Mwenye Hekima Alikuwa na Maana Gani?
“Waone ya Kuwa Wao Wenyewe Wafanana na Wanyama”
Huenda wanadamu wakajivunia ujuzi na maarifa yao. Hata hivyo wanadamu si bora kuliko wanyama, maana maisha yao yanakwisha kwa njia ile ile moja. Mfalme Sulemani mwenye hekima alionyesha jambo hilo, akasema: “Nikasema moyoni mwangu, Ni kwa sababu ya wanadamu, ili Mungu awajaribu, nao waone ya kuwa wao wenyewe wafanana na wanyama. Kwa maana linalowatukia wanadamu linawatukia wanyama; jambo moja lawatukia; anavyokufa huyu ndivyo anavyokufa huyu; naam, wote wanayo pumzi moja; wala mwanadamu hana kitu cha kumpita mnyama; kwa maana yote ni ubatili. Wote huendea mahali pamoja; wote hutoka katika mavumbi; na hata mavumbini hurudi tena.”—Mhu. 3:18-20.
Kabla tu ya kutoa wazo hilo, Sulemani aliandika hivi: “Mungu atawahukumu wenye haki na wasio haki; kwa kuwa kuna wakati huko kwa kila kusudi na kwa kila kazi.” (Mhu. 3:17) Kwa hiyo, katika mstari wa 18, Sulemani anaposema Mungu ‘anajaribu’ wanadamu, huenda akawa na maana ya kwamba nafasi zote anazowapa, vilevile mambo anayoruhusu yawapate, kama matatizo na mashaka, yataonyesha baadaye kama ni wenye haki au ni waovu. Kwa kuwa maisha yanajawa na magumu na mashaka halafu mwishowe yanakwisha mtu anapokufa, inawapasa wanadamu wafahamu kwamba wao wenyewe hawana nguvu za kuendelea kuishi, bali mwisho wao unakuwa kama wa wanyama. Roho au nguvu ya utendaji inayosaidiwa na pumzi kufanya mwanadamu awe hai ndiyo inayofanya mnyama pia awe hai. Baada ya kufa, mwanadamu na mnyama wanarudia mavumbi yasiyo na uhai.—Mhu. 9:4-6.
Kwa kutegemea maoni ya mwanadamu tu, hakuna mtu anayeweza kujibu ulizo ambalo Sulemani aliuliza baada ya hapo: “Ni nani ajuaye kama roho ya binadamu huenda juu, na kama roho ya mnyama huenda chini?”—Mhu. 3:21.
Kwa kuwa kifo kinamaliza kazi zote za mwanadamu sawasawa na za mnyama, Sulemani alikata maneno akasema: “Nikaona ya kwamba hakuna jema kupita mwanadamu kuzifurahia kazi zake; kwa sababu hili ni fungu lake; kwa maana ni nani atakayemrudisha tena ili ayaone yatakayomfuata baadaye”? (Mhu. 3:22) Jambo la hekima ni mtu afurahi sana kwa sababu ya kazi yake ngumu. Mtu akiisha kufa, anaacha kufanya kazi za kibinadamu. Kwa kuwa ni mzoga usio na uhai, hawezi kuona mambo yanayofanywa na wanadamu.—Mhu. 9:5, 10.
Inatupasa tufikirie mambo kwa uzito tunapokumbuka kwamba kifo kinaweza kumfanya mtu awe si kitu, kama mnyama. Inatupasa tukumbuke ubora wa kutumia maisha yetu kutimiza mambo mema, ijapokuwa kuna mashaka na matatizo. Inatupasa pia tumgeukie Mungu, tukijua kwamba yeye ndiye atakayeamua kama atatufufua tukifa.