Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g94 12/22 kur. 21-24
  • Kufanya Wanafunzi wa Kweli Leo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kufanya Wanafunzi wa Kweli Leo
  • Amkeni!—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Aina Maalumu ya Shule
  • Wamishonari wa Namna Tofauti-Tofauti
  • Matunda Yamekuwa Nini?
  • Wamishonari Wasukuma Mpanuko wa Ulimwenguni Pote
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Wamishonari “Mpaka Sehemu ya Mbali Zaidi ya Dunia”
    Jinsi Michango Yako Inavyotumiwa
  • Wamishonari—Wapaswa Kuwa Nini?
    Amkeni!—1994
  • Wamishonari wa Jumuiya ya Wakristo
    Amkeni!—1994
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1994
g94 12/22 kur. 21-24

Wamishonari Mawakili wa Nuru au wa Giza?—Sehemu 6

Kufanya Wanafunzi wa Kweli Leo

YESU KRISTO aliamuru hivi: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza.” (Mathayo 28:19, NW) Everyman’s Encyclopedia yasema kwamba utume huu ‘umetekelezwa na Wakristo katika kila muhula,’ ingawa yaongezea, ‘nyakati fulani kwa nguvu kidogo tu.’ Kitabu The Missionary Myth chauliza hivi: “Je, muhula wa kimishonari umekwisha?”

Katika Januari wa mwaka huu, gazeti Newsweek liliripoti hivi: “Papa John Paul 2 anaupeleka Ukatoliki wa Kiroma barabarani.” Gazeti hilo lilieleza hivi: “Anatuma waeneza-evanjeli 350 wasio makasisi kwenda kutafuta-tafuta waongofu katika madisko ya Roma, masoko makuu ya miji na vituo vya magari-moshi chini ya ardhi. Programu ya kwanza yaanza Jumatano ya Majivu (Feb. 16). Ikifaulu, pontifu huyo atafanya hivyo tufeni pote—hatua ambayo ingeweza kufanya wamishonari Wakatoliki wawe wakibisha hodi milangoni kuanzia Buenos Aires hadi Tokyo.”

Mashahidi wa Yehova, kwa upande ule mwingine, wameelewa tangu zamani wajibu wao wa kufanya kazi ya kueneza evanjeli. (2 Timotheo 4:5) Bila shaka, sio wote wahubirio wakiwa wamishonari katika nchi za kigeni. Lakini wao waweza—nao hufanya—kuhubiri mahali popote walipo. Katika maana hii, wote hao ni wamishonari.

Aina Maalumu ya Shule

Katika miaka ya mapema ya 1940, Watch Tower Society ilianzisha shule ya kuzoeza wahudumu wenye ujuzi watumikie wakiwa wamishonari katika mabara ya kigeni ambako msaada ulihitajiwa hima. Muda wa miaka iliyopita mtaala umerekebishwa, lakini haujatoka kamwe kwenye mradi wao wa msingi wa kukazia funzo la Biblia na kutimiza ile kazi muhimu ya kueneza evanjeli.

Jina lililochaguliwa kwa ile shule mpya lilikuwa Gileadi, ambalo kwa Kiebrania humaanisha “Rundo la Ushahidi.” Kwa kusaidia kurundika rundo la ushahidi kwa heshima ya Yehova, Gileadi imetimiza fungu muhimu sana katika kutekeleza ile kazi ya kuhubiri tufeni pote aliyotabiri Yesu kuwa ingetendeka katika siku yetu.—Mathayo 24:14.

Akihutubia darasa la kwanza la Shule ya Gileadi katika 1943, Nathan H. Knorr, msimamizi wa wakati huo wa Watch Tower Society, alisema hivi: “Nyinyi mnapewa tayarisho zaidi kwa ajili ya kazi iliyo kama ile ya mtume Paulo, Marko, Timotheo, na wengine waliosafiri kwenye sehemu zote za Milki ya Kiroma wakipiga mbiu ya ujumbe wa Ufalme. . . . Kazi yenu kuu ni ile ya kuhubiri ile gospeli ya Ufalme nyumba kwa nyumba kama walivyofanya Yesu na mitume.”

Wakati darasa la kwanza lilipokuwa limemaliza mazoezi yalo, wahitimu walo walitumwa kwenye nchi tisa za Amerika ya Kilatini. Kufikia sasa, zaidi ya wanafunzi 6,500 kutoka zaidi ya nchi 110 wamezoezwa kwenye Shule ya Gileadi na wametumwa wakiwa wamishonari kwenye mabara na vikundi vya visiwa ambavyo ni zaidi ya 200.

Wamishonari wa Namna Tofauti-Tofauti

Makala zilizotangulia katika mfululizo huu zilisimulia juu ya utendaji wa wamishonari wa Jumuiya ya Wakristo wa wakati uliopita. Wengi, kama wale waliotumwa Greenland, waliitafsiri Biblia au sehemu zayo katika lugha ya kienyeji. Hata hivyo, wamishonari hao wa mapema mara nyingi walikuwa na mapendezi mengine yasiyo ya kufundisha watu Biblia.

Kwa kielelezo, wamishonari wa Jumuiya ya Wakristo walioenda Japani walihusika katika “taasisi na shule za kielimu,” yaandika Kodansha Encyclopedia of Japan. Yasema hivi: “Wamishonari kadhaa wamejipambanua wenyewe kupitia usomi wao.” Walipata kuwa wanaisimu au maprofesa, wakifundisha masomo kama fasihi, lugha, historia, falsafa, dini za Asia Mashariki, na hekaya za Kijapani. “Taasisi za ufadhili na za kijamii zilikuwa pia sehemu ya maana ya kazi ya kimishonari,” yaongezea ensaiklopedia hiyo.

Kuihubiri gospeli hakukutangulizwa na wamishonari kwa jumla kuwe jambo la kwanza kabisa. Mara nyingi mno walikazia kutosheleza mahitaji ya kimwili badala ya mahitaji ya kiroho. Ufuatiaji wa mapendezi ya kibinafsi ndio uliokaziwa sana nao. Hivyo, mishonari mmoja wa Kanisa la Uingereza aliyetumwa Japani katika 1889 leo ajulikana zaidi kuwa “baba wa upandaji-milima wa Kijapani.”

Wamishonari waliozoezwa Gileadi watofautiana na wale wa Jumuiya ya Wakristo kwa njia zilizo kubwa. Kitabu Jehovah’s Witnesses—Proclaimers of God’s Kingdom, sura 23, chatoa maoni haya: “Wahitimu wamishonari wa Shule ya Gileadi hufundisha watu Biblia. Badala ya kujenga makanisa na kutazamia watu waje kwao, wao huenda nyumba hadi nyumba . . . , si ili watumikiwe, bali watumikie.”

Matunda Yamekuwa Nini?

Baada ya kuwa na karne za wakati wa kufanya wanafunzi Wakristo katika Ulaya, wamishonari wa Jumuiya ya Wakristo wamefanikiwa kadiri gani? Kitabu A Global View of Christian Missions chajibu hivi: “Watu wakadiriwao kuwa milioni 160 katika Ulaya hawadai kuwa wa dini yoyote. Miongoni mwa wale ambao bado hudai kushikamana na Ukristo mna wachache wachukuao dini yao kwa uzito. . . . Ulaya haiwezi kamwe kuwaziwa kuitwa kontinenti ya Kikristo.”

Namna gani hali katika Asia? Kodansha Encyclopedia of Japan yajibu hivi: “Kwa kadirio la watu wengi Ukristo ungali wachukuliwa kuwa imani ‘ya kigeni,’ . . . isiyowafaa Wajapani wa kawaida. . . . Harakati ya Kikristo yabaki ikiwa nje ya mipaka ya jamii ya Wajapani.” Kwa kweli, chini ya asilimia 4 ya watu katika Japani ni wenye kudai kuwa Wakristo, katika India ni chini ya asilimia 3, katika Pakistan ni chini ya asilimia 2, na katika China ni chini ya asilimia 0.5.

Baada ya karne za utendaji wa kimishonari wa Jumuiya ya Wakristo katika Afrika, hali ikoje huko? Katika ripoti moja juu ya mkutano wa maaskofu wa Kiafrika uliofanywa masika haya katika Roma, gazeti la Kijerumani Focus liliripoti hivi: “Dini za Kiafrika hazipasi kulaumiwa tena kuwa ibada-sanamu ya kipagani. Hati rasmi, isiyochapishwa bado, huweka ‘dini za mapokeo za Kiafrika’ katika kiwango cha wenzi walio wastahiki na wa muhimu. Washirika wao wastahili staha. Ule mkutano wa maaskofu ulikubali kwamba dini zilizokuwa zikilaumiwa hapo kwanza kuwa za kihirizi ‘ndizo mara nyingi zimeamulia hata Mkatoliki aliye msadikifu zaidi ni mtindo-maisha gani wa kufuata.’”a

Baada ya kuwa na karne za wakati wa kufanya wanafunzi wa Kikristo katika zile Amerika, wamishonari wa Jumuiya ya Wakristo wamefanikiwa kadiri gani? Kitabu Mission to the World chajibu hivi: “‘Amerika ya Kilatini’ bado yastahili kuitwa ‘ile kontinenti iliyopuuzwa’ kujapokuwa na hatua kubwa ya kusonga mbele kwa utendaji wa kimishonari katika miongo ya majuzi.” Kuhusu Marekani, Newsweek laandika kwamba machunguzi ya majuzi “yaonyesha kwamba ingawa dini imeienea mandhari ya Kimarekani, ni wachache tu waichukuayo kwa uzito. . . . Nusu ya watu wawaambiao watafuta-maoni kwamba wao hushinda kanisani siku za Jumapili hawasemi kweli. . . . Karibu theluthi moja ya Wamarekani wa miaka 18 na zaidi wana maoni ya kilimwengu kabisa . . . Ni asilimia 19 tu . . . wenye mazoea ya kufuata dini yao kwa ukawaida.”

Kwa muhtasari, katika jitihada zao za kupunguza matatizo ya umaskini, afya mbaya, na ukosefu wa elimu, wamishonari wa Jumuiya ya Wakristo, wakiwa kikundi, wameendeleza miradi ya kibinadamu ambayo kadiri kubwa zaidi ya msaada wayo imekuwa ni kupunguza shida za watu kwa muda tu tena kwa sehemu. Kwa upande ule mwingine, wamishonari wa kweli wa Kikristo huelekeza watu kwenye Ufalme wa Mungu uliosimamishwa, utakaoleta ondoleo kamili la shida tena la kudumu. Hautatuliza matatizo tu; utayatatua. Ndiyo, Ufalme wa Mungu utaletea jamii ya kibinadamu afya kamili, usalama halisi wa kiuchumi, fursa zisizoisha za kazi yenye matokeo mazuri kwa wote, na uhai usio na mwisho!—Zaburi 37:9-11, 29; Isaya 33:24; 35:5, 6; 65:21-23; Ufunuo 21:3, 4.

Wamishonari wa Jumuiya ya Wakristo huenda wakaelekeza kidole kwa watu wadaio kuwa Wakristo ambao pindi kwa pindi huhudhuria ibada za kidini kuhakikisha kwamba wao wamefanya ‘wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, wakiwabatiza.’ Lakini mambo ya hakika yaonyesha kwamba wamishonari hawa wameshindwa kuwafundisha wabatizwa hawa ‘kushika mambo yote ambayo Yesu ameamuru.’—Mathayo 28:19, 20.

Hata hivyo, utendaji wa kufundisha wa Wakristo wa kweli utaendelea mpaka ndani ya ulimwengu mpya wa Mungu. Utasambaa ukafikie mamilioni ya wafufuliwa watakaohitaji mafundisho katika njia za Mungu. Ndipo, pasipo na mwingilio wa kishetani, Wakristo watakuwa na lile pendeleo la kupendeza sana la kuendelea kufanya wanafunzi—sawasawa na vile wamekuwa wakifanya kwa miongo.

[Maelezo ya Chini]

a Ona makala “Kanisa Katoliki Katika Afrika,” katika ukurasa 18.

[Sanduku katika ukurasa wa 24]

Jinsi Wao Wamesaidia Watu

Yanayofuata ni maelezo yaliyotolewa na wale ambao wamenufaika na msaada wa wamishonari waliozoezwa Gileadi.

“Mimi nilistaajabishwa na ushikamano wao, kuchukuliana na mambo mengi sana yaliyotofautiana na bara la kwao: tabia-anga, lugha, desturi, chakula, na dini. Lakini walibaki katika migawo yao, wengine hadi hata kifo. Mazoea yao mema ya kujifunza na bidii katika huduma zilinisaidia kusitawisha mambo hayohayo.”—J. A., India.

“Mimi nilivutiwa na kuwahi kwa yule mishonari alipokuwa akijifunza nami. Mwanamume huyo alionyesha kujidhibiti kwa ajabu katika kuchukuliana na maoni yangu ya kibaguzi na ya kukosa ujuzi.”—P. T., Thailand.

“Mke wangu nami tulithamini utakato ulioonyeshwa na wamishonari Mashahidi. Utendaji wao ulituvuta kufanya utumishi wa wakati wote uwe mradi wetu, na leo sisi tuna ile shangwe ya kuwa wamishonari sisi wenyewe.”—A. C., Msumbiji.

“Maisha yangu yalikuwa yamekuwa ya kujifikiria mwenyewe tu. Kukutana na wamishonari hao kuliandaa kichocheo nilichohitaji ili kubadilika. Niliona ndani yao si furaha ya kijuujuu tu bali ya kweli.”—J. K., Japani.

“Wamishonari wa Jumuiya ya Wakristo waliishi maisha za starehe. Watumishi waliisafisha nyumba, wakapika, wakazifua nguo, wakaitunza bustani, na kuliendesha gari. Mimi nilishangaa kuona wamishonari wa Gileadi wakijifanyia kazi yao ya nyumbani kwa uzuri, huku pia wakisaidia wenyeji kujifunza juu ya Ufalme wa Mungu.”—S. D., Thailand.

“Akina dada wamishonari waliendesha baiskeli kuwazuru watu hata halijoto ilipoongezeka kuwa zaidi ya digrii 46 Selsiasi. Ukaribishaji-wageni na kutopendelea kwao, na pia uvumilivu wao, ulinisaidia kuitambua kweli.”—V. H., India.

“Wamishonari hao hawakujihisi kuwa wakuu zaidi. Walijirekebisha kwa unyenyekevu kulingana na wenyeji na hali za maisha ya kimaskini. Walikuwa wamekuja kutumikia, kwa hiyo hawakulalamika kamwe bali sikuzote walionekana wenye shangwe na kuridhika.”—C. P., Thailand.

“Wao hawakutohoa kweli ya Biblia. Hata hivyo, hawakufanya wenyeji wahisi kwamba mambo yote ya utamaduni wao wa kimapokeo yalikuwa makosa wala kwamba ilikuwa lazima wakubali kufuata njia za Magharibi. Wao hawakufanya kamwe wengine wahisi kuwa wa cheo cha chini wala wasio watoshelevu.”—A. D., Papua New Guinea.

“Tofauti na wamishonari wa Jumuiya ya Wakristo, mwanamke huyo alikuwa tayari kukalia sakafu kwa kukingamanisha miguu, mtindo wa Korea, tulipokuwa tukifanya funzo letu la Biblia. Alikuwa tayari kuyaonja maakuli yetu ya Kikorea. Shauku niliyohisi kwake ilinisaidia kufanya maendeleo.”—S. K., Korea.

“Mimi nilikuwa na miaka kumi na nilitoka shuleni adhuhuri. Mishonari mmoja alinialika niandamane naye nyakati za alasiri katika huduma ya shambani. Alinifundisha kanuni nyingi za Biblia na kukazia ndani yangu uthamini halisi kwa tengenezo la Yehova.”—R. G., Kolombia.

“Wao walinifundisha kushikamana na migawo, kufanya lililohitaji kufanywa bila kulalamika. Nashukuru Yehova na Yesu Kristo kwa ukunjufu wa moyo wangu wote kwa kutupelekea wamishonari hao.”—K. S., Japani.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Wamishonari waliozoezwa Gileadi kutoka nchi 16 wasimulia mambo yaliyoonwa kwenye mkusanyiko mmoja wa majuziy

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki