Kutumia kwa Yehova “Upumbavu” ili Kuwaokoa Wanaoamini
“Maana, kadiri ya hekima ya Mungu, watu hawawezi kumjua Mungu kwa njia ya hekima yao wenyewe. Badala yake, Mungu amependa kuwaokoa wale wanaoamini kwa njia ya kile ambacho wenye hekima wanakiona kuwa ni upumbavu, yaani, ujumbe tunaohubiri.”—1 WAKORINTHO 1:21, HNWW.
1. Yehova angetumia “upumbavu” kwa maana gani, na tunajuaje kwamba ulimwengu haukupata kumjua Mungu kwa hekima yao wenyewe?
ETI nini? Yehova angetumia upumbavu? Sivyo kwa kweli! Lakini anaweza na yeye hutumia kile kionekanacho kuwa upumbavu kwa ulimwengu. Yeye hufanya hivyo ili awaokoe watu wamjuao na kumpenda. Kupitia hekima yao, ulimwengu hauwezi kumjua Mungu. Yesu Kristo alionyesha hilo wazi aliposema hivi katika sala: “Baba mwenye haki, ulimwengu haukukujua.”—Yohana 17:25.
2. Huenda ikaonekanaje kwamba njia za Yehova na njia za ulimwengu zinaenda sambamba, lakini mambo ya hakika ni nini?
2 Maneno ya Yesu huonyesha kwamba njia za Yehova hutofautiana na zile za ulimwengu. Kijuujuu huenda ikaonekana kwamba makusudi ya Mungu na yale ya ulimwengu huu yanaenda sambamba. Huenda ikaonekana kwamba miradi ya ulimwengu huu ina baraka ya Mungu. Kwa mfano, Biblia husema kwamba Mungu angesimamisha serikali yenye uadilifu itakayoiletea ainabinadamu duniani maisha katika amani, furaha, na ufanisi. (Isaya 9:6, 7; Mathayo 6:10) Vilevile, ulimwengu hutangaza kusudi lao la kuwapa watu amani, ufanisi, na serikali nzuri kupitia ule uitwao eti utaratibu wa ulimwengu mpya. Lakini makusudi ya Mungu na yale ya ulimwengu hayako sawasawa. Kusudi la Yehova ni kujitetea mwenyewe akiwa Mwenye Enzi Kuu Aliye Mkuu Zaidi wa ulimwengu wote mzima. Atafanya hilo kupitia serikali ya kimbingu itakayozifutilia mbali serikali zote za kidunia. (Danieli 2:44; Ufunuo 4:11; 12:10) Kwa hiyo Mungu hashiriki jambo lolote na ulimwengu huu. (Yohana 18:36; 1 Yohana 2:15-17) Hiyo ndiyo sababu kwa nini Biblia husema juu ya aina mbili za hekima—“hekima ya Mungu” na “hekima ya ulimwengu.”—1 Wakorintho 1:20, 21, HNWW.
Kasoro ya Msingi ya Hekima ya Ulimwengu
3. Ingawa hekima ya ulimwengu huenda ikaonekana yenye kuvutia, ni kwa nini utaratibu wa ulimwengu mpya wa mwanadamu usingekuwa kamwe wenye kuridhisha?
3 Kwa wale wasioongozwa kwa hekima ya Mungu, hekima ya ulimwengu huonekana kuwa yenye kuvutia. Kuna falsafa za kilimwengu zinazosikika kuwa zenye fahari ambazo huvutia sana akili. Maelfu ya taasisi za masomo ya juu hutoa habari kutoka kwa akili za ainabinadamu zionwazo na wengi kuwa kuu zaidi. Maktaba kubwa-kubwa zimejaa maarifa iliyokusanywa ya karne kadhaa za ujuzi wa kibinadamu. Hata hivyo, yajapokuwa hayo ule utaratibu wa ulimwengu mpya unaokusudiwa na watawala wa kilimwengu ungeweza kuwa tu utawala wa wanadamu wasio wakamilifu, wenye dhambi, wanaokufa. Kwa hiyo utaratibu huo ungekuwa usio mkamilifu, ukirudia-rudia makosa mengi ya zamani na usioweza kamwe kutosheleza mahitaji yote ya ainabinadamu.—Warumi 3:10-12; 5:12.
4. Utaratibu wa ulimwengu mpya unaokusudiwa unaathiriwa na nini, kukiwa na tokeo gani?
4 Utaratibu wa ulimwengu mpya unaokusudiwa na mwanadamu hauathiriwi tu na udhaifu wa kibinadamu bali pia na uvutano wa viumbe-roho waovu—naam, Shetani Ibilisi na roho waovu wake. Shetani amezipofusha akili za watu ili kwamba wasiamini “habari njema zenye utukufu juu ya Kristo.” (2 Wakorintho 4:3, 4, NW; Waefeso 6:12) Kwa hiyo, ulimwengu hupatwa na shida moja baada ya nyingine. Ulimwengu hushindana na kupatwa na maumivu na madhara unapojaribu kwa hasara yao kujitawala wenyewe bila msaada wa Mungu na kwa kupuuza mapenzi ya kimungu. (Yeremia 10:23; Yakobo 3:15, 16) Hivyo, kama vile mtume Paulo alivyosema, “ulimwengu kupitia hekima yao haukupata kumjua Mungu.”—1 Wakorintho 1:21, NW.
5. Ni nini iliyo kasoro ya msingi ya hekima ya ulimwengu?
5 Kwa hiyo, ni nini iliyo kasoro ya msingi ya hekima ya ulimwengu huu, kutia na mipango yao ya utaratibu wa ulimwengu mpya? Ni kwamba ulimwengu hupuuza jambo lisiloweza kupuuzwa kwa mafanikio—enzi kuu ya juu zaidi ya Yehova Mungu. Ulimwengu hukataa kwa kiburi kutambua enzi kuu ya kimungu. Ulimwengu humweka Yehova kando kimakusudi katika mipango yao yote na hutegemea uwezo na mashauri yao yenyewe. (Linganisha Danieli 4:31-34; Yohana 18:37.) Biblia huonyesha wazi kwamba “hofu ya Yehova ni mwanzo wa hekima.” (Mithali 9:10; Zaburi 111:10, NW) Hata hivyo, ulimwengu haujapata hata kujua takwa hilo la msingi la hekima. Kwa hiyo, bila utegemezo wa kimungu, unaweza kufanikiwaje?—Zaburi 127:1.
Kuhubiriwa kwa Ufalme —Jambo la Kipumbavu au Lifaalo?
6, 7. (a) Wale wanaoongozwa na hekima ya Mungu wanahubiri nini, lakini ulimwengu huwaonaje? (b) Makasisi wa Jumuiya ya Wakristo huhubiri kulingana na hekima ya nani, na tokeo likiwa nini?
6 Kwa upande ule mwingine, wale wamjuao Mungu huonyesha hekima ya Mungu na huchagua kuongozwa nayo. Kama vile Yesu alivyotabiri, wao huhubiri “habari njema ya ufalme . . . katika ulimwengu wote.” (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Je! kuhubiri huko kunafaa sasa, wakati dunia yetu imejaa ugomvi, uchafuzi, umaskini, na kuteseka kwa kibinadamu? Kwa wenye hekima wa kilimwengu kuhubiri juu ya Ufalme wa Mungu kunaonekana kuwa upumbavu mtupu, kusikofaa. Wanawaona wahubiri wa Ufalme wa Mungu kuwa wasumbufu wanaoyazuia maendeleo ya Serikali kuelekea serikali ya kisiasa ifaayo kabisa. Wanaungwa mkono katika jambo hilo na makasisi wa Jumuiya ya Wakristo, wanaohubiri kulingana na hekima ya ulimwengu huu na ambao hawaambii watu lile wanalohitaji kujua kuhusu ulimwengu mpya wa Mungu na serikali yao ya Ufalme, hata ingawa hilo ndilo lililokuwa fundisho kuu la Kristo.—Mathayo 4:17; Marko 1:14, 15.
7 Mwanahistoria H. G. Wells alivuta fikira kwenye kushindwa huko kwa makasisi wa Jumuiya ya Wakristo. Aliandika hivi: “Wenye kutokeza ni ule umashuhuri mwingi uliotolewa na Yesu kwa lile fundisho aliloita Ufalme wa Mbinguni, na jinsi kwa ulinganifu linavyokosa maana katika taratibu na mafundisho ya yaliyo mengi ya makanisa ya Kikristo.” Hata hivyo, ili watu wa kizazi hiki waweze kupata uhai, ni lazima kwanza wasikie juu ya Ufalme wa Mungu uliosimamishwa, na ili hilo litimizwe ni lazima mtu fulani ahubiri habari njema kuuhusu.—Warumi 10:14, 15.
8. Kwa nini kuhubiriwa kwa habari njema ya Mungu ni jambo lifaalo zaidi la kufanya leo, lakini ni mwendo gani ambao haungekuwa na faida ya kudumu?
8 Kwa hiyo, kuhubiri habari njema ya Mungu ni jambo lifaalo zaidi la kufanya leo. Ni hivyo kwa sababu ujumbe wa Ufalme huandaa tumaini la kweli linaloijaza mioyo ya kibinadamu shangwe katika siku hizi za mwisho wakati ‘nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo zitakuwa hapa.’ (2 Timotheo 3:1-5, NW; Warumi 12:12; Tito 2:13) Ingawa uhai katika ulimwengu huu unakosa uhakika na ni mfupi, uhai katika ulimwengu mpya wa Mungu utakuwa wa milele, miongo-ni mwa shangwe, wingi, na amani hapa hapa duniani. (Zaburi 37:3, 4, 11) Kama vile Yesu Kristo alivyosema, “atafaidiwa nini mtu akiupata ulimwengu wote, na kupata hasara ya nafsi yake? au mtu atatoa nini badala ya nafsi yake?” Mtu akipoteza haki ya kuishi katika ulimwengu mpya wa Mungu, ulimwengu huu wenye kupitilia mbali una faida gani? Kufurahia kwake sasa vitu vya kimwili kumekuwa jambo lisilofaa kitu, la bure, na la muda mfupi tu.—Mathayo 16:26; Mhubiri 1:14; Marko 10:29, 30.
9. (a) Wakati mwanamume aliyealikwa kuwa mfuasi wa Yesu alipoomba kuahirisha mambo, Yesu alimshauri afanye nini? (b) Jibu la Yesu lapasa lituathirije?
9 Mtu mmoja ambaye Yesu alialika kuwa mfuasi wake alisema hivi: “Bwana, nipe ruhusa kwanza niende nikamzike baba yangu.” Yesu alimshauri afanye nini? Akijua kwamba mwanamume huyo angekuwa akiahirisha kazi ya muhimu sana ili tu kungojea mpaka wazazi wake wafe, Yesu alijibu hivi: “Waache wafu wawazike wafu wao; bali wewe enenda ukautangaze ufalme wa Mungu.” (Luka 9:59, 60) Wale wanaoonyesha hekima kwa kumtii Kristo hawawezi kugeuka kando wasitimize utume wao wa kuhubiri ujumbe wa Ufalme. Hekima ya kimungu huwapa ufahamu wa kwamba ulimwengu huu na watawala wao umehukumiwa kuangamizwa. (1 Wakorintho 2:6; 1 Yohana 2:17) Wale wanaoiunga mkono enzi kuu ya Mungu wanajua kwamba tumaini la pekee la kweli kwa ainabinadamu limo katika mwingilio na utawala wa kimungu. (Zekaria 9:10) Kwa hiyo ingawa wale wenye hekima wa ulimwengu huu hawaamini Ufalme wa Mungu na hawaitaki serikali hiyo ya kimbingu, wale wanaoongozwa kwa hekima ya kimungu hufanya lile linalowaletea wanadamu wenzao faida ya kweli, wakiwatayarisha kwa ajili ya uhai wa milele katika ulimwengu mpya wa Yehova ulioahidiwa.—Yohana 3:16; 2 Petro 3:13.
‘Jambo la Kipumbavu kwa Wale Wanaopotea’
10. (a) Sauli wa Tarso alipoongoka, yeye alianza kazi gani, na aliionaje? (b) Wagiriki wa kale walijulikana kwa ajili ya nini, lakini Mungu aliionaje hekima yao?
10 Sauli wa Tarso, aliyekuja kuitwa Paulo mtume wa Yesu Kristo, alianza kufanya kazi hiyo ya kuokoa uhai. Je! inafaa kufikiri kwamba Yesu Kristo alipomfanya Sauli aongoke, Alikuwa akimpa mgawo wa kushiriki katika utendaji wa kipumbavu? Paulo hakufikiri hivyo. (Wafilipi 2:16) Wakati huo Wagiriki walionwa kuwa watu wenye ujuzi mwingi zaidi ulimwenguni. Waliwaonea fahari wanafalsafa wao wakuu na wanaume wenye hekima. Ingawa Paulo alisema Kigiriki, yeye hakufuata falsafa na mafundisho ya Kigiriki. Kwa nini? Kwa sababu hekima ya ulimwengu huu ni upumbavu kwa Mungu.a Paulo alitafuta hekima ya kimungu, iliyomsukuma ahubiri habari njema nyumba kwa nyumba. Mhubiri mkuu zaidi wa wakati wowote ule, Yesu Kristo, alikuwa ameweka mfano na alikuwa amemwagiza afanye kazi ile ile.—Luka 4:43; Matendo 20:20, 21; 26:15-20; 1 Wakorintho 9:16.
11. Kwa msingi, Paulo alisema nini juu ya utume wake wa kuhubiri na hekima ya ulimwengu?
11 Paulo asema hili juu ya utume wake wa kuhubiri: “Kristo hakunituma kubatiza; bali kuhubiri Habari Njema . . . bila kutegemea maarifa ya hotuba za watu kusudi nguvu ya kifo cha Kristo msalabani [mti wa mateso, NW] isibatilishwe. Maana ujumbe kuhusu kifo cha [dhabihu ya fidia ya] Kristo msalabani [mti wa mateso, NW] ni jambo la kipumbavu kwa wale walio katika mkumbo wa kupotea, lakini kwetu sisi tulio katika njia ya wokovu ujumbe huo ni nguvu ya Mungu. Maana maandiko Matakatifu yasema: ‘Nitaiharibu hekima yao wenye hekima, na elimu ya wataalamu nitaitupilia mbali.’ Yu wapi, basi, mwenye hekima [kama vile mwanafalsafa]? Yu wapi, basi, mwalimu wa Sheria? Naye bingwa wa mabishano wa nyakati hizi yuko wapi? Mungu ameifanya hekima ya ulimwengu kuwa upumbavu. Maana, kadiri ya hekima ya Mungu, watu hawawezi kumjua Mungu kwa njia ya hekima yao wenyewe. Badala yake, Mungu amependa kuwaokoa wale wanaoamini kwa njia ya kile ambacho wenye hekima wanakiona kuwa ni upumbavu, yaani, ujumbe tanaohubiri.”—1 Wakorintho 1:17-21, HNWW.
12. Yehova anatimiza nini kupitia “upumbavu, yaani, ujumbe tunaohubiri,” na wale wanaotaka “hekima itokayo juu” wataitikiaje?
12 Hata lionekane lisilosadikika kama nini, wale wale ambao ulimwengu huwaita wapumbavu ndio wale ambao Yehova hutumia kuwa wahubiri wake. Naam, kupitia upumbavu wa huduma wa wahubiri hao, Mungu huwaokoa wale wanaoamini. Yehova hupanga mambo ili wahubiri wa “upumbavu” huo wasiweze kujitukuza wenyewe, na wanadamu wengine wasiweze kwa haki kuwatukuza wale ambao kupitia kwao wameisikia habari njema. Sababu ya hiyo ni ili kwamba “hakuna mtu awezaye kujivunia chochote mbele ya Mungu.” (1 Wakorintho 1:28-31, HNWW; 3:6, 7) Ni kweli, mhubiri ana daraka lenye maana, lakini ule ujumbe ambao amepewa utume wa kuuhubiri ndio hutokeza wokovu kwa mtu ikiwa anauamini. Wale wanaoitaka “hekima itokayo juu” hawatauchukia ujumbe wa mhubiri kwa sababu yeye huonekana kuwa mpumbavu na mnyenyekevu, mwenye kunyanyaswa, na ambaye huenda nyumba kwa nyumba. Badala ya hiyo, wasikivu watamstahi mpiga mbiu ya Ufalme akiwa mhubiri aliyepewa utume na Yehova na anayekuja kwa jina lake. Watauona kuwa wenye umaana mkubwa ule ujumbe aletao mhubiri kupitia mdomo na vichapo.—Yakobo 3:17; 1 Wathesalonike 2:13.
13. (a) Wayahudi na Wagiriki walikuonaje kuhubiriwa kwa Kristo aliyetundikwa? (b) Watu wengi hawakuitwa kutoka kwa vikundi gani vya watu kuwa wafuasi wa Yesu, na kwa nini?
13 Akiendeleza mazungumzo yake juu ya njia za Mungu, Paulo asema hivi: “Wayahudi wanataka ishara, na Wagiriki wanatafuta hekima; lakini sisi tunamhubiri Kristo aliyesulubiwa [aliyetundikwa, NW]. Kwa Wayahudi jambo hili ni kikwazo, na kwa watu wa mataifa ni upumbavu; lakini kwa wale walioitwa, Wayahudi kwa Wagiriki, Kristo ni nguvu ya Mungu na hekima ya Mungu. Maana kinachoonekana kuwa ni upumbavu wa Mungu, kina busara zaidi kuliko hekima ya binadamu; na kionekanacho kuwa ni udhaifu wa Mungu, kina nguvu kuliko nguvu za binadamu. Ndugu, kumbukeni wakati mlipoitwa: wengi wenu hawakuwa wenye hekima hata kwa fikira za binadamu; wengi hawakuwa wenye nguvu au watu wa tabaka ya juu. Ndiyo kusema, Mungu aliyachagua yale ambayo ulimwengu huyaona ni upumbavu, ili awaaibishe wenye hekima; na aliyachagua yale ambayo ulimwengu huyaona ni dhaifu, ili awaaibishe wenye nguvu.”—1 Wakorintho 1:22-27, HNWW; linganisha Isaya 55:8, 9.
14. (a) Wanapoombwa kuonyesha kustahili kwao, Mashahidi wa Yehova huelekeza kwenye nini? (b) Kwa nini Paulo alikataa kuwapendeza Wagiriki kwa wonyesho wowote wa hekima ya ulimwengu?
14 Yesu alipokuwa duniani, Wayahudi waliomba ishara kutoka mbinguni. (Mathayo 12:38, 39; 16:1) Lakini Yesu alikataa kutoa ishara. Vilevile, Mashahidi wa Yehova leo hawaonyeshi ishara za kustahili kwao. Bali, wao huelekeza kwenye utume wao wa kuhubiri habari njema, kama ilivyorekodiwa katika mistari ya Biblia kama vile Isaya 61:1, 2; Marko 13:10; na Ufunuo 22:17. Wagiriki wa kale walitafuta hekima, elimu ya juu zaidi katika mambo ya ulimwengu huu. Ingawa Paulo alielimishwa katika hekima ya ulimwengu huu, alikataa kuwapendeza Wagiriki kwa kuionyesha kwa njia yeyote. (Matendo 22:3) Alisema na kuandika katika Kigiriki kilichotumiwa na watu wa kawaida, badala ya kutumia Kigiriki bora. Paulo aliwaambia Wakorintho hivi: “Ndugu zangu, mimi nilipokuja kwenu, sikuja niwahubiri siri ya Mungu kwa ufasaha wa maneno, wala kwa hekima. . . . Neno langu na kuhubiri kwangu hakukuwa kwa maneno ya hekima yenye kushawishi akili za watu, bali kwa dalili za Roho na za nguvu, ili imani yenu isiwe katika hekima ya wanadamu, bali katika nguvu za Mungu.”—1 Wakorintho 2:1-5.
15. Petro huwakumbusha nini wale wenye kudhihaki habari njema, na hali ya sasa inafananaje na ile ya siku ya Noa?
15 Katika siku hizi za mwisho, wenye kudhihaki habari njema za ulimwengu mpya wa Mungu unaokuja na mwisho wa ulimwengu unaokaribia wanakumbushwa na mtume Petro kwamba ulimwengu wa siku ya Noa ‘uligharikishwa na maji, ukaangamia.’ (2 Petro 3:3-7) Akiwa anakabili mwisho huo wenye kuleta msiba mkubwa, Noa alifanya nini? Watu wengi humfikiria kuwa mjenga safina tu. Lakini Petro husema kwamba Mungu alipoileta Gharika juu ya ulimwengu wa kale, “alimhifadhi Noa, mhubiri wa uadilifu, pamoja na wengine saba.” (2 Petro 2:5, NW) Katika hekima yao ya kilimwengu, wale watu wa kabla ya Furiko wasiomcha Mungu bila shaka walidhihaki lile ambalo Noa alihubiri na kumwita mpumbavu, asiyeona mambo kihalisi, na asiyefanya mambo yafaayo. Leo, Wakristo wa kweli wanakabili hali iyo hiyo, kwa kuwa Yesu alilinganisha kizazi chetu na kile cha siku ya Noa. Hata hivyo, kujapokuwa wenye kudhihaki, kuhubiriwa kwa habari njema ya Ufalme ni kwa maana zaidi ya kuwa maongezi tu. Sawa na kule kuhubiri kulikofanywa na Noa, kunamaanisha wokovu kwa mhubiri na kwa wale wanaomsikiliza!—Mathayo 24:37-39; 1 Timotheo 4:16.
‘Kuwa Wapumbavu Ili Wapate Kuwa Wenye Hekima’
16. Ni nini kitakachoipata hekima ya ulimwengu huu kwenye Har–Magedoni, na ni nani atakayeokoka kuingia ulimwengu mpya wa Mungu?
16 Hivi karibuni, kwenye Har–Magedoni, Yehova Mungu atasababisha “hekima yao wenye hekima” iharibike. Atatupilia mbali “elimu ya wataalamu” waliotabiri juu ya jinsi utaratibu wa ulimwengu mpya wao ungeiletea ainabinadamu hali bora zaidi. “Vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” itateketeza huo uwongo, falsafa, na hekima yote ya ulimwengu huu. (1 Wakorintho 1:19; Ufunuo 16:14-16) Wale pekee watakaookoka vita hiyo na kupata uhai katika ulimwengu mpya wa Mungu ni wale wanaotii lile ambalo ulimwengu huu huita upumbavu—naam, habari njema za Ufalme za Yehova zenye utukufu.
17. Mashahidi wa Yehova wamekuwaje ‘wapumbavu,’ na wahubiri wa Mungu wa habari njema wameazimia kufanya nini?
17 Mashahidi wa Yehova, wakiongozwa na roho yake, hawaaibishwi kuhubiri kile ambacho ulimwengu huita upumbavu. Badala ya kujaribu kuwa wenye hekima ya kilimwengu, wamekuwa ‘wapumbavu.’ Jinsi gani? Kwa kufanya kazi ya kuhubiri Ufalme ili waweze kuwa wenye hekima, kama vile Paulo alivyoandika: “Kama mtu akijiona kuwa mwenye hekima miongoni mwenu katika dunia hii, na awe mpumbavu, ili apate kuwa mwenye hekima.” (1 Wakorintho 3:18-20) Wahubiri wa Yehova wa habari njema wanajua thamani yenye kuokoa uhai wa ujumbe wao na wao wataendelea kuuhubiri bila kuacha mpaka mwisho wa ulimwengu huu na hekima yao kwenye vita ya Har–Magedoni. Hivi karibuni, Yehova Mungu ataitetea enzi yake kuu ya ulimwengu wote mzima na kuwaletea uhai wa milele wale wote wanaouamini sasa na kutenda kulingana na “upumbavu, yaani, ujumbe tunaohubiri.”
[Maelezo ya Chini]
a Yajapokuwa mabishano ya kifalsafa na uchunguzi wote wa wale wanaume wenye hekima wa Ugiriki wa kale, maandishi yao huonyesha kwamba hawakupata msingi wowote wa tumaini la kweli. Maprofesa J. R. S. Sterrett na Samuel Angus huonyesha hivi: “Hakuna fasihi yoyote iliyo na maombolezo yenye kusikitisha zaidi juu ya mambo ya kuhuzunisha maishani, kupitilia mbali kwa upendo, udanganyifu wa tuamini, na ukatili wa kifo.”—Funk and Wagnalls New “Standard” Bible Dictionary, 1936, ukurasa 313.
Majibu Yako Ni Nini?
◻ Kuna aina gani mbili za hekima?
◻ Ni nini iliyo kasoro ya msingi ya hekima ya ulimwengu?
◻ Kwa nini kuhubiriwa kwa habari njema ni jambo lifaalo zaidi la kufanya?
◻ Ni nini kitakachoipata hekima yote ya ulimwengu hivi karibuni?
◻ Kwa nini Mashahidi wa Yehova hawaaibishwi kuhubiri kile ambacho ulimwengu huita upumbavu?
[Picha katika ukurasa wa 23]
Wagiriki walitafuta hekima ya kilimwengu na mara nyingi walikuona kuhubiri kwa Paulo kuwa upumbavu