Wewe Ni Mtu wa Namna Ambayo Mungu Angechagua?
“Mungu aliyachagua mambo mapumbavu ya dunia awaaibishe wenye hekima.”—1 Wakorintho 1:27.
1. Kwa sababu gani wengi wamechagua kuwa wapumbavu machoni pa ulimwengu?
JE! WEWE ungepuza kazi ya maana kwa sababu tu watu wanaichukua kuwa upumbavu na ishara ya unyonge? Bila shaka hakuna mtu anayependa kuitwa mpumbavu au goigoi—hata mtoto hapendi kuitwa hivyo. Lakini tuseme mgawo wa kazi hiyo ya maana ungetoka kwa mtu mashuhuri mwenye akili sana. Je! hapo hungekuwa na nia ya kuondolea kiburi mbali na kuukubali mgawo huo? Mamilioni ya watu katika historia yote wamefanya lilo hilo. Ni kazi gani ambayo watu hao wameikubali, na mgawo wenyewe umetoka kwa nani? Jibu linapatikana katika barua ya kwanza ya Paulo kwa Wakristo wa Korintho wa kale.
2. Ni utendaji gani unaohesabiwa na ulimwengu kuwa upumbavu?
2 Katika kuonya Wakristo wa huko wasitegemeze ibada yao juu ya mambo waliyoona yakiwa ndiyo yenye kupendwa zaidi na watu wengi, Paulo aliandika hivi: “Maana ujumbe kuhusu kifo cha Kristo [kwenye mti wa mateso] ni jambo la kipumbavu kwa wale walio katika mkumbo wa kupotea, lakini kwetu sisi tulio katika njia ya wokovu ujumbe huo ni nguvu ya Mungu. Maana Maandiko matakatifu yasema: ‘Nitaiharibu hekima yao wenye hekima, na elimu ya wataalamu nitaitupilia mbali.’ Yu wapi, basi, mwenye hekima? Yu wapi basi, mwalimu wa Sheria? Naye bingwa wa mabishano wa nyakati hizi yuko wapi? Mungu ameifanya hekima ya ulimwengu kuwa upumbavu. Maana, kadiri ya hekima ya Mungu, watu hawawezi kumjua Mungu kwa njia ya hekima yao wenyewe. Badala yake, Mungu amependa kuwaokoa wale wanaoamini kwa njia ya kile ambacho wenye hekima wanakiona kuwa ni upumbavu, yaani ujumbe tunaohubiri.”—1 Wakorintho 1:18-21, HNWW.
3. Ni ujumbe gani unaohesabiwa na ulimwengu kuwa upumbavu ambao Mungu anakusudia uhubiriwe ulimwenguni pote?
3 Kwa wale waitwao wenye hekima na wenye akili wa ulimwengu, kunena habari za Kristo akimwaga damu ya uhai wake ya mti wa mateso ni upumbavu. Wao wanalifanyia mzaha wazo la kwamba kwa kuonyesha imani katika dhabihu ya Kristo watu wanaweza kufurahia uzima wa milele katika mfumo mpya wenye uadilifu. Jambo la kwamba Kristo aliinuka kwa wafu na sasa ndiye Mfalme mwenye uwezo mwingi wa Ufalme wa Mungu wa kimbingu ni ndoto nzuri tu kwao. Hata hivyo Mungu Mwenye Nguvu Zote anakusudia kwamba ujumbe huo wenye kuchangamsha moyo ujulishwe ulimwenguni pote. Kwa hiyo mtu ye yote anayependa kuwa mtumishi wake anapewa naye mgawo wa kuzihubiri habari njema hizo za Ufalme wake. Kwa kuwa ujumbe huo ni upumbavu mtupu kwa wenye hekima na wenye akili wa ulimwengu, Mungu anatumia nani kuuhubiri? Sikiliza jibu lililoongozwa na Mungu kutoka Neno Lake mwenyewe:
4. (a) Mungu anatumia nani kuhubiri ujumbe wake? (b) Uchaguzi wake wa watu hao una matokeo gani juu ya wenye hekima wa ulimwengu?
4 “Maana, ndugu zangu, angalieni mwito wenu, ya kwamba si wengi wenye hekima ya mwilini, si wengi wenye nguvu, si wengi wenye cheo walioitwa; bali Mungu aliyachagua mambo mapumbavu ya dunia awaaibishe wenye hekima; tena Mungu alivichagua vitu dhaifu vya dunia ili aviaibishe vyenye nguvu; tena Mungu alivichagua vitu vinyonge vya dunia na vilivyodharauliwa, naam, vitu ambavyo haviko, ili avibatilishe vile vilivyoko; mwenye mwili awaye yote asije akajisifu mbele za Mungu.”—1 Wakorintho 1:26-29.
5. Ni nini kinachoamua kama wewe ni mtu wa namna ambayo Yehova atachagua kutumia?
5 Je! wewe ni mtu wa namna ambayo Mungu angechagua aifanye kazi anayotaka ifanywe leo duniani? Ikiwa ndivyo, maana yake ni kwamba lazima ujitayarishe kuonwa kuwa mpumbavu na ulimwengu. “Hekima ya dunia hii ni upuzi mbele za Mungu,” inasema Biblia. (1 Wakorintho 3:19) Kwa hiyo ili uwe mtumishi mwenye mafanikio wa Yehova Mungu, ni lazima uwe na nia ya kufuata njia itakayokufanya uonekane mpumbavu kulingana na maoni ya ulimwengu. Je! kuna mifano ya kihistoria ya kuonyesha kwamba, zaidi ya watumishi wa Mungu kuonwa kuwa wapumbavu na walimwengu, hekima ya ulimwengu ilikuwa upumbavu pia machoni pa Mungu?
Mifano ya Zamani Zilizopita
6. Ni kwa njia gani utendaji wa Noa ulivyoonekana kuwa upumbavu machoni pa ulimwengu, hata hivyo ukaonyesha hekima ya Mungu?
6 Kulingana na maoni ya wanadamu Noa alijitwalia kazi ya kipumbavu, lakini kwa maoni ya Mungu haikuwa hivyo. Ebu wazia kujenga juu ya nchi kavu sanduku ku-u-bwa sana lenye nafasi ya jumla ya futi-za-miraba-sita 1,300,000 (au mita-za-miraba-sita 36,800) ili lielee juu ya maji. Ilionekana kuwa jitihada ya kukisia-kisia mambo tu, ikaonekana ingekuwa ya bure ianze kuchekwa-chekwa! Watu waliuona kuwa upuzi kwamba Yehova Mungu angeukomesha ulimwengu. Kwa upande wao wenyewe, Noa alikuwa mpumbavu hata athubutu kuhubiri ujumbe wa namna hiyo. (2 Petro 2:5) Hata hivyo, uhakika ni kwamba njia yao ya maisha, njia yao ya kufanya mambo, ndiyo iliyokuja kuwa upumbavu machoni pa Mungu. Walikuwa wakiiharibu dunia, kumfanya Mungu aone uchungu. (Mwanzo 6:5) Kwa hiyo Noa alikuwa na nia ya kukubali aonwe kuwa mpumbavu kuhusiana na hatua ya Mungu ya kuonyesha hekima na uwezo Wake.
7. Kwa sababu gani mwendo wa Musa ulionekana kuwa wa kipumbavu, lakini matokeo yalionyesha nini?
7 Je! wewe ungeacha utajiri na cheo cha umashuhuri ili umpendeze Mungu, na badala ya mambo hayo ukubali kutendwa vibaya? Ndivyo alivyofanya Musa. Ingawa yeye ‘alifundishwa hekima yote ya Wamisri,’ kwa moyo wa kupenda aliiacha hiyo njia ya maisha akaikubali aibu inayokalia mtiwa-mafuta wa Mungu. (Matendo7:22; Waebrania 11:24-26) Kwa uhakika mwendo wa Musa ulionekana kuwa wa kipumbavu machoni pa ulimwengu wa Wamisri, lakini hekima ya ulimwengu huo ndiyo iliyoonyeshwa kuwa upumbavu wakati wenye hekima wa Misri waliposhushiwa cheo na mapigo 10 kisha nguvu za kijeshi za taifa hilo zikamalizwa na Mungu katika Bahari Nyekundu. Mifano hiyo inaonyesha kwamba kwa kweli hekima ya wanadamu ni upumbavu machoni pa Mungu. Haiwezi kulingana na hekima na uwezo wa yule Mwenye Nguvu Zote.
8. (a) Hesabu kubwa ya Wakristo wa kwanza ilitoka katika jamii yenye hali gani? (b) Hata hivyo mahubiri yao yalikuwa na matokeo gani juu ya wenye hekima ya ulimwengu?
8 Namna gani Wakristo wa kwanza? Profesa wa historia aliandika hivi; “Wengi wa Wakristo wa kwanza walikuwa watu waliopata malezi ya hali ya chini, wakiwa ni watu waliotoka katika jamii za hali ya chini za watu wenye biashara ndogo-ndogo za mijini.” (Kitabu The Ancient World, kilichoandikwa na Joseph W. Swain) Kwa kweli wafuasi wa Kristo wa karne ya kwanza walikuwa makabwela tu, na adui zao walikuwa wakiwaonyesha wazi jambo hilo. (Matendo 4:13; Yohana 7:48) Hata hivyo hekima iliyonenwa na wafuasi wa Kristo iliwaaibisha wenye hekima ya kilimwengu. Hawangeweza kuipima ile siri takatifu ya Mungu kuhusu Kristo na Ufalme; kwa maoni yao kusema habari hiyo kulikuwa upumbavu. Ni kama vile Biblia inavyosema: “Ni hekima ambayo watawala wa dunia hii hawakuielewa; maana wangaliielewa, [hawangalimtundika] Bwana wa utukufu.”—1 Wakorintho 2:7, 8, HNWW.
Kazi ya Mungu ya Kueneza Evanjeli
9. (a) Kwa kweli ni nani aliyekuwa chanzo cha maagizo ambayo Yesu alitoa? (b) Ili wauhubiri ujumbe wa Ufalme kwa wenye kustahili, wanafunzi wa Yesu walipaswa kufanya nini?
9 Yesu Kristo alionyesha hekima ya Mungu kwa mfano aliouweka na kwa maagizo aliyoyatoa pia juu ya namna ya kuifanya kazi ya kueneza evanjeli. Kama alivyosema: “Sifanyi neno kwa nafsi yangu, ila kama Baba alivyonifundisha ndivyo ninenavyo.” (Yohana 8:28) Yesu alijipeleka moja kwa moja mpaka mahali watu walipokuwa ili awape ujumbe wa Ufalme. Aliwafundisha hadharani na katika nyumba zao. Fikiria kidogo maagizo aliyowapa wanafunzi wake, wale 12 na wale 70 aliowatuma wakaishiriki kazi ya kueneza evanjeli. Unaweza kuyasoma maagizo hayo katika Mathayo 10:1-14 na Luka 10:1-12. Hapo Yesu aliwaambia wanafunzi wake wakatafute watu. “Ndani ya mji wo wote au kijiji mnachoingia chunguzeni mpate yule anayestahili ndani yake,” akasema. Ndiyo, tafuteni wale wanaotamani kusikiliza. Nao wanafunzi wangewaambia hao nini? “Hubirini, mkisema, ‘Ufalme wa mbingu umekuja karibu,’” Yesu akaagiza.—Mathayo 10:7 NW.
10. (a) Yesu alitoa mwongozo gani juu ya namna ya kumfikia mwenye nyumba? (b) Wanafunzi wake walipaswa kufanya nini mtu asipoonyesha kupendezwa (c) Inaweza kusemwa nini juu ya hekima ya maagizo ya Kristo?
10 Yesu hata alitoa mwongozo juu ya namna ya kufikia mwenye nyumba. Alisema: “Na nyumba yo yote mtakayoingia, semeni kwanza, Amani iwemo nyumbani humu; na akiwamo mwana wa amani, amani yenu itamkalia; la, hayumo, amani yenu itarudi kwenu.” (Luka 10:5, 6) Walipaswa kukaa pamoja na watu waliouitikia ule ujumbe wa Ufalme waliokuwa wakiuhubiri. Lakini kama mwenye nyumba hakupendezwa, hapo basi walipaswa kusonga mbele. Hakika hayo ni maagizo yaliyo mepesi sana kueleweka, lakini yaliyo wazi vya kutosha yaweze kuonyesha waeneza-evanjeli mambo ya kusema na namna ya kuyasema mpaka leo hii! Je! hivyo sivyo ungetazamia hekima ya Mungu ionyeshe?
11. (a) Yesu alionyesha ni nini kinachopasa kuwa kichwa cha ujumbe wa wanafunzi wake? (b) Ili mahubiri yetu juu ya Ufalme yawe na matokeo mazuri, tunahitaji kufanya nini? (c) Unaweza kutumiaje maandiko uonyeshe kwamba ule Ufalme utayatatua matatizo yaliyopangwa katika fungu hili?
11 Kama ilivyotajwa mapema, kokwa (jambo kuu) lililo katika ujumbe wa wale wanaoeneza evanjeli ni ule Ufalme. “Waambieni, Ufalme wa Mungu umewakaribia,” Yesu akaagiza. (Luka 10:9) Inakupasa wewe uwe na kichwa hicho cha habari akilini, kwa maana daraka lako wewe uliye mweneza-evanjeli ni kusaidia wasikilizaji wako wafahamu namna Ufalme unavyoweza kweli kweli kuwa habari njema kwao. Kwa hiyo inakupasa ujaribu kuusawazisha ujumbe wa Ufalme ulingane na utu wao na mahitaji waliyo nayo. Ikitegemea mahitaji au mapendezi ya wasikilizaji wako, mbona usikazie mambo yatakayofanywa na Ufalme ambayo ndiyo yatawavuta sana kuliko yale mengineyo? Kwa mfano, unaweza kuwaonyesha namna Ufalme utakavyotimiza kusudi la Mungu la kuifanya dunia iwe Paradiso ambamo watu wataishi milele, ukitumia maandiko kama Isaya 45:18 na Zaburi 37:29. Halafu, kwa kutumia maandiko yaliyoonyeshwa, unaweza kuwaonyesha namna Ufalme utakavyotatua matatizo yaliyopangwa hapa chini.
Magonjwa: Isaya 35:5, 6; Ufunuo 21:3, 4.
Kifo: Isaya 25:8; 26:19; Yohana 5:28, 29; 1 Wakorintho 15:26.
Upungufu wa chakula: Isaya 25:6; Zaburi 67:6; 72:16.
Makao: Isaya 65:21-23.
Vita: Zaburi 46:8, 9; 72:7, 8.
Uhalifu na jeuri: Zaburi 37:9, 10; Mithali 2:22.
Uchafuzi: Ufunuo 11:18.
12. (a) Mweneza-evanjeli anaweza kujuaje mahitaji ya mtu? (b) Ni nini ufunguo wa kuwa mweneza-evanjeli mwenye matokeo mazuri?
12 Unaweza kujuaje mahitaji ya wasikilizaji? Kwanza, uwe msikilizaji mzuri, mwenye nia ya kutaka kusikia mambo ambayo wao wanasema. Uliza maulizo kisha kwa makini usikilize majibu yao, na usipinge-pinge ikiwa watatoa majibu usiyotazamia. Shahidi mmoja, ambaye amekuwa mtendaji katika kazi ya kueneza evanjeli muda wa miaka zaidi ya 25, alisema hivi: “Mimi najaribu moja kwa moja kumhusisha mwenye nyumba katika mazungumzo. Kwa njia hiyo napata kujua mapendezi yake, badala ya kuendelea tu kusema yale niliyokuja kumwambia.” Ni kama vile mweneza-evanjeli mwingine mwenye ujuzi alivyosema: “Ukitoa mahubiri uliyotangulia kuyakaza kabisa akilini mwako yasiweze kubadilika, huenda maneno unayosema yakagusa masikio yao kidogo tu au yapitilie mbali pamoja na upepo.” Kusema kweli, ufunguo wa kuwa mweneza-evanjeli mwenye matokeo mazuri ni kupendezwa na watu kikweli, kama Yesu. (Mathayo 9:36-38) Acha watu waone kwamba unapendezwa nao binafsi, na kwamba wewe unaziamini kweli kweli habari njema unazowaletea. Ni kama Shahidi mmoja alivyosema: “Maneno yakikutoka kwa njia inayoonyesha hufikirii sana unayosema, watakata shauri moja la kwamba huna usadikisho.”
Njia Inayohitajiwa Kabisa ya Kueneza Evanjeli
13. Biblia inaonyeshaje kwamba Wakristo wa kwanza walitii maelekezo ya Kristo juu ya kuhubiri?
13 Kama vile tumeona, Yesu Kristo aliwatia moyo wafuasi wake wapeleke ujumbe wa Ufalme moja kwa moja mpaka kwenye nyumba za watu. Kwa kufuata maelekezo yake, mitume pia walionyesha hekima ya Mungu kwa kutumia njia hiyo inayohitajiwa kabisa ya kueneza evanjeli. Maandishi ya Biblia yanasema: “Kila siku katika hekalu na nyumba kwa nyumba waliendelea bila kuacha wakifundisha na kuzitangaza habari njema juu ya Kristo, Yesu.” (Matendo 5:42, NW) Baadaye mtume Paulo alirudia kukumbushana na Wakristo wenzake kazi aliyofanya kueneza evanjeli, akisema: “Sikujiepusha kuwaambia ninyi lo lote la mambo yaliyokuwa yenye faida wala kuwafundisha hadharani na nyumba kwa nyumba. Lakini nilitoa ushuhuda kikamilifu kwa wote Wayahudi na Wagiriki juu ya toba kwa Mungu na kumwamini Bwana yetu Yesu.”—Matendo 20:20, 21, NW.
14. Ni nini kinachoonyesha matokeo mazuri ya njia ya kueneza evanjeli kwa kwenda nyumba kwa nyumba?
14 Ingawa kwa ujumla watumishi wa Mungu wamedhihakiwa na kuonwa kuwa wapumbavu kwa sababu ya kutumia njia hiyo ya kimitume ya kuhubiri Ufalme, mafanikio makubwa sana ya njia hiyo yanaonyesha ina ukubali wa Mungu. Kwa mfano, mchunguzi Mwingereza wa hali za kijamii, Bryan Wilson, alichanganua ukuzi wa Mashahidi wa Yehova katika Japani kisha akataarifu hivi: “Sehemu kubwa [asilimia 58.3] ya wale ambao wamekuwa Mashahidi wanatamka kwamba kupendezwa kwao kuliamshwa mara ya kwanza na ziara ya mhubiri aliyewatembelea nyumbani kwao.” Pia, miaka mingi iliyopita, John A. O’Brien padri Mkatoliki aliwaambia mapadri wapatao 200 huko Seminari ya Mt. Joseph mjini New York, kwamba: “Siri ya mafanikio makubwa ajabu ya Mt. Paulo ni kwamba yeye aliitumia bila kuchoka ile njia ya kuongoa wafuasi wapya kwa kwenda nyumba kwa nyumba. Kimekuwa kinyume kisichofaa kwamba njia hii ya kimitume inatumiwa sasa na madhehebu zisizo za Kikatoliki, sana-sana Mashahidi wa Yehova.”
Sababu Inayofanya Tupaswe Kupanga Orodha ya Kueneza Evanjeli
15. Kwa sababu gani ni jambo la maana kupanga katika orodha wakati wa utendaji wetu wa kuhubiri nyumba kwa nyumba?
15 Je! si kweli kwamba orodha inahitajiwa kabisa ili mambo ya maana yaweza kufanywa? Labda wewe una orodha ya wakati wa kula na kulala, na vilevile ya kwenda shuleni au kazini. Ni jambo la maana uwe na orodha (ratiba) ndipo uweze kufanya mambo. Hivyo ndivyo inavyoweza kusemwa juu ya kazi yetu ya kuhubiri nyumba kwa nyumba. Kwa kuwa Shetani anafanya pigano azuie habari njema za Ufalme wa Mungu zisiwafikie watu, tunahitaji kuwa na orodha ndipo tuweze kuwa na ushiriki wa kawaida katika kuuhubiri Ufalme. Ama sivyo, huenda tukawa na maelekeo ya kusema ‘hatuna wakati kabisa’ wa kufanya kazi hiyo. (1 Wakorintho 9:16) Shabaha ya Shetani ni kuona jambo hilo likitukia.
16. Ni mifano gani inayoonyesha ubora wa kuwa na orodha ya utendaji wetu wa kuhubiri?
16 Hivyo, daktari aliye Shahidi kwa muda wa miaka inayozidi 25 anasema kwamba anaona uhitaji wa lazima wa kupangia uenezaji wa evanjeli orodha. Mtu mwenye uwanda mkubwa wa kufugia ng’ombe katika United States (Amerika) anasema: “Karibu na mwaka wa 1944 nilijua kwamba njia ya pekee ambayo ningeweza kuingia katika utumishi ni kuupangia siku fulani.” Anaongeza kusema: “Mpaka leo hii mimi ningali naacha kazi siku moja ya juma ili nifanye utumishi.” Mzee Mkristo, ambaye ni mwanasheria pia, anaona kwamba kuwa na orodha iliyopangwa waziwazi ya kutolea ushuhuda kunamwezesha kuwa na wastani ya saa 15 kwa mwezi katika utendaji wa kuhubiri. Akiwa na shughuli yo yote ya kisheria siku ya Jumamosi, yeye anaipanga aifanye alasiri baada ya utumishi wa shambani wa asubuhi.—Linganisha Wakolosai 4:5.
Mwakilishe Mungu kwa Adhama
17. Tunapokuwa katika kazi ya kueneza evanjeli, tunapaswa kuwa waangalifu juu ya nini kuhusu mavazi?
17 Ingawa huenda ulimwengu ukatuchukua kuwa wapumbavu kwa sababu ya ujumbe wenye kupa uzima tulio nao, inatupasa tujiangalie sura yetu isije kwa njia yo yote ikaondoa fikira za watu kwenye ujumbe huo wa maana kabisa. Kupita vipimo katika mavazi, ama kwa kuwa na mitindo inayozidi mno au ovyo-ovyo, kunaweza kuwa na matokeo hayo. Katika eneo lenye hali ya juu ya maisha huenda tukahitaji kujali zaidi sura zetu na namna ya kujipamba. Je! maana yake ni kwamba tunahitajiwa kabisa tuwe na mavazi mengi ya bei-bei? Hapana. Mweneza-evanjeli mmoja mwenye mafanikio, ambaye amesafiri mahali pengi sana akiwa na mumewe, ana mazoea ya kutazama sana namna watu wa eneo alilomo wanavyovalia. Halafu mwanamke huyo anachagua mtindo wa kiasi unaolingana na mazoea ya mahali hapo. Mavazi tuliyo nayo kwa sasa, hata kama ni ya bei ya chini sana, yatakuwa yametosha yakiwa safi, yakiwa yamepigwa pasi na kuvaliwa kwa njia ya utaratibu mzuri. Ikiwa wewe umevaa koti, je! umekwisha kushonelea vifungo vilivyokatika? Ikiwa umevaa tai, vidoa-vidoa vyote vimeondolewa? Ikiwa umevaa viatu vya kikazi, je! vimepigwa rangi? Kumbuka kwamba sura yako ya usafi na yenye adhama itafanya watu waheshimu ujumbe wako.—Tito 2:10.
18. (a) Toa mfano wa ubora wa kuvaa kwa njia inayolingana na mazoea mazuri ya eneo ulilomo. (b) Kwa sababu gani kuvaa kwa njia inayopita kiasi kunapasa kuepukwa?
18 Kwa sababu ya Shahidi mmoja kufanyia sura yake maendeleo, anasema kwamba bibi ambaye hapo kwanza alikataa kuzungumza naye alimkaribisha ndani ya nyumba. Walipokwisha kuwa na mazungumzo ya Biblia yenye kufurahika, mwenye nyumba huyo akauliza, “Ebu niambie, wewe ni wa kanisa gani?” Alipojibiwa “Mashahidi wa Yehova,” mwenye nyumba alishangaa. Alikuwa hajapata kamwe kuruhusu Mashahidi wa Yehova waingie nyumbani mwake. Shahidi alipomwuliza kilichomfanya amruhusu yeye, mwenye nyumba alijibu ni kwa sababu Shahidi huyo alikuwa malidadi sana. Mwanamke huyo akalazimika kusikiliza maneno ya Shahidi huyo. Funzo la Biblia la ukawaida lilianzishwa. Kwa upande mwingine, katika ujirani wenye watu wa hali za chini, kuvaa mavazi ya kupita kiasi huenda kukawapa maoni ya kwamba ‘Yeye anajidhania kuwa bora kuliko sisi.’ Kwa hiyo, hata tuwe tunafanya kazi katika eneo gani, hata tuwe tunahubiria nani, mavazi na mapambo yetu yanapasa kuwa ya namna itakayovuta watu wausikilize ujumbe wa Ufalme badala ya kugeuzia mbali fikira zao.—1 Wakorintho 9:19-23.
19. (a) Ni nini ufunguo wa kuwa mtu wa namna ambayo Mungu anachagua? (b) Kristo aliweka mfano gani katika habari hii? (c) Kwa kuwa na nia ya kuacha ulimwengu ukuone kuwa mpumbavu, unajiweka katika msimamo wa kuweza kupata mapendeleo gani?
19 Kwa kweli, ni juu yako kulijibu ulizo hili: Je! mimi ni mtu wa namna ambayo Mungu angechagua? Uchaguzi wake hautegemei akili za maarifa ya mtu wala cheo chake cha kilimwengu. Bali, ufunguo ni nia yako ya kupenda kufanya kazi ya Mungu kwa njia ya Mungu, hata kama kwa kufanya hivyo unahesabiwa na ulimwengu kuwa mpumbavu au mtu mnyonge. Yesu Kristo aliuweka mfano. Yeye alikuwa na nia ya kuhesabiwa kuwa mpumbavu na watu wa siku zake ili awe “hekima itokayo kwa Mungu” kwa wale aliowafanya wawe wanafunzi. (1 Wakorintho 1:30) Ikiwa wewe una nia ya kuutangaza ujumbe wa Ufalme, unaohesabiwa na ulimwengu kuwa upumbavu, unajiweka katika msimamo wa kutumiwa na Yehova Mungu kuwa mmoja wa Mashahidi wake na kuifurahia ile zawadi yenye baraka ya uzima wa milele katika mfumo mpya wake wenye uadilifu.—Kutoka The Watchtower, February 1 1983.
Je! Wewe Unaweza Kujibu Maulizo Haya—
□ Ni unenaji gani ambao ni upumbavu machoni pa ulimwengu?
□ Noa na Musa walionyeshaje kwamba kile ambacho huenda ulimwengu ukakihesabu kuwa upumbavu kinaonyesha hasa hekima ya Mungu?
□ Yesu aliwapa wafuasi wake maagizo gani ya kuendeshea kazi ya kueneza evanjeli?
◻ Ni njia gani ya kuendeshea kazi ya kueneza evanjeli inayohitajiwa kabisa, na ni nini kinachoonyesha ina mafanikio?
◻ Kwa sababu gani ni jambo la maana tupangie utendaji wetu wa kueneza evanjeli orodha?
◻ Inatupasa tuvae namna gani tunaposhiriki katika utendaji wa kueneza evanjeli?
[Picha katika ukurasa wa 17]
Kabla Yesu hajatuma wanafunzi wake wakaingie katika utendaji wa kueneza evanjeli, aliwafundisha namna ya kuifanya kazi hiyo
[Picha katika ukurasa wa 18]
Kuhubiri nyumba kwa nyumba ni njia inayokubaliwa na Maandiko ya kueneza evangeli