Historia ya Mashahidi wa Yehova Katika Nyakati za Kisasa—
United States ya Amerika
WATUMISHI wa Yehova wa miaka ya kwanza ya 1920 walikuwa wachache. Kufika 1924 United States ilikuwa na wastani ya Wanafunzi wa Biblia 1,064 tu wenye kuhubiri nyumba kwa nyumba kila juma. Kwa hiyo, wakati huo watu wa Mungu walitambua matokeo makubwa sana ya kutumia radio nao waliiona kama njia nzuri ya kufikia umati wa watu na ujumbe wa Ufalme.
Leseni (ruhusa) ya utangazaji ilikuwa imepatikana kwa serikali. Na herufi zilizotumiwa kujulisha stesheni yenyewe zilikuwa WBBR. Sasa mambo yote yalikuwa tayari kwa utangazaji wa kwanza. Hiyo ilikuwa Jumapili jioni, Februari 24, 1924.
Kwa karibu miaka 33 WBBR ilimtukuza Yehova na kueneza kweli ya Biblia kote kote. Sosaiti iliiuza stesheni (kituo) hii Aprili 15, 1957. Kwa sababu gani? Wakati stesheni ilipoanza kufanya kazi mwaka wa 1924, kulikuwa na kundi moja tu lenye karibu Wanafunzi wa Biblia 200 wenye kwenda miji yote mitano ya jiji la New York, na vilevile Long Island na hata sehemu za New Jersey. Walakini, kufika 1957 kulikuwa na makundi 62 ndani ya jiji la New York na kilele cha watangazaji 7,256 wa Ufalme, licha ya wahubiri 322 wa wakati wote wa habari njema. Kwa hiyo ushuhuda mkubwa ulikuwa ukitolewa. Pia, kunakuwa na matokeo zaidi kusema na watu katika nyumba zao, ambako wanaweza kuuliza maulizo na kupokea mafundisho zaidi ya kutoka katika Neno la Mungu. Pesa zilizotumiwa katika utangazaji wa radio zingeweza kutumiwa kwa njia nyingine kuendeleza faida za ufalme wa Mungu.
Wanafunzi wa Biblia walihusika katika tukio jingine linalojulikana sana la kutumia radio mwaka wa 1928. Katika Detroit, Michigan, Jumapili, Agosti 5, wakati J. F. Rutherford alipotoa hotuba ya watu wote “Mtawala kwa Ajili ya Watu” kwa wasikilizaji 12,000, hotuba yenyewe ilitangazwa na mwungano wa stesheni 107, nayo ilipelekwa maili 35,500 kwa kamba za simu na maili 91,400 kwa telegrafu, tena ilirudiwa kwa short wave kupelekwa Australia na New Zealand.
Programu za radio zilimaliza mwingi wa wakati wa Ndugu Rutherford. Ushuhuda mwingi ulitolewa, lakini hakuweza kusafiri wala kupanga makusanyiko katika sehemu mbalimbali za dunia. Kwa hiyo mwaka wa 1931 Sosaiti ikaamua kufanya programu zilizotiwa katika utepe au sahani za santuri. Kufika mwaka wa 1933, mwaka wenye kilele, stesheni 408 zilikuwa zikitumiwa kupeleka ujumbe kwenye bara sita, na hotuba za Biblia mbalimbali 23,783 zilitangazwa, na nyingi kati yazo zilikuwa za dakika kumi na tano zikiwa zimetiwa katika utepe au sahani za santuri. Siku hizo, mtu akifungua radio angeweza kusikia matangazo ya Watch Tower yakitoka katika stesheni zilizotawanyika sana zote zikisema wakati ule ule. Mara nyingi mawimbi ya hewa yalijawa na maneno ya kweli yaliyomtukuza Mungu.
‘WAFUNDISHWA NA YEHOVA’
Bila shaka Yehova aliwabariki watu wake huko nyuma miaka ya 1920 naye aliwapa vitu walivyohitaji kuendeleza faida za Ufalme. Alijihakikisha pia kuwa Mungu mwenye kufunua mambo kidogo kidogo. Wanafunzi wa Biblia nao waliona ni lazima kurekebisha kuwaza kwao. Lakini walishukuru kwa uongozi wa Mungu nao walikuwa na shauku ya ‘kufundishwa na Yehova.’—Yohana 6:45; Isa. 54:13.
Kwa mfano, iliwapasa watu wa Mungu warekebishe kuwaza kwao juu ya mwaka wa 1925. Walidhani kwamba mwaka huo ungekuwa ndio mwisho wa yubile 70, kila moja ikiwa ya miaka 50 tangu Waisraeli walipoingia nchi ya Kanaani. (Law. 25:1-12) A. D. Schroeder asema hivi: “Ilidhaniwa kwamba wakati huo mabaki ya wafuasi watiwa mafuta wa Kristo wangekwenda mbinguni wakawe sehemu ya Ufalme na kwamba watu waaminifu wa kale, kama Ibrahimu, Daudi na wengine, wangefufuliwa wawe wakuu wa kusimamia serikali ya dunia wakiwa sehemu ya ufalme wa Mungu.”
Mwaka wa 1925 ulikuja na kupita. Wafuasi wa Yesu waliotiwa mafuta walikuwa duniani bado kama jamii. Watu waaminifu wa kale—Ibrahimu, Daudi na wengine—hawakufufuliwa wawe wakuu duniani. (Zab. 45:16)
Watumishi waaminifu wa Mungu hawakuwa wamejiweka wakf kwake mpaka mwaka fulani tu. Walikuwa wamekata maneno kumtumikia milele. Mataraja yasiyotimia kuhusu mwaka wa 1925 hayakuleta mgogoro mkubwa wala kuharibu imani ya watu hao. James Poulos asema, “Kwa waaminifu mwaka wa 1925 ulikuwa mzuri sana. Kupitia kwa ‘mtumwa wake mwaminifu mwenye akili’ Yehova alitufahamisha maana ya sura ya kumi na mbili ya Ufunuo.”
Miaka michache baadaye watu wa Yehova walijifunza kwa mara ya kwanza kwamba Yesu Kristo hakufa juu ya msalaba ulio kama T. Januari 31, 1936, Ndugu Rutherford alitolea jamaa ya Betheli ya Brooklyn kitabu kipya Riches (Mali). Kwa ufupi, kilisema hivi katika ukurasa wa 27 kupatana na Maandiko: “Yesu aliuawa, si juu ya msalaba wa mbao, kama unaoonyeshwa katika sanamu na picha nyingi ambazo hutengenezwa na kuonyeshwa na wanadamu; Yesu aliuawa kwa kugongomewa mwili wake mtini.”
Mkazo zaidi uliendelea kutiwa juu ya jina la kimungu. Kwa mfano, fikiria makala kuu katika matoleo ya Januari 1 ya miaka mingi ya The Watch Tower. Zilikuwa zikisema: “Ni Nani Atakayemheshimu Yehova?” (1926), “Yehova na Kazi Zake” (1927), “Heshimu Jina Lake” (1928), “Nitamsifu Mungu Wangu” (1929) na “Mwimbie Yehova” (1930).
Walakini, kusanyiko la watu wa Mungu katika Columbus, Ohio, la Julai 24-30, 1931, lilitukuza jina la Yehova zaidi sana. Lilikuwa la pekee sana kwa maana makusanyiko yalipangwa yawe mahali pengine 165 duniani mwote. Lakini hilo silo lililokuwa jambo la maana zaidi. Kulikuwa na jambo la maana zaidi. Lilihusiana na herufi zenye fumbo “JW” zilizokuwa katika programu ya kusanyiko iliyochapwa na katika kichwa cha ukurasa wa The Messenger, ambalo ndilo lililokuwa gazeti la kusanyiko—na kwa kweli, zilionekana mahali pengi. “Tulipofika karibu na wanja za kusanyiko,” asema Burnice E. Williams, Sr., “tuliona herufi ‘JW’ kila mahali. Lakini tulishangaa, ‘JW hizi ni za nini?’ kwa maana hatukujua zilisimamia nini.” Dada Herschel Nelson akumbuka haya: “Ilifikiriwa-fikiriwa kwa kukisia-kisia kilichosimamiwa na herufi JW— ikasemwa ni Just Wait (Ngoja Tu), Just Watch (Tazama Tu), na kilichokuwa sahihi . . . ”
Maana ya “JW” ilifunuliwa Jumapili, Julai 26, 1931, wakati wakusanyikaji wenye kusisimka walipochagua kwa moyo azimio lililotolewa na J. F. Rutherford lenye kichwa “Jina Jipya.” Kwa ufupi, lilisema hivi:
“KWA HIYO, sasa ili hali yetu ipate kujulikana, na kwa sababu ya kuamini kwamba hii inapatana na mapenzi ya Mungu, kama yanavyoelezwa katika Neno lake, NA IAZIMIWE kama ifuatavyo:
“KWAMBA sisi tunampenda sana Ndugu Charles T. Russell kwa ajili ya kazi yake, na kwamba tunatambua kwa furaha kwamba Bwana alimtumia akabariki sana kazi yake, lakini hatuwezi kupatana na Neno la Mungu kukubali kuitwa ‘Waruseli’; kwamba Watch Tower Bible and Tract Society na International Bible Students Association na Peoples Pulpit Association ni majina tu ya mashirika tuliyo nayo kama kampuni ya Wakristo, nasi twayasimamia na kuyatumia kuendesha kazi yetu kwa kutii amri za Mungu, hata hivyo hakuna lo lote la majina hayo linalotuhusu wala kutumika kwetu sisi kama jamii ya Wakristo wanaofuata nyayo za Bwana wetu, Kristo Yesu; kwamba sisi tu wanafunzi wa Biblia, lakini kama jamii ya Wakristo walio shirika, tunakataa kujitwalia au kuitwa kwa jina ‘Wanafunzi wa Biblia’ au majina mengine kama hilo ndiyo hali yetu halisi mbele za Bwana itambuliwe; twakataa kuchukua au kuitwa kwa jina la mwanadamu ye yote;
“KWAMBA, kwa kuwa tulinunuliwa kwa damu yenye thamani ya Yesu Kristo Bwana na Mkombozi wetu, aliyehesabiwa kuwa haki na kuzaliwa na Yehova Mungu na kuitwa kwenye ufalme wake, bila kusitasita twatangaza ushikamano na uaminifu wetu wote kwa Yehova Mungu na ufalme wake; kwamba sisi tu watumishi wa Yehova Mungu walioagizwa kufanya kazi kwa jina lake, na kwa kutii amri yake, tutoe ushuhuda wa Yesu Kristo, na kujulisha watu kwamba Yehova ndiye Mungu wa kweli na Mwenye Nguvu Zote; kwa hiyo kwa furaha tunalikubali na kulichukua jina ambalo kinywa cha Bwana Mungu kimelitaja, nasi twataka kujulikana na kuitwa kwa jina hilo, yaani, mashahidi wa Yehova.”
Sasa ilikuwa wazi. Zile herufi zenye fumbo “JW” zilisimamia Mashahidi wa Yehova kwa Kiingereza (Jehovah’s Witnesses). “Sitasahau kamwe vifijo na vigelegele vilivyotokea katika mkutano huo habari hizo zilipojulishwa mwishowe,” asema Arthur A. Worsley. Herbert H. Boehk aongeza hivi: “Katika mji wote wa Columbus ishara zilizokuwa katika madirisha ya maduka zikisema ‘Karibuni I.B.S.A.’ zilishushwa zikawekwa nyingine zenye kusema, ‘Karibuni, Mashahidi wa Yehova.”
Wakati A. H. Macmillan alipokuwa na umri wa miaka 88 alihudhuria “Matunda ya Roho” Kusanyiko la Mashahidi wa Yehova katika mji uo huo. Huko, Agosti 1, 1964, Ndugu Macmillan alitoa maelezo haya ya kupendeza juu ya vile jina hilo lilivyochaguliwa:
“Nilikuwa na pendeleo la kuwa hapa Columbus mwaka wa 1931 tulipopokea . . . lile jina jipya . . . Mimi nilikuwa kati ya wale watano waliopaswa kutoa maelezo juu ya tulivyoliona wazo la kulikubali jina hilo, nami nikawaambia hivi kwa ufupi: Mimi niliona hilo ni wazo zuri sana kwa sababu jina hilo liliueleza ulimwengu tulikuwa tukifanya nini na shughuli yetu ni nini. Kabla ya hapo tulikuwa tukiitwa Wanafunzi wa Biblia. Kwa sababu gani? Kwa sababu ndivyo tulivyokuwa. Kisha mataifa mengine yalipoanza kujifunza nasi, tukaitwa Wanafunzi wa Biblia wa Mataifa Yote (International Bible Students). Lakini sasa tu mashahidi wa Yehova Mungu, nalo jina hilo linaeleza watu wote sisi ni nani na tunafanya nini. . . .
“Mimi naamini Mungu Mwenye Nguvu Zote ndiye aliyeongoza kwenye jambo hilo, kwa maana Ndugu Rutherford mwenyewe aliniambia kwamba aliamka usiku mmoja alipokuwa akitayarisha kusanyiko hilo akasema, ‘Sasa sababu gani nilipendekeza kuwe na kusanyiko la mataifa yote hali sina hotuba wala ujumbe wa pekee kuwapa? Sababu gani niwaite wote hapa?’ Kisha akaanza kufikiria jambo hilo, halafu Isaya 43 ikaingia akilini mwake. Akaamka saa nane usiku akaandika akiwa katika deski yake kwa mwandiko wa shorthand (wa mkato) muhtasari ya hotuba atakayotoa juu ya Ufalme, tumaini la ulimwengu, na juu ya jina jipya. Aliandika mambo yote aliyosema wakati uo huo, yaani saa nane ya usiku. Tena [hamna] shaka akilini mwangu—sikuwa nalo wakati huo wala sasa—kwamba Bwana alimwongoza katika jambo hilo, nalo hilo ndilo jina ambalo Yehova ataka tulichukue nasi tu wenye furaha sana kuwa nalo.”
—Kutoka 1975 Yearbook of Jehovah’s Witnesses.