Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w92 9/15 kur. 24-27
  • Wanapata Furaha ya Kweli Katika “Paradiso”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wanapata Furaha ya Kweli Katika “Paradiso”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Vichwa vidogo
  • Kuhofu Kifo Kunashindwa
  • Kuvutwa na Ukristo wa Kweli
  • Amani na Furaha Zapatikana
  • Dhabihu na Thawabu
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
w92 9/15 kur. 24-27

Wanapata Furaha ya Kweli Katika “Paradiso”

PARADISO! Neno hilo mara nyingi huja akilini wakati watu wanapofikiria Hawaii—na ni kwa sababu nzuri. Hapa kuna wingi wa halijoto yenye kiasi, anga za buluu, minazi yenye kusukasuka, pepo zenye kuburudisha, na fuko zenye mchanga—mambo ambayo wengi huenda wakaona kuwa ya kiparadiso.

Mambo hayo yamewavutia watu kutoka mbali na karibu. Wametoka Esia, Pasifiki, nchi za Amerika, na hata maeneo kama vile visiwa vya Karibia na Ulaya. Wengi wamehamia huku kwa ajili ya halijoto ya mwaka mzima yenye utulivu. Wengine wamekuja wakitafuta usalama wa kiuchumi—na furaha, bila shaka. Tokeo ni mchanganyiko wa vikundi vya kitaifa na vya kikabila, kukiwa na unamna-namna wenye kupendeza wa tamaduni na mawazo ya kidini.

Hata hivyo, hali hiyo ina sehemu nyingineyo. Sawa na maeneo mengi yenye kupendeza duniani, Hawaii hukumbwa na uhalifu, dawa za kulevya, uvunjaji sheria, uchafuzi, na matatizo mengine mengi yanayoishambulia familia ya kibinadamu haidhuru mahali ambapo huenda mtu akaishi. Kupitia kutojali na ubinafsi wa kibinadamu, visiwa vya Hawaii vinanyang’anywa kidato kwa kidato uzuri wavyo wa kiasili. Watu wanataka paradiso, lakini si wote wanaoishi huku wanaojali vya kutosha kufanya au angalau kudumisha visiwa hivyo kuwa paradiso. Mengi zaidi yanahitajiwa kuliko mandhari yenye kupendeza na halijoto ifaayo kufanya paradiso.

Hata hivyo, kuna kikundi chenye kukua cha watu wanaoishi hapa wanaoonea shangwe furaha ya kweli katika mandhari hii ya kiparadiso. Wao ni watu wanaoikubali kweli ya Biblia na wanazingatia moyoni ile ahadi nzuri ajabu ya Mungu: “Mimi naumba mbingu mpya na nchi mpya, na mambo ya kwanza hayatakumbukwa, wala hayataingia moyoni.” Watu hao wanatazamia wakati ujao kwa furaha wakiwa na maneno haya ya mtume Petro akilini: “Kama ilivyo ahadi yake, tunatazamia mbingu mpya na nchi mpya, ambayo haki yakaa ndani yake.” (Isaya 65:17; 2 Petro 3:13) Watu hao ni akina nani? Walipataje kujifunza juu ya lile tumaini zuri ajabu lililotolewa katika Biblia? Na ni mabadiliko gani ambayo yametokezwa maishani mwao?

Kuhofu Kifo Kunashindwa

Isabel na mume wake, George, wametoka Ufilipino. Isabel alilelewa afuate dini ya wazazi wake ya Katoliki ya Kiroma, ingawa hakuwa kamwe amechunguza ndani ya Biblia. Isabel alikuwa amefundishwa kwamba nafsi ya kibinadamu haiwezi kufa. Aliitikiaje fundisho hilo bandia? Alihofu wazo la kufa kwa sababu alikuwa na wazo la kuzikwa milele akiwa hai katika jeneza, nafsi yake eti ikishindwa kuponyoka. Lakini, katika 1973, Isabel alianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Alipojifunza kwamba nafsi ya kibinadamu inaweza kufa na kwamba Mungu atapindua kifo kwa njia ya ufufuo, alifurahia sana na akahisi ametulizwa sana. (Ezekieli 18:4, 20; Yohana 5:28, 29) Kweli ya Biblia ilimvutia sana hivi kwamba alifanya maendeleo kwa haraka.

Namna gani George? Yeye pia alijiunga katika mzungumzo ya Biblia lakini akiwa na wazo tu la kuwathibitisha Mashahidi kuwa wawongo. Hata hivyo, hakuweza kupata kosa lolote katika lile ambalo yeye na mke wake walikuwa wakifundishwa. Kwa kweli, muda mfupi baada ya wao kuanza kujifunza, habari ya damu ilitokea. Kufikia wakati huo, George alikuwa akipenda sana kula vyakula vilivyotayarishwa na damu. Lakini alipoona kwamba Biblia ilishutumu waziwazi ulaji wa damu, aliacha kula vyakula hivyo. (Mwanzo 9:3, 4; Mambo ya Walawi 17:10-12; Matendo 15:28, 29) Aliendelea kushiriki katika funzo la Biblia na alifurahia kwamba alikuwa hatimaye amepata kweli. Leo, George, Isabel, na watoto wao wanne wanaonea shangwe furaha ya kweli katika kuishi kulingana na viwango vya Mungu.

Kuvutwa na Ukristo wa Kweli

Mwanamume Mjapani aitwaye George na mke wake Mreno, Lillian, wamo katika miaka yao ya 60. Wote wawili walizaliwa na kulelewa Hawaii. Kwa kuwa George hakupewa na wazazi wake maagizo yoyote ya kidini, yeye hakuchukua kamwe dini kwa uzito. Hata hivyo, alikuwa ameamini katika Mungu sikuzote. Kwa upande ule mwingine, wazazi wa Lillian walimlea katika dini yao, akiwa Mkatoliki wa Kiroma.

Ingawa George hakuwa msomaji wa Biblia mwenye bidii, alikuwa amekuwa akiyasoma magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! kwa miaka 30 hivi. Hivyo alikuwa amejifunza mambo mengi juu ya Biblia. Hata hivyo, akiwa mvutaji sigareti na mnywaji vileo kwa wingi, alifanya mabadiliko maishani mwake polepole. Miaka ilipopita, George aliendelea kusoma magazeti hayo na mara kwa mara kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwenye Jumba la Ufalme. Kwa nini aliendelea? Ni kwa sababu, kama alivyosema, “dini zile nyingine ni zenye unafiki sana” kwa kuachilia mambo mengi mabaya yanayoshutumiwa katika Biblia. Aliweza kuona kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa tofauti.

Ni nini kilichomvutia Lillian, mke wa George mwaminifu-mshikamanifu, kwenye kweli ya Neno la Mungu hata ingawa alikuwa amevutwa sana na dini ya wazazi wake? Dada yake wa kimnofu alimwalika kwenye mikutano kwenye Jumba la Ufalme. “Niliifurahia sana ile hali ya familia na zile tabasamu zenye urafiki,” akumbuka Lillian. Ule upendo wa kweli alioona miongoni mwa watu wa Yehova ulimsadikisha kwamba hiyo ilikuwa ndiyo kweli. (Yohana 13:34, 35) Alikubali funzo la Biblia, akajiweka wakfu kwa Yehova Mungu hatimaye, na kubatizwa miezi michache baada ya mume wake.

George havuti sigareti tena wala halewi, na Lillian amezitupilia mbali sanamu zake zote za kidini. Wakiwa na mioyo iliyojaa upendo, wanashiriki pamoja na wengine yale ambayo wamejifunza, kutia na wajukuu wao 25 na watoto wa wajukuu wao 4. Ebu zitazame nyuso zao, na kuona jinsi George na Lillian walivyo na furaha!

Amani na Furaha Zapatikana

Patrick mwanamume wa Ailandi wa makamo, na mke wake Myahudi, Nina, wote wawili walihamia Hawaii kutoka kusini-magharibi mwa United States. Hapo mbeleni, walikuwa wamefuata mtindo-maisha uitwao eti kuishi kwa uhuru wa kutumia dawa za kulevya, kujaribu-jaribu dini, na wa maadili malegevu. Walitumia pia miaka mingi wakiwa washiriki wa dhehebu fulani, wakijaribu kupata ufahamu wa juu zaidi kupitia dawa za kulevya, kutafakari, na mwalimu wao binafsi wa dini. Baadaye, Patrick akachoka na ule wivu, ile fitina, na yale mabishano ya daima miongoni mwa washiriki wa dhehebu hilo waliodai kwamba walikuwa wamepata ‘kiwango cha juu zaidi cha ufahamu.’ Aliacha kikundi hicho akarudi Hawaii, ambako alikuwa ameishi wakati mmoja, akitumaini kupata amani ya akili. Baada ya hapo, Patrick alimsadikisha Nina, aliyekuwa rafiki-msichana wake wakati huo, amtembelee. Hatimaye, walifunga ndoa na kukaa Hawaii.

Patrick na Nina hawakutazamia kwamba jitihada zao za kutafuta amani na furaha zingeongoza hatimaye kwenye funzo la Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Akiwa haamini kuwako kwa Mungu maishani mwake mwote, Nina alianza kupata majibu ya Biblia yenye kuridhisha kwa maswali ya kutatanisha kama vile kwa nini uovu uko na kwa nini mambo mabaya hutukia kwa watu wazuri. Jitihada za Patrick za kutafuta kweli za muda wa miaka kumi vilevile zilikuwa na mwisho wenye furaha. Upesi, lile ambalo yeye na Nina walikuwa wakijifunza kutoka kwa Biblia lilianza kubadili maoni yao ya kiadili. Baada ya pambano refu na lililo gumu, Patrick aliweza kushinda uzoevu wake wenye nguvu wa tumbaku. Kwa karibu muda wa miaka kumi sasa, yeye na mke wake wameishi maisha safi, ya kiadili kulingana na viwango vya Mungu. Wakiwa na mioyo na dhamiri safi, wanaonea shangwe ile amani ambayo wamekuwa wakitafuta.

Dhabihu na Thawabu

“Jitahidini kuingia katika mlango ulio mwembamba, kwa maana nawaambia ya kwamba wengi watataka kuingia, wasiweze.” (Luka 13:24) Maneno hayo ya Yesu Kristo yanaonyesha kwa wazi kwamba si rahisi kumtumikia Mungu na kuishi kulingana na viwango vya Kimaandiko. Si lazima tu kwamba kila mtu anayetamani kufanya hivyo ajitahidi inavyohitajiwa bali pia ni lazima atoe dhabihu zinazohitajiwa. Kwa hakika hali imekuwa hivyo kwa wale watu waliotajwa katika usimulizi huu. Lakini wamethawabishwa vizuri ajabu kama nini!

Kwa mfano, fikiria Patrick na Nina, waliotoka tu kutajwa. Walifanya badiliko kubwa kutoka katika mtindo-maisha ambamo walichuma kiasi kikubwa cha pesa hadi kwenye huduma ya Kikristo ya wakati wote iliyotegemezwa na kazi ya kilimwengu isiyo ya wakati wote. Hata hivyo, wanasadiki kwamba faida za kiroho zina umaana wa juu zaidi ya dhabihu zozote za kimwili ambazo wametoa. Na wanafurahi kweli kweli.

Kwa sababu ya umri wao, mabadiliko hayajawa rahisi kufanya kwa George na Lillian. Kushiriki katika mikutano na huduma ya Kikristo kwahitaji wakati, uangalifu, na bidii ya kimwili. Hata hivyo kwa furaha yao kubwa, afya yao imekuwa bora zaidi, na maisha wanayoishi sasa yaweza kuelezwa tu kuwa yenye utendaji, yenye ukamili, na yenye furaha.

Kwa habari ya George na Isabel, hangaiko lao kubwa zaidi limo katika kuwazoeza watoto wao na kuwasaidia kwenye ile barabara iongozayo kwenye uhai. Wakati na jitihada nyingi inahitajiwa ili kuwatayarisha vijana wanne kwa ajili ya mikutano ya Kikristo au ili waweze kujiunga katika huduma ya Kikristo. Wakati mmoja ule mbano wa daima uliwasababisha George na Isabel walegee katika madaraka yao ya kiuzazi. Lakini hotuba ya Biblia yenye kichwa “Kufanya Upya Roho ya Kujidhabihu” iliwasukuma waongeze jitihada zao maradufu ili kuwapa watoto wao uangalifu na mazoezi yote yaliyohitajiwa ‘kuwalea katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.’ Bila shaka, jitihada za jinsi hiyo zimethawabishwa sana.—Waefeso 6:4, NW.

Si ile mandhari yenye kupendeza, ile halijoto ifaayo, au ule mwendo wa maisha wenye ustarehe unaoleta furaha ya kweli kwa watu hao na wengine wengi. Bali, ni ufahamu wa kwamba wanatumia maisha zao kulingana na mapenzi ya Mungu na wanaishi kulingana na viwango vya Neno lake, Biblia. (Mhubiri 12:13) Isitoshe, furaha ya kweli hububujika mioyoni mwao wanapotafakari juu ya ule wakati wenye shangwe ambapo paradiso ya kidunia itarudishwa duniani pote.—Luka 23:43.

[Picha katika ukurasa wa 25]

George, Isabel, na watoto wao hupata furaha katika kusoma Biblia

[Picha katika ukurasa wa 26]

George na Lillian hupata furaha katika huduma ya Kikristo

[Picha katika ukurasa wa 27]

Patrick na Nina wanafurahia amani ya kweli katika utumishi wa Yehova

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki