Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • jv sura 22 kur. 502-520
  • Sehemu ya 5—Kuwa Mashahidi Hadi Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya Dunia

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Sehemu ya 5—Kuwa Mashahidi Hadi Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya Dunia
  • Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Matukio ya Kustaajabisha Nchini Poland
  • Sehemu Kubwa Zaidi ya Ulaya Mashariki Yafungua Milango Yayo
  • Wengi Sasa Wanataka Kusikiliza
  • Mashamba Meupe Tayari kwa Mavuno
  • Kuwafikia Watu Mahali Panapowezekana na Wakati Inapowezekana
  • Jitihada za Kurudiarudia ili Kufikia Mioyo
  • Kueneza Eneo kwa Ukamili Hata Zaidi
  • Kuongeza Bidii Katika Kutoa Ushahidi Mwisho Ukaribiapo
  • ‘Mdogo Awa Elfu’
  • Ni Kadiri Gani ya Ushahidi Umetolewa Katika “Nchi Nyinginezo”?
  • Sehemu ya 4—Kuwa Mashahidi Hadi Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya Dunia
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Mikusanyiko Uthibitisho wa Udugu Wetu
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Sehemu ya 3—Kuwa Mashahidi Hadi Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya Dunia
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Mashahidi wa Yehova Katika Ulaya Mashariki
    Amkeni!—1992
Pata Habari Zaidi
Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
jv sura 22 kur. 502-520

Sura ya 22

Sehemu ya 5—Kuwa Mashahidi Hadi Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya Dunia

Katika 1975 maamuzi muhimu yalifanywa kuhusu njia ambayo utendaji wa Mashahidi wa Yehova ungesimamiwa kutoka makao yao makuu ya ulimwengu. Wakati huo hawakujua ni mashamba gani ambayo yangefunguka ili kutoa ushahidi mwingi kabla ya mwisho wa mfumo uliopo wa ulimwengu au ni mahubiri ya kiasi gani ambayo bado yangefanywa katika nchi ambako walikuwa wamehubiri peupe kwa miaka mingi. Lakini walitaka kutumia kila fursa kwa njia bora zaidi iwezekanayo. Kurasa 502 hadi 520 zinasimulia baadhi ya matukio ya kusisimua.

KUMEKUWAKO mabadiliko makubwa katika Amerika Kusini. Haijapita miaka mingi tangu Mashahidi wa Yehova katika Ekuado walipokabili umati wenye ghasia wa Wakatoliki, mapadri Wakatoliki katika Mexico walipotawala wakiwa kama wafalme katika vijiji vingi, na Mashahidi wa Yehova walipopigwa marufuku na serikali katika Argentina na Brazili. Lakini hali zimebadilika sana. Sasa wengi kati ya wale waliofundishwa kuhofu au kuchukia Mashahidi, wao wenyewe ni Mashahidi wa Yehova. Wengine husikiliza kwa furaha wakati Mashahidi wanapowazuru kushiriki ujumbe wa amani wa Biblia. Mashahidi wa Yehova wanajulikana sana na kustahiwa na wengi.

Ukubwa wa mikusanyiko yao na mwenendo wa Kikristo wa wale wanaohudhuria umevuta fikira. Mikusanyiko miwili kama hiyo, iliyofanywa wakati uleule katika São Paulo na Rio de Janeiro, Brazili, katika 1985, ilikuwa na kilele cha hudhurio cha 249,351. Baadaye, mikusanyiko 23 zaidi, iliyofanywa ili watu wanaopendezwa katika sehemu nyinginezo za Brazili waweze kuhudhuria, iliinua jumla ya hudhurio kuwa 389,387. Matokeo ya kazi ambayo Mashahidi wa Yehova wamekuwa wakifanya katika Brazili wakiwa walimu wa Neno la Mungu yalikuwa dhahiri sana wakati watu 4,825 walipofananisha wakfu wao kwa Yehova kwa uzamisho wa maji kwenye mfululizo huo wa mikusanyiko. Miaka mitano tu baadaye, katika 1990, ilihitaji kufanywe mikusanyiko 110 kotekote katika Brazili ili watu 548,517 waliohudhuria waweze kutoshea. Wakati huo, 13,448 walijitokeza kwa ajili ya uzamisho wa maji. Kotekote nchini mamia ya maelfu ya watu mmoja-mmoja na familia walikuwa wakiwakaribisha Mashahidi wa Yehova wawafunze kutokana na Neno la Mungu.

Namna gani kuhusu Argentina? Baada ya miongo ya vizuizi vya serikali, Mashahidi wa Yehova waliweza tena kukusanyika kwa uhuru katika 1985. Ilikuwa furaha iliyoje kwa 97,167 waliohudhuria kwenye mfululizo wa kwanza wa mikusanyiko! Chini ya kichwa “Ufalme Ambao Unakua—Ule wa Mashahidi wa Yehova,” gazeti la huko liitwalo Ahora lilishangazwa na utaratibu wa umati wa mkusanyiko katika Buenos Aires, kutokuwa kwao na chuki za kikabila au kijamii, hali yao ya amani, na upendo walioonyesha. Kisha likamalizia hivi: “Iwe tunashiriki mawazo na mafundisho yao au la, halaiki hii yote yastahili staha yetu nyingi sana.” Hata hivyo, Waargentina wengi walifanya zaidi ya hiyo. Walianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, na kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme ili kuchunguza jinsi Mashahidi hutumia kanuni za Biblia maishani mwao. Kisha wachunguzi hao wakafanya uamuzi. Katika miaka saba iliyofuata, mamia ya maelfu yao waliweka maisha zao wakfu kwa Yehova, na idadi ya Mashahidi katika Argentina imeongezeka kwa asilimia 71!

Itikio kwa habari njema za Ufalme wa Mungu lilikuwa lisilo la kawaida hata zaidi katika Mexico. Katika miaka ya zamani, Mashahidi wa Yehova huko walikuwa wakidhulumiwa mara kwa mara na umati wenye ghasia uliochochewa na mapadri. Lakini kwa sababu ya uhakika wa kwamba Mashahidi hawakupigana au kutafuta kulipiza kisasi, watu wenye mioyo minyoofu walivutiwa sana. (Rum. 12:17-19) Pia waliona kwamba Mashahidi walitegemeza imani zao zote juu ya Biblia, Neno la Mungu lililopuliziwa roho, badala ya mapokeo ya kibinadamu. (Mt. 15:7-9; 2 Tim. 3:16, 17) Wangeweza kuona kwamba Mashahidi walikuwa na imani ambayo iliwategemeza kikweli wajapokabiliwa na taabu. Familia zaidi na zaidi ziliwakaribisha Mashahidi wa Yehova walipojitoa kuongoza nao mafunzo ya Biblia nyumbani bila malipo. Kwa kweli, wakati wa 1992, asilimia 12 ya mafunzo ya Biblia yaliyokuwa yakiongozwa na Mashahidi ulimwenguni pote yalikuwa katika Mexico, na idadi kubwa yayo yalikuwa ya familia kubwakubwa. Kama tokeo, idadi ya Mashahidi wa Yehova katika Mexico—si wale waliokuwa wakihudhuria tu mikutano yao bali wale waliokuwa wapiga-mbiu wa Ufalme wa Mungu walio watendaji—iliongezeka kutoka 80,481 katika 1975 hadi 354,023 katika 1992!

Katika Ulaya pia, matukio yasiyo ya kawaida yalichangia kuenezwa kwa ujumbe wa Ufalme.

Matukio ya Kustaajabisha Nchini Poland

Ingawa kazi ya Mashahidi wa Yehova ilikuwa imepigwa marufuku nchini Poland kuanzia 1939 hadi 1945 (wakati wa kukaliwa na Wanazi na Wasovieti) na tena kuanzia Julai 1950 (chini ya uongozi wa Wasovieti), Mashahidi wa Yehova hawakuwa wameacha kuhubiri huko. Ingawa idadi yao ilikuwa 1,039 tu katika 1939, katika 1950 kulikuwa na wapiga-mbiu wa Ufalme 18,116, nao waliendelea kuwa waeneza-evanjeli wenye bidii (ingawa wenye busara). (Mt. 10:16) Hata hivyo, kwa habari ya makusanyiko, yalikuwa yamefanywa mahali pasipo peupe—mashambani, katika ghala, na misituni. Lakini, kuanzia 1982, serikali ya Poland iliwaruhusu kufanya makusanyiko ya siku moja ya kiasi kidogo katika majengo yaliyokodiwa.

Kisha, katika 1985 Mashahidi wa Yehova waliweza kufanya mikusanyiko minne mikubwa katika stediamu kubwa zaidi nchini Poland wakati wa mwezi wa Agosti. Wakati mjumbe kutoka Austria alipowasili kwa ndege, alishangaa kusikia tangazo kutoka kwa vikuza-sauti la kuwakaribisha Mashahidi wa Yehova nchini Poland kwa mkusanyiko wao. Akijua kwamba hilo lilionyesha kulikuwa na badiliko katika mtazamo wa serikali, Shahidi Mpoland mzee-mzee aliyekuwa hapo kuwakaribisha wageni hangeweza kujizuia kutokwa na machozi ya shangwe. Waliohudhuria mikusanyiko hiyo walikuwa wajumbe 94,134, kutia vikundi kutoka nchi 16. Je, umma ulijua kile kilichokuwa kikiendelea? Naam, ulijua! Wakati na baada ya mikusanyiko hiyo, walisoma ripoti katika magazeti yao makuu, wakaona umati wa mkusanyiko kwenye televisheni, na kusikia sehemu za programu kwenye redio zao. Wengi wao walipenda yale waliyoona na kusikia.

Mipango kwa ajili ya mikusanyiko mikubwa hata zaidi katika Poland ilikuwa inaendelea, mnamo Mei 12, 1989, serikali ilipotoa utambulisho wa kisheria kwa Mashahidi wa Yehova kuwa shirika la kidini. Katika muda wa miezi mitatu, mikusanyiko mitatu ya kimataifa ilikuwa ikiendelea—katika Chorzów, Poznan, na Warsaw—kukiwa na jumla ya hudhurio la 166,518. Kwa kustaajabisha, maelfu ya Mashahidi kutoka zile nchi zilizokuwa Muungano wa Sovieti (U.S.S.R.) na Chekoslovakia waliweza kupata ruhusa iliyohitajiwa ya kusafiri na walihudhuria. Je, kazi ya kufanya wanafunzi ya Mashahidi wa Yehova ilikuwa inazaa matokeo katika nchi hizo ambako kutoamini kuwako kwa Mungu kulikuwa kumeungwa mkono sana na Serikali kwa miongo ya miaka? Jibu lilikuwa wazi wakati 6,093, kutia na vijana wengi, walipojitoa kwa ajili ya uzamisho wa maji kwenye mikusanyiko hiyo.

Umma ungeweza kuona wazi sana kwamba Mashahidi walikuwa tofauti—kwa njia yenye kufaa sana. Kwenye magazeti ya umma, walisoma taarifa kama zile zifuatazo: “Wale wanaoabudu Yehova Mungu—kama vile wanavyosema wenyewe—huthamini sana vikusanyiko vyao, ambavyo kwa kweli ni udhihirisho wa umoja miongoni mwao. . . . Kuhusu utaratibu, hali ya amani, na usafi, washiriki wa mkusanyiko ni mifano ya kuigwa.” (Życie Warszawy) Baadhi ya watu wa Poland waliamua kufanya zaidi ya kuchunguza tu wakusanyikaji. Walitaka Mashahidi wa Yehova wajifunze Biblia nao. Kama tokeo la mafunzo hayo katika Neno la Mungu, idadi ya Mashahidi wa Yehova nchini Poland iliongezeka kutoka 72,887 katika 1985 hadi 107,876 katika 1992; na wakati wa mwaka huo uliotajwa mwisho, walitoa zaidi ya muda wa saa milioni 16,800,000 kuwaambia wengine kuhusu tumaini la ajabu lililoonyeshwa katika Maandiko.

Hata hivyo, haikuwa nchini Poland tu kwamba mabadiliko ya kusisimua yalikuwa yakitukia.

Sehemu Kubwa Zaidi ya Ulaya Mashariki Yafungua Milango Yayo

Hungaria iliwatambua kisheria Mashahidi wa Yehova katika 1989. Ile Iliyokuwa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Ujerumani (GDR) iliondoa marufuku yayo ya miaka 40 juu ya Mashahidi katika 1990, miezi minne tu baada ya kubomolewa kwa Ukuta wa Berlin kuanza. Mwezi uliofuata Shirika la Kikristo la Mashahidi wa Yehova katika Rumania lilitambuliwa kisheria na serikali mpya ya Rumania. Katika 1991 Wizara ya Sheria katika Moscow ilijulisha kwamba Mkataba wa “Shirika la Kidini la Mashahidi wa Yehova Katika U.S.S.R.” ulisajiliwa rasmi. Mwaka uo huo kazi ya Mashahidi wa Yehova ilitambuliwa kisheria katika Bulgaria. Wakati wa 1992, Mashahidi wa Yehova katika Albania walitambuliwa kisheria.

Mashahidi wa Yehova walifanyaje na uhuru waliopewa? Mwandishi wa habari alimuuliza Helmut Martin, mratibu wa kazi ya Mashahidi wa Yehova katika GDR: “Je, mtaingia katika siasa?” Kwa vyovyote, hivyo ndivyo makasisi wengi wa Jumuiya ya Wakristo walikuwa wakifanya. “La,” akajibu Ndugu Martin, “Yesu aliwapa wanafunzi wake mgawo wa Kimaandiko, na tunaona huo kuwa kazi yetu kuu.”—Mt. 24:14; 28:19, 20.

Kwa kweli Mashahidi wa Yehova hawakuwa ndipo tu wanaanza kushughulikia daraka hilo katika sehemu hii ya ulimwengu. Ingawa ilikuwa lazima kwao kuendeleza utendaji wao chini ya hali ngumu sana kwa miaka mingi, katika nchi nyingi makutaniko (yakikutana katika vikundi vidogo) yalikuwa yakitenda kazi, na kutoa ushahidi kulikuwa kumefanywa. Lakini sasa fursa mpya ilikuwa ikifunguka. Wangeweza kufanya mikutano ambamo wangeweza kuwaalika watu wote kwa uhuru. Wangeweza kuhubiri peupe nyumba hadi nyumba, bila hofu ya kukamatwa. Hizi ni nchi zenye jumla ya idadi ya watu zaidi ya 390,000,000, kulikokuwa na kazi nyingi ya kufanywa. Mashahidi wa Yehova walitenda upesi, wakijua vema kwamba tunaishi katika siku za mwisho za mfumo wa mambo wa sasa wa ulimwengu.

Hata kabla ya kutambuliwa kisheria, washiriki wa Baraza Linaloongoza walikuwa wamezuru hesabu fulani ya nchi kuona yale ambayo yangeweza kufanywa ili kusaidia ndugu zao Wakristo. Baada ya marufuku kuondolewa, walisafiri kwenye sehemu hizo nyingi ili kusaidia kupanga kazi. Katika muda wa miaka michache, walikuwa wamekutana binafsi na kuzungumza na Mashahidi nchini Poland, Hungaria, Rumania, Chekoslovakia, Urusi, Ukrainia, Estonia, na Belarus.

Mikusanyiko ilipangwa ili kuimarisha Mashahidi wanaoishi katika nchi hizo na kujulisha sana umma kuhusu ujumbe wa Ufalme wa Mungu. Katika muda unaopungua miezi mitano baada ya marufuku kuondolewa na ile nchi iliyokuwa GDR wakati huo, mkusanyiko kama huo ulifanywa kwenye Stediamu ya Olympia ya Berlin. Mashahidi kutoka nchi nyinginezo 64 waliitikia kwa utayari mwaliko wa kuhudhuria. Waliihesabu kuwa pendeleo kufurahia pindi hiyo pamoja na ndugu na dada Wakristo ambao kwa miongo ya miaka walionyesha uaminifu-mshikamanifu kwa Yehova wajapokabiliwa na mnyanyaso mkali.

Katika 1990 na 1991 pia, mikusanyiko mingine ilifanywa kotekote katika Ulaya Mashariki. Baada ya makusanyiko manne ya huko kufanywa katika Hungaria katika 1990, mipango ilifanywa kwa ajili ya mkusanyiko wa kimataifa kwenye Népstadion katika Budapest katika 1991. Waliohudhuria walikuwa 40,601 kutoka nchi 35. Kwa mara ya kwanza kwa zaidi ya miaka 40, Mashahidi wa Yehova waliweza kufanya mikusanyiko ya peupe katika Rumania katika 1990. Mfululizo wa makusanyiko kotekote nchini, na baadaye mikusanyiko miwili mikubwa, ilifanywa mwaka huo. Kulikuwa na mikusanyiko minane zaidi katika 1991, kukiwa na hudhurio la 34,808. Katika 1990, katika ile iliyokuwa Yugoslavia, mikusanyiko ilifanywa katika kila mojawapo jamhuri zilizoifanyiza nchi hiyo. Mwaka uliofuata, ingawa kulikuwa na tisho la vita ya wenyewe kwa wenyewe katika nchi hiyo, Mashahidi wa Yehova 14,684 walifurahia mkusanyiko wa kimataifa katika Zagreb, jiji kuu la Kroatia. Polisi walishangaa walipoona Wakroatia, Wamontenegro, Waserbia, Waslovenia, na wengine wakikusanyika kwa amani kusikiliza programu.

Katika ile iliyokuwa wakati huo Chekoslovakia pia, mikusanyiko ilipangwa upesi. Mkusanyiko wa kitaifa katika Prague katika 1990 ulihudhuriwa na 23,876. Wasimamizi wa stediamu walifurahi sana kwa yale waliyoona hivi kwamba waliwapa Mashahidi mahali pakubwa zaidi nchini kwa ajili ya mkusanyiko wao ujao. Kwenye pindi hiyo ya kihistoria, katika 1991, kulikuwa na wahudhuriaji wa mkusanyiko 74,587 wenye idili waliojaa Stediamu ya Strahov katika Prague. Wajumbe Wacheki na Waslovaki walifurahi na kupiga makofi kwa idili tangazo lilipotolewa juu ya kutolewa kwa New World Translation of the Holy Scriptures iliyo kamili katika lugha zao wenyewe, ili itumiwe katika huduma ya shambani na katika funzo la kibinafsi na la kutaniko.

Ilikuwa pia wakati wa 1991 kwamba, kwa mara ya kwanza katika historia, Mashahidi wa Yehova waliweza kufanya mikusanyiko peupe katika sehemu zilizokuwa wakati huo katika Muungano wa Sovieti. Baada ya mkusanyiko katika Tallinn, Estonia, kulikuwa na mwingine katika Siberia. Minne ilifanywa katika majiji makuu katika Ukrainia, na mmoja katika Kazakhstan. Jumla ya hudhurio ilikuwa 74,252. Na kama matokeo ya kazi ya hivi karibuni ya kufanya wanafunzi ya Mashahidi wa Yehova katika maeneo hayo, 7,820 walijitokeza kwa ajili ya uzamisho wa maji. Huo haukuwa uamuzi wa kihisiamoyo uliofanywa kwa sababu walihisi wamechochewa na mkusanyiko. Waliotaka kubatizwa walikuwa wametayarishwa kwa uangalifu kimbele kwa kipindi cha miezi mingi—au miaka katika visa vingine.

Watu hao wote walitoka wapi? Ilikuwa wazi kwamba kazi ya Mashahidi wa Yehova haikuwa ikianza tu katika sehemu hiyo ya dunia. Vichapo vya Watch Tower vilikuwa vimepelekwa kwa posta kwa mtu aliyependezwa katika Urusi huko nyuma katika 1887. Msimamizi wa kwanza wa Watch Tower Society alikuwa amezuru Kishinev (sasa katika Moldova) yeye mwenyewe katika 1891. Baadhi ya Wanafunzi wa Biblia walikuwa wameenda Urusi kuhubiri wakati wa miaka ya 1920; lakini kulikuwa kumekuwa na upinzani mkali wa serikali, na vikundi vichache vilivyoonyesha kupendezwa na ujumbe wa Biblia vilikuwa vidogo. Hata hivyo, hali ilibadilika wakati na baada ya Vita ya Ulimwengu 2. Mipaka ya kitaifa iliwekwa upya, na sehemu kubwa ya idadi ya watu wakawekwa sehemu nyingine. Kama tokeo, zaidi ya Mashahidi elfu moja wanaosema Kiukrainia kutoka kwenye ile iliyokuwa Poland mashariki walijipata katika Muungano wa Sovieti. Mashahidi wengine walioishi Rumania na Chekoslovakia walipata kwamba sehemu walikoishi zilikuwa zimekuwa sehemu za Muungano wa Sovieti. Kwa kuongezea, Warusi waliokuwa wamekuwa Mashahidi wa Yehova walipokuwa katika kambi za mateso katika Ujerumani walirudi nchi zao, na kurudi wakiwa na habari njema za Ufalme wa Mungu. Kufikia 1946, kulikuwa na Mashahidi 4,797 wenye kutenda katika Muungano wa Sovieti. Wengi wao walihamishwa mahalimahali na serikali kwa muda wa miaka. Wengine walifungiwa katika kambi za magereza. Mahali popote walipoenda walitoa ushahidi. Idadi yao ikakua. Hata kabla serikali haijawatambua kisheria, wao wakiwa vikundi walikuwa wenye utendaji toka mbali Lviv upande wa magharibi hadi Vladivostok upande wa mpaka wa mashariki wa Muungano wa Sovieti, ng’ambo ya bahari kutoka Japani.

Wengi Sasa Wanataka Kusikiliza

Mashahidi walipofanya mikusanyiko katika ile iliyokuwa wakati huo U.S.S.R. katika 1991, umma ulikuwa na fursa ya kuwajua vema zaidi. Wao waliitikiaje? Katika Lviv, Ukrainia, ofisa mmoja wa polisi alimwambia mmoja wa wahudhuriaji wa mkusanyiko: “Mnajua sana kufundisha wengine yale yaliyo mema, mnasema juu ya Mungu, na hamjiingizi katika jeuri. Tulikuwa tukizungumza juu ya kwa nini tulikuwa tukiwanyanyasa, na tukafanya mkataa kwamba hatukuwa tumewasikiliza na hatukuwa tumejua lolote kuwahusu.” Lakini sasa wengi walikuwa wakisikiliza, na Mashahidi wa Yehova walitaka kuwasaidia.

Ili kuendeleza kazi yao kwa matokeo zaidi katika nchi hizo, fasihi za Biblia zilihitajiwa. Jitihada nyingi zilifanywa ili kuiandaa upesi. Katika Selters/Taunus, Ujerumani, Mashahidi wa Yehova walijenga vifaa vya uchapishaji vilivyo karibu mara mbili ya vile vya kwanza kwa ukubwa. Ingawa upanuzi huo haukuwa umekamilika, karibu majuma mawili baada ya marufuku kuondolewa katika ile iliyokuwa wakati huo Ujerumani Mashariki, tani 25 za fasihi zilisafirishwa hadi sehemu hiyo kutoka kwa matbaa ya uchapishaji katika Selters. Kuanzia wakati marufuku yalipoondolewa katika nchi za Ulaya Mashariki hadi 1992, karibu tani 10,000 za fasihi katika lugha kuu 14 zilisafirishwa kwenye nchi hizo mbalimbali kutoka Ujerumani, tani nyingine 698 kutoka Italia, na nyinginezo kutoka Finland.

Kwa kuwa Mashahidi walikuwa wametengwa sana kwa miaka mingi, katika nchi fulanifulani walihitaji msaada katika mambo ya usimamizi wa kutaniko na usimamizi wa kitengenezo. Ili kujazia uhitaji huo wa haraka, wazee wenye ujuzi—wale ambao wangeweza kusema lugha ya nchi hiyo, ilipowezekana—walifikiwa katika Ujerumani, Marekani, Kanada, na kwingineko. Je, wangependa kuhamia kwenye mojawapo nchi hizo za Ulaya Mashariki ili kusaidia kujazia uhitaji huo? Itikio lilikuwa lenye kupendeza kwelikweli! Mahali ilipofaa, wazee waliokuwa wamezoezwa kwenye Shule ya Gileadi au katika Shule ya Mazoezi ya Kihuduma walitumwa pia.

Kisha, katika 1992 mkusanyiko wa kimataifa wenye kutokeza ulifanywa katika St. Petersburg, jiji la pili kwa ukubwa katika Urusi. Karibu 17,000 kati ya wajumbe walitoka nchi 27 nje ya Urusi. Utangazaji mkubwa wa mkusanyiko huo ulifanywa. Kati ya wale waliokuja walikuwa watu ambao hawakuwa wamepata kusikia juu ya Mashahidi wa Yehova. Hudhurio lilifikia kilele cha 46,214. Wajumbe walikuwa wametoka sehemu zote za Urusi, wengine wao kutoka mbali sana mashariki kama Kisiwa cha Sakhalin, karibu na Japani. Vikundi vikubwa vilitoka Ukrainia, Moldova, na nchi nyinginezo ambazo hapo awali zilikuwa sehemu ya U.S.S.R. Walikuja na habari njema. Ripoti zilionyesha kwamba makutaniko mbalimbali katika majiji kama vile Kiev, Moscow, na St. Petersburg yalikuwa na wastani wa hudhurio kwenye mikutano yayo ambayo ilikuwa mara mbili au zaidi ya idadi ya Mashahidi. Watu wengi waliotaka Mashahidi wa Yehova wajifunze nao Biblia walilazimika kuwekwa kwenye orodha ya wanaongojea. Kutoka Latvia, wajumbe 600 walikuwa wamekuja na hata wengi zaidi kutoka Estonia. Kutaniko katika St. Petersburg lilikuwa na zaidi ya watu mia moja waliokuwa tayari kubatizwa kwenye mkusanyiko. Wengi wa wale wanaoonyesha kupendezwa ni vijana au watu wenye masomo ya juu. Kwelikweli, kazi kubwa ya mavuno ya kiroho inaendelea katika eneo hilo kubwa ambalo kwa muda mrefu lilionwa na ulimwengu kuwa ngome ya wasioamini kuwako kwa Mungu!

Mashamba Meupe Tayari kwa Mavuno

Mitazamo kuhusu uhuru wa kidini ilipobadilika, nchi nyinginezo pia, ziliondoa vizuizi dhidi ya Mashahidi wa Yehova au zikawapa utambulisho wa kisheria waliokuwa wamenyimwa kwa muda mrefu. Katika nyingi za sehemu hizo, mavuno mengi ya kiroho yalikuwa tayari kukusanywa. Hali ilikuwa kama ile ambayo Yesu alielezea wanafunzi wake aliposema: “Inueni macho yenu na mtazame mashamba, kwamba ni meupe kwa ajili ya kuvunwa.” (Yn. 4:35, NW) Fikiria sehemu chache tu ambako hilo limekuwa kweli barani Afrika.

Huduma ya nyumba hadi nyumba ya Mashahidi wa Yehova ilikuwa imepigwa marufuku katika Zambia katika 1969. Kama tokeo, Mashahidi huko walitumia wakati zaidi kuongoza mafunzo ya Biblia nyumbani kwa waliopendezwa. Wengine pia walianza kuwatafuta Mashahidi ili wapokee mafunzo. Hatua kwa hatua vizuizi vya serikali viliondolewa, na hudhurio la mikutano likaongezeka. Katika 1992, kulikuwa na 365,828 waliohudhuria Mlo wa Jioni wa Bwana katika Zambia, 1 kati ya kila 23 wa idadi ya watu wote!

Kaskazini mwa Zambia, katika Zaire, maelfu zaidi walitaka kujua yale wanayofundisha Mashahidi wa Yehova kuhusu maisha ya Kikristo na kuhusu kusudi la Mungu kwa wanadamu. Katika 1990 hali ziliporuhusu Mashahidi kufungua tena Majumba yao ya Ufalme, katika sehemu nyingine watu kama 500 walikusanyika kwenye mikutano yao. Katika muda wa miaka miwili Mashahidi 67,917 katika Zaire walikuwa wakiongoza mafunzo ya Biblia nyumbani 141,859 na watu hao.

Hesabu ya nchi zilizokuwa zikifunguka ilikuwa yenye kushangaza. Katika 1990, wamishonari wa Watch Tower waliokuwa wamefukuzwa kutoka Benin miaka 14 mapema sasa walipewa fursa rasmi ya kurudi, na mlango ulifunguliwa kwa wengine kuja. Mwaka uo huo, Waziri wa Sheria katika Jamhuri ya Cape Verde alitia sahihi sheria iliyokubali kanuni za Shirika la Mashahidi wa Yehova la huko, hivyo akiwapa utambulisho wa kisheria. Kisha, katika 1991 marufuku iliondolewa juu ya Mashahidi wa Yehova katika Msumbiji (ambako watawala wa zamani walikuwa wamewanyanyasa sana), Ghana (ambako utendaji wao ulikuwa chini ya vizuizi vya serikali), na Ethiopia (ambako haikuwezekana kuhubiri peupe au kufanya makusanyiko kwa miaka 34). Kabla ya mwaka huo kwisha, Niger na Kongo zilikuwa pia zimewatambua kisheria. Mapema katika 1992, marufuku yaliondolewa au utambulisho wa kisheria ukapewa Mashahidi wa Yehova katika Chad, Kenya, Rwanda, Togo, na Angola.

Huko kulikuwa mashamba yaliyokuwa tayari kuvunwa kiroho. Katika Angola, kwa kielelezo, Mashahidi walipata upesi ongezeko la asilimia 31; zaidi ya hiyo, wapiga-mbiu wa Ufalme huko karibu 19,000 walikuwa wakiongoza mafunzo ya Biblia nyumbani karibu 53,000. Ili kuandaa msaada wa usimamizi uliohitajika kwa ajili ya programu kubwa ya elimu ya Biblia katika Angola na pia Msumbiji (ambako wengi husema Kireno), wazee waliostahili kutoka Ureno na Brazili walialikwa kuhamia Afrika ili kuendeleza huduma yao. Wamishonari wenye kusema Kireno walipewa mgawo kwenye eneo jipya lililofunguka la Guinea-Bissau. Na Mashahidi wenye uwezo katika Ufaransa na nchi nyinginezo walialikwa kusaidia kutimiza kazi ya haraka ya kuhubiri na kufanya wanafunzi katika Benin, Chad, na Togo, ambako Kifaransa husemwa na watu wengi.

Kati ya sehemu zile ambazo zimetokeza mazao mengi hasa ya wasifaji wa Yehova ni zile zilizokuwa ngome za Katoliki ya Roma awali. Kwa kuongezea Amerika ya Latin, hilo lilithibitika kuwa kweli kwa Ufaransa (ambako ripoti ya 1992 ilionyesha waeneza-evanjeli Mashahidi kama 119,674, Hispania (ambako kulikuwa na 92,282), Filipino (kukiwa na 114,335), Ireland (yenye ukuzi wa Mashahidi upatao asilimia 8 hadi 10 kila mwaka), na Ureno.

Wakati Mashahidi 37,567 walipohudhuria mkusanyiko katika Lisbon, Ureno, katika 1978, gazeti Opção lilisema: “Kwa yeyote ambaye amepata kwenda Fátima wakati wa kuhiji, hii ni tofauti sana kihalisi. . . . Hapa [kwenye mkusanyiko wa Mashahidi wa Yehova] hali ya kifumbo inatoweka, mahali payo pakichukuliwa na kufanywa mkutano ambapo waamini kwa upatano huzungumzia matatizo yao, imani yao na mtazamo wao wa kiroho. Mwenendo wao kuelekea mmoja na mwenzake hutoa alama yenye kutofautisha ya uhusiano wenye kujali.” Wakati wa mwongo uliofuata, idadi ya Mashahidi katika Ureno iliongezeka kwa karibu asilimia 70.

Vipi kuhusu Italia? Upungufu mkubwa wa wanaotaka kuwa mapadri wa Katoliki unalazimu seminari kadhaa zifunge milango yazo. Makanisa mengi hayana padri wa parishi. Katika visa vingi majengo yaliyokuwa makanisa sasa ni maduka au ofisi. Kujapokuwa yote hayo, kanisa limepiga vita vikali ili kukomesha Mashahidi wa Yehova. Katika miaka iliyopita waliwachochea maofisa kufukuza Mashahidi wamishonari na kutaka kwamba polisi wafunge mikutano yao. Katika maeneo fulani wakati wa miaka ya 1980, mapadri wa parishi waliweka taarifa kwenye milango ya kila mtu (mingine ikiwa ile ya Mashahidi wa Yehova), zilizosema: “Usipige Hodi. Sisi Ni Wakatoliki.” Magazeti ya habari yalikuwa na vichwa vikuu: “Kulalamika Vikali kwa Kanisa Dhidi ya Mashahidi wa Yehova” na “‘Vita Vitakatifu’ Dhidi ya Mashahidi wa Yehova.”

Ukuhani wa Kiyahudi wa karne ya kwanza ulipojaribu kunyamazisha mitume, Gamalieli, mwalimu wa Torati, alishauri hivi kwa hekima: “Ikiwa mpango huu au kazi hii ni kutoka kwa wanadamu, itapinduliwa; lakini ikiwa ni kutoka kwa Mungu, hamtaweza kuwapindua.” (Mdo. 5:38, 39, NW) Tokeo lilikuwa nini wakati ukuhani wa Katoliki ya Roma ya karne ya 20 ilipojaribu kuwanyamazisha Mashahidi wa Yehova? Kazi ya wale Mashahidi 120 katika Italia katika 1946 haikuvunjwa. Badala yake, kufikia 1992, kulikuwa na Mashahidi watendaji 194,013 walioshirikiana na makutaniko 2,462 kotekote nchini. Karibu wameijaza Italia kwa mafundisho yao ya Neno la Mungu. Tangu 1946 wametoa zaidi ya muda wa saa milioni 550 kuzungumza kwa Waitaliano wenzao kuhusu Ufalme wa Mungu. Huku wakifanya hivyo, wameweka mikononi mwao mamilioni ya nakala za Biblia yenyewe kutia na zaidi ya vitabu, vijitabu, na magazeti milioni 400 yanayoeleza Maandiko. Wanataka kuhakikisha kwamba watu wa Italia wana fursa kamili ya kuchukua msimamo upande wa Yehova kabla ya Har–Magedoni kuja. Huku wakifanya hivyo, wanakumbuka yale ambayo mtume Paulo aliandika kwenye 2 Wakorintho 10:4, 5 (NW) yaani: “Kwa maana silaha za shughuli yetu ya vita si za kimwili, bali zenye nguvu kupitia Mungu kwa ajili ya kupindua mambo yaliyotiwa kwa nguvu sana katika mahandaki. Kwa maana sisi tunapindua mawazowazo na kila jambo lililoinuka sana lililoinuliwa dhidi ya ujuzi wa Mungu.”

Mashahidi wa Yehova hawaelekezi fikira tu kwa zile zilizokuwa ngome za Ukatoliki. Wanajua kwamba Yesu Kristo alisema: “Lazima habari njema ihubiriwe kwanza.” (Mk. 13:10, NW) Na hiyo ndiyo kazi ambayo Mashahidi wanafanya. Kufikia 1992, kulikuwa 12,168 wenye shughuli wakiwaambia watu katika India kuhusu Ufalme wa Mungu. Wengine 71,428 walikuwa wakihubiri katika Jamhuri ya Korea. Katika Japani, kulikuwa na 171,438, na idadi yao ilikua kila mwezi. Pia waliendelea kufikia nchi ambako ni kazi ndogo ya kuhubiri au hakuna yoyote iliyopata kufanywa huko.

Hivyo, wakati wa sehemu ya mwisho ya miaka ya 1970, waliweza, kwa mara ya kwanza, kupeleka ujumbe wa Ufalme kwa watu wanaoishi kwenye Visiwa vya Marquesas na Kosrae—vyote katika Bahari ya Pasifiki. Pia walifikia Bhutan, inayoungana na mpaka wa kusini wa China, na visiwa vya Komoro, kutoka pwani ya mashariki mwa Afrika. Wakati wa miaka ya 1980, kazi ya kwanza ya kuhubiri ya Mashahidi wa Yehova iliripotiwa kutoka Visiwa vya Wallis na Futuna, kutia na visiwa vya Nauru na Rota, vyote vikiwa katika kusini-magharibi mwa Pasifiki. Baadhi yavyo vilikuwa sehemu ndogo kwa kadiri fulani; lakini watu huishi huko, na uhai ni wenye thamani. Mashahidi wa Yehova wanajua vema unabii wa Yesu kwamba kabla ya mwisho kuja, ujumbe wa Ufalme ungehubiriwa “katika dunia yote inayokaliwa.”—Mt. 24:14, NW.

Kuwafikia Watu Mahali Panapowezekana na Wakati Inapowezekana

Ingawa mahubiri ya nyumba hadi nyumba yanaendelea kuwa njia kuu inayotumiwa na Mashahidi wa Yehova ili kuwafikia watu, wanatambua kwamba hata kwa njia hiyo ya utaratibu, hawawezi kumfikia kila mtu. Wakiwa na hisi ya uharaka, wanaendelea kuwatafuta watu mahali popote wanapoweza kupatikana.—Linganisha Yohana 4:5-42; Matendo 16:13, 14.

Meli zinapotia nanga kwenye bandari za Ujerumani na Uholanzi, hata zitue kwa muda mfupi, Mashahidi wa Yehova hujitahidi kuzizuru, wakitoa ushahidi kwanza kwa nahodha na kisha kwa mabaharia. Wao hubeba fasihi za Biblia katika lugha nyingi kwa ajili ya wanaume hao. Katika masoko ya wenyeji ya Chad, katika Afrika ya kati, ni jambo la kawaida kuona kikundi cha watu 15 au 20 kimekusanyika kuzunguka mmoja wa Mashahidi wa Yehova anayezungumza nao kuhusu tumaini la Ufalme wa Mungu. Wakifanya kazi kwa zamu, Mashahidi huzungumza na wauzaji na maelfu ya wanunuzi wa Jumamosi asubuhi kwenye masoko yanayouza vitu vilivyokwisha kutumika katika Auckland, New Zealand. Watu wanaopitia stesheni kuu za mabasi katika Guayaquil, Ekuado—wengi wao kutoka sehemu za mbali za nchi—hufikiwa huko na Mashahidi wanaowapa broshua ya wakati ufaao au La Atalaya na ¡Despertad! Mashahidi huwazuru wale wanaofanya kazi katika zamu ya usiku katika masoko ya chakula ya wakati wote katika New York City wakiwa kazini ili wao pia wawe na fursa ya kusikia habari njema.

Wanaposafiri kwa ndege, garimoshi, mabasi, na garimoshi la chini ya ardhi, wengi wa Mashahidi wa Yehova hushiriki kweli za Biblia zenye thamani na abiria wenzao. Wakati wa chakula cha mchana kwenye kazi zao za kimwili na shuleni, pia watu wanapokuja milangoni pao kwa sababu za kibiashara, wao huchukua fursa ya kutoa ushahidi. Wanajua kwamba wengi wa watu hao huenda wasiwe nyumbani Mashahidi wanapofanya ziara zao za kawaida.

Wanapotoa ushahidi kwa wengine, hawasahau washiriki wa karibu wa familia na watu wengineo wa ukoo. Lakini wakati Maria Caamano, Shahidi katika Argentina, alipojaribu kuambia familia yake jinsi alivyochochewa na yale aliyojifunza kutoka kwa Biblia, walimfanyia mzaha au wakampuuza. Yeye hakukata tamaa lakini alisafiri kilometa 1,900 kutolea ushahidi baadhi ya watu wake wa ukoo. Wengine waliitikia ifaavyo. Pole kwa pole, wengine walisikiliza. Kama tokeo, sasa kuna zaidi ya watu wazima 80 na zaidi ya watoto 40 kati ya watu wake wa ukoo ambao wamekubali kweli za Biblia na wanazishiriki na wengine.

Ili kusaidia watu wake wa ukoo, Michael Regan alihama kwenda mji alikozaliwa, Boyle, Wilaya ya Roscommon, katika Ireland. Aliwatolea wote ushahidi. Mpwa wake wa kike alivutiwa na ile roho ya furaha na njia ya maisha inayofaa ya watoto wa Michael. Upesi yeye na mume wake walikubali kujifunza Biblia. Walipobatizwa, baba yake alimkataza kabisa asije kwake. Hata hivyo, hatua kwa hatua, mtazamo wake ukawa mzuri, na akakubali fasihi fulani—akikusudia kufunua “kosa” la Mashahidi. Lakini upesi aling’amua kwamba yale aliyokuwa akisoma yalikuwa ya kweli, na akabatizwa baadaye. Washiriki wa familia zaidi ya 20 sasa wanashirikiana na kutaniko, wengi wao wakiwa tayari wamebatizwa.

Namna gani watu waliomo gerezani? Je, wangeweza kunufaika na ujumbe wa Ufalme wa Mungu? Mashahidi wa Yehova hawawapuuzi. Kwenye gereza moja katika Amerika Kaskazini, mipango ya mafunzo ya Biblia ya kibinafsi na wafungwa, kutia na hudhurio la kawaida la mikutano iliyoongozwa gerezani na Mashahidi wa Yehova, ilikuwa na matokeo mazuri sana hivi kwamba wasimamizi wa gereza walifanya iwezekane kufanya makusanyiko humo. Hayo yalihudhuriwa si na wafungwa tu bali pia maelfu ya Mashahidi kutoka nje. Katika nchi nyinginezo pia, jitihada nyingi zinafanywa ili kutoa ushahidi kwa wanaume na wanawake gerezani.

Mashahidi wa Yehova hawaamini kwamba funzo la Biblia litawabadili wafungwa wote. Lakini wanajua kutokana na yaliyoonwa kwamba wengine wao wanaweza kusaidiwa, na wanataka kuwapatia fursa ya kukubali tumaini la Ufalme wa Mungu.

Jitihada za Kurudiarudia ili Kufikia Mioyo

Mashahidi wa Yehova huwazuru watu tena na tena. Kama vile wanafunzi wa Yesu wa mapema walivyofanya, wao ‘huenda kwa kuendelea’ kwa watu katika maeneo yao waliyogawiwa ili kujaribu kuamsha kupendezwa kwao katika Ufalme wa Mungu. (Mt. 10:6, 7, NW) Katika sehemu nyinginezo wao huweza kuzuru watu wote wa nyumba katika eneo hilo mara moja tu kwa mwaka; kwingineko, wanazuru kila baada ya miezi michache. Katika Ureno, Lisbon jijini na viungani, ambako kuna uwiano wa Shahidi 1 kwa kila 160 ya idadi ya watu wote, watu hutembelewa na Mashahidi kila juma hivi. Katika Venezuela, kuna majiji ambamo maeneo huenezwa kwa ukawaida zaidi ya mara moja kwa juma.

Mashahidi wa Yehova wanapofanya ziara za kurudiarudia, hawajaribu kulazimisha ujumbe wa Biblia kwa watu. Wao wanajitahidi tu kuwapa fursa ya kufanya uamuzi wenye akili. Leo, huenda watu wengine wakasema hawapendezwi; lakini mabadiliko makubwa maishani mwao au katika hali za ulimwengu yaweza kuwafanya wawe wasikivu zaidi wakati mwingine. Kwa sababu ya chuki au kwa sababu tu ya kuwa wenye shughuli mno kuweza kusikiliza, watu wengi hawajapata kusikiliza kikweli yale ambayo Mashahidi hufundisha. Lakini ziara za kurudiarudia zenye urafiki zaweza kuwafanya wasikilize. Mara nyingi watu huvutiwa na unyoofu na uaminifu-maadili wa Mashahidi wanaoishi katika ujirani wao au ambao ni wafanyakazi wenzao. Kama tokeo, baada ya wakati, wengine hupendezwa kiasi cha kutaka kujua lengo la ujumbe wao. Baada ya kupokea fasihi kwa furaha na toleo la funzo la Biblia nyumbani bila malipo, mwanamke mmoja katika Venezuela alisema: “Mtu yeyote hajapata kamwe kunielezea mambo hayo.”

Kwa njia ya fadhili, Mashahidi hujitahidi kufikia mioyo ya wale wanaozungumza nao. Katika Guadeloupe, ambako kulikuwa na Shahidi 1 kwa kila 57 ya idadi ya watu wote katika 1992, ni kawaida kwa wenye nyumba kusema, “Mimi sipendezwi.” Kwa hilo, Eric Dodote alikuwa akijibu: “Ninakuelewa, na ninajua jinsi unavyohisi.” Kisha angeongeza: “Lakini ebu nikuulize, Je, ungependa kuishi katika hali bora kuliko zile zilizoko leo?” Baada ya kusikia yale ambayo mwenye nyumba alisema, alikuwa akitumia Biblia kuonyesha jinsi Mungu atakavyoleta hali hizo katika ulimwengu Wake mpya.

Kueneza Eneo kwa Ukamili Hata Zaidi

Katika miaka ya hivi karibuni, imezidi kuwa vigumu katika nchi nyingine kuwapata watu nyumbani. Mara nyingi, mume na mke pia wameajiriwa, na kwenye miisho juma huenda wakafuatia tafrija mbali na nyumbani. Ili kuwezana na hali hiyo, katika nchi nyingi Mashahidi wa Yehova wanazidi kufanya kiasi kikubwa cha kutoa ushahidi mlango kwa mlango jioni. Katika Uingereza, Mashahidi wengine hawafuatii tu wale wasio nyumbani wakianza kati ya saa 12 na saa 2 za usiku, bali wengine, katika jitihada za kuwafikia watu kabla ya wao kuondoka kwenda kazini, huzuru kabla ya saa 2 asubuhi.

Hata mahali ambapo watu wamo nyumbani, huenda ikawa vigumu sana kuwafikia bila mwaliko wa mapema, kwa sababu ya ulinzi mkali walioweka kwa sababu ya uhalifu mwingi. Lakini katika Brazili wakati wengine walio wagumu kupatikana wanapoenda kutembea mapema asubuhi kwenye mahali pa kutembelea Pwani ya Copacabana, huenda wakafikiwa na Shahidi mwenye bidii ambaye yuko huko mapema vilevile akiwashirikisha wengine katika mazungumzo kuhusu jinsi Ufalme wa Mungu utakavyosuluhisha matatizo ya wanadamu. Katika Paris, Ufaransa, watu wanaporudi kwenye nyumba zao za orofa jionijioni, huenda wakapata mume na mke walio Mashahidi wenye urafiki wakiwa karibu na kiingilio cha jengo hilo, wakingoja kusema na wakazi mmoja-mmoja wanaoweza kusikiliza kwa dakika chache kuhusu njia ambayo Mungu atatumia kuleta usalama wa kweli. Katika Honolulu, New York City, na sehemu nyingi nyinginezo, jitihada hufanywa pia ili kufikia wenyeji wa majengo yenye ulinzi mkali kwa njia ya simu.

Wanapoweza kumfikia kila mtu katika kila nyumba, bado Mashahidi hawahisi kwamba kazi yao imekamilika. Tamaa yao ni kuwafikia watu wengi mmoja-mmoja kadiri iwezekanavyo katika kila nyumba. Wakati mwingine hilo hutimizwa kwa kuzuru siku au wakati tofauti. Katika Puerto Riko wakati mwenye nyumba aliposema hapendezwi, Shahidi alimwuliza ikiwa kulikuwa na mtu mwingine ndani ya nyumba ambaye angezungumza naye. Hilo liliongoza kwenye mazungumzo na mwanamume wa nyumba hiyo, aliyekuwa amekuwa mgonjwa kwa miaka 14 na ambaye alikuwa kitandani kwa muda mwingi. Moyo wake ulichangamshwa na tumaini lililo katika Neno la Mungu. Akipendezwa upya na uhai, aliondoka kitandani upesi, akihudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme, na kushiriki tumaini lake jipya na wengine.

Kuongeza Bidii Katika Kutoa Ushahidi Mwisho Ukaribiapo

Jambo jingine limesaidia sana katika kuongezwa kwa bidii ya kutoa ushahidi katika miaka ya karibuni. Hilo limekuwa ni kuongezeka kwa idadi ya Mashahidi wanaotumikia wakiwa mapainia. Wakitaka sana kutumia wakati wao mwingi kadiri iwezekanavyo kwa utumishi wa Mungu, na kwa kuhangaikia wenzao kwa upendo, wao hupanga mambo yao ili kutumia saa 60, 90, 140 au zaidi kila mwezi katika huduma ya shambani. Kama ilivyokuwa kwa mtume Paulo alipohubiri katika Korintho, Ugiriki, wale wanaoanza utumishi wa painia ‘husongwa sana na lile neno,’ wakitafuta kutoa ushahidi kwa watu wengi iwezekanavyo kwa kadiri iyo hiyo kuhusu Ufalme wa Kimesiya.—Mdo. 18:5.

Katika 1975 kulikuwa na mapainia 130,225 ulimwenguni pote. Kufikia 1992 kulikuwa na 605,610 kwa wastani kila mwezi (kutia na mapainia wa kawaida, wasaidizi, na wa pekee). Hivyo, wakati wa kipindi ambacho idadi ya Mashahidi ulimwenguni pote ilikua kwa asilimia 105, wale waliotenga nafasi ili kushiriki katika huduma ya wakati wote waliongezeka kwa asilimia 365! Kama tokeo, kiasi cha wakati kinachotolewa hasa kwa kutoa ushahidi kuliinuka kutoka milioni 382 hivi hadi saa zaidi ya bilioni moja kwa mwaka!

‘Mdogo Awa Elfu’

Yesu Kristo aliwaagiza wafuasi wake kuwa mashahidi wake hadi sehemu za mbali zaidi sana za dunia. (Mdo. 1:8) Kupitia nabii Isaya, Yehova alitabiri: “Mdogo atakuwa elfu, na mnyonge atakuwa taifa hodari; Mimi, BWANA, nitayahimiza hayo wakati wake.” (Isa. 60:22) Rekodi inaonyesha wazi kwamba Mashahidi wa Yehova wanafanya kazi ambayo Yesu alitabiri, na wamepata aina ya ukuzi ambayo Mungu mwenyewe aliahidi.

Mwishoni mwa Vita ya Ulimwengu 2, walipatikana hasa katika Amerika Kaskazini na Ulaya; na kulikuwa na wengine barani Afrika; na wengine katika vikundi vidogo, walitawanyika duniani pote. Hawakuwa wamefikia hata kidogo kila nchi na ujumbe wa Ufalme, wala hawakuwa wamefikia kila sehemu ya nchi walizokuwa wakihubiri. Hata hivyo, kwa mwendo wa kasi wenye kustaajabisha, hali hiyo imekuwa ikibadilika.

Fikiria Amerika Kaskazini. Bara kuu huenea toka Kanada upande wa kaskazini hadi Panama, nchi tisa zikiwa katikati. Kufikia 1945 kulikuwa Mashahidi 81,410 katika sehemu hiyo kubwa. Nchi nne kati ya hizo ziliripoti Mashahidi chini ya 20 kila moja, na nchi moja haikuwa na kazi ya kuhubiri iliyopangwa kwa vyovyote. Tangu wakati huo, ushahidi mwingi na wa kuendelea umetolewa katika nchi hizo zote. Kufikia 1992, kulikuwa na Mashahidi wa Yehova 1,440,165 katika sehemu hiyo ya dunia. Katika nchi nyingi kati ya hizo, kila Shahidi kwa wastani, sasa ana mamia machache tu ya watu wa kutolea ushahidi. Sehemu kubwa ya watu wote hutembelewa na Mashahidi kila baada ya miezi michache; wengi hutembelewa kila juma. Mafunzo ya Biblia nyumbani zaidi ya 1,240,000 yanaongozwa kwa ukawaida na watu mmoja-mmoja na vikundi vinavyopendezwa.

Vipi kuhusu Ulaya? Sehemu hii ya dunia huenea kutoka Skandinevia hadi kusini mwa Mediterania. Nje ya sehemu kubwa iliyokuwa ikiitwa Muungano wa Sovieti, ushahidi mwingi ulikuwa tayari umetolewa katika Ulaya kabla ya Vita ya Ulimwengu 2. Tangu wakati huo, vizazi vipya vimekua, na hivyo pia vinaonyeshwa kutoka Maandiko kwamba Ufalme wa Mungu karibuni utachukua mahali pa serikali za kibinadamu. (Dan. 2:44) Kutoka mamia kadhaa ya Mashahidi walioendelea na utendaji wao wa kuhubiri chini ya vizuizi vikali wakati wa vita, idadi ya wapiga-mbiu wa Ufalme katika nchi 47 ambazo ziliripoti na kutangazwa katika 1992 ilikuwa imepanda hadi 1,176,259, kutia wale walio katika sehemu ambazo zilikuwa sehemu za U.S.S.R., katika Ulaya na Asia pia. Katika kila mojawapo nchi tano—Italia, Poland, Ufaransa, Uingereza, na Ujerumani—kulikuwa na Mashahidi wenye bidii zaidi ya 100,000. Na Mashahidi hao wote walikuwa wakifanya nini? Ripoti yao ya 1992 inaonyesha kwamba katika mwaka huo, walitoa saa zaidi ya 230,000,000 kwa kuhubiri peupe, kwenda nyumba hadi nyumba, na kuongoza mafunzo ya Biblia nyumbani. Katika kueneza kwao evanjeli, Mashahidi hao hawakupita hata jamhuri ndogo ya San Marino, nchi kama vile Andorra na Liechtenstein, au Gibraltar. Kwelikweli, ushahidi uliotabiriwa ulikuwa ukitolewa.

Afrika pia inapokea ushahidi mwingi. Rekodi zinaonyesha kwamba kufikia 1945, habari njema zilikuwa zimefikia nchi 28 kwenye bara hilo, lakini ni ushahidi mdogo sana uliokuwa umetolewa katika nchi nyingi. Hata hivyo, tangu wakati huo, mengi yametimizwa huko. Kufikia 1992, kulikuwa na Mashahidi wenye bidii 545,044 katika bara la Afrika, wakihubiri habari njema katika nchi 45. Kwenye mwadhimisho wa Mlo wa Jioni wa Bwana mwaka huo, 1,834,863 walikuwapo. Kwa hiyo, si kwamba tu ukuzi umekuwa wa kustaajabisha tu, bali pia uwezekano wa upanuzi zaidi si wa kawaida!

Ripoti kutoka Amerika Kusini inashangaza pia. Ingawa nchi zote 13 isipokuwa moja zilikuwa zimefikiwa na ujumbe wa Biblia kabla ya Vita ya Ulimwengu 2, wakati huo kulikuwa na makutaniko 29 tu kwenye bara lote, na hakukuwa na utendaji wa kuhubiri uliopangwa katika baadhi ya nchi hizo. Kazi nyingi ya kuhubiri Ufalme wakati huo ilikuwa ya wakati ujao. Tangu wakati huo Mashahidi huko wamefanya kazi kwa bidii. Wale ambao wameburudishwa na maji ya uhai hualika wengine kwa furaha, wakisema: ‘Njooni, mchukue maji ya uhai bure.’ (Ufu. 22:17, NW) Katika 1992, kulikuwa na watumishi wa Yehova 683,782 katika makutaniko 10,399 katika Amerika Kusini wakishiriki kwa furaha katika kazi hiyo. Wengine wao walikuwa wakifikia maeneo ambayo hayakuwa yamepata ushahidi kamili. Wengine walikuwa wakizuru tena na tena mahali ambapo ushahidi ulikuwa tayari umetolewa, ili kuwatia watu moyo ‘waonje waone kwamba Yehova ni mwema.’ (Zab. 34:8) Walikuwa wakiongoza mafunzo ya Biblia nyumbani 905,132 kwa ukawaida ili kusaidia wanaopendezwa wafanye njia za Yehova ziwe njia zao wenyewe za maisha.

Fikiria pia Asia na visiwa vingi na vikundi vya visiwa kotekote duniani. Ni nini kimetimizwa huko? Hadi kufikia wakati wa baada ya vita, sehemu nyingi hazikuwa zimepigiwa mbiu ya Ufalme. Lakini Yesu Kristo alitabiri kwamba habari njema hizi za Ufalme zingehubiriwa “katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya kuwa ushahidi kwa mataifa yote.” (Mt. 24:14, NW) Kupatana na hilo, wakati wa miongo ya miaka tangu Vita ya Ulimwengu 2, kuhubiriwa kwa habari njema kulikokuwa kumefikia nchi, visiwa, na vikundi vya visiwa 76 awali kulienea katika vingine 40 kulifanywa kwa bidii zaidi katika sehemu zilizofikiwa kwanza. Katika eneo hilo kubwa, katika 1992 kulikuwa Mashahidi waliojitoa kama 627,537 walioona furaha kubwa kujulisha watu “matendo yake [ya Yehova] makuu, na utukufu wa fahari ya ufalme wake.” (Zab. 145:11, 12) Huduma yao haikuwa rahisi. Katika sehemu nyingine walilazimika kusafiri kwa muda wa saa nyingi kwa meli au ndege ili kufikia visiwa vya mbali katika eneo lao. Lakini wakati wa 1992 walitoa muda wa saa zaidi ya 200,000,000 kwenye kazi ya kueneza evanjeli na wakaongoza mafunzo ya Biblia nyumbani 685,211 kwa ukawaida.

Utimizo wa ahadi kwamba ‘mdogo angekuwa elfu’ umetukia kikweli, tena sana! Katika kila mojawapo nchi 50 na zaidi, ambako hakukuwa hata na ‘mdogo’—ambako hakukuwa na Mashahidi wa Yehova wowote huko nyuma katika 1919, ambako hawakuwa wamehubiri hata kidogo—leo kuna wasifaji wa Yehova zaidi ya elfu moja. Katika baadhi ya nchi hizo, sasa kuna makumi ya maelfu, naam, hata zaidi ya mia moja elfu, ya Mashahidi wa Yehova ambao ni wapiga-mbiu wa Ufalme wa Mungu wenye bidii! Ulimwenguni pote, Mashahidi wa Yehova wamekuwa “taifa hodari”—wengi wakiwa kutaniko lililounganika la duniani kuliko idadi ya watu wote ya mojawapo mataifa huru ya ulimwengu angalau 80.

Ni Kadiri Gani ya Ushahidi Umetolewa Katika “Nchi Nyinginezo”?

Zinazotiwa ndani katika yote yaliyo juu, kufikia 1992, kulikuwa kungali “nchi nyinginezo” 24—ambako Mashahidi wa Yehova walikuwa chini ya vizuizi vikali vya serikali na ambako hakukuwa na ripoti kamili zilizotangazwa. Ushahidi mwingi umetolewa katika baadhi ya nchi hizo. Na bado, katika nchi nyinginezo idadi ya Mashahidi ni ndogo kikweli. Bado kuna watu ambao hawajasikia ujumbe wa Ufalme. Lakini Mashahidi wa Yehova wana uhakika kwamba ushahidi unaohitajika utatolewa. Kwa nini?

Kwa sababu Maandiko yanaonyesha kwamba Yesu Kristo, kutoka kiti chake cha enzi mbinguni, anaongoza kazi hiyo yeye mwenyewe. Chini ya uelekezi wake ‘malaika anayeruka katika mbingu ya kati’ anakabidhiwa daraka la kujulisha habari njema za milele na kuhimiza watu wakaao juu ya ‘kila taifa na kabila na lugha na kikundi cha watu, wamhofu Mungu na kumpa utukufu.’ (Ufu. 14:6, 7, NW) Hakuna uwezo mbinguni au duniani unaoweza kuzuia Yehova asiwavute kwake wale wenye “mwelekeo ufaao kwa ajili ya uhai udumuo milele.”—Mdo. 13:48; Yn. 6:44, NW.

Hakuna sehemu ya dunia iliyo mbali sana hivi kwamba ujumbe wa Ufalme hauwezi kufika. Watu wa ukoo huzuru. Simu na barua huwa na habari. Wafanyabiashara, wafanyakazi, wanafunzi, na watalii hukutana na watu wa mataifa mengine. Kama vile ilivyokuwa zamani, ndivyo na sasa, habari za maana kwamba Yehova amemtawaza Mfalme wake wa kimbingu akiwa na mamlaka juu ya mataifa zaendelea kujulishwa kwa njia hizo. Malaika wanaweza kuhakikisha kwamba wale wanaoona njaa na kiu kwa ajili ya kweli na uadilifu wanafikiwa.

Ikiwa ni mapenzi ya Bwana kwamba mahubiri zaidi ya moja kwa moja ya ujumbe wa Ufalme yafanywe katika maeneo fulani ambako serikali zimeyazuia hadi sasa, Mungu aweza kuleta hali zinazosababisha serikali hizo zibadili miongozo yazo. (Mit. 21:1) Na mahali ambapo milango ya fursa yaweza bado kufunguka, Mashahidi wa Yehova watajitoa wenyewe kwa furaha ili kuhakikisha kwamba watu katika nchi hizo wanapokea msaada mwingi kadiri iwezekanavyo ili wajifunze juu ya makusudi ya Yehova. Wanakusudia kuendelea kutumikia bila kuacha hadi Yehova kupitia Yesu Kristo aseme kazi imekamilika!

Katika 1992, Mashahidi wa Yehova walikuwa wenye shughuli wakihubiri katika nchi 229. Kufikia mwaka huo habari njema za Ufalme wa Mungu zilikuwa zimefika kwenye nchi 235 kwa njia mbalimbali. Kumi kati yazo zilifikiwa kwa mara ya kwanza baada ya 1975.

Ni ushahidi mwingi kadiri gani uliotolewa? Wakati wa miaka 30 ya kwanza baada ya Vita ya Ulimwengu 2, Mashahidi wa Yehova walitoa saa 4,635,265,939 kuhubiri na kufundisha kuhusu jina na Ufalme wa Yehova. Hata hivyo, kukiwa na Mashahidi wengi zaidi na sehemu kubwa yao wakiwa katika utumishi wa wakati wote, wakati wa miaka 15 iliyofuata (nusu tu ya ile miaka ya kwanza), saa 7,858,677,940 zilitolewa katika kutoa ushahidi peupe na nyumba hadi nyumba pamoja na kuongoza mafunzo ya Biblia nyumbani. Na bidii ya kazi iliendelea kuongezeka, waliporipoti saa nyingine 951,870,021 katika utendaji huo wakati wa 1990/91 na zaidi ya saa bilioni moja mwaka uliofuata.

Kiasi cha fasihi za Biblia kilichogawanywa na Mashahidi ili kutangaza Ufalme, kutia na lugha mbalimbali ambazo kwazo zimefanywa zipatikane, hakina kifani katika uwanja wowote wa jitihada ya mwanadamu. Rekodi hazijakamilika; lakini ripoti ambazo zingali zapatikana zaonyesha kwamba vitabu, vijitabu, broshua, na magazeti 10,107,565,269 pamoja na mabilioni ya trakti yasiyohesabiwa katika lugha 294, yalitiwa mikononi mwa watu waliopendezwa kati ya miaka 1920 na 1992.

Wakati wa kuandika habari hii, ushahidi wa duniani pote haujakamilika. Lakini kazi ambayo imekwisha timizwa na hali ambazo imetimizwa chini yazo zatoa uthibitisho wenye kusadikisha wa utendaji wa roho ya Mungu.

[Blabu katika ukurasa wa 502]

Mikusanyiko mikubwa na mwenendo wa Kikristo wa wajumbe ulivuta fikira

[Blabu katika ukurasa wa 505]

“Kuhusu utaratibu, hali ya amani, na usafi, washiriki wa mkusanyiko ni mifano ya kuigwa”

[Blabu katika ukurasa wa 507]

Mikusanyiko ya kihistoria ilifanywa katika mahali ambako Mashahidi walikuwa wamepigwa marufuku kwa miongo mingi

[Blabu katika ukurasa wa 508]

Maelfu ya tani za fasihi za Biblia zilisafirishwa hadi nchi za Ulaya Mashariki

[Blabu katika ukurasa wa 509]

Wazee waliostahili walijitolea kuhamia nchi ambazo kulikuwa na uhitaji wa pekee

[Blabu katika ukurasa wa 516]

Tamaa yao ni kuwafikia watu wengi mmoja-mmoja kadiri iwezekanavyo katika kila nyumba

[Blabu katika ukurasa wa 518]

Ukuzi wa kustaajabisha na uwezekano wa upanuzi zaidi

[Grafu/Picha katika ukurasa wa 513]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Ongezeko la Wapiga-Mbiu wa Ufalme Katika Nchi za Mashariki

India

10,000

5,000

1950 1960 1970 1980 1992

Jamhuri ya Korea

60,000

30,000

1950 1960 1970 1980 1992

Japani

150,000

100,000

50,000

1950 1960 1970 1980 1992

[Picha katika ukurasa wa 503]

Morumbi Stadium, katika São Paulo, Brazili (iliyoonyeshwa chini), na Maracanã Stadium, katika Rio de Janeiro, zilihitajiwa wakati uleule katika 1985 ili umati uweze kukutanika kwa ajili ya mikusanyiko ya Mashahidi wa Yehova

[Picha katika ukurasa wa 504]

Baadhi ya wanaotaka kubatizwa katika Chorzów, Poland, katika 1989

[Picha katika ukurasa wa 506]

Baadhi ya Mikusanyiko ya Kihistoria Katika 1991

Prague, Chekoslovakia

Tallinn, Estonia (kulia)

Zagreb, Kroatia (kulia)

Budapest, Hungaria (juu)

Baia-Mare, Rumania (kulia)

Usolye-Sibirskoye, Urusi (chini)

Alma-Ata, Kazakhstan (juu)

Kiev, Ukrainia (kushoto)

[Picha katika ukurasa wa 511]

Mkusanyiko wa kimataifa wa Mashahidi wa Yehova, katika St. Petersburg, Urusi, katika 1992

Roho changamfu ya kimataifa

Kutoka Urusi

Kutoka Moldova

Kutoka Ukrainia

Vijana wengi walikuwapo

M. G. Henschel (kushoto) azungumza juu ya programu na Stepan Kozhemba (katikati), kwa msaada wa mkalimani

Wajumbe wa nchi za nje walileta Biblia za Kirusi zitumiwe na Mashahidi kotekote Urusi

[Picha katika ukurasa wa 512]

Katika miaka ya 1980 Kanisa Katoliki lilitangaza vita juu ya Mashahidi, kulingana na madondoo haya ya habari ya Italia

[Picha katika ukurasa wa 514]

Meli zinapotia nanga Rotterdam, Uholanzi, Mashahidi huwa huko kuzungumza na wanaume hao kuhusu Ufalme wa Mungu

[Picha katika ukurasa wa 515]

Hata eneo linapoenezwa mara nyingi, kama hapa katika Guadeloupe, Mashahidi huendelea kujaribu kufikia mioyo ya majirani wao kwa habari njema

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki