Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w78 2/1 kur. 15-24
  • Kisa Cha Damu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kisa Cha Damu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Vichwa vidogo
  • NAMNA GANI WAKRISTO?
  • MASIKILIZANO KATI YA MGONJWA NA DAKTARI
  • KUONDOLEA MADAKTARI LAWAMA LA MAMBO YANAYOWEZA KUTOKEA
  • KUMTIBU “MWANADAMU MZIMA”
  • JE! MSIMAMO WA MASHAHIDI WA YEHOVA NI WA KIPUMBAVU?
  • KUPASUA KIUNGO KIKUBWA CHA MWILI BILA KUTUMIA DAMU
  • MITAJO
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
w78 2/1 kur. 15-24

Kisa Cha Damu

DAMU ni ya lazima kwa uhai. Ingawa jambo hilo limekubaliwa tangu kale, uchunguzi wa kisasa unatufahamisha mambo mengi zaidi juu ya vile inavyoendeleza uhai.

Madaktari (waganga) wamezoea sana kutia damu katika wanadamu. Wao pamoja na watu wengine wengi wanaona kwamba kutoa damu ya mwanadamu mmoja na kuitia katika mwanadamu mwingine ni utabibu mzuri unaokubaliwa.⁠1a Lakini kuna watu wasiokubali kutiwa damu. Watu hao ni Mashahidi wa Yehova.

Mashahidi wa Yehova wanathamini na kuheshimu sana uhai. Hiyo ndiyo mojawapo sababu zinazowafanya wasivute sigara, wasitumie dawa za kulevya zenye kuwapa mazoea mabaya, wala wasitoe mimba. Wamejifunza katika Biblia kuuona uhai kama kitu kitakatifu, kitu wanachopaswa kujilindia wenyewe na watoto wao.

Basi, kwa sababu gani Mashahidi wa Yehova wanakataa kutiwa damu? Je! kuna sababu nzuri inayowafanya wakatae damu hata wanapokuwa katika hatari ya kufa? Na je! maoni yao juu ya jambo hilo yanapingana kabisa na maarifa na kanuni za kisasa za utabibu?

Je! Biblia inakubali wanadamu watie damu katika miili yao?

Lazima hata watu wasioiona Biblia kuwa neno lililoandikwa kwa uongozi wa Mungu wakubali kwamba inaeleza mambo mengi juu ya damu. Tangu kitabu cha kwanza cha Biblia mpaka kile cha mwisho, “damu” imetajwa zaidi ya mara mia nne. Mistari fulani ya Biblia inaeleza hasa kama uhai unaweza kuendelezwa kwa kutumia damu. Acha tuichunguze kwa ufupi:

Maandishi ya Biblia yanaonyesha kwamba mwanzoni mwa historia ya mwanadamu Muumba na Mpaji-Uzima alitoa maoni yake juu ya damu. Upesi baada ya gharika iliyotokea duniani pote, wakati Mungu alipowapa wanadamu haki ya kula wanyama kwa mara ya kwanza, aliwaamuru Nuhu na jamaa yake hivi: “Kila kiendacho kilicho hai kitakuwa chakula chenu, kama nilivyowapa mboga za majani, kadhalika nawapeni hivi vyote. Bali nyama pamoja na uhai, yaani, damu yake, msile.”​—Mwa. 9:3, 4.

Kwanza, Muumba alikuwa akitoa sheria ya ulaji katika wakati ambao wanadamu walikuwa wakipata mwanzo mpya. (Linganisha Mwanzo 1:29.) Lakini, Mungu alionyesha kwamba si chakula peke yake kilichohusika wakati wa kuua wanyama. Sababu ni kwamba damu ya kiumbe ilifananisha uhai au nafsi yake. Basi, tafsiri fulani za Biblia zinatafsiri Mwanzo 9:4 kama hivi: “Lakini nyama na uzima wake, ndiyo damu yake, hamutakula.”​—Biblia ya Kiswahili ya Zaire.

Kwa hiyo sheria hiyo ya kimungu haikuwa katazo linalohusu chakula tu, kama vile daktari anavyoweza kushauri mgonjwa asiwe akitumia chumvi au mafuta. Muumba alihusianisha damu na kanuni ya adili iliyo ya maana sana. Kwa kumwaga kiasi cha damu ambayo ingeweza hasa kutoka katika mnyama, Nuhu na wazao wake wangeonyesha waliheshimu uhai kwa sababu ulitokana na Muumba, tena uliendelezwa na yeye. Lakini acha tuendelee kulichunguza jambo hili.

Andiko lililotajwa sasa hivi linahusu damu ya wanyama. Je! kanuni iyo hiyo ingetumika kuhusu damu ya mwanadamu? Ndiyo, tena ikiwa na nguvu zaidi. Hiyo ni kwa sababu Mungu aliendelea kumwambia Nuhu hivi: “Hakika damu yenu ya uhai wenu nitaitaka; . . . Atakayemwaga damu ya mwanadamu, damu yake huyo itamwagwa na mwanadamu; maana kwa mfano wake Mungu alimfanya mwanadamu.” (Mwa. 9:5, 6) Sasa, ikiwa damu ya mnyama (inayofananisha uhai wa mnyama) ni takatifu machoni pa Mungu, ni wazi kwamba damu ya mwanadamu ni takatifu hata zaidi. Watu wenye kufuata maagizo hayo ya kimungu wasingemwaga damu ya wanadamu (kwa kuwaua), wala wasingekula damu ya mnyama wala ya mwanadamu.

Lakini, je! amri hiyo aliyopewa Nuhu ilikuwa ya muda tu? Je! inahusu vizazi vya baadaye, pamoja na kizazi chetu?

Wanafunzi wengi wa Biblia wanatambua kwamba hapa Mungu aliweka sheria iliyohusu wanadamu wote, si kumhusu Nuhu na jamaa yake ya wakati huo tu, kwa maana wote wanaoishi tangu wakati wa Gharika ni jamaa ya Nuhu. (Mwa. 10:32) Kwa mfano, John Calvin, mwalimu wa dini aliyekubaliana na hatua ya kufanya matengenezo katika Kanisa Katoliki, alikubali kwamba “sheria hii ilipewa kwa ulimwengu mzima mara tu baada ya gharika.”⁠2 Naye Gerhard von Rad, mtaalamu katika Chuo Kikuu cha Heidelberg, anasema kwamba Mwanzo 9:3, 4 ni “amri kwa wanadamu wote,” kwa sababu wanadamu wote wametoka kwa Nuhu.⁠3

Namna gani damu ya wanyama wanaouawa kwa kusudi la kuliwa, si kutolewa wawe dhabihu? Mungu aliwaambia waabudu wake kwamba mwindaji aliyenasa mnyama-mwitu au ndege “atamwaga damu yake, na kuifunika mchanga. Kwa maana kuliko huo uhai wa mnyama, hiyo damu yake ni moja na uhai wake; kwa hiyo naliwaambia wana wa Israeli, Msile damu ya mnyama wa aina yo yote; kwa kuwa uhai wa wanyama wote ni katika hiyo damu yake; atakayeila awaye yote atakatiliwa mbali.”‏​—Mambo ya Walawi 17:13, 14; Kumbukumbu la Torati 12:23-25.

Kumwaga damu hivyo hakukuwa desturi ya kidini tu; bali hilo ni jambo jingine lililoongezwa kwa sheria ambayo Nuhu alipewa na Mungu. Wakati mtu anapoua mnyama, inampasa ajue kwamba uhai wa mnyama huyo umetoka kwa Mungu, tena ni mali yake. Kwa kutoila damu, bali ‘kuimwaga’ juu ya madhabahu au chini katika nchi, Mwisraeli alikuwa kama anamrudishia Mungu uhai wa kiumbe hicho.

Kama Mwisraeli alidharau uhai uliofananishwa na damu, alionekana amefanya kosa kubwa sana. Mtu aliyedharau sheria hii ya damu kwa makusudi alipaswa ‘kukatiliwa mbali,’ kuuawa. (Mambo ya Walawi 7:26, 27; Hes. 15:30, 31) Mtu alikuwa na hatia ya kadiri fulani pia kwa sababu ya kula nyama yenye damu ya mnyama aliyekufa mwenyewe au aliyeuawa na mnyama-mwitu.​—Mambo ya Walawi 17:15, 16; linganisha Mambo ya Walawi 5:3; 11:39.

Inafaa kuepuka damu ya wanadamu pia?

Ndiyo. Inafaa kabisa iwe hivyo kwa sababu sheria ya Mungu ilikataza kula ‘damu ya aina yo yote.’ (Mambo ya Walawi 17:10.

NAMNA GANI WAKRISTO?

Jambo hilo lilizungumzwa mwaka 49 W.K., wakati wa kusanyiko la mitume na wanaume wazee wa Yerusalemu waliotumikia kama baraza kuu ya wazee kwa ajili ya Wakristo wote. Kusanyiko hilo lilifanywa ili kufikiria ulizo juu ya kutahiriwa. Baraza hiyo ya mitume iliamua kwamba haikuwa lazima watu wasio Wayahudi walioukubali Ukristo watahiriwe. Katika mazungumzo ndugu mzazi mmoja na Yesu, yaani, Yakobo, aliieleza baraza kwamba aliona lilikuwa jambo la maana watie katika uamuzi wao maneno yenye kusema, “wajiepushe na unajisi wa sanamu, na uasherati, na nyama zilizosongolewa, na damu.” (Matendo 15:19-21) Aliwaelekeza kwenye maandiko yaliyoandikwa na Musa huko nyuma, yanayoonyesha kwamba hata kabla ya Torati kutolewa, Mungu alikuwa amekataza watu wasifanye uasherati, wasifuate ibada ya sanamu wala wasile damu, wala nyama za wanyama wenye damu kwa sababu ya kusongolewa shingo.​—Mwa. 9:3, 4; 19; 1-25; 34:31; 35:2-4.

Makundi ya Kikristo yalipelekewa barua yenye kuyaeleza uamuzi uliofanywa na baraza hiyo. Sasa uamuzi huo umo katika Biblia, na ni sehemu ya Maandiko yaliyoongozwa kwa uongozi wa Mungu, yanayofaa “kwa mafundisho . . . kwa kuwaongoza” watu, au “kunyosha mambo,” kulingana na tafsiri ya New World. (2 Tim. 3:16, 17) Uamuzi huo ndio huu:

“Roho takatifu na sisi wenyewe tumependelea tusiwaongezee mzigo zaidi, isipokuwa mambo haya ya lazima, kuendelea kushika mwiko wa vitu vinavyotolewa dhabihu kwa sanamu na wa damu na wa vitu vinavyonyongwa na wa uasherati. Ikiwa kwa uangalifu mtajiepusha na vitu hivi, mtafanikiwa.”​—Matendo 15:28, 29, NW.

Amri ya ‘kujiepusha na damu’ haikuhusu ulaji tu bali ilikuwa takwa la adili lisilo la kuchezewa na Wakristo, kwa maana kuepuka kula damu kulikuwa jambo zito kama ‘kuepuka ibada ya sanamu au uasherati.’

Eusebius, mwandikaji wa karne ya tatu anayefikiriwa kuwa “baba wa historia ya Kanisa,” anaeleza jambo lililotukia katika Lyons (ambayo sasa imo katika Ufaransa) mwaka 177 W.K. Watu wenye kuchukia dini walishtakia Wakristo uongo wakisema kwamba walikula watoto wachanga. Wakati Wakristo fulani walipokuwa wakiteswa sana mwilini na kuuawa, msichana aliyeitwa Biblias alijibu shtaka hilo la uongo, akasema: “Tunawezaje kula watoto wachanga​—na hali ni haramu kwetu kula damu ya wanyama.”⁠7

Historia ina ushuhuda mwingi ulio wazi kuhakikisha jambo hilo, hata Askofu John Kaye (aliyeishi kuanzia mwaka 1783 mpaka 1853) angeweza kusema hivi waziwazi: “Wakristo wasiokuwa wamestaarabika walijiangalia sana wakafuata agizo lililotangazwa na Mitume katika Yerusalemu, wakajiepusha na vitu vilivyosongolewa, na damu pia.”⁠11

Je! maneno ya Biblia yaliyotajwa yanakataza watu wasikubali kutiwa damu kwa kusudi la kuokoa uhai wao?

Kwa mfano, iangalie amri inayowaambia Wakristo ‘waendelee kushika mwiko wa damu.’ (Matendo 15:29, NW) Hakuna jambo lililotajwa katika amri hiyo kuonyesha kwamba mtu ana haki ya kutofautisha kula damu kwa mdomo na kutiwa katika mishipa. Kwa kweli, kuna tofauti yo yote kati ya njia hizo mbili za kutumia damu?

Madaktari (waganga) wanajua kwamba mtu anaweza kulishwa mdomoni au mishipani. Vivyo hivyo, dawa fulani zinaweza kuingizwa mwilini kwa njia mbalimbali. Kwa mfano, dawa zenye kuua vijidudu zinaweza kumezwa mdomoni ikiwa ni tembe au zinaweza kuingizwa katika minofu ya mwili au damuni kwa kutungwa sindano mishipani. Namna gani kama ungekuwa umemeza tembe fulani ya kuua vijidudu, lakini ukaonywa ujiepushe na dawa hiyo wakati ujao kwa sababu inakuwa na matokeo mabaya ndani yako? Lingekuwa jambo la akili kusema onyo hilo lina maana ya kwamba huwezi kuimeza tembe hiyo, lakini unaweza kuipitisha damuni kwa kutungwa sindano yenye dawa hiyo? Ni vigumu! Jambo la maana lisingekuwa njia ya kuitumia dawa hiyo, bali lingekuwa ni kujiepusha nayo kabisa. Vivyo hivyo, agizo linalosema lazima Wakristo ‘wajiepushe na damu’ linahusu kuingiza damu mwilini, kupitia mdomoni au mishipani.

Kisa hicho ni chenye ubora gani kwa Mashahidi wa Yehova?

Huenda watu fulani wanaofanya maamuzi bila kufikiria matokeo yake wakatia shaka wakisema kwamba kutii sheria ya Mungu juu ya damu hakuna ‘faida.’ Lakini Mashahidi wa Yehova wana hakika kwamba watapata faida za milele kwa kutii maagizo yanayotolewa na Muumba wao.

Hayo yalikuwa maoni ya Wakristo wa kwanza pia. Historia inaonyesha kwamba nyakati nyingine walijaribiwa vikali sana wasimtii Mungu. Katika Milki ya Rumi walikazwa wafanye matendo ya kuabudu sanamu au ya uasherati. Kukataa kufanya hivyo kungeweza kuwafanya waingizwe katika uwanja wa Kirumi wa michezo hatari ili kuraruliwa na wanyama wakali. Lakini Wakristo hao walishikamana na imani yao; walimtii Mungu.

Fikiria yaliyohusika. Kama Wakristo wa kwanza waliokuwa wazazi wangekataa kuvunja sheria ya Mungu, watoto wao wangeweza hata kuuawa. Lakini tunajua kutokana na historia kwamba Wakristo hao hawakuacha kumfuata Mungu wala kanuni zilizoongoza maisha yao kwa sababu ya woga na ukosefu wa imani. Waliyaamini maneno ya Yesu: “Mimi ndimi huo ufufuo, na uzima. Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa anaishi.” (Yohana 11:25) Kwa hiyo, ijapokuwa Wakristo hao wangeweza kupatwa na mabaya wakati huo, walitii agizo lililotolewa na mitume wakajiepusha na vitu vilivyotolewa dhabihu kwa sanamu, uasherati na damu. Waliona lilikuwa jambo la maana sana kufanya hivyo ili wawe waaminifu kwa Mungu.

Mashahidi wa Yehova leo wanaliona kuwa jambo la maana sana pia. Wanajiona wana haki ya kujifanyia wenyewe na watoto wao maamuzi yanayohusu ibada. Kwa hiyo, Mashahidi wa Yehova hawategemei mtu ye yote, awe ni daktari, msimamizi wa hospitali au hakimu, awafanyie maamuzi hayo. Hawataki mtu ye yote ajaribu kuwachukulia wajibu walio nao kwa Mungu, kwa maana hakuna mtu mwingine anayeweza kuwafanyia hivyo. Mkristo peke yake ndiye anayepaswa kujichukulia wajibu alio nao kwa Mungu wake na Mpaji-Uzima.

Inafaa tutie mkazo kwamba, ingawa Mashahidi wa Yehova hawakubali kutiwa damu, wanakubali kupewa matibabu ya namna nyingine yanayoweza kuokoa uhai wao bila kutiwa damu. Basi, kwa nini mtu ye yote asisitize au hata alazimishe mtu mwingine akubali matibabu yanayoharibu kabisa kanuni zake na imani zake za kidini anazothamini sana?

Lakini jambo hilo limetukia. Madaktari (waganga) fulani au wasimamizi wa hospitali hata wamekwenda mahakmani wakapewe ruhusa ya kutia watu damu kwa nguvu. Kwa habari ya wale ambao wamefanya hivyo, Dakt. D. N. Goldstein aliandika yafuatayo katika gazeti The Wisconsin Medical Journal:

“Madaktari wenye maoni hayo wamekataa kukubaliana na watu waliofia imani na kujulikana sana katika historia kwa sababu ya kushikamana sana na kanuni inayofaa hata kwa kupoteza maisha yao wenyewe. Wagonjwa wanaochagua kufa badala ya kuchafua dhamiri ya kidini wako sawa na wale waliokufa kwa sababu ya kumwamini Mungu au waliotundikwa mtini badala ya kukubali wabatizwe [kwa nguvu]. . . . Wajibu wetu ni kuokoa uhai lakini inatupasa pia kuwa na wajibu wa kulinda ukamilifu na haki za watu wachache wanaoendelea kujifanyia maamuzi yao wenyewe katika jamii inayozidi kufuata maoni na maamuzi ya wingi wa watu. . . . Hakuna daktari anayepaswa kuomba aruhusiwe na sheria kuokoa mwili kwa kuua nafsi. Uhai wa mgonjwa ni wake mwenyewe.”⁠23

Je! inampasa daktari aamue mambo kulingana na elimu yake na imani zake za udaktari akiona kwamba mgonjwa anahitaji damu ili uhai wake uokolewe, ingawa mgonjwa mwenyewe ameikataa?

Hakika nyakati kama hizo kunakuwa na tatizo kubwa. Lakini kila mmoja wetu anaweza kujiuliza hivi: Mimi nikiwa mgonjwa halafu daktari atake sana kunisaidia kwa kunipa matibabu yanayopingana na dhamiri yangu, ningefikiri ni njia gani inayopaswa kufuatwa? Yafikirie maelezo yaliyotolewa na Dakt. William P. Williamson katika kusanyiko lililojulikana kama First National Congress on Medical Ethics and Professionalism:

“Hakika, jambo la kwanza ambalo lazima daktari afikirie ni hali ya mgonjwa. Kwa kuwa uhai ni zawadi ambayo Muumba anampa mtu mwenyewe, mgonjwa ndiye mwenye haki ya kufanya uamuzi wa mwisho, kwa sababu mgonjwa huyo ndiye mwenye zawadi hiyo. . . . Inampasa daktari ampe mgonjwa matibabu yanayopatana na maagizo ya dini yake, wala asimlazimishe afuate imani zake mwenyewe za kidini.” (Maneno hayakuwa yamelazwa.)⁠24

Basi, daktari anaweza kufanya nini? Dakt. J. K. Holcomb alisema yafuatayo katika gazeti la mambo ya utabibu:

“Bila shaka sisi madaktari tunavurugika akilI hata kukasirika wakati mgonjwa mwenye moyo mgumu anapokataa matibabu tunayofikiri ndiyo mazuri zaidi. Lakini, inatupasa kweli tujisikie hivyo wakati mgonjwa anapokataa matibabu fulani kwa sababu ya imani yake ya kidini? Ikiwa sisi ni waaminifu, tutakubali kwamba kwa kawaida matibabu tunayowapa wagonjwa wengi siyo yaliyo bora zaidi. . . . Ikiwa tunaweza kufanya hivyo kulingana na imani zetu za udaktari, inatupasa pia tuwe na nia ya kujitahidi tuwezavyo kumsaidia mgonjwa ikiwa imani zake, hasa za kidini, zinatuzuia kumpa matibabu ambayo sisi tunaona yanafaa zaidi. Kwa kawaida, wagonjwa wanaokataa kutiwa damu kwa sababu za kidini, n.k. wanajua kwamba uamuzi wao unaweza kuwatia hatarini, lakini wanakuwa na nia ya kupatwa na hatari hizo, ila wanatuomba sisi tujitahidi tuwezavyo tu.”⁠27

MASIKILIZANO KATI YA MGONJWA NA DAKTARI

Watu wote wanaohangaikia jambo hili na wajue kwa hakika kwamba Mashahidi wa Yehova si wapinga-matibabu wanaoshikilia maoni yao wenyewe tu bila kufikiri sawasawa. Kumbuka kwamba Luka, aliyeandika masimulizi ya Biblia juu ya agizo lililotolewa kusema damu isitumiwe, alikuwa daktari. (Kol. 4:14) Basi, wakati Mashahidi wa Yehova wanapokuwa wagonjwa au wanapopatwa na mkasa (aksidenti), hawatafuti mtu wa kufanya miujiza na kuwaponya kwa sababu ya imani. Bali, wanawaendea madaktari. Wanapofanya hivyo hawajaribu kufundisha madaktari jinsi ya kufanya udaktari wala jinsi ya kutibu ugonjwa walio nao. Jambo la pekee wanaloagiza madaktari nyakati zote ni kwamba wasitumie damu.

KUONDOLEA MADAKTARI LAWAMA LA MAMBO YANAYOWEZA KUTOKEA

Mashahidi wa Yehova wana nia ya kujichukulia lawama la mambo yanayoweza kutokea kwa sababu ya kukataa damu. Wanakubali kutia sahihi hati za kisheria zenye kusema kwamba madaktari wala hospitali haitakuwa na hatia mabaya yakitokea kwa sababu ya kuwapasua bila kutumia damu.

Shirika la udaktari linaloitwa American Medical Association limependekeza wagonjwa wasiokubali damu kwa sababu ya imani za kidini wawe wakijaza karatasi inayoitwa “Kukataa Kutiwa Damu.” Inasema hivi: “Mimi (Sisi) nina- (tuna-) omba damu yo yote au vitu vilivyotengenezwa kwa kutumia damu visitiwe katika . . . . . . . . . . . . ... atakapokuwa hapa hospitalini, hata ikiwa daktari mwenye kumtibu au wasaidizi wake wanaona matibabu ya kutumia damu ni ya lazima ili kuokoa uhai wake au kumponya. Mimi (Sisi) nina- (tuna-) ondolea daktari mwenye kumtibu, wasaidizi wake, hospitali hii na wafanya kazi wake hatia yo yote ya mambo mabaya yanayoweza kutokea kwa sababu ya kukataa kwangu (kwetu) damu isitumiwe wala vitu vilivyotengenezwa kwayo.”⁠30 Hati hiyo itaandikwa tarehe na kutiwa sahihi (au kusainiwa) na mgonjwa pamoja na mashahidi waliopo. Mtu wa ukoo wa mgonjwa, anayehusiana sana naye kama mwenzi wa ndoa au mzazi (ikiwa mtoto ndiye mgonjwa), anaweza pia kutia sahihi katika karatasi hiyo.

Ni hakika kwamba Mashahidi wa Yehova wana nia ya kujichukulia lawama la msimamo wao wa damu kwa sababu wengi wao huwa wameweka mfukoni kadi waliyotia sahihi, yenye kusema “Sitaki Kutiwa Damu’.” Hati hiyo inasema kwamba mwenye kutia sahihi anajua na kukubali kwamba matatizo yanaweza kutokea kwa sababu ya kukataa damu. Kwa hiyo, hata akipelekwa kwa daktari au hospitalini akiwa amepoteza fahamu, hati hiyo aliyotia sahihi inaonyesha wazi msimamo wake imara.

Je! inampasa daktari ajisikie kwamba ni lazima amtie mtoto damu ijapokuwa wazazi na hata labda mtoto mwenyewe amekataa kabisa?

Kusema wazi kabisa, jambo linalofaa na la kanuni ni kwamba daktari atambue kuwa wazazi wenye upendo na wenye kuhangaikia watoto wao wadogo ndio wenye madaraka ya kuwafanyia maamuzi.

Yako mambo yanayoonyesha kwamba madaktari hawasemi mambo yanayopatana wanapotia mtoto damu kwa nguvu ingawa wazazi wake wameomba matibabu ya namna nyingine yatumiwe. Katika hospitali fulani, huenda katika chumba kimoja madaktari wakawa wanatia mtoto damu kwa nguvu. Lakini katika chumba kingine kilicho karibu huenda madaktari wengine wakawa wanatoa mimba za wanawake kulingana na sheria, wakiua vijitoto ambavyo ni vichanga kwa miezi michache tu kuliko yule mtoto anayetiwa damu kwa nguvu, ati kwa kusudi la ‘kuokoa uhai.’ Jambo hilo limefanya watu wenye akili washangae kama kweli nyakati zote madaktari hutia watu damu kwa nguvu wakiwa na kusudi la ‘kuokoa uhai.’

KUMTIBU “MWANADAMU MZIMA”

Madaktari wameanza kufahamu kwamba ni jambo la maana kumtibu “mwanadamu mzima.” Kinachopasa kutibiwa si kikoromeo wala ini tu, bali ni mtu mzima, yaani, mwanadamu aliye na mawazo na imani zinazoweza kumwongoza achague matibabu anayotaka. Katika gazeti Texas Medicine, Dakt. Grant Begley aliandika akasema “wakati mimi ninapotibu ugonjwa unaoambukia mwili, akili, na roho ya mtu ninayetibu, jambo lililo la maana kwangu ni vile yeye anavyoamini. Imani zake, wala si zangu, ndizo zinazomtia woga, mashaka, na hatia. Ikiwa mgonjwa wangu hataki kutiwa damu, jambo la maana kwangu si vile mimi ninavyomfikiria mtu huyo.”⁠42

Basi, daktari anapoheshimu imani za kidini za mgonjwa zinazohusu matumizi ya damu, anakuwa ametumia hekima na kumtibu “mwanadamu mzima.”

JE! MSIMAMO WA MASHAHIDI WA YEHOVA NI WA KIPUMBAVU?

Ingawa Mashahidi wa Yehova wanakataa kutiwa damu kwa sababu za kidini hasa, watu wengi wanauona msimamo wao kuwa wa kipumbavu. Kweli ni wa kipumbavu? Kwa kuwa Mashahidi wanakataa damu wanapopewa matibabu, tutapata faida tukichunguza kifupi sababu zinazowafanya wakatae.

Madaktari 800 wa Ulaya walikusanyika Paris wakakata maneno kwamba “mara nyingi mno damu inafikiriwa kuwa ‘nguvu za mwujiza’ anazopewa mgonjwa awe anazihitaji au hazihitaji.” Madaktari hao walikataza hasa kutia watu damu za painti moja moja, wakasema “haziwafai kitu watu 99 kati ya 100.”⁠44 Uchunguzi mmoja katika United States ulionyesha kwamba kati ya watu mia moja wanaotiwa damu katika maeneo fulani, 72 wanatiwa ‘bila kuihitaji au kwa njia yenye kutiliwa mashaka.’⁠45

Madaktari wanajua kwamba ni vigumu sana, sana, kufahamu jinsi damu ilivyotengenezwa. Ugumu huo unaonekana hata katika namna mbalimbali za damu. Vitabu vinaonyesha kwamba kuna aina kumi na tano mpaka kumi na tisa za damu. Kuhusu aina moja tu, yaani, ile ya aina ya Rh, kitabu kimoja cha karibuni kinachohusu habari za damu kilisema kwamba “kwa sasa inaweza kukisiwa kwamba kuna namna mbalimbali karibu mia tatu za damu ya aina ya Rh.”⁠47

Jambo jingine linalofanya damu ya kila mtu iwe vigumu kufahamika ni namna mbalimbali za chembe zake zinazoshambulia vitu vinavyoweza kuleta madhara.

Kwa kuwa damu ni kitu kigumu sana kufahamika, kinachotofautiana katika mtu na mtu, ni jambo la maana sana kufikiria matokeo yake katika mtu anayetiwa ya mwingine. Jambo hilo lilitajwa na Dakt. Herbert Silver wa Banki ya Damu na idara inayoshughulikia ukosefu wa damu katika Hartford Hospital (Connecticut). Aliandika akasema kwamba, kwa kufikiria zile damu zinazoweza kupimwa zionekane kama zinafaa, “kati ya visa 100,000 vya kutia watu damu, ni chini ya mtu 1 anayeweza kupata damu inayolingana na yake kabisa.”⁠49

Kitabu kimoja cha Serikali ya United States kilikuwa na makala yenye kuonyesha hatari za damu, kikasema kwamba

“ . . . kutoa damu isaidie mtu mwingine kunaweza kulinganishwa na kumpelekea mtu asiyejua neno, au asiye tayari, bunduki iliyojazwa risasi. . . . Kama vile bunduki iliyojazwa risasi ilivyo na kitu cha kuizuia isifyatuke, kuna njia fulani salama ya kutia watu damu za watu wengine. Lakini, ni watu wangapi wamekufa kwa sababu ya kujeruhiwa na bunduki wakidhani kile chombo chenye kuzuia risasi kilikuwa ‘salama’?”⁠52

Huenda mgonjwa wala jamaa yake wasizione hatari zinazohusika mpaka wanapokuwa wamechelewa mno. Dakt. J. Garrot Allen wa Chuo Kikuu cha Stanford, ambaye ni mkuu mwenye ustadi kuhusu tatizo la damu, alikadiri kwamba Waamerika wasiopungua 3,500 wanakufa kila mwaka na wengine 50,000 wanajeruhiwa wanapotiwa damu za watu wengine.⁠54 Lakini kuna uhakika kwamba hesabu hiyo imepunguzwa tu, haikutajwa yote hasa. Kwa mfano, gazeti Southern Medical Journal lilisema majuzi kwamba labda hesabu zinazoonyesha kwamba “kati ya vifo 3,000 na 30,000 vinatokana na kutia watu damu za wengine” hazionyeshi vifo vyote vinavyotokea.⁠55 Tena kumbuka hizo ni hesabu za nchi moja tu, wala hazionyeshi hesabu za nchi nyingine za ulimwengu.

Kutopatana kwa damu kunaharibu upesi sana chembe nyekundu za damu, na kunaweza kufanya figo zisifanye kazi, kumfanya mtu ashtuke na kufa.

Hasa ugonjwa unaoitwa Hepatitis B (kufura na kuwashwa maini kwa sababu ya majimaji ya damu yaliyo maangavu kuambukiwa na ugonjwa) unatokana na kutiwa damu. Huenda damu ya mtu aliyeitoa ikawa ina vijidudu vya ugonjwa huo, navyo vinaweza kuharibu afya ya mwenye kuipokea, au hata kumwua. Kadiri mtu anavyozidi kutiwa damu mara nyingi, ndivyo anavyoelekea zaidi kupatwa na ugonjwa huo. Lakini si lazima atiwe damu nyingi sana ndipo ugonjwa huo umpate. Hata kiasi kinachopungua tone moja kinaweza kukuambukiza; unaweza kupatwa na ugonjwa huo kutokana na damu iliyoambukiwa iliyo ndogo mara milioni kuliko milliliter moja.⁠60

Imesemwa mara nyingi kwamba katika United States kuna visa 30,000 vya watu wanaopatwa na ugonjwa wa kufura na kuwashwa maini kila mwaka kwa sababu ya kutiwa damu, kisha watu kati ya 1,500 na 3,000 wanakufa.⁠63 Kama hiyo ingalikuwa kweli, bado hilo lingalikuwa jambo la kusikitisha sana. Lakini, habari zilizotolewa na idara kuu ya kuzuia magonjwa zinaonyesha kwamba kila mwaka watu 200,000 au zaidi wanapatwa na ugonjwa wa Hepatitis B, ingawa hasa hiyo si hesabu kamili.⁠64 Tena ni nani anayeweza hata kukadiri jumla ya watu wanaoambukiwa na ugonjwa huo kwa sababu ya kutiwa damu katika Amerika yote ya Kaskazini na Kusini, Ulaya, Afrika na Asia?

Mambo yatakuwaje wakati ujao kwa sababu ya hatari zinazotokana na kutiwa damu? Dakt. John A. Collins wa Washington University School of Medicine anasema kwamba, “Kutakuwa na magonjwa mbali-mbali na hesabu yake itaongezeka, kisha huenda kukawa na wasiwasi mwingi wakati vijidudu vingi zaidi vinavyootesha uvimbe usiofaa katika sehemu za mwili vitakapokuwa vikionekana katika damu ya mwanadamu.”⁠74 Kwa hiyo, sasa hospitali nyingi zinahitaji mgonjwa atie sahihi katika hati au mapatano yenye kusema kwamba hatalaumu daktari wala hospitali kwa sababu ya mabaya yatakayotokea akitiwa damu.⁠75

Je! maoni hayo ya kidini yanayofuatwa na Mashahidi wa Yehova yanapingana sana na kanuni za wanadamu na maarifa ya udaktari hivi kwamba hayawezi kukubaliwa?

Ukweli ni kwamba, ingawa wanatumia Biblia kukataa damu, maoni yao yanaweza kukubaliwa mara nyingi kwa kutumia matibabu (dawa) ya namna nyingine.

Kama inavyojulikana sana, wakati mtu anapojifanyia uchaguzi wa kupasuliwa bila kutiwa damu, madaktari wanaweza ‘kuifanya damu ya mgonjwa iongezeke’ kabla ya kumpasua na baada ya hapo, kwa kutumia vitu kama maji yenye protein na michanganyiko ya vitu vingine vyenye chuma, vinavyoweza kuingizwa katika mwili wa mtu kwa kumtunga sindano⁠76b; kwa kufanya hivyo hakuwi na uhitaji mwingi wa kutia mtu damu. Kupunguza joto la mwili wa mgonjwa kumesaidia sana kumfanya asipoteze damu nyingi wakati wa kumpasua, na hata kumesaidia watoto wachanga.⁠78 Vivyo hivyo, kupunguza mkazo wa damu kunaweza kuzuia damu isitoke kwa wingi sana katika mishipa midogo wakati wa kupasua mtu. Labda matokeo yaliyo mazuri zaidi yamepatikana kwa sababu madaktari wamekuwa waangalifu sana wakaziba hata mishipa midogo sana iliyokatwa.

Ni baadhi ya majimaji gani yasiyo na damu yanayotumiwa badala ya kutia watu damu? Je! watu wanapotiwa maji hayo matokeo yanakuwa mazuri? Maji hayo yana faida gani?

Labda njia inayopatikana kwa wingi zaidi na inayotumiwa zaidi ili kurudisha maji ya damu ni saline solution (maji yenye chumvi, ya persenti 0.9%). Ni kazi nyepesi kutayarisha maji hayo yasiyo ya bei kubwa, yaliyo imara na yanayopatana vizuri na damu ya mwanadamu.⁠91 Ringer’s lactate (au Hartmann’s) ni namna nyingine ya chumvi inayoyeyushwa na kutia mkondo wa umeme katika chembe za mwili, nayo imetumiwa ikawa na matokeo mazuri katika watu walioungua sana, na wakati wa kupasua wagonjwa waliopoteza persenti 66 ya maji ya damu yao.⁠92

Njia nyingine ni kurudisha damu iliyopotea kwa kutumia vitu vyororo vyenye kushikamana-shikamana kama dextran. Hiyo ni namna ya sukari ambayo imesaidia sana katika kupasua watu na kuponya walioungua sana na walioshtuka.⁠93 Nyakati nyingine inachanganywa na namna ya chumvi iliyopunguzwa nguvu ili kuunganisha nguvu zote za vitu hivyo viwili. Vilevile majimaji yenye wanga yanayoitwa Haemaccel na hydroxyethyl starch solution (solution d’amidom) yametumiwa yakasaidia sana kueneza mwilini maji ya damu wakati wa kupasua watu.⁠94

Ingawa Mashahidi wa Yehova wanakataa damu wakiwa na sababu za kidini, wao hawakatai kuenezewa maji ya damu mwilini kwa kutumia vitu visivyo na damu. Basi, kulingana na maoni ya daktari, vitu hivyo vina faida kwa sababu vinaweza kutumiwa katika Mashahidi wagonjwa. Lakini ziko faida nyingine nyingi sana.

Mtaalamu E. A. Moffitt wa Canada aliandika akasema kwamba, “vitu ambavyo havikutengenezwa kutokana na viumbe vyenye uhai, vinavyotumiwa badala ya damu, vinaweza kutengenezwa kwa wingi na kuwekwa akibani kwa muda mrefu. . . . Vitu hivyo vinavyoeneza maji ya damu vina faida kwa sababu havileti hatari zinazotokana na kutiwa damu, yaani: vinazuia mtu asiambukiwe na viini au vijidudu vyenye magonjwa, wala asipatwe na mabadiliko mabaya yanayotokea mwilini . . .⁠97

Kuna faida nyingine kubwa ya kutumia vitu vyenye kueneza maji ya damu. Wakati damu ya mwanadamu inapowekwa akibani, lazima dawa fulani ziongezwe isije ikaganda na kushikamana. Baadaye wakati mgonjwa anapopewa damu hiyo, vitu vile vilivyoongezwa vinaweza kuharibu uwezo wa kuganda wa damu yake mwenyewe; basi mgonjwa anaweza kuendelea kupoteza damu. Dakt. Melvin Platt, anayepasua moyo, ameeleza kwamba tatizo hilo linaepukwa wakati “kitu cha namna ya peke yake” kama chumvi inayoitwa Ringer’s lactate solution kinapotumiwa, badala ya kutumia damu iliyokuwa imewekwa akibani.⁠98

KUPASUA KIUNGO KIKUBWA CHA MWILI BILA KUTUMIA DAMU

Madaktari wenye ushujaa ambao wamekubali kupasua Mashahidi wa Yehova bila kutumia damu wamejifunza mengi. Mfano mmoja ni upasuaji wa moyo uliofanywa majuzi. Hapo kwanza, damu nyingi sana ilikuwa ikitumiwa. Lakini kikundi cha madaktari wapasuaji chenye kuongozwa na Dakt. Denton Cooley katika Texas Heart Institute kiliamua kijaribu kupasua Mashahidi wa Yehova. Kwa kuwa madaktari wasingeweza kuwatia damu wakati wa kuwapasua wala baada ya hapo, wala wasingeweza kutumia lile bomba linalopiga-piga damu mwilini baada ya moyo kunyamazishwa, kwa sababu kabla halijaunganishwa na mwili wa mgonjwa linatiwa damu, walitumia vitu vyenye kueneza maji ya damu. Dakt. Cooley anasema: “Tulishangazwa sana na matokeo juu ya Mashahidi wa Yehova hata tukaanza kutumia njia hiyo kwa wagonjwa wetu wote wa moyo. Tumefaulu ajabu hata tukaitumia wakati wa kupandikiza watu mioyo ya watu wengine pia.”

Uchunguzi uliofanywa Canada ulieleza mambo kirefu, ukaonyesha kwamba wakati majimaji yasiyo na damu yalipotumiwa, kama dextran na Ringer’s solution, “hesabu ya vifo ilishuka kutoka persenti 11 kufika 3.8.”⁠101 Upasuaji wa namna hiyo umekuwa na matokeo mazuri juu ya Mashahidi wa Yehova na watoto wao katika Norway, Australia, Afrika, Kusini, Ufaransa, Uingereza na Japan.

Namna gani Mashahidi wa Yehova au watu wengine wanaotaka kutumia Neno la Mungu katika maisha yao?

Mazungumzo yetu juu ya kisa cha damu yapasa yafanye mtu azidi kuheshimu amri za Biblia zinazokataza kuendeleza uhai kwa kutumia damu.

Inafaa kila Mkristo akaze nia kuendelea kuwa imara katika imani yake. Wakati Mkristo anaposhughulika na wafanya kazi wa hospitali, inampasa awe na maoni ya kiasi na kuwa na roho ya masikilizano, lakini awaeleze waziwazi kwamba lazima matibabu yo yote watakayompa yapatane na imani zake za kidini, kama vile kukataa damu. Ikiwa kuna uhitaji wa kupasuliwa, litakuwa jambo la maana kuzungumza na madaktari mapema juu ya msimamo wa Kikristo kuhusu damu, ili kuhakikishiwa nao kwamba hawatatumia damu kamwe kamwe, wakati wa kumpasua wala baada ya hapo. Halafu ikiwa daktari fulani anaona hawezi kumpasua bila kutumia damu, Mkristo atakuwa amejua hivyo mapema na kutafuta msaada wa tabibu mwingine.

Wakati Mashahidi wa Yehova wanapojitahidi kuunga mkono sheria ya Mungu juu ya damu, wanathamini kwamba uhai wao umetoka kwa Muumba na Mpaji-Uzima, na kwamba unamtegemea Yeye. Ndiye amesema katika Biblia kwamba Mkristo anaweza kupata furaha na kuendelea kuishi wakati ujao kwa kuamini na kutii. (1 Yohana 2:3-6) Ndiyo sababu Wakristo wa kwanza walikuwa na nia ya kuhatirisha maisha yao ya wakati huo badala ya kutenda kinyume cha imani zao za kidini. Leo Mashahidi wa Yehova wamekaza nia kwa njia iyo hiyo waendeleze uhusiano mwema walio nao na Mungu. Kwa hiyo wataendelea kuitii amri ya Biblia inayosema ‘tushike mwiko wa damu.’​—Matendo 15:29, NW.

—Kutoka Kijitabu “Blood.”

MITAJO

1. The Gift Relationship (1971), kilichoandikwa na Mtaalamu Richard M. Titmuss, uku. 27.

2. Calvin’s New Testament Commentaries; The Acts of the Apostles, Vol. II, p. 50

3. Genesis​—⁠A Commentary (1961), kilichoandikwa na Gerhard von Rad, uku. 128.

7. The History of the Christian Church (1837), kilichoandikwa na William Jones, uku. 106.

11. The Ecclesiastical History of the Second and Third Centuries (1845), kilichoandikwa na John Kaye, Askolu wa Lincoln, uku. 146.

23. The Wisconsin Medical Journal, Agosti 1967, uku. 375.

24. The Journal of the American Medical Association, Septemba 5, 1966, kur. 794, 795.

27. The Cape County Journal, Juni 1967, uku. 5.

30. Medicolegal Forms with Legal Analysis (1976), uku. 85.

42. Texas Medicine, Desemba 1970, uku. 25.

44. Ouest-France, Machi 10, 1975.

45. Druys (1973), Vol. 6, uku. 130.

47. God, Blood and Society (1972), kilichoandikwa na A.D. Farr, uku. 32.

49. The Journal of the American Medical Association, Aprili 12, 1976, uku. 1611.

52. Oasis, Februari 1976, kur. 23, 24.

54. The National Observer, Januari 29, 1972, uku. 1.

55. Southern Medical Journal, Aprili 1976, uku. 476.

60. The Gift Relationship (1971), kilichoandikwa na Mtaalamu Richard M. Titmuss, uku. 142.

63. Annals of the New York Academy of Sciences, Januari 20, 1975, uku. 191.

64. The American Journal of the Medical Sciences, Septemba-Oktoba 1975, kur. 276, 281; Morbidity and Mortality Weekly Report, Mei 7, 1976,. uku. 3; Inspection News, Novemba​—⁠Desemba 1972, uku. 18.

75. Medicolegal Forms with Legal Analysis (1976), uku. 83.

76. The Journal of Thoracic and Cardiovascuiar Surgery, Julai 1974, uku. 3.

77. Mayo Clinic Proceedings, Novemba 1976, uku. 725.

78. Medical World News, Desemba 4, 1970, uku. 7.

91. Anaesthesia, Julai 1968, kur. 418, 419.

92. Annals of the New York Academy of Sciences, Agosti 14, 1968, uku. 905; The Journal of the American Medical Association, Machi 29, 1971, uku. 2077.

93. Blood Transfusion in Clinical Medicine (1972), kilichoandikwa na Mtaalamu P. L. Mollison, kur. 150, 153.

94. Surgical Clinics of North America, Juni 1975, uku. 671.

97. Canadian Anesthetists’ Society Journal, Januari 1975, uku. 12.

98. The Elks Magazine, Agosti 1976, uku. 14.

101. Gazeti Star la Toronto, Novemba 22, 1975, uku. A8.

[Maelezo ya Chini]

a Vitabu ambavyo vimetumiwa kueleza habari zilizomo vimetajwa mwishoni mwa makala hii.

b Uchunguzi unaonyesha kwamba kwa kutumia chuma katika matibabu, zile chembe nyekundu za damu zinaweza kuongezwa ziwe mara mbili au mara nne zaidi.⁠77

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki