Soma na Ujifunze Kutokana na Vitabu Viwili vya Mambo ya Nyakati
“NI VYA kusudi gani vitabu vya Mambo ya Nyakati?” Wanafunzi wengi wameuliza ulizo hilo wanaposoma Biblia na kuimaliza kwa mara ya kwanza. Wanasoma vitabu vya Samweli na Wafalme na kuona historia ya watu wa Mungu ya kuwa chini ya wafalme ikiwa imeelezwa kwa njia ya waziwazi na ustadi. Halafu sasa wanaelekeana na vitabu viwili vya Mambo ya Nyakati: sura tisa ndefu za vizazi (nasaba) zikifuatwa na kurudia-rudia mengi ya mambo ambayo tayari wameyasoma. Kichapo Eerdmans’ Bible Handbook kinaeleza hivi: “Kwa kuonekana kijuujuu, [vitabu vya] Mambo ya Nyakati vinaonekana ni kama vinarudia kwa njia isiyopendeza na [iliyo] ya adili zaidi mambo ambayo yamo tayari katika 2 Samweli na Wafalme.”
Lakini hayo ni maoni ya kijuujuu tu. Sawa na vile zile Injili nne katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo zinavyozungumza habari zile zile za ujumla, lakini kila moja ikieleza mambo kwa upande tofauti na kuongeza habari fulani zisizoelezwa na injili nyingineyo, ndivyo mwandikaji wa vitabu vya Mambo ya Nyakati anavyoonyesha mambo kutokea upande wake mwenyewe na kutoa habari zisizopatikana kwingineko, ingawa anazungumza habari zile zile za ujumla za vitabu vilivyotangulia. Yeye alikuwa akiandika kwa ajili ya kipindi cha pekee cha wakati na alikuwa na miradi hakika, aliyoikusudia akilini mapema. Tunapofahamu jambo hilo, tunaweza kufurahia kusoma vitabu hivyo na kujifunza masomo yatakayotusaidia leo.
Vilijaza Uhitaji Fulani
Vitabu vya Mambo ya Nyakati viliandikwa, labda na Ezra, kwa faida ya Wayahudi waliorudia Nchi ya Ahadi mwishoni mwa utumwa wa miaka 70 katika Babuloni. Baada ya kueleza juu ya utawala wa Daudi na Solomoni na mgawanyiko uliofuata kati ya watu wa Mungu wakawa mataifa mawili, mwandikaji alikaza fikira juu ya ufalme wa kusini wa Yuda na kueleza historia yao kwa njia ambayo ingewapa masomo wahamishwa waliorudishwa. Alisimulia tangu mwanzo usitawi wa ule ukoo mashuhuri wa kifalme wa Daudi, na kwa kufanya hivyo akajibu maulizo ya maana sana: Kwa sababu gani Yehova aliruhusu taifa lake chaguliwa lihamishwe liwe katika nchi ya kipagani? Nao Wayahudi waliorudishwa (na pia Wakristo wa kweli leo) wangeweza kuepukaje kufanya makosa yaliyowaongoza kwenye adhabu hiyo?
Yale Maelezo ya Maana Kuhusu Vizazi
Sura tisa za kwanza za 1 Mambo ya Nyakati zina orodha ndefu-ndefu za vizazi (nasaba). Kwa sababu gani mwandikaji akatia ndani habari hizo? Kwa sababu habari za vizazi zilikuwa za maana katika Israeli. Mambo ya urithi na mapendeleo yalikamatana navyo. Wengine wa Waisraeli wenye kurudi, kutia na wengine wa jamaa ya kikuhani, hawakuweza kuthibitisha ukoo wao, na jambo hilo lilileta balaa kubwa. (Ezra 2:59-63) Kwa hiyo, jambo hilo la kufuatisha vizazi kwa uangalifu liliwapendeza sana sana.
Lakini namna gani msomaji wa Biblia leo? Je! aruke sura hizo tisa aanze kusoma Kitabu cha Kwanza cha Mambo ya Nyakati kuanzia masimulizi ya kifo cha Sauli katika sura ya 10? Hapana, orodha hizo za mambo ya vizazi ni sehemu ya “kila andiko, lenye pumzi ya Mungu.” (2 Timotheo 3:16) Sura tisa za kwanza za Kitabu cha Kwanza cha Mambo ya Nyakati zina hazina za habari.
Kwa mfano, ni humo tu tunamosoma juu ya Yabesi, mzao wa Yuda aliyejithibitisha mwenye kuheshimika kuliko wale wengine. (1 Mambo ya Nyakati 4:9, 10) Hapa, pia, tunapata orodha yenye mafaa juu ya ukoo wa kifalme wa Daudi, ambayo inafunua uhakika wenye maana kwamba Zerubabeli, gavana wa Wayahudi baada ya kurudi kwao kutoka Babuloni, alikuwa wa ukoo huo.—1 Mambo ya Nyakati 3:10-19.
Kutueleza Mengi Zaidi Juu ya Daudi
Sura zilizobaki za Kitabu cha Kwanza cha Mambo ya Nyakati, zinajazia vizuri masimulizi ya kihistoria yasiyoelezwa kwa ukamili katika vitabu vilivyotangulia, hasa kukamilisha vizuri maarifa yetu ya kumjua Mfalme Daudi. Katika vitabu vilivyotangulia, msomaji wa Biblia alipata kumjua Daudi kuwa mtumishi mwenye kujitolea utumishi wa Yehova, shujaa wa kivita mwenye matendo hodari, mshairi, na kiongozi mzuri wa watu. Katika Kitabu cha Kwanza cha Mambo ya Nyakati tunajifunza kwamba alikuwa pia stadi wa kupanga mambo kitengenezo. Alilitengeneza taifa na jeshi, ana akatengeneza ibada hekaluni, akafanya migawanyo 24 ya makuhani, Walawi, na waimbaji.—1 Mambo ya Nyakati 23:1–27:22.
Kitabu cha Pili cha Samweli kinaeleza tamaa nyingi sana ya Daudi kutaka kujenga “nyumba,” au hekalu, kwa ajili ya sanduku la agano. (2 Samweli 7:2-5) Yehova hakumruhusu Daudi aendelee na mipango yake, na Kitabu cha Kwanza cha Mambo ya Nyakati kinaeleza sababu. Daudi alikuwa mtu wa damu. Hekalu lingejengwa na mrithi wa Daudi, mtu wa amani. (1 Mambo ya Nyakati 22:8-10) Kitabu cha Pili cha Samweli kinatuambia pia namna Daudi alivyokuja kununua sakafu ya kupuria ambapo mwishowe hekalu lilijengwa. (2 Samweli 24:18-25) Kitabu cha Kwanza cha Mambo ya Nyakati kinaongezea jambo hilo kwa kusimulia mchango mkubwa sana ambao Daudi alikusanya na mipango yote aliyoifanya, hivi kwamba wakati Solomoni alipokuwa katika hali ya kuweza kuanza kulijenga hekalu, apate kila kitu kikiwa tayari. (1 Mambo ya Nyakati 22:6-19) Yehova hata alimpa Daudi maelezo ya vile hekalu lingekuwa, naye Solomoni akapitishiwa maelezo hayo kwa uaminifu.—1 Mambo ya Nyakati 28:9-21.
Baraka ya Yehova . . .
Unapoendelea kusoma kitabu cha pili cha Mambo ya Nyakati, utaona kwamba kichwa fulani kinaanza kuonekana wazi: Wakati wafalme wa Yuda walipoonyesha uhakika kamili katika Yehova, walibarikiwa. Walipokosa kufanya hivyo, watu waliumia. Kwa mfano, Abiyamu mwana wa Mfalme Rehoboamu, alipokuwa akipiga vita dhidi ya Israeli, alishindwa maarifa sana na Yeroboamu, mfalme shujaa wa ufalme wa kaskazini. Jeshi la Abiyamu lilijikuta likiwa limezungukwa, kwa hiyo “wakamlilia [Yehova], na makuhani wakapiga mapanda.” Matokeo? “Mungu akampiga Yeroboamu na Israeli wote mbele ya Abiya [Abiyamu] na Yuda.”—2 Mambo ya Nyakati 13:14, 15.
Vivyo hivyo Asa, mwana wa Abiya, alishinda jeshi kubwa sana la Waethiopia milioni moja kwa sababu alimtegemea Yehova. (2 Mambo ya Nyakati 14:9-12) Yehoshafati mwana wa Asa aliokolewa kwenye shambulio la muungano wa Amoni, Moabu, na Waedomi, halafu miaka mingi baadaye mzao wake, Mfalme Hezekia, akaokolewa kwenye nguvu za Ashuru, kwa sababu ya kuwa na uhakika ule ule.—2 Mambo ya Nyakati 20:1-26; 32:9-23.
. . . na Kuchukizwa Kwake
Hata hivyo, wengi wa wafalme hawakuonyesha uhakika huo, kwa kawaida sababu ikiwa ni moja kati ya hizi tatu. Ya kwanza ni kwamba wengi walianguka ndani ya mtego wa kuabudu sanamu. Yoashi, mjukuu wa Yehoshafati, alianza vizuri, lakini akageukia kuabudu sanamu. Yehova aliondoa ulinzi wake, na Yoashi akashindwa katika pigano na Wasiria (Washamu) na mwishowe akauawa. (2 Mambo ya Nyakati 24:23-25) Mwana wa Yoashi, Amazia, alionyesha namna kuabudu sanamu kulivyo na nguvu za kushawishi mtu. Amazia alianza kwa kuonyesha mfano mzuri wa kuamini Yehova. Halafu, baada ya vita yenye mafanikio ambamo alishinda Waedomi, akashangaza sana kwa kuchukua miungu ya Waedomi na kuanza kuiabudu hiyo! (2 Mambo ya Nyakati 25:14) Kwa hiyo, tena, Yehova aliondoa ulinzi wake kwa mfalme huyo.
Labda mfano ulio mbaya zaidi wa kuabudu sanamu ni Manase. Si kwamba tu mfalme huyo aliabudu miungu ya uwongo bali pia aliwatesa kwa bidii wale walioshika sana ibada ya Yehova. Ni kwa sababu “aliujaza Yerusalemu damu zisizo na hatia” kwamba Yehova alikaza nia kuharibu Yuda. “Wala [Yehova] hakukubali kusamehe.” (2 Wafalme 21:11; 23:26; 24:3, 4) Hata hivyo, jambo la kushangaza ni kwamba Manase alikuwa mwana wa Hezekia, mmoja wa wafalme wa Kiyahudi walio waaminifu zaidi. Kwa kweli, yeye alizaliwa kwa muujiza. Alizaliwa baada ya Yehova kurefusha kimuujiza maisha ya Hezekia baba yake. (Isaya 38:1-8; 2 Mambo ya Nyakati 33:1) Na kuna mshangazo mwingine wa mwisho. Baada ya miaka mingi ya kutesa waabudu wa Yehova, Manase alitubu na mwishoni mwa maisha yake akawa ni mtumishi wa Yehova!—2 Mambo ya Nyakati 33:1-6, 12-17.
Jambo la pili lililotega wafalme wa Yuda ni kufanya mapatano na mataifa ya kigeni. Mambo hayo yaliingiza Asa mfalme mwema matatani, na pia Ahazi mfalme asiyekuwa mzuri sana. (2 Mambo ya Nyakati 16:1-5, 7; 28:16, 20) Msiba wa kufanya mapatano ya kigeni ulionekana katika kisa cha Yehoshafati. Kwa kukosa hekima mtumishi mzuri huyo wa Yehova alisitawisha mapatano na Mfalme Ahabu wa Israeli mwenye kuabudu sanamu. Alimfuata Ahabu kwa upumbavu katika safari za kijeshi na kuruhusu Yehoramu, mwanaye, aoe binti ya Ahabu, Athalia. Athalia alikuwa na mavutano mabaya juu ya mumeye, Yehoramu, na juu ya Ahazia, mwanaye, wakati walipopata zamu zao za kuwa wafalme. Halafu, Ahazia alipokufa, mwanamke huyo alinyakua kiti cha enzi na kuua wote ambao wangeweza kumpinga. Jambo la kufurahisha ni kwamba Yehova aliongoza mambo kwa njia ambayo ukoo wa kifalme wa Mfalme Daudi ulihifadhiwa, lakini lo, msiba gani kwa sababu ya kufanya uhusiano wa kigeni usio lazima!
Mtego wa tatu ambamo wengine wa wafalme waliingia ni kiburi. Hicho kilitia madoa katika miaka ya mwisho ya Mfalme Asa mwema, na kwa sababu ya hicho, Mfalme Uzia, yule mwanajeshi mwenye akili nyingi sana, akaishi sehemu ya mwisho ya maisha yake akiwa mkoma-mkaa-peke-yake. Hata Mfalme Hezekia mwaminifu alianguka ndani ya mtego huo alipotembelewa na wajumbe wa siri kutoka Babuloni kisha akawaonyesha kwa kiburi hazina ya hekalu.—2 Mambo ya Nyakati 32:25, 26; Isaya 39:1-7.
Visome na Ujifunze Kutokana Navyo
Ndiyo, vitabu vile viwili vya Mambo ya Nyakati vina habari zenye thamani kubwa sana. Vinaonyesha namna ya mwenendo unaopendeza Yehova, na vinaonyesha kwamba hata wafalme wanaweza kuanguka ndani ya dhambi. Hilo ni onyo kubwa leo, hasa kwa wale walio katika vyeo vya mamlaka katika kundi la Kikristo! Kuabudu sanamu katika nyakati za kisasa ni jambo linaloweza kupata mtu kwa njia ya ujanja sana kama ilivyokuwa katika siku za wafalme Waisraeli, na ni lazima sisi tupige moyo konde kuepuka jambo hilo. (Waefeso 3:19; Wakolosai 3:5; Ufunuo 13:4) Ni lazima sisi, pia, tuepuke uhusiano usio wa lazima pamoja na ulimwengu. (Yohana 17:14, 16; Yakobo 4:4) Na kwa uhakika, udhaifu wa kiburi, au majivuno, ungali ni tatizo ambalo tunapaswa kupigana nalo.—Mithali 16:5, 18; Yakobo 4:6, 16.
Kusoma na kujifunza kutokana na vitabu vile viwili vya Mambo ya Nyakati kutaimarisha nia yetu ya kujikaza tumtumikie Yehova kwa kufuata mifano myema na kuepuka mifano mibaya tunayoonyeshwa kutokana na historia ya Kiyahudi. Kufanya hivyo kutatutia moyo tufuate ile iliyo myema na kuiepuka ile mibaya, ili “kwa saburi na faraja ya maandiko tupate kuwa na tumaini.”—Warumi 15:4.
[Sanduku katika ukurasa wa 29]
Kitabu cha Kwanza cha Mambo ya Nyakati kinasaidiaje kuthibitisha kwamba Yesu hakuzaliwa Desemba 25?
Kulingana na Kitabu cha Kwanza cha Mambo ya Nyakati, Mfalme Daudi aliwapanga makuhani katika vikundi 24, kila kikundi kikapewa mgawo kutumikia kwa juma moja hekaluni. Hivyo, mshiriki wa kila kikundi angepata nafasi ya kutumikia hekaluni mara mbili kwa mwaka, baada ya vipindi vya karibu miezi sita-sita.
Kikundi cha kwanza kilianza kutumikia mara tu baada ya mwisho wa Sikukuu ya Vibanda, karibu na mwisho-mwisho wa Septemba/mapema Oktoba. Kikundi cha nane, kilichoitwa kwa jina la Abiya, kilitumikia juma moja katika mwisho-mwisho wa Novemba/mapema Desemba, halafu juma jingine mwisho-mwisho wa Juni/mapema Julai. Kwa sababu gani zamu ya Abiya ni ya maana? Kwa sababu, kulingana na masimulizi ya Luka, baba ya Yohana Mbatizaji, Zekaria, alikuwa wa “zamu ya Abiya,” na kwa kweli alikuwa akitumikia hekaluni wakati malaika alipomtokea na kutangaza uzawa uliokuwa ukija wa Yohana.—Luka 1:5, 8, 9.
Kama vile maandishi ya Luka yanavyoonyesha, Yohana alichukuliwa mimba muda mfupi sana baada ya hapo. Kwa hiyo, yeye alizaliwa miezi tisa baadaye, ama mapema Septemba ama mapema Aprili. Maandishi ya Luka yanaonyesha pia kwamba Yesu alikuwa na umri mdogo kuliko Yohana kwa miezi sita. (Luka 1:26) Hivyo jambo hilo linalotokana na kitabu cha Mambo ya Nyakati linaonyesha kwamba, badala ya kuzaliwa mwishoni mwa Desemba, Yesu alizaliwa ama mapema Machi, ama mapema Oktoba. Maandiko mengine yanaonyesha kwamba mwezi Oktoba ndio wakati sahihi.—Ili upate habari zaidi, ona Mnara wa Mlinzi (Kiingereza), Juni 15,1954, ukurasa 382.
[Sanduku katika ukurasa wa 30]
Kwa sababu gani Yusufu akawa baba ya makabila mawili ya Israeli, hali ndugu zake walikuwa baba za kabila moja tu kila mmoja wao?
Kitabu cha Kwanza cha Mambo ya Nyakati kinatusaidia kujibu ulizo hilo. Yusufu alipewa sehemu maradufu iliyokuwa mali ya mzaliwa wa kwanza. Ni kweli kwamba Yusufu alikuwa ndiye mwana wa karibu na mwisho kati ya wale wana 12 wa Yakobo, lakini ndiye alikuwa mwana mkubwa wa Raheli, mke mpendwa zaidi wa Yakobo. Kwa kuzaliwa, haki ya mzaliwa wa kwanza ingalipasa kumwendea mwana mkubwa zaidi wa Yakobo, Reubeni, aliyekuwa mzaliwa wake wa kwanza kupitia Lea. Lakini, kama vile Kitabu cha Kwanza cha Mambo ya Nyakati kinavyotuambia, Reubeni aliipoteza kwa sababu ya kutenda dhambi nzito. Maandishi yanasema hivi: “Reubeni . . . ndiye aliyekuwa mzaliwa wa kwanza; lakini, kwa kuwa alikinajisi kitanda cha babaye, haki yake ya mzaliwa wa kwanza walipewa wana wa Yusufu, mwana wa Israeli; tena nasaba isihesabiwe kwa kuifuata hiyo haki ya mzaliwa wa kwanza.” Masimulizi yanaendelea kusema: “Kwani Yuda ndiye aliyeshinda miongoni mwa nduguze, na kwake ndiko alikotoka mtawala; bali haki ile ya mzaliwa wa kwanza alipewa Yusufu.”—1 Mambo ya Nyakati 5:1,2.