Wahudumu wa Wakati Wote Wanaiongoza Kazi
Inawezekana kwamba wa kwanza wa Mashahidi wa Yehova kukutembelea alikuwa mhudumu painia wa wakati wote au mmisionari. Kwa kuwa Mashahidi wa Yehova hawana huduma inayolipwa mshahara, labda umetaka kujua ni jinsi gani watu hao wangeweza kuingia huduma ya wakati wote.
Mashahidi wa Yehova wote walio wakfu na kubatizwa ni wahudumu, lakini idadi kubwa zaidi wana jamaa au madaraka mengine yanayowazuia wasitumie saa nyingi zaidi kila juma katika huduma yao. Hata hivyo, maelfu ya Mashahidi ulimwenguni pote wamepunguza kiwango chao cha kuishi ili walipie gharama zao ndogo kwa kufanya kazi ya saa chache kisha watumie saa 1,000 au zaidi kila mwaka katika huduma.
Ni kweli kwamba wahudumu mapainia wa wakati wote hawana fedha nyingi za kutumia wenyewe, lakini kwao hiyo ni njia ya kutafuta kwanza Ufalme wa Mungu. Nao wanapokea baraka nyingi. Kule tu kuweza kuwaambia wengine juu ya Neno la Mungu kwa kutumia saa 90 hivi kila mwezi ni jambo zuri. Mhudumu wa wakati wote anafanya ustadi wake katika huduma uwe bora na pia ana wakati wa kurudia wanaopendezwa kwa njia inayofaa. Hiyo inafanyiza matokeo yenye kutia moyo sana. Mahitaji ya kimwili yanatimizwa, nao pia wanathamini sana vitu walivyo navyo. —Mathayo 6:33.
Katika Februari 1943, Watch Tower Society ilianzisha Shule ya Biblia ya Gileadi. Kusudi lake lilikuwa ni kuzoeza wahudumu mapainia wa wakati wote na wenye ujuzi watumikie wakiwa wamisionari katika nchi za kigeni. Ule mtaala wa miezi mitano una funzo lenye mambo mengi ya Biblia, historia ya Biblia, tengenezo la Yehova, na masomo yanayohusiana na hayo katika kuwatayarisha kwa ajili ya utumishi katika shamba la kigeni.
Sosaiti inalipa nauli ya kusafiri kwenda kwenye mgawo wa misionari na inatoa vyakula bora na makao ya kiasi katika nyumba za Wamisionari. Pia inampa kila mmisionari alawansi ndogo ya gharama za kibinafsi. Wamisionari wanachukua zamu ya kuendesha nyumba kwa kununua vitu, kupika vyakula, na kusafisha nyumba. Wakiwa na uangalifu huo wa kiasi wamisionari wanaweza kutumia angalau saa 140 kila mwezi wakihubiri nyumba kwa nyumba na kuongoza mafunzo ya Biblia pamoja na watu wanaopendezwa.
Wengi wa wamisionari hao wanapewa migawo maelfu ya kilometa mbali na kwao na jamaa yao. Imewapasa wajirekebishe ili wafuate kiwango cha kuishi kilicho tofauti na utamaduni ulio tofauti, mazoea mapya ya kula, hali ya hewa iliyo tofauti, na kusema lugha nyingine. Wanafanya kazi hiyo kwa sababu wanapenda watu na wanatamani sana kuwasaidia wajifunze juu ya Ufalme wa Mungu.
Tangu mwaka 1943 mpaka 1985, Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower imeongoza madarasa 80 na imetuma wamisionari zaidi ya 6,000. Chini ya usimamizi wa Sosaiti, hao wameongoza mpanuo wa elimu ya Biblia katika sehemu zote za Afrika, Amerika ya Kati na Kusini, nchi za Mashariki, na Pasifiki ya Kusini, nao wametimiza mengi katika Ulaya.
Wawe Mashahidi wa Yehova, wanaishiriki huduma ama kwa wakati wote wakiwa mapainia au wamisionari, ama si kwa wakati wote, wao wanatumikia bila faida ya kifedha. Wanatumia wakati wao wenyewe na fedha zao wenyewe, na kujitumikisha wenyewe, wawasaidie wengine wayapate maarifa yanayoongoza kwenye uzima wa milele. —Yohana 17:3.
• Wengine kati ya Mashahidi wa Yehova wanawezaje kuwa wahudumu wa wakati wote, na ni kwa sababu gani wanafanya hivyo?
• Wahudumu wanazoezwaje wafanye kazi ya misionari?
• Wamisionari wanaruzukwaje katika mgawo wao wa misionari?
[Picha katika ukurasa wa 22]
Kushoto: Chumba cha darasa la Shule ya Gileadi, Brooklyn, N.Y., U.S.A.
Kulia: Mmisionari anafundisha Neno la Mungu katika Papua New Guinea
[Picha katika ukurasa wa 23]
Mapainia wahudumu na wamisionari wanahubiri Neno la Mungu katika nchi mbalimbali
Brazili
Jamhuri ya Dominika
Hispania
Sierra Leone, Afrika