Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • jv sura 22 kur. 462-501
  • Sehemu ya 4—Kuwa Mashahidi Hadi Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya Dunia

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Sehemu ya 4—Kuwa Mashahidi Hadi Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya Dunia
  • Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Wamishonari Wazidisha Ushahidi Katika Indies Magharibi
  • Kutoa Ushahidi Kwanza Katika Majiji Makubwa Zaidi
  • Kutafuta Sana kwa Saburi Wenye Mfano wa Kondoo
  • Kuendeleza Elimu kwa Ajili ya Uhai
  • Kukusanyika Pamoja Chini ya Magumu
  • Kutumikia Sehemu Zenye Uhitaji Mkubwa Zaidi
  • Kujitahidi Kufikia Visiwa vya Pasifiki
  • Ujapokuwa Mkazo wa Familia na Jamii
  • Wakati Kunapokuwa na Upinzani Mwingi wa Makasisi
  • Bubujiko la Maji ya Ile Kweli Barani Afrika
  • Wakati Vizuizi Vilipotokezwa
  • Wanafunzi Waelewao Kikweli
  • Kuliweza Tatizo la Kutojua Kusoma na Kuandika
  • Kufundisha kwa Njia ya Sinema na Maonyesho ya Slaidi
  • Kuwatambua Kondoo wa Kweli
  • Kuvunja Nguvu za Hirizi
  • Wafanyakazi Zaidi Washiriki Katika Mavuno
  • Kutoa Ushahidi kwa Magavana na Wafalme
  • Nchi za Mashariki Yatoa Wasifaji wa Yehova
  • Hali Ilikuwaje Katika Ulaya?
  • Mikusanyiko Ilichangia Kutoa Ushahidi
  • Watu Wasemapo Lugha Nyingine
  • Mavuno Mengi Kujapokuwa Vizuizi
  • Fikira Kwenye Maeneo Yasiyogawiwa Mtu
  • Sehemu ya 5—Kuwa Mashahidi Hadi Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya Dunia
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Sehemu ya 2—Kuwa Mashahidi Hadi Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya Dunia
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Wamishonari Wasukuma Mpanuko wa Ulimwenguni Pote
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Sehemu ya 3—Kuwa Mashahidi Hadi Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya Dunia
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
Pata Habari Zaidi
Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
jv sura 22 kur. 462-501

Sura ya 22

Sehemu ya 4—Kuwa Mashahidi Hadi Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya Dunia

Wakati Vita ya Ulimwengu 2 ilipokuwa ingali inaendelea, Mashahidi wa Yehova walikuwa wakifanya mipango ya kuzidisha utendaji wa wakati wa baada ya vita. Ile ripoti kwenye kurasa 462 hadi 501 huonyesha mambo mengi madogomadogo yenye kusisimua kati ya yale yaliyotukia hasa tokea 1945 hadi 1975 walipokuwa wakiongezeka idadi, wakifikia nchi nyingi zaidi, na kushiriki katika kuhubiri na kufundisha Neno la Mungu kwa njia kamili zaidi ya ilivyopata kuwa katika wakati wowote uliotangulia.

VISIWA vingi vya Indies Magharibi vilikuwa vimefikiwa kwa njia fulani kwa ujumbe wa Ufalme kufikia 1945. Lakini ushahidi kamili zaidi ulihitaji kutolewa. Wamishonari waliozoezwa kwenye Shule ya Gileadi wangetimiza fungu la maana.

Wamishonari Wazidisha Ushahidi Katika Indies Magharibi

Kufikia 1960 wamishonari hao walikuwa wametumikia katika visiwa au vikundi vya visiwa 27 katika Karibea. Nusu ya sehemu hizo hazikuwa na kutaniko la Mashahidi wa Yehova wakati wamishonari walipowasili. Wamishonari walianza na wakaendelea kuongoza mafunzo ya Biblia nyumbani pamoja na watu wenye kupendezwa, na wakapanga mikutano ifanywe kwa ukawaida. Mahali ambako tayari kulikuwa makutaniko, walitoa mazoezi muhimu kwa wahubiri wenyeji. Kama tokeo, kulikuwa na maendeleo katika ubora wa mikutano na mafanikio katika huduma.

Wale Wanafunzi wa Biblia wa mapema walikuwa wametoa ushahidi katika Trinidad tangu kabla ya Vita ya Ulimwengu 1, lakini kufuatia kuwasili kwa wamishonari kutoka Gileadi katika 1946, kazi ya kuongoza mafunzo ya Biblia nyumbani na watu wenye kupendezwa ilipewa nguvu mpya. Katika Jamaika kazi ya kuhubiri habari njema ilikuwa imeanza muda wa karibu nusu karne, na kulikuwa Mashahidi wenyeji elfu moja kufikia wakati wamishonari wa kwanza walipowasili; lakini walifurahi kusaidiwa kufikia watu wenye elimu zaidi, hasa katika sehemu za viunga kuzunguka jiji kuu. Kwa upande mwingine, katika Aruba kazi nyingi ya kutoa ushahidi ilikuwa tayari imefanywa katika jamii ya wenye kusema Kiingereza, hivyo wamishonari walielekeza fikira zao kwa wenyeji. Kila mtu alihitaji kusikia habari njema.

Ili kuhakikisha kwamba watu katika visiwa vyote katika sehemu hiyo ya dunia walikuwa na fursa ya kusikia juu ya Ufalme wa Mungu, katika 1948 Watch Tower Society ilitayarisha ile mashua Sibia yenye urefu wa meta 18 kuwa makao ya wamishonari yenye kuelea. Kikundi cha wafanyakazi kilipewa mgawo kupeleka ujumbe wa Ufalme kwenye kila kisiwa cha Indies Magharibi ambacho hakikuwa na yeyote akifanya kazi ya kuhubiri habari njema. Gust Maki alikuwa ndiye kapteni, na waliokuwa pamoja naye ni Stanley Carter, Ronald Parkin, na Arthur Worsley. Walianza na Visiwa Out vya kikundi cha Bahamas, kisha wakafanya kazi kuelekea kusini-mashariki kupitia Visiwa vya Leeward na Visiwa vya Windward. Ziara zao zilikuwa na matokeo gani? Katika St. Maarten mfanyabiashara mmoja aliwaambia hivi: “Watu hawakuzoea kamwe kuongea juu ya Biblia, lakini tangu mwe hapa kila mtu anaongea juu ya Biblia.” Baadaye, mahali pa Sibia palichukuliwa na mashua kubwa zaidi, Light. Pia kulikuwa badiliko katika wafanyakazi. Katika muda wa mwongo mmoja kazi hiyo ya pekee iliyokuwa ikifanywa kwa kutumia mashua hizo ikawa imekamilishwa, nao wapiga-mbiu wa habari njema wakaao kwenye nchi kavu walikuwa wakifuatia kupendezwa.

Kutoa Ushahidi Kwanza Katika Majiji Makubwa Zaidi

Kama ilivyokuwa katika Indies Magharibi, ndivyo na Amerika ya Kati na ya Kusini, tayari kulikuwa watu katika sehemu nyingi waliokuwa na baadhi ya vitabu vya Watch Tower Society kabla ya kuwasili kwa wamishonari kutoka Shule ya Gileadi. Hata hivyo, ili kufikia kila mtu kwa habari njema na kusaidia wenye moyo mweupe wawe wanafunzi wa kweli, mpango mzuri zaidi wa kitengenezo ulihitajiwa.

Kufikia wakati vita ya ulimwengu ya pili ilipoisha katika 1945, kulikuwa na mamia ya Mashahidi wa Yehova katika Argentina na Brazili; kama elfu tatu katika Mexico; makutaniko machache madogo sana katika Guiana ya Uingereza (sasa Guyana), Chile, Guiana ya Uholanzi (sasa Suriname), Paraguai, na Uruguai; na kikundi kidogo cha wahubiri katika Kolombia, Guatemala, na Venezuela. Lakini kuhusu Bolivia, Ekuado, El Salvador, Honduras, na Nikaragua, utendaji wa Mashahidi wa Yehova haukuanzishwa kwa msingi wowote wa kudumu hadi wamishonari waliozoezwa Shule ya Gileadi walipowasili.

Mwanzoni wamishonari walielekeza fikira za pekee kwenye ile miji mikubwa. Inastahili kuangaliwa kwamba katika karne ya kwanza, mtume Paulo alifanya kazi yake nyingi ya kuhubiri katika miji iliyokuwa kwenye njia kuu za usafiri katika Asia Ndogo na katika Ugiriki. Katika Korintho, mmojawapo miji mashuhuri zaidi ya Ugiriki ya kale, Paulo alitumia miezi 18 akifundisha Neno la Mungu. (Mdo. 18:1-11) Katika Efeso, njia panda ya usafiri na biashara katika ulimwengu wa kale, alipiga mbiu ya Ufalme wa Mungu kwa zaidi ya miaka miwili.—Mdo. 19:8-10; 20:31.

Kwa njia inayofanana na hiyo, wakati Edward Michalec na Harold Morris, wamishonari wahitimu wa Shule ya Gileadi, walipowasili katika Bolivia katika 1945, hawakutafuta mahali penye hali ya hewa yenye kufaa zaidi. Badala ya hivyo, walielekeza fikira zao kwanza katika La Paz, jiji kuu, ambalo liko katika milima ya Andes kwenye mwinuko wa karibu meta 3,700. Inataka jitihada kwa wageni kupanda zile barabara zenye kuinuka kwenye mwinuko huo; mara nyingi mioyo yao ilipigapiga kwa nguvu sana. Lakini wamishonari hao walipata watu wengi wenye kupendezwa na ujumbe wa Biblia. Humo katika jiji kuu, lilikuwa jambo la kawaida kwao kuambiwa: “Mimi ni wa Roma Katoliki ya kimitume, lakini mimi sipendi mapadri.” Katika muda wa miezi miwili tu, wamishonari hao wawili walikuwa wakiongoza mafunzo ya Biblia nyumbani 41.

Wakati wa mwongo uliofuata, kadiri wamishonari zaidi walivyowasili na idadi ya Mashahidi wenyeji ikakua, fikira zilielekezwa kwenye miji mingine ya Bolivia: Cochabamba, Oruro, Santa Cruz, Sucre, Potosí, na Tarija. Baada ya hapo, fikira zaidi zingeelekezwa kwenye miji na majiji madogo zaidi na maeneo ya mashambani pia.

Vivyo hivyo, katika Kolombia wamishonari walianza kupanga kitengenezo kazi ya kuhubiri katika jiji kuu, Bogotá, katika 1945, na katika jiji la pwani la Barranquilla mwaka uliofuata. Baada ya hapo, hatua kwa hatua fikira zilielekezwa Cartagena, Santa Marta, Cali, na Medellín. Watu wengi zaidi wangeweza kufikiwa kwa kipindi kifupi kwa kufanya kazi katika miji mikubwa kwanza. Kwa msaada wa wale waliojifunza kweli humo, ujumbe ungeweza kupelekwa upesi kwenye maeneo yanayozunguka.

Ikiwa ni kupendezwa kidogo sana kulikoonyeshwa katika jiji, wamishonari walihamishiwa mahali pengine. Hivyo, katika Ekuado, wakati miaka mitatu ya kazi katika miaka ya katikati ya 1950 haikuwa imetokeza hata mtu mmoja aliyekuwa na ujasiri wa kuchukua msimamo kwa ajili ya kweli katika Cuenca yenye watu wenye kushikilia dini kishupavu, Carl Dochow alihamishwa akaenda Machala, jiji lenye watu wenye uvumilivu, na wenye akili zilizofunguka. Hata hivyo, kama mwongo mmoja baadaye, watu katika Cuenca walipewa fursa nyingine. Roho tofauti ilipatikana, vizuizi vilishindwa, na kufikia 1992 katika Cuenca, watu zaidi ya 1,200 walikuwa wamekuwa Mashahidi wa Yehova na walikuwa wamepangwa kitengenezo katika makutaniko 25!

Kutafuta Sana kwa Saburi Wenye Mfano wa Kondoo

Saburi nyingi imetakwa ili kutafuta sana watu wenye mfano wa kondoo kikweli. Ili kuwapata katika Suriname, Mashahidi wa Yehova wamehubiria Wahindi wa Amerika, Wachina, Waindonesia, Wayahudi, Walebanoni, wazao wa wahamiaji Waholanzi, na makabila ya mwituni ambayo washiriki wayo ni Wanegro wa Vichakani, ambao babu zao walikuwa watumwa watoro. Miongoni mwao wamepatikana mamia waliokuwa na njaa ya kweli kikweli. Baadhi yao wamelazimika kuvunja kabisa kujitia sana katika mazoea ya kuabudu viumbe na uasiliani-roho. Mmoja wao alikuwa Paitu, mchawi, aliyeamini ujumbe wa Biblia na kisha akatumbukiza sanamu, hirizi, na dawa zake za uchawi mtoni. (Linganisha Kumbukumbu la Torati 7:25; 18:9-14; Matendo 19:19, 20.) Katika 1975 alijiweka wakfu kwa Yehova, yule Mungu wa kweli.

Idadi kubwa ya wakazi wa Peru huishi katika vijiji vidogo vilivyotawanyika juu ya milima ya Andes na katika misitu izungukayo vyanzo vya mto Amazon. Wangeweza kufikiwaje? Katika 1971 familia moja ya Mashahidi kutoka Marekani ilisafiri kwenda Peru ili kutembelea mwana wao mishonari, Joe Leydig. Walipopata kujua juu ya ile hesabu kubwa ya vijiji vinavyojificha hapa na pale katika mabonde ya milimani, kuhangaikia watu hao kuliwasukuma watake kufanya jambo fulani ili kusaidia. Walisaidia kuandaa gari moja kwanza ambalo lingetumika kama nyumba, kisha mengine mawili, pamoja na pikipiki ziwezazo kupitia vijia vyembamba ili zitumiwe kufunga safari ndefu za kuhubiri katika maeneo hayo ya mbali.

Ijapokuwa jitihada iliyofanywa, katika sehemu nyingi ilionekana kwamba wachache sana ndio tu walioonyesha kupendezwa katika ujumbe wa Biblia. Unaweza kuwazia jinsi kikundi cha wamishonari sita wachanga katika Barquisimeto, Venezuela, kilivyohisi katika miaka ya mapema ya 1950, wakati baada ya mwaka mmoja mzima wa bidii-nyendelevu ya kuhubiri, waliona maendeleo kidogo sana. Ijapokuwa watu walikuwa wenye urafiki, wengi wao walikuwa wanajihusisha sana na ushirikina nao walikuona kuwa dhambi kusoma hata andiko moja kutoka katika Biblia. Wowote walioonyesha kupendezwa walivunjwa moyo upesi na washiriki wa familia au majirani. (Mt. 13:19-21) Lakini, wakiwa na uhakika kwamba lazima kuwe na baadhi ya wenye mfano wa kondoo katika Barquisimeto na kwamba Yehova angewakusanya katika wakati wake mwenyewe, wamishonari waliendelea kufanya ziara nyumba hadi nyumba. Hivyo, Penny Gavette alichangamka moyo kama nini siku moja wakati mwanamke mmoja mwenye mvi alipomsikiliza na kisha akasema:

“Senorita, tangu nilipokuwa msichana mdogo, nimengojea mtu aje mlangoni pangu na kunieleza mambo ambayo umeniambia sasa hivi. Waona, nilipokuwa msichana, nilikuwa nikifanya usafi katika makao ya padri, naye alikuwa na Biblia katika maktaba yake. Nilijua kwamba tulikatazwa kuisoma, lakini nilitaka sana kujua sababu, hivi kwamba siku moja wakati hakuna mtu aliyekuwa akitazama, nilienda nayo nyumbani nami nikaisoma kwa siri. Niliyosoma yalinifanya nitambue kwamba Kanisa Katoliki halikuwa limetufundisha kweli na hivyo haikuwa ile dini ya kweli. Niliogopa kusema lolote kwa yeyote, lakini nilikuwa na uhakika kwamba siku moja wale wanaofundisha dini ya kweli wangekuja katika mji wetu. Wakati dini ya Protestanti ilipokuja, nilifikiri kwanza kwamba lazima iwe ndiyo ya kweli, lakini upesi niligundua kwamba walifundisha mengi kati ya mafundisho ya uwongo yaliyofundishwa na Kanisa Katoliki. Sasa, yale ambayo umeniambia sasa hivi ni yale niliyosoma katika Biblia ile miaka mingi iliyopita.” Kwa hamu nyingi alikubali funzo la Biblia na akawa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Ujapokuwa upinzani wa familia, alimtumikia Yehova kwa uaminifu mpaka kifo chake.

Jitihada kubwa ilitakwa ili kukusanya watu kama hao wenye mfano wa kondoo kuwa makutaniko na kuwazoeza kushiriki katika utumishi wa Yehova. Kwa kielelezo, katika Argentina, Rosendo Ojeda alisafiri kwa ukawaida kilometa kama 60 kutoka General San Martín, Chaco, ili kuongoza mkutano katika makao ya Alejandro Sozoñiuk, mtu mmoja mwenye kupendezwa. Safari hiyo mara nyingi ilichukua saa kumi, sehemu yayo kwa baiskeli, na nyingine kwa miguu, nyakati nyingine alipitia katikati ya maji yaliyofika makwapani. Mara moja kwa mwezi kwa miaka mitano alifunga safari hiyo, akikaa juma moja kila wakati ili kutoa ushahidi katika eneo hilo. Je, kulistahili? Yeye hana shaka juu ya jambo hilo kwa sababu matokeo yalikuwa kutaniko la wasifaji wa Yehova wenye furaha.

Kuendeleza Elimu kwa Ajili ya Uhai

Katika Mexico, Mashahidi wa Yehova waliendesha kazi yao kupatana na sheria zilizoongoza mashirika ya kitamaduni humo. Lengo la Mashahidi lilikuwa kutimiza mengi zaidi ya kufanya mikutano tu ambamo hotuba zilitolewa. Walitaka watu wawe kama wale Waberoya katika siku za mtume Paulo walioweza ‘kuyachunguza Maandiko kwa uangalifu kuona kama mambo waliyofundishwa ndivyo yalivyokuwa.’ (Mdo. 17:11, NW) Katika Mexico, kama ilivyo katika nchi nyinginezo nyingi, mara nyingi jambo hilo limehusu kutoa msaada wa pekee kwa watu ambao hawakuwa na elimu lakini ambao walitaka waweze kujisomea wenyewe Neno la Mungu lililopuliziwa roho.

Madarasa ya kufundisha kusoma na kuandika yaliyoongozwa na Mashahidi wa Yehova katika Mexico yamesaidia makumi ya maelfu ya watu humo kujifunza kusoma na kuandika. Kazi hiyo inathaminiwa na Idara ya Elimu ya Umma ya Mexico, na katika 1974 mkurugenzi katika Ofisi Kuu ya Elimu ya Watu Wazima aliandikia La Torre del Vigía de México barua, shirika la kijamii litumiwalo na Mashahidi wa Yehova, akisema hivi: “Nachukua fursa hii ili niwapongeze kwa uchangamfu . . . kwa ushirikiano wenye kusifika ambao shirika lenu limekuwa likiendeleza mwaka baada ya mwaka kunufaisha watu wetu.”

Huku ikitayarisha watu kwa ajili ya uhai wa milele wakiwa raia za Ufalme wa Mungu, elimu inayotolewa na Mashahidi huinua pia maisha ya sasa ya familia. Baada ya hakimu katika El Salto, Mkoa wa Durango, kuwa ameongoza sherehe za ndoa katika pindi mbalimbali kwa ajili ya Mashahidi wa Yehova, alitaarifu hivi katika 1952: “Sisi tunadai kuwa wazalendo na raia wema sana lakini tunaaibishwa na Mashahidi wa Yehova. Wao ni vielelezo bora kwetu kwa sababu hawaruhusu hata mtu mmoja katika tengenezo lao anayeishi kinyumba na hajahalalisha uhusiano wake [wa ndoa]. Na, nyinyi Wakatoliki, karibu nyote mnaishi maisha ya ukosefu wa adili na hamjahalalisha ndoa zenu.”

Programu hiyo ya elimu pia husaidia watu kujifunza kuishi pamoja kwa amani, kupendana mmoja na mwenzake badala ya kuchukiana na kuuana. Wakati Shahidi alipoanza kuhubiri katika Venado, Mkoa wa Guanajuato, alipata kwamba watu wote walikuwa na bunduki na bastola. Uadui wenye kuendelea ulitokeza kuuawa kwa familia nzimanzima. Lakini maagizo ya Biblia yalileta mabadiliko makubwa. Bunduki ziliuzwa ili kununua Biblia. Upesi zaidi ya watu 150 katika eneo hilo wakawa Mashahidi wa Yehova. Kitamathali, ‘walifua panga zao kuwa majembe ya kupogolea’ na kuanza kufuata njia za amani.—Mika 4:3.

Wamexico wengi wenye kumhofu Mungu wamezingatia moyoni yale ambayo Mashahidi wa Yehova wamewafundisha kutoka Neno la Mungu. Kama tokeo, yale maelfu machache ya wahubiri katika Mexico kufuatia Vita ya Ulimwengu 2 upesi yakawa 10,000 kisha 20,000, 40,000, 80,000, na zaidi kadiri Mashahidi walivyoonyesha wengine jinsi ya kutumia shauri la Neno la Mungu na jinsi ya kulifundisha wengine.

Kukusanyika Pamoja Chini ya Magumu

Hata hivyo, kadiri idadi ya Mashahidi wa Yehova ilivyoongezeka, walipata kwamba katika nchi moja baada ya nyingine, walilazimika kushinda vizuizi vigumu ndipo wakusanyike pamoja kwa ajili ya maagizo ya Kikristo. Katika Argentina walipigwa marufuku na serikali katika 1950. Hata hivyo, kwa kumtii Mungu, hawakuacha kuhubiri, wala kukusanyika pamoja. Mipango ilikuwa migumu kidogo, lakini makusanyiko yalifanywa.

Kwa kielelezo, mwishoni-mwishoni mwa 1953, Ndugu Knorr na Ndugu Henschel walizuru Argentina ili kutumikia kusanyiko la kitaifa. Ndugu Knorr aliingia nchini tokea magharibi, na Ndugu Henschel alianzia ziara zake kusini. Walihutubia vikundi vilivyokutana katika mashamba, katika shamba la matunda, katika mandari kando ya kijito cha mlimani, na katika nyumba za watu binafsi. Mara nyingi walilazimika kusafiri mbali sana kutoka kikundi kimoja hadi kile kingine. Wakiwasili katika Buenos Aires, kila mmoja alitumikia katika programu katika mahali tisa tofauti katika siku moja, na katika nyumba 11 siku iliyofuata. Kwa ujumla, walihutubia vikundi 56, kukiwa na hudhurio lililojumlika kuwa 2,505. Ilikuwa ratiba iliyotaka jitihada, lakini walikuwa na furaha kutumikia ndugu zao kwa njia hiyo.

Walipokuwa wakitayarisha kusanyiko katika Kolombia katika 1955, Mashahidi walikodisha jumba katika Barranquilla. Lakini, kwa kukazwa na askofu, meya na gavana waliingilia, nao mkataba huo ukafutwa. Wakijulishwa kwa muda wa siku moja tu, akina ndugu walipeleka kusanyiko mahali pengine, wakapanga kulifanyia kwenye uwanja wa ofisi ya tawi ya Sosaiti. Hata hivyo, kipindi cha kwanza cha jioni kilipokuwa kinaanza, polisi wenye silaha waliwasili wakiwa na amri ya kutawanya kusanyiko. Ndugu waliendelea kujitahidi. Rufani ilikatwa kwa meya kesho yake naye karani wake akaomba msamaha, na watu karibu 1,000 wakasongamana katika uwanja wa Sosaiti kwa ajili ya programu ya siku ya mwisho ya “Ufalme Unaoshinda” Kusanyiko. Zijapokuwa hali zilizokuwa wakati huo, ndugu waliimarishwa kwa shauri la kiroho lililohitajiwa.

Kutumikia Sehemu Zenye Uhitaji Mkubwa Zaidi

Shamba lilikuwa kubwa, na uhitaji wa wafanyakazi ulikuwa mkubwa katika Amerika ya Latin, kama ilivyokuwa katika sehemu nyingine nyingi. Katika 1957, kwenye mikusanyiko ulimwenguni pote, watu mmoja-mmoja na familia waliokuwa Mashahidi wa Yehova wakomavu walitiwa moyo wafikirie kuhamia kihalisi maeneo yenye uhitaji mkubwa zaidi wakakae humo na kuendesha huduma yao humo. Kitia moyo kama hicho kilitolewa kwa njia mbalimbali baadaye. Mwaliko huo ulikuwa kama ule uliotolewa na Mungu kwa mtume Paulo, aliyeona katika njozi mtu aliyemsihi: “Vuka, uingie Makedonia utusaidie.” (Mdo. 16:9, 10, NW) Itikio lilikuwaje kwa mwaliko huo wa kisasa? Watumishi wa Yehova walijitolea kwa hiari.—Zab. 110:3.

Kwa familia yenye watoto wadogo, inataka imani kubwa kuondoka, kuacha watu wa ukoo na makao na kazi ya kimwili, na kusafiri kwenye mazingira mapya kabisa. Kuhama huenda kukataka kukubali kiwango tofauti sana cha maisha na, katika visa fulani, kujifunza lugha mpya. Hata hivyo, maelfu ya Mashahidi mmoja-mmoja na familia wamehama ili kusaidia wengine wajifunze juu ya maandalizi ya Yehova kwa ajili ya uhai wa milele.

Wakiitikia haraka, idadi fulani ya Mashahidi wa Yehova ilihama katika miaka ya mwisho-mwisho ya 1950; wengine katika miaka ya 1960; wengine zaidi katika miaka ya 1970. Na kuhama huko kwa Mashahidi kwenda kwenye maeneo yenye uhitaji mkubwa zaidi huendelea hadi leo hii.

Wametoka wapi? Idadi kubwa kutoka Australia, Kanada, New Zealand, na Marekani. Wengi kutoka Ufaransa, Uingereza, na Ujerumani. Pia kutoka Austria, Denmark, Finland, Italia, Jamhuri ya Korea, Japani, Norway, Sweden, Ubelgiji, Hispania, na Uswisi, miongoni mwa nyinginezo. Kwa kuwa idadi za Mashahidi wa Yehova zimeongezeka katika Argentina, Brazili, Mexico, na nchi nyinginezo za Amerika ya Latin, hizo pia zimetoa wafanyakazi walio tayari kutumikia katika nchi nyinginezo zenye uhitaji mkubwa. Vivyo hivyo, barani Afrika wafanyakazi wenye bidii wamehama kutoka nchi moja kwenda nyingine ili kusaidia kutoa ushahidi.

Wamehamia sehemu zipi? Nchi kama vile Afghanistan, Malasia, na Senegal, na visiwa kama vile Réunion na St. Lucia. Kama 1,000 walihamia Ireland, ambako walitumikia kwa vipindi vya wakati vya urefu tofauti-tofauti. Idadi kubwa ilienda Iceland, vijapokuwa vipindi vyayo virefu vya majira ya baridi yenye utusitusi, na baadhi yao walikaa humo, wakawa nguzo katika makutaniko na kutoa msaada wenye upendo kwa wapya zaidi. Hasa kazi nyingi nzuri imefanywa katika Amerika ya Kati na ya Kusini. Mashahidi zaidi ya 1,000 walihamia Kolombia, zaidi ya 870 walihamia Ekuado, zaidi ya 110 walihamia El Salvador.

Harold na Anne Zimmerman walikuwa miongoni mwa wale waliohama. Walikuwa tayari wametumikia wakiwa walimu wamishonari katika Ethiopia. Hata hivyo, katika 1959, wakati walipokuwa wakikamilisha mipango ya kuhama kutoka Marekani kwenda Kolombia kushiriki katika kueneza ujumbe wa Ufalme huko, walikuwa wakilea watoto wanne, waliokuwa na umri wa kuanzia miezi mitano hadi miaka mitano. Harold alitangulia ili kutafuta kazi. Wakati alipowasili nchini, matangazo ya habari nchini yalimtia wasiwasi. Vita isiyo rasmi ya wenyewe kwa wenyewe ilikuwa ikiendelea, na kulikuwa mauaji mengi katika sehemu za mashambani za nchi. ‘Je, kweli mimi nataka kuleta familia yangu iishi katika hali kama hizi?’ akajiuliza. Alijaribu kukumbuka kielelezo cha kumwongoza au kanuni ya Biblia. Jambo lililokuja akilini mwake ni lile simulizi la Biblia la wapelelezi wenye woga waliorudisha kwenye kambi ya Waisraeli ripoti mbaya kuhusu Bara la Ahadi. (Hes. 13:25–14:4, 11) Jambo hilo lilimwezesha kufikia uamuzi; yeye hakutaka kuwa kama wao! Mara moja akapanga familia yake ije. Ilikuwa ni mpaka pesa zao zilipopungua kufikia dola tatu tu ndipo alipopata kazi ya kimwili aliyohitaji, lakini walikuwa na vitu vya lazima kabisa. Kiasi cha kazi aliyolazimika kufanya ili kuruzuku familia yake kilibadilika kadiri miaka ilivyopita, lakini sikuzote yeye amejitahidi kutanguliza masilahi ya Ufalme. Walipokwenda Kolombia kwanza, kulikuwa Mashahidi kama 1,400 nchini. Lo! ni ukuzi wa kustaajabisha kama nini ambao wameona tangu hapo!

Kutumikia sehemu ambako uhitaji wa Mashahidi ni mkubwa zaidi hakuhitaji sikuzote kwamba mtu ahamie nchi nyingine. Maelfu ya Mashahidi mmoja-mmoja na familia wamehamia maeneo mengine ndani ya nchi yao wenyewe. Familia moja katika Mkoa wa Bahia, Brazili, walihamia mji wa Prado, ambao haukuwa na Mashahidi. Ujapokuwa upinzani kutoka kwa makasisi, waliishi na kufanya kazi katika mji huo na eneo lililozunguka kwa miaka mitatu. Jengo la kanisa lililoachwa lilinunuliwa na kugeuzwa kuwa Jumba la Ufalme. Katika muda mfupi, kulikuwa zaidi ya Mashahidi mia moja wenye bidii katika eneo hilo. Na huo ulikuwa ndio mwanzo tu.

Katika idadi zinazozidi kuongezeka daima, wapendao uadilifu katika Amerika ya Latin wanaitikia mwaliko uliorekodiwa katika Zaburi 148: ‘Msifuni Yah, enyi watu! Msifuni Yehova kutoka dunia, enyi nyote vikundi vya mataifa.’ (Mist. 1, 7-11, NW) Kwelikweli, kufikia 1975 kulikuwa wasifaji wa Yehova katika kila nchi katika Amerika ya Latin. Ripoti ya mwaka huo ilionyesha kwamba 80,481, waliokuwa wamepangwa kitengenezo katika makutaniko 2,998, walikuwa wakitumikia katika Mexico. Wengine 24,703, katika makutaniko 462, walikuwa wakiongea juu ya umaliki wa Yehova katika Amerika ya Kati. Na katika Amerika Kusini, kulikuwa 206,457 wasifaji wa hadharani wa Yehova katika makutaniko 3,620.

Kujitahidi Kufikia Visiwa vya Pasifiki

Wakati upanuzi wa kasi ulipokuwa ukitukia katika Amerika Kusini, Mashahidi wa Yehova walikuwa wakielekeza fikira pia kwenye visiwa vya Pasifiki. Kuna mamia ya visiwa hivyo ambavyo vimetawanyika katikati ya Australia na yale mabara ya Amerika, vingi vyavyo vikiwa vidogo sana. Baadhi yavyo vinakaliwa na familia chache tu; vingine, na makumi ya maelfu ya watu. Mapema katika miaka ya 1950, maoni mabaya yasiyo na sababu ya maofisa yalifanya isiwezekane kwa Watch Tower Society kupeleka wamishonari katika visiwa vingi kati yavyo. Lakini watu huko pia walihitaji kusikia juu ya Yehova na Ufalme wake. Hiyo inapatana na unabii uliorekodiwa kwenye Isaya 42:10-12, usemao: “Mwimbieni BWANA wimbo mpya, na sifa zake tokea mwisho wa dunia . . . Na visiwa, nao wakaao humo.” Hivyo, katika 1951, kwenye mkusanyiko katika Sydney, Australia, mapainia na waangalizi wa mzunguko waliopendezwa na kuwa na ushiriki katika kueneza ujumbe wa Ufalme kwenye visiwa hivyo walialikwa wakutane na Ndugu Knorr. Katika wakati huo kama 30 walijitolea wakaanzishe kazi ya kuhubiri katika visiwa hivyo vya tropiki.

Miongoni mwao walikuwa Tom na Rowena Kitto, waliojipata upesi katika Papua, ambako wakati huo hakukuwako Mashahidi. Walianza kazi yao miongoni mwa watu wa Ulaya katika Port Moresby. Katika muda mfupi, walikuwa wakitumia jioni katika Hanuabada, kile “Kijiji Kikubwa,” pamoja na kikundi cha Wapapua 30 hadi 40 waliokuwa na njaa ya kiroho. Kutoka kwao, ujumbe ukaenea kwenye vile vijiji vingine. Katika muda mfupi, watu wa Kerema wakapeleka ujumbe wakiomba kwamba funzo la Biblia liongozwe pamoja nao. Halafu mkuu wa kijiji kutoka Haima akaja, akisihi: “Tafadhali njooni mfundishe watu wangu juu ya kweli!” Na hivyo kweli ikaenea.

Wenzi wengine wa ndoa, John na Ellen Hubler, walienda New Caledonia kuanzisha kazi huko. Walipowasili katika 1954, walikuwa na visa za watalii za mwezi mmoja tu. Lakini John alipata kazi ya kimwili, nalo hilo likawasaidia kupata kuongezewa muda. Baada ya wakati, Mashahidi wengine—jumla ya 31—wakahamia humo kwa njia iyo hiyo. Mwanzoni, walikuwa wakifanya huduma yao katika maeneo ya viungani ili wasivute fikira sana. Baadaye, walianza kuhubiri katika jiji kuu, Nouméa. Kutaniko likaundwa. Kisha, katika 1959, mshiriki wa Aksio ya Katoliki akapata cheo kikubwa serikalini. Visa za Mashahidi hazikufanywa upya tena. Akina Hubler wakalazimika kuondoka. Vichapo vya Watch Tower vikapigwa marufuku. Hata hivyo, habari njema za Ufalme zilikuwa zimetia mizizi, na idadi ya Mashahidi iliendelea kukua.

Katika Tahiti watu wengi walikuwa wameonyesha kupendezwa na kazi ya Mashahidi wa Yehova wakati ndugu walipozuru kifupi huko. Lakini katika 1957, hakukuwa na Mashahidi wenyeji, kazi yao ilipigwa marufuku, na wamishonari wa Watch Tower hawakuruhusiwa kuingia humo. Hata hivyo, Agnes Schenck, raia wa Tahiti aliyekuwa wakati huo akiishi katika Marekani, alikuwa amekuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Alipopata kujua juu ya uhitaji wa wapiga-mbiu wa Ufalme katika Tahiti, yeye, mume wake, na mwana wao walisafiri kwa meli kutoka California katika Mei 1958. Muda mfupi baada ya hapo, familia nyingine mbili zikajiunga nao, ingawa wangeweza kupata visa za watalii kwa miezi mitatu tu. Kufikia mwaka uliofuata, kutaniko lilikuwa limeundwa katika Papeete. Na katika 1960 serikali ilitambua rasmi shirika la Mashahidi wa Yehova lililokuwa limefanyizwa nchini.

Ili kueneza ujumbe wa Ufalme, dada wawili wamishonari wakiwa njiani kurudi kwenye mgawo wao walitua ili kutembelea mtu wa ukoo kwenye kisiwa cha Niue. Ule mwezi waliotumia humo ulikuwa wenye mazao sana; kupendezwa kwingi kulipatikana. Lakini wakati mashua iliyofuata yenye kusafiri kati ya visiwa ilipowasili, ilikuwa lazima waondoke. Hata hivyo, upesi Seremaia Raibe, Mfiji, alipata mkataba wa kazi katika Idara ya Kazi ya Umma katika Niue kisha akatumia wasaa wake wote kuhubiri. Hata hivyo, kama tokeo la mkazo wa makasisi, ruhusa ya kukaa kwa Ndugu Raibe ilifutwa baada ya miezi michache, na katika Septemba 1961 Bunge liliamua kutoruhusu Mashahidi wa Yehova wowote wengine nchini. Hata hivyo, kazi ya kuhubiri iliendelea humo. Jinsi gani? Wale Mashahidi wenyeji wajapokuwa wapya, walistahimili katika kumtumikia Yehova. Zaidi ya hilo, serikali ya mitaa ilikuwa tayari imemwajiri kazi William Lovini, Mniue aliyekuwa akiishi New Zealand. Kwa nini alikuwa na hamu ya kurudi Niue? Kwa sababu alikuwa amekuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova naye alitaka kutumikia sehemu ambako uhitaji ni mkubwa zaidi. Kufikia 1964 idadi ya Mashahidi ilipanda kufikia 34.

Katika 1973, David Wolfgramm, raia wa Tonga, pamoja na mke wake na watoto wanane, alikuwa akiishi katika makao ya starehe katika New Zealand. Lakini waliacha yote hayo nyuma wakahamia Tonga ili kusogeza mbele masilahi ya Ufalme. Kutoka huko walishiriki katika kusukuma kazi mbele zaidi katika visiwa vya Tonga, karibu 30 kati yavyo vikiwa vinakaliwa.

Wakati, jitihada, na gharama kubwa zimetakwa ili kufikia visiwa hivyo. Lakini Mashahidi wa Yehova huona maisha za wanadamu wenzao kuwa zenye thamani nao hawaachi chochote katika jitihada zao za kuwasaidia ili wanufaike na uandalizi wa Yehova wenye upendo kwa ajili ya uhai wa milele katika ulimwengu wake mpya.

Familia iliyouza shamba lao katika Australia na kuhamia kimojawapo visiwa vya Pasifiki ilitoa muhtasari wa hisia zao kwa njia hii: “Kusikia wanavisiwa hawa wakisema kwamba wamepata kumjua Yehova, kuwasikia wakiita watoto wetu watoto wao, wakifanya hivyo kwa sababu wanawapenda sana kwa sababu ya kweli, kutazama masilahi ya Ufalme na hudhurio kwenye mikutano ikikua, kusikia watu hawa wazuri wakisema: ‘Watoto wangu watafunga ndoa katika Bwana tu,’ na wakisema hivyo baada ya kuwa wameshirikiana kwa karne nyingi na mapokeo na aina ya ndoa za Mashariki, kuwatazama wakinyoosha na kutakasa maisha ya ndoa yenye kutatiza, . . . kuwaona wakijifunza huku wakichunga ng’ombe zao kandokando ya njia, baada ya kufanya kazi ngumu katika mashamba ya mpunga, kujua kwamba wanazungumza juu ya makosa ya ibada ya sanamu, uzuri wa jina la Yehova kwenye duka la mahali na kwingineko, kuwa na mama Mhindi mwenye umri mkubwa akikuita ndugu na dada na kukuomba aandamane nawe akawaambie jamaa juu ya Mungu wa kweli . . . Yote hayo hujumlika kuwa thawabu isiyokadirika thamani kwa kuchukua hatua tuliyochukua katika kujibu mwito kutoka Pasifiki Kusini.”

Hata hivyo, wengi zaidi ya wanavisiwa hawa wa Pasifiki walikuwa wakipata ufikirio. Kuanzia 1964, mapainia wenye ujuzi kutoka Filipino walipewa migawo wakawaongezee nguvu wamishonari wenye bidii ambao tayari walikuwa wakifanya kazi katika Hong Kong, Indonesia, Jamhuri ya Korea, Laos, Malasia, Taiwan, Thailand, na Vietnam.

Ujapokuwa Mkazo wa Familia na Jamii

Mtu anapokuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, sikuzote hilo halikubaliwi na familia yake na jamii kuwa uamuzi wa kibinafsi tu.—Mt. 10:34-36; 1 Pet. 4:4.

Walio wengi kati ya wale ambao wamekuwa Mashahidi wa Yehova katika Hong Kong wamekuwa ni vijana. Lakini vijana hao wamepatwa na mkazo mwingi katika mfumo ambao hufanya elimu ya juu na kazi yenye mshahara mnono kuwa jambo la kutangulizwa. Wazazi huwaona watoto wao kuwa akiba wanayoweka ili kuhakikisha kwamba wataishi kwa starehe katika miaka ya baadaye. Hivyo, wakati wazazi wa kijana mmoja katika Kwun Tong walipojua kwamba funzo la Biblia, hudhurio la mikutano, na utumishi wa shambani wa mwana wao vingeingilia uchumaji wake wa pesa, upinzani wao ukawa mwingi. Baba yake alimkimbiza akiwa na kisu cha kukata nyama; mama yake alimtemea mate hadharani. Matusi yaliendelea kwa miezi mingi karibu bila kukoma. Wakati mmoja kijana huyo aliwauliza wazazi wake: “Je, hamkunilea kwa sababu ya upendo?” Nao wakajibu: “Hapana, kwa sababu ya pesa!” Hata hivyo, kijana huyo aliendelea kutanguliza ibada yake kwa Yehova; lakini alipoondoka nyumbani, aliendelea pia kuwasaidia wazazi wake kifedha kadiri alivyoweza, maana alijua kwamba jambo hilo lingempendeza Yehova.—Mt. 15:3-9; 19:19.

Katika jamii zinazofungamana karibukaribu, mkazo mkali mara nyingi hutoka kwa zaidi ya familia ya mtu ya karibu. Mmoja aliyepatwa na jambo hilo ni Fuaiupolu Pele katika Samoa Magharibi. Lilionwa kuwa jambo lisilowazika miongoni mwa watu kwa Msamoa kukataa desturi na dini ya babu zake, naye Pele alijua kwamba angeshutumiwa na kuhojiwa. Alijifunza kwa bidii na akasali kwa Yehova kwa moyo wa bidii. Wakati alipoitwa na chifu mkuu wa familia aje kwenye mkutano katika Faleasiu, alikabiliwa na machifu sita, wahutubu watatu, mapasta kumi, walimu wawili wa theolojia, yule chifu mkuu aliyesimamia mkutano, na wanaume na wanawake wazee wa familia. Walimlaani na kumshutumu yeye pamoja na mshiriki mwingine wa familia aliyekuwa akionyesha kupendezwa na Mashahidi wa Yehova. Mjadala ukafuata; uliendelea mpaka saa kumi za usiku. Utumizi wa Pele wa Biblia uliudhi waliokuwapo, nao wakapiga kelele hivi: “Iondoe Biblia hiyo! Acha kutumia Biblia hiyo!” Lakini hatimaye yule chifu mkuu akasema kwa sauti hafifu: “Umeshinda, Pele.” Lakini Pele akajibu: “Samahani, Bwana, mimi sikushinda. Usiku huu wewe umesikia ujumbe wa Ufalme. Ni tumaini langu la moyo mweupe kwamba wewe utautii.”

Wakati Kunapokuwa na Upinzani Mwingi wa Makasisi

Wamishonari wa Jumuiya ya Wakristo walikuwa wamewasili katika visiwa vya Pasifiki katika miaka ya 1800. Katika sehemu nyingi, walikuwa wamewasili kwa amani; kwingineko walikuwa wametegemezwa na nguvu za kijeshi. Katika maeneo fulani walikuwa wamegawana visiwa miongoni mwao wenyewe kwa “maafikiano ya kiungwana.” Lakini kulikuwa kumekuwa pia vita vya kidini, ambavyo katika hivyo Wakatoliki na Waprotestanti walikuwa wamepigana ili wapate udhibiti. “Wachungaji” hao wa kidini, makasisi, sasa walitumia kila njia iliyopatikana kuzuia Mashahidi wa Yehova wasiingie katika ile waliyoiona kuwa milki yao. Nyakati fulani waliwakaza maofisa wawafukuze Mashahidi kutoka visiwa fulani. Nyakati nyingine walichukua sheria mikononi mwao wenyewe.

Katika kisiwa cha New Britain, katika kijiji cha Vunabal, kikundi kutoka kabila la Sulka kilionyesha kupendezwa sana na kweli ya Biblia. Lakini Jumapili moja katika 1959, wakati John Davison alipokuwa akiongoza funzo la Biblia pamoja nao, wafanyaghasia Wakatoliki, chini ya mwelekezo wa katekista Mkatoliki, walijisukumiza ndani ya nyumba na kukomesha funzo hilo kwa kelele na matusi yao. Jambo hilo liliripotiwa kwa polisi katika Kokopo.

Badala ya kuwaacha kondoo, Mashahidi walirudi juma lililofuata waendelee kutoa msaada wa kiroho kwa wenye kuthamini katika Vunabal. Padri Mkatoliki alikuwapo pia, ijapokuwa hakualikwa na wanavijiji, naye alikuja na mamia kadhaa ya Wakatoliki wa kabila jingine. Baada ya kuchochewa na padri, wale wa kutoka kanisa lake waliwatusi Mashahidi, wakawatemea mate, wakawatisha kwa ngumi, wakararua Biblia za wanavijiji, huku padri akisimama akiwa amekunja mikono na kutabasamu. Polisi waliojaribu kudhibiti hali walishtuka na kuudhika. Wengi kati ya wanavijiji waliogopa pia. Lakini angalau mmoja wa wanavijiji alithibitika kuwa mwenye ujasiri akachukua msimamo kwa ajili ya yale aliyojua kuwa kweli. Sasa, mamia ya wengine katika kisiwa hicho wamefanya hivyohivyo.

Hata hivyo, si walimu wote wa kidini walioonyesha roho ya uadui kuelekea Mashahidi wa Yehova. Shem Irofa’alu, katika Visiwa vya Solomon, alihisi daraka la kweli kuelekea wale waliomtegemea akiwa kiongozi wao wa kidini. Baada ya kusoma kitabu Kutoka Paradiso Iliyopotea Mpaka Paradiso Iliyopatikana cha Watch Tower Society, aling’amua kwamba mtu fulani alikuwa amemwambia uwongo. Yeye na walimu wa kidini chini ya usimamizi wake walisikiliza mazungumzo waliyokuwa nayo pamoja na Mashahidi, wakauliza maswali, na kuangalia maandiko katika Biblia. Kisha wakaafikiana kwamba wataka kuwa Mashahidi wa Yehova, hivyo wakageuza makanisa katika vijiji vyao 28 kuwa Majumba ya Ufalme.

Bubujiko la Maji ya Ile Kweli Barani Afrika

Hasa kuanzia na miaka ya mapema ya 1920, jitihada nyingi zilifanywa ili watu katika sehemu zote za Afrika waweze kuwa na fursa ya kupata kumjua Yehova, yule Mungu wa kweli, na kunufaika na maandalizi yake yenye upendo. Vita ya ulimwengu ya pili ilipokwisha, kulikuwa Mashahidi wa Yehova watendaji katika nchi 14 katika bara la Afrika. Nchi nyingine 14 za Afrika zilikuwa zimefikiwa kwa ujumbe wa Ufalme, lakini hakukuwa na Mashahidi waliokuwa wakiripoti utendaji katika nchi hizo katika 1945. Wakati wa miaka 30 iliyofuata, kufikia 1975, kazi ya kuhubiri habari njema ilipenya nchi nyinginezo 19 barani Afrika. Katika karibu nchi hizo zote, pamoja na visiwa vinavyozunguka, makutaniko yalianza kufanyizwa—machache katika nchi fulani, zaidi ya elfu moja katika Zambia, karibu elfu mbili katika Nigeria. Yote hayo yalitukiaje?

Kuenezwa kwa ujumbe wa Ufalme kulikuwa kama bubujiko la maji. Kwa sehemu iliyo kubwa, bubujiko hupitia mifereji ya mto, ijapokuwa baadhi yayo hufurika kwenye ardhi iliyo ukingoni; na ikiwa kizuizi chazuia njia, maji hupitia kijia kingine au kiasi cha maji huongezeka na nguvu kuongezeka mpaka yanapojaa pomoni na kupita juu.

Ikitumia mipango yayo ya kawaida ya kitengenezo, Watch Tower Society iliwapa migawo wahudumu wa wakati wote—mapainia, mapainia wa pekee, na wamishonari—kwenye nchi ambazo ni kazi ndogo sana ya kuhubiri iliyokuwa imefanywa. Kokote walikoenda, walialika watu ‘watwae maji ya uhai bure.’ (Ufu. 22:17) Kwa kielelezo, katika Afrika kaskazini, mapainia wanne wa pekee kutoka Ufaransa waliwatolea mwaliko huo watu wa Algeria katika 1952. Upesi mwanamke mpiga-ramli huko akakubali kweli, akatambua kwamba lazima aache kazi yake ili ampendeze Yehova, akaanza kutoa ushahidi kwa wale ambao hapo kwanza walikuwa wateja wake. (Kum. 18:10-12) Mapainia hao walitumia kwa mafanikio kile kitabu “Let God Be True” kusaidia watu mmoja-mmoja wenye moyo mweupe waone tofauti kati ya Biblia Takatifu na mapokeo ya kidini. Kilikuwa chenye nguvu sana katika kukomboa watu na mazoea ya dini bandia hivi kwamba kasisi mmoja alionyesha kitabu hicho akiwa kwenye mimbari na kukilaani, kuwalaani wale waliokuwa wakikigawanya, na kuwalaani wale waliokuwa wakikisoma.

Katika 1954 mishonari mmoja alifukuzwa kutoka Hispania ya Katoliki kwa sababu ya kufundisha Biblia bila kibali cha makasisi; kwa hiyo mwaka uliofuata, yeye na painia mwenzake walianza kuhubiri katika Moroko. Upesi familia ya washiriki watano ya Mashahidi wa Yehova ikajiunga nao ambayo ilikuwa imefukuzwa kutoka Tunisia, ambako msukosuko mwingi ulikuwa umetokea wakati wenzi wa ndoa Wayahudi walipokubali Yesu kuwa Mesiya na upesi wakaanza kushiriki imani yao mpya pamoja na wengine. Kusini zaidi, mapainia kutoka Ghana walipewa mwelekezo waingie Mali katika 1962. Baadaye, mapainia Wafaransa waliokuwa wakitumikia katika Algeria waliombwa pia wasaidie katika Mali. Kisha, idadi kubwa ya wale waliopata kuwa Mashahidi huko baadaye walijiunga na idadi za watumishi wa wakati wote. Katika 1966 mapainia wa pekee wanane kutoka Nigeria walichukua migawo katika Niger, nchi yenye watu wachache ambayo hutia ndani sehemu ya Jangwa la Sahara. Burundi ilipewa fursa ya kusikia ujumbe wa Ufalme wakati mapainia wawili wa pekee walipotumwa huko kutoka Rhodesia Kaskazini (sasa ni Zambia) katika 1963, wakifuatwa na wamishonari wanne waliozoezwa katika Shule ya Gileadi.

Kulikuwa pia wamishonari katika Ethiopia katika miaka ya mapema ya 1950. Serikali ya Ethiopia ilitaka kwamba waanzishe misheni na shule za kawaida, jambo ambalo walifanya. Lakini, kuongezea hilo, walikuwa na shughuli wakifundisha Biblia, na upesi kulikuwa na mmiminiko wa daima wa watu kwenye kao la wamishonari, wapya wakiwasili kila siku kuomba kwamba mtu fulani awasaidie kuelewa Biblia. Wakati wa miongo mitatu kufuatia Vita ya Ulimwengu 2, nchi 39 za bara la Afrika zilinufaika na msaada wa wamishonari hao waliozoezwa Gileadi.

Wakati uleule, maji ya kweli yalikuwa yakitiririka kwa wingi kuingia katika maeneo yenye ukame wa kiroho kupitia Mashahidi wa Yehova ambao kazi yao ya kimwili iliwakutanisha na wengine. Hivyo, wenzi wa ndoa Mashahidi kutoka Misri ambao kazi yao ilitaka wahamie Libya katika 1950 walihubiri kwa bidii wakati wa saa zao za kutokuwa kazini. Mwaka huohuo Shahidi mmoja aliyekuwa mfanya biashara ya sufu, pamoja na familia yake, walihama kutoka Misri kwenda Khartoum, Sudan. Alilifanya kuwa zoea lake kutoa ushahidi kwa wateja kabla ya kufanya biashara nao. Mmoja wa Mashahidi wa kwanza katika Senegal (wakati ule ikiwa sehemu ya Afrika Magharibi ya Ufaransa) alienda huko, katika 1951, akiwa mwakilishi wa shirika la kibiashara. Yeye pia alithamini madaraka yake akiwa Shahidi wa Aliye Juu Zaidi. Katika 1959, kuhusiana na kazi yake ya kimwili, Shahidi mmoja alienda Fort-Lamy (sasa ni N’Djamena), katika ile ambayo baadaye ilikuja kuwa Chad, naye alitumia fursa yake kueneza ujumbe wa Ufalme katika nchi hiyo. Katika nchi zinazopakana na Niger walikuwa wafanya biashara waliokuwa Mashahidi wa Yehova; hivyo, wakati mapainia wa pekee walipokuwa wakihubiri kwa bidii katika Niger kuanzia 1966 kuendelea, wafanyabiashara hao walikuwa pia wakiwahubiri watu wa kutoka Niger waliofanya biashara nao. Na Mashahidi wawili ambao waume wao walienda Mauritania kufanya kazi katika 1966 walitumia fursa kutoa ushahidi katika eneo hilo.

Watu walioburudishwa na ‘maji ya uzima’ waliyashiriki pamoja na wengine. Kwa kielelezo, katika 1947 mtu mmoja aliyekuwa amehudhuria mikutano fulani lakini yeye mwenyewe hakuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova alihama kutoka Kamerun kwenda Ubangi-Shari (sasa ni Jamhuri ya Afrika ya Kati). Kwa kusikia juu ya mtu katika Bangui aliyekuwa anapendezwa sana na Biblia, alipanga kwa fadhili kwamba ofisi ya Watch Tower Society katika Uswisi impelekee kitabu. Etienne Nkounkou, mpokeaji, alifurahia sana chakula cha kiroho chenye afya kilichokuwamo, na kila juma alikisoma mbele ya kikundi cha wengine waliopendezwa. Waliwasiliana na makao makuu ya Sosaiti. Kadiri ujuzi wao ulivyoongezeka, kikundi hicho cha funzo kikawa kikundi cha kuhubiri pia. Ijapokuwa mkazo wa makasisi ulileta marufuku ya serikali juu ya fasihi za Watch Tower, Mashahidi hao wapya waliendelea kuhubiri kwa kutumia Biblia pekee. Watu katika nchi hiyo hupenda kusikia mazungumzo ya Biblia, hivyo kufikia wakati marufuku juu ya vichapo vya Sosaiti ilipoondolewa katika 1957, Mashahidi huko walikuwa tayari zaidi ya 500.

Wakati Vizuizi Vilipotokezwa

Wakati vizuizi vilipozuia mtiririko wa maji yenye kutoa uhai, yalipenya upesi kwa njia nyingine. Ayité Sessi, painia kutoka Dahomey (sasa ni Benin), alikuwa amehubiri katika Togo ya Ufaransa (sasa ni Togo) kwa muda mfupi tu katika 1949 wakati serikali ilipomlazimisha kuhama. Lakini mwaka uliofuata Akakpo Agbetor, aliyekuwa hapo kwanza mwanadondi, aliyetoka Togo hapo kwanza, alirudi katika nchi yake pamoja na ndugu yake mdogo. Kwa kuwa hiyo ilikuwa ndiyo nchi alimozaliwa, aliweza kutoa ushahidi bila vizuizi, hata kufanya mikutano. Ijapokuwa mapainia waliokuwa wamechukua migawo katika Fernando Po (sasa ni sehemu ya Guinea ya Ikweta) kama mwaka 1950 walifukuzwa nchini baada ya muda mfupi kwa sababu ya chuki ya kidini, baadaye Mashahidi wengine waliweza kupata mikataba ya kazi ambayo iliwawezesha kuishi katika eneo hilo. Na, bila shaka, kupatana na amri ya Yesu, walihubiri.—Mk. 13:10.

Emmanuel Mama, mwangalizi wa mzunguko kutoka Ghana, alitumwa Upper Volta (sasa huitwa Burkina Faso) kwa majuma machache katika 1959, naye aliweza kufanya kazi nyingi ya kutoa ushahidi katika Ouagadougou, jiji kuu. Lakini hakukuwa na Mashahidi walioishi nchini. Miaka minne baadaye, Mashahidi saba, waliotoka mwanzoni Togo, Dahomey (sasa ni Benin), na Kongo, walihamia Ouagadougou na kutafuta kazi ili waweze kutumikia katika eneo hilo. Miezi michache baadaye, mapainia wa pekee kadhaa kutoka Ghana wakajiunga nao. Hata hivyo, kwa sababu ya maofisa kukazwa na makasisi, katika 1964, baada ya Mashahidi kuwa humo kwa muda unaopungua mwaka mmoja, walikamatwa, wakafungwa kwa siku 13, kisha wakafukuzwa kutoka nchini. Je, jitihada zao zilikuwa zimestahili? Emmanuel Johnson, mkazi wa nchi, alikuwa amejifunza mahali kweli ya Biblia iwezapo kupatikana. Aliendelea kujifunza na Mashahidi wa Yehova kwa njia ya posta, naye akabatizwa katika 1969. Naam, kazi ya Ufalme ilikuwa imetia mizizi katika nchi nyingine.

Wakati maombi ya visa ambazo zingewezesha wamishonari waliozoezwa Gileadi kutumikia katika Ivory Coast (sasa huitwa Côte d’Ivoire) yalipopelekwa, maofisa Wafaransa walikataa kutoa kibali. Hivyo, katika 1950, Alfred Shooter, kutoka Gold Coast (sasa ni Ghana), alitumwa kwenye jiji kuu la Ivory Coast akiwa painia. Mara alipoimarisha makao, mke wake akajiunga naye; na miezi michache baadaye, wenzi wa ndoa wamishonari, Gabriel na Florence Paterson, wakaja. Matatizo yakazuka. Siku moja, fasihi zao zilikamatwa kwa sababu hazikuwa na kibali cha serikali, nao ndugu wakapigwa faini. Lakini baadaye walipata vitabu vyao vikiuzwa sokoni, kwa hiyo wakavinunua na kuvitumia vizuri.

Wakati huohuo, ndugu hao walitembelea ofisi nyingi za serikali katika jitihada ya kupata visa za kudumu. Bw. Houphouët-Boigny, aliyepata baadaye kuwa rais wa Ivory Coast, alijitolea asaidie. “Kweli,” akasema, “haina kizuizi chochote. Ni kama mto wenye nguvu nyingi; ujengee bwawa nao utafurika juu ya bwawa.” Wakati padri Mkatoliki na mhudumu Mmethodisti walipojaribu kutatiza, Ouezzin Coulibaly, ofisa mdogo wa serikali, akasema: “Mimi nawakilisha watu wa nchi hii. Sisi ndio watu, nasi twawapenda Mashahidi wa Yehova na kwa hiyo sisi twataka wakae katika nchi hii.”

Wanafunzi Waelewao Kikweli

Alipokuwa akitoa maagizo ya ‘kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote,’ Yesu alielekeza pia kwamba wale ambao wangekuwa wanafunzi—wale waaminio mafundisho ya Kristo na kuyatumia—wapaswa kubatizwa. (Mt. 28:19, 20, NW) Kupatana na hilo, kuna mpango wa kubatiza wanafunzi wapya kwenye makusanyiko na mikusanyiko ya pindi kwa pindi ya Mashahidi wa Yehova. Idadi ibatizwayo katika pindi yoyote ile huenda ikawa ndogo kwa kadiri fulani. Hata hivyo, kwenye mkusanyiko mmoja katika Nigeria katika 1970, kulikuwa Mashahidi wapya 3,775 waliozamishwa. Ingawa hivyo, idadi kubwa si ndilo lengo.

Ilipojulikana, katika 1956, kwamba wengine katika Gold Coast waliokuwa wakibatizwa hawakuwa wamejenga imani yao juu ya msingi wa kutosha, mpango ulianzishwa huko wa kuchunguza watakao kubatizwa. Daraka liliwekwa juu ya waangalizi wa kutaniko la mahali katika Gold Coast kuchunguza kibinafsi kila mmoja atakaye kuzamishwa ili kuhakikisha kwamba alikuwa na ujuzi sahihi wa kweli za msingi za Biblia, kwamba alikuwa akiishi kupatana na viwango vya Biblia, na kwamba alielewa waziwazi wajibu uambatanao na kuwa Shahidi wa Yehova aliye wakfu na kubatizwa. Baada ya wakati, utaratibu kama huo ulianza kutumiwa ulimwenguni pote. Muhtasari wenye habari nyingi wa kutumiwa katika kupitia mafundisho ya Biblia ya msingi pamoja na watakao kubatizwa uliandaliwa katika 1967 katika kitabu “Neno Lako Ni Taa ya Miguu Yangu.” Baada ya miaka mingi ya ujuzi, muhtasari huo ukiwa umefanywa kuwa bora zaidi ulitangazwa katika 1983 katika kitabu Tumefanywa Tengenezo Tutimize Huduma Yetu.

Kukiwa na mpango kama huo, je, mahitaji ya watu waliokuwa na elimu ndogo rasmi yalifikiriwa?

Kuliweza Tatizo la Kutojua Kusoma na Kuandika

Katika 1957 Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi, na Tamaduni (UNESCO) lilikadiria kwamba karibu asilimia 44 ya idadi ya watu wa ulimwengu wenye miaka 15 au zaidi hawangeweza kusoma au kuandika. Iliripotiwa kwamba katika nchi 42 barani Afrika, 2 katika mabara ya Amerika, 28 katika Asia, na 4 katika Visiwa vya Bahari, asilimia 75 ya watu wazima walikuwa hawawezi kusoma au kuandika. Hata hivyo, wao pia walihitaji fursa ya kujifunza sheria ya Mungu ili waweze kujitayarisha kuwa raia za Ufalme wake. Wengi ambao hawangeweza kusoma walikuwa na akili chapuchapu (nyepesi) na wangeweza kukumbuka mengi ya yale waliyosikia, lakini bado hawangeweza kujisomea wenyewe Neno la Mungu lenye thamani na kutumia misaada iliyochapwa ya kujifunza Biblia.

Kwa miaka mingi Mashahidi mmoja-mmoja walikuwa wametoa msaada wa kibinafsi kwa watu waliotaka kujifunza kusoma. Hata hivyo, katika 1949 na 1950, Masomo ya kujifunza kusoma na kuandika yalianzishwa na Mashahidi wa Yehova katika kila moja la makutaniko yao katika nchi nyingi za Afrika. Kwa kawaida masomo hayo yaliongozwa katika Majumba ya Ufalme, na katika sehemu fulani kijiji kizima kilialikwa kijinufaishe na programu hiyo.

Mahali ambapo serikali ilikuwa ikidhamini programu za kujifunza kusoma na kuandika, Mashahidi wa Yehova walishirikiana kwa furaha na mpango huo. Hata hivyo, katika maeneo mengi, ilikuwa lazima Mashahidi wafanyize na kutumia vitabu vyao wenyewe vya mafundisho. Makumi ya maelfu ya watu, kutia na maelfu ya wanawake na watu wa umri mkubwa, wamesaidiwa kujua kusoma na kuandika kupitia masomo yaliyoongozwa na Mashahidi wa Yehova. Kama tokeo la namna mtaala ulivyobuniwa, si kwamba tu wamejifunza kusoma na kuandika bali pia wakati uleule wamefahamu kweli za msingi kutoka Neno Takatifu la Mungu. Jambo hilo limewawezesha kustahili kushiriki katika kazi ya kufanya wanafunzi aliyoiamuru Yesu. Tamaa ya kufanya hivyo kwa mafanikio imesukuma wengi wajitahidi sana kujifunza kusoma.

Wakati Shahidi mpya katika Dahomey (sasa ni Benin), Afrika Magharibi, alipofukuzwa na mwenye nyumba kwa sababu Shahidi huyo hakuweza kusoma, Shahidi huyo aliazimia kushinda tatizo hilo. Kuongezea kuhudhuria masomo ya kujifunza kusoma na kuandika, alijitahidi yeye binafsi. Majuma sita baadaye alitembelea mwenye nyumba yuleyule; mwanamume huyo alishangaa sana kusikia mtu huyo, ambaye muda mfupi sana uliopita alikuwa hajui kusoma na kuandika, akimsomea Neno la Mungu hivi kwamba yeye pia alionyesha kupendezwa na yale ambayo Shahidi huyo alikuwa akifundisha. Baadhi ya wale waliopewa maagizo katika masomo hayo ya kujifunza kusoma na kuandika, baada ya wakati, hata wamekuwa waangalizi wasafirio, wakiwa na idadi fulani ya makutaniko ya kufundisha. Ndivyo ilivyokuwa kwa Ezekiel Ovbiagele katika Nigeria.

Kufundisha kwa Njia ya Sinema na Maonyesho ya Slaidi

Ili kusaidia wale waliokuwa wakionyesha kupendezwa na Biblia wajue ukubwa wa tengenezo la Yehova lionekanalo, sinema ilitolewa katika 1954. Sinema hiyo, The New World Society in Action, ilisaidia pia kuondoa chuki ya kijamii kuelekea Mashahidi wa Yehova.

Katika ile ambayo sasa ni Zambia, jenereta yenye kuchukulika ilihitajiwa mara nyingi ili kuonyesha sinema hiyo. Kitambaa cheupe kilichofungwa kati ya miti miwili kilitumika kuwa kiwambo. Katika Mkoa wa Barotse, chifu mkuu alitazama sinema hiyo pamoja na familia yake ya kifalme, kisha akataka ionyeshwe kwa umma. Kama tokeo, jioni iliyofuata watu 2,500 wakaiona. Jumla ya hudhurio la maonyesho ya sinema hiyo katika Zambia kwa kipindi cha miaka 17 ilizidi milioni moja. Wale waliohudhuria walisisimuliwa na yale waliyoona. Kutoka Tanganyika ya karibu (sasa ni sehemu ya Tanzania), iliripotiwa kwamba baada ya sinema hiyo kuonyeshwa, hewa ilijaa vifijo vya umati, “Ndaka, ndaka” (Asante, asante).

Baada ya sinema The New World Society in Action, sinema nyinginezo zilifuata: The Happiness of the New World Society, Proclaiming “Everlasting Good News” Around the World, God Cannot Lie, na Heritage. Kumekuwa pia maonyesho ya slaidi, pamoja na maelezo, juu ya faida yenye kutumika ya Biblia katika nyakati zetu, mashina ya kipagani ya mafundisho na mazoea ya Jumuiya ya Wakristo, na maana ya hali za ulimwengu kwa msaada wa unabii wa Biblia, pamoja na maonyesho ya slaidi kuhusu Mashahidi wa Yehova wakiwa tengenezo, yakionyesha ziara kwenye makao yao makuu ya ulimwengu, mikusanyiko yenye kusisimua katika nchi ambako walikuwa wamepigwa marufuku hapo kwanza, na pitio la historia yao ya kisasa. Maonyesho hayo yote yamesaidia watu kujua kwamba kwelikweli Yehova ana watu duniani na kwamba Biblia ni Neno Lake lililopuliziwa roho.

Kuwatambua Kondoo wa Kweli

Katika nchi fulani, watu waliokuwa tu na baadhi ya vichapo vya Watch Tower walidai kuwa Mashahidi wa Yehova au walitumia jina Watch Tower. Lakini je, walikuwa wamebadili imani na njia yao ya maisha vipatane na viwango vya Biblia? Wakipewa maagizo yaliyohitajiwa, je, wangethibitika kuwa watu wa mfano wa kondoo kwelikweli watiio sauti ya Bwana-Mkubwa, Yesu Kristo?—Yn. 10:4, 5.

Barua yenye kugutusha ilipokewa kwenye ofisi ya tawi ya Watch Tower Society ya Afrika Kusini, katika 1954, kutoka kwa kikundi cha Waafrika katika Baía dos Tigres, gereza katika kusini mwa Angola. Mwandikaji, João Mancoca, alisema hivi: “Kikundi cha Mashahidi wa Yehova katika Angola kina washiriki 1,000. Hao wana Simão Gonçalves Toco akiwa kiongozi wao.” Toco alikuwa nani? Je, wafuasi wake walikuwa kwelikweli Mashahidi wa Yehova?

Mipango ilifanywa ili John Cooke, mishonari awezaye kusema Kireno, azuru Angola. Baada ya mahoji marefu pamoja na ofisa wa kikoloni, Ndugu Cooke aliruhusiwa amtembelee Mancoca. Ndugu Cooke alipata kujua kwamba katika miaka ya 1940, wakati Toco aliposhirikiana na misheni ya Baptisti katika Kongo ya Ubelgiji (sasa ni Zaire), alikuwa amepata baadhi ya fasihi za Watch Tower na alikuwa ameshiriki na washirika wake wa karibu yale aliyojifunza. Lakini, wawasiliani na roho wakawa na uvutano juu ya kikundi hicho, na baada ya wakati, Toco aliacha kabisa kutumia fasihi za Watch Tower na Biblia. Badala ya hivyo, yeye alitafuta mwelekezo kupitia wachawi. Wafuasi wake walirudishwa Angola na serikali na kisha wakatawanywa katika sehemu mbalimbali za nchi.

Mancoca alikuwa amekuwa mmoja wa washiriki wa Toco, lakini Mancoca alijaribu kushawishi wengine waache zoea la kuwasiliana na roho na washikamane na Biblia. Baadhi ya wafuasi wa Toco hawakupenda jambo hilo na walishtaki Mancoca kwa wenye mamlaka Wareno kwa kutumia mashtaka bandia. Kama tokeo, Mancoca na wale walioshiriki maoni yake walipelekwa gerezani. Kutoka humo aliwasiliana na Watch Tower Society na kupata fasihi zaidi za Biblia. Alikuwa mnyenyekevu, mwenye kufikiria mambo kiroho, na mwenye kupendezwa sana na kufanya kazi karibukaribu na tengenezo ambalo kupitia kwalo alikuwa amejifunza kweli. Baada ya Ndugu Cooke kutumia saa nyingi akizungumza kweli za Biblia na kikundi hicho, hakukuwa na shaka akilini mwake kwamba João Mancoca alikuwa kwelikweli mmoja wa kondoo za Bwana. Kujapokuwa hali ngumu sana, Ndugu Mancoca amethibitisha jambo hilo kwa miaka mingi sasa.

Mahoji yalifanywa pia pamoja na Toco na baadhi ya wafuasi wake. Hata hivyo, isipokuwa wachache, wao hawakuonyesha ithibati ya zile sifa za kiroho za wafuasi wa Kristo. Hivyo, wakati huo, hakukuwa na Mashahidi wa Yehova 1,000 katika Angola bali kama 25 tu.

Wakati huohuo, katika Kongo ya Ubelgiji (sasa ni Zaire), mvurugo mwingine wa utambulisho ulitukia. Kulikuwa harakati ya kidini na kisiasa iliyoitwa Kitawala, ambayo nyakati nyingine ilitumia jina Watch Tower. Katika makao ya baadhi ya washiriki wayo vilipatikana vichapo vya Mashahidi wa Yehova, walivyokuwa wamepokea kwa posta. Lakini imani na mazoea ya Kitawala (kutia na ubaguzi wa rangi, kupindua mamlaka ili kuleta mabadiliko ya kisiasa au ya kijamii, na ukosefu mbaya sana wa adili ya ngono kwa kusingizia ibada) hayakuwakilisha hata kidogo yale ya Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, ripoti fulani zilizotangazwa zilijaribu kuhusianisha Watch Tower Society ya Mashahidi wa Yehova na Kitawala.

Jitihada za mara kwa mara za Mashahidi wa Yehova kupeleka wasimamizi waliozoezwa katika nchi hizo zilikataliwa na maofisa Wabelgiji. Vikundi vya Katoliki na Protestanti vilifurahi. Hasa kuanzia 1949 na kuendelea, hatua zenye ukatili za kukandamiza zilichukuliwa dhidi ya wale katika Kongo ya Ubelgiji waliojaribu kujifunza Biblia kwa msaada wa fasihi za Watch Tower. Lakini ilikuwa kama vile mmoja wa wale Mashahidi waaminifu humo alivyosema: “Sisi ni kama gunia la mahindi ya Afrika. Popote watupelekapo, Neno litaanguka, moja moja, mpaka wakati ambapo mvua itakuja, nao watatuona tumeinuka kila mahali.” Na ndivyo ikawa kwamba chini ya hali ngumu, kuanzia 1949 hadi 1960, idadi iliyoripoti utendaji wakiwa Mashahidi wa Yehova iliongezeka kutoka 48 kufika 1,528.

Hatua kwa hatua maofisa wakapata kujua kwamba Mashahidi wa Yehova ni tofauti sana na Kitawala. Mashahidi walipopewa uhuru wa kukusanyika, watazamaji wa serikali walitaja mara nyingi juu ya mwenendo wao mzuri na utaratibu. Wakati kulipokuwa na maandamano yenye jeuri ya kudai uhuru wa kisiasa, watu walijua kwamba Mashahidi wa Yehova hawakuhusika. Katika 1961 msimamizi Shahidi aliyestahili, Ernest Heuse, Jr., kutoka Ubelgiji, hatimaye aliweza kuingia nchini. Kwa bidii nyingi yenye kuendelea, iliwezekana kusaidia akina ndugu hatua kwa hatua wapatanishe kwa ukamili zaidi makutaniko na maisha yao na Neno la Mungu. Kulikuwa mengi ya kujifunza, na ilitaka saburi nyingi.

Wakifikiri kwamba wangejipatia kibali, washiriki wa Kitawala kutoka maeneo fulani walipeleka orodha ndefu ya watu wao waliotaka kutambuliwa kuwa Mashahidi wa Yehova. Kwa hekima, Ndugu Heuse alituma ndugu wenye kustahili kwenye maeneo hayo wapate kujua walikuwa watu wa namna gani. Badala ya kukubali vikundi vikubwa, waliongoza mafunzo ya Biblia na watu mmoja-mmoja.

Baada ya wakati, kondoo wa kweli, wale waliomtegemea Yesu Kristo kwelikweli kuwa Mchungaji wao, wakadhihirika. Na kulikuwa wengi wao. Wao nao, walifundisha wengine. Kwa muda wa miaka iliyopita, makumi ya wamishonari wa Watch Tower kutoka ng’ambo walikuja kufanya kazi pamoja nao, kuwasaidia wapate ujuzi sahihi zaidi wa Neno la Mungu na kuandaa mazoezi yaliyohitajiwa. Kufikia 1975, kulikuwa Mashahidi wa Yehova 17,477 katika Zaire, waliopangwa kitengenezo katika makutaniko 526, wakiwa na shughuli nyingi wakihubiri na kufundisha wengine Neno la Mungu.

Kuvunja Nguvu za Hirizi

Upande wa magharibi mwa Nigeria iko nchi ya Benin (hapo kwanza ilijulikana kuwa Dahomey), yenye idadi ya watu waliogawanyika katika vikundi 60 vya kikabila visemavyo lugha na lahaja zipatazo 50. Kama ilivyo katika sehemu kubwa ya Afrika, kuabudu viumbe ndiyo dini ya kimapokeo, nayo huambatana na ibada ya mababu waliokufa. Mazingira ya kidini kama hayo husumbua maisha za watu kwa ushirikina na hofu. Wengi wadaio kuwa Wakristo huzoea pia ibada ya viumbe.

Tokea miaka ya mwishoni-mwishoni ya 1920 hadi miaka ya 1940, Mashahidi wa Yehova kutoka Nigeria walitawanya mbegu nyingi za kweli ya Biblia katika Dahomey kwa ziara za pindi kwa pindi ili kugawanya fasihi za Biblia. Nyingi kati ya mbegu hizo zilitaka kumwagiliwa maji kidogo tu ndipo zipate kuzaa. Utunzi huo ulitolewa katika 1948 wakati Nouru Akintoundé, mkazi wa Dahomey aliyekuwa akiishi Nigeria aliporudi Dahomey ili kupainia. Katika muda wa miezi minne, watu 300 waliitikia kweli upesi na kushiriki pamoja naye katika utumishi wa shambani. Itikio hilo lilizidi sana mataraja yote ya kiakili.

Kama tokeo la utendaji huo, msukosuko ulitokea upesi si miongoni mwa makasisi wa Jumuiya ya Wakristo tu bali pia miongoni mwa waabuduo viumbe. Wakati sekretari wa makao ya watawa ya hirizi katika Porto-Novo alipoonyesha kupendezwa na kweli, mkuu wa hirizi alisema kwamba sekretari huyo angekufa katika muda wa siku saba. Lakini huyo aliyekuwa hapo kwanza sekretari wa kao la watawa alijibu kwa imara hivi: “Ikiwa ni hirizi iliyomuumba Yehova, basi nitakufa; lakini ikiwa Yehova ndiye Mungu mkuu zaidi, basi yeye atakomesha hirizi.” (Linganisha Kumbukumbu la Torati 4:35; Yohana 17:3.) Ili kufanya matabiri yake yatimie, katika usiku wa siku ya sita, mkuu wa hirizi alishiriki katika namna zote za uchawi kisha akatangaza kwamba huyo aliyekuwa hapo kwanza sekretari wa kao la watawa amekufa. Hata hivyo, kulikuwa mshangao mkubwa miongoni mwa waabudu wa hirizi kesho yake wakati mwanamke huyo alipokuja sokoni katika Cotonou akiwa hai kabisa. Baadaye, ndugu mmoja alikodi gari na kumchukua kupitia Porto-Novo ili wote waweze kujionea wenyewe kwamba alikuwa hai. Kufuatia jambo hilo, waabudu wengine wengi wa hirizi walichukua msimamo imara kwa ajili ya kweli.—Linganisha Yeremia 10:5.

Upesi, kama tokeo la mkazo mwingi wa kidini, vichapo vya Watch Tower vilipigwa marufuku katika Dahomey. Lakini, kwa kumtii Yehova Mungu, Mashahidi waliendelea kuhubiri, mara nyingi kwa kutumia Biblia tu. Nyakati nyingine walikuwa wakishiriki kazi ya nyumba hadi nyumba wakiwa kama “wachuuzi,” wakiwa na bidhaa za aina zote. Ikiwa mazungumzo yalifanikiwa, walikuwa wakigeuza fikira kwenye Biblia, na hata huenda wakatoa kutoka ndani ya mfuko mkubwa wa nguo yao fasihi za Biblia zenye thamani kubwa.

Wakati polisi walipowasumbua sana katika majiji, basi walikuwa wakihubiri katika maeneo ya mashambani. (Linganisha Mathayo 10:23.) Na walipotupwa gerezani, walihubiri humo. Katika 1955, Mashahidi waliokuwa gerezani walipata angalau watu 18 wenye kupendezwa miongoni mwa wafungwa na maofisa wa gereza katika Abomey.

Katika muda wa mwongo mmoja tu baada ya yule ndugu painia Mdahomey kurudi kwenye nchi yao ili kuhubiri, kulikuwa 1,426 waliokuwa wakishiriki katika huduma—kazi yao ijapopigwa marufuku na serikali!

Wafanyakazi Zaidi Washiriki Katika Mavuno

Ilikuwa wazi kwamba kulikuwa watu wengi kotekote barani Afrika waliokuwa wakiona njaa ya kweli. Mavuno yalikuwa mengi, lakini wafanyakazi walikuwa wachache. Kwa hiyo, ilitia akina ndugu moyo kuona jinsi Bwana-Mkubwa wa mavuno, Yehova Mungu, alivyojibu sala zao kwa ajili ya wafanyakazi zaidi ili kusaidia katika mkusanyo wa kiroho.—Mt. 9:37, 38.

Fasihi nyingi ilikuwa imeangushwa nchini Kenya katika miaka ya 1930 na mapainia wasafirio, lakini kulikuwa na kazi ndogo sana ya kufuatia. Hata hivyo, katika 1949, Mary Whittington, akiwa na watoto wake watatu wachanga, alihama kutoka Uingereza ili aishi Nairobi pamoja na mume wake, aliyekuwa ameajiriwa kazi huko. Dada Whittington alikuwa amebatizwa mwaka mmoja hivi uliopita, lakini alikuwa na roho ya painia. Ingawa hakujua Shahidi mwingine yeyote katika Kenya, alianza kusaidia wengine katika eneo hilo kubwa wajifunze kweli. Vijapokuwa vizuizi, yeye hakuacha. Mashahidi wengine walikuja pia—kutoka Afrika Kusini, Australia, Kanada, Marekani, Sweden, Uingereza, na Zambia—wakipanga binafsi kuhamia huko ili kushiriki tumaini la Ufalme pamoja na watu.

Kwa kuongezea, waume na wake wamishonari walitumwa kusaidia kazi ya kuvuna. Mwanzoni wanaume waliwajibika kufanya kazi ya kimwili ili wakae nchini, na hivyo walikuwa na wakati mdogo tu kwa ajili ya huduma. Lakini wake zao walikuwa huru kutumikia wakiwa mapainia. Baada ya wakati, zaidi ya wamishonari mia moja waliozoezwa Gileadi walikuja Kenya. Wakati uhuru ulipokaribia, ukikomesha ubaguzi wa rangi uliokuwa umelazimishwa na utawala wa kikoloni wa Uingereza, Mashahidi wa Ulaya walijifunza Kiswahili na upesi wakapanua utendaji wao kufikia Waafrika wenyeji. Idadi ya Mashahidi katika sehemu hii ya shamba la duniani pote ikakua upesi.

Katika 1972, Botswana pia ilipokea msaada katika kazi ya mavuno ya kiroho wakati Mashahidi kutoka Afrika Kusini, Kenya na Uingereza walipohamia majiji yayo makubwa zaidi. Miaka mitatu baadaye, wamishonari waliozoezwa Gileadi walikuja pia. Hata hivyo, kwa kadiri iliyo kubwa, idadi ya watu imetawanyika katika vijiji vya sehemu za mashambani. Ili kuwafikia, Mashahidi kutoka Afrika Kusini wamesafiri kuvuka ile sehemu ya jangwa iitwayo Kalahari. Katika jamii zilizo peke yazo, wametoa ushahidi kwa mkuu wa kijiji, walimu wa shule, na mara nyingi kwa vikundi vya wasikilizaji 10 au 20 wenye kuthamini. Mwanamume mmoja wa umri mkubwa alisema hivi: “Mlisafiri njia hiyo yote ili kuja kutuambia mambo hayo? Hiyo ni fadhili, fadhili sana.”

“Bible Brown” alikuwa ametoa hotuba za Biblia zenye nguvu katika Liberia wakati wa miaka ya 1920, lakini kulikuwa upinzani mwingi. Kazi ya kuvuna kiroho huko kwa kweli haikufanya maendeleo mpaka walipowasili wamishonari waliozoezwa kwenye Shule ya Gileadi. Harry Behannan, aliyekuja katika 1946, alikuwa ndiye wa kwanza. Wengi zaidi walishiriki katika miaka iliyofuata. Waliberia wenyeji walijiunga nao hatua kwa hatua katika kazi na kufikia 1975 idadi ya wasifaji wa Yehova ilizidi elfu moja.

Kazi ya kuhubiri hata zaidi ilikuwa imefanywa na “Bible Brown” katika Nigeria. Hilo lilikuwa taifa lililogawanyika kuwa falme nyingi, majiji ya majimbo, na mifumo ya kijamii, watu wakisema zaidi ya lugha na lahaja 250. Dini ilikuwa sababu nyingine ya migawanyiko. Wakiwa bila busara lakini wakiwa na hoja za Kimaandiko zenye nguvu, Mashahidi wa mapema huko walifunua makasisi na mafundisho yao bandia. Wakati fasihi zao zilipopigwa marufuku wakati wa Vita ya Ulimwengu 2, ndugu walihubiri kwa kutumia Biblia pekee. Watu waliopenda kweli waliitikia kwa uthamini. Waliacha makanisa, halafu wakaacha zoea la kuwa na wake wengi na kuachana na uchawi, mambo ambayo makanisa yalikuwa yamekubali. Kufikia 1950 idadi ya Mashahidi wa Yehova waliokuwa wakishiriki katika kupiga mbiu ya ujumbe wa Ufalme katika Nigeria ilikuwa 8,370. Kufikia 1970, kulikuwa zaidi ya mara kumi ya idadi hiyo.

Ilikuwa lazima vizuizi vya kisheria vyenye kuendelea vishindwe ili kutoa msaada wa kiroho kwa wenye kupendezwa katika Rhodesia Kusini (sasa inajulikana kuwa Zimbabwe). Jitihada za kupata utambulisho wa kisheria zilikuwa zimeanza katika miaka ya katikati ya 1920. Katika 1932, mapainia kutoka Afrika Kusini waliamriwa waondoke nchini nao waliambiwa kimabavu kwamba hakuna rufani ingeweza kukatwa. Hata hivyo walikata rufani. Mashtaka kwamba fasihi za Watch Tower zilikuwa ni za uhaini yalikuwa lazima yashughulikiwe mahakamani. Katika miaka ya mapema ya 1940, ndugu walitiwa gerezani kwa sababu waligawanya vichapo vilivyoeleza Biblia. Haikuwa mpaka 1966 kwamba Mashahidi wa Yehova wakapewa utambulisho kamili wa kisheria wakiwa tengenezo la kidini katika Zimbabwe. Kwa zaidi ya miaka 40, kazi ya kuvuna ya kiroho ilikuwa imefanywa chini ya magumu mengi, lakini wakati wa pindi hiyo wafanyakazi wajasiri walikuwa wamesaidia zaidi ya watu 11,000 wawe watumishi wa Yehova Mungu.

Kutoa Ushahidi kwa Magavana na Wafalme

Yesu alijua kwamba wanafunzi wake wangekabiliana na upinzani katika huduma yao. Aliwaambia kwamba wangepelekwa mbele ya “mahakama za mahali,” hata mbele ya “magavana na wafalme,” na kwamba hiyo ingekuwa “kuwa ushahidi kwao na kwa mataifa.” (Mt. 10:17, 18, NW) Mashahidi wa Yehova wamepatwa barabara na yale ambayo Yesu alitabiri, na kupatana na yale aliyosema, wamejaribu kutumia fursa hiyo kutoa ushahidi.

Baadhi ya maofisa wameruhusu hofu iwazuie kuwatendea mema wafuasi wa Kristo. (Yn. 12:42, 43) Llewelyn Phillips aliona ithibati ya jambo hilo katika 1948 wakati alipokuwa na mahoji ya faragha na idadi fulani ya maofisa wa serikali katika Kongo ya Ubelgiji, kwa kusudi la kuleta kitulizo kwa Mashahidi wenye kunyanyaswa huko. Aliwaeleza wanaume hao imani na utendaji wa Mashahidi wa Yehova. Lakini wakati wa mahoji, gavana mkuu aliuliza kwa huzuni hivi: “Na nikiwasaidia, itakuwaje kwangu?” Alijua kwamba Kanisa la Katoliki ya Roma lilikuwa na uvutano mwingi katika nchi hiyo.

Hata hivyo, chifu mkuu wa taifa la Swazi, Mfalme Sobhuza 2, hakuhangaikia sana maoni ya makasisi. Yeye alikuwa ameongea mara nyingi na Mashahidi wa Yehova, alikuwa na fasihi nyingi zao, naye alikuwa na mwelekeo wa fadhili kwao. Katika “Ijumaa Njema” kila mwaka, alikuwa akiwaalika makasisi Waafrika kwenye kraal (kijiji) yake ya kifalme. Alikuwa akiwaruhusu waongee, lakini pia alikuwa akimwita mmoja wa Mashahidi wa Yehova aseme. Katika 1956 Shahidi mmoja alisema juu ya fundisho la kutokufa kwa nafsi na majina ya cheo ya viongozi wa kidini. Alipomaliza, chifu mkuu aliwauliza makasisi: “Je, haya yanayosemwa hapa na mashahidi wa Yehova ni ya kweli au ni ya bandia? Ikiwa ni ya bandia, eleza jinsi gani.” Hawangeweza kuyakanusha. Katika pindi moja chifu mkuu hata aliangua kicheko kwa kuona makasisi wakishangaa juu ya yale yaliyosemwa na Shahidi mmoja.

Polisi ndio mara nyingi waliotumwa kutaka kujua kutoka kwa Mashahidi sababu za yale waliyokuwa wakifanya. Kutoka kutaniko katika Tangier, Moroko, Mashahidi walifanya safari za ukawaida kwenda Ceuta, bandari moja chini ya udhibiti wa Hispania lakini ambayo ilikuwa kwenye pwani ya Moroko. Wakiwa wamesimamishwa na polisi katika pindi moja katika 1967, Mashahidi walihojiwa kwa saa mbili, wakati ambapo ushahidi mzuri ulitolewa. Kwenye pindi moja, mainspekta wawili wa polisi waliuliza kama Mashahidi waliamini katika “Bikira Maria.” Walipoambiwa kwamba masimulizi ya Gospeli huonyesha kwamba Maria alikuwa na watoto wengine baada ya kuzaliwa kwa Yesu na bikira, na kwamba hao walikuwa ndugu na dada wenye mzazi mmoja na Yesu, maofisa hao walitoa mtweto wa mshangao na kusema kwamba jambo kama hilo halingeweza kuwa katika Biblia. Walipoonyeshwa Yohana 7:3-5, mmojawapo wa maofisa hao aliitazama kwa muda mrefu bila kusema neno; hivyo yule mwingine akasema: “Nipe Biblia hiyo. Mimi nitalieleza andiko hilo!” Yule ofisa wa kwanza akajibu: “Usijisumbue. Andiko hili li wazi sana.” Maswali mengine mengi yaliulizwa na kujibiwa katika hali ya starehe. Baada ya hapo, Mashahidi hawakuingiliwa sana na wenye mamlaka walipokuwa wakihubiri katika eneo hilo.

Wanaume mashuhuri katika serikali wamepata kufahamiana sana na Mashahidi wa Yehova na huduma yao. Baadhi yao huthamini kwamba kazi ifanywayo na Mashahidi hunufaisha watu kikweli. Mwishoni-mwishoni mwa 1959, wakati matayarisho yalipokuwa yakifanywa kwa ajili ya uhuru wa Nigeria, gavana mkuu, Dakt. Nnamdi Azikiwe, aliomba kwamba W. R. Brown awepo akiwa mwakilishi wa Mashahidi wa Yehova. Aliliambia Baraza lake la Mawaziri: “Kama madhehebu yote ya kidini yangekuwa kama mashahidi wa Yehova, hatungekuwa na mauaji ya kukusudia, uvunjaji wa nyumba, utundu wa watoto, wafungwa na mabomu ya atomu. Milango haingefungwa daima.”

Vuno kubwa kwelikweli la kiroho lilikuwa likikusanywa barani Afrika. Kufikia 1975, kulikuwa Mashahidi 312,754 wakihubiri habari njema katika nchi 44 katika bara la Afrika. Katika tisa kati ya nchi hizo, kulikuwa wachache kuliko 50 waliokuwa wakichukua msimamo kwa ajili ya kweli ya Biblia na kushiriki katika kazi ya kueneza evanjeli. Lakini Mashahidi huona maisha ya kila mmoja wao kuwa yenye thamani kubwa. Katika 19 kati ya nchi hizo, wale walioshiriki katika huduma ya nyumba hadi nyumba wakiwa Mashahidi wa Yehova walikuwa maelfu. Maongezeko yenye kutokeza yaliripotiwa katika maeneo fulani. Kwa kielelezo, katika Angola, kutoka 1970 kufika 1975, idadi ya Mashahidi iliongezeka kutoka 355 kufika 3,055. Katika Nigeria, katika 1975, kulikuwa Mashahidi wa Yehova 112,164. Hao hawakuwa watu waliofurahia kusoma tu fasihi za Watch Tower, wala hawakuwa wale ambao huenda wakahudhuria mikutano pindi kwa pindi kwenye Jumba la Ufalme. Wote walikuwa wapiga-mbiu wa Ufalme wa Mungu wenye bidii.

Nchi za Mashariki Yatoa Wasifaji wa Yehova

Kama ilivyokuwa katika sehemu nyinginezo nyingi, utendaji wa Mashahidi wa Yehova katika Filipino ulipanuka kwa kasi baada ya Vita ya Ulimwengu 2. Upesi kadiri ilivyowezekana baada ya kufunguliwa kwake kutoka gerezani katika Machi 13, 1945, Joseph Dos Santos aliwasiliana na ofisi ya Watch Tower Society katika New York. Alitaka kupata habari yote ya funzo la Biblia na maagizo ya kitengenezo ambayo akina ndugu katika Filipino walikuwa wamekosa wakati wa vita. Kisha akatembelea kibinafsi makutaniko ili kuyaunganisha na kuyaimarisha. Mwaka huohuo mkusanyiko wa kitaifa ulifanywa katika Lingayen, mkoa wa Pangasinan, ambapo maagizo yalitolewa juu ya jinsi ya kufundisha watu wenye njaa ya kweli kwa njia ya mafunzo ya Biblia nyumbani. Katika miaka iliyofuata jitihada kubwa ilifanywa ya kutafsiri na kuchapa habari zaidi katika lugha za wenyeji—Tagalog, Iloko, na Cebuano. Msingi ulikuwa ukiwekwa kwa ajili ya mpanuko, nao ulikuja upesi.

Katika muda wa mwongo mmoja baada ya vita kwisha, idadi ya Mashahidi katika Filipino iliongezeka kutoka kama 2,000 kufika zaidi ya 24,000. Katika muda wa miaka mingine 20, kulikuwa zaidi ya wasifaji wa Yehova 78,000 huko.

Miongoni mwa nchi za Mashariki za kwanza kupelekewa wamishonari waliozoezwa kwenye Shule ya Gileadi ilikuwa China. Harold King na Stanley Jones waliwasili katika Shanghai katika 1947; Lew Ti Himm, katika 1949. Wale mapainia watatu Wajerumani waliokuwa wameanza kazi huko katika 1939 walikuwapo ili kuwalaki. Hii ilikuwa nchi ambayo wengi kati ya watu walikuwa Wabuddha nao hawakuitikia upesi mazungumzo ya Biblia. Ndani ya makao yao mlikuwamo vihekalu na madhabahu. Vioo vikiwa vinaning’inia milangoni, walijaribu kufukuzia mbali roho waovu. Vibandiko vyekundu vyenye semi za ‘bahati njema’ na picha za miungu ya Kibuddha yenye kuogofya vilipamba malango. Lakini hiyo ilikuwa miaka ya mabadiliko makubwa katika China. Chini ya utawala wa Kikomunisti kila mtu alitakwa ajifunze ‘mawazo ya Mao Tse-tung.’ Baada ya kazi ya kimwili, walitakiwa wahudhurie vipindi virefu ambamo Ukomunisti ulifafanuliwa. Katikati ya hayo yote, ndugu zetu waliendelea kuhubiri kwa bidii habari njema za Ufalme wa Mungu.

Wengi kati ya wale waliokuwa na nia ya kujifunza na Mashahidi wa Yehova walikuwa wameijua Biblia wakati uliopita kupitia makanisa ya Jumuiya ya Wakristo. Ndivyo ilivyokuwa kwa Nancy Yuen, mfanyakazi wa kanisa na mke nyumbani aliyekuwa mwenye shukrani kwa ajili ya yale ambayo Mashahidi walikuwa wamemwonyesha katika Biblia. Upesi alikuwa akishiriki kwa bidii katika kazi ya nyumba hadi nyumba na kuongoza mafunzo ya Biblia yeye mwenyewe. Wengine ambao waliwahubiria walikuwa wa malezi halisi ya Kichina na Kibuddha nao hawakutangulia kuwa na maarifa ya Biblia. Katika 1956 kilele cha wahubiri 57 kilifikiwa. Hata hivyo, mwaka huohuo, baada ya kukamatwa mara sita kwa ajili ya kuhubiri, Nancy Yuen alifungwa gerezani. Wengine ama walikamatwa ama walilazimishwa kuondoka nchini. Stanley Jones na Harold King walikamatwa katika Oktoba 14, 1958. Kabla ya kuletwa kuhukumiwa, walizuiliwa kwa miaka miwili, wakati ambapo walihojiwa daima. Wakati hatimaye walipopelekwa mahakamani katika 1960, walihukumiwa vipindi virefu vya kukaa gerezani. Hivyo, katika Oktoba 1958 utendaji wa hadharani wa Mashahidi wa Yehova katika China ulisimamishwa kwa nguvu. Lakini kazi yao ya kuhubiri haikukoma kabisa. Hata gerezani na katika kambi za kazi ngumu, kulikuwa njia za kutoa ushahidi. Katika wakati ujao je, mengi zaidi yangefanywa katika nchi hii kubwa? Hilo lingejulikana wakati uwadiapo.

Kwa sasa, ni nini lililokuwa likitukia katika Japani? Ni Mashahidi wa Yehova kama mia moja tu waliokuwa wakihubiri huko kabla ya vita ya ulimwengu ya pili. Walipokabiliwa na hatua za kinyama za kukandamiza wakati wa miaka ya vita, wengi wao waliridhiana. Ijapokuwa wachache walidumisha uaminifu-maadili wao, kazi ya kuhubiri hadharani iliyopangwa kitengenezo ilipata kusimama. Hata hivyo, kupiga mbiu ya Ufalme wa Yehova kulipewa mwanzo mpya katika sehemu hiyo ya ulimwengu wakati Don Haslett, mishonari aliyezoezwa Gileadi, alipowasili katika Tokyo katika Januari 1949. Miezi miwili baadaye, mke wake, Mabel, aliweza kuungana naye huko. Hili lilikuwa shamba ambamo wengi walikuwa na njaa ya kweli. Maliki alikuwa amekana dai lake la uungu. Ushinto, Ubuddha, Ukatoliki, na Kyodan (dini iliyofanyizwa kwa vikundi mbalimbali vya Protestanti katika Japani) zote zilikuwa zimepoteza heshima ya watu kwa sababu ya kuunga mkono jitihada za vita za Japani, zilizokuwa zimeishia katika ushinde.

Kufikia mwishoni mwa 1949, wamishonari 13 kutoka Shule ya Gileadi walikuwa wakishughulika katika Japani. Wengi zaidi wakafuata—jumla ya zaidi ya 160. Kulikuwa na fasihi kidogo sana ya kufanya kazi nayo. Baadhi ya wamishonari walikuwa wamesema Kijapani cha mtindo wa kale katika Hawaii, lakini ilikuwa lazima wajifunze lugha ya kisasa. Wale wengine walikuwa wamejifunza maneno machache ya msingi lakini walilazimika mara nyingi kuziendea kamusi zao za Kijapani-Kiingereza mpaka walipopata kufahamu vizuri zaidi lugha yao mpya. Kabla ya muda mrefu, familia za akina Ishii na Miura, ambao hawakuwa wameiacha imani yao wakati wa miaka ya vita, waliwasiliana na tengenezo na kwa mara nyingine tena wakaanza kushiriki katika huduma ya hadharani.

Makao ya wamishonari yaliendelea kufunguliwa katika Kobe, Nagoya, Osaka, Yokohama, Kyoto, na Sendai. Tokea 1949 hadi 1957, jitihada kuu ilikuwa kuanzisha kazi ya Ufalme katika ile miji mikubwa katika kisiwa kikuu cha Japani. Kisha wafanyakazi wakaanza kuhamia ile miji mingine. Shamba lilikuwa kubwa. Ilikuwa wazi kwamba ikiwa Japani yote ingepokea ushahidi kamili, wahudumu wengi mapainia wangehitajiwa. Hilo lilikaziwa, wengi wakajitokeza, na kulikuwa itikio zuri kwa jitihada zilizounganishwa za wahudumu hao wenye kufanya kazi kwa bidii! Ule mwongo wa kwanza ulizaa wasifaji wa Yehova 1,390. Kufikia miaka ya katikati ya 1970, kulikuwa wasifaji wa Yehova wenye bidii 33,480 waliotawanyika kotekote katika Japani. Na mwendo wa kukusanya ndani ulikuwa ukiongezeka.

Katika mwaka uleule aliowasili Don Haslett katika Japani, 1949, kazi ya Ufalme katika Jamhuri ya Korea ilipewa pia kichocheo kikubwa. Korea ilikuwa imekuwa chini ya utawala wa Japani wakati wa vita ya ulimwengu, nao Mashahidi walikuwa wamenyanyaswa kikatili. Ijapokuwa kikundi kidogo kilikuwa kikikutana kwa ajili ya funzo baada ya vita, hakukuwa na uwasiliano na tengenezo la kimataifa mpaka baada ya Choi Young-won kuona ripoti moja juu ya Mashahidi wa Yehova katika 1948 katika gazeti la habari la Jeshi la Amerika Stars and Stripes. Mwaka uliofuata kutaniko la wahubiri 12 lilifanyizwa katika Seoul. Baadaye mwakani Don na Earlene Steele, wamishonari wa kwanza kutoka Shule ya Gileadi, wakawasili. Miezi saba baadaye, wamishonari wengine sita walifuata.

Walikuwa wakipata matokeo mazuri sana—wastani wa mafunzo ya Biblia 20 kila mmoja na hudhurio la mikutano la wengi kufikia 336. Halafu Vita ya Korea ikaanza. Kabla ya miezi mitatu kwisha tangu kile kikundi cha mwisho cha wamishonari kuwasili, wote walihamishiwa Japani. Ilikuwa zaidi ya mwaka mmoja kabla Don Steele kuweza kurudi katika Seoul na mwaka mwingine kabla ya Earlene kuweza kujiunga naye. Wakati huohuo ndugu Wakorea waliendelea kuwa imara na walikuwa wamekuwa wenye bidii katika kuhubiri, ijapokuwa uhakika wa kwamba makao yalikuwa yameharibiwa na wengi wao walikuwa wakimbizi. Lakini sasa, kupigana kukiwa kumekwisha, fikira zilielekezwa katika kuandaa fasihi zaidi katika Kikorea. Mikusanyiko na mmiminiko zaidi wa wamishonari vilitoa kichocheo kwa kazi. Kufikia 1975, kulikuwa Mashahidi wa Yehova 32,693 katika Jamhuri ya Korea—wengi karibu kuwa kama wale waliokuwa katika Japani—na kulikuwa uwezekano wa ukuzi bora zaidi, kwa sababu mafunzo ya Biblia nyumbani zaidi ya 32,000 yalikuwa yakiongozwa.

Hali Ilikuwaje Katika Ulaya?

Mwisho wa Vita ya Ulimwengu 2 katika Ulaya haukutokeza uhuru kamili kwa Mashahidi wa Yehova huko ili kuendeleza kazi yao ya elimu ya Biblia bila kupingwa. Katika sehemu fulani maofisa waliwastahi kwa sababu ya msimamo wao imara wakati wa vita. Lakini sehemu nyinginezo mielekeo yenye nguvu ya utukuzo wa taifa na uhasama wa kidini vilitokeza mnyanyaso zaidi.

Miongoni mwa Mashahidi katika Ubelgiji walikuwamo wale waliokuwa wametoka Ujerumani kushiriki katika kuhubiri habari njema. Kwa sababu hawangeweza kuunga mkono utawala wa Nazi, Gestapo walikuwa wamewawinda kama hayawani mwitu. Lakini sasa maofisa Wabelgiji walishtaki baadhi ya Mashahidi haohao kuwa Wanazi na kuamuru watiwe gerezani na kisha wakawafukuza nchini. Yajapokuwa hayo yote, idadi ya Mashahidi waliokuwa wakishiriki katika huduma ya shambani katika Ubelgiji ilikuwa zaidi ya mara tatu katika muda wa miaka mitano baada ya vita.

Ni nini kilicholeta mnyanyaso mwingi? Kanisa la Katoliki ya Roma ndilo lililotokeza mnyanyaso ulio mwingi. Popote lilipokuwa na mamlaka ya kufanya hivyo, lilipiga vita bila kukoma ili kukomesha Mashahidi wa Yehova.

Wakijua kwamba watu wengi wa Magharibi walihofu Ukomunisti, makasisi Wakatoliki katika jiji la Ireland la Cork, katika 1948, walichochea upinzani dhidi ya Mashahidi wa Yehova kwa kuwarejezea daima kuwa “maibilisi Wakomunisti.” Kama tokeo, wakati Fred Metcalfe alipokuwa akishiriki katika huduma ya shambani, alikabiliwa na wafanyaghasia waliompigapiga ngumi na kumpiga mateke na kutawanya fasihi zake za Biblia barabarani. Kwa furaha, polisi mmoja alikuja wakati huohuo na kutawanya genge hilo. Yajapokuwa hayo yote, Mashahidi walistahimili. Si watu wa Ireland wote waliokubaliana na jeuri hiyo. Baadaye, hata baadhi ya wale waliokuwa wameishiriki jeuri hiyo waliona laiti hawangalifanya hivyo. Walio wengi kati ya Wakatoliki katika Ireland hawakuwa wameona Biblia. Lakini, kwa saburi ya upendo, baadhi yao walisaidiwa washike kweli iwekayo watu huru.—Yn. 8:32.

Ingawa Mashahidi katika Italia walikuwa na idadi ipatayo mia moja tu katika 1946, miaka mitatu baadaye kulikuwa makutaniko 64—madogo lakini yenye kufanya kazi kwa bidii. Makasisi walikuwa na wasiwasi. Wakishindwa kupinga kweli za Biblia walizohubiri Mashahidi wa Yehova, makasisi Wakatoliki walikaza wenye mamlaka wa serikali wajaribu kuwaondolea mbali. Hivyo, katika 1949, wamishonari walio Mashahidi waliamriwa waondoke nchini.

Kwa kurudiarudia makasisi wa Roma Katoliki walijaribu kukatiza au kuzuia makusanyiko ya Mashahidi katika Italia. Walitumia watu wenye kusumbua ili kukatiza kusanyiko katika Sulmona katika 1948. Katika Milan walimkaza mkuu wa polisi afute ruhusa ya kufanya mkusanyiko katika Teatro dell’Arte katika 1950. Tena, katika 1951, walitumia uvutano juu ya polisi wakafuta ruhusa ya kufanya kusanyiko katika Cerignola. Lakini katika 1957, wakati polisi walipoamuru mkusanyiko wa Mashahidi katika Milan ukomeshwe, vyombo vya habari vya Italia vilipinga, na maswali yalizushwa bungeni. Gazeti la habari la kila juma la Roma Il Mondo, la Julai 30, 1957, halikusita kutaarifu kwamba tendo hilo lilichukuliwa ili “kumridhisha askofu mkuu,” Giovanni Battista Montini, aliyepata baadaye kuwa Papa Paul wa 6. Ilijulikana vema kwamba kwa karne nyingi Kanisa Katoliki lilikuwa limekataza kuenezwa kwa Biblia katika lugha zitumiwazo na umma kwa ujumla. Lakini Mashahidi wa Yehova waliendelea kusaidia Wakatoliki wenye moyo mweupe wajionee wenyewe yaliyosemwa na Biblia. Tofauti kati ya Biblia na mafundisho yaliyoshikiliwa na kanisa bila msingi ilikuwa wazi. Zijapokuwa jitihada za Kanisa Katoliki za kuzuia hilo, maelfu walikuwa wakiacha kanisa, na kufikia 1975 kulikuwa Mashahidi wa Yehova 51,248 katika Italia. Wote hao walikuwa waeneza-evanjeli wenye bidii, na idadi yao ilikuwa ikiongezeka kasi.

Katika Hispania ya Katoliki, wakati utendaji wa Mashahidi wa Yehova uliopangwa kitengenezo ulipofufuliwa hatua kwa hatua baada ya 1946, haikushangaza kwamba makasisi huko pia walikaza maofisa wa serikali ili kujaribu kuwakomesha. Mikutano ya kutaniko ya Mashahidi wa Yehova ilikatizwa. Wamishonari walilazimishwa kuondoka nchini. Mashahidi walikuwa wakikamatwa kwa kuwa tu na Biblia au fasihi za Biblia. Mara nyingi walizuiwa katika magereza machafumachafu kwa muda kama wa siku tatu, kisha kuachiliwa—ili tu kukamatwa tena, kuhojiwa, na kutiwa gerezani. Wengi walitumikia vifungo vya mwezi au zaidi. Mapadri waliwahimiza wenye mamlaka wa serikali wawinde yeyote aliyekuwa akijifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Hata baada ya Sheria ya Uhuru wa Kidini kupitishwa katika 1967, mabadiliko yalikuja hatua kwa hatua. Hata hivyo, kufikia wakati Mashahidi wa Yehova walipopewa utambulisho wa kisheria hatimaye katika 1970, kulikuwako tayari zaidi ya 11,000 yao katika Hispania. Na miaka mitano baadaye, walikuwa zaidi ya 30,000, kila mmoja wao akiwa mweneza-evanjeli mwenye bidii.

Vipi Ureno? Huko pia, wamishonari waliamriwa waondoke nchini. Wakihimizwa na makasisi Wakatoliki, polisi walipekuapekua makao ya Mashahidi wa Yehova, wakawanyang’anya fasihi zao, na kukatiza mikutano yao. Katika Januari 1963 kamanda wa Polisi wa Usalama wa Umma katika Caldas da Rainha hata alitoa amri iliyoandikwa akiwakataza ‘wasifanye utendaji wao wa kusoma Biblia.’ Lakini Mashahidi hawakuachia mbali utumishi wao kwa Mungu. Kulikuwa zaidi ya 13,000 kufikia wakati walipopata utambulisho wa kisheria katika Ureno katika 1974.

Katika sehemu nyingine za Ulaya, wenye mamlaka wa serikali walizusha vizuizi kwa kazi ya kuhubiri habari njema kwa kuuona ugawanyaji wa fasihi za Biblia kuwa ni utendaji wa kibiashara, ulio chini ya sheria za kibiashara. Katika majimbo kadhaa ya Uswisi, sheria za uchuuzi zilitumiwa kuhusu ugawanyaji wa fasihi za Mashahidi wa Yehova kwa mchango wa hiari. Mashahidi walipokuwa wakiendesha utendaji wao, walikuwa wakikamatwa mara nyingi na hatua za mahakama kuchukuliwa. Hata hivyo, wakati kesi hizo zilipoletwa mahakamani, mahakama fulani, kutia na Mahakama Kuu ya jimbo la Vaud, katika 1953, zilikata kauli kwamba utendaji wa Mashahidi wa Yehova haungeweza kwa kufaa kuonwa kuwa uchuuzi. Wakati huohuo, katika Denmark jitihada zilifanywa kupunguza saa ambazo katika hizo Mashahidi wangeweza kutoa fasihi zao, utendaji wao ukiwekewa mipaka uendeshwe katika nyakati zile zilizoruhusiwa na sheria kuendesha maduka ya kibiashara. Ilikuwa lazima pia kupigania jambo hilo mahakamani. Vijapokuwa vizuizi, Mashahidi wa Yehova waliendelea kupiga mbiu ya Ufalme wa Mungu kuwa tumaini pekee la wanadamu.

Suala jingine lililohusu Mashahidi wa Yehova katika Ulaya, pamoja na sehemu nyingine za dunia, ni kutokuwamo kwa Kikristo. Kwa sababu dhamiri zao za Kikristo hazingewaruhusu kujihusisha katika mapambano kati ya wenye kuzozana wa ulimwengu, walihukumiwa kufungwa gerezani katika nchi moja baada ya nyingine. (Isa. 2:2-4) Jambo hilo liliwatoa vijana kwenye huduma yao ya kawaida ya nyumba hadi nyumba. Lakini tokeo moja lenye manufaa lilikuwa ule ushahidi mwingi uliotolewa kwa wanasheria, mahakimu, maofisa wa kijeshi, na walinzi wa gereza. Hata wakiwa gerezani Mashahidi walipata njia fulani za kuhubiri. Ijapokuwa walitendwa kinyama katika baadhi ya magereza, Mashahidi waliofungwa katika gereza la Santa Catalina katika Cádiz, Hispania, waliweza kutumia baadhi ya saa zao kutoa ushahidi kwa barua. Na katika Sweden utangazaji mwingi ulifanywa kuhusu njia ambayo kesi zilizohusu kutokuwamo kwa Mashahidi wa Yehova zilishughulikiwa. Hivyo, kwa njia nyingi watu walijulishwa juu ya uhakika wa kwamba Yehova ana mashahidi duniani na kwamba wao hushikamana kwa imara na kanuni za Biblia.

Kulikuwa jambo jingine lililofanya Mashahidi wajulikane sana na umma. Lilikuwa pia na tokeo lenye nguvu, la kutia nguvu kazi yao ya kueneza evanjeli.

Mikusanyiko Ilichangia Kutoa Ushahidi

Mashahidi wa Yehova walipofanya mkusanyiko wa kimataifa katika Paris, Ufaransa, katika 1955, ripoti za habari za televisheni zililipa taifa zima fursa ya kuona yaliyotukia. Katika 1969 mkusanyiko mwingine ulifanywa karibu na Paris, na ilikuwa wazi kwamba huduma ya Mashahidi ilikuwa imekuwa yenye mazao. Wale waliobatizwa kwenye mkusanyiko huo walikuwa na idadi ya 3,619, au asilimia kama 10 ya wastani wa hudhurio. Kuhusu hilo, gazeti la habari la Paris la jioni lenye kupendwa sana France-Soir la Agosti 6, 1969, lilisema hivi: “Kinachowatia wasiwasi makasisi wa zile dini nyingine si ile njia yenye kutazamisha ya ugawanyaji wa vichapo itumiwayo na mashahidi wa Yehova, bali, kule kufanya waongofu. Kila mmoja wa mashahidi wa Yehova ana wajibu wa kutoa ushahidi au kupiga mbiu ya imani yake kwa kutumia Biblia nyumba hadi nyumba.”

Wakati wa pindi ya majuma matatu katika kiangazi hicho cha 1969, mikusanyiko mingine minne mikubwa ya kimataifa ilifanywa katika Ulaya—katika London, Copenhagen, Roma, na Nuremberg. Mkusanyiko wa Nuremberg ulihudhuriwa na 150,645 kutoka nchi 78. Pamoja na ndege na meli, magari kama 20,000, mabasi 250, na magarimoshi ya pekee 40 yalihitajiwa kusafirisha wajumbe kwenye mkusanyiko huo.

Mikusanyiko hiyo si kwamba tu iliwaimarisha na kuwatayarisha Mashahidi wa Yehova kwa ajili ya huduma yao bali pia iliwapa umma fursa ya kujionea wenyewe Mashahidi wa Yehova ni watu wa aina gani. Mkusanyiko wa kimataifa uliporatibiwa kufanywa Dublin, Ireland, katika 1965, mkazo mwingi wa kidini ulitumiwa ili kulazimisha kufutwa kwa mipango hiyo. Lakini mkusanyiko ulifanywa, na wenye nyumba wengi katika Dublin waliwaandalia wajumbe mahali pa kulala. Kwa tokeo gani? “Hatukuambiwa ukweli juu yenu,” wakaeleza baadhi ya mabibi wenye nyumba baada ya mkusanyiko. “Mapadri walituambia uwongo, lakini sasa kwa kuwa tunawajua, sikuzote tutakuwa na furaha kuwapokea tena.”

Watu Wasemapo Lugha Nyingine

Katika miongo ya karibuni Mashahidi wa Yehova katika Ulaya wamepata kwamba kuwasiliana na watu wa mataifa mengine kumetokeza tatizo la pekee. Idadi kubwa wamehama nchi moja kwenda nyingine ili kujifaidi na fursa za kazi ya kuajiriwa. Baadhi ya majiji ya Ulaya yamekuwa makao ya mashirika makubwa ya kimataifa, yenye wafanyakazi ambao si wote wanaosema lugha ya wenyeji.

Bila shaka, eneo la wasemao lugha nyingi limekuwa uhakika wa maisha kwa karne nyingi katika sehemu fulani. Kwa kielelezo, katika India kuna lugha kuu 14 na labda lugha ndogo-ndogo na lahaja 1,000. Papua New Guinea ina zaidi ya lugha 700. Lakini ilikuwa hasa wakati wa miaka ya 1960 na ya 1970 kwamba Mashahidi katika Luxembourg walipata kwamba eneo lao limekuwa eneo lililotia ndani watu kutoka mataifa zaidi ya 30—na baada ya hapo angalau watu wa mataifa mengine 70 waliwasili. Sweden yaripoti kwamba imegeuka kutoka nchi yenye lugha moja yenye kutumiwa na karibu kila mtu kuwa jamii isemayo lugha 100 mbalimbali. Mashahidi wa Yehova wameshughulikiaje hilo?

Mwanzoni, mara nyingi walijitahidi tu kujua lugha ya mwenye nyumba na kisha wakajaribu kupata fasihi fulani ambayo angeweza kusoma. Katika Denmark, mirekodi ya tepu ilifanywa ili kuwezesha Waturuki wenye mioyo myeupe wasikie ujumbe katika lugha yao wenyewe. Uswisi ilikuwa na kundi kubwa la wafanyakazi wageni kutoka Italia na Hispania. Jambo lililoonwa na Rudolf Wiederkehr katika kusaidia baadhi yao ni kielelezo cha jinsi mambo yalivyoanza. Yeye alijaribu kutoa ushahidi kwa mwanamume Mwitalia, lakini hakuna yeyote wao aliyejua sana lugha ya mwingine. Ni jambo gani lingeweza kufanywa? Ndugu yetu alimwachia Mnara wa Mlinzi la Kiitalia. Lijapokuwa tatizo la lugha, Ndugu Wiederkehr alirudi. Funzo la Biblia lilianzishwa pamoja na mwanamume huyo, mke wake, na mwana wao wa miaka 12. Kitabu cha funzo cha Ndugu Wiederkehr kilikuwa katika Kijerumani, lakini aliipa ile familia nakala za Kiitalia. Maneno yalipokosekana, ishara zilitumiwa. Nyakati nyingine, mvulana huyo mchanga, ambaye alikuwa akijifunza Kijerumani shuleni, alitumikia kuwa mkalimani. Familia hiyo yote ilikubali kweli na upesi ikaanza kuishiriki pamoja na wengine.

Lakini kihalisi mamilioni ya wafanyakazi kutoka Ugiriki, Italia, Ureno, Hispania, Uturuki, na Yugoslavia walikuwa wakihamia Ujerumani na nchi nyinginezo. Msaada wa kiroho ungeweza kutolewa kwao kwa mafanikio zaidi katika lugha zao wenyewe. Upesi baadhi ya Mashahidi wenyeji walianza kujifunza lugha za wafanyakazi wageni. Katika Ujerumani masomo ya Kituruki hata yalipangwa na ofisi ya tawi. Mashahidi kutoka nchi nyinginezo waliojua lugha hizo zilizohitajiwa walialikwa wahamie sehemu ambazo kulikuwa na uhitaji wa pekee wa msaada.

Baadhi ya wafanyakazi kutoka ng’ambo hawakuwa wamepata kamwe kukutana na Mashahidi wa Yehova hapo awali na walikuwa kwelikweli na njaa ya kiroho. Walikuwa wenye shukrani kwa ajili ya jitihada iliyokuwa ikifanywa kuwasaidia. Makutaniko mengi ya lugha za kigeni yalifanyizwa. Baada ya wakati, baadhi ya wafanyakazi hao wageni walirudi nchi zao kuendesha huduma katika maeneo ambayo wakati uliopita hayakuwa yamepewa ushahidi kamili kuhusu Ufalme wa Mungu.

Mavuno Mengi Kujapokuwa Vizuizi

Mashahidi wa Yehova hutumia njia zilezile za kuhubiri kotekote duniani. Katika Amerika Kaskazini wamekuwa wakieneza evanjeli kwa bidii kwa zaidi ya karne moja. Basi, haishangazi kwamba kumekuwa vuno jingi la kiroho huko. Kufikia 1975, kulikuwa Mashahidi wa Yehova watendaji 624,097 katika bara la Marekani na Kanada. Hata hivyo, hiyo haikuwa kwa sababu kazi yao ya kuhubiri katika Amerika Kaskazini ilikuwa ikifanywa bila upinzani.

Ijapokuwa serikali ya Kanada ilikuwa imeondoa marufuku yayo juu ya Mashahidi wa Yehova na mashirika yao ya kisheria kufikia 1945, manufaa kutokana na uamuzi huo hazikuonekana mara hiyo katika mkoa wa Quebec. Katika Septemba 1945, wafanyaghasia Wakatoliki walishambulia Mashahidi wa Yehova katika Châteauguay na Lachine. Mashahidi walikamatwa na kushtakiwa uhaini kwa sababu fasihi walizogawanya zilichambua Kanisa la Katoliki ya Roma. Wengine walitiwa gerezani kwa sababu waligawanya fasihi za Biblia ambazo hazikuwa zimekubaliwa na mkuu wa polisi. Kufikia 1947, kulikuwa kesi 1,700 dhidi ya Mashahidi zilizongojea kukatwa katika mahakama za Quebec.

Wakati jitihada za pekee zilipokuwa zikifanywa ili baadhi ya kesi zilizo kigezo zifanywe na mahakama, Mashahidi waliagizwa wahubiri gospeli kwa mdomo, wakitumia Biblia tu—ile Douay Version ya Katoliki inapowezekana. Wahudumu wa wakati wote kutoka sehemu nyingine za Kanada walijitolea kujifunza Kifaransa na kuhamia Quebec ili kushiriki katika kueneza ibada ya kweli huko.

Wakatoliki wengi wenye mioyo myeupe waliwaalika Mashahidi ndani ya makao yao na kuuliza maswali, ingawa walisema mara nyingi: ‘Mimi ni wa Katoliki ya Roma nami sitabadilika kamwe.’ Lakini walipojionea wenyewe yale ambayo Biblia inasema, makumi ya maelfu yao, kwa sababu ya kupenda kweli na tamaa ya kumpendeza Mungu, walibadilika.

Katika Marekani vilevile, ilikuwa lazima kuthibitisha mbele ya mahakama ili kuimarisha haki ya Mashahidi wa Yehova ya kuhubiri hadharani na nyumba hadi nyumba. Tokea 1937 hadi 1953, kulikuwa kesi kama hizo 59 zilizohusu Mashahidi ambazo zilipelekwa hadi Mahakama Kuu Zaidi katika Washington, D.C.

Fikira Kwenye Maeneo Yasiyogawiwa Mtu

Lengo la Mashahidi wa Yehova si kufanya jambo fulani tu katika kuhubiri habari njema bali ni kufikia kila mtu awezaye kufikiwa na ujumbe wa Ufalme. Kwa kusudi hilo, Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova limegawia kila ofisi ya tawi daraka kwa sehemu hususa ya shamba la ulimwengu. Kadiri makutaniko yafanyizwavyo ndani ya eneo la tawi, kila kutaniko hupewa sehemu ya eneo hilo ambamo lapasa kuhubiri. Kisha kutaniko hugawanya eneo kuwa sehemu ambazo laweza kugawia vikundi na wahudumu mmoja-mmoja kutanikoni. Hao hujitahidi kufikia kila familia kwa ukawaida. Lakini namna gani yale maeneo ambayo hayajagawiwa makutaniko?

Katika 1951 orodha ilifanywa ya wilaya zote katika Marekani kuamua ni zipi ambazo hazikuwa zikipokea ziara za ukawaida kutoka kwa Mashahidi wa Yehova. Wakati huo, karibu asilimia 50 hazikuwa zikifanyiwa kazi au zilikuwa zikienezwa kwa sehemu tu. Mipango ilifanywa ili Mashahidi waendeshe huduma yao katika maeneo hayo wakati wa miezi ya kiangazi au katika nyakati nyingine zilizofaa, kwa kusudi la kusitawisha makutaniko. Wakati watu hawakuwamo nyumbani, nyakati fulani ujumbe uliochapwa, pamoja na fasihi za Biblia ziliachwa. Mafunzo ya Biblia yaliongozwa kupitia barua. Baadaye, mapainia wa pekee walitumwa kwenye maeneo hayo ili kufuatia kupendezwa kulikopatikana.

Utendaji huo haukuwa wa miaka ya 1950 tu. Ulimwenguni pote, katika nchi ambako miji mikubwa inapokea ushahidi lakini maeneo yasiyogawiwa mtu yeyote yako, jitihada za bidii ya moyo huendelea kufanywa kufikia watu ambao hawafikiwi kwa ukawaida. Katika Alaska katika miaka ya 1970, asilimia ipatayo 20 ya idadi ya watu iliishi katika vijiji vilivyo mbali. Wengi wa watu hao wangeweza kufikiwa vizuri zaidi katika wakati wa majira ya kipupwe wakati ambapo kazi ya uvuvi karibu husimama. Lakini huo ndio wakati ambao huwa na hali yenye baridi kali na utusitusi ambao hufanya kuruka kwa ndege kuwe hatari. Hata hivyo, idadi za Waeskimo, Wahindi na Waaleut walihitaji fursa ya kujifunza juu ya uandalizi kwa ajili ya uhai wa milele chini ya Ufalme wa Mungu. Ili kuwafikia, kikundi cha Mashahidi 11 kikitumia ndege ndogo kadhaa kiliruka kwenda kwenye vijiji vipatavyo 200 vilivyotapakaa katika eneo la kilometa za mraba 844,000 wakati wa kipindi cha miaka miwili. Yote hayo yalifanywa kwa fedha zilizochangwa kwa kujitolea na Mashahidi wenyeji.

Kuongezea safari hizo za kuhubiri, Mashahidi waliokomaa wametiwa moyo wafikirie kuhamia hasa maeneo yaliyo katika nchi yao wenyewe ambayo uhitaji wa wapiga-mbiu wa Ufalme ni mkubwa zaidi. Maelfu wameitikia. Miongoni mwa wale waliofanya hivyo katika Marekani ni Eugene na Delia Shuster, ambao waliondoka Illinois katika 1958 kutumikia katika Hope, Arkansas. Wamekaa kwa zaidi ya miongo mitatu wakitafuta watu wenye kupendezwa, kuwapanga kitengenezo kuwa makutaniko, na kuwasaidia kukua kufikia ukomavu wa Kikristo.

Kwa kitia-moyo cha mwangalizi wao wa mzunguko, katika 1957, Alexander B. Green na mke wake waliondoka Dayton, Ohio, wakatumikie katika Mississippi. Kwanza walipewa mgawo kwenda Jackson na miaka miwili baadaye Clarksdale. Baada ya wakati, Ndugu Green alitumikia katika sehemu nyingine tano. Zote hizo zilikuwa na makutaniko madogo yaliyokuwa na uhitaji wa usaidizi. Alijiruzuku kwa kufanya kazi ya bawabu, kutunza bustani, kutengeneza fanicha, kurekebisha magari, na kadhalika. Lakini jitihada zake kuu zilielekezwa katika kuhubiri habari njema. Alisaidia Mashahidi wenyeji kukua kiroho, akafanya kazi nao kufikia watu katika eneo lao, na mara nyingi akawasaidia kujenga Jumba la Ufalme kabla ya kusonga mbele.

Katika 1967, Gerald Cain alipopata kuwa Shahidi katika magharibi mwa Marekani, yeye na familia yake walihisi sana uharaka wa kazi ya kueneza evanjeli. Hata kabla ya yeyote wao kubatizwa, walikuwa wakifanya mipango ya kutumikia sehemu ambako kuna uhitaji mkubwa zaidi. Kwa miaka minne walifanya kazi na kutaniko la Needles, California. Hilo lilikuwa na daraka juu ya eneo lililotia ndani sehemu za majimbo matatu katika magharibi mwa Marekani. Matatizo ya kiafya yalipotaka wahame, kwa mara nyingine tena walichagua mahali palipokuwa na uhitaji wa pekee wa msaada, nao waligeuza sehemu ya kao lao huko kuwa Jumba la Ufalme. Kuhama zaidi kumefuata, lakini sikuzote fikira nyingi zimekuwa kukaa mahali ambapo wangeweza kuwa wenye msaada zaidi katika kutoa ushahidi.

Kadiri ambavyo idadi ya makutaniko imeongezeka, katika sehemu fulani uhitaji wa wazee waliostahili umehisiwa sana. Ili kutimiza uhitaji huo, maelfu ya wazee wamejitolea kusafiri kwa ukawaida (na kwa gharama zao wenyewe) kwenda kwenye makutaniko nje ya mtaa wao. Wao husafiri mara tatu, nne, tano, au zaidi kwa juma—kushiriki katika mikutano ya kutaniko na katika huduma ya shambani na pia kuchunga kutaniko. Hilo limefanywa si katika Marekani pekee bali pia katika El Salvador, Japani, Uholanzi, Hispania, na nchi nyinginezo nyingi. Katika visa fulani wazee na familia zao wamehama, ili kutimiza uhitaji huo.

Matokeo yamekuwa nini? Fikiria nchi moja tu. Huko nyuma katika 1951, wakati mipango ya kufanya kazi katika maeneo yasiyogawiwa mtu ilipotangazwa kwa mara ya kwanza, kulikuwa makutaniko kama 3,000 katika Marekani, yenye wastani wa wahubiri 45 kila kutaniko. Kufikia 1975, kulikuwa makutaniko 7,117, na wastani wa idadi ya Mashahidi watendaji walioshirikiana na kila kutaniko ilikuwa imepanda kufikia karibu 80.

Ushahidi uliotolewa kwa jina na Ufalme wa Yehova tokea 1945 kufikia 1975 ulikuwa mwingi sana kuliko ule uliokuwa umepata kutolewa kufikia wakati huo.

Idadi ya Mashahidi ilikuwa imekua kutoka 156,299 katika 1945 kufikia 2,179,256 duniani pote katika 1975. Kila mmoja wao alishiriki binafsi katika kuhubiri hadharani kuhusu Ufalme wa Mungu.

Katika 1975, Mashahidi wa Yehova walikuwa na shughuli katika nchi 212 (zikihesabiwa kulingana na jinsi ramani ilivyokuwa imegawanywa katika miaka ya mapema ya 1990). Katika bara la Marekani na Kanada, 624,097 wao walikuwa wakifanya huduma yao. Katika Ulaya, nje ya ile iliyokuwa wakati huo Muungano wa Sovieti, kulikuwa wengine 614,826. Afrika ilikuwa ikisikia ujumbe wa kweli ya Biblia kutoka kwa Mashahidi 312,754 waliokuwa wakishiriki katika kazi huko. Mexico, Amerika ya Kati, na Amerika Kusini zilikuwa zikitumikiwa na Mashahidi 311,641; Asia, na 161,598; Australia na visiwa vingi duniani pote, na 131,707.

Wakati wa miaka 30 kufika 1975, Mashahidi wa Yehova walitumia saa 4,635,265,939 katika kazi ya kuhubiri na kufundisha hadharani. Pia waliangusha vitabu, vijitabu, na magazeti 3,914,971,158 kwa watu wenye kupendezwa kuwasaidia wathamini jinsi wangeweza kunufaishwa na kusudi lenye upendo la Yehova. Kupatana na amri ya Yesu ya kufanya wanafunzi, walifanya ziara za kurudia 1,788,147,329 kwa watu wenye kupendezwa, na katika 1975 walikuwa wakiongoza kwa wastani mafunzo ya Biblia nyumbani bila malipo 1,411,256 kwa watu mmoja-mmoja na familia.

Kufikia 1975 kazi ya kuhubiri ilikuwa kwa kweli imefikia nchi 225. Katika nchi zaidi ya 80 ambazo habari njema zilikuwa zimefika kufikia 1945 lakini ambako hakukuwa na makutaniko mwaka huo, makutaniko ya Mashahidi wenye bidii yalikuwa yakistawi kufikia 1975. Miongoni mwa sehemu hizo ni Jamhuri ya Korea ikiwa na makutaniko 470, Hispania ikiwa na 513, Zaire ikiwa na 526, Japani ikiwa na 787, na Italia ikiwa na 1,031.

Wakati wa pindi ya kutoka 1945 hadi 1975, idadi kubwa zaidi ya watu waliopata kuwa Mashahidi wa Yehova hawakudai kuwa watiwa-mafuta kwa roho ya Mungu wakitazamia uhai wa kimbingu. Katika masika ya 1935, idadi ya walioshiriki mifano kwenye Mlo wa Jioni wa Bwana walikuwa na jumla kamili ya asilimia 93 ya wale waliokuwa wakishiriki katika huduma ya shambani. (Baadaye katika mwaka huohuo, ile “halaiki kubwa” ya Ufunuo 7:9 (KJ) ilitambulishwa kuwa ya watu ambao wangeishi milele duniani.) Kufikia 1945 idadi ya Mashahidi waliokuwa wakitazamia uhai katika dunia iliyo paradiso ilikuwa imeongezeka kufikia hatua ya kwamba walijumlika kuwa asilimia 86 ya wale waliokuwa wakishiriki katika kuhubiri habari njema. Kufikia 1975 wale waliodai kuwa Wakristo watiwa-mafuta kwa roho hawakuzidi nusu moja ya asilimia 1 ya jumla ya tengenezo la Mashahidi wa Yehova la ulimwenguni pote. Ingawa walitawanyika katika karibu nchi 115 wakati huo, watiwa-mafuta hao waliendelea kutumikia wakiwa baraza lililoungana chini ya Yesu Kristo.

[Blabu katika ukurasa wa 463]

“Tangu mwe hapa kila mtu anaongea juu ya Biblia”

[Blabu katika ukurasa wa 466]

“Yale ambayo umeniambia sasa hivi ni yale niliyosoma katika Biblia ile miaka mingi iliyopita”

[Blabu katika ukurasa wa 470]

Maelfu walihamia maeneo yaliyo ndani ya nchi yao wenyewe ambayo yalikuwa na uhitaji mkubwa zaidi wa Mashahidi

[Blabu katika ukurasa wa 472]

“Thawabu isiyokadirika thamani”

[Blabu katika ukurasa wa 475]

Mashahidi wanaostahili walitumwa kwenye nchi zilizokuwa na uhitaji wa pekee

[Blabu katika ukurasa wa 486]

Wakiwa na hoja za Kimaandiko zenye nguvu, Mashahidi wa mapema katika Nigeria walifunua makasisi na mafundisho yao bandia

[Blabu katika ukurasa wa 497]

Maneno yalipokosekana, ishara zilitumiwa

[Blabu katika ukurasa wa 499]

Lengo lao? Kufikia kila mtu awezaye kufikiwa na ujumbe wa Ufalme

[Ramani/Picha katika ukurasa wa 489]

Jitihada nyingi zilifanwa kufikia watu wa China kwa habari njema za Ufalme wa Yehova

Kutoka Chefoo, maelfu ya barua, trakti, na vatabu vilipelekwa nje kwa posta kati ya 1891 na 1900

C. T. Russell alihutubu katika Shanghiai na kuzuru miji na vijiji 15, katika 1912

Makolpota waligawanya fasihi nyingi huku na huku katika pwani ya China, wakifany ziara fupi ndani ya bara, 1912-1918

Makilpota Wajapani walitumikia hapa, 1930-1931

Matangazo ya redio yalifanwa katikia Kichina kutoka Shanghai, Peking, na Tientsin wakati wa miaka ya 1930; kama tokeo, barua za kuomba fasihi zilipokewa sehemu nyingi za China

Mapainia kutoka Australia na Ulaya walitoa ushahidi katkia Shanghai, Peking, Tientsin, Tsingtao, Pei-tai-ho, Chefoo, Weihaiwei, Canton, Swatow, Amoy, Foochow, Hankow, na Nanking wakati wa miaka ya 1930 na 1940. Wengine walikuja kupitia Babara ya Burma na kutoa ushahidi katika Pao-shan, Chunking, Ch’eng-tu. Mapainia wenyeji walitumikia katika Shensi na Ningpo

[Picha]

Wamishonari walizoezwa Gileadi, kama vile Stanley Jones (kushoto) na Harold King (Kulia), walitumikia hapa kuanzia 1947 hadi 1958, pamoja na familia za Mashahidi wenyeji wenye bidii

[Ramani]

CHINA

[Ramani/Picha katika ukurasa wa 462]

Mashua “Sibia” ilitumika kuwa kao la kimishonari lenye kuelea katika Indies Magharibi

G. Maki

S. Carter

R. Parkin

A. Worsley

[Ramani]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

BAHAMAS

VISIWA VYA LEEWARD

VISIWA VYA VIRGIN (MAREKANI)

VISIWA VYA VIRGIN (UINGEREZA)

VISIWA VYA WINDWARD

[Ramani katika ukurasa wa 477]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Maji ya kweli yenye kutoa uhai yalitiririka kuvuka mipaka ya kitaifa kwenda katika pande nyingi barani Afrika

MISRI

SENEGAL

KENYA

AFRIKA KUSINI

GHANA

MALAWI

NIGERIA

SIERRA LEONE

ZAMBIA

[Picha katika ukurasa wa 464]

Wakiwa wamishonari katika Bolivia, Edward Michalec (kushoto) na Harold Morris (kulia) walihubiri kwanza hapa katika La Paz

[Picha katika ukurasa wa 465]

Ile mashua “El Refugio,” iliyojengwa na Mashahidi katika Peru, ilitumiwa kupeleka ujumbe wa Ufalme kwa watu waishio kandokando ya mito katika mkoa wa Amazon ya juu

[Picha katika ukurasa wa 467]

Madrassa ya kujifunza kusoma na kuandia yanayoongozwa na Mashahidi katika Mexico yamewezesha makumi ya maelfu ya watu kusoma Neno la Mungu

[Picha katika ukurasa wa 468]

Ndugu Knorr (mbele kulia) alikutana na Mashahidi katika vikusanyiko vidogovidogo mashambani na milimani katika Argentina waliponyimwa uhuru wa kukusanyika wazi zaidi

[Picha katika ukurasa wa 469]

Miongoni mwa maelfu ya Mashahidi waliohamia nchi nyinginezo kutumikia sehemu ambako uhitaji ulikuwa mkubwa zaidi walikuwa familia, kama vile Harold na Anne Zimmerman pamoja na watoto wao wanne wachanga (Kolombia)

[Picha katika ukurasa wa 471]

Katika kuitikia mwito uliotolewa wa wenye kujitolea, Tom na Rowena Kitto walihamia Papua kufundisha kweli ya Biblia

[Picha katika ukurasa wa 471]

John na Ellen Hubler, wakifuatwa na Mashahidi wengine 31, walihamia New Caledonia. Kabla ya kulazimika kuondoka, kutaniko lilikuwa limesimamishwa imara huko

[Picha katika ukurasa wa 473]

Akiwa kijana katika Samoa Magharibi, Fuaiupolu Pele alikabili mkazo mwingi wa familia na jamii alipoamua kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova

[Picha katika ukurasa wa 474]

Baada ya Shem Irofa’alu na washiriki wake kusadikishwa kwamba yale ambayo Mashahidi wa Yehova walikuwa wakifundisha yalikuwa kwa kweli ndiyo kweli, makanisa katika vijiji 28 katika Visiwa vya Solomon yaligeuzwa kuwa Majumba ya Ufalme

[Picha katika ukurasa wa 476]

Ili wahubiri katika Ethiopia katika miaka ya mapema ya 1950, Mashahidi walitakwa waanzishe misheni na kufundisha shule

[Picha katika ukurasa wa 478]

Alipotishwa kufukuzwa nchini, Gabriel Paterson (anayeonyeshwa hapa) alipewa uhakikishio na ofisa mashuhuri: ‘Kweli ni kama mto wenye nguvu nyingi; ujengee bwawa nao utafurika juu ya bwawa’

[Picha katika ukurasa wa 479]

Katika 1970 kwenye mkusanyiko mmoja katika Nigeria, Mashahidi wapya 3,775 walizamishwa; uangalifu ulitumiwa kuhakikisha kwamba kila mmoja alistahili

[Picha katika ukurasa wa 481]

Maonyesho ya sinema (barani Afrika na ulimwenguni pote) yaliwawezesha watazamaji kuona kidogo ukubwa wa tengenezo la Yehova lionekanalo

[Picha katika ukurasa wa 482]

João Mancoca (anayeonyeshwa hapa na mke wake, Mary) ametumikia Yehova kwa uaminifu-mshikamanifu kwa miongo mingi zijapokuwako hali ngumu sana

[Picha katika ukurasa wa 483]

Katika 1961, Ernest Heuse, Jr., akiwa na familia yake, aliweza kuingia Zaire (wakati huo iliitwa Kongo) kusaidia kutoa maagizo ya kiroho kwa wale waliotaka kikweli kumtumikia Yehova

[Picha katika ukurasa wa 485]

Ingawa alikuwa amebatizwa kwa mwaka mmoja tu naye hakujua Mashahidi wengine wowote katika Kenya, Mary Whittington alianza kusaidia wengine wajifunze kweli

[Picha katika ukurasa wa 487]

Mary Nisbet (mbele katikati), akiwa na wanawe Robert na George kwenye pande zake, waliopainia katika Afrika Mashariki katika miaka ya 1930, na (nyuma) mwanaye William na mke wake Muriel, waliotumikia katika Afrika Mashariki tokea 1956 hadi 1973

[Picha katika ukurasa wa 488]

Kwenye mkusanyiko katika Filipino katika 1945, maagizo yalitolewa juu ya jinsi ya kufundisha kupitia mafunzo ya Biblia nyumbani

[Picha katika ukurasa wa 490]

Don na Mabel Haslett, wamishonari wa kwanza wa wakati wa baada ya vita katika Japani, wakishiriki kutoa ushahidi barabarani

[Picha katika ukurasa wa 491]

Kwa miaka 25 Lloyd Barry (kulia) alitumikia katika Japani, kwanza akiwa mishonari kisha akiwa mwangalizi wa tawi

[Picha katika ukurasa wa 491]

Don na Earlene Steele, wa kwanza kati ya wamishonari waliotumikia katika Jamhuri ya Korea

[Picha katika ukurasa wa 492]

Miaka mingi iliyopita, nyakati fulani wafanyaghasia walifukuza Fred Metcalfe alipojaribu kuhubiri kutoka Biblia katika Ireland; lakini baadaye watu walipochukua wakati wa kusikiliza, maelfu wakawa Mashahidi wa Yehova

[Picha katika ukurasa wa 493]

Ujapokuwa upinzani wa makasisi, maelfu walimiminika kwenye mikusanyiko ya Mashahidi katika Italia (Roma, 1969)

[Picha katika ukurasa wa 494]

Wakati wa marufuku, mikutano ya kutaniko mara nyingi ilifanywa katika sehemu za mashambani, kwa mtindo wa mandari, kama vile hapa katika Ureno

[Picha katika ukurasa wa 495]

Mashahidi waliokuwa gerezani katika Cádiz, Hispania, waliendelea kuhubiri kwa kuandika barua

[Picha katika ukurasa wa 496]

Mikusanyiko mikubwa iliupa umma fursa ya kujionea na kusikia wenyewe Mashahidi walikuwa watu wa aina gani

Paris, Ufaransa (1955)

Nuremberg, Ujerumani (1955)

[Picha katika ukurasa wa 498]

Ili kufikia kila mtu katika Luxembourg kwa hbari njema, imewabidi Mashahidi wa Yehova watumie fasihi katika luga za watu wa kutoka mataifa mia moja

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki