Kisiwa Chenye Urafiki Chasikiliza—Ripoti Kutoka Sri Lanka
USEMI wa Yesu wa unabii kwamba habari njema za Ufalme ‘zingehubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda’ ulionyesha kungekuwa na kazi yenye kuenea pote. (Mt. 24:14, NW) Mojawapo ya nchi ambazo “habari njema” zimefika katika wakati huu wa mwisho ni kisiwa chenye urafiki cha Sri Lanka, kilichojulikana kama Ceylon mpaka hivi karibuni. Kisiwa hiki chenye umbo kama la tone la machozi, chenye ukubwa wa maili za mraba 25,322 (kilometres za mraba 65,584), ambacho kiko upande wa kusini wa Bara Hindi katika Bahari ya Hindi kina urefu wa maili 270 (kilometres 435) tu na upana wa maili 140 (kilometres 225).
Mwandikaji Mwamerika Mark Twain, aliyetembelea Sri Lanka katika mwaka 1896, aliueleza mji wake mkuu, Colombo, katika maneno haya: ‘Lo! ilikuwa ndoto kama nini ya uzuri wa sehemu zenye jua na uzuri wa mavazi ya Mashariki yanayometameta kama moto unaowaka! Vikundi vyenye kutembea vya wanaume, wanawake, wavulana, wasichana, vitoto—kila kikundi ni kama nyumba inayowaka moto kwa rangirangi.’ Mambo ya asili yenye kuvutia ya kisiwa hiki kizuri cha sehemu zenye jua, pamoja na urafiki wa ukaribishaji wa watu wake wenye furaha, unaonekana mpaka hivi sasa.
Kwa wale mashahidi wa Yehova 550 au zaidi walioko Sri Lanka, kuutangaza ufalme wa Mungu ni mgawo wenye kupendeza. Bila kujali mahali unapochagua kuhubiri “habari njema” katika kisiwa hiki, kwa kawaida watu wanakukaribisha katika nyumba zao. Unapoeleza ujumbe wa Biblia pamoja na ahadi yake ya wakati wake ujao wenye furaha kwa wanadamu, huenda ukapewa kikombe cha chai yenye kuburudisha ambayo imefanya nchi hii ijulikane sana. Vilevile, wahubiri wa ujumbe wa Ufalme wanakaribishwa katika mahekalu ya Wabuddha wazungumze juu ya tumaini linalotolewa na Biblia na kuhani mkuu pamoja na makuhani wadogo.
KUITIKIA “HABARI NJEMA”
Je! kutangazwa kwa “habari njema” na mashahidi Wakristo wa Yehova kumewasaidia Wabuddha, Mabanyani na Waislamu wajifunze na kuikubali kweli? Yamekuwako matokeo mema yanayopaswa kuangaliwa kati ya Mabanyani. Waliokuwa Mabanyani hapo zamani wamo kati ya watangazaji wa muda na wa wakati wote wa Ufalme katika makundi yao. Hata wazee na watumishi wa huduma fulani walikuwa Mabanyani hapo zamani. Mmoja kama huyo sasa ni mwangalizi katika kundi moja naye amekuwa na juhudi sana akaweza kumsaidia mkewe, dada zake na wakweze wajifunze kweli. Tatizo (gumu) lisilo la kawaida lilitokea kwa habari ya mama yake ambaye alikuwa amekuwa akitafuna popoo katika maisha yake yote. Meno yake yalikuwa yamelika kufikia fizi za kinywa chake, na mara tu alipoacha kuzitafuna, meno yake yalianza kuuma. Yeye hangestahili kubatizwa awe mmoja wa Mashahidi wa Yehova asipoacha kutafuna dawa hiyo ya kulevya ya popoo. Tatizo hilo lilimalizwaje? Tabibu wa meno alisaidia akang’oa vipande vya meno yake vilivyokuwa vimebaki. Ndipo alipobatizwa.
Wachache waliokuwa Wabuddha hapo zamani sasa ni wahubiri wa “habari njema” na mmoja hata anatumikia akiwa painia wa wakati wote. Ijapokuwa maendeleo kati ya Waislamu yamekuwa madogo sana, Mashahidi wa Yehova katika Sri Lanka wanafurahia uhakika wa kwamba mzee mmoja na mtumishi wa huduma mmoja hapo zamani walikuwa wafuasi wa dini ya Kiisilamu.
Vijana na wazee wanaona makosa ya mafundisho na mazoea ya taratibu za Makanisa ya Jumuiya ya Wakristo. Kushindwa kwao kutoa mafundisho yanayoridhisha kwa washiriki wao kunaonyeshwa na yaliyoonwa na kijana mmoja aliyekuwa na miaka kama 25 hivi aliyekuwa amezaliwa akiwa Mkatoliki. Alipokosa kuridhishwa na mafundisho ya kanisa lake, aligeukia dini ya Buddha ili apate majibu kwa maswali yake mengi. Lakini alikuwa bado hajafanya uamuzi. Ndipo mtu mmoja alipompa gazeti la Mnara wa Mlinzi. Katika upande wa nyuma wa jalada palikuwa na tangazo lililokuwa na kichwa “Je! Imani Yako Imetikisika?” Mara hiyo aliiandikia afisi ya tawi ya Sosaiti iliyoko katika nchi yake. Shahidi “painia wa pekee” alimtembelea nyumbani mwao akazungumza naye pamoja na wazazi wake juu ya imani. Leo washiriki wote watatu wa jamaa hii ni wahubiri wa “habari njema.” Mapainia wanaofanya kazi katika maeneo ya Wakatoliki wana mambo mengi mazuri yaliyoonwa kama hili wanayoweza kusimulia.
MAENDELEO BAADA YA KUPITA MIAKA
“Habari njema” zililetwa katika Sri Lanka kwa mara ya kwanza mapema sana katika mwaka 1910, wakati ambapo mbegu za kweli zilipandwa katika mioyo ya watu wachache wenye kupendezwa pamoja na jamaa zao. Katika mwaka wa 1912 Ndugu C. T. Russell, aliyekuwa wakati huo msimamizi wa International Bible Students Association, alitembelea nchi hii. Baadaye katika mwaka 1917 sinema iitwayo Photo-Drama of Creation ilionyeshwa katika miji ya Colombo na Kandy. Kwa miaka mingi maendeleo ya kweli yalikuwa madogo mpaka wamisionari walipotumwa kusaidia katika mwaka wa 1947. Tangu wakati huo kazi imesonga mbele ikiwa imesimamiwa vizuri zaidi, kukawa na matokeo.
Bidii pamoja na uvumilivu wa wamisionari waaminifu umesaidia sana kujenga makundi ya Mashahidi wa Yehova katika nchi hii. Leo kuna makundi 17 ya Mashahidi wa Yehova katika miji yote mikubwa kisiwani pote. Kilele cha wahubiri walioripoti katika mwaka 1977 kilikuwa 552. Watu 49 walibatizwa katika mwaka uo huo. Mashahidi wa Yehova katika Sri Lanka walikuwa na sababu ya kufurahi wakati kilele cha watu 1,662 walipohudhuria Ukumbusho wa mauti ya Yesu tarehe 3 Aprili, 1977 katika mahali mbalimbali 23 katika kisiwa hicho. Hudhurio hilo linaonyesha kwamba kuna uwezekano mzuri wa ongezeko zaidi katika wakati ujao.
Kuenezwa kwa trakiti za Habari za Ufalme, ambako huungwa mkono kwa shauku nyingi, kumesaidia kupeleka “habari njema” kwa watu wengi walio peke yao, wanaopendezwa sasa na ujumbe wa Biblia. Itikio lenye kutokeza sana lilionekana wakati wa kuenezwa kwa trakiti iliyokuwa ikiitwa “Namna Uvunjaji wa Sheria na Jeuri Vitakomeshwa.” Maombi mengi ya vitabu vya kujifunza Biblia yalitumwa katika afisi ya tawi ya Sosaiti katika Sri Lanka. Vilevile watu wengine waliomba mafunzo ya Biblia ya nyumbani, ambayo Mashahidi wenyeji walifurahia kuwatolea.
KUTOA USHUHUDA KATIKA MAENEO YA MASHAMBANI
Unapokaribia nyumba ya mashambani unaweza kuona watu waliomo wakitenda kwa haraka sana wanapowaletea kiti kimoja au viwili wewe na mwenzako mkalie. Kisha wanasimama kwa heshima sana wasikilize yale mnayosema. Mara nyingi watasisitiza mkae mpate kinywaji chenye kuburudisha cha kurumba au thambili, ambacho ni namna mbalimbali ya mnazi mchanga. Sehemu ya ndani ya matunda haya yana maji matamu sana nayo yanafurahisha sana kuyaonja. Unaweza kushangaa kwa vile unaweza kutumia kiasi kikubwa sana katika asubuhi moja unapoendelea kutangaza “habari njema” kwa bidii nyumba kwa nyumba katika sehemu hii yenye jua kali.
Nyakati nyingine shauku ya watu hawa wakaribishaji na wanyenyekevu wa mashambani inaweza kuvuta sana moyo, kama ilivyokuwa kwa Mashahidi painia wawili wanaohubiri eneo kama hili. Walimfikia mwanamke mmoja mzee aliyejulishwa ujumbe na kutolewa kitabu cha kumsaidia kujifunza Biblia. Yule mwanamke mzee aliingia ndani ya nyumba yake akarudi na fedha alizokuwa ameweka akiba zikiwa ndani ya chombo cha udongo. Alikifungua, ndani yake kukatoka sarafu (fedha) nyingi zenye thamani ndogo na zenye kung’aa. Kwa subira alihesabu sarafu hizo 150—zile zinazolingana na rupee tatu (Ksh. 1.50; 25K) za Sri Lanka, akawapa wale mapainia kama mchango wake kwa ajili ya kitabu hicho alichokuwa na hamu sana ya kukipata.
UCHAWI NA USHIRIKINA UNAENEA POTE
Watu wa jamii mbalimbali na wanaofuata dini mbalimbali wanajulikana kwamba wanafuata sana ushirikina. Mazoea ya uchawi yanayoenea pote yanawalazimu Wakristo wawe macho wasinaswe nao. Hii inaonyeshwa na jambo lililompata shahidi wa Yehova, ambaye mjukuu wake wa kike alikuwa ametumia mafuta fulani kutuliza kichwa kilichokuwa kikiuma. Mafuta hayo yalikuwa ya binti-mkwe wa Shahidi huyo ambaye ni mfuasi wa Buddha naye alikuwa ameyatoa hekaluni. Mara tu alipopaka mafuta hayo kichwani pake, mjukuu huyo wa kike ambaye ni shahidi wa Yehova aliye wakf, alianza kufanya mambo yasiyo ya kawaida. Alielekea kupotelewa na akili na alikuwa akiuliza-uliza nyanya yake maulizo, kama vile “Niko wapi?” “Wewe ni nani?” Nyanya alifahamu kwamba huenda ikawa ni kwa sababu ya mafuta hayo, kwa hiyo akayaosha na kuyaondoa mara moja. Tendo hilo lilikuwa na matokeo yaliyohitajiwa, kwa kuwa mtoto alirudiwa na akili zake.
Kwa kuwa watu wengi katika Sri Lanka wamenaswa na mazoea ya uchawi, mashahidi wa Yehova katika nchi hii wamefurahia sana kupata kitabu cha Kiingereza kilichochapwa hivi karibuni Good News to Make You Happy, kwa kuwa kitatosheleza mahitaji ya watu katika nchi hii ya Mashariki. Wengi wa wahubiri wanaoongea lugha ya Sinhal na ya Tamil wanangojea kitabu hiki katika lugha zao kwa hamu kubwa sana ili waweze kufundisha vizuri zaidi katika eneo lao.
KUITIKIA MWITO WA WAFANYA KAZI ZAIDI
Katika kuitikia mwito wa wafanya kazi zaidi katika mavuno ya mwisho, hesabu fulani ya vijana wameingia utumishi wa wakati wote wa “upainia.” (Mt. 9:38) Wengine hata wameacha kazi nzuri sana kwa sababu ya kuona uhitaji mkubwa ulioko wa wafanya kazi zaidi wa kusaidia kazi hii ya mwisho ya kukusanya. Kati ya hawa kuna vijana wawili waliooana walioacha kazi zao za kimwili wakachukua upainia wakatumwa kutumikia katika sehemu iliyokuwa na uhitaji mkubwa. Leo Wanafurahi kwa kuwa kundi limeanzishwa katika sehemu yaliyohitajiwa, kwa kuwa mtoto alirudiwa na hiyo.
Katika nchi hii si vyepesi kupata kazi ya muda kumsaidia ye yote ambaye angetaka kufanya kazi ya upainia wa kawaida huku akijitafutia riziki. Hata hivyo, hesabu fulani wamefanya mabadiliko fulani katika kazi zao ili waweze kushiriki zaidi katika kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. (Mt. 24:14; 28:19, 20) Wahubiri wengi wa “habari njema” wanaujaribu utumishi wa upainia kwa kuufanya kwa muda. Katika Aprili 1976, ambao ni mwezi shule hufungwa na kunakuwa na sikukuu nyingi, wahubiri wa Ufalme 79 walikuwa na kazi nyingi katika utumishi wa upainia wa kawaida na wa msaidizi.
MAKUNDI YENYE FURAHA YA WATU WA YEHOVA
Waangalizi wawili wasafirio wanaotembelea makundi wanaona furaha sana kutokana na mgawo wao kwa sababu ya roho nzuri sana ya upendo pamoja na ukaribishaji inayoenea pote. Mmoja wa wahudumu hawa wasafirio, anatembelea makundi kwa pikipiki pamoja na mke wake na wana wao wawili wachanga.
Watu wa Yehova katika Sri Lanka huenda wakawa si wengi sana, walakini wanafurahia ufanisi wa kiroho ambao unawatia nguvu wawe watendaji katika kuitangaza imani yao po pote walipo. Hili ni jambo linalofadhaisha (linalowasumbua) sana makanisa ya Jumuiya ya Wakristo katika kisiwa hiki, ambayo mara nyingi wajumbe wao wanachapa vitabu vya kuwaonya washiriki wao juu ya utendaji wenye juhudi wa watangazaji hawa wa “habari njema.” Vingine vya vitabu hivi vyenye kuwapinga Mashahidi vinavyochapwa na wale wa makanisa ya Jumuiya ya Wakristo vinasema kwa wivu juu ya bidii na juhudi ya Mashahidi wa Yehova, na hata kutia moyo washiriki wa makanisa waonyeshe sifa hizo katika kutegemeza imani zao. Mashahidi wa Yehova katika Sri Lanka wanafanya maendeleo kweli kweli kwa msaada wa Yehova nao wanatazamia mbele katika kuwasaidia watu wengi zaidi wenye mfano wa kondoo waiokoke “dhiki kubwa.”—Mt. 24:21, 22.