Maswali Kutoka kwa Wasomaji
● Mungu afufuapo watu duniani katika wakati ujao, je! watakuwa karibu umri ule ule na sura ile ile kama walivyokuwa hapo kwanza?
Maandiko hayaelezi jambo hili waziwazi, walakini akili nzuri pamoja na mambo fulani yanayotolewa na Biblia yanaonyesha kwamba ndivyo watakavyokuwa.
Kwa habari ya ufufuo wa kiroho, Biblia inatumia mfano wa mbegu za mmea na inasema hivi: “Mungu huipa mwili kama apendavyo.” Ndiyo, yeye hutoa linalofaa na linalohitajiwa. (1 Kor. 15:35-44) Tunaweza kutazamia ilo hilo kwa habari ya ufufuo wa kidunia.
Masimulizi ya Biblia ya ufufuo katika wakati uliopita hayaonyeshi kwamba wanadamu waliofufuliwa walikuwa wamebadilika sana katika umri na sura. Wakati kijana katika Shunemu alipokufa akafufuliwa na Elisha, alifufuka akiwa na umri na sura aliyokuwa nayo alipokufa. (2 Fal. 4:32-37) Vilevile ebu fikiria namna Lazaro alivyofufuliwa na Yesu, ambaye alikuwa amekufa siku nne na ambaye mwili wake ulikuwa umeanza kuoza. Je! Lazaro alifufuka akiwa amebadilika sana au sehemu za mwili wake zikiwa zimeoza? Hapana. Alikuwa na sura ile ile aliyokuwa nayo hapo kwanza. Kama sivyo, adui za kidini za Yesu zingetumia uhakika huo kumvunjia sifa yake njema. —Yohana 11:32-47.
Zaidi ya hayo, tunajua kwamba Yehova ni Mungu mwenye utaratibu, fadhili na rehema. Hiyo inaondoa mawazo ya kwamba yeye atamfufua mtu bila mguu au mkono au akiwa na sura iliyoharibiwa na ugonjwa ambao mwishowe ulimwua. (Yak. 1:17; Luka 11:13) Hata hivyo, hii haimaanishi kwamba mtu atafufuliwa akiwa kijana. Ikiwa mtu fulani alikufa kwa sababu ya ugonjwa wa moyo akiwa na umri wa miaka 75, sababu gani Mungu asimfufue akiwa na mwili unaofanana na ule, lakini awe na moyo ambao ungeendelea kupiga-piga damu? Ndipo, uwezo wa kuponya wa mipango ya Yehova, kutia na ubora wa dhabihu ya Yesu, utakapoendelea kutumiwa, mtu huyo angefanya maendeleo kufikia ukamilifu.—Ufu. 22:1, 2, 17.
Walakini, si jambo lenye faida au linalofaa kufuatia maulizo juu ya hali ya watakaofufuliwa. Mungu angetia ndani katika Biblia mambo mengi juu ya yale atakayofanya. Uhakika wa kwamba hakufanya hivyo unaonyesha kwamba haoni hii kuwa habari ya maana kwetu sasa. Yeye alitoa habari fulani katika Biblia juu ya ufufuo uliofanywa kwa uwezo wake. Na katika Maandiko ameweka uhakikisho kwamba kutakuwako “ufufuo wa wafu, wenye haki na wasio haki pia.” (Matendo 24:15; Yohana 5:28, 29) Kisha akatuachia sisi uamuzi wa kusitawisha imani katika Neno lake na ahadi zake. Tunaweza kuwa na hakika kwamba ikiwa sisi tutaonyesha imani, na kwa njia hiyo tuokoke na kuingia katika Taratibu Mpya, Mungu atahakikisha kwamba hakutakuwapo magumu yasiyoweza kuondolewa kwa habari ya ufufuo. Tutakuwa na furaha ya kupokea tena, kufahamu na kusaidia wale watakaofufuliwa kutoka kwa wafu.