Sura ya 23
Wamishonari Wasukuma Mpanuko wa Ulimwenguni Pote
UTENDAJI wa bidii wa wamishonari walio tayari kutumikia popote wanapohitajiwa umekuwa jambo la maana katika kupiga mbiu ya Ufalme wa Mungu duniani pote.
Muda mrefu kabla ya Watch Tower Bible and Tract Society kuanzisha shule kwa kusudi hilo, wamishonari walikuwa wakitumwa kwenda nchi nyinginezo. Msimamizi wa kwanza wa Sosaiti, C. T. Russell, alitambua uhitaji wa watu waliostahili ili kuanzisha na kuchukua uongozi katika kuhubiri habari njema katika mashamba ya kigeni. Alituma wanaume kwa kusudi hilo—Adolf Weber hadi Ulaya, E. J. Coward kwenye eneo ya Karibea, Robert Hollister hadi nchi za Mashariki, na Joseph Booth hadi kusini mwa Afrika. Kwa kusikitisha, Booth alithibitika kuwa mwenye kupendezwa na mipango yake mwenyewe; hivyo, katika 1910, William Johnston alitumwa kutoka Scotland hadi Nyasaland (sasa Malawi), mahali ambako uvutano mbaya wa Booth ulikuwa umehisiwa hasa. Baada ya hapo, Ndugu Johnston alipewa mgawo wa kuanzisha ofisi ya tawi ya Watch Tower Society katika Durban, Afrika Kusini, na baadaye akatumikia akiwa mwangalizi wa tawi katika Australia.
Baada ya vita ya ulimwengu ya kwanza, J. F. Rutherford alituma wamishonari wengi hata zaidi—kwa kielelezo, Thomas Walder na George Phillips kutoka Uingereza hadi Afrika Kusini, W. R. Brown kutoka kwenye mgawo katika Trinidad hadi Afrika Magharibi, George Young kutoka Kanada hadi Amerika Kusini na Ulaya, Juan Muñiz kwanza hadi Hispania kisha hadi Argentina, George Wright na Edwin Skinner hadi India, wakifuatwa na Claude Goodman, Ron Tippin, na wengine wengi. Wao walikuwa mapainia halisi, wakifikia sehemu ambako ni kazi ndogo ya kuhubiri habari njema au hakuna yoyote iliyokuwa imefanywa na kuweka msingi imara kwa ajili ya ukuzi wa kitengenezo wa wakati ujao.
Kulikuwa na wengine pia, ambao roho yao ya mishonari iliwachochea waanze kuhubiri nje ya nchi yao wenyewe. Miongoni mwao walikuwa Kate Goas na binti yake Marion, waliotoa miaka mingi kwa utumishi wenye bidii katika Kolombia na Venezuela. Mwingine alikuwa Joseph Dos Santos, aliyeondoka Hawaii kwenda kwenye safari ya kuhubiri iliyoongoza kwenye miaka 15 ya huduma katika Filipino. Pia kulikuwa na Frank Rice, aliyesafiri kwa meli ya mizigo kutoka Australia ili aanzishe kazi ya kuhubiri habari njema katika kisiwa cha Java (sasa ni Indonesia).
Hata hivyo, katika 1942 mipango ilifanywa ya kuwa na shule yenye mtaala uliofanyizwa hasa kuzoeza wanaume na wanawake pia walio tayari kuanza utumishi huo wa mishonari mahali popote walipohitajiwa katika shamba la duniani pote.
Shule ya Gileadi
Katikati ya vita ya ulimwengu, huenda lilionekana kuwa jambo lisiloweza kufanya kazi kwa maoni ya kibinadamu kupanga kwa ajili ya mpanuko wa utendaji wa kuhubiri Ufalme katika mashamba ya kigeni. Na bado, katika Septemba 1942, kwa kumtegemea Yehova, waelekezi wa mashirika mawili kati ya mashirika makuu halali yaliyotumiwa na Mashahidi wa Yehova yalikubali pendekezo la N. H. Knorr la kuanzisha shule iliyokusudiwa kuwazoeza wamishonari na wengine kwa ajili ya utumishi maalumu. Ingeitwa Watchtower Bible College of Gilead. Baadaye jina hilo lilibadilishwa likawa Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower. Hakuna pesa za mafunzo zingelipwa, na wanafunzi wangepewa malazi na chakula kwa gharama ya Sosaiti katika kipindi cha mazoezi yao.
Miongoni mwa wale walioalikwa kusaidia kupanga mtaala wa mafunzo alikuwa Albert D. Schroeder, aliyekuwa tayari amepata ujuzi mwingi katika Idara ya Utumishi kwenye makao makuu ya Sosaiti katika Brooklyn na akiwa mwangalizi wa tawi la Sosaiti katika Uingereza. Mtazamo wake unaofaa, vile alivyojitoa mwenyewe kusaidia wengine, na kupendezwa kwa uchangamfu na wanafunzi kuliwafanya wale aliowafunza wampende wakati wa miaka 17 aliyotumikia akiwa msajili na mfunzi katika shule hiyo. Katika 1974 akawa mshiriki wa Baraza Linaloongoza, na mwaka uliofuata alipewa mgawo wa kutumikia katika Halmashauri ya Kufundisha yayo.
Ndugu Schroeder na wafunzi wenzake (Maxwell Friend, Eduardo Keller, na Victor Blackwell) walipanga mtaala wa mafunzo wa miezi mitano uliokazia funzo la Biblia yenyewe na tengenezo la kitheokrasi, pia mafundisho ya Biblia, kusema mbele ya watu, huduma ya shambani, utumishi wa mishonari, historia ya kidini, sheria ya kimungu, jinsi ya kushughulika na maofisa wa serikali, sheria ya kimataifa, kuweka maandishi, na lugha moja ya kigeni. Mtaala umerekebishwa kwa muda wa miaka iliyopita, lakini funzo la Biblia yenyewe na umaana wa kazi ya kueneza evanjeli nyakati zote ni mambo ambayo yamechukua mahali pa kwanza. Kusudi la mtaala huo ni kutia nguvu imani ya wanafunzi, kuwasaidia wasitawishe sifa za kiroho zinazohitajika ili kuweza kushinda magumu ya utumishi wa mishonari. Mkazo umewekwa juu ya umaana wa kumtegemea Yehova kabisa na kuwa na uaminifu-mshikamanifu kwake. (Zab. 146:1-6; Mit. 3:5, 6; Efe. 4:24) Wanafunzi hawapewi majibu yaliyokaririwa kwa kila kitu lakini huzoezwa kufanya utafiti na husaidiwa kuthamini kwa nini Mashahidi wa Yehova huamini yale wanayoamini na kwa nini wao hushikamana na njia fulani za kufanya mambo. Wanajifunza kutambua kanuni wanazoweza kufanya kazi nazo. Hivyo msingi huwekwa kwa ajili ya ukuzi zaidi.
Mialiko kwa waliotazamiwa kuwa wanafunzi kwa ajili ya darasa la kwanza ilipelekwa Desemba 14, 1942. Ilikuwa ni katikati ya kipupwe wakati wanafunzi 100 waliofanyiza darasa hilo walipojiandikisha kwenye majengo ya shule yaliyoko katika upande wa juu wa jimbo la New York, katika South Lansing. Walikuwa wenye nia, wenye hamu, na kidogo wenye wasiwasi. Ingawa mafunzo ya darasa ndiyo yaliyokuwa hangaiko la mara hiyo, hawangeweza kujizuia kujiuliza ni wapi katika shamba la ulimwengu wangeweza kutumwa baada ya kuhitimu.
Katika hotuba moja kwa darasa hilo la kwanza katika Februari 1, 1943, siku ya kufungua shule, Ndugu Knorr alisema: “Mnapewa matayarisho zaidi kwa ajili ya kazi inayofanana na ile ya mtume Paulo, Marko, Timotheo, na wengine waliosafiri kwenda sehemu zote za Milki ya Roma wakipiga mbiu ya ujumbe wa Ufalme. Iliwabidi waimarishwe kwa Neno la Mungu. Iliwabidi wawe na ujuzi wa wazi kuhusu makusudi Yake. Katika sehemu nyingi iliwabidi wasimame imara wakiwa peke yao dhidi ya wenye vyeo na wakuu wa ulimwengu huu. Huenda mkapatwa na mambo ayo hayo; na Mungu atakuwa nguvu yenu wakati huo.
“Kuna sehemu nyingi ambako ushahidi kuhusu Ufalme haujatolewa kwa kadiri kubwa. Watu wanaoishi katika sehemu hizo wamo gizani, wamezuiwa humo na dini. Katika baadhi ya nchi hizo ambako kuna Mashahidi wachache imeonwa kuwa watu wa nia njema huwa tayari kusikiliza na wangejishirikisha na tengenezo la Bwana, ikiwa wangefunzwa ifaavyo. Lazima kuwe na mamia na maelfu zaidi ambao wangeweza kufikiwa ikiwa kungekuwa na wafanyakazi wengi zaidi shambani. Kwa neema ya Bwana, kutakuwa na wengi zaidi.
“SI kusudi la koleji hii kuwatayarisha kuwa wahudumu walioagizwa rasmi. Nyinyi tayari ni wahudumu na mmekuwa watendaji katika huduma kwa miaka mingi. . . . Mtaala wa mafunzo katika koleji ni kwa kusudi hususa la kuwatayarisha kuwa wahudumu wenye uwezo zaidi katika maeneo ambako mtaenda. . . .
“Kazi yenu kuu ni ile ya kuhubiri gospeli ya Ufalme nyumba hadi nyumba kama vile Yesu na mitume wake walivyofanya. Mtakapokwisha kupata sikio lenye kusikia, pangeni kufanya ziara ya kurudia, anzeni funzo la nyumbani, na kupanga kampuni [kutaniko] ya watu wote kama hao katika jiji au mji. Si kwamba tu itawapendeza kupanga kampuni, bali ni lazima mwasaidie waelewe Neno, mwaimarishe, mwasemeze pindi kwa pindi, mwasaidie katika mikutano yao ya utumishi na katika mipango yao ya kitengenezo. Watakapokuwa wenye nguvu na waweza kujiendeleza na kuhubiri eneo, mnaweza kuondoka kwenda kwenye jiji jingine ili kupiga mbiu ya Ufalme. Pindi kwa pindi huenda mkahitaji kurudi ili kuwajenga katika imani takatifu zaidi na kuwaimarisha katika mafundisho; kwa hiyo kazi yenu itakuwa ile ya kuchunga ‘kondoo wengine’ wa Bwana, na si kuwaacha. (Yn. 10:16) Kazi yenu halisi ni kuwasaidia watu wa nia njema. Ni lazima mchukue hatua ya kwanza kutimiza mambo, lakini mkitegemea uongozi wa Mungu.”a
Miezi mitano baadaye washiriki wa darasa hilo la kwanza walikamilisha mazoezi yao maalumu. Wao walipata viza, mipango ya usafiri ikafanywa, na wakaanza kwenda kwenye nchi tisa za Amerika ya Latin. Miezi mitatu baada ya kuhitimu kwao, wamishonari waliozoezwa Gileadi wa kwanza kuondoka Marekani walikuwa njiani kuelekea Kuba. Kufikia 1992, wanafunzi zaidi ya 6,500 kutoka nchi zaidi ya 110 walikuwa wamezoezwa na baadaye wakatumikia katika nchi na vikundi vya visiwa zaidi ya 200.
Hadi kufikia wakati wa kifo chake miaka 34 baada ya kuanzishwa kwa Shule ya Gileadi, Ndugu Knorr alionyesha kupendezwa sana binafsi na kazi ya wamishonari. Kila muhula wa shule, alikuwa akizuru darasa la wakati huo mara kadhaa kadiri ilivyowezekana, akitoa mihadhara na kuandamana na washiriki wengine wa wafanyakazi wa makao makuu ili kusema na wanafunzi. Baada ya wahitimu wa Gileadi kuanza utumishi wao katika nchi za kigeni, alizuru kibinafsi vikundi vya wamishonari, akawasaidia kutatua matatizo, na kuwapa kitia-moyo kilichohitajiwa. Hesabu ya vikundi vya wamishonari ilipoongezeka, alipanga kuwe na ndugu wengine wanaostahili vizuri wafanye ziara hizo pia, ili kwamba wamishonari wote, hata wawe walitumikia wapi, wangepokea uangalifu wa kibinafsi wa kawaida.
Wamishonari Hawa Walikuwa Tofauti
Wamishonari wa Jumuiya ya Wakristo wamejenga hospitali, vituo vya wakimbizi, na vya watoto yatima ili kutunza mahitaji ya kimwili ya watu. Wakitenda kana kwamba ndio wategemezaji wa watu maskini, wamechochea pia mapinduzi na kushiriki katika vita vya kuvizia. Kwa kutofautisha, wahitimu wamishonari wa Shule ya Gileadi hufundisha watu Biblia. Badala ya kujenga makanisa na kutazamia watu waje kwao, wao huenda nyumba hadi nyumba ili kupata na kufundisha wale ambao wana njaa na kiu ya uadilifu.
Wakishikamana kwa ukaribu na Neno la Mungu, Mashahidi wamishonari huonyesha watu kwa nini utatuzi wa kweli na wa kudumu kwa matatizo ya wanadamu ni Ufalme wa Mungu. (Mt. 24:14; Luka 4:43) Tofauti iliyo kati ya kazi hiyo na ile ya wamishonari wa Jumuiya ya Wakristo ilikaziwa kwa Peter Vanderhaegen katika 1951 alipokuwa njiani kuelekea kwenye mgawo wake katika Indonesia. Abiria mwingine pekee katika meli ya mizigo alikuwa mishonari Mbaptisti. Ingawa Ndugu Vanderhaegen alijaribu kumzungumzia kuhusu habari njema za Ufalme wa Mungu, Mbaptisti huyo alieleza kwamba kupendezwa kwake kwingi kulikuwa ni kuunga mkono jitihada za Chiang Kai-shek katika Taiwan ili arudi kwenye mamlaka barani.
Hata hivyo, watu wengine wengi wamekuja kuthamini thamani ya yale yaliyosemwa katika Neno la Mungu. Katika Barranquilla, Kolombia, wakati Olaf Olson alipotoa ushahidi kwa Antonio Carvajalino, aliyekuwa muungaji mkono mshupavu wa chama fulani cha kisiasa, Ndugu Olson hakumuunga mkono wala hakupendekeza wazo lolote lile la kisiasa. Badala yake, alijitoa kujifunza Biblia na Antonio na dada zake bila malipo. Upesi Antonio aling’amua kwamba kwa kweli Ufalme wa Mungu ndio tumaini pekee kwa watu maskini wa Kolombia na ulimwengu wote. (Zab. 72:1-4, 12-14; Dan. 2:44) Antonio na dada zake wakawa watumishi wa Mungu wenye bidii.
Uhakika wa kwamba wamishonari Mashahidi wako tofauti na wamejitenga na mfumo wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo ulikaziwa kwa njia nyingine katika tukio moja katika Rhodesia (sasa Zimbabwe). Wakati Donald Morrison alipozuru nyumba ya mmoja wa wamishonari wa Jumuiya ya Wakristo huko, mishonari huyo alilalamika kwamba Mashahidi hao hawakuwa wanastahi mipaka iliyowekwa. Mipaka ipi? Dini za Jumuiya ya Wakristo zilikuwa zimegawanya nchi katika sehemu ambazo kila mojayapo ingeweza kuendesha shughuli bila kuingiliwa na dini nyinginezo. Mashahidi wa Yehova hawangeweza kufuata mpango kama huo. Yesu alikuwa amesema kwamba ujumbe wa Ufalme ungehubiriwa katika dunia yote inayokaliwa. Bila shaka Jumuiya ya Wakristo haikuwa ikifanya hivyo. Wamishonari waliozoezwa Gileadi walikusudia kufanya kazi hiyo kikamilifu, kwa kumtii Kristo.
Wamishonari hao walitumwa, si ili watumikiwe, bali watumikie. Ilikuwa wazi kwa njia nyingi kwamba kwa kweli hilo ndilo walilojitahidi kufanya. Hakuna ubaya kukubali upaji wa kimwili unaotolewa kwa hiari (na si ukiwa tokeo la kuombwaombwa) kwa kuthamini msaada wa kiroho. Lakini ili kufikia mioyo ya watu katika Alaska, John Errichetti na Hermon Woodard waliona kuwa inanufaisha kuchukua angalau wakati kidogo kufanya kazi kwa mikono yao ili kuandaa mahitaji yao ya kimwili, kama vile alivyofanya mtume Paulo. (1 Kor. 9:11, 12; 2 The. 3:7, 8) Utendaji wao mkuu ulikuwa kuhubiri habari njema. Lakini walipopokea ukaribishaji-wageni, wao pia walisaidia katika kazi zilizohitaji kufanywa—kwa kielelezo, kutengeneza paa la mwanamume mmoja kwa sababu waling’amua kwamba alihitaji msaada. Na waliposafiri mahalimahali kwa mashua, walisaidia kupakua shehena. Upesi watu waling’amua kwamba wamishonari hao hawakuwa kama makasisi wa Jumuiya ya Wakristo hata kidogo.
Katika sehemu nyingine wamishonari Mashahidi walilazimika kufanya kazi ya kimwili kwa wakati fulani ili tu kujiwekea msingi katika nchi fulani ndipo waweze kuendelea na huduma yao huko. Hivyo, wakati Jesse Cantwell alipoenda Kolombia, alifundisha Kiingereza katika idara ya utabibu ya chuo kikuu hadi hali ya kisiasa ilipobadilika na vizuizi vya kidini vikaondolewa. Baada ya hapo aliweza kutumia ujuzi wake katika huduma ya wakati wote akiwa mwangalizi asafiriye wa Mashahidi wa Yehova.
Katika sehemu nyingi, wamishonari walilazimika kuanza wakiwa na viza za utalii zilizowaruhusu kuwa nchini kwa mwezi mmoja au labda miezi kadhaa. Kisha walilazimika kuondoka na kurudi tena. Lakini waliendelea, wakirudiarudia utaratibu huo hadi hati za ukazi zilizohitajiwa zilipopatikana. Mioyo yao iliwekwa juu ya kusaidia watu katika nchi walizokuwa wamegawiwa.
Wamishonari hao hawakujifikiria kuwa wakuu kuliko wenyeji. Akiwa mwangalizi asafiriye, John Cutforth, aliyekuwa mwalimu wa shule katika Kanada hapo awali, alizuru makutaniko pamoja na Mashahidi walio mbali katika Papua New Guinea. Aliketi sakafuni nao, akala nao, na akakubali mialiko ya kulala kwenye mkeka sakafuni katika nyumba zao. Alifurahia ushirika pamoja nao walipotembea pamoja katika huduma ya shambani. Lakini hilo liliwashangaza wasio-Mashahidi walioona jambo hilo, kwa kuwa mapasta wa Ulaya wa misheni za Jumuiya ya Wakristo walijulikana kuwa walijitenga na watu wenyeji, wakishiriki na wanaparishi wao kwa muda mfupi tu kwenye baadhi ya mikutano yao, lakini hawakula nao kamwe.
Watu waliotumikiwa na Mashahidi hao walihisi upendezi wenye upendo wa wamishonari na wa tengenezo lililokuwa limewatuma. Kwa kujibu barua iliyotoka kwa João Mancoca, Mwafrika mnyenyekevu aliyefungiwa katika gereza la wafungwa katika Afrika Magharibi ya Ureno (sasa Angola), mishonari wa Watch Tower alitumwa kuandaa msaada wa kiroho. Akikumbuka ziara hiyo, Mancoca alisema hivi baadaye: “Sikuwa na shaka tena kwamba hili lilikuwa tengenezo la kweli lenye utegemezo wa Mungu. Sikuwa nimefikiri au kuamini kamwe kwamba tengenezo lingine lolote la kidini lingeweza kufanya hivyo: bila malipo, kutuma mishonari kutoka mbali azuru mtu duni kwa sababu tu aliandika barua.”
Hali za Maisha na Desturi
Mara nyingi hali za maisha za nchi ambazo wamishonari walitumwa hazikuwa za juu kama zile za sehemu walizotoka. Robert Kirk alipofika Burma (sasa Myanmar) mapema katika 1947, matokeo ya vita yalikuwa yangali dhahiri, na nyumba chache zilikuwa na taa za stima (umeme). Katika nchi nyingi, wamishonari walipata kwamba nguo zilifuliwa mojamoja juu ya ubao au juu ya miamba kwenye mto badala ya kufuliwa kwa mashine ya kufulia ya stima. Lakini walikuwa wamekuja kufundisha watu kweli ya Biblia, kwa hiyo walijipatanisha na hali za huko na wakajishughulisha na huduma.
Katika siku hizo za mapema, mara nyingi ilikuwa kawaida kwamba hakuna aliyekuwa akingoja kuwakaribisha wamishonari. Ilikuwa ni juu yao kupata mahali pa kuishi. Wakati Charles Eisenhower, pamoja na wengine 11, walipowasili Kuba katika 1943, usiku wa kwanza walilala sakafuni. Siku iliyofuata walinunua vitanda na kutengeneza makabati wakitumia kreti za matofaa. Wakitumia michango yoyote waliyopokea kwa fasihi walizoangusha, pamoja na alawansi ya kiasi iliyoandaliwa na Watch Tower Society kwa mapainia wa pekee, kila kikundi cha wamishonari kilimtegemea Yehova ili abariki jitihada zao za kulipa kodi ya nyumba, kupata chakula, na kulipa gharama nyingine muhimu.
Nyakati nyingine matayarisho ya chakula yalitaka mtu abadili njia ya kufikiri. Mahali ambapo hakukuwa na friji, safari za kila siku kwenda sokoni zilihitajika. Katika nchi nyingi upishi ulifanywa kwa makaa au mioto ya kuni badala ya gesi au stovu (jiko) ya stima. George na Willa Mae Watkins, waliogawiwa Liberia, walipata kwamba stovu yao ilikuwa ni miamba mitatu tu iliyotumiwa kuegemeza birika la chuma.
Namna gani kuhusu maji? Akitazama nyumba yake mpya katika India, Ruth McKay alisema: ‘Hapa kuna nyumba ambayo sijapata kuona. Jikoni hamna bakuli la kuoshea, ni mfereji tu wa maji kwenye ukuta ulio kwenye kona wenye saruji iliyoinuliwa ili kuzuia maji yasitiririke sakafuni kote. Mfereji hautoi maji kwa saa 24, bali inabidi maji yahifadhiwe kwa ajili ya nyakati ambapo hakuna maji.’
Kwa sababu hawakuwa wamezoea hali za huko, baadhi ya wamishonari walisumbuliwa na magonjwa wakati wa miezi ya mapema katika migawo yao. Russell Yeatts alishikwa na ugonjwa wa kuhara mara kwa mara alipowasili Kurasao katika 1946. Lakini ndugu mwenyeji alikuwa ametoa sala ya bidii ya shukrani kwa Yehova kwa ajili ya wamishonari hivi kwamba wamishonari hao hawangeweza kufikiria kuondoka. Walipowasili Upper Volta (sasa Burkina Faso), Brian na Elke Wise walijipata katika hali ya anga inayoathiri afya ya mtu. Walilazimika kujifunza kuwezana na hali-joto za mchana za Sentigredi 43. Wakati wa mwaka wao wa kwanza, joto jingi pamoja na malaria ilimfanya Elke awe mgonjwa kwa majuma kadhaa kwa wakati mmoja. Mwaka uliofuata, Brian alilala kitandani kwa miezi mitano akiwa na ugonjwa wa mchochota wa ini. Lakini upesi walipata kwamba walikuwa na mafunzo ya Biblia mengi mazuri kadiri ambayo wangeweza kuongoza—na mengine zaidi. Kuwapenda watu hao kuliwasaidia wavumilie; na ndivyo na uhakika wa kwamba waliona mgawo wao kuwa pendeleo na mazoezi mazuri kwa lolote ambalo Yehova alikusudia kwa ajili yao wakati ujao.
Kadiri miaka ilivyopita, wamishonari wengi walikaribishwa kwenye migawo yao na wale waliowatangulia au Mashahidi wenyeji. Wengine walipewa mgawo kwenda kwenye nchi ambako majiji makuu yalikuwa ya kisasa. Kuanzia 1946, Watch Tower Society pia ilijitahidi kuandaa makao mazuri na fanicha inayohitajiwa kwa kila kikundi cha wamishonari pamoja na fedha za chakula, hivyo kuwaondolea masumbuko na kuwawezesha kuelekeza uangalifu zaidi kwenye kazi ya kuhubiri.
Katika sehemu kadhaa, usafiri ulikuwa ono lililojaribu uvumilivu wao. Katika Papua New Guinea, baada ya mvua kunyesha, dada wengi wamishonari walijipata wakibeba ugavi katika mfuko wa kubebea mgongoni huku wakitembea kupitia kichaka kwenye kijia cha miguu chenye kuteleza kilichokuwa na matope mengi sana hivi kwamba nyakati nyingine viatu vyao vilitoka. Katika Amerika Kusini, wamishonari wengi wamesafiri kwa basi kwa njia inayoogopesha sana kwenye vibarabara vyembamba vilivyo juu kwenye Milima ya Andes. Ni ono lisilosahaulika upesi wakati basi lenu, likiwa kwenye sehemu ya nje ya barabara, linapopita gari jingine kubwa linaloenda upande mnaotoka kwenye kona isiyo na vyuma vya usalama nawe unahisi basi likianza kuegemea upande wa mtelemko wa ghafula!
Katika sehemu fulani mapinduzi ya kisiasa yalionekana kuwa sehemu ya kawaida ya maisha, lakini Mashahidi wamishonari walikumbuka taarifa ya Yesu kwamba wanafunzi hawangekuwa “sehemu ya ulimwengu”; kwa hiyo hawakupendelea upande wowote kuhusiana na mahitilafiano hayo. (Yn. 15:19, NW) Walijifunza kushinda udadisi wowote ambao ungewaweka hatarini. Mara nyingi, jambo bora zaidi lilikuwa ni kuepuka barabara hadi hali zituliapo. Wamishonari tisa katika Vietnam walikuwa wakiishi katikati kabisa mwa jiji la Saigon (sasa Jiji la Ho Chi Minh) wakati vita ilipokumba jiji hilo. Wangeweza kuona mabomu yakiangushwa, mioto kotekote jijini, na maelfu ya watu wakitoroka kuokoa maisha zao. Lakini wakithamini kwamba Yehova alikuwa amewatuma ili watoe maarifa yenye kuleta uhai kwa watu wenye njaa ya kiroho, walimtegemea ili wapate ulinzi.
Hata kulipokuwa na amani ya kiasi, ilikuwa vigumu kwa wamishonari kuendelea na huduma yao katika sehemu za majiji ya Waasia. Kutokea tu kwa mgeni katika barabara nyembamba za sehemu ya maskini katika Lahore, Pakistan, kulitosha kuvuta umati wa watoto wachafu, wasio nadhifu wa kila umri. Wakipiga makelele na kusukumana, wangewafuata wamishonari nyumba hadi nyumba, mara nyingi wakiingia ndani ya nyumba huku wakiwafuata wahubiri. Upesi nyumba zote barabarani zingeambiwa bei ya magazeti na kwamba mgeni huyo alikuwa ‘anafanyiza Wakristo.’ Katika hali hizo, mara nyingi ilifaa kuondoka sehemu hiyo. Mara nyingi mtu angeondoka huku akiandamwa na mayowe, makofi, na nyakati nyingine mawe yaliyorushwa na watoto.
Desturi za mahali mara nyingi zilitaka wamishonari wabadilikane. Katika Japani walijifunza kuacha viatu vyao kwenye milango ya nyumba wanapoingia nyumba. Na walilazimika kuzoea, ilipowezekana, kuketi sakafuni mbele ya meza fupi kwenye mafunzo ya Biblia. Katika sehemu fulani za Afrika, walijifunza kwamba kutumia mkono wa kushoto ili kumpa mtu kitu kulionwa kuwa ni kufanya udhia. Na walipata kwamba katika sehemu hiyo ya ulimwengu, ilikuwa tabia mbaya kujaribu kueleza sababu ya kuzuru kwao kabla ya kushiriki katika mazungumzo ya kawaida—kujuliana hali za afya na kujibu maswali kuhusu kule mtu ametoka, ana watoto wangapi, na kadhalika. Katika Brazili wamishonari walipata kwamba badala ya kugonga milango, walihitaji kupiga makofi kwenye lango la mbele ili kumwita mwenye nyumba.
Hata hivyo, katika Lebanoni wamishonari walikabiliwa na desturi za aina nyingine. Ni ndugu wachache walioleta wake zao na mabinti zao mikutanoni. Wanawake waliohudhuria walikaa nyuma nyakati zote, si miongoni mwa wanaume kamwe. Wamishonari, bila kujua desturi hiyo, walisababisha usumbufu mkubwa katika mkutano wao wa kwanza. Wenzi waliooana waliketi mbele, na wasichana wamishonari waseja waliketi mahali popote palipokuwa wazi. Lakini baada ya mkutano mazungumzo juu ya kanuni za Kikristo yalisaidia kuondoa kutokuelewa. (Linganisha Kumbukumbu la Torati 31:12; Wagalatia 3:28.) Mtengano huo ukakoma. Wake na mabinti wengi zaidi wakahudhuria mikutano. Pia walijiunga na dada wamishonari katika huduma ya nyumba hadi nyumba.
Ugumu wa Lugha Mpya
Kikundi kidogo cha wamishonari waliowasili Martinique katika 1949 walikuwa na maarifa kidogo sana ya Kifaransa, lakini walijua kwamba watu walihitaji ujumbe wa Ufalme. Wakiwa na imani halisi walianza kwenda mlango kwa mlango, wakijaribu kusoma mistari michache ya Biblia au dondoo kutoka kwa kichapo walichokuwa wakitoa. Kwa saburi Kifaransa chao kikawa bora hatua kwa hatua.
Ingawa ilikuwa tamaa yao kusaidia Mashahidi wenyeji na watu wengine wanaopendezwa, wamishonari wenyewe ndio mara nyingi waliohitaji msaada kwanza—wa lugha. Wale waliopelekwa Togo walipata kwamba sarufi ya Kiewe, lugha kuu ya wenyeji, ilikuwa tofauti na ile ya lugha za Ulaya, pia kwamba kadiri ya sauti ambayo neno linatamkwa yaweza kubadilisha maana. Hivyo, neno lenye herufi mbili kama vile to, linapotamkwa kwa sauti ya kadiri ya juu, laweza kumaanisha sikio, mlima, baba-mkwe, au kabila; kwa sauti ya chini, linamaanisha nyati. Wamishonari walioanza utumishi katika Vietnam walikabiliwa na lugha iliyotumia namna sita za sauti mbalimbali kwa neno moja, kila namna ya sauti ikitokeza maana tofauti.
Edna Waterfall, aliyepewa mgawo Peru, hakusahau upesi nyumba ya kwanza aliyojaribu kutoa ushahidi kwa Kihispania. Huku akitokwa jasho kwa kuona wasiwasi, alijikwaakwaa katika utoaji wake uliokaririwa, akatoa fasihi, na kupanga kuwa na funzo la Biblia pamoja na bibi mzee-mzee. Kisha mwanamke huyo akasema katika Kiingereza safi: “Ni sawa basi. Nitajifunza nawe na tutafanya hivyo katika Kihispania tu ili nikusaidie ujifunze Kihispania.” Akiwa ameshtuka, Edna alijibu: “Wajua Kiingereza? Na uliniacha niseme yote hayo katika Kihispania changu cha jikoni?” “Ilikufaa,” yule mwanamke akajibu. Na, kwa kweli, ilimfaa! Kama vile Edna alivyokuja kuthamini baadaye, hasa kusema katika lugha fulani ni sehemu muhimu ya kujifunza lugha hiyo.
Katika Italia, wakati George Fredianelli alipojaribu kusema lugha hiyo, alipata kwamba yale aliyofikiri kuwa maneno ya Kiitalia (lakini hasa yalikuwa maneno ya Kiingereza yaliyofanywa kuwa ya Kiitalia) hayakuwa yanaeleweka. Ili kukabili tatizo hilo, aliamua kuandika hotuba zake za makutaniko kikamili na kuzitoa kwa kutumia hati. Lakini wengi katika wasikilizaji wake wangelala usingizi. Kwa hiyo alitupilia mbali hati, akazungumza bila kutazamia, na akawaomba wasikilizaji wamsaidie alipokwama. Hilo liliwafanya wakae macho, na likamsaidia kufanya maendeleo.
Ili kuwaanzisha wamishonari katika lugha yao mpya, mtaala wa mafunzo ya Gileadi wa madarasa ya mapema ulitia ndani lugha kama vile Kihispania, Kifaransa, Kiitalia, Kireno, Kijapani, Kiarabu, na Kiurdu. Kwa muda wa miaka, lugha zaidi ya 30 zilifunzwa. Lakini kwa kuwa wahitimu wa darasa lolote lile hawakuenda wote kwenye sehemu ambazo lugha ileile ilitumiwa, badala ya madarasa hayo ya lugha, baadaye mipango ilifanywa kwa ajili ya kipindi kirefu cha mafunzo mengi ya lugha yaliyosimamiwa walipowasili katika migawo yao. Katika mwezi wa kwanza, wapya walijitia kikamili katika funzo la lugha kwa saa 11 kila siku; na mwezi uliofuata, nusu ya muda wao ilitumiwa katika kujifunza lugha nyumbani, na nusu ile nyingine ilitumiwa katika kutumia ujuzi huo katika huduma ya shambani.
Hata hivyo, ilionwa kwamba utumizi wenyewe wa lugha katika huduma ya shambani ulikuwa ufunguo mkuu wa kufanya maendeleo; hivyo marekebisho yalifanywa. Wakati wa miezi mitatu ya kwanza kwenye mgawo, wamishonari wapya ambao hawakujua lugha ya wenyeji wangetumia muda wa saa nne kila siku wakiwa na mwalimu mwenye sifa za kustahili, na kuanzia mwanzoni kabisa, kwa kutoa ushahidi kwa wenyeji kuhusu Ufalme wa Mungu, wangetumia yale waliyokuwa wakijifunza.
Vikundi vingi vya wamishonari walifanya kazi pamoja ili kufanya ufahamu wao wa lugha uwe bora. Wangezungumzia maneno mapya machache, au mengi kama 20, kila siku wakati wa kiamshakinywa na kisha kujitahidi kuyatumia katika huduma ya shambani.
Kujifunza lugha ya mahali kumekuwa jambo la muhimu katika kupata utumainifu wa watu. Katika maeneo fulani, kuna kutoamini wageni kwa kiasi fulani. Hugh na Carol Cormican wametumikia wakiwa waseja au wakiwa wenzi waliooana katika nchi tano za Afrika. Wanajua vema kuhusu kutoaminiana ambako huwa kati ya Waafrika na watu wa Ulaya. Lakini wanasema: “Kusema katika lugha ya mahali huondoa hisi hizo upesi. Zaidi ya hiyo, wengine ambao hawaelekei kusikiliza habari njema kutoka kwa wananchi wenzao wanakuwa wenye utayari wa kutusikiliza, kuchukua fasihi, na kujifunza, kwa sababu tumefanya jitihada ili kusema nao katika lugha yao wenyewe.” Ili kufanya hivyo, Ndugu Cormican alijifunza lugha tano, mbali na Kiingereza, na Dada Cormican alijifunza sita.
Bila shaka, kwaweza kuwa na matatizo wakati mtu anapojaribu kujifunza lugha mpya. Katika Puerto Riko ndugu aliyejitolea kucheza kwa kutumia kinanda ujumbe wa Biblia uliorekodiwa kwa wenye nyumba angefunga kinanda chake na kwenda kwenye mlango uliofuata wakati mtu alipojibu, “¡Como no!” Kwake, ilisikika kama “La,” na ilichukua muda kabla hajajua kwamba maneno hayo yalimaanisha “Ndiyo bila shaka!” Kwa upande ule mwingine, wakati mwingine wamishonari hawakuelewa wakati mwenye nyumba aliposema hapendezwi, kwa hiyo waliendelea tu kuhubiri. Kama tokeo, wenye nyumba wachache wenye huruma walinufaika.
Kulikuwa na hali za kuchekesha pia. Leslie Franks, katika Singapore, alijifunza kwamba ni lazima awe mwangalifu asiseme juu ya nazi (kelapa) alipomaanisha kichwa (kepala), na nyasi (rumput) alipomaanisha nywele (rambut). Mishonari mmoja katika Samoa, kwa sababu ya kutamka vibaya, alimuuliza mwenyeji, “Ndevu zako zikoje?” (yule mwenyeji hakuwa na ndevu), wakati lile lililokusudiwa lilikuwa kuulizia kwa adabu hali ya mke wake. Katika Ekuado, wakati dereva wa basi alipoanza kuendesha basi kwa ghafula, Zola Hoffman, aliyekuwa amesimama ndani ya basi, alitupwa kinyumenyume na kuanguka mapajani mwa mwanamume mmoja. Huku akiona aibu, alijaribu kuomba msamaha. Lakini lile alilosema lilikuwa, “Con su permiso” (Ukiniruhusu). Wakati mwanamume yule kwa ucheshi alipojibu, “Haya basi, endelea kuketi, Bibi,” abiria wale wengine waliangua kicheko.
Hata hivyo, matokeo mazuri katika huduma yalikuwa yanapatikana kwa sababu wamishonari walijitahidi. Lois Dyer, aliyewasili Japani katika 1950, akumbuka shauri alilopewa na Ndugu Knorr: “Fanya yote uwezayo, na, hata iwapo ukifanya makosa, fanya jambo fulani!” Yeye alifanya hivyo, na ndivyo na wengine wengi. Wakati wa miaka 42 iliyofuata, wamishonari waliotumwa Japani waliona idadi ya wapiga-mbiu wa Ufalme ikiongezeka kutoka wachache tu hadi zaidi ya 170,000 na ukuzi umezidi kuendelea tu. Ni thawabu kubwa jinsi gani kwa sababu, baada ya kumtegemea Yehova ili kupata mwelekezo, walikuwa wenye nia ya kujaribu!
Kufungua Mashamba Ramaniya, Kusitawisha Mengine
Katika hesabu fulani ya nchi na vikundi vya visiwa, ilikuwa ni wamishonari waliozoezwa Gileadi ambao ama walianza kazi ya kuhubiri Ufalme au wakaipa nguvu mpya baada ya kiasi kidogo cha kutoa ushahidi kufanywa na wengine. Inaonekana kwamba walikuwa Mashahidi wa Yehova wa kwanza kuhubiri habari njema katika Somalia, Sudan, Laos, na vikundi vingi vya visiwa duniani pote.
Mahubiri fulani yalikuwa yamefanywa mapema katika sehemu kama vile Bolivia, Jamhuri ya Dominika, Ekuado, El Salvador, Honduras, Nikaragua, Ethiopia, Gambia, Liberia, Kambodia, Hong Kong, Japani, na Vietnam. Lakini hakukuwa na Shahidi wa Yehova yeyote aliyekuwa akiripoti utendaji katika nchi hizo wakati wahitimu wamishonari wa Shule ya Gileadi walipowasili. Mahali ilipowezekana, wamishonari walianza kueneza nchi nzima kwa utaratibu, wakikaza fikira kwanza kwenye majiji makubwa zaidi. Hawakuangusha fasihi tu na kusonga mbele, kama walivyofanya makolpota zamani. Kwa saburi waliwarudia waliopendezwa, wakaongoza mafunzo ya Biblia pamoja nao, na kuwazoeza katika huduma ya shambani.
Nchi nyingine zilikuwa na wapiga-mbiu wa Ufalme kumi hivi tu (na, pindi nyingi, wachache zaidi) kabla ya kuwasili kwa wahitimu wamishonari wa Shule ya Gileadi. Zilizotiwa ndani ya hizo ni Kolombia, Guatemala, Haiti, Puerto Riko, Venezuela, Burundi, Ivory Coast (sasa ni Côte d’Ivoire), Kenya, Mauritius, Senegal, Kusini-Magharibi mwa Afrika (sasa ni Namibia), Ceylon (sasa ni Sri Lanka), China, na Singapore, kutia na vikundi vingi vya visiwa. Wamishonari waliweka kielelezo kizuri cha bidii katika huduma, wakasaidia Mashahidi wenyeji kufanya uwezo wao uwe bora, wakapanga makutaniko kitengenezo, na wakasaidia ndugu wastahili kuchukua uongozi. Katika sehemu nyingi pia walifungua kazi ya kuhubiri katika maeneo ambayo hayakuwa yamehubiriwa awali.
Kwa msaada huo idadi ya Mashahidi ilianza kukua. Katika nchi nyingi kati ya hizo, sasa kuna maelfu ya Mashahidi wa Yehova watendaji. Katika baadhi yazo, kuna wasifaji wa Yehova makumi ya maelfu, au hata zaidi ya mia moja elfu.
Watu Wengine Walikuwa na Hamu ya Kusikia
Katika maeneo mengine, wamishonari walipata watu wengi wenye nia na hamu ya kujifunza. Wakati Ted na Doris Klein, wahitimu wa darasa la kwanza la Gileadi, walipowasili katika Visiwa vya Virgin katika 1947, kulikuwa na watu wengi sana waliotaka kujifunza Biblia hivi kwamba mara nyingi hawakumaliza siku yao ya utumishi hadi usiku wa manane. Katika mhadhara wa kwanza wa peupe ambao Ndugu Klein alitoa katika Soko Kuu la Charlotte Amalie, kulikuwa watu elfu waliohudhuria.
Joseph McGrath na Cyril Charles walitumwa kwenye eneo la Amis katika Taiwan katika 1949. Walijipata wakiishi katika nyumba zenye paa za nyasi na sakafu za udongo. Lakini kusudi lao la kuwa huko lilikuwa kusaidia watu. Baadhi ya watu wa kabila la Waamis walikuwa wamepokea fasihi za Watch Tower, wakapendezwa na yale waliyosoma, na wakashiriki habari njema na wengine. Sasa wamishonari walikuwa huko kuwasaidia wakue kiroho. Waliambiwa kwamba watu 600 walipendezwa na kweli, lakini jumla ya 1,600 walihudhuria mikutano waliyofanya walipohama kutoka kijiji hadi kijiji. Watu hao wanyenyekevu walikuwa na nia ya kujifunza, lakini walikosa ujuzi sahihi wa mambo mengi. Kwa saburi ndugu walianza kuwafunza, wakikazia somo moja kwa wakati mmoja, mara nyingi wakitumia muda wa saa nane au zaidi katika mazungumzo ya maswali na majibu juu ya mambo fulani kwenye kila kijiji. Mazoezi yaliandaliwa pia kwa wale 140 walioonyesha tamaa ya kushiriki katika kutoa ushahidi nyumba hadi nyumba. Hilo lilikuwa ono la kupendeza jinsi gani kwa wamishonari! Lakini mengi bado yalihitaji kufanywa ikiwa kungekuwa na ukuzi imara wa kiroho.
Karibu miaka 12 baadaye, Harvey na Kathleen Logan, wamishonari waliozoezwa Gileadi waliokuwa wakitumikia Japani, walipewa mgawo wa kuandaa msaada zaidi kwa ndugu Waamis. Ndugu Logan alitumia wakati mwingi akiwasaidia waelewe mafundisho na kanuni za msingi za Biblia na mambo ya kitengenezo. Dada Logan alifanya kazi pamoja na dada Waamis katika utumishi wa shambani kila siku, baada ya hapo akijitahidi kujifunza kweli za msingi za Biblia pamoja nao. Halafu, katika 1963, Watch Tower Society ilipanga kwamba wajumbe kutoka nchi 28 wakusanyike pamoja na Mashahidi wenyeji huko katika kijiji cha Shou Feng, kuhusiana na mkusanyiko wa ulimwenguni pote. Yote hayo yalianza kuweka msingi imara kwa ajili ya ukuzi zaidi.
Katika 1948, wamishonari wawili, Harry Arnott na Ian Fergusson, waliwasili katika Rhodesia Kaskazini (sasa Zambia). Wakati huo tayari kulikuwa na makutaniko 252 ya Mashahidi Waafrika wenyeji, lakini sasa uangalifu ulikaziwa kwa watu wa Ulaya pia waliohamia huko kuhusiana na shughuli za kuchimba shaba. Itikio lilikuwa la kusisimua. Fasihi nyingi ziliangushwa; mafunzo ya Biblia yalifanya maendeleo upesi. Mwaka huo kulikuwa na ongezeko la asilimia 61 la idadi ya Mashahidi watendaji katika huduma ya shambani.
Katika sehemu nyingi lilikuwa jambo la kawaida kwa wamishonari kuwa na orodha ya watu wanaongoja ili wapate mafunzo ya Biblia. Nyakati nyingine watu wa ukoo, majirani, na marafiki wangekuwapo wakati mafunzo yalipokuwa yakiongozwa. Hata kabla watu hawajaweza kuwa na funzo lao la kibinafsi la Biblia, huenda wakahudhuria mikutano kwa ukawaida katika Jumba la Ufalme.
Hata hivyo, katika nchi nyinginezo, ingawa jitihada nyingi zilifanywa na wamishonari, mavuno yalikuwa madogo sana. Mapema kama 1953, wamishonari wa Watch Tower walitumwa Pakistan Mashariki (sasa Bangladesh), ambako idadi kubwa ya watu, ambayo sasa yapita 115,000,000 ni Waislamu na Wahindu. Jitihada nyingi zilitiwa ili kusaidia watu hao. Na bado, kufikia 1992, kulikuwa na waabudu wa Yehova 42 tu katika nchi hiyo. Hata hivyo, machoni pa wamishonari wanaotumikia katika sehemu hizo, kila mtu anayeitikia ibada ya kweli ni mwenye thamani hasa—kwa sababu ni wachache sana wanaopatikana.
Msaada Wenye Upendo kwa Mashahidi Wenzi
Kazi ya msingi ya wamishonari ni kueneza evanjeli, kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu. Lakini walipokuwa wakishiriki binafsi katika utendaji huo, waliweza pia kuandaa msaada mwingi kwa Mashahidi wenyeji. Wamishonari wamewaalika waende nao katika huduma ya shambani na wameshiriki nao madokezo juu ya jinsi ya kushughulikia hali ngumu. Kwa kuwatazama wamishonari, Mashahidi wenyeji mara nyingi wamejifunza jinsi ya kuendesha huduma yao kwa njia yenye utaratibu zaidi na jinsi ya kuwa walimu wenye matokeo zaidi. Wamishonari nao wamesaidiwa na Mashahidi wenyeji wajipatanishe na desturi za huko.
Alipowasili Ureno katika 1948, John Cooke alichukua hatua ili kupanga kazi ya nyumba hadi nyumba kwa utaratibu. Ingawa walikuwa wenye nia, Mashahidi wengi wenyeji walihitaji mazoezi. Baadaye alisema: “Sitasahau kamwe moja kati ya ziara zangu za kwanza katika huduma pamoja na akina dada katika Almada. Naam, dada sita walienda kwenye nyumba ileile moja pamoja. Unaweza kuwazia kikundi cha wanawake sita wakisimama mlangoni wakati mmoja wao alipokuwa akitoa mahubiri! Lakini hatua kwa hatua mambo yalianza kusitawi na kufanya maendeleo.”
Kielelezo chenye ujasiri cha wamishonari kiliwasaidia Mashahidi katika Visiwa vya Leeward wawe wajasiri, na si wenye kuhofishwa na wapinzani waliojaribu kuzuia kazi. Imani iliyoonyeshwa na mishonari mmoja iliwasaidia akina ndugu katika Hispania waanze huduma ya nyumba hadi nyumba, kujapokuwa udikteta wa Ufashisti wa Katoliki ambao ulitawala wakati huo. Wamishonari waliotumikia katika Japani baada ya Vita ya Ulimwengu 2 waliweka kielelezo cha kuwa wenye busara—bila kukazia kushindwa kwa dini ya kitaifa, baada ya maliki wa Japani kukana umungu wake, lakini badala yake wakitoa ithibati yenye kusadikisha ya imani katika Muumba.
Mashahidi wenyeji waliwatazama wamishonari na mara nyingi waliathiriwa sana katika njia ambayo wamishonari hawangeweza kung’amua wakati huo. Katika Trinidad, matukio yaliyoonyesha unyenyekevu wa wamishonari, nia yao ya kuvumilia hali ngumu, na kazi yao ngumu katika utumishi wa Yehova kujapokuwa na hali ya hewa yenye joto, bado huzungumzwa na wengi miaka mingi baada ya hapo. Mashahidi katika Korea walivutiwa sana na roho ya kujidhabihu ya wamishonari ambao kwa miaka kumi hawakuondoka nchini ili kuzuru familia zao kwa sababu serikali haingepeana idhini ya kuingia tena nchini isipokuwa katika hali chache za dharura za “huruma za kibinadamu.”
Wakati na baada ya mafunzo yao ya kwanza ya Gileadi, wamishonari wengi walikuwa na mwono wa karibu wa utendaji wa makao makuu ya tengenezo la Yehova linaloonekana. Mara nyingi walikuwa na fursa nyingi ya kushirikiana na washiriki wa Baraza Linaloongoza. Baadaye, katika migawo yao ya mishonari, waliweza kuwaeleza Mashahidi wenyeji na watu waliopendezwa karibuni juu ya ripoti walizojionea wao wenyewe kuhusu jinsi tengenezo linavyofanya kazi pamoja na uthamini waliokuwa nao kulielekea. Kina cha uthamini walichotoa kuhusu utendaji wa kitheokrasi wa tengenezo mara nyingi kilikuwa jambo la maana katika ukuzi uliopatikana.
Katika mahali pengi ambapo wamishonari walitumwa, hapakuwa na mikutano ya kutaniko walipowasili. Kwa hiyo walifanya mipango iliyohitajika, wakaongoza mikutano, na kushughulikia sehemu nyingi za mikutano hadi wengine walipostahili kushiriki mapendeleo hayo. Wakati wote walikuwa wakiwazoeza ndugu wengine ili kwamba waweze kustahili kuchukua madaraka. (2 Tim. 2:2) Mara nyingi mahali pa kwanza pa kukutania palikuwa penye makao ya wamishonari. Baadaye, mipango ilifanywa kwa ajili ya Majumba ya Ufalme.
Mahali ambapo makutaniko yalikuwapo tayari, wamishonari walichangia kwa kufanya mikutano iwe yenye kupendeza na yenye mafunzo zaidi. Maelezo yao yaliyotayarishwa vizuri yalithaminiwa na upesi yakaweka kigezo ambacho wengine walijaribu kuiga. Wakitumia mazoezi yao ya Gileadi, ndugu waliweka kielelezo kizuri katika kusema mbele ya watu na kufundisha, na kwa furaha walitumia wakati pamoja na ndugu wenyeji ili kuwasaidia wajifunze ustadi huo. Katika nchi ambako watu walikuwa wenye mwendo wa polepole kidesturi na si wenye kuwahi, wamishonari pia waliwasaidia kwa saburi watambue thamani ya kuanza mikutano kwa wakati na kuwatia moyo wote wafike kwa wakati.
Hali walizopata katika sehemu nyingine zilionyesha kwamba msaada ulihitajiwa ili kujenga uthamini katika umaana wa kushikamana na viwango vya uadilifu vya Yehova. Kwa kielelezo, katika Botswana walipata kwamba bado dada fulani walivalisha watoto wao nyuzi au shanga kuwa ulinzi dhidi ya madhara, bila kutambua kikamili kwamba desturi hiyo ilikuwa ya kishirikina na uchawi. Katika Ureno walipata hali zilizosababisha mtengano. Kwa saburi, msaada wenye upendo, na kuwa imara ilipohitajika, afya ya kiroho iliyofanya maendeleo ilidhihirika.
Wamishonari waliopewa mgawo wa vyeo vya uangalizi katika Finland walitoa wakati na jitihada nyingi kuwazoeza ndugu wenyeji kutoa sababu juu ya matatizo kwa msaada wa kanuni za Biblia na hivyo kufikia mkataa unaopatana na njia ya Mungu ya kufikiri. Katika Argentina walisaidia ndugu pia wajifunze thamani ya ratiba, jinsi ya kuweka maandishi, umaana wa kuweka faili. Katika Ujerumani walisaidia ndugu waaminifu-washikamanifu ambao kwa njia fulani walikuwa wagumu katika maoni yao, kwa sababu ya vita vyao vya kuokoka katika kambi za mateso, waige kwa ukamili zaidi njia za upole za Yesu Kristo wanapochunga kundi la Mungu.—Mt. 11:28-30; Mdo. 20:28.
Kazi ya baadhi ya wamishonari ilitia ndani kushughulika na maofisa wa serikali, kujibu maswali yao, na kupeleka maombi ili kazi ya Mashahidi wa Yehova itambuliwe kisheria. Kwa kielelezo, katika muda wa karibu miaka minne, Ndugu Joly, aliyepewa mgawo kwenda Kamerun pamoja na mke wake, alitia jitihada nyingi za kupata kutambuliwa kisheria. Alizungumza na maofisa Wafaransa na Waafrika mara nyingi. Hatimaye, baada ya badiliko la serikali, walitambuliwa kisheria. Kufikia wakati huo Mashahidi walikuwa wamekuwa watendaji katika Kamerun kwa miaka 27 na tayari walikuwa na idadi ya zaidi ya 6,000.
Kushinda Magumu ya Utumishi wa Kusafiri
Baadhi ya wamishonari walikuwa wamegawiwa kutumikia wakiwa waangalizi wasafirio. Kulikuwa na uhitaji wa pekee katika Australia, ambako kwa kukosa hekima, baadhi ya jitihada za akina ndugu zilikuwa zimekengeushwa kutoka faida za Ufalme hadi kwenye kufuatia faida za kimwili wakati wa Vita ya Ulimwengu 2. Hilo lilitatuliwa baadaye, na wakati wa ziara ya Ndugu Knorr katika 1947, mkazo ulitolewa juu ya umaana wa kuweka kazi ya kuhubiri Ufalme mbele. Baadaye, idili, kielelezo chema, na njia za kufundisha za wahitimu wa Gileadi waliotumikia wakiwa waangalizi wa mzunguko na wa wilaya zilisaidia zaidi kusitawisha hali ya kiroho ifaayo miongoni mwa Mashahidi huko.
Kushiriki katika utumishi huo wa kusafiri mara nyingi kumetaka moyo wa kupenda ili kutoa jitihada nyingi na kukabili hatari. Wallace Liverance alipata kwamba njia pekee ya kufikia familia ya wahubiri walio mbali katika Volcán, Bolivia, ilikuwa ni kutembea kilometa 90 kwenda na kurudi kupitia sehemu kavu iliyochongoka katika jua lenye kuchoma kwenye kimo cha meta 3,400, huku akibeba mfuko wake wa kulalia, chakula, na maji, pamoja na fasihi. Ili kutumikia makutaniko katika Filipino, Neal Callaway alisafiri mara nyingi kwa mabasi ya mashambani yenye watu wengi huku nafasi ikitumiwa si na watu tu bali pia wanyama na bidhaa. Richard Cotterill alianza kazi yake akiwa mwangalizi asafiriye katika India wakati ambapo maelfu ya watu walikuwa wakiuawa kwa sababu ya chuki ya kidini. Alipotaka kutumikia akina ndugu katika sehemu yenye ghasia, karani wa reli alijaribu kumwambia asiende. Ilithibitika kuwa safari ya kuhofisha sana kwa wasafiri wengi, lakini Ndugu Cotterill alikuwa na upendo mwingi kwa ndugu zake, bila kujali mahali walipoishi au lugha waliyozungumza. Akimtegemea Yehova, alitoa sababu hivi: “Ikiwa ni mapenzi ya Yehova, nitajaribu kufika huko.”—Yak. 4:15.
Kuwatia Moyo Wengine Washiriki Katika Utumishi wa Wakati Wote
Kama tokeo la roho ya bidii iliyoonyeshwa na wamishonari, wengi ambao walifunzwa nao wameiga mifano yao kwa kuingia katika utumishi wa wakati wote. Katika Japani, ambako wamishonari 168 wametumikia, kulikuwa na mapainia 75,956 katika 1992; zaidi ya asilimia 40 ya wahubiri katika Japani walikuwa katika aina fulani ya utumishi wa wakati wote. Katika Jamhuri ya Korea uwiano ulikuwa uo huo.
Katika nchi ambazo uwiano wa Mashahidi kwa idadi ya watu wote ni mzuri, wahudumu wengi wa wakati wote wamealikwa wapokee mazoezi kwenye Shule ya Gileadi na kisha wametumwa kutumikia katika sehemu nyingine. Idadi kubwa ya wamishonari wametoka Marekani na Kanada; karibu 400 kutoka Uingereza; zaidi ya 240 kutoka Ujerumani; zaidi ya 150 kutoka Australia; zaidi ya 100 kutoka Sweden; kuongezea idadi kubwa kutoka Denmark, Finland, Hawaii, Uholanzi, New Zealand, na nyinginezo. Baadhi ya nchi ambazo zenyewe zilisaidiwa na wamishonari baadaye ziliandaa pia wale waliotazamiwa kuwa wamishonari kwa ajili ya utumishi katika nchi nyinginezo.
Kujazia Mahitaji Katika Tengenezo Lenye Kukua
Kadiri tengenezo limekua, ndivyo wamishonari wenyewe wamechukua madaraka zaidi. Idadi kubwa yao wametumikia wakiwa wazee au watumishi wa huduma katika makutaniko ambayo wamesaidia kusitawisha. Katika nchi nyingi wao walikuwa waangalizi wa mzunguko na wa wilaya wa kwanza. Kwa kuwa ukuzi zaidi umefanya ifae kwa Sosaiti kuanzisha ofisi mpya za tawi, idadi fulani ya wamishonari wamekabidhiwa daraka kuhusiana na uendeshaji wa tawi. Katika visa fulani wale ambao wamekuja kujua lugha vizuri wameombwa wasaidie katika kutafsiri na kuhakikisha usahihi wa fasihi za Biblia.
Hata hivyo, hasa wamehisi wamethawabishwa, wakati wale ambao walijifunza Neno la Mungu nao, au akina ndugu ambao waliwasaidia kufanya ukuzi wa kiroho, walipostahili kuchukua madaraka. Hivyo wenzi waliooana katika Peru walifurahi kuona baadhi ya wale waliojifunza nao wakitumikia wakiwa mapainia wa pekee, wakisaidia kuimarisha makutaniko mapya na kufungua eneo jipya. Mmoja kati ya washiriki wa Halmashauri ya Tawi ya nchi ya Sri Lanka alitoka katika familia iliyokuwa funzo la mishonari mmoja. Wamishonari wengine wengi wamekuwa na shangwe kama hizo.
Wamekabili upinzani pia.
Kukabili Upinzani
Yesu aliwaambia wafuasi wake kwamba wangenyanyaswa, kama vile alivyonyanyaswa. (Yn. 15:20) Kwa kuwa wamishonari kwa kawaida huja kutoka ng’ambo, mara nyingi kulipotokea mnyanyaso mwingi nchini, hilo lilimaanisha kufukuzwa nchini.
Katika 1967, Sona Haidostian na wazazi wake walikamatwa katika Aleppo, Siria. Waliwekwa gerezani kwa miezi mitano na kisha wakafukuzwa kutoka nchini bila vitu vyao. Margarita Königer, kutoka Ujerumani, alipewa mgawo kwenda Madagaska; lakini kufukuzwa kwa mara kwa mara kulimpeleka kwenye migawo mipya katika Kenya, Dahomey (Benin), na Upper Volta (Burkina Faso). Domenick Piccone na mke wake, Elsa, walifukuzwa kutoka Hispania katika 1957 kwa sababu ya kuhubiri kwao, kisha kutoka Ureno katika 1962, na kutoka Moroko katika 1969. Hata hivyo, katika kila nchi, huku wakijaribu kuzuia amri ya kufukuzwa, mema yalitimizwa. Ushahidi ulitolewa kwa maofisa. Kwa kielelezo, katika Moroko, walikuwa na fursa ya kutoa ushahidi kwa maofisa katika Sécurité Nationale, hakimu wa Mahakama Kuu, mkuu wa polisi katika Tangier, na mabalozi wa Marekani katika Tangier na Rabat.
Kufukuzwa kwa wamishonari hakujatokeza kukomeshwa kwa kazi ya Mashahidi wa Yehova, kama vile maofisa wengine walivyotazamia. Mbegu za kweli ambazo tayari zimepandwa huendelea kukua mara nyingi. Kwa kielelezo, wamishonari wanne walifanya huduma yao kwa miezi michache tu katika Burundi kabla ya serikali kuwalazimisha kuondoka katika 1964. Lakini mmoja wao aliendelea kuwasiliana kwa barua na mtu aliyependezwa, aliyeandika kusema kwamba alikuwa akijifunza Biblia na watu 26. Shahidi Mtanzania aliyehamia Burundi karibuni pia alikuwa mwenye shughuli katika kuhubiri. Hatua kwa hatua idadi yao ikakua hadi mamia wakawa wakishiriki ujumbe wa Ufalme na wengine.
Kwingineko, kabla ya kuamuru kufukuzwa kwao, maofisa walitumia jeuri kwa ukatili ili kujaribu kufanya kila mtu atii madai yao. Katika Gbarnga, Liberia, katika 1963, askari waliwakusanya wanaume, wanawake, na watoto 400 waliokuwa wakihudhuria mkusanyiko wa Kikristo huko. Askari waliwapigisha miguu hadi kwenye uwanja wa wanajeshi, wakawatisha, wakawapiga, na kudai kwamba kila mtu—bila kujali taifa au imani ya kidini—aisalimu bendera ya Liberia. Miongoni mwa kikundi hicho alikuwamo Milton Henschel, kutoka Marekani. Kulikuwa pia wamishonari kadhaa, kutia na John Charuk kutoka Kanada. Mmoja wa wahitimu wa Gileadi aliridhiana, kama vile alivyokuwa amefanya katika kisa cha mapema (ingawa hakuwa amejulisha hilo), na bila shaka hilo liliwafanya wengine waliokuwa kwenye kusanyiko waridhiane. Ikawa dhahiri ni nani kweli waliomhofu Mungu na ni nani waliohofu binadamu. (Mit. 29:25) Kufuatia hilo, serikali iliwaagiza Mashahidi wote wamishonari kutoka ng’ambo waondoke nchini, ingawa baadaye mwaka huohuo agizo rasmi kutoka kwa rais liliwaruhusu warudi.
Mara nyingi, hatua zinazochukuliwa na maofisa wa serikali dhidi ya wamishonari zimechochewa na makasisi. Nyakati nyingine uchochezi huo uliletwa kwa njia yenye hila. Nyakati nyingine, kila mtu alijua ni nani aliyekuwa akiamsha upinzani. George Koivisto hatasahau kamwe asubuhi yake ya kwanza katika utumishi wa shambani katika Medellín, Kolombia. Kwa ghafula genge la watoto wa shule wenye kupiga makelele lilitokea, likirusha mawe na mabonge ya udongo. Mwenye nyumba, ambaye hakuwa amepata kumwona tena, alimvuta ndani na kufunga mbao za dirisha, huku akiomba msamaha kwa tabia ya genge lililokuwa nje. Polisi walipowasili, wengine wao walimlaumu mwalimu kwa kuwaachilia wanafunzi wao. Lakini sauti nyingine ilisema: “Si hivyo! Ilikuwa ni padri! Alitangaza kwa vikuza-sauti kwamba wanafunzi waachiliwe ‘wakarushe mawe kwa Protestantes.’”
Ujasiri wa kimungu pamoja na kuwapenda kondoo kulihitajiwa. Elfriede Löhr na Ilse Unterdörfer walipewa mgawo kwenda kwenye bonde la Gastein katika Austria. Kwa muda mfupi, fasihi nyingi za Biblia ziliangushwa kwa watu waliokuwa na njaa ya chakula cha kiroho. Lakini makasisi wakachukua hatua. Waliwahimiza watoto wa shule wapigie wamishonari kelele kwenye barabara na kukimbia mbele yao ili kuwaonya wenye nyumba wasisikilize. Watu wakaogopa. Lakini kwa ustahimilivu wenye upendo, mafunzo machache mazuri yalianzishwa. Mhadhara wa Biblia wa watu wote ulipopangwa, padri alisimama kwa kutisha mbele ya mahali pa kukutania. Lakini wamishonari walipoenda barabarani kuwaalika watu, padri huyo alitoweka. Alimwita polisi na kisha akarudi, akitumaini kuvunja mkutano. Lakini jitihada zake hazikufaulu. Baadaye kutaniko zuri lilifanyizwa hapo.
Katika miji iliyo karibu Ibarra, Ekuado, Unn Raunholm na Julia Parsons walikabili tena na tena magenge yaliyochochewa na mapadri. Kwa sababu padri alifanyiza ghasia kila wakati wamishonari walipoenda San Antonio, dada waliamua kukazia fikira mji mwingine, uitwao Atuntaqui. Lakini siku moja mkuu wa eneo hilo akiwa mwenye wasiwasi alimhimiza Dada Raunholm aondoke mji huo upesi. “Padri anapanga maandamano dhidi yako, na sina watu wa kutosha kukulinda,” akajulisha. Yeye akumbuka waziwazi: “Umati ulikuwa unatujia! Ile beramu nyeupe na ya manjano ya Vatikani ilipeperushwa mbele ya kikundi hicho huku padri akipaza sauti shime kama vile ‘Kanisa Katoliki na lidumu daima!’ ‘Waprotestanti na watokomee mbali!’ ‘Ubikira wa Bikira na uendelee daima!’ ‘Maungamo na yaendelee daima!’ Kila wakati, umati ungerudia shime hizo neno kwa neno baada ya padri.” Wakati uo huo, wanaume kadhaa wakawaalika Mashahidi hao ndani ya Nyumba ya Wafanyakazi ili wapate usalama. Humo, wamishonari hao walijishughulisha kutoa ushahidi kwa watu wenye udadisi waliokuja kuona kile kilichokuwa kikiendelea. Waliangusha fasihi zote walizokuwa nazo.
Mitaala Iliyofanyizwa ili Kujazia Mahitaji ya Pekee
Wakati wa miaka tangu wamishonari wa kwanza kutumwa kutoka Shule ya Gileadi, tengenezo la Mashahidi wa Yehova limepata ukuzi kwa kiwango cha kustaajabisha. Katika 1943, shule ilipofunguliwa, kulikuwa Mashahidi 129,070 tu katika nchi 54 (lakini nchi 103 kulingana na vile ramani ilivyokuwa imegawanywa katika miaka ya mapema ya 1990). Kufikia 1992, kulikuwa na Mashahidi 4,472,787 katika nchi na vikundi vya visiwa 229 ulimwenguni pote. Kadiri ukuzi huo umetokea, mahitaji ya tengenezo yamebadilika. Ofisi za tawi ambazo wakati mmoja zilishughulikia Mashahidi wasiozidi mia moja walio katika makutaniko machache sasa yanasimamia utendaji wa makumi ya maelfu ya Mashahidi, na matawi mengi yameona kuwa yahitaji kuchapa fasihi humo nchini ili kuwatayarisha wale wanaoshiriki katika kazi ya kueneza evanjeli.
Ili kujazia mahitaji yanayobadilika, miaka 18 baada ya kufunguliwa kwa Shule ya Gileadi, mtaala wa miezi kumi wa mazoezi kwenye makao makuu ya Sosaiti uliandaliwa hasa kwa ndugu waliokuwa wakibeba mzigo mzito wa daraka katika ofisi za tawi za Watch Tower Society. Baadhi yao walikuwa wamehudhuria hapo awali mitaala ya miezi mitano ya wamishonari katika Gileadi; wengine hawakuwa wamehudhuria. Wote wangeweza kunufaika kutokana na mazoezi maalumu kwa ajili ya kazi yao. Mazungumzo juu ya jinsi ya kushughulikia hali mbalimbali na kujazia mahitaji ya kitengenezo kupatana na kanuni za Biblia yalikuwa na matokeo ya kuunganisha. Mtaala wao ulikuwa na somo la mchanganuo wa mstari kwa mstari wa Biblia nzima. Pia uliandaa pitio la historia ya dini; mazoezi katika mambo mengi yanayohusika katika kuendesha ofisi ya tawi, Kao la Betheli, na matbaa; na maagizo juu ya kuongoza huduma ya shambani, kupanga makutaniko mapya kitengenezo, na kufungua mashamba mapya. Mitaala hiyo (kutia na ule wa mwisho uliopunguzwa kuwa wa miezi minane) iliongozwa kwenye makao makuu ya ulimwengu, katika Brooklyn, New York, kuanzia 1961 hadi 1965. Wahitimu wengi walirudishwa kwenye nchi walizokuwa wakitumikia; wengine walipewa mgawo kwenye nchi nyinginezo ambako wangeweza kutoa msaada uliohitajiwa kwa kazi.
Kuanzia Februari 1, 1976, mpango mpya ulianzishwa katika ofisi za tawi za Sosaiti ili kujitayarishia upanuzi zaidi uliotazamiwa kulingana na unabii wa Biblia. (Isa. 60:8, 22) Badala ya kuwa na mwangalizi mmoja tu wa tawi, pamoja na msaidizi wake, ili kuandaa usimamizi kwa kila tawi, Baraza Linaloongoza liliweka ndugu watatu au zaidi wanaostahili ili watumikie kwenye kila Halmashauri ya Tawi. Matawi makubwa zaidi yangeweza kuwa na wengi kama saba kwenye halmashauri. Ili kuandaa mazoezi kwa ajili ya ndugu hao wote, mtaala maalumu wa Gileadi wa majuma matano katika Brooklyn, New York, ulipangwa. Madarasa 14 yaliyofanyizwa na washiriki wa Halmashauri ya Tawi kutoka sehemu zote za ulimwengu walipewa mazoezi maalumu kwenye makao makuu ya ulimwengu kuanzia mwishoni mwa 1977 hadi 1980. Ilikuwa fursa nzuri ya kuunganisha pamoja na kurekebisha utendaji.
Shule ya Gileadi iliendelea kuwazoeza wale waliokuwa na miaka mingi ya ujuzi katika huduma ya wakati wote na waliokuwa na nia na ambao wangeweza kutumwa nchi za ng’ambo, lakini wengi zaidi wangeweza kutumiwa. Ili kupanua mazoezi hayo, shule zilianzishwa katika nchi nyinginezo zikiwa upanuzi wa Gileadi ili wanafunzi wasilazimike kujifunza Kiingereza kabla ya kustahili kuhudhuria. Katika 1980-1981, Shule ya Uelimishaji ya Gileadi ya Mexico iliandaa mazoezi kwa wanafunzi wenye kusema Kihispania waliosaidia kujazia uhitaji wa haraka wa wafanyakazi wanaostahili katika Amerika ya Kati na Kusini. Katika 1981-1982, 1984, na tena katika 1992, madarasa ya Shule Iliyopanuliwa ya Gileadi yaliongozwa pia katika Ujerumani. Kutoka huko wahitimu walitumwa Afrika, Amerika Kusini, Ulaya Mashariki, na mataifa ya visiwa mbalimbali. Madarasa mengine yalifanyiwa India katika 1983.
Mashahidi wenyeji wenye bidii walipojiunga na wamishonari katika kupanua ushahidi wa Ufalme, idadi ya Mashahidi wa Yehova imeongezeka haraka, na hilo limeongoza kwenye kufanyizwa kwa makutaniko zaidi. Kati ya 1980 na 1987, hesabu ya makutaniko ulimwenguni pote iliongezeka kwa asilimia 27, hadi kwenye jumla ya 54,911. Katika maeneo mengine, ingawa wengi walikuwa wakihudhuria mikutano na kushiriki katika huduma ya shambani, wengi wa akina ndugu walikuwa wapya. Kulikuwa na uhitaji wa haraka wa wanaume Wakristo wenye ujuzi wa kutumikia wakiwa wachungaji wa kiroho na walimu, na pia kuchukua uongozi katika kazi ya kueneza evanjeli. Ili kusaidia kujazia uhitaji huo, katika 1987 Baraza Linaloongoza lilianzisha Shule ya Mazoezi ya Kihuduma ikiwa sehemu ya programu ya Shule ya Gileadi ya elimu ya Biblia. Mtaala wa majuma manane unatia ndani funzo lenye bidii la Biblia pamoja na uangalifu wa kibinafsi kwa ukuzi wa kiroho wa kila mwanafunzi. Mambo ya kitengenezo na ya kihukumu, pamoja na madaraka ya wazee na watumishi wa huduma, hufikiriwa, na mazoezi maalumu huandaliwa katika kusema mbele ya watu. Bila kuingilia madarasa ya kawaida ya kuwazoeza wamishonari, shule hii imetumia vifaa vingine, ikifanyiwa katika nchi mbalimbali. Wahitimu sasa wanajazia mahitaji ya maana katika nchi nyingi.
Hivyo mazoezi yaliyopanuliwa yaliyoandaliwa na Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower yameenda sambamba na mahitaji yanayobadilika ya tengenezo la kimataifa linalokua haraka.
“Mimi Hapa, Nitume Mimi”
Roho inayoonyeshwa na wamishonari ni kama ile ya nabii Isaya. Yehova alipomfahamisha kuhusu fursa ya utumishi wa pekee, yeye aliitikia: “Mimi hapa, nitume mimi.” (Isa. 6:8) Moyo huo wa hiari umesukuma maelfu ya wanaume na wanawake vijana kuacha nyuma mazingira wanayojua na watu wa ukoo ili wakatumike kwa ajili ya kuendelezwa kwa mapenzi ya Mungu mahali popote wanapohitajiwa.
Hali za familia zimeleta mabadiliko katika maisha za wamishonari wengi. Idadi fulani ya wale waliopata watoto baada ya kuwa wamishonari waliweza kubaki katika nchi walikopewa mgawo, wakifanya kazi ya kimwili iliyohitajiwa na kufanya kazi pamoja na makutaniko. Wengine, baada ya miaka ya utumishi, walilazimika kurudi kwenye nchi yao ili kutunza wazazi wao wazee-wazee, au kwa sababu nyinginezo. Lakini walihesabu kuwa pendeleo kushiriki katika utumishi wa mishonari kwa muda mrefu kadiri walivyoweza.
Wengine wameweza kufanya utumishi wa mishonari uwe kazi yao ya maisha. Ili kuifanya, wote wamelazimika kushughulikia hali ngumu. Olaf Olson, ambaye amefurahia kazi-maisha ya mishonari ya muda mrefu katika Kolombia, alikiri hivi: “Mwaka wa kwanza ulikuwa ndio mgumu zaidi.” Hiyo hasa ilikuwa kwa sababu ya kutoweza kujieleza mwenyewe vizuri vya kutosha katika lugha yake mpya. Yeye aliongeza: “Ikiwa ningeendelea kufikiri kuhusu nchi niliyokuwa nimeacha, nisingekuwa mwenye furaha, lakini niliamua kuishi kimwili na kiakili pia katika Kolombia, kufanya urafiki na ndugu na dada walio katika kweli huko, kuendelea kujaza maisha yangu na huduma, na upesi nikazoea mgawo wangu.”
Kustahimili kwao katika migawo yao hakukuwa kwa sababu waliona mazingira yao yaliyowazunguka kuwa bora kabisa. Norman Barber, aliyetumikia katika Burma (sasa Myanmar) na India, kutoka 1947 hadi kifo chake katika 1986, alijieleza mwenyewe hivi: “Ikiwa mtu anashangilia kwa kutumiwa na Yehova, basi mahali pamoja pafaa kama penginepo. . . . Kusema wazi, hali ya hewa ya kitropiki sio wazo langu la hali ya hewa bora kabisa ya kuishi. Wala maisha ya watu wa tropiki si ndiyo maisha ambayo ningechagua binafsi. Lakini kuna mambo mengine ya maana zaidi ya kufikiria kuliko mambo hayo madogo. Kuweza kutoa msaada kwa watu ambao ni maskini wa kiroho kwelikweli ni pendeleo linalopita uwezo wa kibinadamu kuweza kueleza.”
Wengi zaidi hushiriki maoni hayo, na roho hiyo ya kujidhabihu imechangia sana utimizo wa unabii wa Yesu kwamba habari njema za Ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa, kuwa ushahidi kwa mataifa yote, kabla ya mwisho kuja.—Mt. 24:14.
[Maelezo ya Chini]
a Mnara wa Mlinzi (Kiingereza), Februari 15, 1943, kur. 60-64.
[Blabu katika ukurasa wa 523]
Mkazo juu ya umaana wa kumtegemea Yehova kabisa na kuwa na uaminifu-mshikamanifu kwake
[Blabu katika ukurasa wa 534]
Uchesi ulisaidia
[Blabu katika ukurasa wa 539]
Saburi, msaada wenye upendo, na kuwa imara inapohitajika
[Blabu katika ukurasa wa 546]
‘Kutoa msaada kwa watu ambao ni maskini wa kiroho kwelikweli ni pendeleo linalopita uwezo wa kibinadamu kuweza kueleza’
[Sanduku katika ukurasa wa 533]
Madarasa ya Gileadi
1943-1960: Shule katika South Lansing, New York. Katika madarasa 35, wanafunzi 3,639 kutoka nchi 95 walihitimu, wengi wao wakipewa mgawo wa utumishi wa mishonari. Waangalizi wa mzunguko na wa wilaya waliotumikia katika Marekani walitiwa ndani pia katika madarasa hayo.
1961-1965: Shule katika Brooklyn, New York. Katika madarasa 5, wanafunzi 514 walihitimu na wakatumwa kwenye nchi ambako Watch Tower Society ilikuwa na ofisi za tawi; wahitimu wengi zaidi walikabidhiwa migawo ya usimamizi. Manne kati ya madarasa hayo yalikuwa na mitaala ya miezi 10; mmoja, mtaala wa miezi 8.
1965-1988: Shule katika Brooklyn, New York. Katika madarasa 45, kila darasa likiwa na mtaala wa majuma 20, wanafunzi wengine 2,198 walizoezwa, wengi wao kwa ajili ya utumishi wa mishonari.
1977-1980: Shule katika Brooklyn, New York. Mtaala wa Gileadi wa majuma matano kwa washiriki wa Halmashauri ya Tawi. Madarasa 14 yalifanywa.
1980-1981: Shule ya Uelimishaji ya Gileadi ya Mexico; mtaala wa majuma 10; madarasa matatu; wahitimu 72 wenye kusema Kihispania walijitayarisha kwa ajili ya utumishi katika Amerika ya Latini.
1981-1982, 1984, 1992: Shule Iliyopanuliwa ya Gileadi katika Ujerumani; mtaala wa majuma 10; madarasa manne; wanafunzi 98 wanaosema Kijerumani kutoka nchi za Ulaya.
1983: Madarasa katika India; mtaala wa majuma 10, yakiongozwa katika Kiingereza; vikundi 2; wanafunzi 46.
1987- : Shule ya Mazoezi ya Kihuduma, yenye mtaala wa majuma manane, hufanywa katika mahali pakuu katika sehemu mbalimbali za ulimwengu. Kufikia 1992, wahitimu walikuwa tayari wamekuwa wakitumikia katika nchi zaidi ya 35 nje ya nchi zao za uzawa.
1988- : Shule katika Wallkill, New York. Mtaala wa majuma 20 katika kujitayarisha kwa ajili ya utumishi wa mishonari kwa sasa huongozwa huko. Kuna mpango wa kuhamisha shule hiyo kuipeleka kwenye Watchtower Educational Center katika Patterson, New York, hiyo itakapokamilishwa.
[Sanduku katika ukurasa wa 538]
Baraza la Wanafunzi la Kimataifa
Wanafunzi ambao wamehudhuria Shule ya Gileadi wamewakilisha mataifa mengi na wamekuja shuleni kutoka nchi zaidi ya 110.
Kikundi cha kwanza cha kimataifa kilikuwa darasa la sita, katika 1945-1946.
Maombi yalifanywa kwa serikali ya Marekani ili wanafunzi wa kigeni waandikishwe chini ya uandalizi wa viza za mwanafunzi zisizo za kuhamia nchini. Katika kujibu, Ofisi ya Elimu ya Marekani iliitambua Shule ya Gileadi kuwa inatoa elimu inayolingana na ya koleji za kazi za ustadi na taasisi za elimu. Hivyo, tangu 1953, mabalozi wa Marekani kotekote ulimwenguni waliiweka Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower kwenye orodha yao ya taasisi za elimu zilizokubaliwa. Kufikia Aprili 30, 1954, shule hiyo ilitokea katika kichapo chenye kichwa “Educational Institutions Approved by the Attorney General.”
[Picha katika ukurasa wa 522]
Wanafunzi wa darasa la kwanza la Shule ya Gileadi
[Picha katika ukurasa wa 524]
Albert Schroeder akizungumza na wanafunzi wa Gileadi juu ya sehemu za tabenakulo
[Picha katika ukurasa wa 525]
Maxwell Friend akitoa mhadhara katika jumba la mihadhara la Shule ya Gileadi
[Picha katika ukurasa wa 526]
Sherehe za kuhitimu za Gileadi zilikuwa jambo kuu la kiroho
. . . nyingine kwenye mikusanyiko mikubwa (New York, 1950)
. . . nyingine kwenye chuo cha shule (ambapo N. H. Knorr anaonyeshwa akisema mbele ya maktaba ya shule, katika 1956)
[Picha katika ukurasa wa 527]
Uwanja na majengo ya Shule ya Gileadi katika South Lansing, New York, kama yalivyoonekana wakati wa miaka ya 1950
[Picha katika ukurasa wa 528]
Hermon Woodard (kushoto) na John Errichetti (kulia) wakitumikia katika Alaska
[Picha katika ukurasa wa 529]
John Cutforth akitumia michoro ili kufundisha katika Papua New Guinea
[Picha katika ukurasa wa 530]
Wamishonari katika Ireland, wakiwa na mwangalizi wa wilaya, katika 1950
[Picha katika ukurasa wa 530]
Wahitimu wakielekea kwenye migawo ya mishonari katika nchi za Mashariki katika 1947
[Picha katika ukurasa wa 530]
Baadhi ya wamishonari na wafanyakazi wenzi katika Japani mwaka 1969
[Picha katika ukurasa wa 530]
Wamishonari katika Brazili mwaka 1956
. . . katika Uruguai mwaka 1954
. . . katika Italia mwaka 1950
[Picha katika ukurasa wa 530]
Wamishonari wanne wa kwanza waliozoezwa Gileadi waliotumwa Jamaika
[Picha katika ukurasa wa 530]
Makao ya kwanza ya wamishonari katika Salisbury (sasa Harare, Zimbabwe), katika 1950
[Picha katika ukurasa wa 530]
Malcolm Vigo (Gileadi, 1956-1957 ) na mke wake Linda Louise; wakiwa pamoja wametumikia katika Malawi, Kenya, na Nigeria
[Picha katika ukurasa wa 530]
Robert Tracy (kushoto) na Jesse Cantwell (kulia) wakiwa na wake zao—wamishonari katika kazi ya kusafiri nchini Kolombia katika 1960
[Picha katika ukurasa wa 532]
Darasa la lugha katika makao ya wamishonari katika Côte d’Ivoire
[Picha katika ukurasa wa 535]
Ted na Doris Klein, waliopata watu wengi wenye hamu ya kusikia kweli ya Biblia katika Visiwa vya Virgin vya Marekani katika 1947
[Picha katika ukurasa wa 536]
Harvey Logan (mbele katikati) pamoja na Mashahidi Waamis mbele ya Jumba la Ufalme, katika miaka ya 1960
[Picha katika ukurasa wa 540]
Victor White, mwangalizi wa wilaya aliyezoezewa Gileadi, akihutubu katika Filipino katika 1949
[Picha katika ukurasa wa 542]
Margarita Königer, katika Burkina Faso, akiongoza funzo la Biblia nyumbani
[Picha katika ukurasa wa 543]
Unn Raunholm, mishonari tangu 1958, alilazimika kukabili magenge yaliyoongozwa na mapadri katika Ekuado
[Picha katika ukurasa wa 545]
Shule ya Mazoezi ya Kihuduma
Darasa la kwanza, Coraopolis, Pa., Marekani, katika 1987 (juu)
Darasa la tatu nchini Uingereza, katika Manchester, mwaka 1991 (kulia)