JINSI MICHANGO YAKO INAVYOTUMIWA
Wamishonari “Mpaka Sehemu ya Mbali Zaidi ya Dunia”
JUNI 1, 2021
Yesu aliwaambia wanafunzi wake: “Mtakuwa mashahidi wangu . . . mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Matendo 1:8) Leo, Mashahidi wa Yehova wanatimiza utume huo kwa bidii. Hata hivyo, sehemu fulani za dunia, kutia ndani maeneo fulani makubwa na yaliyo na watu wengi bado hayajahubiriwa kikamili. Na nchi fulani zina Mashahidi wachache tu. (Mathayo 9:37, 38) Tunafanya nini ili kuwafikia watu wengi kadiri iwezekanavyo?
Ili kutekeleza amri ya Yesu, Halmashauri ya Utumishi ya Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova huwatuma wamishonari walio shambani kwenda maeneo yenye uhitaji mkubwa ulimwenguni pote. Kwa sasa, kuna wamishonari 3,090 hivi walio shambani ulimwenguni pote.a Wengi wao wamepata mazoezi katika shule ya Biblia kama vile Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme. Wamishonari wako tayari kuondoka nyumbani na kuhamia nchi nyingine. Kwa sababu ya ukomavu, mazoezi na uzoefu wao, wamishonari hao waaminifu husaidia kueneza habari njema na wamewawekea wanafunzi wapya mfano mzuri.
Wamishonari husaidia kuhubiri habari njema katika maeneo yaliyo na uhitaji mkubwa wa Mashahidi
Kuwasaidia Wamishonari Wawasaidie Wengine
Katika kila ofisi ya tawi, Idara ya Wahudumu Walio Shambani katika Idara ya Utumishi hufanya kazi pamoja na Halmashauri ya Tawi ili kushughulikia mahitaji ya wamishonari kama vile kuandaa makazi, matibabu, na posho ndogo. Katika mwaka wa utumishi wa 2020, Mashahidi wa Yehova walitumia dola milioni 27 hivi (za Marekani) ili kuwatunza wamishonari. Kwa sababu ya maandalizi haya wamishonari wanaweza kukazia fikira na kutumia nguvu zao zote kwenye huduma na pia kuimarisha kutaniko lao.
Wamishonari husaidia kuimarisha makutaniko
Wamishonari walio shambani wameleta matokeo gani katika kazi ya kuhubiri? Frank Madsen anayetumikia katika Halmashauri ya Tawi ya Malawi anasema hivi: “Kwa sababu ya ujasiri na ustadi wao, wamishonari wamesaidia makutaniko kushughulikia maeneo magumu kama vile nyumba zenye ulinzi mkali na maeneo ya lugha ya kigeni. Na pia, kwa sababu ya jitihada zao za kujifunza lugha na tamaduni za nchi hii, wamewasaidia vijana wengi kufikiria kuanza utumishi wa wakati wote. Tunamshukuru Yehova kwa wamishonari walio shambani.”
Mshiriki wa Halmashauri ya Tawi katika nchi nyingine anasema hivi: “Wamishonari wanathibitisha kwamba watu wa Yehova wana umoja ulimwenguni pote. Hata watu ambao si Mashahidi wanaona waziwazi kwamba hatujatenganishwa na tamaduni lakini mafundisho ya Biblia yametusaidia kuwa na umoja ulimwenguni pote.”
Wamishonari walio shambani wanawasaidiaje wahubiri? Paulo, anayeishi Timor-Leste, anathamini kuwa na wamishonari katika kutaniko lao. Anasema hivi: “Eneo letu lina joto kali sana. Ingawa wamishonari wanatoka sehemu yenye baridi kali, hawaruhusu hali ya hewa iwazuie kuhubiri. Siku zote wanakuwa kwenye mikutano ya utumishi wa shambani asubuhi. Mara nyingi ninawaona wakifanya ziara za kurudia mchana, wakati kuna joto sana, na pia jioni. Wamewasaidia watu wengi kujifunza, kutia ndani mimi. Kwa bidii na shauku, wanatumia maisha yao yote kumtumikia Yehova na hilo hulichochea kutaniko lote kumtumikia kwa bidii zaidi.”
Ketti, ambaye ni painia wa kawaida nchini Malawi anaeleza jinsi wenzi wa ndoa ambao ni wamishonari walivyoisaidia familia yake: “Wenzi wa ndoa ambao ni wamishonari walipotumwa katika kutaniko letu, ni mimi tu niliyekuwa Shahidi katika familia yangu. Lakini wenzi hao walinisaidia sana, na wakawa na uhusiano wa karibu sana na familia yetu. Mfano wao mzuri uliwasaidia watoto wangu kuona kwamba kumtumikia Yehova kunaweza kuwaletea maisha yenye furaha na yenye kuridhisha. Kwa sababu ya mfano mzuri wa wamishonari hao, binti zangu watatu sasa wanatumikia wakiwa mapainia wa kawaida na mume wangu ameanza kuhudhuria mikutano.”
Gharama za kuwatunza wamishonari walio shambani zinashughulikiwaje? Kupitia michango kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote ambayo sehemu kubwa hutolewa kupitia mbinu zilizoonyeshwa kwenye donate.jw.org. Michango hiyo ya ukarimu inathaminiwa sana.
a Wamishonari hao wanatumwa kwenye makutaniko ambapo kuna uhitaji katika kazi ya kuhubiri. Wamishonari wengine 1,001 walio shambani hutumikia wakiwa waangalizi wa mzunguko.