Maswali kutoka kwa Wasomaji
● Samweli wa pili sura 8:13 inasema kwamba, Daudi aliwaua Waedomi katika Bonde la Chumvi, walakini 1 Nyakati 18:12 inasema tendo hilo lilifanywa na Abishai, na maneno yaliyo kichwa ya Zaburi 60 (NW) yanasema kwamba Yoabu ndiye aliyewashinda. Kwa sababu gani mambo yako hivyo?
Masimulizi hayo matatu kwa wazi yanaeleza kushindwa kwa Waedomi kutokana na maoni matatu tofauti-tofauti. Katika 2 Samweli, inasemekana Daudi ndiye aliyeshinda kwa sababu yeye alikuwa ndiye mfalme, amiri-jeshi wa Israeli na ndiye aliyetoa ruhusa ya kufanya vita. Kwa kuwa Yoabu ndiye aliyekuwa jemadari mkuu, anasifiwa kuwa ndiye aliyeupata ushindi katika maneno yaliyo kichwa ya Zaburi 60 (NW). Abishai alikuwa jemadari wa kikosi kimoja chini ya uongozi wa Yoabu na bila shaka alifanya sehemu kubwa katika shughuli hiyo ya kijeshi. Jambo hilo linaonyesha sababu gani anasemekana ndiye aliyepata ushindi katika masimulizi ya Nyakati. Kwa hiyo hakuna kupingana ko kote. Hata leo ni jambo la kawaida kusema jambo fulani lilitimizwa na yule aliyetoa ruhusa au yule aliyefanya sehemu kubwa katika kulifanya litimie kwa kufanikiwa.