Wewe Unawezaje Kuwa na Matazamio Mazuri?
ILI kuwa na matazamio mazuri juu ya wakati ujao, watu wanahitaji kuwa na tumaini lenye msingi imara. Mtu wa pekee anayeweza kuwapa tumaini hilo ni Muumba wa mwanadamu, Yehova Mungu, naye amekwisha wapa kwa kutumia Neno lake, Biblia. Paulo mtume Mkristo aliandika hivi: “Yote yaliyotangulia kuandikwa yaliandikwa ili kutufundisha sisi; ili kwa saburi na faraja ya maandiko tupate kuwa na tumaini.”—Rum. 15:4.
Watu wanaokataa uongozi wa Neno la Mungu na kutazamia vitu vingine viwape tumaini lenye kuaminika juu ya wakati ujao watakata tamaa bila shaka. Hivyo ndivyo unabii wa Isaya ulivyoonyesha Waisraeli wasio waaminifu, waliotenda kinyume cha sheria ya Mungu wakategemea wachawi, watabiri na hata wafu ili wawaeleze mambo ya wakati ujao.
Isaya 8:19-22 inaelekea kuonyesha kwamba Waisraeli hao wasio waaminifu wangetia waaminifu moyo wafanye vivyo hivyo, halafu inaonyesha mambo yaliyowapata wale waliokataa chanzo cha uongozi na tumaini la kweli, yaani, Yehova. Tunasoma hivi: “Wakati watakapokuambia, Tafuta habari kwa watu wenye pepo na kwa wachawi; waliao kama ndege na kunong’ona; je! haiwapasi watu kutafuta habari kwa Mungu wao? je waende kwa watu waliokufa kwa ajili ya watu walio hai? Na waende kwa sheria na ushuhuda; ikiwa hawasemi sawasawa na neno hili, na shaka kwa hao hapana asubuhi. Nao atapita katikati yake, wamedhikika sana na kuwa na njaa; na itakuwa watakapoona njaa, watalalamika na kuapa kwa mfalme wao, na kwa Mungu wao, na kuelekeza nyuso zao juu; nao wataiangalia nchi, na, tazama, shida na giza; hapana changamko kwa sababu ya dhiki; nao watafukuzwa na kuingia katika giza kubwa.”
Kusingekuwa na “asubuhi” kwa wale wenye kutia wenzao moyo waendee wachawi, watabiri na wafu. Baada ya kupatwa na msiba, wasingekuwa na kitu cha kuwachangamsha katika matazamio yao. Msiba ambao ungetokea, unaosimuliwa katika unabii wa Isaya, ni kushambuliwa na Waashuru kama ilivyotabiriwa. Waokokaji wangedhikika sana,’ yaani, wangetaabishwa. Kwa kuwa kushindwa kwa nchi kungefanya mashamba yaliyolimwa, bustani zenye matunda na mashamba ya mizabibu yaharibiwe pia, waokokaji wangeona njaa. Waisraeli wasio na imani, walioepuka kifo na vilevile wakaepuka kupelekwa utumwani, wangefadhaika ‘walalamike’ au wakasirike kwa sababu ya njaa. Wao wangeona kwamba haikufaa waletewe mabaya kwa sababu ya kutoaminika kwao. Bali, wangemlaani mfalme na Aliye Juu Zaidi, wawalaumu kwa sababu ya taabu zao. Wakati watu hao wangeelekeza nyuso zao mbinguni, wasingeona dalili yo yote nzuri yenye kuwapa tumaini la kutazamia nyakati bora. Watazamapo vitu duniani, vyote vingewatia huzuni tu. Kwa sababu ya kukataa “sheria na ushuhuda” wa Mungu, wasingeweza kuona hata dalili iliyo ndogo zaidi ya kwamba wakati ujao kungekuwa na mambo mazuri.
Vivyo hivyo, siku hizi watu wengi wanaogopeshwa na mambo wanayoona yakitendeka duniani—uhalifu ukiongezeka, hewa, nchi na maji zikichafuliwa, na msukosuko kati ya mataifa. Ingawa Wakristo wa kweli wanapatwa na mambo hayo, wao hawana huzuni watazamiapo mambo ya wakati ujao. Kwa sababu gani? Ni kwa sababu wanajua kutokana na Neno la Mungu kwamba hali iliyopo ulimwenguni inatimiza unabii na kuonyesha kwamba ukombozi unakaribia kuletwa na Yesu Kristo kupitia kwa ufalme wa Mungu. Basi, wao wanafanya kama vile walivyotiwa moyo na Yesu Kristo: “Mambo hayo yaanzapo kutokea, changamkeni, mkaviinue vichwa vyenu, kwa kuwa ukombozi wenu umekaribia.” (Luka 21:28) Je! wewe pia una hakika ya kuuona ukombozi huo kwa sababu ya kuukubali ujumbe wa Biblia kuwa “neno la Mungu”?—1 The. 2:13.