Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w74 12/1 kur. 540-546
  • Je! Wewe Unayo Roho ya Kueneza Injili?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Wewe Unayo Roho ya Kueneza Injili?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • UBORA WA ROHO YA KUENEZA INJILI
  • KUZITANGAZA HABARI NJEMA KATIKA KARNE YA KWANZA
  • SI LAZIMA KUENEZA INJILI KUTIE NA KUSAFIRI
  • KUENEZA INJILI KWAMAANISHA MENGI ZAIDI KULIKO KUTANGAZA TU
  • KUJENGA NA KUZOEZA
  • “Fanya Kazi ya Mweneza-injili”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
  • Uenezaji wa Evanjeli—Mahali Pao Katika Ibada ya Kweli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Ni Lazima Wakristo wa Kweli Wote Wawe Waeneza Evanjeli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Mashahidi wa Yehova —Waeneza-Evanjeli wa Kweli
    Huduma Yetu ya Ufalme—1998
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
w74 12/1 kur. 540-546

Je! Wewe Unayo Roho ya Kueneza Injili?

1. Kwa sababu gani kazi ya kuzitangaza habari njema ni mojawapo ya kazi zilizo za maana sana zinazofanywa duniani?

KAZI ya kuzitangaza habari njema za Ufalme ni mojawapo ya kazi zilizo za maana zaidi zilizopata kufanywa duniani. Kwa sababu gani? Kwa maana ndio msingi ambao kwao wanadamu wanahukumiwa. Kuzikubali na kuzitii habari njema kunaleta wokovu; kuzikataa na kutokuzitii kwamaanisha uharibifu.

2, 3. (a) Toa mfano wa namna habari njema zinavyoifunua nia hasa ya mtu. (b) Ni maulizo gani awezayo mtu kujiuliza mwenyewe kwa kufaa juu ya habari njema?

2 Kwa mfano, huenda mtu akawa mpenda dini sana. Huenda akaonekana kuwa na utu mwema, kuwa mkarimu, mwenye huruma. Lakini anavyoziitikia habari njema yaonyesha wazi kama yeye ni rafiki ya Mungu kweli. Kwa maana Mungu aijua mioyo ya wanadamu. “Kila njia ya mtu ni sawa machoni pake mwenyewe,” asema mwandikaji wa Mithali, “bali [Yehova] huipima mioyo.” (Mit. 21:2) Lazima Mkristo awe na utu mwema, lakini bila ya kujali hali hiyo au nyingine yo yote, ikiwa yeye hampendi Mungu wala wanadamu wenzake, yeye ni bure tu.​—1 Kor. 13:1-3.

3 Je! wewe unazikubali habari njema? Je! unazitii? Je! unataka kuwaeleza wengine juu yazo? Je! ni lazima kwako uzitangaze habari njema ili upate kuzitii?

UBORA WA ROHO YA KUENEZA INJILI

4. Kwa sababu gani tutake kuzitangaza habari njema?

4 Habari zo zote njema tuzipokeazo tunataka kuzieleza kwa wengine, nasi mara nyingi twafanya hivyo kwa sababu ya furaha nyingi ya kuzieleza. Walakini, habari njema za Ufalme zinatuharakisha tuzieleze kwa wengine, si kwa sababu ya furaha tu, bali pia kwa sababu ya kuwapenda wanadamu wenzetu. Roho ya kueneza injili ni ya upendo kwa Mungu na jirani. Habari njema zamaanisha uzima kwa mpokeaji, na kwa hiyo ni lazima zitangazwe kote kote. Katika mojawapo ya barua zake za kwanza zilizoongozwa kwa roho, mtume Paulo aliandika kwamba wakati wa ufunuo wa Kristo kutoka mbinguni “wao wasioitii Injili ya Bwana wetu Yesu” ‘wangeadhibiwa kwa maangamizi ya milele.’​—2 The. 1:8, 9.

5. Mtume Petro alionyeshaje ubora wa habari njema?

5 Mtume Petro aliusisitizia ubora wa kuzijua na kuzitii habari njema alipozungumza juu ya kuhukumiwa kwa Wakristo, akisema hivi: “Na [hukumu] ikianza kwetu sisi, mwisho wao [Wakristo wa kujidai] wasioitii injili ya Mungu utakuwaje?” Akaongeza: “Na mwenye haki akiokoka kwa shida, yule asiyemcha Mungu na mwenye dhambi ataonekana wapi?” (1 Pet. 4:17, 18) Kwa hiyo, roho inayompasa mtangazaji wa habari njema kuwa nayo si ya kuzitangaza tu, bali kuziimarisha mioyoni mwa wasikiaji. Kwa sababu gani? Kwa maana hata mtu mwenye haki kati ya Wakristo wa kujidai ataokolewa “kwa shida” sana.

6. Biblia inalitumiaje neno “mhubiri wa injili” kwa njia ya pekee?

6 Neno la Kigiriki lililotumiwa katika Biblia la “habari njema” ni eu·ag·geʹli·on, au “injili.” Biblia inalitumia neno “mhubiri wa injili” kwa habari ya watu fulani walioagizwa, kwa maana inatuambia kwamba Yesu aliwapa wanadamu zawadi alipopaa mbinguni, “wengine kama mitume, wengine kama manabii, wengine kama wahubiri wa injili, wengine kama wachungaji na waalimu, kwa kusudi la kutengenezwa upya kwa watakatifu, kwa kazi ya huduma, kwa kujengwa kwa mwili wa Kristo.” (Efe. 4:11, 12, NW) Hawa “wahubiri wa injili” wanaelekea kuwa walipewa roho ya Mungu yenye nguvu kwa njia ya pekee katika kuhubiri, kuzoeza na kujenga wengine. Filipo alikuwa mmoja wao.​—Matendo 21:8, 9.

7. Imewapasa watangazaji wote wa habari njema waweje wahubiri wa injili, katika maana ya jumla?

7 Hata hivyo, watangazaji wote wa habari njema ni wahubiri wa injili, katika maana ya jumla. Bila shaka imewapasa wawe na roho ya kueneza injili. Imewapasa wazitangaze habari njema, lakini wasiachie hapo. Imewapasa wafanye yote wawezayo kuzoeza na kujenga wengine ili nao waweze kuwa na roho ile ile yenye nguvu. Ili wafanye hivi imewapasa watumie nafasi zote kuzungumza juu ya habari njema. Wakristo wa karne ya kwanza wanatutolea mifano mingi.

KUZITANGAZA HABARI NJEMA KATIKA KARNE YA KWANZA

8. Ni kwa njia gani na wapi Yesu alifanya kazi ya kueneza injili?

8 Yesu mwenyewe “alikuwa akizunguka-zunguka katika miji na vijiji akihubiri na kuitangaza habari njema ya ufalme wa Mungu; na wale Thenashara walikuwa pamoja naye.” (Luka 8:1) Karibu safari zote za Yesu alitembea kwa miguu. Wakati fulani aliwatuma wanafunzi wake wamtangulie ili kijiji au mji umtazamie na kuwa tayari kumsikiliza. (Luka 10:1) Yeye alifundisha alipoweza kufikia watu. Huenda ikawa ni kijijini, katika mahali pake mwenyewe alipoishi, masinagogini, pwani, juu ya mlima. Naye alizungumza na wale aliokutana nao njiani, au akipumzika​—kwa ufupi, wakati wo wote na mahali po pote watu walipokuwa.​—Mt. 5:1; 13:1, 2; 26:6-13; Marko 2:1, 2; 3:1-5; Yohana 4:6-10.

9, 10. Filipo aliienezaje injili, naye anaweza kulinganishwa namna gani na wengine wa mashahidi wa Yehova leo?

9 Wengine wa wahubiri wa injili katika karne ya kwanza walisafiri sana. Walikwenda mahali ambapo Mungu alifunua ulikuwako uhitaji wa utumishi wao. Twasoma kwamba Filipo alishuka kwenda Samaria. Baada ya kufanya kazi njema huko aliamriwa na malaika wa Yehova aelekee kusini kwenye njia ya kutoka Yerusalemu kwenda Gaza. Huko alimweleza towashi wa Ethiopia habari njema. Roho ya Mungu ilimwondoa huko kumwelekeza Azoto “na alipokuwa akipita akahubiri Injili katika miji yote, hata akafika Kaisaria.” (Matendo 8:4-40) Huko twamkuta baadaye akiwa katika nyumba moja, akiwa mwanamume mwenye jamaa.​—Matendo 21:8, 9.

10 Kwa njia fulani, Filipo anaweza kulinganishwa na “mapainia,” “mapainia wa pekee” na wamisionari kati ya mashahidi wa Yehova, ambao wana agizo la pekee la kuhubiri. Lakini roho njema ya kueneza injili inaonyeshwa na wale wanaohama kwenda sehemu zilizo na uhitaji mkubwa kwa wengine kuhubiri. Wengine wao wana jamaa, kama vile Filipo alivyokuwa na jamaa.

11. Paulo aliienezaje injili?

11 Paulo alikuwa mmoja wa wahubiri wa injili waliofanya kazi sana. Alisafiri sana katika Asia na Ulaya, akizitangaza habari njema mahali pote alipokwenda. Alijaribu kuhubiri mahali ambapo habari njema hazikuwa zimetangazwa hasa. Mahali pengine alikaa muda mrefu, aanzishe makundi na kuyatia nguvu. Inapendeza kuona kwamba katika utendaji huu wa kueneza injili Paulo alijiruzuku mwenyewe kwa kufanya biashara fulani.​—2 Kor. 10:13-16; Matendo 18:1-4; 19:8-10; 1 Kor. 9:15-18.

SI LAZIMA KUENEZA INJILI KUTIE NA KUSAFIRI

12. Je! kusafiri ni sehemu ya lazima ya kueneza injili?

12 Ijapokuwa ni kweli kwamba hawa wahubiri wa injili walisafiri sana, si lazima tusafiri kwenda mahali pengine tukahubiri ikiwa tunayo roho ya kueneza injili. Kwa maana roho ya kueneza injili siyo roho ya kusafiri wala ya kuonyesha ujasiri wa mtu kwa tendo fulani. Ikiwa mtu hana madaraka yanayoweza kumzuia asihame, anaweza kupewa mgawo wa kwenda mahali palipotajwa wazi ambako utumishi wake unahitajiwa sana, kupitia kwa wale wanaosimamia kazi ya kuhubiri katika nchi fulani, ikiwa yeye anajitoa afanye hivyo. Kusafiri kwake huenda kukakomea hapo, kwa maana huenda akawa mkaaji wa huko, kama vile Filipo alivyofanya katika Kaisaria, na kuendelea kuzitangaza habari njema, kujenga kundi huko. Huenda akakaa huko miaka mingi, hata maisha yote, kama vile wengi wa wamisionari wa mashahidi wa Yehova.

13. Ni mfano gani unaotuonyesha kwamba twaweza kueneza injili bila ya kuhama kutoka nyumbani kwetu?

13 Lakini huenda watu wengine wasiweze kuhama, kwa sababu ya madaraka ya jamaa, afya au sababu nyingine. Hata hivyo, ikiwa wao wana roho ya kueneza injili wanaweza kutimiza mambo mengi mema pale pale wanapoishi. Kwa mfano, kuna kundi dogo katika tarafa ya Arkansas, United States. Shahidi mmoja ameishi huko miaka mingi. Mwenendo wake umekuwa mwema hata kila mtu maili nyingi kumzunguka anamjua kama mwenye utu wa Kikristo, naye ana sifa njema kwa sababu ya uaminifu na unyofu. Kundi ni dogo, lakini kama wote wale waliozisikia habari njema wakazikubali kwa sababu ya kuhubiri kwake na mfano wake wangalibaki katika eneo hilo, kungalikuwa na kundi kiasi cha mtaa huo mdogo. Lakini mwanamume huyu na mkewe walijitahidi sana, nao waliweka mfano mwema wa upendo na maisha ya Kikristo, wakazoeza wapya waliozikubali habari njema vema, hata wakatia roho ya kueneza injili katika wasikiaji wao kwa kadiri ya kwamba wao, pia, walihamia sehemu ambako uhitaji ni mkubwa. Hesabu kubwa ajabu ya watu wametoka katika kundi hili kuelekea kwenye shule ya Gileadi ya umisionari nao wakapelekwa nchi za ugenini wakatumikie. Je! mwanamume huyu na mkewe wavunjike moyo kwa sababu hawakuweza kusafiri kwenye sehemu ambako habari njema hazikutangazwa sana hivyo? Hata kidogo. Yehova amewabariki sana, na kazi yao nyumbani imekuwa na matokeo ya ulimwenguni pote.

14. Ikiwa unayo roho ya kueneza injili, ni kwa njia gani ulivyo na nafasi nyingi kuhubiri pale pale mtaani pako?

14 Kwa hiyo, po pote ulipo, unazo nafasi nyingi za kuhubiri. Kuna kuhubiri mlango kwa mlango kwa habari njema. Halafu wako wale usiowakuta nyumbani kwao mara nyingi. Unaweza kuwaona hawa kazini pako kila siku, dukani kwako au unaposafiri. Unawakuta wameketi katika magari katika viwanja vya kuwekea magari, katika vibanda vya petroli, katika bustani za starehe. Ikiwa unayo roho ya kutaka kuzishiriki habari njema na wengine, si lazima sikuzote uwe na wakati wa pekee. Wewe u shahidi wa Yehova wakati wote! Unawaeleza wengine habari njema kwa maana zimo moyoni mwako, nawe unajikuta ukizungumza juu yazo au ukitafuta nafasi za kuzungumza juu yazo chini ya hali zote.​—Yer. 20:9.

KUENEZA INJILI KWAMAANISHA MENGI ZAIDI KULIKO KUTANGAZA TU

15. Ni kwa njia gani kulivyo na mengi zaidi katika roho ya kueneza injili kuliko tu kuwaeleza wengine habari njema?

15 Sasa, kuna mengi yanayohitajiwa katika roho ya kueneza injili kuliko kuwaeleza wengine tu habari njema. Mna maana nyingi sana katika habari njema, na mambo mengine “ni vigumu kuelewa nayo.” (2 Pet. 3:16) Inahitaji kuwaza kwa upande wako kuamua namna ya kumweleza mwanafunzi wako wa habari njema mambo haya. Si hayo tu, bali ni jambo moja kutia maarifa akilini na jingine kutia mambo moyoni ndani. Utaona kwamba mbegu ilianguka wapi, katika mfano wa Yesu wa mpanzi? Mioyoni. Wewe kama mhubiri wa habari njema unataka kuisitawisha mbegu moyoni mwa mwanafunzi wako.​—Mt. 13:19.

16. Paulo alikuwaje mfano mwema wa mweneza injili kweli kweli?

16 Lazima mhubiri wa injili apende watu, kama vile mtume Paulo alivyoonyesha, na kama anavyoeleza, akisema hivi: “Nasi tukiwatumaini kwa upendo mwingi, tuliona furaha kuwapa, si Injili ya Mungu tu, bali na [nafsi] zetu pia, kwa sababu mmekuwa wapendwa wetu.” (1 The. 2:8) Paulo na wenzake walijitoa kabisa kwa ajili ya wale waliokuwa Thesalonike waliokuwa wamezikubali habari njema. Wakati na nguvu za Paulo zilitumiwa kwa ajili yao, naye alitaka na kujaribu kwa moyo wake wote kuwafanya wawe na upendo ule ule wenye shauku nyingi juu ya habari njema kwa kuuonyesha katika kila upande wa maisha zao.

17. Ikiwa unayo roho ya kweli ya kueneza injili, utawaonaje na kufanyaje kazi pamoja na wale unaowatangazia habari njema?

17 Je! wewe unajisikia hivyo na kujitahidi kwa ajili ya wale unaowapelekea habari njema? Ikiwa ndivyo, hutakuwa mchoyo kwao. Hutawahesabu kama “kondoo” zako, bali utawaangalia kama mali ya Bwana Yesu Kristo, Mchungaji Mkuu. (1 Pet. 5:1-4) Utajaribu kutia ndani yao roho ya Mungu. Utajaribu kuwafahamisha sana na wengine wa kundi kama iwezekanavyo, kwa maana unajua kwamba “pana tofauti za karama; bali [roho ni ile ile]. Tena pana tofauti za huduma, na Bwana ni yeye yule. Kisha pana tofauti za kutenda kazi, bali Mungu ni yeye yule azitendaye kazi zote katika wote. Lakini kila mmoja hupewa ufunuo wa [roho] kwa kufaidiana.” (1 Kor. 12:4-7) Utafahamu kwamba wewe huna uwezo wote wala ufunuo wote wa roho ya Yehova. Lakini unajua kwamba kwa kushirikiana na kundi, watu wapya wanaopendezwa watakuwa mahali ambapo roho ya Yehova inatenda sana nao watakomazwa na ushirika huo.

KUJENGA NA KUZOEZA

18. Lengo lako ni nini unapojifunza Biblia na mtu?

18 Roho ya kueneza injili haionyeshwi na kadiri ya wakati tu uliotumiwa kwa kuhubiri wengine. Inatia na matokeo ya kujenga kwa mtu na kuzoeza kwake wengine. Huenda mtu unayejifunza naye akayashika mengine ya mafundisho ya msingi, kama vile ukweli wa paradiso ya kidunia, makosa ya mafundisho kama vile kutokufa kwa nafsi ya kibinadamu, moto wa mateso na Utatu. Huenda akawa na maarifa mengi kichwani juu ya mambo haya. Huenda akaweza kuyajibu vema maulizo katika funzo. Lakini huelekezi lengo lako kichwani hasa bali moyoni. Basi, je! mambo unayotaka kuyatia moyoni mwake kumwimarisha, kumfanya Mkristo aliyekomaa ni nini?​—Ebr. 6:1-3.

19. (a) Taja mengine ya mambo ya lazima sana utakayoyakumbuka uyatie moyoni mwa mwanafunzi wako. (b) Imempasa apate maoni gani juu ya Mungu?

19 Utataka uchunguze sikuzote na kukumbuka sikuzote mambo yafuatayo yaliyo ya lazima, na ni juu yako kujitahidi kumsaidia yule unayejifunza naye ayaelewe: Je! mwanafunzi wako anapata kumjua Yehova, yaani, yeye anaelewa sababu gani Yehova anataka habari njema zipelekwe kwake na kwa wengine? Je! anaelewa sababu gani Mungu ameacha uovu uendelee kwa kitambo na sababu gani haufutilii mbali mara moja, kulingana na tamaa ya wanadamu? Je! analielewa vizuri ulizo la enzi kuu ya Yehova, na fadhili za upendo za Mungu katika kuruhusu wakati utumiwe kulijibu ulizo? Je! anaona kwamba mambo yanayotukia duniani yanamwudhi Mungu zaidi kuliko yanavyotuudhi sisi? kwamba Mungu anajizuia kwa ajili ya faida ya wanadamu wenyewe, ijapokuwa anaweza kukomesha mabaya? (Linganisha Mwanzo 6:3, 5-7.) Je! anafahamu kwamba sifa zote njema tulizo nazo kwa kadiri fulani, Mungu anazo kwa kadiri kubwa zaidi​—upendo, shukrani, huruma, fadhili, rehema, uvumilivu? Je! yeye anamwona Mungu kama rafiki mkubwa, kama anayetaka kumfanyia lo lote la kumfaidi? Lazima apate kumjua Mungu kama Mthamini wa wale wanaomtumikia hata katika utumishi mdogo zaidi wanaoutoa kwa moyo. Yeye anayempendeza Mungu lazima aamini kwamba ndiye Mthawabishaji wa wale wanaomtafuta. (Ebr. 11:6) Yeye ni Mungu wa namna hiyo. Wale wote walio na roho hii ya kweli ya kueneza injili wanajua hii ni kweli, na kwa hiyo wanajaribu kuitia tamaa ii hii katika wengine wampende Yeye na kumtumikia kwa ajili ya sifa zake zisizo na kifani.​—Kut. 34:6, 7; Zab. 145:8-21.

20, 21. (a) Tunataka wanafunzi wetu wa Biblia wapate nini? (b) Twawezaje kuwasaidia wasitawishe uhusiano wa kipekee na Mungu, badala ya kututegemea sisi kama waalimu wao?

20 Kwa hiyo, unapowafundisha na kuwazoeza wale wanaozikubali habari njema, imekupasa sikuzote uyakumbuke sana mambo haya, na kuyatia sikuzote mioyoni mwa wasikiaji wako. Unawataka wakomae, ambako kunatia na uwezo wa kufahamu yaliyo haki na mabaya. (Ebr. 5:14) Lo lote uwafundishalo, lo lote wajifunzalo, lihusianishe na upendo wa Yehova, rehema, huruma na sifa nyingine. Waonyeshe kwamba Yehova ndiye anayependezwa nao, na kwamba yote wanayojifunza yanatokana na Chanzo hicho kikuu, na kwa sababu ya yeye kuwahurumia wao.

21 Waelekeze wanafunzi wako wajue kwamba wanaweza kuwa na uhusiano wa kipekee na Mungu. Hawajifunzi mafundisho yasiyowahusu, wala hawaelewi kwa sababu ya akili yao au wema wao wenyewe. Kupendezwa kwa Mungu na wanadamu ndiko kumewafanya wazielewe habari njema. Waonyeshe ni kibali ya Mungu iliyofanya Yeye aone inafaa kuwaruhusu waelewe; bila ya utendaji wa roho yake habari njema zisingalieleweshwa kwao kamwe. Wenye hekima wa ulimwengu huu wana akili nyingi sana, lakini hawawezi kuzielewa habari njema. (Mt. 11:25; 1 Kor. 1:19-21) Wajulishe kwamba wewe u chombo tu cha kukazia mambo kwenye fikira zao. Yehova ndiye Mwalimu Mkuu wa watu wake.​—Isa. 30:20; 54:13.

22. Twawezaje kumtayarisha mwanafunzi wetu kwa mateso yatakayompata?

22 Unapomzoeza mtu mpya anayependezwa, unajua kwamba atapingwa na hata kuteswa. Mtayarishe kwa haya, na umwonyeshe sababu gani mateso yanakuja, na sababu gani Mungu anayaruhusu. Msaidie aelewe maandiko ya Biblia yanayoonyesha kwamba wale wanaoteswa wana pendeleo kubwa sana. Ni uhakikisho wa kwamba roho ya Mungu i juu ya mtu. Si jambo la kuaibikia au kuonea haya, bali jambo analopaswa kuruka kwa furaha kwa ajili yake. (Mt. 5:11, 12; Flp. 1:27, 28; 2 Tim. 1:8; Yak. 1:2, 12; 1 Pet. 4:12-14) Mtie nguvu apambane na upinzani uwezao kutokana na jamaa au rafiki kwa maneno ya Yesu katika Marko 10:29, 30. Unaweza kumtia moyo avumilie kwa uaminifu akitumaini kwamba mwishowe huenda akaweza kuwaletea wokovu wale anaohusiana nao na wapendwa wake.

23. Ni jambo gani la maana tusilopaswa kusahau kabla ya kuwatia wanafunzi wetu wa Biblia moyo waende nasi katika utumishi wa shambani, nasi twawezaje kulishughulikia jambo hili?

23 Kwa kuwa roho ya kueneza injili inatia na kuzoeza, lazima tuhakikishe kwamba wanafunzi wanastahili kuwa wahubiri wa habari njema, tunapowafanya wawe kama Bwana yao Yesu Kristo. Watu wasikaribishwe kushiriki pamoja na washiriki wa kundi kuhubiri kabla hawajasafisha maisha zao kabisa waweze kustahili. Lazima wajue kwamba inawapasa wote wanaovichukua vyombo vya Yehova wawe safi. (Isa. 52:11; 2 Kor. 7:1) Lazima waone kwamba kupata “alama” ya utu wa Kikristo ndiko kunakompendeza Mungu na kuizuia hasira yake isiwajie.​—Eze. 9:4-6; Efe. 4:23, 24.

24, 25. (a) Ni watu wa namna gani peke yao ambao Mungu anataka wamtumikie? (b) Je! twaweza kudai kwamba mwanafunzi wa Biblia aziache tabia zake zote na mazoea yaliyo mabaya mara moja, au namna gani?

24 Mungu anataka kutumikiwa na watu walio Wakristo kabisa kabisa. Yeye hapendezwi na wingi, kuwa na hesabu kubwa tu ya wahubiri wa habari njema. Lakini anawatoa wale wanaotaka kujisafisha katika hii taratibu chafu ya mambo. Roho yake, anayoiweka juu ya wale wanaomtii, ni nguvu ya usafi. Ikiwa mtu anafuata mwendo mchafu, analipinga kusudi la Mungu kutuma roho yake, nayo roho hiyo haitamsaidia.​—1 The. 4:7, 8.

25 Kwa hiyo ni jambo la hekima kutia kanuni hizi za maisha yafaayo mioyoni mwa watu wanaopendezwa tangu mwanzo. Kwa kweli, hawawezi kutazamiwa wasafishe maisha zao mara moja, lakini wewe utajitahidi kidogo kidogo uufikie mradi huo ikiwa unayo roho ya kueneza injili. Hii yaweza kufanywa kwa fadhili na busara na bila ya kupeleleza-peleleza maisha zao isivyofaa. Kusudi lako ni kumjua mwanafunzi wako na kumsaidia anapohitaji msaada. Ndipo unapoweza kwenda pamoja naye, ukimzoeza kuzitangaza habari.

26. Ni nini lililo la lazima kabla ya kumtia mtu mpya moyo abatizwe?

26 Vivyo hivyo, usimtie mtu moyo abatizwe mpaka ujue kwamba amesafisha maisha yake kweli kweli na ameishi akiwa katika hali hii safi muda mrefu wa kutosha kuonyesha kwamba hatarudia tabia na mazoea mabaya.

27. Ni nini thawabu za kuwa na roho ya kueneza injili?

27 Roho ya kueneza injili inaleta furaha nyingi sana. Hakuna furaha iliyo kuu kupita ile ya kuweza kulitetea jina la Yehova katika ulimwengu usiomcha yeye, na kuwaletea wengine nuru na tumaini. Halafu, unapowaona wale unaowasaidia wakipata kumjua na kumthamini Yehova na Yesu Kristo na yale waliyoyafanya, furaha yako inaongezeka. Roho ya kueneza injili inaondosha roho ya wivu au kijicho. Inafurahia maendeleo ya kiroho ya wengine, hasa wale unaowasaidia. Unajisikia kama vile mtume Paulo alivyotaka Timotheo ajisikie katika habari hii: “Mambo yale uliyoyasikia kwangu mbele ya mashahidi wengi, hayo uwakabidhi watu waaminifu watakaofaa kuwafundisha na wengine.”​—2 Tim. 2:2; 1 Kor. 10:24.

28. Ikiwa unajisikia kupungukiwa kidogo na roho ya kueneza injili, unaweza kufanya nini uipate au uiongeze?

28 Kwa hiyo, watumishi wote wa kweli wa Yehova wanatamani kuisitawisha roho ya kueneza injili ndani yao wenyewe na ndani ya wengine. Ikiwa unatamani kuzidisha roho hii ndani yako mwenyewe, ushirikiane sana na wale walio na hii nia njema, na uombe msaada wa wazee kundini. Wao watafurahia kukusaidia, kwa maana wanajua kwamba inamtukuza Mungu na kusaidia kuleta wokovu wao wenyewe na wa wale wanaowasaidia.​—1 Tim. 4:16.

[Picha katika ukurasa wa 542]

Filipo alikuwa na roho ya kueneza injili . . .

[Picha katika ukurasa wa 543]

. . . Je! wewe unayo?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki