Sura ya 17
Mikusanyiko Uthibitisho wa Udugu Wetu
MIKUSANYIKO imekuwa sehemu ya kawaida ya tengenezo la kisasa la Mashahidi wa Yehova. Lakini mikusanyiko ya kitaifa na kimataifa ya waabudu wa Yehova ilifanywa muda mrefu kabla ya karne ya 20.
Yehova aliamuru wanaume wote katika Israeli la kale wakusanyike Yerusalemu kwa ajili ya sikukuu tatu za kimajira kila mwaka. Baadhi ya wanaume walikuja na familia yao yote. Kwa kweli, Sheria ya Musa iliamuru kwamba kila mshiriki wa familia—wanaume, wanawake, na watoto—wawepo katika pindi fulani. (Kut. 23:14-17; Kum. 31:10-13; Luka 2:41-43) Mwanzoni, wahudhuriaji walikuwa watu walioishi ndani ya mipaka ya Israeli. Baadaye, Wayahudi walipotawanyika sana, wahudhuriaji wakaja kutoka mataifa mengi. (Mdo. 2:1, 5-11) Walisukumwa waje si kwa sababu tu Israeli na Abrahamu walikuwa babu zao bali kwa sababu walimtambua Yehova kuwa Baba yao mkuu wa kimbingu. (Isa. 63:16) Sikukuu hizo zilikuwa pindi za furaha. Pia zilisaidia wote waliokuwapo kuweka akili zao juu ya neno la Mungu na kutojihusisha sana na mambo ya kila siku ya maisha hivi kwamba wangesahau mambo ya kiroho yaliyo ya maana zaidi.
Vivyo hivyo, mikusanyiko ya Mashahidi wa Yehova katika nyakati za kisasa hutegemea masilahi ya kiroho. Kwa watazamaji wenye mioyo myeupe mikusanyiko hiyo hutoa uthibitisho usiokanushika kwamba Mashahidi wanaunganishwa na vifungo imara vya udugu wa Kikristo.
Mikusanyiko ya Mapema ya Wanafunzi wa Biblia
Mipango ya mikusanyiko ya Wanafunzi wa Biblia kutoka majiji na nchi mbalimbali ilisitawi hatua kwa hatua. Tofauti na vikundi vya makanisa ya kimapokeo, Wanafunzi wa Biblia, kwa njia ya mikusanyiko yao, walipata kujua upesi waamini wenzao katika sehemu nyinginezo. Mwanzoni, mikusanyiko hiyo ilifanywa Allegheny, Pennsylvania, kuhusiana na mwadhimisho wa kila mwaka wa kifo cha Bwana. Katika 1891 tangazo lilitolewa hususa kwamba kungekuwako na “mkusanyiko kwa ajili ya funzo la Biblia na kwa ajili ya kuadhimisha Ukumbusho wa Mlo wa Jioni wa Bwana.” Mwaka uliofuata Watch Tower lilikuwa na kichwa chenye kutokeza kikitangaza “MKUSANYIKO WA WAAMINI, ALLEGHENY, PA., . . . APRILI 7 HADI 14, KUTIA NDANI TAREHE HIZO MBILI, 1892.”
Umma kwa ujumla haukualikwa kwenye mikusanyiko hiyo ya mapema. Lakini, katika 1892, watu kama 400 waliokuwa wametoa uthibitisho wa imani katika fidia na kupendezwa kwa moyo mweupe na kazi ya Bwana walikuwapo. Programu ilitia ndani siku tano za funzo la Biblia lenye bidii na siku nyingine mbili za shauri lenye kusaidia kwa makolpota.
Mwanamume mmoja aliyekuwapo kwa mara ya kwanza kwenye mikusanyiko hiyo alisema hivi: “Nimekuwa kwenye Mikusanyiko mingi, lakini sijapata kamwe kabla ya hapo kuwa kwenye mmoja kama huu, ambapo mapenzi na mpango wa Mungu ndiyo mazungumzo pekee na yasiyokoma tokea kuamka hadi kwenda kulala; nyumbani, barabarani, kwenye mkutano, kwenye chakula cha mchana na kila mahali.” Kuhusu roho iliyoonyeshwa na wajumbe, mwanamume mmoja kutoka Wisconsin, Marekani, aliandika: “Nilivutiwa sana na roho ya upendo na fadhili za kidugu zilizodhihirishwa katika pindi zote.”
Badiliko katika mipango kwa ajili ya mkusanyiko wa kila mwaka lilitukia katika 1893. Ili kujifaidi na nauli zenye nafuu za garimoshi kuhusiana na Columbian Exposition kiangazi hicho Wanafunzi wa Biblia walikusanyika katika Chicago, Illinois, kuanzia Agosti 20 hadi 24. Huo ulikuwa ndio mkusanyiko wao wa kwanza nje ya eneo la Pittsburg. Hata hivyo, ili kutumia vizuri zaidi iwezekanavyo wakati na pesa kwa kazi ya Bwana, hakuna mikusanyiko zaidi mikuu iliyofanywa kwa miaka kadhaa.
Halafu, kuanzia 1898, Wanafunzi wa Biblia katika sehemu mbalimbali walianza kuchukua hatua ya kwanza katika sehemu zao kupanga makusanyiko, ambayo yangehudhuriwa na watu katika eneo dogo. Katika 1900 kulikuwa mikusanyiko 3 iliyopangwa na Sosaiti; lakini kulikuwa pia makusanyiko 13 ya mahali katika Marekani na Kanada, iliyo mingi yayo ilikuwa ya siku moja tu na mara nyingi ilifanywa kuhusiana na ziara ya mmoja wa mapilgrimu. Hesabu ilizidi kukua. Kufikia 1909 kulikuwa angalau makusanyiko 45 ya mahali katika Amerika Kaskazini kuongezea mikusanyiko iliyotumikiwa na Ndugu Russell katika safari za pekee zilizompeleka kwenye sehemu mbalimbali za bara hilo. Sehemu ya programu kwenye makusanyiko ya siku moja ilikusudiwa hasa kuchochea kupendezwa upande wa umma. Hudhurio lilikuwa la kuanzia labda mia moja kufika maelfu kadhaa.
Kwa upande mwingine, mikusanyiko mikuu, iliyohudhuriwa sanasana na Wanafunzi wa Biblia, ilikazia funzo kwa ajili ya wale walioimarika kwa kadiri fulani katika njia ya kweli. Kwa ajili ya mikusanyiko hiyo, magarimoshi ya pekee yakiwa yamejaa wajumbe yalikuwa yakija kutoka majiji makubwa. Pindi kwa pindi hudhurio lilikuwa juu kama 4,000, hata kutia wajumbe wachache kutoka Ulaya. Hizo zilikuwa nyakati za kiburudisho cha kweli cha kiroho kilichotokeza bidii na upendo ulioongezeka upande wa watu wa Yehova. Mwishoni mwa mkusanyiko mmoja katika 1903 kama huo ndugu mmoja alisema hivi: “Singepokea dola elfu kwa ajili ya wema ambao nimepokea kutoka Mkusanyiko huu;—ingawa mimi ni mtu maskini.”
Ndugu mapilgrimu ambao huenda wakawa katika eneo hilo walisema kwenye makusanyiko hayo. Ndugu Russell pia alijitahidi kuhudhuria na kutumikia katika programu kwenye makusanyiko ya mahali na kwenye mikusanyiko mikubwa zaidi katika Marekani na mara nyingi katika Kanada. Hilo lilihusisha kusafiri sana. Kwingi kati ya huko kulifanywa katika safari za mwisho wa juma. Lakini, katika 1909, ndugu mmoja katika Chicago alikodi mabehewa kadhaa ya garimoshi ili kusafirisha wajumbe waliosafiri pamoja na Ndugu Russell kutoka mkusanyiko mmoja hadi mwingine katika safari. Katika 1911 na 1913, magarimoshi mazima yalikodiwa na ndugu huyohuyo ili kupeleka mamia ya wajumbe katika safari za mkusanyiko zilizoendelea kwa mwezi mmoja au zaidi na kuenea magharibi mwa Marekani na Kanada.
Safari katika garimoshi la mkusanyiko kama hilo lilikuwa jambo la kukumbukwa. Katika 1913, Malinda Keefer alipanda moja katika Chicago, Illinois. Miaka mingi baadaye, alisema hivi: “Haikuchukua muda mrefu kujua kwamba tulikuwa familia moja kubwa . . . na garimoshi lilikuwa makao yetu kwa mwezi mmoja.” Garimoshi lilipokuwa likiondoka kituoni, wale waliokuja kuaga waliimba “Mungu Awe Nanyi Hadi Tuonanapo Tena,” muda wote huo wakipungapunga kofia na vitambaa vyao mpaka garimoshi lilipotoweka. Dada Keefer aliongeza: “Kwenye kila kituo safarini ilikuwako mikusanyiko iliyokuwa ikifanywa—mingi ilikuwa ya siku tatu, nasi tulikaa siku moja na kila mkusanyiko. Wakati wa vituo hivyo Ndugu Russell alitoa hotuba mbili, moja kwa akina ndugu alasiri, na nyingine kwa umma jioni juu ya kichwa ‘Baada ya Kifo.’”
Pia katika nchi nyingine makusanyiko yalikuwa yakiongezeka. Mara nyingi yalikuwa madogo sana. Kama 15 walikuwapo kwa ajili ya ule wa kwanza katika Norway, katika 1905; lakini ulikuwa mwanzo tu. Miaka sita baadaye, wakati Ndugu Russell alipotembelea Norway, jitihada ya pekee ilifanywa kualika umma, na hudhurio katika pindi hiyo lilikadiriwa kuwa 1,200. Wakati wa 1909, alipohudhuria mikusanyiko katika Scotland, alisema kwa watu karibu 2,000 katika Glasgow na wengine 2,500 katika Edinburgh juu ya habari yenye kuamsha kupendezwa “Mwivi Katika Paradiso, Tajiri Katika Helo, na Lazaro Kifuani mwa Abrahamu.”
Kwenye umalizio wa mikusanyiko ya mapema, ndugu walikuwa na kile walichokiita karamu ya upendo, kuonyesha hisia yao ya udugu wa Kikristo. Hiyo “karamu ya upendo” ilitia ndani nini? Kama kielelezo, wasemaji walikuwa wakipanga mstari wakiwa na sahani za mikate iliyokatwakatwa kuwa vipande vya umbo la dadu, kisha wasikilizaji walikuwa wakipita kwa mstari wakishiriki mkate, kusalimu kwa mkono, na kuimba “Na Vibarikiwe Vifungo Vifungavyo Mioyo Yetu Katika Upendo wa Kikristo.” Mara nyingi machozi ya shangwe yalikuwa yakitiririka mashavuni mwao walipokuwa wakiimba. Baadaye, kadiri hesabu zao zilivyokua, waliacha kusalimu kwa mkono na kushiriki mkate lakini walikuwa wakimalizia kwa wimbo na sala na, mara nyingi, kupiga makofi sana kuonyesha uthamini wao.
Kuanzisha Kampeni ya Duniani Pote ya Kupiga Mbiu ya Ufalme
Mkusanyiko mkubwa wa kwanza baada ya Vita ya Ulimwengu 1 ulifanywa Cedar Point, Ohio (kwenye Ziwa Erie, kilometa 96 magharibi mwa Cleveland), kutoka Septemba 1 hadi 8 katika 1919. Kufuatia kifo cha Ndugu Russell, baadhi ya wale waliokuwa wameshirikiana kimashuhuri na tengenezo waliacha kweli. Ndugu walipatwa na mitihani mikali. Mapema kidogo katika 1919, msimamizi wa Sosaiti na washirika wake walikuwa wamefunguliwa kutoka kifungo chao kisicho cha haki gerezani. Hivyo kulikuwa tarajio kubwa sana. Ijapokuwa hudhurio la siku ya kwanza lilikuwa chini, baadaye katika siku hiyo wajumbe zaidi waliwasili kwa magarimoshi ya pekee. Ndipo mameneja wa hoteli mbalimbali waliokuwa wamejitolea kuwapa wajumbe mahali pa kulala wakalemewa sana na kazi. R. J. Martin na A. H. Macmillan (wote wawili walikuwa miongoni mwa kile kikundi kilichofunguliwa toka gerezani karibuni) wakajitolea kusaidia. Walifanya kazi kuwagawia wajumbe vyumba mpaka kupita usiku wa manane, na Ndugu Rutherford na wengi kati ya wale wengine walifurahia kutumikia wakiwa wabeba-mizigo, wakibeba mizigo na kusindikiza akina ndugu kwenye vyumba vyao. Mlikuwamo roho yenye kuenea ya idili miongoni mwao wote.
Kama 2,500 walitazamiwa kuhudhuria. Hata hivyo, katika kila njia mkusanyiko ulithibitika kuwa zaidi ya ilivyotarajiwa. Kufikia siku ya pili, tayari jumba lilikuwa limejaa kupita kiasi na majumba zaidi yalitumiwa. Hilo lilipothibitika kuwa halitoshi, vipindi vilihamishwa kupelekwa nje katika eneo lililokuwa na bustani nzuri ya miti. Wanafunzi wa Biblia kama 6,000 kutoka Marekani na Kanada walikuwapo.
Kwa ajili ya hotuba kuu Jumapili, angalau 1,000 wa umma walikuja pia, hiyo iliongeza wasikilizaji kufikia 7,000 kamili, ambao msemaji alihutubia peupe bila msaada wowote wa maikrofoni au mfumo wa vikuza-sauti. Katika hotuba hiyo, “Tumaini kwa Ajili ya Wanadamu Wenye Kutaabika,” J. F. Rutherford alionyesha wazi kwamba Ufalme wa Kimesiya wa Mungu ndio utatuzi kwa matatizo ya wanadamu, na alionyesha pia kwamba Ushirika wa Mataifa (uliokuwa wakati huo ukizaliwa na ambao ulikuwa tayari umepewa kibali na makasisi) haukuwa hata kidogo wonyesho wa kisiasa wa Ufalme wa Mungu. Register gazeti la Sandusky lilikuwa na ripoti ndefu juu ya hotuba hiyo, pamoja na muhtasari wa utendaji wa Wanafunzi wa Biblia. Nakala za gazeti hilo zilipelekwa kwenye mashirika ya magazeti ya habari kotekote katika Marekani na Kanada. Lakini kulikuwako mengi zaidi yaliyomaanishwa na utangazaji uliotokana na mkusanyiko huo.
Upeo halisi wa mkusanyiko wote ulikuwa “Hotuba kwa Wafanyakazi Wenzi” ya Ndugu Rutherford, ambayo baadaye ilitangazwa chini ya kichwa “Kuutangaza Ufalme.” Ilielekezwa kwa Wanafunzi wa Biblia wenyewe. Wakati wa hotuba hiyo umaana wa herufi GA zilizokuwa zimeonekana katika programu ya mkusanyiko na katika mahali mbalimbali katika mahali pa mkusanyiko ulipata kuwa wazi. Tangazo lilitolewa kuhusu kuchapwa kwa gazeti jipya kulikokuwa kukikaribia, The Golden Age, ambalo lingetumiwa katika kuelekeza fikira za watu kwenye Ufalme wa Kimesiya. Baada ya kueleza kazi ipasayo kufanywa, Ndugu Rutherford aliambia wasikilizaji hivi: “Mlango wa fursa unafunguka mbele yenu. Uingieni upesi. Kumbukeni kwamba mwendapo mbele katika kazi hii hamsihi watu mkiwa mawakili wa gazeti tu, bali nyinyi ni mabalozi wa Mfalme wa wafalme na Bwana wa mabwana, mkitangazia watu kwa njia hiyo yenye kuheshimikia kuja kwa Enzi Bora Kabisa, ufalme wenye utukufu wa Bwana na Mkubwa wetu, ambao Wakristo wa kweli wameutumaini na kuuomba kwa karne nyingi.” (Ona Ufunuo 3:8.) Msemaji alipouliza ni wangapi waliotaka kushiriki katika kazi hiyo, itikio lenye idili lilikuwa lenye kuchochea kuliona. Wasikilizaji 6,000, wakasimama kwa umoja. Kufikia mwaka uliofuata, zaidi ya 10,000 walikuwa wakishiriki katika utumishi wa shambani. Mkusanyiko mzima ulikuwa na matokeo yenye kuleta umoja na kutia nguvu wahudhuriaji.
Miaka mitatu baadaye, katika 1922, mkusanyiko mwingine wenye kukumbukwa ulifanywa Cedar Point. Ilikuwa programu ya siku tisa, tokea Septemba 5 hadi 13. Kuongezea wajumbe kutoka Marekani na Kanada, wengine walikuja kutoka Ulaya. Mikutano iliongozwa katika lugha kumi. Wastani wa hudhurio kila siku ulikuwa kama 10,000; na kwa ajili ya hotuba “Mamilioni Wanaoishi Sasa Hawatakufa Kamwe,” wengi sana kati ya umma walikuwamo kati ya wasikilizaji hivi kwamba hudhurio lilikaribia kuwa mara mbili.
Wanafunzi wa Biblia hawakukusanyika kwenye mkusanyiko huo wakiwa na wazo la kwamba walikuwa wakipangia kazi hapa duniani ambayo ingeendelea kwa makumi ya miaka katika wakati ujao. Kwa kweli, walisema kwamba huenda ukawa ndio mkusanyiko wao mkuu wa mwisho kabla ya “kanisa kukombolewa . . . kuingizwa katika sehemu ya kimbingu ya ufalme wa Mungu, na kwa kweli katika kuwapo kwenyewe na kuliko halisi kwa Bwana wetu na Mungu wetu.” Lakini hata wakati uwe mfupi jinsi gani, kufanya mapenzi ya Mungu kulikuwa ndilo hangaiko lao la kwanza. Akifikiria hilo, katika Ijumaa, Septemba 8, Ndugu Rutherford alitoa hotuba yenye kukumbukwa “Ule Ufalme.”
Kabla ya hapo, beramu kubwa zenye herufi ADV zilikuwa zimeangikwa katika sehemu mbalimbali za uwanja. Wakati wa hotuba maana ya herufi hizo ikawa wazi msemaji alipohimiza hivi: “Iweni mashahidi waaminifu na wa kweli wa Bwana. Songeni mbele katika vita mpaka kila kisehemu cha Babiloni kiwe ukiwa. Utangazeni ujumbe kotekote. Lazima ulimwengu ujue kwamba Yehova ni Mungu na kwamba Yesu Kristo ni Mfalme wa wafalme na Bwana wa mabwana. Hii ndiyo siku ya siku zote. Tazameni, Mfalme atawala! Nyinyi ndio mawakili wa kumtangaza. Kwa hiyo mtangazeni, mtangazeni, mtangazeni, Mfalme na ufalme wake.” Wakati huo beramu kubwa, yenye urefu wa meta 11, ikakunjuka mbele ya wasikilizaji. Juu yake ilikuwapo ile shime yenye kuchochea “Mtangazeni [Kiingereza: ‘Advertise,’ ikiwakilishwa na ‘ADV’] Mfalme na Ufalme.” Ulikuwa muda wenye kutazamisha. Wasikilizaji walipiga makofi kwa idili. Ndugu Pfannebecker mwenye umri mkubwa, katika okestra ya kusanyiko, alipungapunga zeze lake juu ya kichwa chake na kusema kwa sauti kubwa kwa lahaja yake nzito ya Kijerumani: “Ach, Ya! Und now ve do it, no [Naam, na sasa tutaifanya, sivyo?]?” Nao waliifanya.
Siku nne baadaye, wakati mkusanyiko ulipokuwa ungali unaendelea, Ndugu Rutherford alishiriki binafsi pamoja na wakusanyikaji wengine walipokuwa wakishiriki kazi ya kupiga mbiu ya Ufalme nyumba hadi nyumba katika eneo ambalo halikuzidi umbali wa kilometa 72 kutoka uwanja wa mkusanyiko. Haikuishia hapo. Kazi ya kupiga mbiu ya Ufalme ilikuwa imepewa msukumo wenye nguvu ambao ungefika duniani pote. Mwaka huo zaidi ya wafanyakazi 17,000 wenye bidii katika nchi 58 walishiriki kutoa ushahidi. Miongo mingi ya miaka baadaye, George Gangas aliyekuwa kwenye mkusanyiko huo na ambaye baadaye akawa mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alisema hivi kuhusu programu katika Cedar Point: “Ni jambo lililokazwa kikiki katika akili na moyo wangu, ambalo sitasahau kamwe maadamu ninaishi.”
Hatua za Maana Katika Ukuzi wa Kiroho
Mikusanyiko yote imekuwa nyakati za burudisho na funzo katika Neno la Mungu. Lakini baadhi yayo imekumbukwa kwa miongo ya miaka kuwa ilikuwa hatua kubwa za kiroho.
Mikusanyiko saba kati ya hiyo, ilifanywa mwaka mmoja baada ya mwingine, kuanzia 1922 hadi 1928, katika Marekani, Kanada, na Uingereza. Sababu moja ya umaana wa mikusanyiko hiyo ilikuwa yale maazimio yenye nguvu yaliyokubaliwa, yote saba yanaorodheshwa katika kisanduku katika ukurasa ufuatao. Ijapokuwa Mashahidi walikuwa wachache, waligawanya nakala nyingi kufikia milioni 45 za azimio moja, na nyingine kadhaa milioni 50, katika lugha nyingi ulimwenguni pote. Baadhi yayo yalisambazwa katika redio za kimataifa zilizounganishwa. Hivyo ushahidi wenye kutokeza ukatolewa.
Mkusanyiko mwingine tena wenye kufanyiza historia ulifanywa Columbus, Ohio, katika 1931. Jumapili, Julai 26, baada ya Wanafunzi wa Biblia kusikia hoja za Kimaandiko walikubali jina jipya—Mashahidi wa Yehova. Lilifaa kama nini! Hapa palikuwa na jina ambalo huelekeza uangalifu wa kwanza kwa Muumba mwenyewe na ambalo hutambulisha daraka la wale wamwabuduo. (Isa. 43:10-12) Kukubaliwa kwa jina hilo kuliwatia akina ndugu bidii nyingi zaidi ya vile walivyopata kuwa wakati wowote wakiwa wapiga-mbiu wa jina na Ufalme wa Mungu. Kama vile barua moja iliyoandikwa mwaka huo na Shahidi Mdenmark ilivyolieleza jambo hilo: “Oh, ni jina tukufu kama nini, Mashahidi wa Yehova, naam, kwelikweli sisi sote na tuwe hivyo.”
Katika 1935 mkusanyiko mwingine wenye kukumbukwa ulifanywa, katika Washington D.C. Katika siku ya pili ya mkusanyiko huo, Ijumaa, Mei 31, Ndugu Rutherford alizungumza juu ya halaiki kubwa, au umati mkubwa, urejezewao kwenye Ufunuo 7:9-17. Kwa zaidi ya nusu karne, Wanafunzi wa Biblia walikuwa wamejaribu bila mafanikio kutambulisha kikundi hicho kwa usahihi. Sasa, wakati wa Yehova ulipowadia, kwa msaada wa matukio ambayo tayari yalikuwa yakitukia, ilielezwa kwamba hao ni watu walio na taraja la kuishi milele papa hapa duniani. Uelewevu huo uliipa kazi ya kueneza evanjeli umaana mpya na ukaeleza Kimaandiko badiliko lililokuwa likianza tu kutukia wakati huo katika muundo wa tengenezo la kisasa la Mashahidi wa Yehova.
Mkusanyiko katika St. Louis, Missouri, katika 1941, hukumbukwa na wengi waliokuwapo kwa ajili ya hotuba ya siku ya kufungua yenye kichwa “Uaminifu-Maadili,” ambayo Ndugu Rutherford alikazia fikira lile suala kuu linalokabili viumbe vyote vyenye akili. Tangu itolewe ile hotuba “Mtawala kwa Ajili ya Watu,” katika 1928, masuala yaliyozushwa na uasi wa Shetani yameelekezewa uangalifu mara nyingi. Lakini sasa ilionyeshwa kwamba “suala kuu lililozushwa na ushindani wenye ukaidi wa Shetani lilikuwa na lingali ni lile la UTAWALA WA ULIMWENGU WOTE MZIMA.” Kuthamini suala hilo na umaana wa kudumisha uaminifu-maadili kwa Yehova akiwa Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote Mzima kumekuwa msukumo wenye nguvu katika maisha za watumishi wa Yehova.
Katikati ya Vita ya Ulimwengu 2, katika 1942, wakati wengine walipokuwa wakitaka kujua kama kazi ya kuhubiri ilikuwa labda karibu kwisha, hotuba ya watu wote ya mkusanyiko iliyotolewa na N. H. Knorr, msimamizi mpya aliyewekwa wa Watch Tower Society, ilikuwa “Amani—Je, Inaweza Kudumu?” Ule ufafanuzi uliotolewa katika hotuba hiyo juu ya yule “hayawani-mwitu wa rangi-nyekundu-nyangavu” wa Ufunuo sura ya 17 uliwafungulia Mashahidi wa Yehova waone kipindi kilichofuata Vita ya Ulimwengu 2 ambacho katika hicho kungekuwako fursa ya kuelekeza watu zaidi kwenye Ufalme wa Mungu. Hilo lilitoa msukumo kwa kampeni ya duniani pote ambayo kwa muda wa miaka iliyopita imefika katika nchi zaidi ya 235 na haijakwisha.
Hatua nyingine ya maana ilifikiwa wakati wa mkusanyiko katika Yankee Stadium ya New York katika Agosti 2, 1950. Katika pindi hiyo wasikilizaji wenye kushangaa na wenye furaha sana walipokea kwa mara ya kwanza New World Translation of the Christian Greek Scriptures. Sehemu iliyobaki ya New World Translation ilitolewa kwa visehemu wakati wa mwongo wa miaka uliofuata. Tafsiri hiyo ya lugha ya kisasa ya Maandiko Matakatifu ilirudisha jina la kibinafsi la Mungu kwenye mahali palifaapo katika Neno lake. Uaminifu wayo kwa yale yaliyo katika lugha za awali za Biblia umeifanya kuwa kitu chenye thamani kubwa kwa Mashahidi wa Yehova katika funzo lao wenyewe la Maandiko na katika kazi yao ya kueneza evanjeli.
Katika siku iliyotangulia ile ya mwisho ya mkusanyiko huo, F. W. Franz, wakati huo akiwa makamu wa msimamizi wa Watch Tower Society, alihutubia wasikilizaji juu ya “Mfumo Mpya wa Mambo.” Kwa miaka mingi Mashahidi wa Yehova walikuwa wameamini kwamba hata kabla ya Har–Magedoni baadhi ya watumishi wa Yehova wa kabla ya Ukristo wangefufuliwa kutoka kwa wafu wawe wakuu wa ulimwengu mpya, kwa utimizo wa Zaburi 45:16. Basi, waweza kuwazia matokeo juu ya idadi kubwa ya wasikilizaji msemaji alipouliza: “Je, kusanyiko hili la kimataifa lingefurahi kujua kwamba hapa, usiku huu, katikati yetu, mna idadi fulani ya watarajiwao kuwa wakuu wa ile dunia mpya?” Kukawa na makofi mengi yenye kuendelea sana pamoja na vigelegele vya shangwe. Halafu msemaji akaonyesha kwamba matumizi ya Kibiblia ya neno litafsiriwalo “mkuu” pamoja na rekodi ya uaminifu wa wengi wa “kondoo wengine” katika nyakati za kisasa huruhusu kuwe na imani ya kwamba baadhi ya wale wanaoishi sasa huenda wakateuliwa na Yesu Kristo kwa ajili ya utumishi wa kuwa wakuu. Hata hivyo, alieleza pia kwamba, wale wakabidhiwao utumishi huo hawangepewa majina ya cheo. Akimalizia hotuba yake, alihimiza hivi: “Haya basi, tusonge mbele, tukiwa imara, sisi sote pamoja, tukiwa jamii ya Ulimwengu Mpya!”
Kumekuwa hotuba nyingine nyingi zenye maana sana zilizotolewa kwenye mikusanyiko ya Mashahidi wa Yehova: Katika 1953, “Sosaiti ya Ulimwengu Mpya Yashambuliwa Kutoka Kaskazini ya Mbali” ulikuwa ufafanuzi wenye kunasa fikira juu ya umaana wa shambulio lifanywalo na Gogu wa Magogu kama ielezwavyo katika Ezekieli sura ya 38 na 39. Mwaka huohuo, ile hotuba: “Kuijaza Nyumba Utukufu” ilisisimua wale walioisikia walipoona mbele ya macho yao uthibitisho dhahiri wa utimizo wa ahadi ya Yehova, kwenye Hagai 2:7, wa kuleta ndani ya nyumba ya Yehova, vitu vyenye thamani, vile vitu vyenye kutamanika, kutoka kwa mataifa yote.
Hata hivyo, mkusanyiko wenye kutokeza zaidi wa nyakati za kisasa ulifanywa New York katika 1958, wakati zaidi ya watu robo milioni walipojaa na kufurika vifaa vikubwa zaidi vilivyopatikana ili kusikia hotuba “Ufalme wa Mungu Watawala—Je, Mwisho wa Ulimwengu U Karibu?” Wajumbe walikuwapo kutoka nchi 123, nazo ripoti zao kwa wasikilizaji wa mkusanyiko zilisaidia kuimarisha vifungo vya udugu wa kimataifa. Ili kuchangia ukuzi wa kiroho wa wale waliokuwapo na kuvitumia kufundisha wengine, vichapo vilitolewa kwa lugha 54 wakati wa mkusanyiko huo wenye kutokeza.
Katika 1962, mfululizo wa hotuba juu ya kichwa “Kujitiisha Chini ya Mamlaka Zilizo Kubwa” ulisahihisha uelewevu waliokuwa nao Mashahidi kuhusu maana ya Warumi 13:1-7. (NW) Katika 1964, “Kupita Kutoka Kwenye Kifo Kuja Kwenye Uhai” na “Kutoka Makaburini Kuja Kwenye Ufufuo” ilipanua uthamini wao wa rehema kuu ya Yehova kama idhihirishwavyo katika uandalizi wa ufufuo. Na mambo makuu mengi zaidi kama hayo ya mikusanyiko yangeweza kutajwa.
Kila mwaka kuna makumi ya maelfu, naam, mamia ya maelfu, ya wapya wahudhuriao mikusanyiko. Ijapokuwa habari itolewayo si mpya siku zote kwa tengenezo kwa ujumla, mara nyingi huwafungulia wahudhuriaji wapya uelewevu wa mapenzi ya kimungu ambayo huwasisimua kwelikweli. Huenda wakaona na kusukumwa wachukue fursa ya utumishi ambao hubadili mwendo wao wote wa maisha.
Kwenye mikusanyiko mingi fikira zimekazwa juu ya maana ya vitabu fulani vya Biblia. Kwa kielelezo, katika 1958 na tena katika 1977, vitabu vilivyojalidiwa vilitolewa ambavyo vilizungumzia hasa unabii uliorekodiwa na nabii Danieli kuhusu kusudi la Mungu la kuwa na serikali moja ya ulimwengu Kristo akiwa Mfalme. Katika 1971, kitabu cha Ezekieli ndicho kilichoelekezewa fikira, pamoja na mkazo wacho juu ya julisho la kimungu, “Mataifa yatalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.” (Eze. 36:23, NW) Katika 1972, unabii mbalimbali uliorekodiwa na Zekaria na Hagai ulizungumzwa kirefu. Katika 1963, 1969, na 1988, yalikuwako mazungumzo mapana ya unabii wenye kusisimua wa Ufunuo, ambao hutabiri waziwazi kuanguka kwa Babiloni Mkubwa na kuja kwa mbingu mpya na dunia mpya za Mungu zenye utukufu.
Mikusanyiko imekazia vichwa mbalimbali—Ongezeko la Theokrasi, Ibada safi, Wafanyakazi Wenye Umoja, Wahudumu Wajasiri, Matunda ya Roho, Kufanya Wanafunzi, Habari Njema kwa Mataifa Yote, Jina la Kimungu, Enzi Kuu ya Kimungu, Utumishi Mtakatifu, Imani Ishindayo, Uaminifu-Mshikamanifu wa Ufalme, Washika Uaminifu-Maadili, Tumaini Katika Yehova, Ujitoaji Kimungu, Wachukuaji Nuru, na vingine vingi. Kila kimojawapo kilichangia ukuzi wa kiroho wa tengenezo na wale washirikianao nalo.
Kichocheo cha Kufanya Kazi ya Kueneza Evanjeli
Mikusanyiko mikubwa, pamoja na makusanyiko madogo zaidi imekuwa kitia-moyo kikubwa kuhusiana na kazi ya kuhubiri habari njema. Hotuba na maonyesho zimetoa mafunzo yenye kutumika. Mambo yenye kufurahisha yaliyoonwa katika huduma ya shambani pamoja na yale yaliyosimuliwa na watu waliosaidiwa karibuni kujifunza kweli ya Biblia huwa sikuzote katika programu. Kwa kuongezea, utumishi halisi wa shambani ulioratibiwa wakati wa mkusanyiko kwa miaka mingi ulikuwa wenye kunufaisha sana. Ulitoa ushahidi mzuri katika jiji la mkusanyiko na ulikuwa chanzo cha kitia-moyo kwa Mashahidi wenyewe.
Utumishi wa shambani ulipata kuwa sehemu ya utendaji ulioratibiwa wa mkusanyiko katika Winnipeg, Manitoba, Kanada, katika Januari 1922. Pia ulikuwa sehemu ya mkusanyiko mkuu uliofanywa katika Cedar Point, Ohio, baadaye mwaka huo. Baada ya hapo, likawa zoea la kawaida kutenga siku moja, au sehemu ya siku au sehemu za siku kadhaa, ili wajumbe washiriki pamoja katika utendaji wa kuhubiri humohumo katika jiji la mkusanyiko. Katika maeneo ya majiji makubwa, hilo liliwapa watu wanaopatikana mara chache fursa ya kusikia habari njema juu ya kusudi la Mungu la kuwapa uhai wa milele wapendao uadilifu.
Katika Denmark ya kwanza ya siku hizo za utumishi kwenye mkusanyiko ilipangwa katika 1925, wakati 400 hadi 500 walipokutana katika Nørrevold. Kwa wengi kati ya wale 275 walioshiriki katika utumishi wa shambani kwenye mkusanyiko huo, ulikuwa ndio wakati wao wa kwanza. Baadhi yao walikuwa na hofu. Lakini baada ya kuwa wameuonja, wakawa waeneza-evanjeli wenye idili katika maeneo ya kwao pia. Kufuatia mkusanyiko huo na mpaka mwisho wa Vita ya Ulimwengu 2, kulikuwa na makusanyiko mengi ya siku moja ya utumishi yaliyofanywa katika Denmark, na ndugu walialikwa kutoka majiji ya karibu. Bidii yenye kuongezeka ilionekana wazi waliposhiriki kwa umoja katika huduma na kisha wakakutana kusikia hotuba kadhaa. Makusanyiko ya utumishi kama hayo—lakini ya urefu wa siku mbili—yalifanywa katika Uingereza na Marekani.
Kwenye mikusanyiko mikubwa zaidi utendaji wa shambani ulikuwa wa kadiri kubwa. Kuanzia 1936, hotuba ya watu wote ya mkusanyiko ilitangazwa kwa gwaride zenye utaratibu za Mashahidi waliovaa mabango na kugawanya vikaratasi vya kukaribisha umma wahudhurie mkusanyiko. (Mwanzoni mabango hayo yaliitwa “ishara za pachipachi” kwa sababu yalivaliwa moja mbele na moja nyuma.) Nyakati nyingine, Mashahidi elfu moja au zaidi walishiriki katika gwaride hizo kwenye mkusanyiko wowote ule mmoja. Wengine walishiriki katika ziara za kawaida za nyumba hadi nyumba, wakiwaalika wote waje wasikie programu. Lilikuwa jambo lenye kutia moyo sana kwa Mashahidi mmoja-mmoja kufanya kazi na kuona mamia, hata maelfu, ya Mashahidi wengine wakishiriki katika huduma pamoja nao. Wakati uleule, umma waliokuwa katika umbali mkubwa toka mjini walikuja kujua kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa mjini; watu walikuwa na fursa ya kusikia wao wenyewe yale ambayo Mashahidi walifundisha na kutazama wao wenyewe mwenendo wao.
Mara nyingi hotuba zilizotolewa kwenye mikusanyiko zilisikiwa na wengi sana, zaidi ya wasikilizaji wenye kuonekana. Ndugu Rutherford alipotoa hotuba, “Uhuru kwa Ajili ya Vikundi vya Watu,” kwenye mkusanyiko katika Toronto, Kanada, katika 1927, ilipelekwa kwenye idadi kubwa ya wasikilizaji wa redio wa kimataifa kwa mfululizo wenye kufanyiza historia wa vituo 53 vya usambazaji. Mwaka uliofuata, kutoka Detroit, Michigan (Marekani), ile hotuba “Mtawala kwa Ajili ya Watu” ilisambazwa na vituo vingi mara mbili ya hivyo, na mawimbi mafupi ya redio yaliipeleka kwa wasikilizaji waliokuwa mbali sana kama vile Australia, New Zealand, na Afrika Kusini.
Katika 1931, mifumo mikubwa ya redio ilikataa kushirikiana na mipango ya kusambaza hotuba ya Ndugu Rutherford; hivyo Watch Tower Society, ikifanya kazi pamoja na American Telephone and Telegraph Company, ilifanyiza mfumo wayo wenyewe wa vituo 163, kutia ndani mfumo mkubwa zaidi wa nyuzi zilizounganishwa uliopata kusambazwa, ili kupeleka mbali ujumbe “Ufalme, Tumaini la Ulimwengu.” Kuongezea, zaidi ya vituo vingine 300 katika sehemu nyingi za ulimwengu vilisambaza programu hiyo kwa kutumia sahani za santuri.
Wakati wa mkusanyiko katika Washington, D.C., katika 1935, Ndugu Rutherford alisema juu ya habari “Serikali,” akivuta fikira kwa nguvu kwenye uhakika wa kwamba karibuni mahali pa serikali zote za kibinadamu patachukuliwa na Ufalme wa Yehova chini ya Kristo. Zaidi ya 20,000 katika Washington Auditorium waliisikia. Hotuba hiyo ilipelekwa pia kwa redio na kwa nyuzi za simu duniani pote, ikafika Amerika ya Kati na ya Kusini, Ulaya, Afrika Kusini, na visiwa vya Pasifiki, na nchi za Mashariki. Wale waliosikia hotuba hiyo kwa njia hiyo huenda ikawa ilifikia mamilioni. Magazeti mawili makubwa ya habari ya Washington yalivunja mikataba ya kusambaza hotuba hiyo. Lakini magari yenye vikuza-sauti yalipelekwa na akina ndugu kwenye vituo 3 katika jiji na mahali pengine 40 katika Washington, na kutoka kwayo hotuba ilisambazwa upya kwa idadi zaidi ya wasikilizaji waliokadiriwa kuwa 120,000.
Halafu, katika 1938, ile hotuba yenye kutoboa mambo “Yakabili Mambo ya Hakika” ilipelekwa kwenye majiji 50 ya mkusanyiko duniani pote, kutoka Royal Albert Hall, katika London, Uingereza, kukiwa na jumla ya hudhurio la 200,000 hivi. Kwa kuongezea, idadi kubwa ya wasikilizaji wa redio walisikiliza hotuba hiyo.
Hivyo, ijapokuwa Mashahidi wa Yehova walikuwa wachache, mikusanyiko yao ilitimiza fungu la maana katika kupiga mbiu ya ujumbe wa Ufalme hadharani.
Mikusanyiko ya Baada ya Vita Katika Ulaya
Kwa wale waliokuwapo, mikusanyiko fulani huwa yenye kutokeza kuliko mingine. Ndivyo ilivyokuwa kuhusu ile ya Ulaya mara tu baada ya Vita ya Ulimwengu 2.
Mkusanyiko mmoja kama huo ulifanywa Amsterdam, Uholanzi, Agosti 5, 1945, miezi iliyopungua minne baada ya Mashahidi kufunguliwa kutoka kambi za mateso za Ujerumani. Wajumbe kama 2,500 walitarajiwa; 2,000 wao wangehitaji mahali pa kulala. Ili kutimiza uhitaji huo wa mahali pa kulala Mashahidi wenyeji walitandaza nyasi juu ya sakafu ya nyumba zao. Wajumbe walikuja kutoka pande zote kwa kila njia iwezekanayo—kwa mashua, kwa malori, kwa baiskeli, na kwa kuomba usaidizi wa usafiri barabarani.
Kwenye mkusanyiko huo walicheka na kutoa machozi, waliimba na kumshukuru Yehova kwa wema wake. Kama vile mmoja aliyehudhuria alivyosema: “Yao ilikuwa shangwe isiyoneneka ya tengenezo la kitheokrasi lililofunguliwa sasa hivi kutoka minyororo!” Kabla ya vita, kulikuwako Mashahidi karibu 500 katika Uholanzi. Jumla ya 426 walikamatwa na kutiwa gerezani; kati ya hao, 117 walikufa likiwa tokeo la moja kwa moja la mnyanyaso. Ilikuwa shangwe kama nini wakati wengine walipowapata kwenye kusanyiko wapendwa wao waliokuwa wamefikiria walikufa! Wengine walitoa machozi walipokuwa wakitafuta sana bila mafanikio. Jioni hiyo 4,000 walisikiliza kwa hamu sana hotuba ya watu wote iliyoeleza kwa nini Mashahidi wa Yehova walikuwa wamekuwa shabaha ya mnyanyaso mkali sana hivyo. Yajapokuwa yale yaliyokuwa yamewapata, walikuwa wakijipanga kitengenezo wasonge mbele na kazi waliyopewa na Mungu.
Mwaka uliofuata, 1946, akina ndugu katika Ujerumani walipanga kuwe na mkusanyiko katika Nuremberg. Waliruhusiwa kutumia Zeppelinwiese, zilizokuwa hapo kwanza nyanja za kufanyia gwaride za Hitler. Katika siku ya pili ya mkusanyiko, Erich Frost, ambaye alikuwa amepatwa kibinafsi na unyama wa Gestapo na alikuwa ametumia miaka kadhaa katika kambi ya mateso ya Nazi, alitoa hotuba ya watu wote “Wakristo Watahiniwa Vikali.” Watu 3,000 kati ya umma wa Nuremberg walijiunga na wale Mashahidi 6,000 waliohudhuria kwa pindi hiyo.
Siku ya mwisho ya mkusanyiko ilithibitika kuwa wakati ambapo hukumu zingetangazwa kwenye majaribio ya uhalifu wa wakati wa vita huko katika Nuremberg. Wenye mamlaka wa kijeshi walitangaza kafyu kwa siku hiyo, lakini baada ya mazungumzo marefu walikubali kwamba kwa sababu ya msimamo ambao Mashahidi wa Yehova walichukua ujapokuwa upinzani wa Nazi, haingefaa kuwazuia wasimalizie mkusanyiko wao kwa amani. Hivyo, katika siku hiyo ya mwisho, ndugu walikusanyika wasikie ile hotuba yenye kuchochea hisia “Wasio na Hofu Ijapokuwa Njama ya Ulimwengu.”
Waliona mkono wa Yehova katika yale yaliyokuwa yakitukia. Wakati uleule ambao wanaume waliowakilisha utawala wa kimabavu uliokuwa umejaribu kuwaangamiza walipokuwa wakihukumiwa, Mashahidi wa Yehova walikuwa wakikutana kumwabudu Yehova mahali penyewe ambapo Hitler alikuwa ameonyesha nguvu zake za Kinazi zenye kutazamisha. Mwenyekiti wa mkusanyiko alisema: “Kuweza kuona tu siku hii, ambayo ni ono tu la kimbele la ushindi wa watu wa Mungu juu ya maadui wao kwenye vita ya Har–Magedoni, ilistahilisha miaka tisa ya kuwa katika kambi ya mateso.”
Mikusanyiko Mingine Yenye Kukumbukwa
Kadiri ambavyo utendaji wa Mashahidi wa Yehova umepanuka, mikusanyiko imefanywa duniani pote. Yote imekuwa na sehemu zenye kutokeza kwa wale waliokuwapo.
Katika Kitwe, Rhodesia Kaskazini (sasa Zambia), katika kitovu cha Kanda ya Shaba, mkusanyiko uliratibiwa ufanywe wakati wa ziara ya msimamizi wa Watch Tower Society katika 1952. Mahali palikuwa eneo kubwa katika viunga vya mojawapo kambi za kuchimba shaba, katika mahali pajulikanapo sasa kuwa Chamboli. Sehemu ya juu ya kichuguu ilisawazishwa, na paa ikajengwa juu yayo itumike kuwa jukwaa. Vibanda vingine vilijengwa kwa ajili ya mahali pa kulala, pamoja na vitanda, kimoja juu ya kingine, zikitokeza meta 180 kutoka eneo kuu la kuketi kama njukuti (spoku) katika gurudumu la baiskeli. Wanaume na wavulana walilala katika baadhi yavyo; na wanawake na wasichana katika vile vingine. Baadhi ya wajumbe walikuwa wamesafiri kwa baiskeli kwa majuma mawili ili wawepo. Wengine walikuwa wametembea kwa siku kadhaa na kisha wakamaliza safari kwa kupanda basi la kikale.
Wakati wa vipindi wale waliokuwa miongoni mwa wasikilizaji walisikiliza kwa hamu sana, ingawa waliketia mabenchi magumu ya mianzi katika mahali palipo wazi. Walikuwa wamekuja kusikia, nao hawakutaka kukosa neno hata moja. Uimbaji wa idadi hiyo ya wasikilizaji 20,000 na kutoa machozi machoni—ulikuwa mzuri sana. Hakukuwa na ufuatishaji wa vyombo vya muziki, lakini upatano wa sauti ulikuwa mzuri sana. Si katika kuimba kwao tu bali katika kila njia, umoja ulidhihirika miongoni mwa Mashahidi hawa, ingawa walitoka katika malezi ya namna nyingi na makabila mengi.
Na je, unaweza kuwazia hisia za Mashahidi wa Yehova wa Ureno wakati baada ya kupigania uhuru wa ibada kwa karibu miaka 50, Mashahidi walipata kutambuliwa kisheria katika Desemba 18, 1974. Wakati huo walikuwa na idadi kama 14,000 tu. Katika muda wa siku chache, 7,586 wao walijaa jengo la michezo katika Porto. Siku iliyofuata, 39,284 walijaa na kuzidi stediamu ya mpira wa miguu katika Lisbon. Ndugu Knorr na Ndugu Franz walikuwa pamoja nao kwa ajili ya pindi hiyo ya furaha, ambayo wengi hawatasahau kamwe.
Kupanga Kitengenezo Mikusanyiko ya Kimataifa
Kwa zaidi ya nusu karne, Mashahidi wa Yehova wamefanya mikusanyiko mikubwa, mikusanyiko iliyofanywa sawia katika majiji mengi katika nchi nyingi. Hisi yao ya udugu wa kimataifa imeongezeka katika pindi hizo walipokuwa wameweza wote kusikia hotuba kuu zikitoka jiji moja kuu.
Hata hivyo, haikuwa mpaka 1946, wakati mkusanyiko mkubwa wa kimataifa ulipoleta pamoja katika jiji moja wajumbe kutoka sehemu nyingi za dunia. Hiyo ilikuwa katika Cleveland, Ohio. Ijapokuwa bado ilikuwa vigumu kusafiri baada ya vita, hudhurio lilifika 80,000, kutia wajumbe 302 kutoka nchi 32 nje ya Marekani. Vipindi viliongozwa kwa lugha 20. Mafunzo mengi mazuri yenye kutumika yalitolewa kwa lengo la kupanua kazi ya kueneza evanjeli. Mojawapo mambo makuu ya mkusanyiko lilikuwa hotuba ya Ndugu Knorr juu ya matatizo ya kujenga upya na kupanua. Wasikilizaji walipiga makofi kwa idili waliposikia mipango ya kuongeza vifaa vya uchapaji na vya ofisi vya makao makuu ya Sosaiti, pamoja na vifaa vyao vya usambazaji wa redio na kuanzisha ofisi za tawi katika nchi kubwakubwa za ulimwengu, kupanua vifaa vyayo vya usambazaji wa redio, kuongezea kazi ya mishonari. Mara baada ya mkusanyiko huo, mambo mengi yalitayarishwa ili Ndugu Knorr na Ndugu Henschel waweze kufunga safari ya ulimwenguni pote kutekeleza yaliyokuwa yamezungumzwa.
Katika miaka iliyofuata, mikusanyiko yenye kufanyiza historia kwelikweli ilifanywa katika Yankee Stadium ya New York City. Kwenye ule wa kwanza wayo, kuanzia Julai 30 hadi Agosti 6, 1950, wajumbe walikuwapo kutoka nchi 67. Programu ilitia ndani ripoti fupi zilizotolewa na watumishi wa matawi, wamishonari, na wajumbe wengine. Hao waliupa mkusanyiko mambo yenye kusisimua kuonyesha ile kazi ya bidii ya kueneza evanjeli iliyokuwa ikifanywa katika nchi zote walikokuwa wametoka. Siku ya mwisho, hudhurio lilipanda kufika 123,707 kwa ajili ya hotuba “Je, Unaweza Kuishi Milele kwa Furaha Duniani?” Kichwa cha mkusanyiko kilikuwa “Ongezeko la Theokrasi.” Uangalifu ulielekezwa kwenye ongezeko kubwa la idadi. Hata hivyo, kama vile mwenyekiti, Grant Suiter, alivyoonyesha kwa mkazo, hilo halikufanywa ili kusifu watu wenye akili sana katika tengenezo lionekanalo. Bali, alijulisha: “Yehova ndiye wa kusifiwa kwa ajili ya idadi hiyo kubwa. Yapaswa kuwa hivyo, nasi hatungetaka iwe vingine.”
Katika 1953, mkusanyiko mwingine ulifanywa Yankee Stadium katika New York. Wakati huo hudhurio lilikuwa na kilele cha 165,829. Kama ilivyokuwa kwa mkusanyiko wa kwanza hapo, programu ilijaa mazungumzo ya unabii mbalimbali wa Biblia wenye kusisimua, shauri lenye kutumika juu ya jinsi ya kufanya kazi ya kuhubiri habari njema, na ripoti kutoka nchi nyingi. Ijapokuwa vipindi vilianza kama saa 3:30 asubuhi, kwa kawaida havikumalizika mpaka 3:00 au 3:30 usiku. Mkusanyiko huo uliandaa siku nane kamili za karamu ya kiroho yenye shangwe.
Kwa ajili ya mkusanyiko wao mkubwa kupita yote, katika New York katika 1958, ilikuwa lazima kutumia Yankee Stadium na pia Polo Grounds ulio karibu pamoja na maeneo ya ziada nje ya stediamu ili umati wa ziada wa mkusanyiko upate mahali pa kukaa. Siku ya mwisho, wakati kila kiti kilipokuwa kimekaliwa, ruhusa ya pekee ilitolewa kutumia hata sehemu ya ndani ya uwanja wa michezo wa Yankee Stadium, na ilisisimua kama nini kuona maelfu yakimiminika, yakatoa viatu, na kuketi kwenye nyasi! Idadi ilionyesha kuwa 253,922 walihudhuria kusikia hotuba ya watu wote. Uthibitisho zaidi wa baraka ya Yehova juu ya huduma ya watumishi wake ulionwa wakati 7,136 kwenye mkusanyiko huo walipoonyesha wakfu wao kwa uzamisho wa maji—zaidi ya mara mbili ya idadi ya waliobatizwa katika ile pindi yenye kufanyiza historia ya Pentekoste 33 W.K., kama ilivyoripotiwa katika Biblia!—Mdo. 2:41.
Uendeshaji wote wa mikusanyiko hiyo ulitoa uthibitisho wa jambo lililo zaidi ya tengenezo lenye ufanisi. Ulikuwa udhihirisho wa roho ya Mungu ikifanya kazi miongoni mwa watu wake. Upendo wa kidugu ambao msingi wao ni kumpenda Mungu ulionekana wazi kila mahali. Hakukuwa na wapangaji mambo wenye kulipwa mshahara. Kila idara iliendeshwa na wenye kujitolea wasiolipwa. Ndugu na dada Wakristo, mara nyingi vikundi vya familia, walishughulikia viburudisho. Pia walitayarisha milo yenye moto, na katika mahema makubwa nje ya stediamu, walipakulia wajumbe milo kwa mwendo wa kufikia elfu moja kwa dakika moja. Makumi ya maelfu—wote wakiwa na furaha ya kushiriki kazi—walitumikia wakiwa wakaribishaji na wakashughulikia ujenzi wote uliohitajiwa, upishi na upakuaji wa milo, usafi, na mengi zaidi.
Wenye kujitolea wengine wengi walitumia mamia ya maelfu ya saa ili kutimiza mahitaji ya mahali pa kulala ya wajumbe. Katika miaka fulani, ili kutimiza mahitaji ya angalau baadhi ya wakusanyikaji, majiji yalipangwa kwa kutumia mahema na trela. Katika 1953 Mashahidi walimvunia mkulima mmoja katika New Jersey hekta 16 za nafaka bila malipo, ambaye aliwakodisha shamba lake kwa ajili ya jiji lao la trela. Vyoo, umeme, mabafu, madobi, kafeteria, na maduka, yalijengwa ili kutimiza mahitaji ya idadi iliyozidi 45,000. Walipoingia mahali hapo, jiji lilijengwa kwa usiku mmoja. Maelfu mengi zaidi walipata mahali pa kulala katika mahoteli na nyumba za watu binafsi katika New York. Ilikuwa kazi kubwa mno. Kwa baraka za Yehova, ilitimizwa kwa mafanikio.
Mikusanyiko Katika Mwendo
Washiriki wa udugu huu wa kimataifa wanapendezwa sana na Mashahidi wenzao katika nchi nyinginezo. Likiwa tokeo, wametumia fursa ili kuhudhuria mikusanyiko nje ya nchi za nyumbani kwao.
Wakati kusanyiko la kwanza kati ya ule mfululizo wa Ibada Safi Kusanyiko lilipofanywa katika Wembley Stadium katika London, Uingereza, katika 1951, Mashahidi kutoka nchi 40 walikuwapo. Programu ilikazia upande wenye kufaa wa ibada ya kweli na kufaa kwa mtu kufanya huduma kuwa kazi yake ya maisha. Kutoka Uingereza, Mashahidi wengi walisafiri kwenda Bara Ulaya, ambapo mikusanyiko mingine tisa ilifanywa wakati wa miezi miwili iliyofuata. Mkubwa kupita yote kati yayo ulikuwa katika Frankfurt am Main, Ujerumani, ambapo 47,432 walikuwapo kutoka nchi 24. Uchangamfu wa akina ndugu ulionyeshwa mwishoni mwa programu wakati okestra ilipoanza kupiga muziki nao ndugu Wajerumani wakaanza ghafula kuimba kutoka moyoni wimbo wa kuaga wakiwakabidhi kwa Mungu Mashahidi wenzao waliokuwa wamekuja kutoka ng’ambo kujiunga nao. Vitambaa vya mkononi vilipungwapungwa, na mamia wakamiminika uwanjani kuonyesha uthamini wao binafsi kwa ajili ya karamu hiyo nzuri ya kitheokrasi.
Katika 1955, Mashahidi zaidi walipanga kutembelea ndugu zao Wakristo katika ng’ambo wakati wa mkusanyiko. Kwa njia ya meli mbili zilizokodiwa (kila moja ikiwa na abiria 700) na ndege 42 zilizokodiwa, wajumbe kutoka Marekani na Kanada walienda Ulaya. Chapo la Ulaya la gazeti The Stars and Stripes, lililosambazwa katika Ujerumani, lilieleza mmiminiko wa Mashahidi kuwa ‘labda ndio Waamerika wengi zaidi waliopata kwenda Ulaya tangu uvamizi wa Mataifa Marafiki wakati wa Vita ya Ulimwengu 2.’ Wajumbe wengine walikuja kutoka Amerika ya Kati na ya Kusini, Asia, Afrika, na Australia. Zijapokuwa jitihada za makasisi wa Jumuiya ya Wakristo za kuzuia Mashahidi wasifanye mikusanyiko yao katika Roma na Nuremberg, hiyo miwili na mingine sita ilifanywa katika Ulaya wakati wa kiangazi. Hudhurio lilikuwa kuanzia 4,351 katika Roma kufika 107,423 katika Nuremberg. Kikundi kingine cha 17,729 kilikusanyika Waldbühner katika ile iliyokuwa wakati huo Berlin Magharibi, ambapo ndugu kutoka eneo la Mashariki la enzi hiyo wangeweza kufika bila hatari kubwa. Wengi kati yao walikuwa wamekuwa katika gereza kwa ajili ya imani yao au walikuwa na washiriki wa familia waliokuwa gerezani wakati huo, lakini walikuwa wangali thabiti katika imani. Kichwa cha mkusanyiko kilifaa kama nini—“Ufalme Wenye Kushinda”!
Ingawa tayari kulikuwa kumekuwa mikusanyiko mingi ya kimataifa, lililotukia katika 1963 lilikuwa la kwanza la aina yake. Ulikuwa mkusanyiko wa ulimwenguni pote. Ukianzia Milwaukee, Wisconsin, katika Marekani, ulisonga mbele kwenda New York; kisha, kwenye majiji makubwa manne katika Ulaya; kupitia Mashariki ya Kati; kusonga mbele hadi India, Burma (sasa Myanmar), Thailand, Hong Kong, Singapore, Filipino, Indonesia, Australia, Taiwan, Japani, New Zealand, Fiji, Jamhuri ya Korea, na Hawaii; na kisha kurudi kwenye bara la Amerika Kaskazini. Kwa ujumla, wajumbe kutoka nchi 161 walikuwapo. Jumla ya hudhurio ilizidi 580,000. Walikuwapo 583, kutoka nchi kama 20, walioandamana na mkusanyiko, wakihudhuria katika nchi moja baada ya nyingine, duniani pote. Safari za utalii za pekee ziliwawezesha kuona sehemu za kidini zenye kupendeza, na pia walishiriki pamoja na ndugu na dada wenyeji katika huduma ya nyumba hadi nyumba. Wasafiri hao walijilipia gharama zao wenyewe.
Wajumbe wa Amerika ya Latin walikuwa wamewakilishwa vizuri kwenye mingi ya mikusanyiko hiyo ya kimataifa. Lakini katika 1966-1967, ilikuwa zamu yao ya kuwa wakaribishaji wa mikusanyiko. Wale waliohudhuria hawatasahau kamwe ile drama iliyolifanya kuwa na uhai lile simulizi la Biblia kuhusu Yeremia na ambayo ilisaidia kila mtu kuthamini maana yalo kwa siku yetu.a Vifungo vya upendo wa Kikristo viliimarishwa wageni walipokuwa wakijionea wenyewe hali ambazo katika kampeni kubwa ya elimu ya Biblia ilikuwa ikitimizwa katika Amerika ya Latin. Walivutwa sana na imani yenye nguvu ya waamini wenzao, wengi wao walikuwa wameshinda vizuizi vilivyoelekea kutoshindika—upinzani wa familia, mafuriko, kupoteza mali—ili wahudhurie. Walitiwa moyo sana na mambo yaliyoonwa kama lile la dada painia wa pekee kutoka Uruguai dhaifu aliyehojiwa na ambaye alikuwa jukwaani na wengi kati ya watu 80 ambao tayari alikuwa amesaidia kufanya maendeleo kufikia hatua ya ubatizo wa Kikristo! (Kufikia 1992, dada huyo alikuwa amesaidia watu 105 kufikia hatua ya ubatizo. Yeye alikuwa angali dhaifu na angali ni painia wa pekee!) Pia ilichangamsha moyo kama nini kukutana na wamishonari kutoka yale madarasa ya mapema zaidi ya Gileadi wakiwa wangali wanafanya kazi katika migawo yao! Mikusanyiko hiyo ilikuwa kichocheo kizuri kwa kazi iliyokuwa ikifanywa katika sehemu hiyo ya ulimwengu. Katika nyingi za nchi hizo, sasa kuna wasifaji wa Yehova wengi kama mara 10, 15, au hata 20 kama wale waliokuwako wakati ule.
Miaka michache baadaye, katika 1970-1971, iliwezekana kwa Mashahidi kutoka ng’ambo kuwa na ushirika pamoja na ndugu zao kwenye mikusanyiko ya kimataifa iliyofanywa barani Afrika. Mkubwa kupita yote kati ya mikusanyiko hiyo ya Kiafrika ulikuwa Lagos, Nigeria, ambapo ilikuwa lazima kujenga vifaa vyote kuanzia chini kwenda juu. Ili kukinga wajumbe na jua kali, jiji la mianzi lilijengwa—maeneo ya kuketi, mabweni, kafeteria, na idara nyinginezo. Ilitaka nguzo za mianzi 100,000 na mikeka mikubwa 36,000, iliyofumwa kwa matete—yote ikiwa imetayarishwa na ndugu na dada. Programu ilitolewa katika lugha 17 wakati uleule mmoja. Hudhurio lilifika 121,128, na Mashahidi wapya 3,775 wakabatizwa. Vikundi vingi vya Kikabila viliwakilishwa, na wengi wa wale waliokuwapo walikuwa watu waliozoea kupigana. Lakini sasa, ilikuwa shangwe kama nini kuwaona wakiwa wameungana katika vifungo vya udugu halisi wa Kikristo!
Baada ya mkusanyiko, baadhi ya wajumbe wa nchi za kigeni walisafiri kwa basi kwenda nchi ya Waigbo kuona lile eneo lililoathiriwa vibaya sana na vita ya hivi karibuni ya wenyewe kwa wenyewe. Udadisi mwingi ulitokezwa katika mji baada ya mji wageni walipokuwa wakisalimiwa na kukumbatiwa na Mashahidi wenyeji. Watu walikimbia barabarani kutazama. Wonyesho huo wa upendo na umoja kati ya weusi na weupe ulikuwa jambo ambalo hawakuwa wamepata kuona kamwe.
Katika nchi fulani idadi ya Mashahidi wa Yehova hufanya isiwezekane kwao wote kukusanyika pamoja katika mahali pamoja. Hata hivyo, pindi kwa pindi, mikusanyiko kadhaa imefanywa kwa wakati mmoja, mingine zaidi ikifuata, juma baada ya juma. Katika 1969, umoja uliohisiwa kwenye mikusanyiko iliyopangwa kwa njia hiyo ulizidishwa na uhakika wa kwamba baadhi ya wasemaji wakuu walisafiri kwa ndege kwenda na kurudi kati ya mikusanyiko hiyo, hivyo kuitumikia yote. Katika 1983 na 1988, umoja kama huo ulihisiwa wakati idadi fulani ya mikusanyiko mikubwa yenye kutumia lugha moja ilipounganishwa pamoja, hata kimataifa, kwa kupisha kwa njia ya simu hotuba kuu zilizotolewa na washiriki wa Baraza Linaloongoza. Hata hivyo, msingi halisi wa umoja miongoni mwa Mashahidi wa Yehova ni uhakika wa kwamba wote humwabudu Yehova akiwa ndiye Mungu wa pekee wa kweli, wote hushikamana na Biblia ikiwa mwongozo wao, wote hunufaika kutokana na programu ileile moja ya ulishaji wa kiroho, wote humtegemea Yesu Kristo akiwa Kiongozi wao, wote hutafuta kudhihirisha matunda ya roho ya Mungu katika maisha zao, wote huweka tumaini lao katika Ufalme wa Mungu, na wote hushiriki katika kupelekea wengine habari njema za Ufalme huo.
Wamefanywa Tengenezo ili Wamsifu Yehova Kimataifa
Mashahidi wa Yehova wameongezeka idadi kiasi cha kuzidi idadi ya watu wa mataifa mengi moja moja. Ili mikusanyiko yao itimize mengi zaidi yaliyo mema, mipango mingi ya uangalifu hutakwa. Hata hivyo, maombi sahili yaliyochapwa kuhusu mahali ambapo Mashahidi kutoka maeneo mbalimbali wapaswa kuhudhuria kwa kawaida ndiyo tu huhitajiwa ili kuhakikisha kwamba kutakuwa nafasi ya kutosha kwa kila mtu. Mikusanyiko ya kimataifa inapopangwa, mara nyingi sasa Baraza Linaloongoza linahitaji kufikiria idadi ya Mashahidi kutoka nchi nyingine ambao wangependa kwenda na walio katika hali ya kuweza kufanya hivyo na pia ukubwa wa vifaa vipatikanavyo vya mkusanyiko, idadi ya Mashahidi wenyeji ambao watahudhuria, na kiasi cha mahali pa kulala panapopatikana kwa ajili ya wajumbe; kisha tarakimu isiyopasa kuzidi yaweza kugawiwa kila nchi. Ndivyo ilivyokuwa kuhusu ile Mikusanyiko mitatu ya “Ujitoaji Kimungu” iliyofanywa Poland katika 1989.
Kwa ajili ya mikusanyiko hiyo Mashahidi wa Yehova kama 90,000 walitazamiwa kutoka Poland kuongezea maelfu ya watu wapya wenye kupendezwa. Pia wengi walialikwa wahudhurie kutoka Uingereza, Kanada, na Marekani. Vikundi vikubwa vya wajumbe vilikaribishwa kutoka Italia, Ufaransa, na Japani. Vingine vilikuja kutoka nchi za Skandinevia na Ugiriki. Angalau nchi 37 ziliwakilishwa. Kwa ajili ya sehemu fulani za programu, ilikuwa lazima kutafsiri Kipoland au Kiingereza katika lugha nyingine nyingi kama 16. Jumla ya hudhurio ilikuwa 166,518.
Vikundi vikubwa vya Mashahidi kwenye mikusanyiko hiyo vilikuwa vimekuja kutoka ule uliokuwa wakati huo Muungano wa Sovieti na kutoka Chekoslovakia; vikundi vikubwa vilikuwapo pia kutoka nchi nyingine za Ulaya Mashariki. Hoteli na mabweni ya shule hayangeweza kuwaandalia wote mahali pa kulala. Kwa ukaribishaji-wageni, Mashahidi Wapoland walifungua mioyo na makao yao, wakishiriki kwa furaha walivyokuwa navyo. Kutaniko moja la wahubiri 146 liliandalia wajumbe zaidi ya 1,200 mahali pa kulala. Kwa baadhi ya wale waliohudhuria mikusanyiko hiyo, ilikuwa mara ya kwanza ambayo walipata wakati wowote kuwa kwenye mkusanyiko mkubwa wa watu wa Yehova zaidi ya 15 au 20. Mioyo yao ilijaa uthamini walipokuwa wakitazama makumi ya maelfu katika stediamu hizo, wakijiunga katika sala, na kuunganisha sauti zao katika nyimbo za sifa kwa Yehova. Walipochangamana pamoja kati ya vipindi, kulikuwako kukumbatiana kwa uchangamfu, hata ingawa tofauti za lugha mara nyingi ziliwazuia kusema kwa maneno yale yaliyokuwa mioyoni mwao.
Mkusanyiko ulipokuwa ukifikia mwisho, mioyo yao ilijaa shukrani kwa Yehova, aliyeyawezesha yote. Katika Warsaw, baada ya maelezo ya kuaga ya mwenyekiti, wasikilizaji walipiga makofi ghafula ambayo yaliendelea bila kupungua kwa angalau dakika kumi. Baada ya wimbo na sala ya mwisho, makofi yakarudiwa, nao wasikilizaji walikawiakawia vitini kwa muda mrefu. Walikuwa wamengojea pindi hiyo kwa miaka mingi, nao hawakutaka iishe.
Mwaka uliofuata, 1990, muda ulio punde kuliko miezi mitano baada ya kuondolewa marufuku ya miaka 40 juu ya Mashahidi wa Yehova katika ile iliyokuwa wakati ule Ujerumani Mashariki, mkusanyiko mwingine wa kimataifa wenye kusisimua ulifanywa, huo katika Berlin. Miongoni mwa wale 44,532 waliokuwapo mlikuwamo wajumbe kutoka nchi 65 tofauti. Kutoka nchi fulani, ni wachache tu waliokuwa wamekuja; kutoka Poland, kama 4,500 walikuja. Maneno hayangeweza kueleza zile hisia zenye kina za wale ambao hawakuwa wamepata kamwe uhuru wa kuhudhuria mkusanyiko kama huo, na wakati wasikilizaji wote walipojiunga katika nyimbo za sifa kwa Yehova, hawangeweza kuzuia machozi ya shangwe.
Baadaye mwaka huo, mkusanyiko kama huo ulipofanywa katika São Paulo, Brazili, stediamu mbili kubwa zilihitajiwa kukaliwa na wasikilizaji wa kimataifa 134,406. Hiyo ilifuatwa na mkusanyiko katika Argentina, ambako kwa mara nyingine tena stediamu mbili zilitumiwa sawia kuandaa mahali pa kuketi kwa ajili ya wasikilizaji wa Kimataifa. Mwaka 1991 ulipokuwa ukianza, mikusanyiko zaidi ya kimataifa ilikuwa ikianza katika Filipino, Taiwan, na Thailand. Idadi kubwa za wasikilizaji kutoka mataifa mengi zilikuwapo pia mwaka huo kwa ajili ya mikusanyiko katika Ulaya Mashariki—katika Hungaria, Chekoslovakia, na ile ambayo sasa ni Kroatia. Na katika 1992, wajumbe kutoka nchi 28 waliliona kuwa pendeleo la pekee kuwa miongoni mwa wale 46,214 waliokuwa katika St. Petersburg kwa ajili ya mkusanyiko wa kwanza ulio wa kimataifa kwelikweli wa Mashahidi wa Yehova katika Urusi.
Fursa za Burudisho la Kiroho la Ukawaida
Si mikusanyiko yote ifanywayo na Mashahidi wa Yehova huwa mikusanyiko ya kimataifa. Hata hivyo, Baraza Linaloongoza hupangia mikusanyiko mikubwa mara moja kwa mwaka, na programu ileile moja hufurahiwa ulimwenguni pote katika lugha nyingi. Mikusanyiko hiyo yaweza kuwa mikubwa sana, ikiandaa fursa ya ushirika pamoja na Mashahidi wengine kutoka sehemu nyingi, au yaweza kuwa midogo zaidi ikifanywa katika majiji mengi, ikifanya iwe rahisi kwa wapya kuhudhuria na kuwezesha umma katika mamia ya majiji madogo zaidi kujionea karibukaribu kikundi kikubwa chenye kuwakilisha Mashahidi wa Yehova.
Kwa kuongezea, mara moja kwa mwaka kila mzunguko (labda wenye makutaniko 20) hukusanyika kwa ajili ya programu ya siku mbili ya shauri na kitia-moyo cha kiroho.b Pia, tangu Septemba 1987, siku ya kusanyiko la pekee, programu ya siku moja yenye kujenga, hupangiwa kila mzunguko mara moja kwa mwaka. Inapowezekana, mshiriki wa wafanyakazi wa makao makuu ya Sosaiti au mtu fulani kutoka katika ofisi ya tawi ya mahali hutumwa akashiriki katika programu hiyo. Programu hizo huthaminiwa sana na Mashahidi wa Yehova. Katika maeneo mengi mahali pa kusanyiko hapako mbali wala si vigumu kupafika. Lakini haiwi hivyo sikuzote. Mwangalizi mmoja asafiriye hukumbuka mume na mke wenye umri mkubwa waliotembea kilometa 76 wakiwa na masanduku na mablanketi ili kuhudhuria kusanyiko la mzunguko katika Zimbabwe.
Utumishi wa shambani wakati wa mkusanyiko hauwi sehemu tena hata kidogo kwenye makusanyiko hayo, lakini hiyo si kwa sababu Mashahidi huuona kwa vyovyote kuwa wenye maana ndogo. Katika visa vingi watu wanaoishi karibu na mahali pa makusanyiko wanatembelewa sasa kwa ukawaida na Mashahidi wenyeji—katika visa fulani, kila baada ya majuma machache. Wajumbe wa kusanyiko hufuliza kuwa macho waone fursa za kutoa ushahidi wa vivi hivi, na mwenendo wao wa Kikristo hutoa ushahidi wenye nguvu kwa njia nyingine.
Uthibitisho wa Udugu wa Kweli
Udugu udhihirikao miongoni mwa Mashahidi kwenye mikusanyiko hiyo huonekana wazi kwa urahisi na watazamaji. Wanaweza kuona kwamba hakuna upendeleo miongoni mwao na kwamba uchangamfu halisi uko wazi hata miongoni mwa wale ambao huenda wakakutana kwa mara ya kwanza. Wakati wa Mapenzi ya Kimungu Kusanyiko la Kimataifa katika New York katika 1958, gazeti Amsterdam News la New York (Agosti 2) liliripoti hivi: “Kila mahali Wanegro, weupe na watu wa Mashariki, kutoka tabaka zote maishani na sehemu zote za ulimwengu, walichangamana pamoja kwa furaha na uhuru. . . . Mashahidi waabuduo kutoka nchi 120 wameishi na kuabudu pamoja kwa amani, wakawaonyesha Waamerika jinsi hilo linavyowezekana kwa urahisi. . . . Kusanyiko hilo ni kielelezo bora sana cha kuonyesha jinsi watu wanavyoweza kufanya kazi na kuishi pamoja.”
Hivi karibuni zaidi, Mashahidi wa Yehova walipofanya mikusanyiko wakati uleule mmoja katika Durban na katika Johannesburg, Afrika Kusini, katika 1985, kati ya wajumbe mlikuwamo vikundi vyote vikubwa vya kijamii na vya lugha katika Afrika Kusini, pamoja na wawakilishi kutoka nchi nyingine 23. Ushirika mchangamfu miongoni mwa watu 77,830 waliohudhuria ulionekana wazi kwa urahisi. “Hii ni maridadi sana,” akasema mwanamke mmoja kijana Mhindi. “Kuona Machotara, Wahindi, weupe, na weusi wote wakichangamana pamoja kumebadili maoni yangu yote juu ya maisha.”
Hisia hii ya udugu huwa ni zaidi ya tabasamu, salamu za mkono, na kuitana “ndugu” na “dada.” Kikiwa kielelezo, mipango ilipokuwa ikifanywa kwa ajili ya “Habari Njema za Milele” Kusanyiko ulimwenguni pote katika 1963, Mashahidi wa Yehova walijulishwa kwamba ikiwa wangependa kusaidia wengine kifedha wahudhurie mkusanyiko mmoja, Sosaiti ingefurahia kuhakikisha kwamba fedha hizo zilinufaisha ndugu katika sehemu zote za dunia. Hakukuwa na kuombaomba, na hakuna kitu kilichochukuliwa kwa ajili ya gharama za usimamizi. Fedha zote zilitumiwa kwa kusudi lile lililotaarifiwa. Kwa njia hiyo, 8,179 walisaidiwa kuhudhuria mkusanyiko. Wajumbe kutoka kila nchi ya Amerika ya Kati na ya Kusini walipewa msaada, pamoja na maelfu kutoka Afrika na wengi katika Mashariki ya Kati na Mashariki ya Mbali. Kadiri kubwa ya wale waliosaidiwa walikuwa ndugu na dada waliokuwa wametumia miaka mingi katika huduma ya wakati wote.
Kuelekea mwisho wa 1978, mkusanyiko uliratibiwa kufanywa katika Auckland, New Zealand. Mashahidi katika Visiwa vya Cook walijua juu yao na walitamani kuwapo. Lakini uchumi katika visiwa hivyo ulikuwa katika hali ya kwamba ingalimgharimu kila mmoja kiasi kikubwa kufanya safari hiyo. Hata hivyo, ndugu na dada za kiroho wenye upendo katika New Zealand walichanga nauli za kwenda na kurudi za wanavisiwa kama 60. Walifurahi kama nini kuwapo ili kushiriki karamu ya kiroho pamoja na ndugu zao Wamaori, Wasamoa, Waniue, na Wakaukasi!
Kielelezo cha roho iliyo miongoni mwa Mashahidi wa Yehova ni jambo lililotukia kwenye umalizio wa “Haki ya Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya katika Montreal, Kanada, katika 1988. Kwa siku nne wajumbe Waarabu, Wafaransa, Wagiriki, Wahispania, Waingereza, Waitalia, na Wareno walikuwa wamekuwa wakifurahia programu ileile moja lakini katika lugha zao wenyewe. Hata hivyo, mwishoni mwa kipindi cha mwisho, wote 45,000 walijiunga pamoja katika Olympic Stadium katika wonyesho wenye kuvutia wa udugu na umoja wa kusudi. Pamoja waliimba, kila kikundi kwa lugha yacho chenyewe, “Imba nasi . . . ‘Atawala; E dunia.’”
[Maelezo ya Chini]
a Drama 70 zaidi kama hiyo zilionyeshwa kwenye mikusanyiko wakati wa miaka 25 iliyofuata.
b Kuanzia 1947 hadi 1987, yalikuwa yakifanywa mara mbili kwa mwaka. Kufikia 1972, yalikuwa makusanyiko ya siku tatu; kisha ile programu ya siku mbili ikaanzishwa.
[Blabu katika ukurasa wa 255]
“Nilivutiwa sana na roho ya upendo na fadhili za kidugu”
[Blabu katika ukurasa wa 256]
Magarimoshi ya mkusanyiko—wote wamo ndani!
[Blabu katika ukurasa wa 275]
Si wapangaji wa mkusanyiko wenye kulipwa mshahara mnono, bali wenye kujitolea wasiolipwa
[Blabu katika ukurasa wa 278]
Umoja kati ya weusi na weupe
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 261]
Maazimio Saba ya Mkusanyiko Yenye Umaana
Katika 1922, azimio lenye kichwa “Mwito kwa Viongozi wa Ulimwengu” uliwataka wathibitishe kwamba wanadamu wana hekima ya kutawala dunia hii, la sivyo wakubali kwamba amani, uhai, uhuru, na furaha isiyo na mwisho vyaweza kuja tu kutoka kwa Yehova kupitia Yesu Kristo.
Katika 1923, kulikuwa “Onyo kwa Wakristo Wote” juu ya uhitaji wa haraka wa kukimbia matengenezo yanayodai kwa kusingizia kumwakilisha Mungu na Kristo.
Katika 1924, “Makasisi Washtakiwa” lilifunua wazi mafundisho na mazoea yasiyo ya Kimaandiko ya makasisi wa Jumuiya ya Wakristo.
Katika 1925, “Ujumbe wa Tumaini” lilionyesha kwa nini wale ambao hudai kuwa mianga yenye kuongoza ya ulimwengu wameshindwa kutosheleza uhitaji mkubwa zaidi wa mwanadamu na jinsi ni Ufalme wa Mungu tu uwezao kufanya hivyo.
Katika 1926, “Ushuhuda kwa Watawala wa Ulimwengu” liliwajulisha kwamba Yehova ndiye Mungu wa pekee wa kweli na kwamba sasa Yesu Kristo atawala akiwa Mfalme wa dunia anayestahili. Liliwahimiza watawala watumie uvutano wao wageuze akili za watu kuelekea Mungu wa kweli ili wasipatwe na msiba.
Katika 1927, “Azimio kwa Watu wa Jumuiya ya Wakristo” lilifunua wazi muungano wa kifedha, kisiasa, na kidini ambao hukandamiza wanadamu. Lilihimiza watu waiache Jumuiya ya Wakristo na kuweka tumaini lao katika Yehova na Ufalme wake ulio mikononi mwa Kristo.
Katika 1928, “Tangazo Dhidi ya Shetani na la Kusimama Upande wa Yehova” lilionyesha wazi kwamba Mfalme mtiwa-mafuta wa Yehova, Yesu Kristo, atamzuia Shetani karibuni na kuharibu tengenezo lake bovu, nalo lilihimiza wote wapendao uadilifu wachukue msimamo wao upande wa Yehova.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 272, 273]
Pande za Baadhi ya Mikusanyiko Mikubwa
Mamia ya wajumbe wenye idili waliwasili kwa meli, maelfu kwa ndege, makumi ya maelfu kwa magari na basi
Mpango mzuri wa kitengenezo ulihitajiwa na wafanyakazi wengi wenye moyo wa kupenda walitakwa ili kupata na kugawa mahali pa kulala pa kutosha
Wakati wa mikusanyiko hiyo ya siku nane, milo yenye moto—makumi ya maelfu yayo—walipakuliwa wajumbe kwa ukawaida
Katika 1953, jiji la trela na la mahema liliwapa makao wajumbe zaidi ya 45,000
New York City, katika 1958, watu 7,136 walibatizwa—wengi zaidi ya wakati mwingine wowote tangu Pentekoste ya 33 W.K.
Ishara zenye salamu kutoka nchi nyingi zilionyeshwa, na vipindi viliongozwa katika lugha 21, New York City katika 1953
[Picha katika ukurasa wa 256]
Wajumbe kwenye mkusanyiko wa IBSA katika Winnipeg, Manitoba, Kanada, katika 1917
[Picha katika ukurasa wa 258]
J. F. Rutherford akisema kwenye Cedar Point, Ohio, katika 1919. Aliwahimiza wote washiriki kwa bidii katika kutangaza Ufalme wa Mungu, kwa kutumia “The Golden Age”
[Picha katika ukurasa wa 259]
Mkusanyiko katika Cedar Point katika 1922. Mwito ulitolewa: “Tangazeni Mfalme na Ufalme”
[Picha katika ukurasa wa 260]
George Gangas alikuwapo Cedar Point katika 1922. Kwa miaka kama 70 tangu hapo amepiga mbiu ya Ufalme wa Mungu kwa bidii
[Picha katika ukurasa wa 262, 263]
Wajumbe kwenye mkusanyiko wa 1931 katika Columbus, Ohio, ambao kwa idili walikubali jina Mashahidi wa Yehova
[Picha katika ukurasa wa 264]
“New World Translation of the Christian Greek Scriptures” ikitolewa na N. H. Knorr katika 1950
[Picha katika ukurasa wa 264]
Hotuba zikitolewa na F. W. Franz juu ya utimizo wa unabii wa Biblia zilikuwa jambo kuu la mkusanyiko (New York, 1958)
[Picha katika ukurasa wa 265]
Kwa miaka mingi utumishi wa shambani ulikuwa sehemu kuu ya kila mkusanyiko.
Los Angeles, Marekani, 1939 (chini kabisa); Stockholm, Sweden, 1963 (picha ndogo)
[Picha katika ukurasa wa 266]
J. F. Rutherford aliposema kutoka Washington, D.C., katika 1935, ujumbe ulipelekwa kwa redio na nyuzi za simu kwenye mabara sita
[Picha katika ukurasa wa 268]
Katika Nuremberg, Ujerumani, mwaka 1946, Erich Frost alitoa hotuba motomoto “Wakristo Watahiniwa Vikali”
[Picha katika ukurasa wa 269]
Mkusanyiko wa mahali palipo wazi katika Kitwe, Rhodesia Kaskazini, wakati wa ziara ya N. H. Knorr katika 1952
[Picha katika ukurasa wa 270, 271]
Katika 1958 idadi ya wasikilizaji 253,922, walijaa pomoni na wakazidi stediamu mbili kubwa katika New York, walisikia ujumbe “Ufalme wa Mungu Watawala—Je, Mwisho wa Ulimwengu U Karibu?”
Polo Grounds
Yankee Stadium
[Picha katika ukurasa wa 274]
Grant Suiter, mwenyekiti wa mkusanyiko katika Yankee Stadium katika 1950
[Picha katika ukurasa wa 274]
John Groh, (aketiye), akizungumzia mipango ya mkusanyiko pamoja na George Couch katika 1958
[Picha katika ukurasa wa 277]
Katika 1963 mkusanyiko wa ulimwenguni pote ulifanywa, wajumbe kutoka nchi zipatao 20 wakisafiri nao duniani pote
Kyoto, Japani, (chini kushoto), lilikuwa moja la majiji 27 ya mkusanyiko. Wajumbe katika Jamhuri ya Korea walipata kujuana (katikati). Salamu ya Kimaori katika New Zealand (chini kulia)
[Picha katika ukurasa wa 279]
Mkusanyiko uliotumikia vikundi 17 vya lugha wakati uleule mmoja, katika jiji la mianzi lililojengwa kwa ajili ya pindi hiyo (Lagos, Nigeria, 1970)
[Picha katika ukurasa wa 280]
Mikusanyiko mikubwa mitatu ilifanywa Poland katika 1989, wajumbe wakiwepo kutoka nchi 37
T. Jaracz (kulia) alihutubia wajumbe katika Poznan
Maelfu walibatizwa katika Chorzów
Wasikilizaji walipiga makofi kwa muda mrefu sana katika Warsaw
Wajumbe kutoka iliyokuwa wakati huo U.S.S.R. (chini)
Visehemu vya programu katika Chorzów vilitafsiriwa katika lugha 15