Mwisho wa “Mbingu Zilizo Sasa, na Dunia”
(Funzo la Kitabu)
1, 2. (a) Katika kuonya, mtume Petro anavuta fikira kwenye wakati gani? (b) Nani aliyekuwa ametangulia kutaja jambo hilo, na limepaswa kutufahamisha nini?
MTUME Petro anaendelea kusema kwa kuonya hivi: “Lakini mbingu zilizo sasa, na dunia, zimewekwa akiba kwa moto kwa neno hili, zikilindwa hata siku ya hukumu na uharibifu wao wasioogopa Mungu. Lakini wapenzi, musisahau neno hili moja, kwamba kwa [Yehova] siku moja ni kama miaka elfu moja, na miaka elfu moja ni kama siku moja.”—2 Pet. 3:7, 8, ZSB.
2 Nabii Musa alikuwa ndiye mtu wa kwanza kuongozwa na Mungu kulinganisha miaka elfu moja ya kuwako kwa wanadamu na siku moja yenye saa 24 katika ujuzi wa Muumba wa mbingu na dunia. Ulinganifu huu wa kwanza unapatikana katika Zaburi 90:1-4, kama ilivyoandikwa na Musa, katika maneno haya akimwambia Muumba: “[Yehova], umekuwa makao yetu, kizazi baada ya kizazi. Kabla haijazaliwa milima, wala hujaiumba dunia, na tangu milele hata milele ndiwe Mungu. Wamrudisha mtu mavumbini, usemapo, Rudini, enyi wanadamu. Maana [kwa sababu ya Mungu kumrudisha mtu mwenye dhambi kwenye mavumbi ya ardhi katika mauti baada ya muda huo mfupi wa kuishi] miaka elfu machoni pako ni kama siku ya jana [yenye muda wa saa 24] ikiisha kupita, na kama kesha la usiku [la saa nne].” (Angalia maandishi ya juu ya Zaburi 90 katika Biblia ya NW) Pia Yehova Mungu alimwongoza Musa aseme juu ya vipindi vya uumbaji vyenye muda wa miaka 7,000 kama “siku.” (Mwa. 1:1-31; Kut. 20:11) Wakati unaoonekana kuwa muda mrefu sana kwa mwanadamu anayekufa ni muda mfupi sana sana kwa Mungu asiyeweza kufa.
3. Gharika ya siku za Nuhu ilifanyiza matokeo gani juu ya dunia yenyewe?
3 Mungu alipoileta gharika katika siku za Nuhu, hakuharibu dunia yetu halisi. Ilibaki isiharibiwe na Gharika ikafanyiza mabonde ya maji yote yaliyoigharikisha.
“MBINGU ZILIZO SASA, NA DUNIA”
4. (a) Hivyo je! “mbingu zilizo sasa, na dunia” ni ardhi mpya yenye anga mpya, tofauti na zile zilizokuwako kabla ya Gharika? (b) Twajuaje kwamba, wakati Mungu alipoumba wanadamu, hakuwa na nia ya kutumia yaliyoinuliwa juu ya dunia kwa makusudi yenye kuharibu?
4 Hivyo, wakati 2 Petro 3:7 inaposema juu ya “mbingu zilizo sasa, na dunia,” haingeweza kumaanisha ardhi mpya pamoja na “anga” mpya yenye hewa kuizunguka. Na ifahamike pia kwamba, katika mistari ya 5 na 6, mtume Petro hakusema kwamba “mbingu zilikuwa tangu zamani, na inchi iliyofanyizwa” ziliwekwa akiba kwa maji na zilipaswa ziwekwe akiba kwa siku ya hukumu. Mungu hakukusudia jambo kama hilo awali wakati alipozifanya mbingu halisi na dunia akaweka wanadamu juu ya dunia. Wakati huo Mungu alimpa mwanamume na mwanamke mkamilifu nafasi ya kuishi katika paradiso ya kidunia milele bila siku ya hukumu.—Mwa. 2:17-25.
5. (a) Je! “mbingu zilizo sasa, na dunia” ni za namna ile ile ya mbingu na dunia zinazotajwa katika 2 Petro 3:5? (b) Hivyo sababu gani “moto” unaotajwa katika mstari wa 7 ni wa mfano pia?
5 Kwa hiyo, “mbingu zilizo sasa, na dunia” zimewekwa akiba, si kwa maji ya gharika ya dunia yote, bali kwa moto na kuwekwa akiba kwa siku ya hukumu na ya “uharibifu wao wasioogopa Mungu.” Kwa wazi hii inamaanisha mbingu na dunia za namna tofauti na ile ya mbingu na dunia halisi za awali. Kwa hiyo, basi ule “moto” unaotajwa bila shaka ni tofauti na moto halisi, hivyo ni “moto” wa mfano, kama unavyosemekana mara nyingi katika Maandiko matakatifu.
6, 7. (a) Ni “moto” gani unaotajwa katika Sefania 3:8, 9? (b) Ni mtajo gani wa “moto” unaopatikana katika Maombolezo 2:3, 4?
6 Sefania 3:8, 9 husema juu ya “moto” huo wa mfano hivi: “Basi ningojeni, asema [Yehova], hata siku ile nitakapoondoka kuteka mateka; maana nimeazimia kuwakusanya mataifa, ili nizikutanishe falme, nipate kuwamwagia ghadhabu yangu; naam, ukali wote wa hasira yangu; kwa maana dunia yote itateketezwa kwa moto wa wivu wangu. Maana hapo ndipo nitakapowarudishia mataifa lugha iliyo safi, wapate kuliitia jina la [Yehova], wamtumikie kwa nia moja.”
7 Pia, baada ya uharibifu wa mji wa Yerusalemu kwa majeshi ya Kibabeli katika mwaka wa 607 K.W.K., nabii Yeremia alitoa ombolezo hili juu ya hatua ambayo Yehova Mungu alichukua: “Ameikata pembe yote ya Israeli katika hasira yake kali; ameurudisha nyuma mkono wake wa kuume mbele ya hao adui, naye amemteketeza Yakobo kama moto uwakao, ulao pande zote. Ameupinda upinde wake kama adui, amesimama na mkono wake wa kuume kama mtesi; naye amewaua hao wote waliopendeza macho; katika hema ya binti Sayuni amemimina kani yake kama moto.”—Omb. 2:3, 4.
8, 9. Baada ya gharika ya siku za Nuhu, ni ahadi gani yenye kutumainisha ambayo Mungu alitoa, inayokumbushwa na upinde?
8 Mara baada ya gharika ya siku za Nuhu Mungu alifanyiza upinde uonekane na kumwambia Nuhu na jamaa yake hivi: “Na agano langu nitalithibitisha nanyi; wala kila chenye mwili hakitafutwa tena kwa maji ya gharika; wala hakutakuwa tena gharika, baada ya hayo, kuiharibu nchi. Mungu akasema, Hii ndiyo ishara ya agano nifanyalo kati yangu na ninyi, na kila kiumbe hai kilichoko pamoja nanyi, kwa vizazi vyote hata milele; mimi nauweka upinde wangu winguni, nao utakuwa ni ishara ya agano kati yangu na nchi. Hata itakuwa nikitanda mawingu juu ya nchi, upinde utaonekana winguni, nami nitalikumbuka agano langu, lililoko kati yangu na ninyi, na kila kiumbe hai katika wote wenye mwili, wala maji hayatakuwa gharika tena kuwaharibu wote wenye mwili. Basi huo upinde utakuwa winguni; nami nitauangalia, nipate kulikumbuka agano la milele lililoko kati ya Mungu na kila kiumbe hai katika wote wenye mwili kilichoko katika nchi.”—Mwa. 9:11-16.
9 Katika Isaya 54:9 Yehova Mungu aliongeza uhakikisho huu: “Kama nilivyoapa ya kwamba maji ya Nuhu hayatapita juu ya dunia tena.”
“ZIMEWEKWA AKIBA KWA MOTO”
10. Ni mambo gani kadha ya hakika yanayoonyesha upumbavu wa kudhani ule moto unaotajwa katika 2 Petro 3:7 ni moto halisi?
10 Ikiwa, badala yake, Mungu angekusudia kuigharikisha dunia yote kwa moto halisi, kuwa na moto mkubwa halisi wa ulimwenguni pote, usemi huo ulioapwa juu ya kutoleta gharika nyingine ya dunia yote usingekuwa wenye faraja sana kwa wanadamu. Pia, ikiwa usemi huu “mbingu zilizo sasa, na dunia” ungetia nyota za mbinguni zinazoonekana kwa macho ya kibinadamu, moto halisi wa namna hiyo ungezifanyia nini jua, mwezi, sayari na nyota nyingine zote ambazo tayari ni matufe yenye moto mkali zaidi kushinda na mioto inayowashwa hapa duniani? Kuteketeza dunia yetu iwe makaa matupu kwa moto mkubwa wa dunia yote kusingepatana hata kidogo na kusudi la Mungu lililotangazwa la kugeuza dunia hii iwe paradiso kubwa kupitia kwa ufalme wake wa Kimasihi.
11. (a) Basi, ni nini maana ya “moto” katika andiko hilo? (b) Na ni “mbingu” gani ambazo “zimewekwa akiba kwa moto”?
11 Kwa wazi, basi, ule “moto” ambao kwa huo “mbingu zilizo sasa, na dunia zimewekwa akiba” ni moto wa mfano unaoharibu vitu vilivyolaaniwa sawasawa kama moto halisi unavyoharibu vitu vyenye kuwaka moto. Kwa sababu hiyo, usemi huu “mbingu zilizo sasa, na dunia” una maana ya mfano. Basi zile “mbingu” zafananisha taratibu za kiserikali, mamlaka zitawalazo “zilizo sasa” ambazo wanadamu wanatii. Katika Warumi 13:1 Paulo mtume wa Kikristo anaziita hizi “mamlaka iliyo kuu,” akisema: “Kila mtu na aitii mamlaka iliyo kuu; kwa maana hakuna mamlaka isiyotoka kwa Mungu; na ile iliyopo imeamriwa na Mungu.”
12. (a) Kupatana na hilo, ni “dunia” gani ambayo ‘imewekwa akiba kwa moto’? (b) Toa mfano wa Maandiko wa matumizi ya usemi huu “dunia.”
12 Kwa hiyo, “dunia” iliyo chini ya mbingu hizi yafananisha jamii ya kibinadamu iliyo chini na inayoitii “mamlaka iliyo kuu.” Wakati mmoja, kwa zaidi ya karne moja baada ya gharika ya siku za Nuhu, jamii hii ya kibinadamu ilisema lugha moja. Mwanzo 11:1, ZSB yaelekeza kwa hili, ikisema: “Na dunia nzima ilikuwa na lugha moja na usemi mumoja.”
13, 14. (a) Serikali za kisiasa zafananishwa katika Maandiko na kitu gani kinginecho cha juu? (b) Onyesha mfano wa hili kutokana na Isaya sura ya 34 na Mika sura ya 1.
13 Kwa kupatana kabisa na mtajo wa “mamlaka iliyo kuu” kama “mbingu” Biblia inafananisha serikali hizo za kisiasa na “milima.” Kama mfano, katika Isaya 34:2-5 Bwana Mungu Mwenye Enzi Kuu anasema hivi: “[Yehova] ana ghadhabu juu ya mataifa yote, na hasira kali juu ya jeshi lao lote; amewaangamiza kabisa, amewatoa waende kuchinjwa. Watu wao waliouawa watatupwa nje, na uvundo wa maiti zao utapaa juu, na milima itayeyushwa kwa damu yao. Na jeshi lote la mbinguni litafumuliwa, na mbingu zitakunjwa kama karatasi, na jeshi lao lote litanyauka kama vile jani la mzabibu linyaukavyo na kupukutika, na kama jani la mtini linyaukavyo na kupukutika. Maana upanga wangu umekunywa na kushiba mbinguni; tazama, utashukia Edomu, na juu ya watu wa laana yangu, ili kuwahukumu.” Kwa kuharibiwa kwa majeshi katika “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” inayokuja katika Har–Magedoni, serikali ambazo majeshi hayo yaliunga mkono zitayeyuka, zitafumuliwa, kama milima inayoyeyuka katika damu ya majeshi yaliyouawa.
14 Mfano mwingine wa kufumuliwa kwa milima ya mfano iliyo mirefu kama mbingu unatolewa katika Mika 1:3, 4 katika maneno haya: “Kwa maana, angalieni, [Yehova] anakuja akitoka mahali pake, naye atashuka, na kupakanyaga mahali pa dunia palipoinuka. Na hiyo milima itayeyuka chini yake, nayo mabonde yatapasuliwa, kama vile nta iliyo mbele ya moto, kama maji yaliyomwagika tena kutelemka gengeni.” Upesi, wakati Yehova Mungu Mwenye Nguvu Zote, kwa njia ya majeshi yake ya kimbinguni yenye kuua, atakapokutana na milima ya kiserikali ya taratibu hii ya mambo, itakuwa kama kuitia katika joto lenye moto mkali wenye kung’aa. Hali yao ya ugumu itayeyuka!
15. Hivyo ni nini litakalozipata “mbingu zilizo sasa, na dunia” na “wasioogopa Mungu” wakati ujao, na kwa sababu gani?
15 Hivyo ile “siku ya hukumu na uharibifu wao wasioogopa Mungu” ambayo kwa hiyo “mbingu zilizo sasa, na dunia, zimewekwa akiba,” kwa jinsi ya mfano, itakuwa yenye moto kwa uharibifu wote ambao itafanyiza. Itakuwa ndiyo siku ya kufikiliza hukumu za kimungu juu ya taratibu nzima ya mambo inayoonekana. Pia, itakuwa siku ya “uharibifu wao wasioogopa Mungu,” kwa vile hawamwoni na kumtendea Yehova Mungu kama Mtukufu, Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Wote. Si wenye kuonyesha heshima kwa Yeye, Mtakatifu.
SI MUNGU WA POLEPOLE
16, 17. Ijapo kuja kwa “siku ya hukumu” ya Yehova huenda kukaonekana kukawia kwa maoni ya wenye kudhihaki, ni uhakika gani juu ya wakati unaopaswa kufikiriwa?
16 Ni “kwa neno hili,” yaani, “neno la Mungu,” kwamba “mbingu zilizo sasa, na dunia” pasipo kubadilika “zimewekwa akiba kwa moto . . . zikilindwa hata siku ya hukumu na uharibifu wao wasioogopa Mungu.” Hili ni jambo ambalo inawapasa wafikirie wale wenye dhihaka wa leo, wanaokuona “kuwapo” kwa Bwana na Mwokozi Yesu Kristo kuwa bado kutukia. “Neno hili” la Mungu, lililotangaza kwa mamlaka kusudi la kuruhusiwa kwa “mbingu zilizo sasa, na dunia” kuwako kwa muda mrefu sana, litatimizwa pasipo kushindwa. Sasa hautakuwa muda mrefu! Huenda kwa wenye dhihaka na “wasioogopa Mungu” kuja kwa “siku” hiyo kumeonekana kuwa muda mrefu, lakini kwa Mungu asiye na mwanzo na bila mwisho, ambaye ni wa milele, umekuwa si muda mrefu. Ndiyo sababu mtume Petro sasa asema hivi:
17 “Lakini wapenzi, musisahau neno hili moja, kwamba kwa [Yehova] siku moja ni kama miaka elfu moja, na miaka elfu moja ni kama siku moja. [Yehova] hakawii kutimiza ahadi yake, kama wengine wanavyozania kukawia; lakini ni muvumilivu kwenu asiyetaka mutu mumoja kupotea, lakini wote wafike kutubu. Lakini siku ya [Yehova] itakuja kama mwizi.”—2 Pet. 3:8-10, ZSB.
18. (a) Je! muda unaoonekana kama mrefu sana ambao Mungu ameruhusu umekuwa bila huruma kwa wanadamu? (b) ‘Siku moja kwa Yehova ni kama miaka elfu’ kwa wanadamu namna gani?
18 Unaoonekana kuwa muda mrefu kwa wanadamu ni muda mfupi sana kwa Mungu. Hivyo, yeye aweza kuruhusu wanadamu unaoonekana kuwa muda mrefu kwa faida yao. “Miaka elfu moja” ni nini kwake Yeye, inapokuwa kama siku tu yenye saa 24 ikilinganishwa na umilele wake wa kuwako? Kwa upande mwingine, siku moja yenye saa 24 kwa Mungu ni kama miaka elfu moja kwa wanadamu, wakati wanadamu wanapoona kwamba jambo ambalo ingewachukua miaka elfu kutimiza lingeweza kutimizwa na Yehova Mungu Mwenye Nguvu Zote katika “siku moja.” Kwa maelfu ya miaka wanadamu wasioridhika wamekuwa wakijaribu kuitengeneza taratibu hii ya mambo au wakijaribu kuigeuza iwe bora, lakini mpaka sasa wamekuwa hawawezi kufanya hivyo. Walakini, Yehova atafanya hivyo katika “siku” yake, katika muda mfupi ambao katika huo atafikiliza hukumu zake juu ya taratibu hii ya mambo kana kwamba kwa moto na atawaharibu wote wale wanaoisaidia na kuiunga mkono. Kwa kweli hili ni jambo ambalo inawapasa wenye kudhihaki wafikilie.
19. Badala ya kuwa wasiosubiri kwa sababu ya namna Mungu anavyoshughulika na mambo, inawapasa wanadamu wafikirie kwa uzito maulizo gani?
19 Inaonyesha kukosa ufahamu wa namna Mungu anavyoshughulika na mambo, wakati bila subira mtu anaposema hivi: ‘Sababu gani Mungu hakufanya lo lote juu ya hali mbaya ya ulimwengu kabla ya sasa? Yampasa afanye haraka afanye jambo fulani kwa faraja ya wanadamu, ili niweze kufaidika nalo—upesi!’ Ulizo kubwa ambalo imempasa mtu huyo mwenye kukosa subira ajiulize ni: ‘Je! mpaka sasa mimi sijafikia kumtubia Mungu?’ Au: ‘Je! mimi nautumia wakati vizuri nisaidie wengine wengi kama inavyowezekana wafikie kutubu?’
20. (a) Kushughulika kwa Mungu na wanadamu kumeonyeshaje kweli “uvumilivu” wake usiolinganika, na kwa kusudi gani? (b) Wakati wa kipindi hiki cha wakati, Mungu amefanya nini kwa kusudi la wokovu wa wengi kadiri iwezekanavyo?
20 Ni nani anayeweza kumshtaki Mungu kwa kufaa kwamba anakawiza ahadi yake ya kuondolea dunia hii uovu na kusimamisha serikali ya haki yenye kudumu, wakati miaka elfu moja ya muda wa wanadamu ni kama siku moja tu yenye saa 24 kwa Mungu wa Milele? Yeye ameweka siku yake ya kuchukua hatua, na siku hiyo iliyowekwa imeruhusu idadi isiyo na hesabu ya wanadamu wakati wa kutosha wafikie kutubu. Badala yao kuona kama Mungu ‘anakawia,’ imewapasa waone kwamba kuwekwa kwa “siku” yake mpaka sasa tangu mwanzo wa “mbingu zilizo sasa, na dunia” achukue hatua wakati ujao ni ‘uvumilivu’ usiolinganika kwa upande wake. Kumekuwako uvumilivu huu wa kimungu kwa sababu Yeye hataki ye yote apotee, aharibiwe. Hivyo, wakati wa maelfu hayo ya miaka ambayo ameruhusu mpaka ifike “siku” yake isiyobadilika iliyowekwa, alimtuma Mwana wake mpendwa kutoka mbinguni aje atende kama Mwalimu Mkuu duniani na kufa kama dhabihu ya ukombozi kwa wanadamu wote, ili uweko wokovu wa wengine kadiri iwezekanavyo. (Gal. 4:4) Tangu kuja huko kwa kwanza kwa Mwana wake mpendwa mwaminifu duniani, toba ya kusamehewa dhambi imehubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu. Toba hiyo imehubiriwa kwa zaidi ya karne kumi na tisa.
21. Ijapo wenye kudhihaki hawathamini, Mungu ameshughulikaje hata na wao?
21 Wale wenye kudhihaki leo hawafaidiki na wakati wa uvumilivu wa Mungu ili wafikie kutubu wasije wakaharibiwa. Ijapokuwa hawathamini, Mungu amewatendea fadhili sana akitazamia watubu. Kama mtume Paulo alivyoandika, katika barua yake iliyoongozwa na Mungu kwa kundi la Kirumi lililokuwa na washiriki Wayahudi wa Kikristo na Mataifa: “Unazarau utajiri wa wema wake na saburi na uvumilivu wake, usijue ya kama wema wa Mungu unakupeleka kwa toba”?—Rum. 2:4, ZSB.
22, 23. (a) Hata tangu mwaka wa 1914, uvumilivu wa Mungu umekuwaje si wa bure? (b) Kujizuia na uvumilivu wa Mungu wafananishwaje katika Ufunuo 7:1-3?
22 Ule uvumilivu ambao Mungu ametumia wakati huu wa “kuwapo” kwa Bwana na Mwokozi Yesu Kristo katika mamlaka ya Ufalme tangu mwaka wa 1914 W.K. haukuwa wa bure. Umeruhusu nafasi na kutokeza kukusanywa kwa mabaki ya mwisho ya Waisraeli wa kiroho na pia kukusanywa kwa washiriki wasio na hesabu wa “mkutano mkubwa,” ambao ni wenzi waaminifu wa mabaki waliotiwa mafuta. Kujizuia na uvumilivu wa Mungu kwa ajili ya wale wanaoweza kuongozwa watubu kunafananishwa katika Ufunuo, sura ya saba. Kwa habari ya upepo wa uharibifu unaokuja ulimwenguni pote, mtume Yohana anaandika hivi:
23 “Baada ya hayo nikaona malaika wanne wamesimama katika pembe nne za nchi, wakizizuia pepo nne za nchi, upepo usivume juu ya nchi, wala juu ya bahari, wala juu ya mti wo wote. Nikaona malaika mwingine, akipanda kutoka maawio ya jua, mwenye muhuri ya Mungu aliye hai; akawapigia kelele kwa sauti kuu wale malaika wanne waliopewa kuidhuru nchi na bahari, akisema, Msiidhuru nchi, wala bahari, wala miti, hata tutakapokwisha kuwatia muhuri watumwa wa Mungu wetu juu ya vipaji vya nyuso zao.” (Ufu. 7:1-3) Huku kulipatana na uvumilivu wa Mungu.
24. (a) Ni jambo gani limetokana na wonyesho huu uvumilivu wa Mungu?(b) Ni hatua gani inayochukuliwa na wale wanaothamini sasa uvumilivu wa Mungu, na ni taraja gani la ajabu limewekwa mbele yao?
24 Ilikuwa faida gani ya wonyesho huu wa uvumilivu wa Mungu? Mabaki ya Waisraeli wa kiroho waliohitajiwa walitiwa muhuri juu ya vipaji vya nyuso zao, ili mwishowe waweko Waisraeli wa kiroho 144,000 waliotiwa muhuri kama ilivyoamriwa mbele na Yehova Mungu. (Ufu. 7:4-8) Walakini, zaidi ya Waisraeli wa kiroho wanaotazamiwa kutawala pamoja na Kristo katika Mlima Sayuni wa kimbinguni wamefaidika na uvumilivu wa Mungu katika huu “wakati wa mwisho.” Watu wenye tumaini lenye Maandiko la uzima wa milele katika paradiso ya kidunia wamefaidika. Tangu mwaka wenye maana wa 1935 W.K., wametoka katika mataifa yote na kabila na jamaa na lugha na wamejiweka wakf kwa Yehova kama Mungu wao. Hivyo wamebatizwa katika mfano wa wakf huu kama Yesu Kristo alivyoamuru ifanywe na wale wanaokuwa wanafunzi wake. Taraja la ajabu la kupita na kuokoka “dhiki ile iliyo kuu” yenye upepo inayomalizia huu “wakati wa mwisho” limewekwa mbele ya “mkutano mkubwa” huu usio na kipimo unaotokea sasa. Mfano wa unabii, katika Ufunuo 7:9-17, wa huu “mkutano mkubwa” kama umetoka salama katika “dhiki ile iliyo kuu” wasonga mbele sasa kuelekea utimizo wenye utukufu!—Kutoka Kitabu Man’s Salvation Out of World Distress at Hand’, sura ya 16.