Mithali Yenye Hekima
“Kwa mpumbavu hekima haipatikani; hafumbui kinywa chake langoni,” alisema Sulemani katika Mithali 24:7.
Lo! namna mithali hii ilivyo shauri fupi lenye akili! Kwa mtu mpumbavu, hekima ya kweli iko juu sana, kama kwamba haifikiki kwake. Hana nia ya kutia jitihada ili kuipata. Namna nyingine ya matumizi ya Kiebrania cha kwanza ni kwamba “hekima ni kama marijani.” Kati ya vitu vya kuvutia vya kale, marijani ya kupamba ilikuwa ghali (yenye bei kubwa). Inaweza kusemwa kwamba kwa mpumbavu hekima ya kweli ni ghali sana. Hana nia ya kulipa bei ya kujitahidi au kutoa mambo yanayohitajiwa ili kuipata.
Katika Israeli wa kale wanaume wazee wenye hekima walikusanyika kwenye lango la mji ili watoe maamuzi juu ya magomvi na kutoa mashauri. Hapo hapakuwa mahali pa mpumbavu kuzungumza kwa sauti. Hata hangepatikana hapo akiomba mashauri yenye hekima. Mahali pa kufunua kinywa chake katika malango, angekuwa mahali penginepo akipayuka tu.
Kwa kusimulia mambo ya hakika juu ya “mpumbavu,” Sulemani anatusaidia kuona thamani ya kweli ya hekima.