Bidii ya Umisionari—Alama ya Wakristo wa Kweli
“HAWAKUWA na wakati usio wa kazi hata wa kula.” Maneno hayo yanaeleza kwa ufupi mwendo wa Yesu Kristo alipokuwa akitimiza mgawo wake wa umisionari kutoka kwa Babaye wa kimbinguni. (Marko 6:31) Yeye alikuwa amejitoa kwa nafsi yote, hata kufikia hatua ya kusema: “Chakula changu ndicho hiki, niyatende mapenzi yake aliyepeleka, nikaimalize kazi yake.” (Yohana 4:34) Katika nchi yote Yesu alienda akihubiri “habari njema.” (Luka 8:1) Ulikuwa wonyesho kama nini wa bidii ya umisionari!
Ili kuharakisha kazi hiyo, Yesu kwa njia ya sala aliwachagua wale wanafunzi 12 na akawatuma katika mwaka 31 W.K. Yeye aliwaagiza hivi: “Katika njia ya mataifa msiende, . . . afadhali shikeni njia kuwaendea kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli. Na katika kuenenda kwenu, hubirini, mkisema, Ufalme wa mbinguni umekaribia.” (Mt. 10:5-7) Wakati huo maagizo kamili yalitolewa juu ya namna ya kuifanya kazi hiyo na pia maneno hayo yaliwekea kipimo cha eneo lao la kuhubiri. Katika maeneo hayo wao pamoja na Bwana yao walijitumikisha kwa bidii mpaka mwaka 33 W.K.
Wakiwa na vipimo hivyo vya eneo akilini, baadhi ya wanafunzi wa Yesu pengine waliduwazwa na yale aliyokuwa amesema muda mfupi kabla ya kifo chake. Yesu aliwapa “ishara” yenye kuonyesha mwisho wa “taratibu ya mambo” na akatabiri kwamba “habari njema” ingehubiriwa wakati huo katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa “ushuhuda kwa mataifa yote” kabla ya mwisho kuja. Baadaye, Yesu aliyefufuliwa alikazia wanafunzi wake kwamba walipaswa kufanya “wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.” Mwishowe, kabla tu hajapaa, yeye aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Mtapokea nguvu wakati roho takatifu itakapofika juu yenu ninyi, na ninyi mtakuwa Mashahidi wangu mimi katika Yerusalemu na katika Yudea yote na katika Samaria na kwenye sehemu ya mbali sana ya dunia.”—Mt. 24:3,14, NW; 28:19, NW; Matendo 1:8, NW.
Pentekoste ya mwaka 33 W.K. ilipofika kumiminwa kulikoahidiwa kwa roho takatifu, kulifuata, na Petro alipewa mamlaka ya kutumia ‘ufunguo wa Ufalme’ wa kwanza. Kwa sababu hiyo karibu Wayahudi na waongofu 3,000 wakawa Wakristo. (Mt. 16:18, 19; Matendo 2:1-4, 14-41) Katika miaka mitatu na nusu iliyofuata, Petro alitumia “funguo” nyingine mbili, hata kwamba kazi ya misionari ikawa inawafikia kweli kweli watu wa mataifa yote. (Matendo 8:14-17; 10:23-48) Ilikuwa kweli kama nini kwamba roho takatifu ilikuwa imewapa “nguvu” hata kwamba roho ile ile ya umisionari ambayo Yesu alikuwa ameionyesha kwa mara nyingine ilikuwa inaonekana wazi sana! Masimulizi ya kazi ya umisionari ya hao Wakristo wa kwanza kama yanavyopatikana katika kitabu cha Biblia cha Matendo, yanatoa ushuhuda ulio wazi wa bidii nyingi, nyingi sana. Lazima iwe ilimpendeza mtume Paulo kuweza kusema, katika mwaka 61 W.K. kwamba “habari njema” zilikuwa ‘zimehubiriwa katika kuumba kote kuliko chini ya mbingu’!—Kol. 1:23, NW.
BIDII YA KIMISIONARI YAANZISHWA TENA KATIKA NYAKATI ZA KISASA
Hata hivyo, kwa sababu ya uasi-imani (ukafiri) uliofuatana na kupoteza roho ya Mungu, juhudi hiyo ya umisionari ilipotea kwa miaka zaidi ya 1,700. Mahali pake, Jumuiya ya Wakristo iliuchukua upanga wa vita, ukoloni na njia nyingine zisizo za Kimaandiko za kufanya “waongofu.” Je! bidii ya umisionari ya Kristo na wanafunzi wake wa kweli ilikuwa imepotea milele? Hiyo haingewezekana, kwa maana Yesu mwenyewe alikuwa ametabiri kwamba habari njema za Ufalme zingehubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote wakati wa kuwapo kwake kulikoanza mwaka 1914.
Katika miaka iliyoanza na wa 1870 ilikuwa wazi kwamba roho takatifu ya Mungu ilikuwa pamoja na Charles T. Russell na wanafunzi wa Biblia wanyofu waliokuwa wakishirikiana naye. Basi, bidii ya kweli ya umisionari kwa mara nyingine ikaanza kuonekana. Upesi ecclesias (makundi) za Wanafunzi wa Biblia zikatokea kote kote katika kontinenti ya Amerika kaskazini. Afisi ya tawi ya kwanza ya Sosaiti nje ya United States ilianzishwa huko London, Uingereza, katika mwaka 1900. Russell alifanya safari za kuhubiri katika Ulaya, na katika ya pili ya hizo, katika 1903, afisi ya tawi ya Sosaiti ilianzishwa katika Ujeremani. Mwaka uliofuata tawi jingine lilianzishwa, wakati huu katika Australia ambapo kazi ya umisionari ilikuwa imeanza wakati wa mwaka uliotangulia. Katika 1911 na 1912 Russell na wengine walifanya ziara ya ulimwenguni pote, wakihubiri katika sehemu kama Singapore, Filipino, Uchina na Japan. Kweli kweli, bidii ya umisionari iliyokuwa imeonyeshwa na Yesu kwa mara nyingine ilikuwa ikionekana waziwazi sana. Hata hivyo, kama ilivyokuwa kwa habari ya Yesu, bidii yao ya kutoa ushuhuda ilichochea upinzani wa Shetani wa waziwazi. Kwa hiyo kazi ya umisionari ilikuwa pamoja na matatizo na majaribu.
Katika 1915 Ndugu Russell alisema maoni yake kwamba kungali kulikuwa kazi nyingi ya umisionari ya kufanywa. Walakini katika 1916 aliumaliza mwendo wake wa kidunia. Je! kikundi hicho kidogo cha Wakristo wenye kuteswa kingeendelea kuonyesha bidii ya umisionari? Kilifanya hivyo. J. F. Rutherford, msimamizi wa pili wa Sosaiti, kwa kujikaza sana alitia moyo Wakristo hao wote (leo wanajulikana kuwa Mashahidi wa Yehova) washiriki kwa bidii katika utendaji wao wa umisionari. Wale walioweza kuhamia nchi za ugenini walialikwa wafanye hivyo, na kwa hiyo vikundi vidogo vidogo vilienda Afrika, India, Burma, Thailand, Uchina na visiwa vingi vya bahari. Wakati Viti ya Ulimwengu ya Pili ilipofyatuka, angaa kipimo kidogo cha kazi ya umisionari kilikuwa kikifanywa katika nchi zaidi ya 60. Wengine waliokwenda kwenye sehemu hizo za mbali wangali wakitumikia huko baada ya miaka 40 au 50!
MPANGO MPYA WASITAWISHA KAZI YA UMISIONARI WA UGENINI
Vita ya Ulimwengu ya Pili ilizuia sana kazi ya umisionari iliyokuwa ikifanywa katika nyingi ya nchi hizo. Je! vita hiyo ingeelekeza kwenye Har–Magedoni? (Ufu. 16:14, 16, Authorized Version) Je! kazi ya umisionari iliyoanzishwa na Yesu ilikuwa ikifikia kikamilisho chayo? Maulizo hayo yalimalizwa na ufahamu ulio wa wazi wa Ufunuo 17:8, uliotolewa katika hotuba ya watu wote “Amani—Inaweza Kudumu?” kwenye kusanyiko la 1942 la Mashahidi wa Yehova. Katika hotuba hiyo Mashahidi walijifunza kwamba kungekuwa na kipindi cha amani baada ya vita. Akiwa na jambo hilo akilini, N. H. Knorr, msimamizi wa tatu wa Sosaiti, pamoja na wengine wa baraza ya wasimamizi wa Sosaiti, alifanya mipango ya kutumia vizuri kipindi hicho cha amani walichokuwa wakitazamia wakati huo.
Shule iliyokusudiwa kuzoeza Wakristo kwa ajili ya utumishi wa umisionari wa ugenini ilipangwa, pamoja na mazoezi zaidi ya kundini kwa kazi ya umisionari ya sehemu-sehemu. Katika Februari 1, 1943, darasa la kwanza la Shule ya Gileadi ya Sosaiti lilianza mafunzo yalo. Jambo hilo lilionyesha imani kama nini! Hakukuwa nchi ambazo misionari hao wangeweza kupelekwa. Hata hivyo, wakiwa wanajua kwamba kungekuwako kipindi cha amani ambacho kingeweza kutumiwa, walikuwa wakizoezwa.
Mwishowe, wengi wa misionari wa madarasa hayo ya kwanza ya Shule ya Gileadi walianza kuingia katika nchi za Amerika ya Kati na Kusini na visiwa vya Caribbea, na huko watumie mazoezi yao kuwasaidia wengine. Katika siku hizo, kulikuwa matatizo mengi ya kushinda. Kupata mahali pa kuishi, lugha, desturi, chakula, upinzani wa viongozi wa kidini na imani za ushirikina yote hayo yalikuwa magumu ambayo misionari hao wapya walipaswa kukabili. Katika nyingi ya nchi hizo, ni mtu mmoja au wawili tu waliokuwa wakipendezwa au waliokuwa wakitenda katika kazi ya Kikristo ya kutoa ushuhuda wakati misionari hao walipofika. Vijapokuwa vizuizi hivyo vyote, hata hivyo, wengi wa misionari hao wa kwanza wangali wakitumikia katika nchi hizo. Wao ni wenye furaha kama nini kwamba sasa kuna Mashahidi zaidi ya 380,000 wakitumikia pamoja nao katika Amerika ya Kati na ya Kusini na Caribbea!
Shule ya Gileadi iliwatayarishaje misionari hao? Misionari mmoja, ambaye ametumikia kwa miaka 24 katika nchi za Mashariki anatoa maelezo haya: “Kwa kuwa chombo chetu kikuu katika shamba la umisionari kilikuwa Biblia, funzo la Biblia kupitia kitabu kimoja baada ya kingine na mara nyingi mstari baada ya mstari wa Biblia, pamoja na mitaala yenye kuhusiana na hayo juu ya historia, jiografia na njia ya maisha ilivyokuwa katika nyakati za Biblia, akilini mwangu ndiyo yaliyokuwa sehemu ya maana sana ya mazoezi yangu. Pamoja na hayo, tulikuwa na vipindi vya mazoezi ya kuongeza uwezo wetu wa kuzungumza na kufundisha watu. Tulisaidiwa tuone ni marekebisho gani ambayo yangehitajiwa ili kufurahia maisha katika mazingira mapya. Jambo jingine lililonisaidia sana ilikuwa miezi mitano ya kuishi huko Gileadi pamoja na ‘jamaa’ ya namna zote za maisha. Jambo hilo lilinisaidia kujirekebisha kuishi na ‘jamaa’ ya misionari inayotia washiriki wa mazingira tofauti tofauti.” Kwa kadiri ambavyo miaka hiyo imepita, mafundisho ya kawaida ya Gileadi yamefanywa yakawa ya kisasa ili kuyafanya yafae hata zaidi na yawe yenye matokeo zaidi katika kusaidia misionari wapya wajitayarishe kwa ajili ya migawo ya ugenini.
Basi, ni nani wanaoweza kustahili kupokea mazoezi hayo yenye mwelekeo mmoja? Kwa kusema kwa ujumla, matakwa ni kwamba wale wanaotoa maombi wawe wenye umri wa kati ya 21 na 40, bila watu wa kuwategemea au madaraka mengine yanayoweza kuwazuia wasitumikie mahali pengine po pote duniani. Wanaweza kuwa waseja (wasioa au wasioolewa), au wawe wameoana angaa kwa muda wa miaka miwili, na wanapaswa kuwa na afya njema. Lazima wawe walibatizwa angaa miaka mitatu iliyopita, na kwa wakati uliopo (wa kutoa maombi) wawe wametumikia angaa miaka miwili bila kukatiza wakiwa watangazaji wa Ufalme wa wakati wote. Vilevile wenye kutoa maombi wanapaswa kuwa na roho ya misionari ya kweli—wala si kuchochewa na roho ya kutembea-tembea—bali mahali pake, wachochewe na tamaa ya kufanya kazi waliyogawiwa. Jambo hilo linataka wachochewe na upendo mwingi kwa Yehova na wanadamu wenzao katika migawo waliyopewa. Wakichochewa na namna hiyo ya upendo wanaweza kutosheka kikweli katika migawo yao, hata ikiwa huenda mambo yasifae na yasiwe ya starehe kama walivyokuwa wamezoea hapo kwanza.—Luka 10:27.
JE! WEWE UNA BIDII YA MISIONARI YA KWELI?
Bila shaka ni sehemu ndogo tu ya Mashahidi wa Yehova wanaoweza kutumikia wakiwa misionari wa ugenini. Hata hivyo, watumishi wote walio wakf wa Yehova Mungu wanapaswa kuwa na bidii iyo hiyo ya misionari. Hata hivyo, lazima ikubaliwe kwamba inahitaji jitihada kuendeleza bidii hiyo, kwa kuwa kuna vishawishi vingi.
Nyakati nyingine Mashahidi vijana katika shule za masomo ya juu wanaonyesha tamaa ya kufanya mradi wao uwe kazi ya wakati wote ya umisionari, ama nyumbani au ugenini. Walakini wakati unapofika wanapoweza kustahili utumishi huo wa pekee, bidii hiyo ya hapo kwanza inakuwa imekwisha kupotea. Ni jambo gani limekuwa limetokea? Je! wameruhusu roho ya ulimwengu iwakengeushe? Roho ya ulimwengu ni ya kujitafutia anasa, kufuatia anasa na kuchukizwa na kazi ngumu na madaraka. Roho hiyo imekuwa na matokeo juu ya wengine hata wakafikia hatua ya kutokupata uradhi kutokana na kufanya kazi vizuri. Kwa wengi katika ulimwengu, ni lazima kazi iwe inaleta “furaha inayotokana na mchezo,” “kusisimua,” au “mambo kuonekana mazuri yasivyokuwa.” Kama sivyo, haiwavutii. Kwa hiyo, wanaume na wanawake vijana Wakristo sana-sana wanahitaji kujiuliza hivi: Je! kadiri fulani ya upendo huo wa maisha yasiyo magumu imenipata? Je! roho ya ulimwengu—au kitu kingine cho chote—imepunguza bidii yangu ya kazi ya umisionari?
Hata umri wako uwe nini, na hata ingawa huenda usiwe mmoja anayeweza kushiriki wakati wote katika kazi ya umisionari ama nyumbani ama ugenini, ingefaa kujichunguza mwenyewe uamue kama una bidii ya umisionari ama la. Ukiona kwamba kwa njia fulani bidii yako ya umisionari haitoshi, unaweza kufanya nini juu ya jambo hilo?
Pengine kuchunguza Matendo sura ya 4 kutakusaidia uone sehemu zinazohitaji kuangaliwa zaidi ili uweze kuiga kwa ukamilifu zaidi bidii ya umisionari ya Wakristo wa karne ya kwanza. Angalia kwamba kulingana na Mdo 4 mstari wa 13, wapinzani walitambua kwamba mitume “walikuwa pamoja na Yesu.” Pengine kufuatia anasa mbalimbali za maisha haya kumezuia usiwe ‘pamoja na Yesu’ kupitia funzo la Biblia hata kufikia kupoteza bidii yako uliyokuwa nayo hapo kwanza.
Mdo 4 Mstari wa 23 unaonyesha kwamba hata baada ya kukabili jaribu, haraka ilivyowezekana, mitume, kwa mara nyingine walikutana pamoja na waamini wenzao ili watiane nguvu kiroho na kujengana bidii. Tofauti na hilo, wakati mtu anaporuhusu starehe na utendaji mwingine ambao si kosa umzuie asihudhurie mikutano kwa ukawaida pamoja na Wakristo wenzake, polepole atapoteza bidii ya umisionari ya kweli. Sala nzuri ambayo imeandikwa katika Mdo 4 mistari ya 24 mpaka 30 inatoa uongozi zaidi kwa wale wanaotafuta kuongeza bidii. Angalia jinsi wanafunzi wa Yesu walivyotoa sala ya kutaka ujasiri wa kusema. Je! unatafuta uwezo wa roho ya Mungu ukusaidie uongeze bidii yako, ukifanya hivyo kwa juhudi kama walivyofanya waamini hao katika sala hiyo? Ikiwa ndivyo, basi unaweza kutazamia matokeo kama hayo yaliyoandikwa katika Mdo 4 mstari 31. Yehova alijibu sala yao, walijazwa kwa roho takatifu na walikuwa “wakinena neno la Mungu kwa ujasiri.”
Yesu alisema “habari njema” zingehubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda. Katika kufanya kazi hiyo iliyo pendeleo Wakristo wengine wanaonyesha bidii ya umisionari katika eneo lao la nyumbani, wengine katika mashamba ya ugenini. Kwa shauku, ‘wananena neno la Mungu kwa ujasiri.’
Kwa fadhili zisizostahilika za Yehova ujumbe wa Ufalme sasa unasikiwa katika nchi zaidi ya 200, kwa kulinganisha na zile nchi 54 wakati shule ya Gileadi ilipoanzishwa. Maisha ya misionari yako namna gani? Mahitaji yao ya kimwili yanatolewaje? Wanaishi wapi? Wanashughulikaje na matatizo ya lugha? Ikiwa unafikiria juu ya utumishi wa umisionari wa ugenini, masimulizi yafuatayo yatakutuliza kweli kweli.