Ongezeke la Kiroho la Ireland—Kuvuna Kilichopandwa
“KAMA vile mvua ishukavyo, . . . wala hairudi huko; bali huinywesha ardhi, na kuizalisha na kuichipuza.” (Isa. 55:10) Mkulima Mwireland anajua vizuri sana ukweli wa maneno haya. Kwa sababu ya mvua yake nyingi, Ireland inajaa miti na mimea, nayo inabarikiwa kuwa na milima mizuri na mabonde yenye kuvutia. Mito, vijito na maziwa ya maji yote yanaongeza uzuri wa nchi hii. Walakini si nchi inayolimwa peke yake inayotoa maongezo. Ongezeko la kiroho linajitokeza baada ya watangazaji wa ufalme wa Mungu kuvumilia kwa uaminifu pamoja na kufanya kazi ngumu bila kuchoka kwa muda wa miaka mingi. Sasa wanavuna walichokipanda.—Gal. 6:9.
Katika mwaka wa 1977 wafanya kazi wenye furaha 1,874 walishiriki kuzungumza na wengine juu ya usalama wa kiroho waliokuwa wamepata, si katika sehemu ya kusini yenye amani ya kiasi peke yake, yaani, Jamhuri ya Ireland, bali pia katika mkoa wenye matata wa Ulster, Ireland ya Kaskazini. Karibu mara mbili ya hesabu hiyo, yaani, 3,350, walikusanyika pamoja waadhimishe kifo cha Yesu Kristo. Ikilinganishwa na namna kazi ilivyokuwa ikifanywa katika makumi ya miaka yaliyopita, huu unakuwa ushuhuda wa ongezeko zuri sana la kiroho. Kwa kuwa kazi ya Yehova katika Ireland imepitia katika nyakati zenye taabu nyingi sana!
NGOME YA KIKATOLIKI
Mwandikaji mmoja ameiita Jamhuri ya Ireland kuwa “ngome yenye nguvu zaidi ya Kikatoliki katika [sehemu ya] ulimwengu inayoongea Kiingereza.” Zaidi ya 95 kwa mia ya wakazi wake ni washiriki wa Kanisa Rumi Katoliki. Mwanzoni kazi ya kueneza Injili ya mashahidi Wakristo wa Yehova ilipokewa kwa jeuri nyingi sana. Watangazaji wa kwanza wa “habari njema” za Ufalme walipokewa kwa uadui.
Wale waliojaribu kueneza ujumbe wa kweli, sana sana katika sehemu za mashambani, mara nyingi walifukuzwa kutoka nyumba zao. Walilazimika kuelekeana na watu wenye ghasia waliotisha kufanya na mara nyingi wakafanya jeuri, au waliowanyang’anya vitabu vyao na kuviharibu mbele ya macho yao.
Mashahidi wawili katika kusini mwa Ireland walikutana na wanawake wenye ghasia ambao kwa hasira waliwashtaki kuwa Wakomunisti. Ijapokuwa walijaribu sana kuzungumza kiakili na wanawake hao wenye ghasia, waliendelea kufisha zaidi na zaidi. Mmoja wa Mashahidi hao alijaribu kujiokoa kwa kupanda bas (bus) iliyokuwa karibu, walakini, mahali pa kupata kimbilio mle alianza kushambuliwa na wale waliokuwa ndani, pia. Mwishowe, alipigwa kwa mawe lakini aliweza kuponyoka huku sauti zikilia masikioni mwake “mtupeni mtoni.” Kisha watu hao wenye ghasia walitumia bas hiyo wakamfuatilia yule Shahidi mwingine wakamshambulia vikali sana, na kuharibu vitabu vyake. Aliokoka kufanyiwa madhara makubwa zaidi kwa sababu tu polisi walifika.
Vilevile kulikuwako mashambulio ya maneno. Watangazaji wa habari walimripoti kasisi mmoja akisema hivi juu ya Mashahidi wa Yehova: “Manabii hawa wa uongo . . . wako tu kama Waislamu; kwa kweli wao ni wabaya zaidi, kwa kuwa hao hawaamini kutokufa kwa nafsi. . . . Kuwasikiliza ni kumkana Kristo.” Wale walioonyesha kupendezwa ko kote na ujumbe wa kweli waliwekwa mara hiyo chini ya mikazo ya kijamii na kidini, ili wavunje ushirika wao na hawa “manabii wa uongo.” Mara nyingi, sana sana katika Jamhuri ya Ireland, wale walioitikia kweli hawakuweza kabisa kuendelea kukaa katika sehemu za kwao kwa sababu walinyang’anywa njia zao za kujipatia riziki. Wengine hata waliondoka nchini ili wasizuiwe kuendelea kukua kiroho.
Walakini leo mambo ni tofauti kabisa! Kwa kawaida, watu wa Ireland ni wenye uvumilivu zaidi na wanakuwa na nia ya kuzungumza juu ya mambo ya kiroho. Mashahidi wanatumia vizuri nafasi wazungumze juu ya tumaini lao wanapoendelea na kazi zao za maisha ya kila siku. Katika njia hiyo mara nyingi jamaa nzima zinakuja kupendezwa na yanayosemwa na Biblia. Mmoja aliyeanza kupendezwa hivi karibuni alizungumza na mfanya kazi mwenzake juu ya yale aliyokuwa akijifunza akaamsha kupendezwa katika mfanya kazi mwenzake. Yeye pia alionana na Mashahidi, akaanza kusema na wengine yale aliyokuwa akijifunza. Sasa zaidi ya washiriki wa jamaa yake 30 ni Mashahidi au wanaonyesha kupendezwa na Biblia. Kuvunjika-vunjika kwa uadui wa zamani kunafanya mambo yawe rahisi siku hizi.
KATIKA KASKAZINI YENYE MATATA
Katika sehemu ya kaskazini ya Ireland, ambayo wengi ni Waprotestanti na watukuzaji sana wa taifa, hali katika siku za mwanzoni hazikuwa bora zaidi. Hapa pia kulikuwako mashambulio makali sana, nao uadui ulioimarika sana kati ya jamii za Wakatoliki na Waprotestanti umeendelea kuwa tisho kwa Mashahidi wa Yehova, sana sana kwa sababu Wakatoliki wengine kwa makosa bado wanawaona Mashahidi kuwa “Waprotestanti.” Lakini sasa watu zaidi na zaidi wanakuja kujua kwamba Mashahidi wamejitenga kabisa na dini nyingine zote, za Kikatoliki au za Kiprotestanti.—Ufu. 18:4.
Katika wakati mmoja jeshi la Jamhuri ya Ireland lilitisha kwamba wangelipua makombora ikiwa hotuba ya watu wote haingeacha kutolewa. Polisi na majasusi (wapelelezi) walilazimika kulinda jumba la kusanyiko. Katika wakati mwingine Mashahidi wawili wakitumia “motokaa yenye sauti” waliingia katika eneo la Wakatoliki bila kujua, wakachukuliwa kwa makosa kuwa Waprotestanti. Walianza kutupiwa vitu vingi sana. Walirudisha vyombo vyao upesi katika motokaa yao wakatoka katika eneo hilo, walakini si kabla ya kioo cha mbele cha motokaa hiyo pamoja na sehemu nyingine kuharibiwa na watu hao wenye ghasia kwa fito vya chuma.
Lakini, baada ya kupita muda mambo yalianza kubadilika, maoni ya watu yaliendelea kuwa mazuri, nao wafanya kazi hawa hodari na wenye subira walianza kuona matunda ya kazi yao ngumu. Kazi yao haikuwa ya bure, ijapokuwa hata mpaka hivi karibuni katika mwaka wa 1960 kwa wastani walikuwako Mashahidi wanaopungua mia mbili waliokuwa wakiripoti utumishi wa Ufalme katika Jamhuri hiyo.
BADILIKO KUBWA
Tukio lililoleta badiliko kubwa katika mambo ya Mashahidi wa Yehova katika Ireland lilikuwa kusanyiko la kwanza la mataifa yote lililokuwa kubwa kwa kulinganishwa lililokuwa katika Dublin, katika mwaka 1965. Mahali palikuwa uwanja wa mpira mjini humo. Habari ilipotangazwa kwamba Mashahidi wa Yehova watatumia uwanja huo, vita ikaanza! Kukawa na upinzani mkali sana. Kwa muda fulani haikujulikana kama kungekuwa na kusanyiko. Baraza ya mji ambayo ndiyo iliyokuwa na mamlaka juu ya uwanja huo ilikuwa chini ya mkazo usio na mwisho isiruhusu uwanja huo utumiwe na hawa “wapinga Ukristo na sana sana wapinga Wakatoliki,” kama walivyoitwa. Ijapokuwa Mashahidi waliitwa “hatari” na “tisho,” nayo maoni ya zamani ya ushupavu yakaanza kujitokeza tena, mwishowe ruhusa ilitolewa na kukawa na kusanyiko zuri sana.
Kulikuwako shida nyingine kubwa katika kutayarisha kusanyiko hili. Kwa mfano, kwa sababu ya mikazo ya kidini mahali pa kulala zaidi ya elfu moja palifutwa kabla tu ya kusanyiko kuanza, hata hivyo, wahudhuriaji wote 3,948 walipata mahali pa kulala. Mwenye nyumba mmoja mwanamke alisema hivi baadaye: “Hatukuelezwa ukweli juu yenu ninyi watu, lakini kwa vile sasa tumewajua sikuzote tutafurahia kuwa nanyi tena.”
ONGEZEKO LA HARAKA LA KIROHO
Mara nyingi ukuzi wa haraka wa kiroho unafuata wakati kweli inapopandwa mara ya kwanza. Hapa kuna mfano: Alipokuwa akitembelea wazazi wake katika sehemu yenye matata ya Ireland ya Kaskazini, kijana mmoja alipokea trakiti yenye kurasa nne iliyokuwa imechapwa na Mashahidi wa Yehova. Alithamini sana yaliyosemwa na trakiti hiyo juu ya ufalme wa Mungu, na aliweza kuona kwamba hilo ndilo suluhisho peke yake la uadui mkali unaoletwa na mgawanyiko wa kidini unaoiharibu Ireland ya Kaskazini. Kazi yake ya walimu katika shule za Kikatoliki ilimpeleka Uingereza, ambako aliweza kushirikiana na kundi la Mashahidi wa Yehova. Baada ya miezi minne tu aliamua kurudi katika mji wa kwao asaidie kueneza “habari njema” humo. Na bila shaka msaada ulihitajiwa kwa kuwa wengine watano tu ndio waliokuwa wakitangaza ufalme wa Mungu katika eneo hilo lote.
Alipofika, alipanga barua yake aliyoandikia watu wa mji wao, iliyokuwa ikieleza sababu ya kurudi kwake humo ichapwe na magazeti matatu mbalimbali ya mahali hapo. Hii iliamsha kupendezwa kwingi sana na ikafungua njia ya kuwa na mazungumzo mengi. Ameweza kusaidia wengine wengi waendelee kuithamini kweli ya Biblia. Hawa wanatia ndani rafiki yake ya zamani aliyekuwa ametiwa gerezani kwa sababu ya makosa ya matendo ya uhalifu yenye kuogopesha yaliyohusiana na Jeshi la Jamhuri ya Ireland. Sasa rafiki huyu anaona ubatili wa kutumia jeuri, na kwamba amani na haki yenye kuendelea inaweza kuja tu kupitia kwa utawala wa Ufalme wa Mungu juu ya dunia.
WAFANYA KAZI WA WAKATI WOTE WASHIRIKI
Mengi ya maongezeko haya ya kiroho katika nchi hii ambayo hapo kwanza ilikuwa bila matokeo yamepatikana katika hali zenye shida nyingi sana. Wanaume na wanawake waliojitoa sana wamefanya kutumikia watu wa Ireland kuwa kazi yao ya maisha. Kazi kubwa sana imefanywa kwa uhodari na wafanya kazi wa wakati wote 300 au zaidi waliopo sasa na wale wote waliowatangulia. Karibu 15 kwa mia ya Mashahidi wote katika Ireland wanatumikia sasa kwa wakati wote wakipanda mbegu za kweli na kumwagilia maji.
Utumishi huu wa wakati wote umekuwa na matokeo makubwa. Ripoti kutoka kwa gazeti moja juu ya utendaji wa wanawake wawili vijana Mashahidi wanaosafiri kwa pikipiki inaonyesha namna unavyofanywa: “Donegal umevamiwa tena na pigo la watu wenye kusumbua, wajanja kuliko mbweha. Jeshi la wanaume na wanawake, wengine wao wakisafiri kwa piki-piki, wakitembea nyumba kwa nyumba mijini na mashambani, na kuacha magazeti yao ya bure.” Ni pigo kwa wengine, bali kwa wale wenye mioyo minyofu ni injili ya amani!
KUTUMIKIA KULIKO NA UHITAJI MKUBWA ZAIDI
Vilevile, kazi katika Ireland ilipata msaada mkubwa sana wakati jamaa kutoka nchi nyingine walipoitikia mwaliko wa kutoka katika sehemu zilizo na Mashahidi wengi wahamie sehemu za Ireland zilizo na wachache. Wengine wa hawa wamekuwa watangazaji wa Ufalme wa muda, wengine wa wakati wote, lakini wote walionyesha roho ya kweli ya upainia. Kwa kuwa Mashahidi wengi wapya wa Ireland walilazimika kuondoka nchini kwa sababu ya mikazo, hii imekuwa njia nzuri sana ya kurudisha wengine mahali pao. Kazi inayostahili sifa imefanywa na wafanya kazi hawa wenye furaha wanaoonyesha bidii ile ile ya kimisionari iliyoonyeshwa na Wakristo wenzao waliowatangulia.
Makundi katika sehemu zote za Ireland yametiwa nguvu kwa kuongezewa wasaidizi hawa. Si jambo rahisi kuhamia nchi nyingine na kukaa humo. Kulikuwako magumu mengi, lakini yote hayo yalimalizwa kwa ujasiri na kwa akili. Kundi moja lililosaidiwa katika njia hii linasitawi sasa katika mji mmoja katika Jamhuri hii, mahali ambapo miaka michache tu iliyopita, wengine wa Mashahidi wa Yehova walishambuliwa na kupigwa na watu wenye ghasia wakiongozwa na padre wa mahali hapo.
Makundi haya sasa yanatoa mahali panapoonekana kwa urahisi ambapo watu wenye mioyo minyofu wanaweza kuja. Mwanamume mmoja ambaye hapo kwanza alikuwa Mkatoliki na ambaye alikuwa ameacha dini kabisa aliishi katika eneo la mojawapo la makundi hayo. Mkewe ambaye alikuwa mhudhuriaji wa kanisa mwenye juhudi na ambaye bado alikuwa akitumaini kwamba angeweza kumsaidia mumewe arudi kanisani, mwanzoni alijiepusha kabisa na wale waliowatembelea kuzungumza juu ya Biblia. Lakini mumewe alikuwa ameanza kupendezwa. Mafundisho yenye subira yalianza polepole kuwa na matokeo. Mwishowe wote wawili walifanya mipango ya kuhudhuria mojawapo la makusanyiko ya mzunguko ya Mashahidi wa Yehova yanayofanywa mara mbili kwa mwaka, wakajitafutia njia zao wenyewe za kufika huko na kujitafutia mahali pa kulala. Ushirika huo mzuri uliwasaidia sana, na ijapokuwa mikazo ya jamaa zao, wote wawili walifanya maendeleo mazuri ya kiroho na mwishowe walibatizwa pamoja. Mumewe alipotoka katika maji ya ubatizo, alimwona Shahidi mwingine ambaye alikuwa ndio amebatizwa. Walipokuwa vijana, wote wawili walikuwa wakitumikia pamoja madhabahuni!
USHUHUDA ULIOPO WA UFANISI
Sasa makundi ya Mashahidi wa Yehova 66, licha ya vikundi vidogo 30 vilivyo peke yake, yanatumikiwa na waangalizi wa mzunguko 5 wanaotembelea kila moja yayo mara mbili kila mwaka ili kuyatia moyo kiroho. Makundi haya pamoja na vikundi vilevile hufaidika sana kutokana na makusanyiko mazuri sana yanayofanywa kwa ukawaida katika Ireland yote.
Watu wanaompenda Mungu na kanuni nzuri kutoka katika sehemu ya Kaskazini na ya Kusini ya mpaka katika Ireland wanakua kiroho, wakiimarishwa katika imani yao. (Efe. 3:17) Kama ilivyo kwa mkulima anayengojea mazao yakue, wale wote walioshiriki katika kupanda na kulimia mbegu za kweli walihitaji kuonyesha subira nyingi sana. Lakini sasa Mungu anazifanya zikue.—1 Kor. 3:6, 7.