Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w78 3/15 kur. 4-7
  • Je! Wewe U Tayari Kueleza Watu Habari za Biblia?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Wewe U Tayari Kueleza Watu Habari za Biblia?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • UHITAJI WA KUTUMIA BIBLIA WAKATI WA KUSEMA
  • LENGO LETU NI KUSAIDIA WATU
  • KITU CHA WATU WOTE
  • ‘KUTUMIA KWA HALALI NENO LA KWELI’
  • Jitoe Mwenyewe kwa Usomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Soma Neno la Mungu na Umtumikie Katika Kweli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Je! Wewe ni Mwenye Matokeo Katika Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Tumia kwa Ustadi “Upanga wa Roho”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
w78 3/15 kur. 4-7

Je! Wewe U Tayari Kueleza Watu Habari za Biblia?

“MIMI naamini kwamba Biblia ndiyo zawadi nzuri kupita zote ambazo Mungu amepata kumpa mwanadamu,” akasema Abraham Lincoln, rais wa kumi na sita wa United States. Ingawa Lincoln hakujiunga na kanisa lolote, alikuwa msomaji wa Biblia tangu ujana wake. Kwa kweli, wakati yeye alipokuwa akienda shuleni siku zile zisizokuwa na maendeleo mengi, Biblia ilikuwa ikitumiwa masomoni. Na inasemekana kwamba, wakati Lincoln alipokuwa rais, mara nyingi alikuwa akisoma Biblia fulani kuukuu ya jamaa yao, katika miaka 1861-1865.

Abraham Lincoln ni mmoja tu wa watu wengi mashuhuri ambao wameiona Biblia kuwa na ubora mwingi sana maishani. Lakini namna gani wewe? Kweli unayaona Maandiko kama zawadi kutoka kwa Mungu? Labda umejiweka wakf kwa Yehova Mungu na una pendeleo la kueleza wengi “Habari Njema ya utukufu wa Mungu ahimidiwaye.” (1 Tim. 1:11) Ikiwa ndivyo, unaweza kutumia Maandiko kwa njia yenye matokeo mazuri? Je! wewe u tayari kueleza watu habari za Biblia?

UHITAJI WA KUTUMIA BIBLIA WAKATI WA KUSEMA

Wakristo wanahitajiwa waijue sana Biblia ili kutimiza agizo la ‘kufanya watu wa mataifa yote kuwa wanafunzi, kuwafundisha kushika mambo yote’ ambayo Yesu Kristo aliagiza. (Mt. 28:19, 20) Yesu mwenyewe alikuwa ameyafahamu sana Maandiko. Aliyatumia kuvipinga vishawishi vya Shetani Ibilisi. (Mt. 4:1-11) Yesu alisomea wengine Neno la Mungu pia, kama vile katika sinagogi Nazareti. (Luka 4:16-21) Mara nyingi, alipokuwa akiongea na watu alikuwa akisema, “Imeandikwa,” halafu anatumia maneno ya Maandiko ya Kiebrania. (Luka 7:27; 19:46; Yohana 2:17) Lo! aliwekea wafuasi wake mfano mwema namna gani!

Mtume Paulo alifuata mfano wa Yesu, akatumia Neno la Mungu katika kazi yake ya kuhubiri na kufundisha. Kwa mfano, alipokuwa katika Thesalonike alikwenda kwenye sinagogi la Wayahudi “akahojiana nao kwa maneno ya maandiko sabato tatu, akiyafunua na kuwaeleza ya kwamba ilimpasa Kristo kuteswa, na kufufuka katika wafu.” (Matendo 17:1-3) Ni wazi kwamba kwa ujumla Wakristo wa karne ya kwanza waliweza kueleza watu habari za Biblia, tena walikuwa na hamu nyingi ya kufanya hivyo.

Wakristo hao wa kwanza waliujua uhitaji wa kueleza watu mambo kutokana na Maandiko. Ndiyo sababu walitaka kuwa na Neno la Mungu kwa namna ambayo lingeweza kuwafaa zaidi. Akiandika juu ya “Vitabu vya Zamani Zaidi vya Kikristo” (katika Kiingereza), C. C. McCown alisema hivi: “Mambo ambayo yamevumbuliwa majuzi juu ya jinsi Wakristo wa kwanza walivyotumia codex (hati nyingi zilizounganishwa kuwa kitabu kimoja), yameonyesha kwamba wao walitaka kuwa wasomaji wazuri, wasiojionyesha elimu yao. Si watu wenye vyeo vya juu peke yao waliopaswa kusoma vitabu vya kidini vya Wakristo, yaani, Agano la Kale na maandishi mapya yaliyokuwa yakielekea kuwa matakatifu. Wafanya kazi wenye bidii walitaka kusoma sana vitabu ili wafaidike navyo kama iwezekanavyo. Wafanya kazi hao pamoja na wamisionari Wakristo wenye bidii walitaka waweze kufungua andiko hili au hili upesi ili kuhakikisha mambo ,bila ya kutaabika wakikunjua sehemu ndefu sana ya kitabu cha mafunjo. Wao hawakutaka kujionyesha kuwa wenye elimu ya vitabu.” Basi, waliunganisha Maandiko yao yakawa namna ya kitabu, kama ile ile tunayotumia hata leo hii,​—The Biblical Archaeologist Reader, uku. 261.

Mmoja wa Wakristo hao wa kwanza waliokuwa tayari kueleza watu habari za Maandiko alikuwa Apolo. Alipofika Akaya, aliweza kusaidia wengine kiroho, “kwa maana aliwashinda Wayahudi kabisa kabisa mbele ya watu wote, akionyesha kwa maneno ya maandiko ya kuwa Yesu ni Kristo.” (Matendo 18:24-28) Hakika ni furaha kuweza kumtetea Mungu na Neno lake kwa ‘kuwa tayari sikuzote kumjibu kila mtu akuulizaye habari za tumaini lililo ndani yako.’ (1 Pet. 3:15) Naam, ni furaha kujibu watu wanyofu maulizo yao kwa kutumia Neno la Mungu, Biblia. (Kol. 4:6) Tena furaha ya mtu inaongezeka wakati anapoeleza mwanafunzi wake habari za Maandiko na kumwona akifanya maendeleo katika funzo la nyumbani la Biblia.

LENGO LETU NI KUSAIDIA WATU

Lengo kubwa la Mashahidi wa Yehova ni kusaidia watu kiroho, si kuwaangushia vitabu vya habari za Biblia tu. Mahali pengi watu wametembelewa mara nyingi, kwa hiyo huenda wakawa hawahitaji vitabu zaidi. Bali, wanahitaji mazungumzo ya Biblia yenye kuwajibu maulizo yao, yenye kuwafanya watake kujifunza vitabu pamoja na Biblia zao, na kuwaongoza wachukue hatua ya kumwabudu Mungu “kwa roho na kweli.”​—Yohana 4:23, 24.

Wakati wewe shahidi Mkristo wa Yehova unapotumia Biblia kwa unyofu ili kuzungumza na watu, ujumbe wa Ufalme unakuwa na nguvu zaidi za kusihi watu, nguvu ambazo vitabu havina kuweza kusihi watu wengi. Ni jambo la maana kuwa mwepesi kuona mahitaji ya watu na kuwa na nia ya kuwapa msaada wa kiroho kwa kutumia Neno la Mungu. Hata vijana na watu wapya wanaweza kutumia Biblia wanapozungumza na watu. Hawana haja ya kusitasita kufanya hivyo ikiwa wanasoma Maandiko kwa ukawaida na kuandika maandiko ya Biblia ya kutumia wakati wanapoeleza watu kweli ya Mungu. Ukisoma Maandiko kila siku utaweza kueleza watu wa kila namna habari za Biblia.

KITU CHA WATU WOTE

Kuna kitu fulani katika Biblia kinachofaa watu wa hali zote za maisha. Kwa hiyo, Wakristo wanaposoma Neno la Mungu wanaweza kuandika habari zitakazowasaidia kueleza watu juu ya Biblia, wawe ni wanasayansi, madaktari, akina mama wenye kutunza nyumba au wengineo. Ebu angalia mifano michache.

Huenda mwanasayansi, au mtu anayependa mambo ya sayansi, akashangaa sana kujua kwamba, karibu miaka 2,200 kabla wanadamu kwa ujumla hawajakubali kwamba dunia ni mviringo (duara), Isaya nabii Mwebrania aliandika hivi: “Yeye [Mungu] ndiye anayeketi juu ya duara ya dunia.” (Isa. 40:22) Neno la Kiebrania lililotafsiriwa “duara” hapa ni hhug, nalo linaweza kutafsiriwa kuwa “anga” pia, kulingana na Concordance (fahirisi) ya Davidson. Tena, labda mtu anayependa mambo ya sayansi atakubaliana na Biblia akionyeshwa Ayubu 26:7, panaposema kwamba Mungu ‘anautundika ulimwengu pasipo kitu.’ Wanasayansi wanajua kwamba dunia haikalii kitu fulani ili kuizuia isianguke.

Tuseme tabibu amefikiwa na Mkristo mwenye kuwapa watu ushuhuda nyumba kwa nyumba. Je! si daktari huyo angependezwa sana kujua kwamba Biblia inakubaliana na kanuni inayosema afya ya mtu ya mwili inaweza kuharibiwa au kutengenezwa na maoni yake ya moyoni? Hakika atakubali kwamba kijicho, woga, pupa, chuki na mambo kama hayo yanaharibu afya ya mtu, lakini upendo, furaha, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole na kujiweza, yaani, matunda ya roho ya Mungu, yanampa mtu afya nzuri. (Gal. 5:22, 23) Unaweza pia kumwonyesha mithali ile inayosema: “Moyo uliochangamka ni dawa nzuri; bali roho iliyopondeka hukausha mifupa.” (Mit. 17:22) Tena, huenda daktari akapendezwa kujua kwamba mmoja wa waandikaji Biblia, yaani, Luka, alitajwa katika Maandiko kuwa “yule tabibu mpendwa.”​—Kol. 4:14.

Una mambo mengi ya kumwambia mama mtunza nyumba unapotaka kumweleza habari za Biblia. Tuseme unataka kurudia mwanamke aliyeonyesha kwamba anapendezwa na Maandiko. Unaweza kuongea naye juu ya kazi za nyumbani, naye huenda akapendezwa sana kujua habari za “mke mwema,” anayesimuliwa katika Mithali 31:10-31. Mke huyo anasemekana kwamba anaangalia sana mavazi yanayovaliwa na watu wa jamaa yake, anawapikia chakula kizuri na kusimamia mambo ya kinyumbani kwa njia nzuri. Yeye ni mwenye bidii na uhodari wa kufanya kazi, tena ni mkarimu na hutendea watu wasio wa nyumba yake mambo mema. Huenda mwanamke wa kisasa akashangaa kujua kwamba Biblia inaeleza habari nyingi sana za kinyumbani. Tena huenda akafurahishwa na maneno yanayosema kwamba “uzuri wa sura unaweza kudanganya, na urembo unaweza kuwa bure; lakini mwanamke anayemwogopa Yehova ndiye anayejipatia sifa.”​—Mit. 31:30, NW.

Yako mambo mengi pia ya kutumia wakati wa kuongea na watoto habari za Biblia. Wakati unapozungumza habari za Biblia na watoto, huenda ikafaa uwaonyeshe sana uhitaji wa kuepuka kiburi, kufanya mema na kuwa wanyenyekevu. Labda unajua kwamba hadithi nyingi za watoto zinaanza kwa maneno haya, “Siku moja.” Basi, unabii wa Yothamu mwana wa Gideoni ulianza kwa kutumia maneno ayo hayo. “Siku moja,” akasema Yothamu, “miti ilitoka ili kuutia mmoja mafuta uwe mfalme juu yao.” Hapo mzeituni, mtini na mzabibu ulikataa kupewa cheo cha utawala, lakini mti mdogo wa miiba ukakubali cheo hicho. Miti hiyo bora ilifananisha watu wenye kustahili lakini wasiotafuta cheo cha kuwa mfalme juu ya Waisraeli wenzao, na hali mti huo mdogo wa miiba, uliofaa kutumiwa kama kuni tu, uliufananisha ufalme wa Abimeleki, aliyekuwa mtu mwenye kiburi na mwuaji, akataka kutawala watu wengine kwa nguvu lakini akauawa ili kutimiza unabii wa Yothamu. (Amu. sura ya 9) Ni mtoto gani angependa kukua akiwa kama mti huo wa miiba?

‘KUTUMIA KWA HALALI NENO LA KWELI’

Hakika yako mambo mengi yenye kupendeza katika Neno la Mungu. Lakini Mkristo anahitajiwa ajitahidi ndipo aweze kuwa na ujuzi mwingi wa kuutumia ‘upanga wa roho ambao ni neno la Mungu.’ (Efe. 6:17) Basi, mtume Paulo alikuwa na sababu nzuri ya kumsihi Timotheo mfanya kazi mwenzake hivi: “Jitahidi kujionyesha kuwa umekubaliwa na Mungu, mtenda kazi asiye na sababu ya kutahayari, ukitumia kwa halali neno la kweli.”​—2 Tim. 2:15.

Hakika mtu atapata faida akimwomba Yehova Mungu hekima ya kuweza kueleza watu habari za Biblia. Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Mtu wa kwenu akipungukiwa na hekima, na aombe dua kwa Mungu, awapaye wote kwa ukarimu, wala hakemei; naye atapewa.” (Yak. 1:5-8) Wakristo wanatakiwa wazidi kuyafahamu mafundisho yanayopatikana katika Maandiko. Lakini, wanapoendelea kulisoma Neno la Mungu kwa ukawaida, wanaona masimulizi mengi, maneno na semi zenye hekima zitakazopendeza watu wa namna zote za maisha. Waeleze kwa bidii mambo mema ambayo wewe Mkristo umejifunza, na kwa njia hiyo uwatie moyo wao pia waisome Biblia. Uwe na uhakika wa kwamba Yehova atakuwa pamoja nawe unapoeleza watu habari za Biblia.​—Matendo 11:19-21.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki