Kugeuza Utu wa Watu Katika Paradiso ya Kenya
MAMILIONI ya watalii wameanza safari zao za kuona wanyama wa mwitu wakiwa Nairobi, ambao ndio mji mkuu wa Kenya. Wanaingia katika mbuga (pori) za taifa wakitafuta simba, ndovu, vifaru, chui na viumbe vingine vyenye kufurahisha katika makao yavyo ya asili.
Simba, ambaye ndiye mkubwa kuliko wanyama wote wenye kula nyama, anawapendeza sana wasafiri hao. Jambo linalowafurahisha wengi wao ni kumwona hayawani huyo hodari akinyemelea-nyemelea mnyama mwingine mtulivu wa uwandani, kisha kumkamata na kumtafuna-tafuna. Kwa sababu ya tamasha hiyo, huenda unabii mwingi wa Biblia ulio katika Isaya sura ya 11 ukaonekana kuwa wa ajabu sana, ambapo simba anaonyeshwa akila majani kama ng’ombe na kulala kwa amani akiwa na wanyama wengine.
Lakini, guezo la kiroho lililo la kushangaza zaidi linafanyika leo ndani ya watu wenye mioyo myeupe, nao wanaingia katika paradiso ya kiroho wakiisha kujifunza kweli ya Biblia, kisha wanatupilia mbali tabia za ukorofi walizokuwa nazo na kuvaa utu wenye amani na fadhili. Geuzo hilo limefanyika mara nyingi katika makundi karibu 90 ya Mashahidi wa Yehova katika Kenya. Tena, katika taratibu mpya ya Mungu, inaweza kutazamiwa kwamba hata mnyama-mwitu aliye mkali zaidi atafugwa, aishi kwa amani pamoja na wanadamu na viumbe vingine vyote vya Mungu vilivyo duniani.
Huu ni mfano mmoja wa kugeuza utu wa watu:
Kijana mmoja aliyezaliwa katika eneo lenye kahawa karibu na Nairobi alikuwa ameishi maisha ya kutanga-tanga yenye vituko vingi, akiwa na kazi mbalimbali kama ya kuuza vitu dukani, kukamata nyoka, na kuuza pombe katika jumba la pombe. Alipigana na mapolisi, akasaidla watu kutoa mimba kinyume cha sheria, akapiga watu wengi, akawa mtu wa kukamatwa mara nyingi. Siku moja aliudhiwa na tajiri wake mpaka akaamua “kumng’oa macho,” hata akawaeleza jirani zake hivyo bila kuogopa. Mwanamke jirani, ambaye ni shahidi wa Yehova aliye wakf, alimsaidia kuwa na mawazo mazuri kwa kumjibu hivi: “Kama ungekuwa ukijifunza Biblia, ungekuwa mwenye furaha wala usingetaka kumtenda tajiri wako ubaya huo.” Lo! awe mwenye furaha—hivyo ndivyo alivyotaka kuwa! Funzo la Biblia lilianzwa alipotaka kujua jinsi ya kuwa mwenye furaha. Wakati wa ubatizo wake katika “Utumishi Mtakatifu” Kusanyiko la Wilaya la Mashahidi wa Yehova, yeye alisema hivi: “Tangu wakati huo sijajaribu kamwe kumtenda tajiri wangu wala mtu mwingineyo ubaya wo wote. Nakuambia sasa mimi ni mwenye furaha sana.”
Lo! hilo ni geuzo kubwa namna gani la utu!
MAGUMU HAPO KWANZA
Huko nyuma mwaka 1956 wakati wamisionari wa kwanza wa Mashahidi wa Yehova walipoiingia nchi hii yenye hali nzuri walipata magumu mengi wakati wa kusaidia watu wapate maarifa sahihi ya Biblia kwa kusudi la ‘kujivika utu mpya wa Kikristo.’ (Kol. 3:10) Kenya ni tofauti na nchi nyingine za Afrika kwa maana ina mchanganyiko wa makabila yenye hali, desturi na lugha zisizopatana hata kidogo. Makabila hayo yanayotofautiana sana yalihamia nchi hiyo kutoka sehemu mbalimbali kama Bonde la Mto Nailo (Nile), msitu wa Afrika ya kati na mkono wa nchi ya Arabuni. Kenya inakaliwa na makabila zaidi ya 40 yaliyotokana na mafungu manne ya jamii mbalimbali za watu, yaani, Wabantu, Wanailo-Hamu, Wanailo, na wahamu. Licha ya nchi hiyo kuwa na idadi kubwa ya watu, ambao sasa ni karibu milioni kumi na nne wenye kusema lugha nyingi mbalimbali, kulikuwa na magumu ya desturi za kikabila, kutojua kusoma wala kuandika na uasherati, nao watu wengi waliishi katika vijumba vilivyo mbali mbali, vyenye kuzungukwa na mashamba yao.
Dini za Jumuiya ya Wakristo zilikuwa zimeanzisha makanisa mbalimbali katika sehemu nyingi za kati na magharibi ya Kenya. Upande wa pwani dini ya Waislamu ilikuwa imeenea kwa sababu ya Waarabu kuwako. Makabila mengine yalikataa kufuata dini zilizoletwa na wageni, kwa hiyo yakaendelea kufuata ibada zao za kimila.
Ili kusaidia watu wapate maarifa ya Biblia, Mashahidi wa Yehova wameitumia njia yao inayojulikana sana ya kuwahubiri watu nyumba kwa nyumba na vilevile kutumia vitabu. Vitabu vyenye mafunzo ya Biblia vimetolewa katika “lugha ya kazi” ya mashariki ya Afrika yaani, Kiswahili, na katika lugha nne kubwa za Kenya.
MAGEUZO YA UTU KATI YA MAKABILA MBALIMBALI
Wakamba, ambao ni Wabantu wanaokaa katika vilima na nyanda zenye mashamba mashariki ya Nairobi, wanajulikana kwa sababu ya kuchonga sanamu nzuri za miti, kwa sababu ya mila yao ya kupenda mashamba na ng’ombe, na kwa sababu hapo kwanza walikuwa wakioa wake wengi. Hata hivyo, kazi iliyofanywa mwanzoni na wamisionari wa Mashahidi wa Yehova imekuwa na matokeo mazuri kwa maana leo eneo hilo lina makundi kumi na tisa yenye bidii. Wahubiri wengi wa “habari njema” wanaoitwa “mapainia wa pekee” ni wa kabila hilo lenye watu wachangamfu, walio hodari kwa kuimba na kucheza ngoma. Angalia jambo hili lililoonwa:
Shahidi mmoja, ambaye sasa ametumikia miaka mingi kama mhudumu mwenye kusafiri na ‘kupainia’ katika maeneo mapya, alifanya mabadiliko mengi katika utu wake. Alipofika umri wa miaka kumi na mitatu alikuwa amezoea sana uasherati, wivu, uvutaji wa sigara na kutumia dawa za kulevya, kwa maana aliwaona watu wa makamu wenye kujiita Wakristo wakiweka mfano mbaya, tena yeye hakuwa na uongozi ufaao wa Biblia. Vijana wawili ambao zamani walikuwa katika shule moja naye walimpelekea kweli, kisha yeye akakubaliana nao kwa maana aliona kwamba wao wenyewe waliyafanya mambo waliyokuwa wakimwambia. Watu wa eneo hilo walistaajabu kumwona amebadili nia yake na utu wake, akawa mtu safi na mwenye kuheshimika, mwenye kutaka amani na kusaidia kuleta tabia njema katika mtaa huo.
Katika miinuko yenye rutuba ya lile Bonde Kuu, miti ya chai inafanya mashamba yapendeze sana. Watu wenye maungo wa eneo hilo, ambao ni wa jamii ya Wanailo-Hamu inayoitwa Kalenjin, walikuwa mashujaa wakali wa vita nyakati zilizopita. Leo wanajivunia uhakika wa kwamba wengine wa wapiga mbio za mwendo mrefu, walio hodari na wanaojulikana zaidi ulimwenguni, ni watu wa kabila lao. Wangali wanashikilia desturi nyingi za zamani, pamoja na sherehe ndefu za kuingiza vijana wao jandoni (katika shule ya vijana wanaotahiriwa), na kuwafundisha sana mila na desturi za kabila lao. Jambo lifuatalo linaonyesha jinsi kweli ya Biblia inavyoendelea kuingia kati ya watu hao:
Mwaka 1968, mwanamume mmoja alihangaika alipoliona jina la Mungu, Yehova, katika kimojawapo vitabu vya Mashahidi wa Yehova. Alipoangalia Biblia yake katika Zaburi 83:18, alijua kwamba dini yake ya Katoliki ilikuwa imemficha jina hilo. Kwa sababu ya kujawa na mashaka, alimwungamia padre wake kwamba alisoma kitabu chenye maelezo juu ya Biblia. Padre alimlaumu sana, akasali kwa Kilatin ili kumwombea msamaha wa “dhambi zake,” kisha akamweleza waziwazi kwamba lazima aache kutafuta kweli ya Biblia mahali penginepo. Mwanamume huyo hakupata Mashahidi wo wote katika eneo hilo, lakini aliona vitabu vyao katika duka la mtu mmoja aliyemfahamu. Ingawa mwenye duka hilo alimruhusu achunguze vitabu hivyo hapo dukani, hakutaka kumpa akavisome kwa maana alivithamini sana. Baadaye rafiki yetu kijana alikipata kitabu Kutoka Paradiso Iliyopotea Mpaka Paradiso Iliyopatikana, nacho kikamwonyesha waziwazi habari za kweli juu ya jina la Mungu, na ubaya wa kuungama pia unaozoewa na dini yake. (Kut. 6:2, 3; Isa. 42:8; 1 Tim. 2:5) Hata kabla hajaonana na Shahidi, aliamua kujitenga kabisa na kanisa lake. Muda mfupi baadaye, alipata habari juu ya mwanamke mmoja aliyekuwa amehamia eneo hilo “akihubiri dini ya ajabu.” Alikwenda kumtafuta, akakuta kwamba mwanamke huyo ni Shahidi, kisha akachukua kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele na kumaliza kukisoma kwa muda wa siku tatu. Wakati alipokuwa akijifunza Biblia alipingwa sana na wazazi wake, rafiki zake wa zamani na jirani, lakini baadaye aliweza kusaidia wengine wa wapinzani hao wakaanza kujifunza Biblia. Leo yeye ni “painia” mwenye kuzihubiri “habari njema,” naye anaonyesha wengine ile kweli, ambayo hata yule rafiki yake mwenye duka amekwisha ikubali pia.
Tukisonga mbele magharibi, tunazifikia pwani na Ziwa Victoria lenye kupendeza, na huko ndiko wanakokaa Wanailo wa pekee wapatikanao Kenya, yaani, Waluo. Waluo, ambao ni watu waliohama kutoka Bonde la upande wa juu wa Mto Nailo, wana mfufulizo wa sherehe za kutia vijana wao jandoni, na wakati wa sherehe hizo vijana fulani wanakubali kung’olewa meno mawili au zaidi katika taya la chini ili kuhakikisha wao ni mashujaa. Desturi zao za kufanya maziko na matanga (maombolezo) ya muda mrefu zinaonyesha wanaamini sana kwamba wanaweza kupashana habari na mababu waliokufa. Katika Kisumu, ambayo ndiyo makao makuu ya eneo hilo, na ambao ndio mji wa tatu kwa ukubwa katika Kenya, mkuu mmoja wa serikali alielezwa kweli ya Biblia kwa mara ya kwanza mwaka 1965 na mfanya kazi mwenzake. Ingawa hakuanza kujifunza Biblia kwa makini, nyakati zote aliwasalimu kirafiki Mashahidi waliopita karibu na afisi yake. Miaka kumi ilipita, lakini lo! alifurahi namna gani kuonyesha wakf wake kwa kubatizwa majini mwaka juzi! Kwa sababu ya furaha aliyopata aliomba apewe pendeleo la kulipa gharama ya jumba ambamo kusanyiko la mzunguko lilifanywa wakati wa juma ya kubatizwa kwake. Baada ya muda mfupi amesaidia wengine walio karibu yake, kutia na mkewe, wakaiona kweli na kugeuza nia zao.
Wanaokaa katika mwinuko ulioko mashariki ya kaskazini ya Ziwa Victoria mpaka kwenye eneo la chini la Mlima Elgon, wenye urefu wa mita 4,322 (futi 14,178), ni watu wanaoitwa Abaluhya, nalo hilo ni jina la mwungano wa jamii kubwa ya Wabantu. Watu hao wanazikubali habari njema kwa kuzithamini mioyoni mwao. Mwaka juzi, katika kijiji kimoja kilicho karibu sana na ikweta katika eneo hilo la magharibi, kijana wa miaka kumi na mitano alivumilia upinzani mwingi na kuweka maisha yake wakf kwa Yehova. Ndipo alipopata habari kwamba miezi mitatu baadaye kungekuwa na kusanyiko “Utumishi Mtakatifu” Nairobi, kilomita 340 (maili 210) kutoka hapo, kisha akatafuta kazi apate fedha za safari hiyo. Mwangalizi-msimamizi ndiye akawa ‘banki’ yake ya kumwekea fedha. Ajabu ni kwamba, alipopata pesa za kumwezesha kusafiri, alianza kutafuta nyingine pia, Ziwe za nani? Ziwe za rafiki mwenye kupendezwa wa umri wake, maana alimtaka yeye awe na nafasi iyo hiyo ya kufurahia kipindi cha Kusanyiko la wilaya!
GUMU LA TABIA
Kati ya makabila yote ya Kenya, labda Wamasai ndio wanaojulikana zaidi ulimwenguni pote. Wao ni wenye sifa ya kuwa na uhodari mwingi sana na kukaa peke yao wakijisimamia wenyewe. Desturi zao nyingi za zamani zingali hazijageuzwa na desturi za Kizungu. Wao wanavaa vazi lenye rangi kama ya udongo mwekundu na kujipamba kwa kuvaa shanga, huku chakula chao kikiwa ni maziwa hasa yenye damu nyingi ya ng’ombe. Wangali wanashikilia mpango wa “moran,” ambapo vijana wanaume wanatengwa peke yao na kuwekewa sheria ngumu za kujinyima vitu mpaka watakapostahili kuwa wazee, ijapokuwa wanaruhusiwa kulala na wanawake. Jambo la ajabu linalofanywa na Waelgeyo/Marakwet ni kukubali kuoana baada ya mke kuchukua mimba, lakini si kabla ya hapo. Maisha ya makabila hayo mawili yanaonyesha mengine ya matatizo ya tabia yanayowapata pamoja na wengine wanaotaka kugeuza utu wao upatane na kanuni njema za Biblia.
Desturi imeenea sana ya wanaume na wanawake kuishi pamoja na kuzaa watoto bila ya kuoana kisheria maisha yao yote. Watu wengi wanatosheka wanapooana kwa muda tu, kwa kufuata mipango ya kabila lao. Mara nyingi watu wanakawia kuoana kisheria kwa sababu ya mahari nyingi sana kudaiwa. Lakini, baada ya kujifunza kanuni bora za Mungu, wengi wamefanya bidii kwa moyo mweupe wakaandikisha ndoa zao. Wazee wa Mashahidi wa Yehova, waliowekwa rasmi na serikali na kupewa cheti, wamewasaidia sana watu hao kwa sababu wanatoa utumishi wao bila malipo, si kama wachungaji wa Jumuiya ya Wakristo ambao kwa kawaida wanaomba malipo mengi. Hivyo, waume na wake karibu 600 wamesaidiwa kuoana kupatana na kanuni njema za Mungu. Huu ni mfano wa mume na mke waliooana:
Mwanamume mmoja alijaribu kumzuia mama ya watoto wake asijifunze Biblia na Mashahidi. Lakini, mwanamke huyo alivumilia na kuzidi kufanya maendeleo, akitaka kumpendeza mungu. Mwanamume huyo alipokataa kuandikisha mwungano wao kisheria, mwanamke huyo alimwacha akavumilia kuishi maisha yasiyo na gharama nyingi. Aliona ukweli wa maneno yaliyo katika Zaburi 37:25, yanayoonyesha kwamba Mungu atasaidia wapendao haki, basi akaweza kuwapa riziki watoto alioachiwa. Jambo hilo lilimshangaza mwanamume huyo, lakini aliendelea kufanya upinzani kiasi cha kuwaomba wanasiasa waipige marufuku kazi ya Mashahidi wa Yehova nchini. Lakini kwa njia ya ajabu akaanza ‘kugeuza nia yake.’ Alipokuwa akipeleka watoto wake katika matembezi mafupi, mwana wake wa miaka mitatu alimwambia maneno fulani yakamsumbua moyo. Mtoto huyo alikuwa akimwambia mambo kama haya: “Baba, utakapoacha kuvuta sigara na kunywa pombe kisha ununue kitabu cha nyimbo na Biblia, tutakwenda kwenye Jumba la Ufalme wala hutaharibiwa.” Mwishowe, mtu huyo alikubali kujifunza Biblia, akafanya maendeleo, akaandikisha ndoa yake kisheria, na kuanza kumtumikia Mungu pamoja na jamaa yake ambayo sasa ina umoja.
MAENDELEO YA MIAKA YA KARIBUNI
Tangu mwaka 1973 mwendo wa mpanuko umeongezwa. Hali zilionyesha wazi sana mwaka huo kwamba ingewapasa Mashahidi wenyeji wachukue madaraka makuu ya kupelekea wengine “habari njema.” Kwa kusaidiwa na Yehova wameweza kutimiza madaraka hayo na kupeleka ujumbe kwenye maeneo ya mbali zaidi ya nchi. Wakati uo huo, kulikuwa na mfululizo wa matukio katika nchi jirani yakaonyesha kwamba hali ya mambo inazidi kuharibika nyakati zote. Ukavu mwingi ulitokea ukafanya watu wengi wafikirie jinsi wanavyomtegemea Mpaji wetu wa mbinguni. Bei za vitu zinazopanda na hatari mbalimbali za nchi jirani zimesaidia wengine kuona kwamba unabii wa Biblia unasema kweli. Matatizo yanayopatikana ulimwenguni pote ya ulevi, uvunjaji sheria, matumizi mabaya ya dawa za kulevya na kuvunjika kwa jamaa yameenea sana, yakafanya wengine, sana sana vijana, wajue kwamba viongozi wao wa kidini wameshindwa kuwapa uongozi na kwa hiyo lazima wategemee uongozi mzuri mahali pengine. Katika maeneo yote ya nchi, na kati ya watu wa namna zote, Mashahidi wa Yehova wanawaendea na kuwasaidia watu wanaotaka kwa moyo mweupe kuuvaa utu mpya na kugeuza maisha yao.
Miaka ya karibuni wahubiri na waalimu wa “habari njema” wanaoitwa “mapainia” wamehamia maeneo mengi mapya, na mengine kati ya hayo yakawa na maendeleo yenye kutia sana moyo. Limuru, ambao ni mji wenye viwanda karibu na ukingo wa mashariki wa lile Bonde Kuu, umekuwa hauna wahubiri wa Ufalme, lakini baada ya muda unaopungua miaka mitatu sasa una wahubiri kumi na sita wanaohubiri kweli ya Biblia kwa bidii. Katika kipindi icho hicho eneo lenye rutuba la Wakikuyu, ambao ni watu wenye bidii, pamoja na eneo la Wameru na Waembu katika mitelemko ya Mlima Kenya wenye theluji, limekuwa na ongezeko la kutoka Mashahidi 30 wenye bidii likawa na zaidi ya 140. Kati yao kuna mzee Mkikuyu aliyezaliwa miaka karibu 80 iliyopita, wakati ambao watu walikuwa wakitobolewa matundu masikioni kisha yanarefushwa na kukunjiliwa upande wa juu wa sikio. Kwa kawaida yeye anatembea kilomita karibu 20 (maili 12), akipanda vilima na kutelemka, ili kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Hata pawe ni mahali gani, kando-kando ya Mlima Kenya, katika mitelemko yenye misitu inayopendeza ya Bonde la Mau magharibi ya Nakuru, au katika eneo lenye mashamba mengi sana kando-kando ya Kisii katika magharibi ya kusini ya Kenya, ukuzi umekuwa mkubwa sana.
Katika pwani ya Bahari Kuu ya Bara Hindi, karibu na Mombasa, mume na mke mmoja wanaongoza jumla ya mafunzo ya Biblia kumi na tisa katika nyumba za wenye kupendezwa. Wanaufurahia sana utumishi wao kiasi cha kwamba walimwita mtoto wao wa kwanza “Painia.” Katika Kenya nzima, watu zaidi ya 1,045 walibatizwa kuonyesha wakf wao miaka mitatu na nusu iliyopita. Wengine zaidi wanataka kuvaa utu mpya, kama inavyoonekana kutokana na hesabu ya wanaohudhuria mikutano, ambayo ni mara mbili ya Mashahidi waliopo. Hesabu ya waliohudhuria mwadhimisho wa Chakula cha Bwana cha Jioni Aprili 3 (mwaka jana) walizidi 5,000 kwa mara ya kwanza, wakiwa ni watu 5,582.
Ndiyo, utu unageuzwa kati ya makabila yote ya Kenya, na humu tumetaja machache tu. Kutoka mito yenye barafu ya Mlima Kenya, iliyo juu kuliko mito yo yote katika milima ya Amerika au ya Ulaya, mpaka kwenye kando za pwani zinazopendeza sana na zenye joto jingi, na kutoka maeneo makavu ya kaskazini yenye jangwa, kuja kwenye misitu iliyo milimani na katika mashamba yaliyoinuka yenye rutuba mpaka kwenye nyanda zenye manyasi za Masai Mara, katika ukingo wa nyanda za Serengeti, watu wanausikia ujumbe wa Biblia na kubadili nia zao. Kwa hiyo, uifikiriapo Kenya pamoja na wanyama wake walio katika makao ya asili, na vilevile umfikiriapo simba hodari akimwendea swala polepole ili ajipatie chakula, ufikirie pia utu na tabia zinazogeuzwa kwa uwezo wa Neno la Mungu. Uzifikiriapo desturi mbalimbali, mazoea na lugha mbalimbali, fikiria pia jinsi watu hao wanavyounganishwa kuwa jamaa moja yenye furaha ya wanaume na wanawake Wakristo wanaomtumikia Muumba kwa sababu ya kugeuza utu wao. Hakika, utu wa watu unageuzwa sana katika paradiso ya kiroho ya Kenya.
[Picha katika ukurasa wa 4]
“Na simba atakula majani kama ng’ombe.—Isa. 11:7.”