Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w78 11/1 kur. 19-20
  • Mwenye Hekima Alikuwa na Maana Gani?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mwenye Hekima Alikuwa na Maana Gani?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Vichwa vidogo
  • Hata upumbavu mdogo Unaweza Kudhuru
  • Unapopaswa Moyo Kuwa
  • Kosa Kubwa
  • Watu Wasiostahili Wanaopata Vyeo Wasionewe Wivu
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
w78 11/1 kur. 19-20

Mwenye Hekima Alikuwa na Maana Gani?

Hata upumbavu mdogo Unaweza Kudhuru

TENDO moja la upumbavu laweza kumharibia mtu sifa yake. Mfalme Sulemani mwenye hekima aliandika hivi: “Mainzi yaliyokufa hufanya mafuta ya mtengenezaji wa marashi yanuke, yatoe uvundo. Upumbavu mdogo hufanya vivyo hivyo kwa mtu anayethaminiwa kwa hekima na utukufu [wake].” (Mhu. 10:1, NW) Jina zuri au sifa nzuri inalinganishwa na mafuta yanayonukia vizuri ambayo yanaweza kuharibiwa kwa urahisi na kitu kisicho na maana kama vile mainzi yaliyokufa. Kuoza kwa wadudu hawa kutafanya mafuta yanuke na kuchachuka, “yatoe uvundo.” Vivyo hivyo, huenda mtu akapoteza sifa njema ya kuwa mtu mwenye hekima na mheshimiwa kwa tendo lisilo la hekima, “upumbavu mdogo.”

Sababu ni kwamba watu wanatazamia mengi zaidi kutoka kwa mtu anayejulikana kwa sababu ya hekima yake. Kwa hiyo, lazima awe mwangalifu sana katika usemi na matendo yake. Sifa yake njema inaweza kuharibiwa na mambo kama vile hasira ya ghafula yenye kuharibu, tendo moja baya kwa sababu ya utumiaji usio wa kiasi wa vileo au tendo moja la uasherati.

Unapopaswa Moyo Kuwa

Ili kuepuka kuangukia upumbavu, mtu anahitaji kuwa na moyo ulio na maelekeo mema. Mwenye hekima aliandika hivi: “Moyo wake mwenye hekima upo [mkono] wa kuume; bali moyo wake mpumbavu upo mkono wa kushoto. Naam, huyo mpumbavu tena, aendapo njiani, hupungukiwa na fahamu zake; hata humwambia kila mtu ya kuwa yeye ni mpumbavu.”

Katika matumizi ya Biblia, “mkono wa kuume” unasimamia mara nyingi kibali. (Linganisha Mathayo 25:33.) Kwa hiyo, moyo wa mtu mwenye hekima kuwa katika mkono wake wa kuume kungeonyesha kwamba unamwelekeza katika mwendo mwema, wenye kibali. Walakini, mpumbavu anaelekezwa katika njia mbaya, moyo wake ukiwa katika “mkono wa kushoto.” Yeye anakuwa sawasawa na mtu anayezoea kutumia mkono wake wa kuume ambaye ikiwa hawezi kutumia mkono wake wa kuume, anaweza kutatizwa sana anapotumia mkono wake wa kushoto, akishindwa kufanya vizuri jambo ambalo lazima lifanywe. Kwa kukosa maelekeo mema, “moyo” katika mkono wake wa kuume, mpumbavu anaonekana alivyo vyepesi. Ni kama kwamba alikuwa ‘akimwambia kila mtu kwamba yeye ni mpumbavu.’ Kwa kutotaka kuonyeshwa makosa yake na kushauriwa, mtu wa namna hiyo vilevile ni mwepesi katika kusema kwamba wale wanaojaribu kumsaidia ni ‘wapumbavu.’

Kosa Kubwa

Wakati mtawala anapofanya kosa kubwa katika kuchagua watu watakaochukua vyeo vya juu, madhara makubwa yanafanyika. Mfalme Sulemani mwenye hekima alitaja kosa kama hilo kuwa msiba. Aliandika hivi: “Liko baa [msiba] nililoliona chini ya jua, nalo ni kama kosa litokalo kwake yeye atawalaye; ya kuwa upumbavu huwekwa mahali pa juu sana, nao wakwasi [‘waungwana,’ New Berkeley Version] hukaa mahali pa chini. Mimi nimeona watumwa wamepanda farasi, na wakuu wakienda kwa miguu juu ya nchi kama watumwa.”

Sulemani anasema juu ya wanaostahili kuchukua vyeo vya juu kuwa “wakwasi” (“matajiri,” ZSB). Hatupaswi kufahamu hili likiwa na maana ya kwamba yeye alipendelea utawala wa matajiri. Kwa wazi Sulemani alikuwa akifikiria watu wanaotumia uamuzi mzuri na kufanya mambo yao vizuri. Bila shaka watu wa namna hiyo wanaonyesha kwamba wanao uwezo mkubwa zaidi wa kutawala kuliko wale ambao wametumia mali zao vibaya.

Kwa sababu ya uamuzi wenye makosa wa mwenye mamlaka, wakuu au waungwana huenda wakanyimwa heshima wanayostahili na huenda wakatendwa kama watumwa. Walakini, huenda watu wasiostahili, watumishi vivi hivi tu, wakawa wakipanda farasi kama waungwana. Hali hii inafanya mambo kuwa magumu kwa raia ambao wanalazimika kutii wakuu wasiostahili. Kwa kweli maneno ya Sulemani yanakazia uhitaji wa kuchagua watu wanaostahili wa kuangalia kazi ya maana.

Watu Wasiostahili Wanaopata Vyeo Wasionewe Wivu

Huenda kutoweza kitu kusionekana mara ya kwanza. Watu wengine wanao uwezo wa kuvutia wengine na kile kinachoonekana kuwa akili nyingi. Huenda wakachaguliwa wachukue madaraka, wakati watu wenye hekima ya kweli wanapoachwa. Wakati watu wasiostahili wanapokuwa na cheo kikubwa, huenda wengine wakawaonea wivu. Lakini, kwa kweli, watu wasioweza hawapaswi kuonewa wivu. Sikuzote wanakuwa katika hatari ya kupoteza kile ambacho huenda wakawa walikuwa wamepata. Kwa kukosa hekima inayohitajiwa, huenda baada ya wakati fulani ikaonekana walivyo kweli kweli wapatwe na anguko baya sana, wapatwe na dhara na aibu.

Kwa wazi Sulemani alikuwa akitoa mfano wa kuonyesha kwamba sikuzote kutoweza kitu kunakuwa na hatari alipokuwa akilekeza kwa vitu vingine vinavyotokeza hatari nyakati zote. Aliandika hivi: “Mwenye kuchimba shimo atatumbukia ndani yake [kwa sababu shimo linatokeza hatari sikuzote]; naye abomoaye boma [“ukuta wa mawe,” NW], nyoka [ambaye hufanya makao yake katika kuta zilizobomoka] atamwuma. Mwenye kuchonga mawe ataumizwa kwayo; naye apasuaye miti huona hatari katika hiyo.” (Mhu. 10:8, 9) Kuchonga mawe na kupasua miti ni kazi zenye hatari, kwa hiyo, zinapaswa kufanywa kwa ungalifu.

Bila shaka, mtu atimizaye mambo ana hali bora zaidi ya yule aliye na uwezo lakini akose hekima ya kuutumia ifaavyo. Akionyesha jambo hili, Sulemani anasema hivi: “Iwapo chuma [hakikati], wala mtu hakinoi; ndipo hana budi kutumia nguvu zaidi.” Ungekuwa upumbavu kutumia shoka lisilo na ukali kukata mti, mtu akitumia nguvu nyingi bila sababu na bado asifanye kazi nzuri. “Walakini,” aendelea Mfalme Sulemani, “yafaa kutumia hekima, na kufanikiwa.” (Mhu. 10:10) Ndiyo, hekima inayotumiwa ndiyo yenye faida. Huenda mtu akawa na maarifa. Lakini maarifa hayo yangekuwa na faida gani ikiwa yeye hajui namna ya kuyatumia. Sulemani anasema hivi: “Nyoka akiuma asijatumbuizwa, basi hakuna faida ya mtumbuizi.” (Mhu. 10:11) Uwezo wa kumtumbuiza (kumtuliza) nyoka ni wa bure wakati yule mwenye uwezo huo anapoumwa kabla ya kumtumbuiza. Septuagint Version inasomwa hivi: “Nyoka akiuma kipindi cha katikati anapotumbuizwa, hakuna faida kwa mwenye kumtumbuiza.” Hivyo mtu anapaswa aseme kwa matokeo mema.

Kwa hiyo, mahali pa kuwaonea wivu watu wasioweza kitu wanaopata vyeo vyenye mamlaka, mtu anapaswa kujua hali ya hatari waliyo nayo, na katika hali yake mwenyewe, ajaribu kutumia vizuri maarifa na uwezo wake kwa hekima. Mwishowe, mwenye hekima, hata wakati ambapo maamuzi yake mema hayakubaliwi, bado yeye ni afadhali kuliko mtu aliyetukuzwa lakini asiyeweza kitu.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki