‘Mkono wa Yehova Ulikuwa Pamoja Nao’
“Hivyo ndivyo neno la Bwana [Yehova, NW] lilivyozidi na kushinda kwa nguvu.”—MATENDO 19:20.
1. (a) Adui za Ukristo walifanya lalamiko gani katika karne ya kwanza W.K.? (b) Ni nini kilichofuata mahali popote ambapo Paulo alihubiri habari njema za Ufalme wa Mungu, na sikuzote ni nini kilichokuwa pamoja na Wakristo wa mapema?
ZAIDI ya miaka 1,900 iliyopita, adui za ujumbe wa Kikristo na wapinzani wa mtume-misionari Paulo walilalamika hivi: “Watu hawa walioupindua ulimwengu wamefika huku nako,. .. na [wao] wanatenda mambo yaliyo kinyume cha amri za Kaisari, wakisema [ya] kwamba yupo mfalme mwingine, aitwaye Yesu.” (Matendo 17:6, 7) Kokote ambako Paulo misionari Mkristo alijulisha habari njema za Ufalme wa Yehova, kulikuwako kitendo na kitendo-itikizo, na mara nyingi mnyanyaso. Wakristo wengine wa mapema walinyanyaswa pia. Lakini sikuzote “mkono wa Bwana [Yehova, NW] ukawa pamoja nao.”—Matendo 11:21.
2. Ni nani aliyeanzisha utendaji wa umisionari wa Kikristo, na jinsi gani?
2 Ni nani aliyekuwa ameanzisha utendaji huo muhimu wa umisionari wa Kikristo? Alikuwa Yesu, mtu asiye na kifani mwenye ujumbe wa kuchochea na njia isiyo ya kikawaida ya kuuenezea. Kumbuka kwamba Yesu, Mwana wa Mungu, aliwajia Wayahudi akiwa na tangazo la kugutusha juu ya Ufalme wa Mungu. Lakini wao walipendezwa na wokovu wao wenyewe tu kupitia kazi za Sheria.—Mathayo 4:17; Luka 8:1; 11:45, 46.
“Kwa Mataifa Yote”
3. Ni unabii gani uliotolewa na Yesu ambao lazima uwe ulishangaza wanafunzi wake Wayahudi, na kwa nini?
3 Hivyo, tunaweza kuwazia mshangao wa wanafunzi wa Yesu Wayahudi wakati yeye alipowaambia hivi siku tatu kabla ya kifo chake: “Na habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia nzima yote inayokaliwa kwa ajili ya ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakuja.” Lazima wanafunzi wake wawe walishangaa wakijiuliza wangewezaje kweli kuhubiri habari njema “kwa mataifa yote” Kikundi kidogo hivyo cha waitikadi kingewezaje kweli kutimiza mgawo mkubwa jinsi hiyo?—Mathayo 24:14, NW; Marko 13:10.
4. Yesu mfufuliwa aliwapa wanafunzi wake amri gani?
4 Baadaye, Yesu mfufuliwa aliongeza amri moja, akisema: “Mamlaka yote imepewa kwangu mimi katika mbingu na katika dunia. Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru nyinyi.” Hivyo walipewa agizo wapeleke ujumbe wa Bwana wao kwa “watu wa mataifa yote.”—Mathayo 28:18-20, NW.
5, 6. (a) Kuhubiriwa kwa habari njema za Ufalme wa Mungu kulifikiaje wasio Wayahudi, na tokeo likawa nini? (b) Wazee katika Yerusalemu walijibuje wakati Petro alipowasimulia yaliyompata kuhusiana na Kornelio asiye Myahudi?
5 Ujumbe huo ulikuja kutia ndani kuhubiria wasio Wayahudi, hilo likiwa takwa gumu. Mwelekeo wa Petro miaka mitatu baadaye ni uthibitisho wa kwamba lilikuwa gumu. Kupitia njozi moja, Petro aliambiwa ale viumbe waliotiwa unajisi. Mungu alipomwonyesha kwamba vitu ambavyo hapo kwanza vilionwa kuwa najisi vilipasa sasa kutazamwa kwa rai ya kwamba ni vitu safi, Petro alifadhaika. Halafu Petro akaelekezwa na roho ya Mungu azuru nyumba ya Kornelio asiye Myahudi, Mroma mwenye amri juu ya askari mia. Akiwa huko, alitanabahi kwamba lilikuwa penzi la Mungu kwamba amhubirie Kornelio, ingawa hapo kwanza alifikiri kilikuwa kinyume cha sheria kuwa pamoja na watu wa asili nyinginezo za kijamii. Petro alipokuwa akinena, roho takatifu iliangukia jamaa hiyo isiyokuwa ya Kiyahudi, na hiyo ikaonyesha, kwa kweli, kwamba shamba la utendaji wa umisionari wa Kikristo lazima sasa lipanuliwe litie ndani ulimwengu wa wasio Wayahudi.—Matendo 10:9-16, 28, 34, 35, 44.
6 Petro alipoeleza wazee katika Yerusalemu juu ya tukio hilo, “wakanyamaza [wakakubali kwa unyamavu, NW], wakamtukuza Mungu, wakisema, Basi, Mungu amewajalia hata mataifa nao toba liletalo uzima.” (Matendo 11:18) Sasa mataifa yasiyo ya Kiyahudi yangeweza kupokea kwa uhuru zile habari njema za Kristo na za Ufalme wake!
Wamisionari kwa Mataifa
7. Utendaji wa umisionari wa Kikristo ulianzaje kuenea katika mabara yenye kuzunguka Mediterania, na rai ya Yehova ilikuwa nini juu ya hilo?
7 Kazi ya kuhubiri, iliyokuwa imepata mwendo baada ya kuuawa kwa Stefano, sasa ilipiga hatua tofauti. Kundi katika Yerusalemu lilikuwa limetawanyika, isipokuwa mitume. Kwanza, waitikadi hao Wayahudi wenye kunyanyaswa walihubiria Wayahudi tu katika Foinike, Kipro (Saiprasi), na Antiokia. “Lakini baadhi ya hao . . . watu wa Kipro na Kirene . . . wakasema na Wayahudi wa Kiyunani, wakihubiri habari njema za Bwana Yesu.” Yehova alikuwa na rai gani juu ya huo utendaji wa kimisionari kwa mataifa? “Mkono wa Bwana [Yehova, NW] ukawa pamoja nao; watu wengi wakaamini, wakamwelekea Bwana.” Asante kwa ujasiri wa Wakristo hao wa mapema, utendaji wa kimisionari wenye matokeo ulikuwa ukianza kuenea katika mabara yenye kuzunguka Mediterania. Lakini mengi zaidi yangekuja.—Matendo 4:31; 8:1; 11:19-21.
8. Mungu alionyeshaje hatua ya kukata maneno kupanua kazi ya kimisionari?
8 Yapata 47-48 W.K., Mungu, kupitia roho takatifu, alionyesha hatua ya kukata maneno kupanua kazi ya kimisionari. Maandishi kwenye Matendo 13:2-4, NW, yanatuambia: “Roho takatifu ilisema: ‘Kati ya watu wote wekeni Barnaba na Sauli kando kwa ajili yangu kwa ajili ya kazi ambayo mimi nimewaitia.’ . . . Kwa hiyo wanaume hao, kwa kutumwa nje na roho takatifu, wakateremka kwenda Seleukia [bandari ya Antiokia ya Shamu], na kutoka huko wakatweka kwenda mbali Saiprasi.” Lazima iwe Paulo na Barnaba walisisimuliwa sana na jambo hilo—kutweka kwenda kwenye mgawo wao wa kwanza wa nchi ya kigeni! Mtume Paulo alikuwa mshika-usukani wa utendaji wa umisionari wa Kikristo. Pia alikuwa akiweka msingi kwa ajili ya kazi ambayo ingekamilishwa katika karne yetu ya 20.
9. Mtume Paulo alitimiza nini kupitia ziara zake za umisionari?
9 Paulo aliendelea kufanya ziara tatu za kimisionari zilizo katika maandishi, kuongeza na safari yake ya kwenda Roma akiwa mfungwa-gereza. Akiwa katika safari hizo, alifungua kazi katika majiji kadhaa katika Ulaya na akahubiri ujumbe wa Ufalme katika nchi na visiwa ambavyo leo vinajulikana kuwa Siria (Shamu), Saiprasi, Krete, Uturuki, Ugiriki, Malta, na Sisili. Hata huenda ikawa alifika Hispania. Yeye alisaidia kuanzisha makundi katika majiji mengi. Siri ya utendaji wake wa kimisionari wenye matokeo ilikuwa nini?
Kufundisha kwa Njia Yenye Matokeo
10. Kwa nini Paulo alikuwa mwenye matokeo sana katika utendaji wake wa kimisionari?
10 Paulo aliiga njia ya Kristo ya kufundisha. Kwa hiyo alijua jinsi ya kujihusianisha na watu kwa upatano mzuri. Alijua jinsi ya kufundisha na jinsi ya kuzoeza wengine wawe walimu. Alitegemeza fundisho lake juu ya msingi wa Maandiko. Hakujaribu kuvutia wengine kwa kuwastaajabisha na hekima yake mwenyewe, bali alisababu mambo kutokana na Maandiko. (Matendo 17:2, 3, NW) Paulo alijua pia jinsi ya kujirekebisha apatane na hali za wasikilizaji wake na jinsi ya kutumia hali za mahali ziwe kianzishio cha ujumbe wake. Kama yeye alivyosema: “Nalijifanya mtumwa wa wote, ili nipate watu wengi zaidi. Nalikuwa kama Myahudi kwa Wayahudi . . . Kwa wale wasio na sheria nalikuwa kama sina sheria ... Kwa wanyonge nalikuwa mnyonge, ili niwapate wanyonge. Nimekuwa hali zote kwa watu wote, ili kwa njia zote nipate kuwaokoa watu [baadhi yao, NW].—1 Wakorintho 9:19-23; Matendo 17:22, 23.
11. Ni nini kinachoonyesha kwamba Paulo na waandamani wake walikuwa wamisionari wenye matokeo, na huduma ya Kikristo ilienea kwa mapana gani?
11 Paulo na waandamani wake walikuwa wamisionari wenye matokeo. Kwa kutumia udumifu na uvumilivu, walianzisha na wakaimarisha makundi ya Kikristo kila walikokwenda. (Matendo 13:14, 43, 48, 49; 14:19-28) Huduma ya Kikristo ya mapema ilikuwa imeenea sana hivi kwamba Paulo angeweza kuandika hatimaye juu ya “kweli ya Injili [habari njema, NW]; iliyofika kwenu, kama ilivyo katika ulimwengu wote, na kuzaa matunda na kukua . . . iliyohubiriwa katika viumbe vyote vilivyo chini ya mbingu.” Utendaji wa umisionari wa mapema wa Kikristo uliathiri watu kikweli. —Wakolosai 1:5, 6, 23.
12. Ni nini kilichosababisha kazi asilia ya umisionari wa Kikristo ikome kwa muda?
12 Hata hivyo, kufikia mwanzo wa karne ya pili W.K., uasi-imani ulikuwa ukitambaa kuingia ndani ya kundi la Kikristo, sawa na vile Yesu na mitume walivyokuwa wameonya. (Mathayo 7:15, 21-23; Matendo 20:29, 30; 1 Yohana 2:18, 19) Katika karne zilizofuata, theolojia na fundisho la kipagani vilididimiza ujumbe wa Ufalme. Jumuiya ya Wakristo ilituma nje wamisionari, si kuhubiri Ufalme wa Mungu ulio wa kweli, bali kutwika juu ya wenyeji wasio na kinga—kwa kutumia upanga mara nyingi—ule ufalme wa mabwana-wakubwa na wadhamini wao wa kisiasa. Kazi ya umisionari asilia wa Kikristo ilikoma lakini si milele.
13. Kampeni moja ya umisionari ilianzaje katika nyakati za ki-siku-hizi, na ni nini lililotimizwa kufikia mwisho wa 1916?
13 Kuelekea mwisho wa karne ya 19, Charles T. Russell, msimamizi wa kwanza wa Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi, aliona uhitaji wa utendaji wa kimisionari. Hivyo yeye akapanga kampeni ya ushuhuda wenye kuenezwa sana, naye mwenyewe akazuru majiji mengi katika United States, akasafiri ulimwenguni pia kwa meli ili kuzuru nchi nyingi kwa kadiri ilivyowezekana. Miandiko yake yenye msingi wa Biblia ilitangazwa katika lugha 35. Inasemwa kwamba yeye alisafiri zaidi ya kilometa milioni 1.6 akiwa mhadhiri na akahubiri mahubiri zaidi ya 30,000 kabla ya kifo chake katika 1916.
14. Joseph F. Rutherford alifanya nini kusogeza mbele zaidi utendaji wa kimisionari?
14 Mwandamizi wake, Joseph F. Rutherford, alitambua pia uhitaji muhimu wa utendaji wa kimisionari. Katika miaka ya mapema ya 1920, yeye aliwatuma nchi tofauti-tofauti wanaume hodari wakasaidie kuanzisha kazi ya kuhubiri. Wamisionari walipainia katika kazi hiyo ya Ufalme katika Hispania, Amerika ya Kusini, na Afrika ya Magharibi. Katika 1931 ombi lilitolewa kuitisha wenye kujitolea ili wakaongeze kani kwenye kazi katika Hispania. Vijana watatu wa kiume kutoka Uingereza waliitikia na kutumikia huko chini ya mastakimu ngumu sana zenye kuwatoa jasho kweli kweli kwa muda wa miaka minne hadi kufoka kwa Vita ya Hispania ya Wenyewe kwa Wenyewe katika 1936. Ndipo wakalazimika kukimbia waponyoshe uhai wao.
15. Ni jambo gani lililotukia katika miaka ya 1940 kupanua kazi ya kimisionari kwa kadiri kubwa?
15 Katika mwongo wa miaka ya 1940, mambo mazuri zaidi yangekuja katika utendaji wa kimisionari. Msimamizi wa tatu wa Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi, Nathan H. Knorr, alikuwa na kikoa cha wanaume wenye bidii wakifanya kazi naye. Kwa uwazi ikiwa ni chini ya mwelekezo wa roho takatifu, katika 1942 yeye aliona uhitaji wa kufungua shule ya wamisionari kwa kujitayarisha kwa ajili ya dai gumu la baada ya Vita ya Ulimwengu 2. Katikati ya hiyo vita ya ulimwengu, yeye mwenyewe alichukua hiari ya uanzishi, na Shule ya Biblia ya Gileadi ya Mnara wa Mlinzi ikazinduliwa katika Mkoa wa New York kaskazini katika Februari 1943. Ikiwa na wakufunzi wanne, kila miezi sita shule hiyo iliwapa wahudumu mapainia wenye bidii zaidi ya mia moja, wa kiume na wa kike, mazoezi yenye msingi wa Biblia kwa ajili ya utumishi wa kimisionari. Je! utendaji wao kutokana nayo umekuwa wenye matokeo?
16. (a) Ni Mashahidi wangapi waliokuwa wakihubiri katika 1943, na hiyo inalinganaje na leo? (b) Wamisionari wamekuwa na sehemu gani katika ongezeko hilo? Eleza.
16 Katika 1943 kulikuwa na Mashahidi 126,329 tu wakihubiri katika nchi 54. Hali ikoje leo? Sasa, miaka 45 baadaye, kuna hesabu iliyo mara 28 za hiyo, wahudumu watendaji zaidi ya milioni tatu na nusu katika nchi na visiwa vya bahari 212. Sehemu kubwa ya ongezeko hilo imetokana na msingi bora uliowekwa na wamisionari zaidi ya 6,000 ambao wamehitimu kwenye Shule ya Gileadi. Wao wametoka nchi 59 na wametumwa nje kwenye mabara 148 tofauti-tofauti muda wa miongo mitano iliyopita. Kwa msaada wao, badala ya kuwako Mashahidi wanaozidi kidogo tu mia moja elfu katika ulimwengu mzima, kama walivyokuwa miaka 45 iliyopita, sasa kuna nchi kumi ambazo kila moja ina wahudumu zaidi ya mia moja elfu wakihubiri na kufundisha habari njema. Katika yaliyo mengi kati ya mataifa hayo, wamisionari wa Gileadi wamekuwa kwenye mstari wa mbele wa kazi ya kueneza evanjeli.
17. Ni mambo gani matatu ambayo yamefanya kazi ya umisionari wa mapema na umisionari wa Kikristo wa ki-siku-hizi uwe na matokeo?
17 Tuwe tunarejezea kazi ya umisionari wa mapema au tunarejezea kazi ya ki-siku-hizi ya umisionari wa Kikristo, kuna mambo fulani ya msingi ambayo yamefanya iwe na matokeo. Jambo moja ni kule kuonana moja kwa moja na watu ambako kunatokana na huduma ya nyumba kwa nyumba na ushuhuda wa vivi hivi, vilevile mpango wa funzo la Biblia la kimaskani. (Yohana 4:7-26; Matendo 20:20) Jambo jingine ni ule ujumbe wa moja kwa moja ulio rahisi kueleweka ambao msingi wao ni Biblia, unaokazia kuwa Ufalme wa Mungu ndio utatuzi mmoja tu wa kudumu kwa matatizo ya aina ya binadamu. (Matendo 19:8; 28:16, 23, 30, 31) Na wengi wa wamisionari wetu wanatumikia katika nchi zilizo changa kimaendeleo, ambako inaonekana wazi sana kwamba utawala mwadilifu wa Mungu unahitajiwa. Jambo la tatu ni upendo ambao Kristo alifundisha na ambao wamisionari wetu wa ki-siku-hizi wanadhihirisha katika shughuli zao za kila siku pamoja na watu wa aina na awali zote. Hakuna shaka kwamba, katika muda wa miaka 45 iliyopita, wamisionari wa Mnara wa Mlinzi wamechangia kwa njia kubwa mpanuko wa duniani pote wa tengenezo la Yehova.—Warumi 1:14-17; 1 Wakorintho 3:5, 6.
Roho ya Upainia Yatia Mizizi
18. Ni nani wengine ambao wamefyonza ile roho ya bidii ya umisionari hali moja na wahitimu wa Gileadi?
18 Bila shaka kielelezo cha bidii ya wahitimu wa Gileadi kilichochea wengine wawe na tamaa ya kuwa wahudumu wa wakati wote. Leo, kuna mamia ya maelfu ya mashahidi wengine wa Yehova ambao wameifyonza roho hiyo hiyo ya bidii ya umisionari. Wao pia ni mapainia katika maana ile halisi, wakifuata hatua za Yesu, “Painia wa wokovu wao.”—Waebrania 2:10; 12:2, Moffatt.
19. Mashahidi wengi walio na roho ya upainia wamejitolea kufanya nini, nao wanahisi kuwa wamethawabishwaje?
19 Tangu miaka ya 1960 imekuwa vigumu sana kutuma wamisionari ndani ya nchi kadhaa. Shule ya Biblia ya Gileadi ya Mnara wa Mlinzi inaendelea kugawa wamisionari, kwa kadiri inayowezekana, kulingana na uhitaji katika mabara ya kigeni. Hata hivyo, ulimwenguni pote kuna shamba kubwa sana kwa ajili ya Mashahidi walio na roho ya kweli ya upainia. Wengi wamejitolea kufanya mipango yao wenyewe wakatumikie katika mabara ambako uhitaji ni mkubwa zaidi. Je! wewe ni mmoja ambaye ungeweza kujiunga nao? Mara nyingi hao wanaeleza kwamba magumu yanayowapata na dhabihu wanazofanya hulipiwa mara nyingi zaidi na shangwe kuu ya kuwalisha kweli za Ufalme watu walio mfano wa kondoo katika nchi zinazoendelea kusitawi. Wao wanathawabishwa mara mia kwa kupata “ndugu na dada na akina mama na watoto” wapya na katika kushiriki pamoja nao tumaini zuri ajabu la uhai wa milele katika “mfumo wa mambo unaokuja.”—Marko 10:28-30, NW.
20. (a) Ni nani wanaofanya sehemu kubwa zaidi ya kuhubiri katika nchi nyingi? (b) Imekuwaje kwamba Japani huripoti kila mwaka jumla ya saa za utumishi wa shambani zinazozidi karibu nchi nyingine yoyote? (c) Ni swali gani ambalo tungefanya yema kulifikiria?
20 Waaidha, kuna mamia ya maelfu ya watumishi wa Yehova leo wanaoripoti utumishi mtakatifu kila mwezi wakiwa mapainia wa kawaida au wasaidizi. Walio wengi wanafanya kazi kwa bidii-endelevu katika maeneo ya maskani zao. Katika nchi nyingi, wao ndio hufanya sehemu iliyo kubwa zaidi ya kuhubiri, na mara nyingi wanatembelea maskani zile zile juma baada ya juma. Tumaini lao la Ufalme linaonekana katika sura zao nyangavu na mwelekeo wa shangwe wanapofanya urafiki na watu wapya na kusitawisha upendezo mwingi katika maeneo yao. Kuwako kwa mapainia wengi zaidi kunamaanisha saa nyingi zaidi katika kusifu Mungu. Kwa zaidi ya mwongo mmoja, Japani, ambako walio wengi sana wa Mashahidi wa Yehova ni watu waliokuwa Wabuddha hapo kwanza, imeripoti kila mwaka jumla ya saa za utumishi wa shambani zinazozidi nchi nyingine yoyote iliyo nje ya United States. Hiyo ni kwa sababu karibu nusu moja ya wahubiri wayo wa Ufalme wanapainia. Je! wewe pia unaweza kupanga mambo yako ili ushiriki katika hilo pendeleo la mapendeleo yote, utumishi wa painia?
21. (a) Mashahidi wengine ambao hali yao haiwawezeshi kujiandikisha kuwa mapainia wa kawaida wanaweza kuonyeshaje bado roho ya upainia? (b) Vijana wanaweza kuonyeshaje roho ya upainia?
21 Kuna Mashahidi wengine ambao ni ‘wenye bidii kwa ajili ya kazi zilizo bora.’ (Tito 2:14, NW) Hao ni kutia ndani walio wazee-wazee, wale walio na afya mbaya, wengi walio na madaraka ya jamaa, na vijana walio shuleni bado ambao hali yao haiwaruhusu kujiandikisha wawe mapainia wa kawaida. Hao pia wanaweza kuonyesha roho ya upainia kwa kuwapa mapainia utegemezo wa kuwatia moyo, wakishiriki katika utumishi pamoja nao kwa kadiri inayowezekana, na kudumisha mwelekeo chanya kuhusu fursa zao wenyewe za kutoa ushuhuda. Vijana wanaweza kufanya utumishi wa wakati wote wa Ufalme uwe mradi wao na, mara wakiisha kubatizwa, washiriki katika upainia msaidizi mara kwa mara. Kama Timotheo kijana, wao wanaweza kufikiria sana mambo hayo ili wafanye maendeleo ya kiroho pamoja na watu wote wa Mungu.—1 Timotheo 4:15, 16.
22. Hata kama tuna hali gani maishani, tunapaswa kupiga moyo konde kufanya nini, na kwa tokeo gani bora?
22 Hata kama tuna hali gani maishani, sisi sote na tusukumwe na roho ya Yehova kushiriki kwa ukamili katika utumishi wake. “Mkono wa Bwana [Yehova, NW]” na uendelee kuwa pamoja na kila mmoja wetu ili iweze kusemwa kuhusu jitihada zetu za unyenyekevu kwamba “hivyo ndivyo neno la Bwana [Yehova, NW] lilivyozidi na kushinda kwa nguvu.”—Matendo 11:21; 19:20.
Maswali kwa Kupitia
◻ Kazi ya umisionari wa Kikristo ilianzaje, nayo ingekuja kuenea kwa kadiri gani?
◻ Mtume Paulo alikuwa na fungu gani katika kupanua kazi ya kimisionari?
◻ Ni jinsi gani kazi ya kimisionari ilivyohuishwa upya katika nyakati za ki-siku-hizi?
◻ Ni mambo gani ambayo yamefanya utumishi wa kimisionari na wa painia uwe na matokeo?
◻ Sisi tunaweza kufyonzaje roho ya upainia leo?
[Chati katika ukurasa wa 13]
Utendaji wa Ufalme Katika Nchi Kumi—1988
(Zote hizi ziliripoti zaidi ya wahubiri 100,000)
Nchi Kilele cha Wastani Saa za Hudhurio la
Wahubiri Mapainia Kuhubiri Ukumbusho
U.SA. 797,104 96,947 161,478,732 1,822,607
Meksiko 248,822 32,117 58,061,457 1,004,062
Brazili 245,610 22,725 44,218,022 718,414
Italia 160,584 25,477 43,354,687 330,461
Naijeria 134,543 14,022 27,800,623 398,555
Japani 128,817 52,183 60,626,840 297,171
Ujeremani 125,068 8,416 22,020,942 215,385
Uingereza 113,412 11,927 22,103,713 211,060
Ufilipino 107,679 21,320 26,337,621 305,087
Ufaransa 103,734 9,189 21,598,308 205,256
[Picha katika ukurasa wa 10]
Paulo na Barnaba waondoka kwenda kwenye kazi ya kimisionari ya upainia