Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w80 3/15 kur. 20-24
  • “Mkutano Mkubwa” Waliitia Jina Lile

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Mkutano Mkubwa” Waliitia Jina Lile
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Vichwa vidogo
  • UFUFUO WA MFANO
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
w80 3/15 kur. 20-24

“Mkutano Mkubwa” Waliitia Jina Lile

(Funzo la Kitabu)

1. Wakati wa Vita ya Pili ya Ulimwengu, wakati ambayo mnyama apandaye kutoka kuzimu alipopiga vita juu ya mabaki ya watiwa mafuta, sababu gani hawakupatwa na yale yaliyowapata katika wakati wa Vita ya Kwanza ya Ulimwengu?

KATIKA miaka ya 1939-1945 vita ya pili ya ulimwengu iliwaangamiza sana wanadamu. Walakini je! yaliyowapata mabaki ya Waisraeli wa kiroho waliotiwa nguvu mpya, ambao tangu mwaka 1931, walipata kujulikana kama Mashahidi wa Yehova yaliwapata tena? Yajapokuwako mateso ya kidini yaliyo makali zaidi wakati wa Vita ya Pili ya Ulimwengu, wakati ambapo ‘yule mnyama apandaye kutoka kuzimu’ alipopiga vita juu ya mabaki, maandishi yanajibu Hapana! Mateso yenye jeuri hayakufaulu kuua kazi ya kushuhudia Ufalme iliyokuwa ikiendeshwa na mabaki ya watiwa mafuta. Waliendelea ‘kujazwa roho’ kutoka kwa Mpaji-Uzima wao wa kimbinguni. (Efe. 5:18) Waliendelea kushikilia uzima wa kiroho kwa kuwa watendaji katika kazi ya kushuhudia Ufalme, hata kichini-chini, ilipokuwa lazima. Walipokatazwa na serikali za kisiasa na za kijeshi wasihubiri habari njema za ufalme wa Yehova uliosimamishwa, walimwomba awape ujasiri waendelee kwa uaminifu kutimiza agizo lao la kuhubiri.

2. Matokeo juu ya hayo yaliyotajwa hapo juu yalikuwaje kwa mabaki kama vile ilivyokuwa katika habari inayoripotiwa katika Matendo 4:31?

2 Matokeo kwao yalikuwa kama yale ya kundi la Yerusalemu, baada ya mitume kuagizwa na mamlaka ya kidini waache kuhubiri Kristo. “Wote wakajaa [roho takatifu], wakanena neno la Mungu kwa ujasiri.” Vivyo hivyo, mpaka sasa, mabaki wanaonyesha kwamba wanajawa na roho takatifu nao wanaendelea kwa nguvu nyingi ‘kunena neno la Mungu kwa ujasiri.’ Kwa sababu hiyo, “kinara cha taa” cha mabaki hakijaondolewa mahali pake.

3. (a) Mabaki ya watiwa mafuta wanafanya nini juu ya jina la Mungu? (b) Kulingana na yanayosemwa katika Ufunuo 6:14-17, kwa nini kuna sababu ya watu kuuliza kama mabaki ndio peke yao ‘watakaoponywa’ katika siku ya Yehova?

3 Mabaki ya watiwa mafuta wenyewe ‘wanaliitia jina la Yehova’ na kulitangaza ulimwenguni pote. Hata hivyo, je! wao peke yao ndio wanaotumainia ‘kuponywa’ wakati wa “siku ya [Yehova] iliyo kuu na itishayo” inayokaribia? (Yoeli 2:31, 32) Hili ni ulizo ambalo wengi ambao si sehemu ya mabaki wangependa kuona likijibiwa, kwa kuwa kwa habari ya hiyo “siku . . . itishayo,” Ufunuo 6:14-17 wasema hivi:

“Mbingu [serikali za kisiasa zilizo juu ya wanadamu] zikaondolewa kama ukurasa ulivyokunjwa, na kila mlima na kisiwa kikahamishwa kutoka mahali pake. Na wafalme wa dunia, na wakuu, na majemadari, na matajiri, na wenye nguvu, na kila mtumwa, na mwungwana, wakajificha katika pango na chini ya miamba ya milima, wakiiambia, Tuangukieni, tusitirini, mbele za uso wake yeye aketiye juu ya kiti cha enzi, na hasira ya Mwana-Kondoo. Kwa maana siku iliyo kuu, ya hasira yao, imekuja; naye ni nani awezaye kusimama?”

4. (a) Ni nini jibu la ulizo la hao wanaotajwa hapo juu kuhusu kama wataokoka katika siku ya Yehova? (b) Ni nani wasiojiunga na wafalme wa dunia na wasaidizi wao katika kuuitia ulinzi wa kidunia?

4 Jibu la ulizo la wote hao wanaotajwa hapo juu walioshindwa kuliitia jina la Yehova waokolewe ni, hapana hata mmoja wao atakayesimama akiwa amekubalika na kuhifadhiwa hai katika hiyo “siku iliyo kuu” Yake. Upepo wa mfano utakaowaharibu unatajwa katika sura ifuatayo ya kitabu hiki, katika Ufunuo 7:1-3. Baada ya mtajo huo, tunapashwa habari za watumwa wa Mungu 144,000 waliotiwa muhuri katika vipaji vya nyuso zao kwa “muhuri ya Mungu aliye hai.” Hawa waitwa Waisraeli, si Waisraeli wa mwili wa asili kama wale waliokubali kuuawa kwa Mwana-Kondoo wa Mungu, bali ni Waisraeli wa kiroho wanaomfuata Mwana-Kondoo Yesu aliye Masihi. (Ufu. 7:4-8; 14:1-5) Baada tu ya kuona mambo haya, ni jambo gani linalofunuliwa kwetu? Ni watu wasiojulikana hesabu yao ambao hawajiungi na wafalme wa dunia na wasaidizi wao katika kuiitia milima ya kiserikali pamoja na miamba iwafiche na kuwasitiri kutokana na hasira ya Mungu na Mwana-Kondoo wake. Wao hawaiogopi hasira ya kimungu.

5. Huu “mkutano mkubwa” unawahesabia nani wokovu, kukiwa na faida gani kwao?

5 Tusomapo Ufunuo 7:9-17, ebu na tuangalie kwamba “mkutano” huu usiohesabika wasemekana kwamba ndio “wanatoka katika dhiki ile iliyo kuu”:

“Tazama, mkutano mkubwa sana ambao hapana mtu awezaye kuuhesabu, watu wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha, wamesimama mbele ya kile kiti cha enzi, na mbele za Mwana-Kondoo, wamevikwa mavazi meupe, wana matawi ya mitende mikononi mwao; wakilia kwa sauti kuu wakisema, Wokovu una Mungu wetu aketiye katika kiti cha enzi, na Mwana-Kondoo.

“. . . Je! watu hawa waliovikwa mavazi meupe ni akina nani? nao wametoka wapi? . . . Hao ndio wanatoka katika dhiki ile iliyo kuu, nao wamefua mavazi yao, na kuyafanya meupe katika damu ya Mwana-Kondoo. Kwa hiyo wako mbele ya kiti cha enzi cha Mungu, nao wanamtumikia mchana na usiku katika hekalu lake, na yeye aketiye katika kiti cha enzi atatanda hema yake juu yao. Hawataona njaa tena, wala hawataona kiu tena, wala jua halitawapiga, wala hari iliyo yote. Kwa maana huyo Mwana-Kondoo, aliye katikati ya kiti cha enzi, atawachunga, naye atawaongoza kwenye chemchemi za maji yenye uhai, na Mungu atayafuta machozi yote katika macho yao.”

6. Ni mambo gani yanayotofautisha huu “mkutano mkubwa” na Waisraeli wa kiroho 144,000 waliotangulia kutajwa, na sababu gani wanastahili kumtumikia Mungu katika hekalu lake la kiroho?

6 “Mkutano mkubwa” huo usio na hesabu si sehemu ya hao 144,000 walio na hesabu kamili wa Israeli wa kiroho. Wao hawakutiwa muhuri juu ya vipaji vya nyuso zao kwa “muhuri ya Mungu aliye hai.” Hawakuonwa katika njozi wakisimama katika Mlima Sayuni wa mbinguni wakiwa pamoja na Mwana-Kondoo wa Mungu. Haisemwi juu yao kwamba “wamenunuliwa katika wanadamu, malimbuko kwa Mungu na kwa Mwana-Kondoo.” Kwa habari ya taifa, wakilinganishwa na Waisraeli wa kiroho 144,000, wao ni watu wa Mataifa yasiyo ya Kiyahudi kwa vile walivyo watu wa mataifa yote. Hata hivyo wamepata kumjua Yehova Mungu na kutambua kwamba anaketi katika kiti cha enzi cha ulimwengu wote, akiwa Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote. Wao wanamjua Mwana-Kondoo wa Mungu aliyechinjwa na kumkiri, kwa kuwa wanaonyesha imani katika uwezo wa damu yake yenye kutakasa na kusafisha ili wapate msimamo safi mbele ya Mungu aketiye katika kiti chake cha enzi. Wakiwa wamesafishwa hivyo, wamtolea utumishi mtakatifu mchana na usiku katika nyua za kidunia za hekalu lake la kiroho.

7. “Mkutano mkubwa” wanaonyeshwa kuwa washiriki wa “kondoo” wapi, nao wana tumaini gani la uzima wakati ujao?

7 Namna gani juu ya tumaini lililo lao wote? Si tumaini la kimbinguni. Ufunuo 7:17 wawafananisha na kondoo, ambao Mwana-Kondoo ndiye Mchungaji wao. “Chemchemi za maji yenye uhai” ambazo kwazo awaongoza ni “chemchemi” zinazobubujika na kutoa mipango ya kimungu ya kutoa uzima mkamilifu wa kibinadamu katika paradiso ya kidunia iliyoahidiwa. Wao ni sehemu ya “kondoo” wa mfano ambao kwa ajili yao Mchungaji Mwema alitoa uhai wake wa kibinadamu. Baada ya kuzungumza juu ya “zizi” ambalo Yohana Mbatizaji akiwa “bawabu” alifungua mlango wake katika mwaka 29 W.K., Yesu aliendelea kusema hivi: “Na kondoo wengine ninao, ambao si wa zizi hili; na hao nao imenipasa kuwaleta; na sauti yangu wataisikia; kisha kutakuwako kundi moja na mchungaji mmoja.” (Yohana 10:3, 16) Kwa hiyo, huo “mkutano mkubwa” wa Ufunuo 7:9-17 ni washiriki wa “kondoo wengine” walio hai leo na ambao wamejitoa kumfuata Yesu Kristo, Mchungaji Mwema.

8. “Mkutano mkubwa” wanakuwa “kundi moja” na akina nani chini ya “mchungaji mmoja”?

8 Basi, huu “mkutano mkubwa” ulipata kuwa “kundi moja” na akina nani chini ya “mchungaji mmoja”? Na “kondoo” wa lile “zizi” jingine, yaani mabaki ya lile “kundi dogo” la Waisraeli wa roho. (Luka 12:32; 1 Pet. 2:25) Ijapokuwa huo “mkutano mkubwa” haumo katika lile agano jipya ambalo Yesu Kristo alipatanisha kwa ajili ya Israeli wa kiroho yeye huwaunganisha pamoja na hao mabaki ya watiwa mafuta kama kwamba wao ni “kundi moja” katika zizi moja. Mchungaji Mwema amekuwa akifanya hivyo tangu wakati gani na kuendelea?

9, 10. (a) Kuanza kukusanywa kwa “mkutano mkubwa” kulionyeshwa kwa tukio gani? (b) Ni taraja gani lililowekwa mbele yao, kwa furaha yao?

9 Tangu mwaka 1935 na kuendelea, Mwishoni mwa Mei wa mwaka huo kusanyiko la siku tano la Mashahidi Wakristo wa Yehova lilikuwa likiendelea huko Washington, Wilaya ya Columbia, U.S.A. Kulikuwako watu waliokuwa wamealikwa kipekee katika kusanyiko hili waliokuwa wakishirikiana na mabaki ya watiwa mafuta na ambao hata hivyo walipendezwa na kuokoka “dhiki ile iliyo kuu” na kuingia, pasipo kufa, katika taratibu mpya ya Mungu pamoja na paradiso yake ya kidunia. Wao hawakuwa na matarajio ya kimbinguni. Uzima wa milele katika dunia ya paradiso ungetosheleza kabisa tamaa ya mioyo yao.

10 Hivyo, basi, furaha yao ilikuwa kuu katika kusanyiko hilo la Washington msimamizi wa Sosaiti alipozungumza habari ya “mkutano mkubwa,” unaotajwa katika Ufunuo 7:9-17. Alieleza waziwazi kwamba “mkutano” huo haukuwa jamii ya kiroho au ya waliozaliwa kwa roho; haingekuwa na hali ya kimalaika huko mbinguni ili ipate kusaidia warithi wa shirika pamoja na Kristo 144,000. Ilikuwa hasa jamii ya kidunia ikiwa na tumaini la uzima wa milele wa kibinadamu katika paradiso ya kidunia chini ya ufalme wa Kristo. Sasa kwa njia ya Yesu Kristo Mchungaji Mwema, Yehova Mungu alikuwa ameanza kukusanya huu “mkutano” katika utumishi wenye utendaji pamoja na mabaki ya watiwa mafuta.

11. “Roho” ya huo “mkutano mkubwa” ililiitikiaje tumaini lililowekwa mbele yao, na tangu wakati huo ni tumaini gani limewekwa mbele ya wote wanaomtafuta Mungu?

11 Mioyo ya watu mia nyingi waliokuwapo katika kusanyiko hilo la Washington haikuwa imepata kusisimuliwa na taraja la kuwa warithi wa shirika pamoja na Kristo. Walakini sasa tumaini la kidunia linalopatikana katika Ufunuo 7:9-17 lilipoelezwa waziwazi, “roho” yao, nguvu yenye kutendesha iliyokuwamo mioyoni mwao, iliwasukuma waitikie kwa moyo wote. Walilikubali tumaini hilo kwa kishindo kikubwa cha kushangilia. Baadaye wakati elfu nyingine nyingi waliposoma katika safu za gazeti la Mnara wa Mlinzi mazungumzo ya “mkutano mkubwa” yaliyorudiwa kuandikwa humo, “roho” yao, vilevile, ikaitikia. Tangu wakati huo, tumaini la “mkutano mkubwa” limewekwa mbele ya wote wenye kumtafuta Mungu duniani mwote. Mia elfu nyingi wamepata kubatizwa katika jina la Mwana wa Mungu nao wamewekwa katika mstari wa kutimiziwa tumaini hilo zuri sana.

12. Ni kwa sababu ya tofauti gani zilizo kati yao na mabaki ya watiwa mafuta ulizo latokezwa kama “kondoo wengine” walio wakf na kubatizwa wana roho takatifu ndani yao?

12 Bila shaka “kondoo wengine” hao walio wakf na kubatizwa wa “mkutano mkubwa,” hawakuzaliwa kwa roho wapate kuwa wana wa kiroho wa Mungu, wakiwa na urithi wa kimbinguni. Wao si Waisraeli wa kiroho. Hawakuingizwa katika agano jipya wakiwa na nafasi ya kuwa “ufalme wa makuhani, taifa takatifu” la Mungu. (Kut. 19:5, 6) Hawajapata kamwe kutiwa muhuri kwa roho ya Mungu na kuwa na taraja la kuwa warithi wa shirika pamoja na Kristo katika Ufalme wake wa kimbinguni. (Isa. 61:1-3; 1 Yohana 2:20, 27; 2 Kor. 1:21, 22) Walakini hata hivyo je! wanayo roho takatifu?

13. Kuna ushuhuda gani wa Maandiko kuonyesha kama mtu ambaye amejitoa kwa Mungu duniani lazima azaliwe kwa roho ya Mungu ili roho takatifu itende kazi juu yake?

13 Mambo ya hakika yanajibu kwa nguvu sana Ndiyo! Sana sana tangu mwaka 1935 W.K., “mkutano mkubwa” wamefanya kazi pamoja na mabaki ya watiwa mafuta waliozaliwa kwa roho. Wametoa ushuhuda wenye kusadikisha kwamba roho takatifu ya Mungu inatenda juu yao. Si lazima mtu duniani azaliwe kwa roho ya Mungu ili nguvu ya utendaji Yake ianze kutenda juu yake. Ebu mtazame nabii Musa, Mwamuzi Othnieli, Mwamuzi Gideoni, Mwamuzi Samsoni, Mfalme Daudi, Yohana Mbatizaji. Ndiyo, ebu watazame manabii wote wa kabla ya Ukristo ambao juu yao roho ya Yehova ilitenda kuwaongoza waandike vitabu vya Biblia kutoka Mwanzo mpaka Malaki. Ni wazi kwamba hakuna tumaini la kimbinguni lililowekwa mbele ya watu hao wa kale, hata hivyo Yehova Mungu aliweka roho yake juu yao kwa kuwa walijitoa kwake kwa upendo kwa ajili ya utumishi wake. Mungu aliwafunika kwa nguvu yake ya utendaji. Aliwajaza roho takatifu. Ilitenda juu yao.

14. Kwa sababu ya hesabu ndogo ya wale walio washiriki wa mabaki ya watiwa matuta leo, Mungu amehakikishaje kwamba kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi imefanywa ulimwenguni pote?

14 Leo, mabaki ya Waisraeli wa kiroho waliotiwa mafuta kwa roho takatifu ni wangapi? Kulingana na hesabu ya wale wanaoshiriki mifano ya mkate na divai wakati wa sherehe ya kila mwaka ya Chakula cha Bwana cha Jioni, hesabu yao sasa ni kama 10,000. Lakini wale Wakristo waliobatizwa ambao roho yao inaitikia kwa kuthamini lile tumaini la uzima wa milele katika paradiso hapa duniani ni zaidi ya milioni mbili. Hivyo, basi, ni nani wanaofanya sehemu iliyo kubwa zaidi ya kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi ulimwenguni pote? (Mt. 24:14; 28:19, 20) Mabaki ya watiwa mafuta wanaoendelea kuzeeka, wakiwa hesabu ndogo namna hiyo, hawangeweza kufanya sehemu iliyo kubwa ya kazi hiyo. Hivyo, roho ya Mungu ikitenda kazi kwa nguvu sana juu ya “mkutano mkubwa” wa “kondoo wengine,” imewawezesha wakiwa pamoja na mabaki ya watiwa mafuta wafanye kazi ya kutoa ushuhuda ulimwenguni pote isiyo na kifani katika historia ya Ukristo.

15, 16. (a) Kwa sababu ya kutimizwa kwa utangazaji wa ufalme wa Kimasihi ulimwenguni pote, wale wanaoshiriki kazi hiyo wanampa nani sifa? (b) Ni kwa sababu ya maandiko gani wanaamini kwamba wamekuwa wakiongozwa na malaika?

15 Kutangazwa kwa Injili ya Ufalme kunasikika sasa katika nchi na visiwa vya bahari 205 kuzunguka dunia yote. Makundi zaidi ya 42,000 ya watangazaji watendaji wa Ufalme yanasitawi katika paradiso ya kiroho duniani pote.a

16 Kutangazwa huku kwa ufalme wa Mungu kwa ajili ya taratibu yake mpya kwenye kufika mbali sana, hata kufikia sehemu za mbali zaidi za dunia, kuliwahitaji wale wenye kufanya utangazaji huo wafanye kazi nyingi ngumu na yote hiyo wakiifanya bila malipo. (Mt. 10:8) Walakini watangazaji hawa wa Ufalme, Mashahidi Wakristo wa Yehova, hawajitwalii sifa kwa kuitimiza kazi hii kubwa sana. Wao wanakubali kwamba wao ni vyombo tu vinavyotumiwa na Mungu. Wanakubali kwamba ujasiri na nguvu ya kufanya kazi hii iliyokusudiwa wamepewa na roho ya Mungu. Wanajua vilevile kwamba wamekuwa wakisaidiwa na kuongozwa na malaika wanapofanya kazi hii inayokubaliwa na Mungu. Wanaamini Waebrania 1:14 linavyosema juu ya malaika wa kimbinguni wakiwa “roho watumikiao, wakitumwa kuwahudumu wale watakaourithi wokovu.” Vilevile, kuhusiana na wakati wetu, “mwisho wa taratibu ya mambo,” Yesu alisema hivi: “Atawatuma malaika zake pamoja na sauti kuu ya parapanda, nao watawakusanya wateule wake toka pepo nne, toka mwisho huu wa mbingu mpaka mwisho huu.”​—Mt. 24:3, 30, 31, NW.

17. (a) Ni kwa sababu gani kutumiwa huku kwa malaika si jambo lisilo la kawaida? (b) Kwa ajili ya kazi kutenganishwa kwa Wakristo wa kuiga na wale wa kweli, na kukusanywa kwa ule “mkutano mkubwa” wa kondoo wengine ni msaada wa nani usioonekana uliotabiriwa?

17 Je! hilo ni jambo lisilo la kawaida? Hapana! Kwani, hata katika nyakati za kale, za kabla ya Ukristo, malaika wa kimbinguni waliwasaidia na kuwaongoza waabudu waaminifu wa Yehova Mungu. (Mwa. 32:1, 2, 24-30; Kut. 14:19, 20; 2 Fal. 6:15-17; Isa. 37:36; Zab. 34:7) Leo ni wakati wa kukusanya pamoja wale warithi wa kweli wa ufalme wa Mungu na wa kuwatenga hawa na Wakristo wa kuiga wa Jumuiya ya Wakristo, na kwa hiyo kwa ajili ya wakati huu wa hatari mabaki ya watiwa mafuta walipaswa kusaidiwa na malaika, kulingana na Mathayo 13:39-43, 49, 50, na Ufunuo 14:6. Kwa hiyo, malaika wakiwa chini ya Kristo, Mfalme, wanashiriki sehemu ya kuongoza pasipo kuonekana katika kazi ya kukusanya mabaki ya wanafunzi watiwa mafuta, “wateule wake.” Malaika wakiwa chini ya amri yake anawatumia vilevile katika kukusanya mkutano ulio mkubwa zaidi ya mabaki ya watiwa mafuta, yaani, ule “mkutano mkubwa” wa “kondoo wengine” wake.​—Mt. 25:31-46; Yohana 10:16.

UFUFUO WA MFANO

18, 19. (a) Ni kwa sababu gani hakuna sababu ya kudharau siku ya mambo madogo kwa sababu ya mwujiza wa ajabu wa Mungu kama vile ulivyofananishwa katika Ezekieli 37:1-14? (b) Kwa ajili ya kukalishwa tena katika nchi yao kwa Waisraeli wahamishwa, Yehova angetia nini ndani yao?

18 Hivyo, basi, kuna sababu yo yote ya ‘kudharau siku ya mambo madogo’? (Zak. 4:10) Lo! namna ulivyo mfululizo wenye kushangaza wa mambo yaliyotimizwa ulioanza kufanywa huko nyuma, katika mwaka 1919 W.K., wakati ambapo “roho ya uhai itokayo kwa Mungu [ilipowaingia],” yaani, ilipowaingia mabaki ya watiwa mafuta walioonekana kana kwamba walikuwa wamekufa! (Ufu. 11:11) Ulikuwa mwujiza wa kisasa kwa upande wa Mungu Mwenye Nguvu Zote. Unalingana na maono ya nabii Ezekieli, wakati alipoona njozi ya bonde lililojaa mifupa iliyokauka na isiyokuwa na mwili ya Waisraeli waliokuwa wamekufa, Miili ya Waisraeli hao ilipata kurudishwa, walakini miili hiyo bado ililala ikiwa imekufa. Kisha, kwa kutii amri ya Mungu, Ezekieli alitabiri juu yake. Ikawaje? “Pumzi ikawaingia, wakaishi, wakasimama kwa miguu yao, jeshi kubwa mno.”​—Eze. 37:1-10.

19 Je! njozi ya Ezekieli ingetimizwa juu ya watu wateule wa Mungu waliokuwa wakati huo wakisinzia huko Babeli? Ili kuwahakikishia kwamba njozi hii ya kurudishwa ingetimizwa, Yehova alimwogoza Ezekieli aseme hivi: “Nitatia roho yangu ndani yenu, nanyi mtaishi, nami nitawawekeni katika nchi yenu, nanyi mtajua ya kuwa mimi, [Yehova] nimesema hayo, na kuyatimiza, asema [Yehova].”​—Eze. 37:11-14; linganisha Isaya 32:15-18.

20. (a) Alipowarudisha mabaki wake watiwa mafuta, alitia roho yake juu yao kwa kusudi gani? (b) Matokeo ya kuhuishwa huku yamepatanaje na Warumi 8:11?

20 Katika karne yetu ya 20, baada ya kumalizika Vita ya Kwanza ya Ulimwengu katika mwaka 1918, mabaki ya watiwa mafuta yalitiwa nguvu upya kiroho wakatoka katika utumwa wa Babeli Mkuu, milki ya ulimwengu ya dini ya uongo, ili waurudie utumishi wao wa Ufalme. Kwa hiyo, Yehova aliwarudisha katika hali yao ifaayo duniani, katika uhusiano wenye kibali pamoja naye. Alitia roho yake ndani yao, watende kwa uhuru, waseme waziwazi, katika utumishi wa Ufalme. ‘Ilipo roho ya Yehova, pana uhuru.’ (2 Kor. 3:17) Tangu wakati huo, juhudi ya namna gani waliyoionyesha mabaki waliowekwa huru katika utumishi wake wa ushikamanifu, na vilevile, baadaye, ule “mkutano mkubwa” wa wafanya kazi wenzao wenye mfano wa kondoo! Nguvu takatifu ya utendaji ya Yehova ndiyo iliyowezesha hili, kama vile Warumi 8:11, NW, linavyotukumbusha, likisema: “Ikiwa, sasa, roho yake yeye ambaye alimwinua Yesu kutoka kwa wafu yakaa ndani yenu, yeye ambaye alimwinua Kristo Yesu kutoka kwa wafu atafanya vilevile miili yenu yenye kufa iishi kupitia kwa roho ambayo yakaa ndani yenu.”

21. Ni nguvu gani iko pamoja na mabaki na “mkutano mkubwa” walio na umoja?

21 Basi, kwa umoja, songeni mbele, enyi mabaki na ninyi “mkutano mkubwa”! Nguvu isiyoonekana inayotegemeza taratibu mpya ya Mungu inayokuja i pamoja nanyi. (Zak. 4:6) Kuendelea kwenu kuhubiri “habari njema hizi za ufalme” kutawaletea mateso na kudhihakiwa zaidi. Walakini kupatwa na hayo kwa ajili ya Yehova Mungu na Kristo wake ndilo pendeleo lililo kubwa zaidi mwezalo kupata. Kumbukeni: ‘Mkilaumiwa kwa ajili ya jina la Kristo ni heri yenu; kwa kuwa roho ya utukufu, na ya Mungu inawakalia.’ (1 Pet. 4:14) Kushutumiwa na adui za ufalme wa Mungu si ishara ya kukosa kibali yake. Kuyavumilia kunashuhudia kwamba mnayo roho ya Mungu. Kuwa na roho yake ikiwakalia kunawaletea utukufu, si aibu. Kunawapa heshima na kuwafanya mwe kama Kristo. Kunafanya mstahili kupata utumishi wenye utukufu katika taratibu mpya ya Mungu inayokuja. Hivyo jihesabuni kuwa wenye furaha, waliopendelewa sana!

—Kutoka Holy Spirit—The Force Behind, the Coming New Order, Sura ya 8.

[Maelezo ya Chini]

a Tazama 1976 Yearbook of Jehovah’s Witnesses, kurasa 24-31.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki