Ni Lazima Wakristo wa Kweli Wote Wawe Waeneza Evanjeli
“Fanya kazi ya mweneza evanjeli [au, mishonari].”—2 TIMOTHEO 4:5, NW, kielezi-chini.
1. Habari njema iliyohubiriwa na waeneza evanjeli wa karne ya kwanza ilikuwa nini?
KUNAMAANISHA nini leo kuwa mweneza evanjeli? Je! wewe ni mmoja? Maneno “mweneza evanjeli” hutokana na neno la Kigiriki eu·ag·ge·li·stesʹ, linalomaanisha “mhubiri wa habari njema.” Tangu mwanzo wa kundi la Kikristo katika 33 W.K., habari njema ya Kikristo ilikazia njia ya Mungu ya wokovu na ilipiga mbiu kwamba Yesu Kristo angerudi katika wakati wa baadaye ili kuanza utawala wake wa Ufalme juu ya ainabinadamu.—Mathayo 25:31, 32; 2 Timotheo 4:1; Waebrania 10:12, 13.
2. (a) Yaliyomo katika habari njema yameongezewaje ubora katika siku yetu? (b) Wakristo wa kweli wote leo wana wajibu gani?
2 Tangu 1914 na kuendelea, ushuhuda ulianza kuongezeka wa kwamba ile ishara ambayo Yesu alikuwa ametoa kuhusu kurudi kwake na kuwapo kwake kusikoonekana ilikuwa ikitimizwa. (Mathayo 24:3-13, 33) Mara nyingine tena, habari njema ingeweza kutia ndani ule usemi “ufalme wa Mungu u karibu.” (Luka 21:7, 31; Marko 1:14, 15) Kwa kweli, wakati ulikuwa umekuja wa ule unabii wa Yesu uliorekodiwa kwenye Mathayo 24:14 kutimizwa kwa ukubwa zaidi: “Habari njema ya ufalme itahubiriwa katika ulimwengu wote, kuwa ushuhuda kwa mataifa yote; hapo ndipo ule mwisho utakapokuja.” Kwa hiyo, kueneza evanjeli sasa hutia ndani kutangaza kwa bidii Ufalme wa Mungu uliosimamishwa na baraka utakazoiletea ainabinadamu hivi karibuni. Wakristo wote wako chini ya amri ya kufanya kazi hiyo na ‘kuwafanya wanafunzi.’—Mathayo 28:19, 20; Ufunuo 22:17.
3. (a) Maneno “mweneza evanjeli” yana maana gani ya ziada? (Ona Insight on the Scriptures, Buku 1, ukurasa 770, safu 2, fungu 2.) (b) Hilo linatokeza maswali gani?
3 Kuongezea kuhubiriwa kwa habari njema kwa ujumla, Biblia hutumia maneno “mweneza evanjeli” katika maana ya pekee kuhusu wale wanaoacha eneo lao la nyumbani ili kuhubiri habari njema katika maeneo yasiyopata kuhubiriwa. Katika karne ya kwanza, kulikuwako waeneza evanjeli wamishonari wengi, kama vile Filipo, Paulo, Barnaba, Sila, na Timotheo. (Matendo 21:8; Waefeso 4:11) Lakini namna gani wakati wetu wa pekee tangu 1914? Je! watu wa Yehova leo wamejitolea wapatikane kuwa waeneza evanjeli wa mahali fulani na kuwa wamishonari pia?
Maendeleo Tangu 1919
4, 5. Ni yapi yaliyokuwa mataraja ya kazi ya kueneza evanjeli muda mfupi baada ya 1914?
4 Vita ya Ulimwengu 1 ilipokaribia mwisho katika 1918, watumishi wa Mungu walipatwa na upinzani wenye kuongezeka kutoka kwa waasi-imani pamoja na makasisi wa Jumuiya ya Wakristo na marafiki wao wa kisiasa. Kwa kweli, uenezaji evanjeli wa kweli wa Kikristo karibu ukome katika Juni 1918 wakati maofisa wenye kuongoza wa Watch Tower Society katika United States walipohukumiwa kifungo cha gerezani cha miaka 20 chini ya mashtaka bandia. Je! maadui wa Mungu walikuwa wamefaulu kukomesha kuhubiriwa kwa habari njema?
5 Bila kutazamiwa, katika Machi 1919 maofisa wa Sosaiti waliachiliwa na baadaye kuondolewa mashtaka yale bandia yaliyokuwa yamesababisha kufungwa kwao gerezani. Wakiwa na uhuru wao mpya, Wakristo hao wapakwa-mafuta walitambua kwamba kulikuwako kazi nyingi ya kufanywa kabla ya wao kuweza kukusanywa ili kupata thawabu yao ya kimbingu wakiwa warithi washirika katika Ufalme wa Mungu.—Warumi 8:17; 2 Timotheo 2:12; 4:18.
6. Kazi ya kueneza evanjeli iliendeleaje kati ya 1919 na 1939?
6 Huko nyuma katika 1919 kulikuwako punde kuliko 4,000 walioripoti wakishiriki katika kueneza habari njema. Wakati wa miongo miwili iliyofuata, idadi fulani ya wanaume walijitolea kuwa waeneza evanjeli wamishonari, na baadhi yao walitumwa kwenda nchi za Afrika, Esia, na Ulaya. Kufikia 1939, baada ya miaka 20 ya kuhubiriwa kwa Ufalme, Mashahidi wa Yehova walikuwa wameongezeka hadi zaidi ya 73,000. Ongezeko hilo lenye kutokeza, lililotimizwa ujapokuwa mnyanyaso mwingi, lilifanana na lile lililotukia katika miaka ya mapema ya kundi la Kikristo.—Matendo 6:7; 8:4, 14-17; 11:19-21.
7. Katika miaka ya 47 W.K. na 1939, ni hali gani yenye kufanana iliyokuwako kuhusu kazi ya kueneza evanjeli ya Kikristo?
7 Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova wengi wakati huo walikuwa katika nchi za Kiprotestanti zilizosema Kiingereza. Kwa kweli, zaidi ya asilimia 75 ya wale wapiga mbiu ya Ufalme 73,000 walitoka Australia, Uingereza, Kanada, New Zealandi, na United States. Sawa na jinsi hali ilivyokuwa yapata 47 W.K., jambo fulani lilihitajiwa ili kuwatia moyo waeneza evanjeli watolee uangalifu mwingi zaidi nchi za dunia zisizohubiriwa sana.
8. Kufikia 1992, Shule ya Gileadi ilikuwa imetimiza nini?
8 Vizuizi na minyanyaso ya wakati wa vita haingeweza kuizuia roho takatifu ya Yehova yenye nguvu isiwachochee watumishi wake watayarishe kwa ajili ya upanuzi mkubwa zaidi. Katika 1943, wakati Vita ya Ulimwengu 2 ilipokuwa katika upeo wayo, tengenezo la Mungu lilianzisha ile shule ya Watchtower Bible School of Gilead likiwa na kusudi la kueneza habari njema katika mahali pengi zaidi. Kufikia Machi 1992, shule hiyo ilikuwa imetuma wamishonari 6,517 kwenye nchi tofauti-tofauti 171. Kwa kuongezea, wanaume walizoezwa kutunza matawi ya Watch Tower Society katika nchi za kigeni. Kufikia 1992, kati ya waratibu wa Halmashauri ya Tawi 97, ni 75 waliokuwa wamezoezwa Gileadi.
9. Ni programu zipi za mazoezi ambazo zimesaidia katika maendeleo ya kazi ya kueneza evanjeli na kufanya wanafunzi?
9 Zaidi ya Shule ya Gileadi, programu nyinginezo za mazoezi zimewasaidia watu wa Yehova wapanue na kufanyia maendeleo kazi yao ya kueneza evanjeli. Kwa mfano Shule ya Huduma ya Kitheokrasi huongozwa katika makundi ya Mashahidi wa Yehova kotekote duniani. Mpango huo, pamoja na Mkutano wa Utumishi wa kila juma, umezoeza mamilioni ya wahubiri wa Ufalme kuwa wenye mafanikio katika huduma ya peupe. Pia kuna ile Shule ya Huduma ya Ufalme, inayowaandalia wazee na watumishi wa huduma mazoezi yenye thamani ili waweze kuyatunza vema zaidi makundi yanayokua. Shule ya Utumishi wa Painia imewasaidia waeneza evanjeli wengi wa wakati wote wawe na mafanikio zaidi katika utendaji wao wa kuhubiri. Hivi karibuni zaidi, Shule ya Mazoezi ya Kihuduma imeongozwa katika nchi tofauti-tofauti ili kuwasaidia wazee na watumishi wa huduma wasiofunga ndoa wawe akina Timotheo wa ki-siku-hizi.
10. Tokeo limekuwa nini la yale mazoezi yote bora sana yaliyoandaliwa na tengenezo la Mungu? (Tia ndani habari iliyomo katika sanduku.)
10 Tokeo la mazoezi hayo limekuwa nini? Katika 1991, Mashahidi wa Yehova walikuwa wamefikia kilele cha wahubiri wa Ufalme wenye kutenda wanaozidi milioni nne kwa mbali katika nchi 212. Hata hivyo, tofauti na ile hali iliyokuwako katika 1939, zaidi ya asilimia 70 ya hao hutoka nchi za Katoliki, Orthodoksi, zisizo za Kikristo, na, nyinginezo ambako Kiingereza si lugha inayozungumzwa na wengi.—Ona sanduku “Upanuzi Tangu 1939.”
Sababu Kwa Nini Wamefanikiwa
11. Mtume Paulo alimhesabia nani mafanikio yake akiwa mhudumu?
11 Mashahidi wa Yehova hawajisifu kwa ajili ya upanuzi huo. Badala ya hivyo, wao huona kazi yao kwa njia ambayo mtume Paulo aliiona, kama alivyoeleza katika barua yake kwa Wakorintho. “Basi Apolo ni nani? na Paulo ni nani? Ni wahudumu ambao kwao mliamini na kila mtu kama Bwana alivyompa. Mimi nilipanda, Apolo akatia maji; bali mwenye kukuza ni Mungu. Hivyo apandaye si kitu, wala atiaye maji, bali Mungu akuzaye. Maana sisi tu wafanya kazi pamoja na Mungu; ninyi ni shamba la Mungu, ni jengo la Mungu.”—1 Wakorintho 3:5-7, 9.
12. (a) Neno la Mungu lina daraka gani katika uenezaji evanjeli wa Kikristo wenye mafanikio? (b) Ni nani ambaye amewekwa rasmi kuwa Kichwa cha kundi la Kikristo, na ni njia gani moja ya maana ya kuonyesha ujitiisho wetu kwa ukichwa wake?
12 Hakuna shaka kwamba ukuzi huo wa ajabu unaoonwa na Mashahidi wa Yehova ni kwa sababu ya baraka ya Mungu. Ni kazi ya Mungu. Kwa kutambua jambo hilo la hakika, wao huendelea kujitahidi kujifunza Neno la Mungu kwa kawaida. Wao hutegemeza juu ya Biblia kila jambo wafundishalo katika kazi yao ya kueneza evanjeli. (1 Wakorintho 4:6; 2 Timotheo 3:16) Ufunguo mwingine wa uenezaji evanjeli wao wenye mafanikio ni kumtambua kwao kikamili Yule ambaye Mungu ameweka rasmi kuwa Kichwa cha kundi, yaani, Bwana Yesu Kristo. (Waefeso 5:23) Wakristo wa karne ya kwanza walionyesha hilo kwa kushirikiana na wale ambao Yesu aliweka rasmi kuwa mitume. Wanaume hao, pamoja na wazee wengine wa kundi la Yerusalemu, walifanyiza lile baraza linaloongoza la Kikristo la karne ya kwanza. Kutoka mbinguni Bwana Yesu Kristo alitumia kikundi hicho cha Wakristo wakomavu ili kusuluhisha masuala na kuelekeza kazi ya kueneza evanjeli. Ushirikiano wa Paulo wenye bidii na mpango huo wa kimungu ulitokeza maongezeko katika makundi ambayo alitembelea. (Matendo 16:4, 5; Wagalatia 2:9) Leo vilevile, kwa kushikamana sana na Neno la Mungu na kushirikiana kwa bidii na mwelekezo unaokuja kutoka kwa Baraza Linaloongoza, waeneza evanjeli Wakristo wanahakikishiwa mafanikio katika huduma yao.—Tito 1:9; Waebrania 13:17.
Kuwaona Wengine Kuwa Bora Zaidi
13, 14. (a) Mtume Paulo alitoa shauri gani kama lilivyorekodiwa kwenye Wafilipi 2:1-4? (b) Kwa nini ni jambo la maana kukumbuka shauri hilo tunaposhiriki katika kazi ya kueneza evanjeli?
13 Mtume Paulo aliwaonyesha watafutaji kweli upendo wa kweli na yeye hakuonyesha mtazamo wa kuwa bora zaidi au wa ubaguzi. Hivyo, angeweza kuwashauri waamini wenzake ‘wawahesabu wenziwe kuwa bora kuliko nafsi zao.’—Wafilipi 2:1-4.
14 Kwa njia iyo hiyo, waeneza evanjeli Wakristo wa kweli leo hawajioni wenyewe kuwa bora zaidi wanaposhughulika na watu wa rangi na malezi tofauti-tofauti. Mmoja wa Mashahidi wa Yehova kutoka United States aliyepewa mgawo wa kufanya kazi akiwa mishonari katika Afrika, asema hivi: “Mimi najua tu kwamba sisi si bora zaidi. Labda tuna pesa nyingi zaidi na ile iitwayo elimu rasmi, lakini wao [watu wa mahali hapo] wana sifa zinazoshinda zetu.”
15. Wale wanaopewa mgawo wa kufanya kazi katika nchi za kigeni wanaweza kuwaonyeshaje wale watakaokuwa wanafunzi staha ya kweli?
15 Kwa hakika, kwa kuwaonyesha staha ya kweli wale tunaoshiriki nao habari njema, tutakufanya kuwe rahisi zaidi kwao kukubali ujumbe wa Biblia. Inasaidia pia wakati mweneza evanjeli mishonari anapoonyesha anafurahia kuishi miongoni mwa watu ambao amepewa mgawo kuwasaidia. Mishonari mmoja mwenye mafanikio ambaye ametumia miaka 38 iliyopita katika Afrika hueleza hivi: “Ninahisi ndani yangu kabisa kwamba haya ni makao yangu na wale waliomo kundini ambamo nimepewa mgawo ni ndugu na dada zangu. Wakati ambapo nimerudi Kanada nikiwa likizoni, kwa kweli sijihisi nikiwa nyumbani. Katika juma la mwisho hivi katika Kanada, mimi hutamani sana kurudi kwenye mgawo wangu. Mimi huhisi hivyo sikuzote. Ninawaambia wanafunzi wangu wa Biblia na ndugu na dada jinsi ambavyo nimefurahi kurudi tena, nao wanathamini kwamba ninataka kuwa nao.”—1 Wathesalonike 2:8.
16, 17. (a) Wamishonari na waeneza evanjeli wa mahali fulani wamekubali kujitahidi kufanya nini ili kuwa wenye mafanikio zaidi katika huduma yao? (b) Mishonari mmoja alikuwa na ono gani kwa sababu ya kusema katika lugha ya huko?
16 Wanapopata kikundi kikubwa cha watu wanaosema lugha ya kigeni katika maeneo yao, baadhi yao wamejitahidi kujifunza hiyo lugha, wakionyesha kwa hilo kwamba wao huwaona wengine kuwa bora zaidi. “Katika kusini mwa Afrika,” aonelea mishonari mmoja, “nyakati nyingine kuna hisia ya kushuku kati ya Waafrika na Wazungu. Lakini kusema kwetu katika lugha ya kwao huondosha upesi hisia hiyo.” Kusema lugha ya wale tunaoshiriki habari njema nao ni msaada mkubwa wa kufikia mioyo yao. Kunahitaji jitihada nyingi na udumifu wenye unyenyekevu. Mishonari mmoja katika nchi moja ya Esia, asema hivi: “Kufanya-fanya makosa huku ukichekwa daima kwaweza kuwa mtihani. Huenda ikaonekana kuwa rahisi zaidi kukata tamaa.” Hata hivyo, kumpenda Mungu na jirani kulimsaidia mishonari huyo avumilie.—Marko 12:30, 31.
17 Kwa kueleweka, watu huchochewa wanapomwona mgeni akijitahidi kushiriki habari njema katika lugha yao. Nyakati nyingine inatokeza baraka zisizotazamiwa. Mishonari mmoja katika ile nchi ya Afrika ya Lesotho alikuwa akisema katika Kisesotho na mwanamke mwingine, aliyekuwa akifanya kazi katika duka la mazulia ya ukuta. Waziri wa serikali kutoka nchi nyingine ya Afrika alikuwa akitalii jumba hilo akasikia mazungumzo hayo. Waziri huyo alimjilia dada na kumpongeza kwa uchangamfu, kisha dada huyo akaanza kusema na waziri huyo wa serikali katika lugha yake mwenyewe. “Kwa nini usije [nchini mwangu] na kufanya kazi miongoni mwa watu wetu, kwa kuwa wajua Kiswahili pia?” akauliza. Kwa busara, huyo mishonari akajibu: “Ingekuwa vizuri sana. Lakini mimi ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova, na kwa sasa kazi yetu imepigwa marufuku katika nchi yenu.” “Tafadhali,” akajibu, “usihisi kwamba sisi sote huipinga kazi yenu. Wengi wetu tunawapenda Mashahidi wa Yehova. Labda siku moja mtaweza kufundisha bila kizuizi miongoni mwa watu wetu.” Wakati fulani baadaye, mishonari huyo alisisimuka kupata kujua kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa wamepewa uhuru wa ibada katika nchi ile waliyozungumzia.
Kuwa na Nia ya Kujinyima Haki
18, 19. (a) Paulo alijitahidi kumwiga Bwana Mkubwa wake, Yesu Kristo, katika njia gani ya maana? (b) Simulia ono (lile lililomo katika fungu au lako mwenyewe) kuonyesha umaana wa kuepuka sababu yoyote ya kuwakwaza wale tunaoshiriki habari njema nao.
18 Mtume Paulo alipoandika: “Mnifuate mimi kama mimi ninavyomfuata Kristo,” alikuwa ametoka tu kuzungumzia uhitaji wa kuepuka kuwakwaza wengine, akisema: “Mlapo, au mnywapo, au mtendapo neno lo lote, fanyeni yote kwa utukufu wa Mungu. Msiwakoseshe Wayahudi wala Wayunani wala kanisa la Mungu; vile vile kama mimi niwapendezavyo watu wote katika mambo yote, nisitake faida yangu mwenyewe, ila faida yao walio wengi, wapate kuokolewa.”—1 Wakorintho 10:31-33; 11:1.
19 Waeneza evanjeli kama Paulo, walio na nia ya kutoa dhabihu ili kuwanufaisha wale wanaowahubiri, huvuna baraka. Kwa mfano, katika nchi moja ya Afrika, wenzi wa ndoa wamishonari walienda kwenye hoteli moja ya huko kula mlo wa jioni ili kusherehekea ukumbusho wa kila mwaka wa arusi yao. Mwanzoni walitaka kuagiza divai pamoja na mlo huo, kwa kuwa utumizi wa vileo wenye kiasi haushutumiwi katika Biblia. (Zaburi 104:15) Lakini wenzi hao wa ndoa waliamua kutofanya hivyo iwapo ingewaudhi watu wa huko. “Wakati fulani baadaye,” akumbuka mume, “tulikutana na mtu mmoja aliyekuwa mpishi kwenye hoteli hiyo tukaanza funzo la Biblia pamoja naye. Baadaye zaidi alituambia: ‘Je! mwakumbuka wakati mlipokuja kwenye hoteli kula mlo wa jioni? Sisi sote tulikuwa nyuma ya mlango wa jikoni tukiwatazama. Ni hivi, wamishonari wa kanisa walituambia kwamba ni vibaya kwetu kunywa vileo. Hata hivyo, wanapokuja kwenye hoteli, wao huagiza divai bila kusita. Kwa hiyo tuliamua kwamba ikiwa ninyi mngeagiza kileo, tusingewasikiliza wakati mngekuja kutuhubiri.’” Leo, mpishi huyo na wengine waliofanya kazi kwenye hoteli hiyo ni Mashahidi waliobatizwa.
Kuna Mengi ya Kufanya Bado
20. Kwa nini ni jambo la muhimu tuvumilie tukiwa waeneza evanjeli wenye bidii, na wengi wanajitwalia pendeleo gani lenye shangwe?
20 Mwisho wa mfumo huu mbovu unapokaribia kwa kasi, wengi bado hutamani kusikia habari njema, na ni jambo la muhimu zaidi ya wakati mwingine wowote kwa kila Mkristo kuvumilia akiwa mweneza evanjeli mwaminifu. (Mathayo 24:13) Je! wewe waweza kupanua kushiriki kwako katika kazi hii kwa kuwa mweneza evanjeli katika namna ya pekee kama vile Filipo, Paulo, Barnaba, Sila, na Timotheo? Wengi wanafanya jambo linalofanana na hilo kwa kujiunga katika idadi ya mapainia na kujifanya wenyewe wapatikane ili kutumikia katika sehemu zenye uhitaji mkubwa zaidi.
21. “Mlango mkubwa unaoongoza kwenye utendaji” umefunguliwaje kwa watu wa Yehova?
21 Hivi karibuni, mashamba makubwa ya kuenezea evanjeli yamefunguliwa katika nchi za Afrika, Esia, Ulaya ya Mashariki, ambako kazi ya Mashahidi wa Yehova ilikuwa imezuiliwa mbeleni. Kama vile kwa habari ya mtume Paulo, “mlango mkubwa unaoongoza kwenye utendaji umefunguliwa” kwa watu wa Yehova. (1 Wakorintho 16:9, NW) Kwa mfano, wale waeneza evanjeli wamishonari waliowasili hivi karibuni katika nchi ya Afrika ya Msumbiji hawawezi kuongoza mafunzo ya Biblia na watu wote wanaotaka kujifunza. Twaweza kufurahi kama nini kwamba kazi ya Mashahidi wa Yehova imehalalishwa kisheria katika nchi hiyo tangu Februari 11, 1991!
22. Iwe eneo la kwetu limefanyiwa kazi sana au sivyo, ni lazima sisi sote tuazimie kufanya nini
22 Katika nchi nyingi ambako tumekuwa na uhuru wa ibada sikuzote, ndugu zetu wanaonea shangwe pia maongezeko yenye kuendelea. Naam, popote tuishipo, bado kuna “mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.” (1 Wakorintho 15:58, NW) Hali ikiwa hivyo, acheni tuendelee kutumia kwa hekima wakati unaobaki sote ‘tunapofanya kazi ya mweneza evanjeli, tukitimiza huduma yetu kikamili.’—2 Timotheo 4:5, NW; Waefeso 5:15, 16.
Je! Waweza Kueleza?
◻ Mweneza evanjeli ni nini?
◻ Yaliyomo katika habari njema yaliongezewaje ubora baada ya 1914?
◻ Kazi ya kueneza evanjeli iliendeleaje tangu 1919?
◻ Ni sababu gani kuu ambazo zimechangia mafanikio ya kazi ya kueneza evanjeli?
[Sanduku katika ukurasa wa 19]
UPANUZI TANGU 1939
Fikiria mifano kutoka mabara matatu ambako wamishonari waliozoezwa Gileadi walitumwa. Huko nyuma katika 1939 kulikuwako wapiga mbiu ya Ufalme 636 tu walioripoti kutoka Afrika Magharibi. Kufikia 1991 idadi hiyo imekua hadi zaidi ya 200,000 katika nchi 12 za Afrika Magharibi. Wamishonari wamechangia pia maongezeko ya ajabu katika nchi za Amerika Kusini. Moja ni Brazili, iliyoongezeka kutoka wapiga mbiu ya Ufalme 114 katika 1939 hadi kilele cha 335,039 katika 1992. Ukuzi kama huo ulifuata kuwasili kwa wamishonari katika nchi za Esia. Wakati wa Vita ya Ulimwengu 2, ile hesabu ndogo ya Mashahidi wa Yehova katika Japani walinyanyaswa vikali, na kazi yao ikakoma. Halafu, katika 1949, wamishonari 13 waliwasili ili kusaidia kupanga kazi kitengenezo tena. Katika mwaka huo wa utumishi, wahubiri wenyeji walio punde kuliko kumi waliripoti utumishi wa shambani katika Japani nzima, lakini katika Aprili 1992 jumla ya hesabu ya wahubiri ilifika 167,370.
[Sanduku katika ukurasa wa 21]
JUMUIYA YA WAKRISTO NA TATIZO LA LUGHA
Baadhi ya wamishonari wa Jumuiya ya Wakristo walijitahidi kujifunza ulimi wa kigeni, lakini wengi waliwatazamia wenyeji waseme lugha yao ya Ulaya. Kama aelezavyo Geoffrey Moorhouse katika kitabu chake The Missionaries:
“Tatizo lilikuwa kwamba kujifunza lugha ya kienyeji kulionwa mara nyingi sana kuwa njia tu ya kutafsiri Maandiko. Jitihada ndogo sana kwa kulinganisha iliwekwa, ama na watu mmoja mmoja ama na jamii zilizowaajiri kazi, ili kuhakikisha kwamba mishonari angeweza kusema na mwenyeji katika ulimi wa mwenyeji huyo kwa ufasaha ambao peke yao ungeweza kutokeza uelewevu wenye kina kirefu kati ya wanadamu wawili. Kila mishonari alikuwa akijifunza sehemu ndogo tu ya msamiati wa lugha ya kienyeji . . . Zaidi ya hayo, uwasiliano ulifanywa hasa katika yale matamko yenye kuchukiza na ya kiupuzi ya ile iitwayo eti Kiingereza cha kuvunjia, kilichowalazimisha wenyeji wafuate lugha ya wageni. Kwa vyovyote vile, hilo lilikuwa dhihirisho jingine la ubwana mkubwa wa kirangi.”
Katika 1922 Shule ya Masomo ya Mashariki na ya Afrika katika London ilitangaza kwa chapa ripoti juu ya tatizo la lugha. “Tunaona kwamba,” ripoti hiyo ikasema, “kiwango cha wastani cha ufasaha unaopatwa na wamishonari katika lugha za kienyeji . . . ni cha chini sana kwa njia ya kusikitisha na ya hatari.”
Wamishonari wa Watch Tower Society sikuzote wamekuona kujifunza lugha ya kienyeji kuwa jambo la lazima, ambalo husaidia kueleza mafanikio yao katika shamba la umishonari.