Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w78 3/15 kur. 8-12
  • Kusoma Biblia pamoja na jamaa yako

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kusoma Biblia pamoja na jamaa yako
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • BAADHI YA FAIDA ZA KUFANYA HIVYO
  • KUUNGANISHA MAMBO MAPYA NA YA ZAMANI
  • JARIBU KUONA MATUKIO YA BIBLIA
  • KUONGEZA MOTO NA HALI YA KUPENDEZA
  • FAIDA ZENYE KUDUMU
  • Jitoe Mwenyewe kwa Usomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • “Mwanamke Bora Sana”
    Igeni Imani Yao
  • Mambo Makuu Katika Kitabu cha Ruthu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • “Mwanamke Bora Sana”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
w78 3/15 kur. 8-12

Kusoma Biblia pamoja na jamaa yako

HAKIKA Wakristo wanaiona Biblia kama zawadi kutoka kwa Mungu. Vilevile, wanapotimiza agizo walilopewa la kuzihubiri “habari njema hizi za ufalme,” wanataka sana kuitumia Biblia na kueleza watu ujumbe wake wenye faraja. (Mt. 24:14, NW; Rum. 15:4) Lakini wanatakiwa wasome na kujifunza Neno la Mungu kwa ukawaida ndipo waweze kueleza watu kwa njia nzuri.

Kuna wakati ambao jamaa nyingi zilikuwa zikisoma Biblia kwa ukawaida. Lakini, katika ulimwengu wa kisasa, ambamo mambo yanakwenda mbio-mbio, ambamo television na vitu vingine vinavuta kando fikira za watu, jamaa zimesahau sana kuisoma Biblia. Lakini namna gani jamaa ya Kikristo? Hakika utapata furaha nyingi kufaidika Kwa sababu hiyo, wavulana na wasichana walikua wakiwa wanajua hadithi za Biblia na kuweza kutumia kanuni za Maandiko katika maisha yao. usomapo Biblia pamoja na jamaa yako.

BAADHI YA FAIDA ZA KUFANYA HIVYO

Tuseme jamaa inatumia kipindi fulani cha jioni kila juma kusoma Biblia pamoja; labda saa nzima hivi. Juma zitakapoendelea kupita, watu wanaotajwa katika Biblia wataonekana kama watu halisi, nayo mambo ya kutazamisha yatakuwa kama kwamba yanaonekana pia. Loo, jamaa yenye kusoma Biblia inaweza kuona vitu mbali-mbali vikiumbwa na Muumba! Wanaweza kuona jinsi maskani ya kwanza ya mwanadamu ilivyokuwa katika hali ya paradiso. Wanaweza ‘kutembea’ pamoja na wazee wa ukoo kama Ibrahimu, Isaka na Yakobo. Wanaweza kuvuka Bahari ya Shamu na mto Yordani ukiwa mkavu, wakiwa pamoja na Waisraeli. Wanaweza ‘kuwapo’ wakati Daudi kijana mchungaji anapolishinda jitu la Kifilisti, Goliathi. Wasomaji wa Biblia wanaweza kuona hekalu la Yehova likijengwa Yerusalemu, wanaweza ‘kuona’ likiharibiwa na majeshi ya Kibabeli na kuona pia likijengwa upya chini ya usimamizi wa Liwali Zerubabeli.

Jamaa yenye kusoma Biblia inaweza ‘kusikia’ pamoja na wachungaji wanyenyekevu walio karibu na Bethlehemu malaika wakitangaza kuzaliwa kwa Yesu. Wanaweza ‘kumsikia’ Mungu akisema maneno ya kumkubali Mwanawe wakati anapobatizwa katika Mto Yordani. Wanaweza ‘kufuatana’ na Yesu na mitume wake, tena wanaweza ‘kuwapo’ wakati Yesu anapokufa, na wakati anapofufuliwa. Wanaweza kusafiri na mtume Paulo na ‘kuona’ makundi yakianzwa Korintho na kwingineko, huku Ukristo wa kweli ukienea wakati wa karne ya kwanza. Tena, wanaweza kuwa na mitume Yohana wakifurahia njozi nzuri sana juu ya wakati ujao, kutia na utawala wa miaka elfu wa Kristo, kama inavyoonyeshwa katika kitabu cha Ufunuo.

Vilevile, wakati wanajamaa wanaposoma Maandiko kwa zamu, uwezo wao wa kusoma unaweza kuongezeka. Lakini, jambo la maana zaidi ni kwamba watakuwa wakitwaa sheria na kanuni za Mungu wanapofanya hivyo. Wataweza kumkaribia Yehova zaidi, nao watazidi kumpenda. Ni kama vile wimbo wa Asafu uelezavyo: “Nami kumkaribia Mungu ni kwema kwangu; nimefanya kimbilio kwa Bwana [Yehova], niyahubiri matendo yako yote.” (Zab. 73:28) Hiyo itasaidia wanajamaa wawe kama Musa aliyeendelea kuwa “kama amwonaye yeye asiyeonekana.”​—Ebr. 11:27.

KUUNGANISHA MAMBO MAPYA NA YA ZAMANI

Bila shaka kila Mkristo atakubali kwamba kuna wakati mmoja ambao hakujua mambo mengi juu ya Yehova Mungu na makusudi yake. Lakini, leo anaweza kueleza tangu habari za uumbaji na kuingia kwa mwanadamu katika dhambi, juu ya kusudi la dhabihu ya ukombozi wa Kristo na uharibifu unaokuja wa taratibu hii ya mambo na hata kutumia Biblia kueleza jinsi paradiso itakavyorudishwa katika dunia hii na jinsi wanadamu watiifu watakavyoinuliwa wafikie ukamilifu. Amewezaje kufanya hivyo? Ameweza kwa sababu ameendelea kidogo kidogo kuunganisha mambo mapya na yale ya zamani aliyokwisha fahamu, kwa kujifunza Biblia na vitabu vya Kikristo.

Basi, wakati jamaa inaposoma Biblia, inaweza kupata faida nyingi kwa kuunganisha mambo mapya na yale waliyojifunza zamani. Bila shaka, mtu anatakiwa ‘ajiangalie jinsi asikiavyo.’ (Luka 8:18) Wakati jamaa inaposoma Biblia, usiache akili zako zife ganzi hata mambo ya maana yakupite bila kujua. Wakati maneno, kanuni, sheria au mawazo mbalimbali yasiyoweza kuonekana yanapotajwa, yaunganishe na mambo ambayo umekwisha jua. Zihusianishe habari hizo na ukweli unaofahamu. Linganisha mawazo kisha utafute habari mpya au tofauti, au zenye maelezo mengi zaidi, zinazoweza kukusaidia urekebishe kuwaza kwako au ueleze watu habari za kweli ya neno la Mungu.

Unaposoma habari za mwenendo wa kibinadamu, jaribu kuona kanuni zilizohusika. Unaweza kuzitafakari, kisha ukate maneno na kuamua vile wewe ungalifanya kama ungalikuwa katika hali kama hizo. Hilo ni jambo la maana weee! Kwa mfano, Yusufu mwana wa Yakobo alikataa mara nyingi kufanya uasherati na mke wa Potifa, akisema: “Nifanyeje ubaya huu mkubwa nikamkose Mungu?” (Mwa. 39:7-9) Hapa msomaji anaona kanuni fulani katika masimulizi ya kweli yenye kusisimua, kanuni anayoweza kufikiria na kuihusianisha na maneno mengine yaliyo katika Neno la Mungu, tena anaweza kuikumbuka imsaidie wakati ashawishwapo kufanya uasherati.

JARIBU KUONA MATUKIO YA BIBLIA

Wakati masimulizi fulani ya Biblia yanaposomwa, wanajamaa wanaweza kujaribu kujifanya kama kwamba wao wenyewe ndio waliomo katika tukio hilo. Habari zenyewe zikisomwa kwa uchangamshi, kwa njia moto-moto na kwa shauku, jamaa inaweza kuona linalotukia katika akili zao. Kujaribu kuona kisa kinachoendelea kutasaidia kila mmoja afahamu na kukumbuka mambo yaliyotokea zamani za kale.

Kwa mfano: Labda jamaa inasoma Waamuzi sura ya 7. Jaribu kuona jambo linalotukia. Kwa mfano, angalia mistari 19 mpaka 22. Gideoni na wale mashujaa mia tatu walio pamoja naye wamejipanga sasa hivi karibu na kambi ya Wamidiani. Ni karibu saa 4 ya usiku, mwanzoni mwa “zamu ya kati,” tena walinzi wamepangwa mahali pao sasa hivi. Giza limeikalia kambi ya adui waliolala, Gideoni na watu wake wana tarumbeta na mitungi ya maji iliyofunika mienge waliyoshika kwa mikono yao ya kushoto. Haya, kwa ghafula wale watu mia tatu wapiga tarumbeta zao na kuitupa mitungi yao na kuivunja vipande vipande. Halafu ‘unasikia’ mlio wa tarumbeta na mshindo wa kuvunjwa kwa mitungi. Vile vikosi vitatu vyenye askari mia moja kila kimoja vyapiga tarumbeta, vyavunjavunja mitungi ile mikubwa, kisha vyashika mienge yao na kuanza kupaza sauti wakisema: “Upanga wa [Yehova] na wa Gideoni”! Weee! unawaona’ na ‘kuwasikia’ wakifanya hivyo! Halafu waitazama kambi ya Wamidiani. Loo, huku Gideoni na watu wake mia tatu wameendelea kusimama mahali pao na kule kambi nzima yaanza kuondoka upesi, kisha yaanza makelele na kupiga mbio! Wale watu mia tatu waendelea kupiga tarumbeta kisha Yehova afanya Wamidiani waanze kukatana kwa panga katika kambi yao. Naam, Wamidiani wamekimbizwa. Yehova amewapa watu wake ushindi!

Tena, tuseme jamaa inasoma kitabu cha Biblia cha Ruthu. Unamwona Ruthu Mmoabu akifuatana na Naomi mama-mkwewe, ambaye ni mjane, kurudi Bethlehemu, kisha unamsikia Ruthu akisema: “Watu wako watakuwa watu wangu, na Mungu wako atakuwa Mungu wangu.” (Ruthu 1:16) Baada ya muda mfupi Ruthu anatia bidii akiokota masazo ya wavunaji katika shamba la Boazi. Baadaye Boazi amsifu, akisema: “Mji wote pia wa watu wangu wanakujua ya kwamba u mwanamke mwema.” (Ruthu 3:11) Boazi amwoa Ruthu kisha amzalia “Naomi” mwana kupatana na mpango wa ndoa ya kishemeji, naye awa ndiye bibi mkubwa wa Daudi, na mwishowe wa Yesu Kristo.​—Ruthu 4:17-22; Mt. 1:1, 5, 6.

Je! si watoto katika jamaa watapendezwa sana na hadithi ya wale Waebrania watatu waaminifu, Shadraki, Meshaki na Abednego? Hakika. Lakini labda baba anaweza kufanya masimulizi hayo yawe moto-moto anapoyasoma, huku akimtia moyo kila mtu ajaribu kuona mambo yanayotukia. Kwanza kuna lile jitu la sanamu ya dhahabu inayofika juu angani katika uwanda wa Dura! Maamiri, manaibu, maliwali, mawaziri na wakuu wengine wamekwisha kusanywa. Ishara yatolewa kwa kupiga ngoma za namna zote, kisha watu hao wote waanguka na kuiabudu sanamu ya dhahabu aliyoisimamisha Mfalme Nebukadreza. Watatu tu ndio wasiosimama. Shadraki, Meshaki na Abednego wamwambia mfalme kwa heshima na imara kwamba wao hawatatumikia miungu yake wala kuabudu sanamu hiyo ya dhahabu. Ndio hao, wanatupwa katika tanuru iliyowashwa moto isivyo kawaida. Lakini, ebu ngoja! Nebukadreza aona watu wanne mashujaa katika tanuru, na mmoja wao “ni mfano wa mwana wa miungu.” (Dan. 3:25) Wale Waebrania watatu waondolewa upesi katika tanuru ya moto, naye Nebukadreza amhimidi Mungu wao.

KUONGEZA MOTO NA HALI YA KUPENDEZA

Masimulizi ya Biblia kama hayo yanasisimua. Yanafundisha na kutia moyo. Tena, wakati ambao jamaa inasoma Biblia, inawezekana kuongeza moto na hali ya kupendeza kwa njia mbalimbali.

Kwanza, Biblia isomwe kwa kutamka maneno vizuri bila kumeza silabi za mwisho, na vilevile kwa uchangamshi, moto na shauku nyingi sana. Wakati wa kusoma sehemu fulani za Maandiko, huenda ikawezekana mwanajamaa mmoja​—labda baba​—asome maneno yale ya kawaida katika masimulizi, huku Wengine wakisoma sehemu zenye maneno yaliyosemwa na watu wanaotajwa katika Biblia. Wanajamaa wanaweza kugawiwa mapema sehemu za watu hao. Baba anaweza kusoma yale masimulizi ya kawaida mpaka atakapofikia maneno ya mtu fulani anayetajwa na Biblia. Halafu, mwanajamaa aliyepewa mgawo wa kuwa kama mtu huyo anaweza kusoma maneno yake kwa njia yenye kuonyesha maana halisi.

Kwa mfano, katika kitabu cha Ruthu, mwanajamaa mmoja anaweza kuwa katika sehemu ya Naomi, mwingine katika ya Ruthu. Mwingine naye anaweza kuwa katika sehemu ya Boazi, na vivyo hivyo. Vijana kwa wazee wanaweza kufurahia sana jambo hilo. Linaweza kuwasaidia kuikumbuka hadithi hiyo ya Biblia yenye kusisimua.

Hali ya kupendezwa itaongezeka jamaa ikirudia kujikumbusha, kuuliza maulizo na kuyajibu baada ya kusoma kisehemu fulani. Huenda neno fulani au maneno fulani yakawa hayakufahamika, au huenda usemi fulani ukahitaji kuelezwa waziwazi. Kwa kutumia Watch Tower Publications Index, au fahirisi nyinginezo zinazopatikana katika lugha yako, unaweza kupata majibu ya maulizo hayo ya Biblia. Vilevile, kitabu Aid to Bible Understanding kinaweza kuangaliwa, huku wanajamaa wakitazama vichwa vinavyofaa ili kuzungumza mambo yenye kupendeza sana. Kamusi itasaidia vijana wafahamu maana ya maneno. Kwa njia hiyo, usomaji wa Biblia unakuwa na uchunguzi mzuri wenye kuongezea jamaa maarifa ya Maandiko.

FAIDA ZENYE KUDUMU

Kila mmoja katika jamaa anaweza kupata furaha na faida kwa kusoma Biblia kwa ukawaida. Jamaa yote ikifanya hivyo, sheria na kanuni za Mungu zinaweza kukazika katika akili za wazee kwa vijana. Tena kila mmoja anaweza kujifunza jambo lenye faida katika masimulizi ya kweli yaliyoandikwa katika Neno la Mungu. Basi, ni jambo la maana sana kufikiri na kujichunguza wakati Biblia inaposomwa. Hata ikiwa habari zenyewe zinahusu mafundisho, unabii, au jambo jinginelo, wakati wa kusoma yapasa akili izuiwe kulala.

Baada ya kisehemu fulani kusomwa, kichwa cha jamaa anaweza kuuliza hivi: Jambo hilo linatuhusuje? Je! habari hizi zinatuhitaji tufanye mabadiliko yo yote katika maisha yetu? Jambo hili linahusianaje na mafundisho yale mengine ambayo tumekwisha jifunza? Tunawezaje kutumia mambo haya tunapowahubiri wengine “habari njema”?

Neno la Mungu lina mambo mengi sana ya kusomwa! Yale masimulizi juu ya Gideoni na watu wake mia tatu yanatufundisha kuwa na ushujaa na kumtegemea Yehova. Mfano mwema wa Ruthu wa kuwa na bidii na uaminifu unapasa uongoze mwanamke ye yote Mkristo awe kama yeye, yaani, awe “mwanamke mwema.” Na wakati wanapopatwa na majaribu ya ukamilifu wao shuleni, ni vijana gani Wakristo wasioweza kufaidika kwa kujikumbusha msimamo imara wa wale Waebrania watatu waaminifu? Vijana wenye kumcha Mungu wanafuata mfano wao kwa kusema wokovu una Yehova na kuepuka matendo ya ibada yanayoweza kumchukiza Baba yao wa mbinguni.​—Zab. 3:8.

Ikiwa jamaa yenu ni ya Kikristo na inaheshimu sana Neno la Mungu, someni Biblia kwa ukawaida. Mjifanye kama kwamba ninyi ndio watu wale wanaosimuliwa katika Biblia. Kazeni akilini sheria na kanuni za Maandiko. Tumia wakati ili upate furaha na faida inayopatikana kwa kusoma Biblia pamoja na jamaa yako.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki