tukingoja kwenda mbinguni; ilitupasa kufanya kazi.”
KAZI NG’AMBO
Watu waliendelea kutaka vitabu vingi vya kusaidia kujifunza Biblia. Kwa mfano, ndivyo ilivyokuwa Canada ambako marufuku iliyokuwa imewekwa juu ya vitabu vya Watch Tower iliondolewa Januari 1, 1920. Mateso katika nchi hiyo yalielekea kuchochea watu wa Mungu wawe na juhudi zaidi ya kuhubiri na kuendeleza ibada ya kweli.
Agosti 12, 1920, J. F. Rutherford na washirika wachache walipanda meli kuelekea Ulaya. Makusanyiko yalifanywa London, Glasgow na miji mingine ya Uingereza. Akiwa na watu wengine, Rutherford alisafiri kuelekea Misri na Palestina. Maafisi mbalimbali na madarasa ya kujifunza Biblia yalitembelewa yakatiwa nguvu za kiroho. Afisi ya tawi ya Sosaiti ilianzishwa Ramallah. Katika ripoti ya mwisho wa mwaka, Ndugu Rutherford alieleza wazi kwamba Sosaiti ingeanzisha Afisi Kuu ya Ulaya ya kusimamia kazi ya kuhubiri katika Switzerland, Ufaransa, UbeIgiji, Uholandi, Ujeremani, Austria na Italia.
KITABU KIPYA CHAONGEZA MAENDELEO
Kwa miaka mingi sehemu za kitabu Studies in the Scriptures zilikuwa zimesomwa na kuenezwa sana na Wanafunzi wa Biblia. Walakini, mwaka wa 1921 kitabu kipya kilichapwa—The Harp of God (au Kinubi cha Mungu), kikiwa kimeandikwa na J. F. Rutherford. Mwishowe mwenezo wake ukawa nakala 5,819,037 katika lugha 22. “The Harp of God kilipotokea, hiyo ilikuwa baraka halisi, lilikuwa jibu kwa sala zetu,” asema Carrie Green, na kuongeza: “Kilifanya kweli ifahamike kwa wepesi zaidi, nayo kweli yote, habari zote mbalimbali zilifananishwa na ‘nyuzi za kinubi.’”
KURUDI CEDAR POINT
Muda mfupi baada ya Sosaiti kuanza kuendesha kiwanda chake cha uchapaji katika Concord Street, Brooklyn, New York, watu wa Mungu walikusanyika katika kusanyiko la mataifa yote Septemba 5-13, 1922. Mahali penyewe? Cedar Point, Ohio, ambapo kusanyiko kuu la Wanafunzi wa Biblia lilifanyiwa mwaka wa 1919. Miaka mitatu iliyokuwa katikati kulikuwa na ukuzi. Wajumbe waliofika kwenye kusanyiko la 1922 walitoka United States, Canada na Ulaya. Hudhurio la wastani la kila siku lilikuwa 10,000, na kati ya watu 18,000 na 20,000 walikuwako Jumapili. Waliobatizwa walikuwa 361.
Jiwazie ukiwa kati ya wasikilizaji wengi hao Rutherford anapoelekea kumaliza hotuba yake kwa njia ya kusisimua sana. Wamsikiliza sana anaposema haya:
“. . . Tangu mwaka wa 1914 Mfalme mwenye utukufu ametwaa uwezo wake naye atawala. Ameisafisha midomo ya jamii ya hekalu naye awatuma wakiwa na ujumbe huo. Ujumbe wa ufalme ni wa maana sana. Ni ujumbe bora kuliko ujumbe mwingine wo wote. Ndio ujumbe wa maana saa hii. Ni wajibu wa wale walio wa Bwana kuutangaza. Ufalme wa mbinguni umekaribia; Mfalme atawala; milki ya Shetani inaanguka; mamilioni ya watu wanaoishi sasa hawatakufa kamwe.
“Je! mnaamini hayo? . . .
“Basi rudini shambani, Enyi wana wa Mungu aliye juu zaidi! Jivikeni silaha zenu! Iweni na kiasi, kesheni, iweni wenye bidii, iweni mashujaa. Iweni mashahidi waaminifu na wa kweli wa Bwana. Songeni mbele katika vita mpaka kila kisehemu cha Babeli kiwe ukiwa. Utangazeni ujumbe kote kote. Lazima ulimwengu ujue kwamba Yehova ni Mungu na kwamba Yesu Kristo ni Mfalme wa wafalme na Bwana wa mabwana. Hii ndiyo siku ya siku zote. Tazameni, Mfalme atawala! Ninyi ndio mawakili wa kumtangaza. Kwa hiyo mtangazeni, mtangazeni, mtangazeni, Mfalme na ufalme wake.”
—Kutoka 1975 Yearbook’ of Jehovah’s Witnesses.