Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w96 5/15 kur. 10-15
  • Jitoe Mwenyewe kwa Usomaji

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jitoe Mwenyewe kwa Usomaji
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Mwenye Furaha Ni Yeye Asomaye kwa Sauti Kubwa”
  • Fikiri kwa Bidii na Utafakari
  • Shirikisha Mambo Mapya na Yale ya Zamani
  • Piga Picha Akilini Matukio ya Kimaandiko
  • Kujifunza Masomo Yenye Thamani
  • Nufaikeni Kutokana na Kusoma Biblia Mkiwa Familia
  • Kusoma na Huduma ya Kikristo
  • Kusoma Biblia pamoja na jamaa yako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Jitahidi Uwe Msomaji Mzuri
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
  • Kunufaika kwa Usomaji wa Biblia Kila Siku
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Usomaji wa Biblia—Wenye Kufaidi na Wenye Kupendeza
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
w96 5/15 kur. 10-15

Jitoe Mwenyewe kwa Usomaji

“Hata nitakapokuja, ufanye bidii katika kusoma na kuonya na kufundisha.”—1 TIMOTHEO 4:13.

1. Tunaweza kupataje manufaa kutokana na kusoma Biblia?

YEHOVA MUNGU amewapa wanadamu uwezo wa ajabu wa kujifunza kusoma na kuandika. Pia ameandaa Neno lake, Biblia, ili tuweze kufundishwa vizuri. (Isaya 30:20, 21) Kitamathali, kurasa zayo hutusaidia “kutembea” pamoja na wazee wa ukoo wenye kumhofu Mungu kama Abrahamu, Isaka, na Yakobo. Twaweza “kuona” wanawake wa kimungu kama Sara, Rebeka, na Ruthu Mmoabi aliyekuwa mwaminifu-mshikamanifu. Ndiyo, nasi twaweza “kusikia” Yesu Kristo akitoa Mahubiri ya Mlimani. Twaweza kupata raha hiyo yote na mafundisho matukufu kutoka kwa Maandiko Matakatifu ikiwa sisi ni wasomaji wazuri.

2. Ni nini kinachoonyesha kwamba Yesu na mitume wake waliweza kusoma vizuri?

2 Bila shaka, mtu mkamilifu Yesu Kristo alikuwa na uwezo bora wa kusoma, na hakika yeye alijua Maandiko ya Kiebrania vizuri sana. Basi, aliposhawishiwa na Ibilisi, Yesu aliyarejezea kwa kurudia-rudia akisema, “Imeandikwa.” (Mathayo 4:4, 7, 10) Pindi moja katika sinagogi huko Nazareti, yeye alisoma mbele ya watu wote na kuhusisha sehemu ya unabii wa Isaya kwake mwenyewe. (Luka 4:16-21) Vipi juu ya mitume wa Yesu? Katika maandishi yao, mara nyingi walinukuu Maandiko ya Kiebrania. Ingawa watawala wa Wayahudi waliwaona Petro na Yohana kuwa wasio na elimu na watu wa kawaida tu kwa sababu hawakuelimishwa katika shule za Kiebrania za masomo ya juu, barua zao zilizopuliziwa kimungu kwa wazi zilithibitisha kwamba wao waliweza kusoma na kuandika vema. (Matendo 4:13) Lakini, je, kweli uwezo wa kusoma ni muhimu?

“Mwenye Furaha Ni Yeye Asomaye kwa Sauti Kubwa”

3. Kwa nini ni muhimu sana kusoma Maandiko na vichapo vya Kikristo?

3 Kutwaa na kutumia ujuzi sahihi wa Maandiko kwaweza kutokeza uhai wa milele. (Yohana 17:3) Basi Mashahidi wa Yehova hutambua kwamba ni muhimu sana kusoma na kujifunza Maandiko Matakatifu na vichapo vya Kikristo vinavyoandaliwa na Mungu kupitia jamii ya mtumwa mwaminifu mwenye akili ya Wakristo watiwa-mafuta. (Mathayo 24:45-47) Kwa hakika, kwa kutumia vichapo vya Watch Tower vilivyotayarishwa kipekee, maelfu ya watu wamefundishwa kusoma na hivyo kupokea ujuzi wa Neno la Mungu wenye kuleta uhai.

4. (a) Kwa nini kusoma, kujifunza, na kutumia Neno la Mungu hutokeza furaha? (b) Kwa habari ya usomaji, Paulo alimwambia Timotheo nini?

4 Furaha hutokana na kusoma, kujifunza, na kutumia Neno la Mungu. Ndivyo ilivyo kwa sababu kwa kufanya hivyo sisi humfurahisha na kumheshimu Mungu, hupokea baraka yake, na kupata shangwe. Yehova hutaka watumishi wake wawe na furaha. Hivyo, yeye aliwaamuru makuhani wasome Sheria yake kwa watu wa Israeli la kale. (Kumbukumbu la Torati 31:9-12) Mnakili Ezra na wengine waliposoma Sheria mbele ya watu waliokusanyika Yerusalemu, maana yayo ilidhihirishwa, na tokeo likawa “furaha nyingi.” (Nehemia 8:6-8, 12) Mtume Mkristo, Paulo, baadaye alimwambia mfanyakazi mwenzake Timotheo: “Hata nitakapokuja, ufanye bidii katika kusoma na kuonya na kufundisha.” (1 Timotheo 4:13) Tafsiri nyingine husema: “Jitoe mwenyewe kwa usomaji wa Maandiko mbele ya watu wote.”—New International Version.

5. Ufunuo 1:3 huunganishaje furaha pamoja na usomaji?

5 Jambo la kwamba furaha yetu hutegemea kusoma na kutumia Neno la Mungu ladhihirishwa kwenye Ufunuo 1:3. Hapo twaambiwa hivi: “Heri asomaye [“Mwenye furaha ni yeye asomaye kwa sauti kubwa,” NW] na wao wayasikiao maneno ya unabii huu, na kuyashika yaliyoandikwa humo; kwa maana wakati u karibu.” Ndiyo, twahitaji kusoma kwa sauti kubwa na kusikia maneno ya Mungu ya kiunabii katika Ufunuo na katika Maandiko yote. Mtu ambaye kwa kweli ni mwenye furaha ni yule ambaye “sheria ya BWANA ndiyo impendezayo, na sheria yake huitafakari mchana na usiku.” Tokeo ni nini? “Kila alitendalo litafanikiwa.” (Zaburi 1:1-3) Basi, kwa sababu nzuri, tengenezo la Yehova huhimiza kila mmoja wetu kusoma na kujifunza Neno lake akiwa peke yake, wakiwa familia, na pamoja na marafiki.

Fikiri kwa Bidii na Utafakari

6. Yoshua aliagizwa asome nini, na kufanya hivyo kulikuwaje na manufaa?

6 Unaweza kufaidikaje zaidi na usomaji wako wa Neno la Mungu na vichapo vya Kikristo? Yaelekea utapata kuwa ni jambo lenye manufaa kufanya yale aliyofanya Yoshua, kiongozi wa Israeli la kale aliyemhofu Mungu. Yeye aliamriwa: “Kitabu hiki cha torati kisiondoke kinywani mwako, bali yatafakari [“uyasome kwa sauti ya chini,” NW] maneno yake mchana na usiku, upate kuangalia kutenda sawasawa na maneno yote yaliyoandikwa humo; maana ndipo utakapoifanikisha njia yako, kisha ndipo utakapositawi sana.” (Yoshua 1:8) ‘Kusoma kwa sauti ya chini’ kwamaanisha kujisemea mwenyewe maneno kwa sauti ya chini. Huko ni msaada wa kukumbuka, kwa kuwa kunakazia habari akilini. Yoshua alipaswa kusoma Sheria ya Mungu “mchana na usiku,” au kwa ukawaida. Kulikuwa ndiko njia ya kufanikiwa na kutenda kwa hekima katika kutekeleza madaraka aliyopewa na Mungu. Kusoma Neno la Mungu kwa ukawaida hivyo kwaweza kukusaidia kwa njia iyo hiyo.

7. Kwa nini hatupaswi kukazia akili kusoma kwa kasi tusomapo Neno la Mungu?

7 Usikazie akili kusoma kwa kasi unaposoma Neno la Mungu. Ikiwa ulipanga kutumia wakati fulani kusoma Biblia au kichapo fulani cha Kikristo, soma kwa mwendo wa pole. Hili ni la maana sana unapojifunza ukiwa na lengo la kukumbuka mambo makuu. Unaposoma, fikiri kwa bidii. Changanua taarifa za mwandikaji wa Biblia. Jiulize, ‘Anakazia nini? Naweza kutumiaje habari hii?’

8. Kwa nini kuna manufaa kutafakari tunaposoma Maandiko?

8 Chukua wakati wa kutafakari unaposoma Maandiko Matakatifu. Kufanya hivyo kutakusaidia kukumbuka masimulizi ya Biblia na kutumia kanuni za Kimaandiko. Kutafakari Neno la Mungu na kwa kufanya hivyo ukikazia mambo makuu akilini pia kutakusaidia kusema kutoka moyoni, ukiwapa wauliza-maswali wanyoofu majibu sahihi badala ya kusema jambo ambalo huenda ukaghairi baadaye. Mithali moja iliyopuliziwa kimungu husema: “Moyo wa mwenye haki hufikiri jinsi atakavyojibu.”—Mithali 15:28.

Shirikisha Mambo Mapya na Yale ya Zamani

9, 10. Usomaji wako wa Biblia waweza kuboreshwaje kwa kushirikisha mambo mapya ya Kimaandiko pamoja na yale ambayo tayari unayajua?

9 Wakristo walio wengi ni lazima wakiri kwamba pindi moja walijua machache juu ya Mungu, Neno lake, na makusudi yake. Hata hivyo, leo wahudumu hao Wakristo, kuanzia uumbaji wa mwanadamu na kutumbukia kwake katika dhambi, waweza kueleza kusudi la dhabihu ya Kristo, waweza kueleza uharibifu wa mfumo huu mwovu wa mambo, nao waweza kuonyesha jinsi wanadamu watiifu watakavyobarikiwa kwa uhai wa milele katika dunia iliyo paradiso. Hilo lawezekana hasa kwa sababu watumishi hao wa Yehova wametwaa “ujuzi wenyewe wa Mungu” kwa kujifunza Biblia na vichapo vya Kikristo. (Mithali 2:1-5, NW) Polepole wao wameshirikisha mambo mapya waliyojifunza pamoja na ya zamani ambayo tayari walikuwa wameyaelewa.

10 Kushirikisha mambo mapya ya Kimaandiko pamoja na yale ambayo tayari unayajua ni kwenye manufaa nako huthawabisha. (Isaya 48:17) Wakati sheria za Biblia, kanuni, au hata mawazo fulani yasiyo wazi sana yanapotokezwa, uyashirikishe pamoja na yale ambayo tayari unayajua. Patanisha habari hiyo na yale ambayo tayari umejifunza kuhusu “kielelezo cha maneno yenye uzima.” (2 Timotheo 1:13) Tafuta habari ambayo inaweza kukusaidia kuimarisha uhusiano wako na Mungu, kuboresha utu wako wa Kikristo, au kukusaidia kushiriki kweli za Biblia na wengine.

11. Unaweza kufanya nini unaposoma jambo ambalo Biblia husema juu ya mwenendo? Toa kielezi.

11 Unaposoma jambo fulani ambalo Biblia husema juu ya mwenendo, jaribu kufahamu kanuni ihusikayo. Litafakari, na uamue lile ungefanya chini ya hali kama hizo. Mwana wa Yakobo, Yosefu, sikuzote alikataa kujiingiza katika ukosefu wa adili pamoja na mke wa Potifa, akiuliza: “Nifanyeje ubaya huu mkubwa nikamkose Mungu?” (Mwanzo 39:7-9) Katika simulizi hili lenye kugusa moyo, unapata kanuni ya msingi—ukosefu wa adili ni dhambi dhidi ya Mungu. Unaweza kushirikisha kanuni hii akilini pamoja na taarifa nyinginezo zilizomo katika Neno la Mungu, nawe unaweza kuikumbuka na kunufaika nayo ukishawishiwa kujiingiza katika kosa kama hilo.—1 Wakorintho 6:9-11.

Piga Picha Akilini Matukio ya Kimaandiko

12. Kwa nini upige picha akilini masimulizi ya Biblia unapoyasoma?

12 Ili kukazia mambo akilini mwako unaposoma, piga picha akilini kile kinachotukia. Ona akilini mandhari, makao, na watu. Sikia sauti zao. Nusa mkate unaookwa katika tanuu. Wazia mandhari hizo tena. Ndipo usomaji wako utakapokuwa ono lenye kugusa moyo, kwa kuwa unaweza kuona jiji fulani la kale, kukwea mlima wenye kimo cha juu, kustaajabia maajabu ya uumbaji, au kushirikiana na wanaume na wanawake wenye imani kubwa.

13. Unaweza kufafanuaje yale yaliyorekodiwa kwenye Waamuzi 7:19-22?

13 Tuseme unasoma Waamuzi 7:19-22. Piga picha akilini kile kinachotukia. Mwamuzi Gideoni na wanaume mashujaa mia tatu wa Israeli wametwaa mahali pao ukingoni mwa kambi ya Wamidiani. Ni karibu saa nne za usiku, mwanzo wa “zamu ya kati.” Walinzi wa Wamidiani walikuwa wameanza tu kushika zamu, nalo giza lafunika kambi ya maadui wa Israeli wanaolala usingizi. Tazama! Gideoni na wanaume wake wana mabaragumu. Wao wana mitungi mikubwa inayofunika mienge wanayobeba katika mikono yao ya kushoto. Kwa ghafula, vikosi vitatu vya watu mia moja kila kimoja vyapiga mabaragumu, vyavunja mitungi, vyainua mienge juu, na kusema kwa sauti kuu: “Upanga wa BWANA na wa Gideoni.” Unatazama kambi. Wamidiani wote watoroka na kuanza kupiga makelele! Wale mia tatu waendeleapo kupiga mabaragumu yao, Mungu afanya panga za Wamidiani ziwe dhidi yao wenyewe kwa wenyewe. Wamidiani wametoroka, na Yehova amepatia Israeli ushindi.

Kujifunza Masomo Yenye Thamani

14. Waamuzi sura ya 9 yaweza kutumiwaje kufundisha mtoto uhitaji wa kuwa mnyenyekevu?

14 Kwa kusoma Neno la Mungu, twaweza kujifunza masomo mengi. Kwa kielelezo, labda unataka kukazia watoto wako uhitaji wa kuwa wanyenyekevu. Inapasa kuwa rahisi kupiga picha akilini na kuelewa kile kilichosemwa katika unabii wa Yothamu mwana wa Gideoni. Anza kusoma kwenye Waamuzi 9:8. “Siku moja,” akasema Yothamu, “miti ilitoka ili kuutia mmoja mafuta uwe mfalme juu yao.” Mzeituni, mtini, na mzabibu ikakataa kutawala. Lakini mti wa miiba wa hali ya chini ulifurahi kuwa mtawala. Baada ya kuwasomea watoto wako simulizi hilo kwa sauti kubwa, unaweza kueleza kwamba mimea yenye thamani iliwakilisha watu wenye ustahiki ambao hawakutafuta umaliki juu ya Waisraeli wenzao. Mti wa miiba, ambao ulifaa kutumiwa kama kuni tu, uliwakilisha utawala wa Abimeleki mwenye kiburi, muuaji-kimakusudi aliyetaka kudhibiti wengine lakini aliyekufa kwa utimizo wa unabii wa Yothamu. (Waamuzi, sura 9) Ni mtoto yupi angetaka kukua na kuwa kama mti wa miiba?

15. Umuhimu wa uaminifu-mshikamanifu wakaziwaje katika kitabu cha Ruthu?

15 Umuhimu wa uaminifu-mshikamanifu wadhihirishwa katika kitabu cha Biblia cha Ruthu. Tuseme washiriki wa familia yako wanasoma kwa zamu simulizi hilo kwa sauti kubwa na kujaribu kuelewa linalosema. Mwaona Ruthu Mmoabi akiwa safarini kwenda Bethlehemu akiwa pamoja na mama-mkwe wake aliye mjane, Naomi, nanyi mwasikia Ruthu akisema: “Watu wako watakuwa watu wangu, na Mungu wako atakuwa Mungu wangu.” (Ruthu 1:16) Ruthu mwenye bidii aonekana akiokota masazo nyuma ya wavunaji katika shamba la Boazi. Mwamsikia Boazi akimpongeza, akisema: “Mji wote pia wa watu wangu wanakujua ya kwamba u mwanamke mwema.” (Ruthu 3:11) Upesi, Boazi amwoa Ruthu. Kwa kupatana na mpango wa ndoa ya ndugu-mkwe, kupitia Boazi Ruthu amzaa mwana “[kwa] Naomi.” Ruthu awa mzazi wa kale wa Daudi na hatimaye wa Yesu Kristo. Kwa hiyo yeye alipokea “thawabu kamili.” Na zaidi, wale wanaosoma hilo simulizi la Kimaandiko hujifunza somo muhimu: Uwe mwaminifu-mshikamanifu kwa Yehova, na utabarikiwa sana.—Ruthu 2:12; 4:17-22; Mithali 10:22; Mathayo 1:1, 5, 6.

16. Wale Waebrania watatu walipitia mtihani gani, na simulizi hilo laweza kutusaidiaje?

16 Simulizi la Waebrania walioitwa Shadraka, Meshaki, na Abednego laweza kutusaidia kuwa waaminifu kwa Mungu katika hali zenye kujaribu. Piga picha akilini tukio hilo wakati Danieli sura ya 3, inaposomwa kwa sauti kubwa. Sanamu kubwa sana ya dhahabu yasimama katika uwanda wa Dura, ambako maofisa Wababilonia walikuwa wamekusanywa. Kwa mlio wa ala za muziki, wao waanguka na kuabudu sanamu ambayo Mfalme Nebukadreza alikuwa amesimamisha. Wote ila Shadraka, Meshaki, na Abednego wafanya hivyo. Kwa staha, lakini kwa uthabiti, wao wamwambia mfalme kwamba hawatatumikia miungu yake na kuabudu ile sanamu ya dhahabu. Waebrania hao wachanga watupwa ndani ya ile tanuri iliyopashwa moto kupita kiasi. Lakini ni nini ambalo latendeka? Akitazama ndani, mfalme aona wanaume wanne wenye nguvu, mmoja wao akiwa “mfano wa mwana wa miungu.” (Danieli 3:25) Wale Waebrania watatu waondolewa kutoka ndani ya tanuri, naye Nebukadreza abariki Mungu wao. Imethawabisha kupiga picha akilini simulizi hilo. Nayo yaandaa somo lililoje kuhusu uaminifu kwa Yehova chini ya jaribu!

Nufaikeni Kutokana na Kusoma Biblia Mkiwa Familia

17. Taja kifupi baadhi ya mambo yenye manufaa ambayo familia yako yaweza kujifunza kwa kusoma Biblia pamoja.

17 Familia yako yaweza kupata manufaa nyingi ikiwa mnatumia wakati kwa ukawaida kusoma Biblia pamoja. Ukianza na Mwanzo, mwaweza kushuhudia uumbaji na kuchungulia makao ya mwanadamu ya Paradiso ya awali. Mnaweza kushiriki mambo waliyoona wazee wa ukoo waaminifu na familia zao na kufuata Waisraeli wavukapo Bahari Nyekundu ikiwa imekauka. Mwaweza kuona kijana mchungaji Daudi akilishinda jitu Mfilisti Goliathi. Familia yako yaweza kuona ujenzi wa hekalu la Yehova katika Yerusalemu, yaweza kuona likifanywa ukiwa na majeshi ya Babiloni, na kuona likijengwa upya chini ya Gavana Zerubabeli. Pamoja na wachungaji wanyenyekevu karibu na Bethlehemu, mwaweza kusikia tangazo la kimalaika la kuzaliwa kwa Yesu. Mwaweza kupata mambo madogo-madogo kuhusu ubatizo na huduma ya Yesu, kumwona akitoa uhai wake wa kibinadamu ukiwa fidia, na kushiriki shangwe ya kufufuliwa kwake. Kisha mwaweza kusafiri pamoja na mtume Paulo na kutazama kuanzishwa kwa makutaniko huku Ukristo ukienea. Kisha, katika kitabu cha Ufunuo, familia yako yaweza kufurahia ono tukufu la mtume Yohana la wakati ujao, kutia ndani Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Kristo.

18, 19. Ni madokezo gani yanayotolewa kuhusu usomaji wa Biblia wa familia?

18 Ikiwa mnasoma Biblia kwa sauti kubwa mkiwa familia, mwisome kwa uwazi na kwa idili. Mnaposoma sehemu fulani za Maandiko, mshiriki mmoja wa familia—labda baba—huenda akasoma maneno ya usimulizi. Wengine wenu mwaweza kuchukua sehemu za wahusika wa Biblia, mkisoma sehemu zenu kwa hisia zifaazo.

19 Mnaposhiriki katika usomaji wa Biblia mkiwa familia, uwezo wenu wa kusoma waweza kuboreka. Yaelekea, ujuzi wenu juu ya Mungu utaongezeka, na hilo lapaswa kuwavuta karibu naye zaidi. Asafu aliimba: “Nami kumkaribia Mungu ni kwema kwangu; nimefanya kimbilio kwa Bwana MUNGU, niyahubiri matendo yako yote.” (Zaburi 73:28) Hili litasaidia familia yako kuwa kama Musa, ambaye “alistahimili kama amwonaye yeye asiyeonekana,” yaani, Yehova Mungu.—Waebrania 11:27.

Kusoma na Huduma ya Kikristo

20, 21. Utume wetu wa kuhubiri unahusianaje na uwezo wa kusoma?

20 Tamaa yetu ya kumwabudu “yeye asiyeonekana” yapaswa kutusukuma kufanyia kazi kuwa wasomaji wazuri. Uwezo wa kusoma vizuri hutusaidia kutoa ushahidi kutoka kwa Neno la Mungu. Kwa hakika hutusaidia kuendelea katika kazi ya kuhubiri juu ya Ufalme ambayo Yesu aliagiza wafuasi wake kuihusu aliposema hivi: “Enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu; na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi.” (Mathayo 28:19, 20; Matendo 1:8) Kutoa ushahidi ndiyo kazi kuu ya watu wa Yehova, na uwezo wa kusoma hutusaidia kuitimiza.

21 Jitihada inahitajika ili kuwa msomaji mzuri na mwalimu stadi wa Neno la Mungu. (Waefeso 6:17) Basi, ‘jitahidi kujionyesha kuwa umekubaliwa na Mungu, ukitumia kwa halali neno la kweli.’ (2 Timotheo 2:15) Ongeza ujuzi wako wa kweli ya Kimaandiko na uwezo wako ukiwa Shahidi wa Yehova kwa kujitoa mwenyewe kwa usomaji.

Majibu Yako Ni Yapi?

◻ Furaha hutegemeaje kusoma Neno la Mungu?

◻ Kwa nini utafakari juu ya yale usomayo katika Biblia?

◻ Kwa nini ushirikishe na kupiga picha akilini mambo unaposoma Maandiko?

◻ Ni yapi baadhi ya masomo ya kujifunza kutokana na usomaji wa Biblia?

◻ Kwa nini msome Biblia kwa sauti kubwa mkiwa familia, na kuna uhusiano gani kati ya kusoma na huduma ya Kikristo?

[Picha katika ukurasa wa 13]

Mnaposoma Biblia mkiwa familia, pigeni picha akilini masimulizi na kutafakari umaana wayo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki