Uenezaji wa Evanjeli—Mahali Pao Katika Ibada ya Kweli
“Imani yenu haipasi kutegemea falsafa ya kibinadamu bali uwezo wa Mungu.”—1 Wakorintho 2:5, THE JERUSALEM BIBLE.
1. (a) Mashahidi wa Yehova wanajulikana ulimwenguni pote kwa ajili ya utendaji gani? (b) Utendaji huo ni wa maana kadiri gani?
MASHAHIDI WA YEHOVA wanajulikana kimataifa kuwa waenezaji wa evanjeli, yaani, wajumbe wa habari njema. Mchunguzi wa hali za kijamii aliye Mwingereza, J. A. Beckford, aliandika hivi katika kichapo Social Compass cha Januari 1977: “Mashahidi ni kati ya waenezaji wa evanjeli na watu wenye kugeuza wengine kidini kwa bidii nyingi zaidi katika ulimwengu wa kisasa.” Aliongezea hivi: “Kwa wazi hiyo ni sababu iliyo wazi inayofanya Sosaiti hiyo iongezeke, ingawa mara nyingi sababu yenyewe inapuzwa na watu wale wengine.” Lakini je! kazi ya kuuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi inampendeza Yehova? Historia na mambo ya uhakika ya siku hizi yanajibu Ndivyo! Uenezaji wa evanjeli, yaani, kuzihubiri habari njema za Ufalme wa Mungu, ndiyo kazi ya msingi ya Ukristo. Ndiyo alama yenye kuonyesha watu walio wa Mungu, ya zamani na ya sasa.
2. Kuuhubiri Ufalme kunatimiza nini?
2 Kazi ya kuuhubiri Ufalme inatimiza nini? Kwanza, inawezesha mtu kwa njia yenye kuonekana wazi aonyeshe upendo na hali ya kuthamini kuelekea Mungu Mwenye Nguvu Zote na uumbaji Wake wa kibinadamu. (Mathayo 22:37-39) Jambo la maana zaidi ni kwamba, kupitia uenezaji wa evanjeli sifa za Yehova za hekima isiyolinganika na uwezo wa kustaajabisha zinajulishwa kwa wengine.—Matendo 1:8; 4:33; Waefeso 3:10
Yehova Anazidhamini Habari Njema
3. (a) Kwa sababu gani Yehova anaweza kusemwa kuwa ni mweneza-evanjeli? (b) Habari njema zinategemea nani hasa, naye alipewa agizo gani?
3 Yehova alikuwa ndiye Mweneza-Evanjeli wa kwanza, au mleta-habari-njema. Unabii wake wa kwanza ulitangaza habari njema za ukombozi kwa wanadamu wasio wakamilifu, kupitia “uzao” fulani ulioahidiwa. (Mwanzo 3:15) Baadaye, Mungu alimtumia Isaya kuwa mneni wake wa kiunabii kutabiri kwamba Masihi, Yesu Kristo, ‘angewahubiri wanyenyekevu habari njema,’ akiwa ndiye Mkuu katika huo “uzao.” (Isaya 61:1) Kwa hiyo Yehova alikusudia Kristo awe mhubiri wa habari njema—mweneza-evanjeli.
4, 5. Ni kwa njia gani malaika wametenda kama waeneza-evanjeli?
4 Yehova ameagiza wengine wahubiri habari njema. Viumbe wa kiroho walio hodari kwa nguvu, yaani malaika, wameshiriki kazi hiyo iliyokubaliwa na Mungu. Jambo la kupendeza ni kwamba katika Kiebrania na Kigiriki pia, neno “anjeli” (malaika) linamaanisha kwa halisi “mjumbe,” na neno “mweneza-evanjeli” limetolewa katika maneno mawili ya Kigiriki yanayomaanisha “-ema” na “anjeli” (malaika, au “mjumbe”). Kwa mfano, malaika wa Mungu ‘alimhubiri Abrahamu habari njema zamani.’ (Wagalatia 3:8; Mwanzo 22:15-18) Habari njema hizo zilikuwa kwamba ukoo wa Abrahamu ungetokeza ule “uzao” ulioahidiwa, na kwamba mataifa yote yangejibariki hakika kupitia “uzao” huo. (Mwanzo 12:2, 3) Karne 20 baadaye, yule malaika Gabrieli akitumikia kama mweneza-evanjeli alitangazia Zekaria uzawa uliokuwa ukija wa Yohana Mbatizaji, akisema: “Nimetumwa niseme nawe, na kukupasha habari hizi njema.” Yohana Mbatizaji aliitayarisha njia kwa ajili ya yule mkuu wa “Uzao” wa Abrahamu, Yesu Kristo.—Luka 1:19.
5 Akiendelea kutenda kama mweneza-evanjeli, Gabrieli alimtokea Mariamu kumletea ujumbe wa furaha juu ya uzawa uliokuwa ukija wa Yesu. (Luka 1:26-38) Miezi kadha baadaye, wachungaji walishtushwa na malaika-mweneza-evanjeli aliyetangaza hivi: “Msiogope; kwa kuwa mimi ninawaletea habari njema ya furaha kuu itakayokuwa kwa watu wote.” Halafu malaika huyo akaungwa mkono na umati wa viumbe wa kiroho wenye kuuthibitisha ujumbe huo wa habari njema. (Luka 2:8-14) Ushuhuda mkubwa isivyo kawaida wa kuonyesha uwezo wa Mungu wa kuzidhamini habari njema kupitia malaika haukukoma wakati Mwanaye alipozaliwa, bali uliendelea muda wote wa historia ya karne ya kwanza ya kundi la Kikristo. Malaika aliwafungua mitume waliotiwa gerezani kisha akaamuru hivi: “Mwendelee kuwaambia watu.” (Matendo 5:20, NW) Mwelekezo wa kimalaika ulitolewa ili wapate watu wa kupendezwa na kusudi watumishi wa Mungu wasaidike. (Matendo 8:26; 10:3; 12:7-11) Naye mtume Yohana, aliyesimulia kwa uongozi wa Mungu matukio ambayo yangekuwa katika “siku ya Bwana,” aliona kwa njozi ‘malaika akiruka katikati ya mbingu, mwenye Injili ya milele aihubiri’—ni kama kusema afanye uangalizi juu ya mweneo wa duniani pote wa ujumbe wa Ufalme unaotolewa na watumishi wa kidunia wa Yehova.—Ufunuo 1:10; 14:6.
Mgawo wa Kristo: Eneza Evanjeli!
6. (a) Yesu aliuwekea msingi gani utangazaji wa habari njema? (b) Yesu alihakikishaje kwamba kazi ya kueneza evanjeli ingeendelea baada ya kifo chake?
6 Kwa sababu gani kundi la kwanza la Kikristo lilikuwa na ujasiri mwingi hivyo na ukakawanifu katika utoaji walo wa ushuhuda? Ni kwa sababu Kristo, aliye Mwanzilishi, alitumia hekima na uwezo wa Mungu kujenga juu yake mwenyewe tengenezo imara sana la waeneza-evanjeli. Kristo alifanya hivyo kwa njia mbili. Kwanza, alitimiza mgawo wake mwenyewe wa ‘kuwahubiri wanyenyekevu habari njema. (Isaya 61:1) Na pili, yeye binafsi alizoeza washirika wake 12 wa karibu kuhubiri, kisha akazoeza wengine 70. Hivyo Kristo alianzisha chanzo imara cha wahubiri ili waiendeleze kazi ya kueneza evanjeli baada ya kifo chake.—Mathayo 10:5-42; Luka 10:1-16.
7. Katika kuletea watu habari njema, hekima ya Mungu imetofautianaje na hekima ya kibinadamu?
7 Yesu alikuwa hodari wa matendo katika kuuhubiri Ufalme. Alijishughulisha sana kueneza evanjeli kwa sababu alijua watu walihitaji kuzisikia habari njema za Ufalme wa Mungu—ile serikali mpya ya kimbingu itakayoleta amani ya kudumu duniani na kuondoa mambo yote yanayosababisha taabu nyingi. Kwa hiyo alipomaliza ziara ya kueneza evanjeli katika miji na vijiji na akawa ameona hali ya kiroho yenye kusikitisha ya halaiki ya watu, yeye aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Mavuno ni mengi, lakini watenda kazi ni wachache. Basi mwombeni Bwana wa mavuno, apeleke watenda kazi katika mavuno yake.” (Mathayo 9:37, 38) Yesu alifanya haraka akaanza kutimiza ombi hilo. Moja la maagizo ya kwanza aliyowapa mitume wake ni hili: “Katika kuenenda kwenu, hubirini, mkisema, Ufalme wa mbinguni umekaribia.” Wahubirieni watu, ukawa ndio mwito wake. Ili kutuliza wanadamu wenye kusumbuka moyoni, hekima ya kibinadamu ingaliweza kumsukuma aanzishe mpango wa kijamii wa kufanya jambo lo lote lile kupendeza wingi wa watu, au kuanzisha baraza la mapinduzi ili kutimiza kazi hiyo; lakini Kristo alionyesha hekima ya Mungu. Lilikuwa jambo jepesi tu: “Katika kuenenda kwenu, hubirini,” na basi.—Mathayo 10:7.
8. Kristo alijisikiaje wakati wanafunzi wake waliporudi kutoka mahubiri yao, na kwa sababu gani?
8 Baada ya kutoa maagizo hayo, Yesu alinena na wengine akawaambia hata wao waeneze evanjeli. Wahubiri hao waliporudi wakiwa na habari za mafanikio, Yesu aliterema na kusema: “Nakushukuru [hadharani], Bwana wa mbingu na nchi, kwa kuwa mambo haya umewaficha wenye hekima na akili; umewafunulia watoto wachanga.” (Luka 10:21) Hao “watoto wachanga” walikuwa ni wanafunzi wa Kristo waliokuwa watu wazima, na uenezaji wa evanjeli ulikuwa ndio chombo chao cha kufunulia wengine kweli ya Mungu. Basi, falsafa wala nguvu za kibinadamu sizo zilizouimarisha sana Ukristo wa kweli, bali ni hekima na uwezo wa kimungu ulioonyeshwa kupitia mahubiri ya Ufalme.
Wanafunzi Wote Walieneza Evanjeli
9. Toa mifano ya namna wanahistoria wanaonyesha kwamba msingi wa Ukristo wa kwanza ulikuwa kuuhubiri Ufalme.
9 Ikiwa kuhubiri habari njema za Ufalme ndiko kazi ya msingi ya Ukristo, basi Wakristo wote wa kwanza wangalipaswa kuwa waeneza-evanjeli. Je! ndivyo walivyokuwa? Ndivyo! yajibu historia. Angalia yanayosemwa na vitabu hivi juu ya Wakristo wa karne ya kwanza:
“Siku hizo, ye yote kati ya Wakristo, ndiyo, wote, walikuwa ‘wamisionari.’”—History of Western Civilization.
“Utendaji huu wa kwanza wa kimisheni unaonyesha kwamba kile kikosi cha kwanza cha umisheni hakikuwa hata kidogo cha Mitume peke yao. Bali, jamii yote ya Wakristo ilihusika kwa ujumla.”—New Catholic Encyclopedia.
“Kila Mkristo anatazamiwa awe na tamaa ya kutolea imani yake ushuhuda, tena hiyo iwe njia yake ya maisha.”—Encyclopedia Americana.
10. (a) Ni wakati gani kundi la Kikristo lilipopata kuwa tengenezo lenye kueneza evanjeli? (b) Ni zawadi (karama) gani ya kimwujiza ambayo Mungu aliwapa Wakristo wa kwanza, na kwa kusudi gani?
10 Tangu pale pale mwanzoni mwa kundi la Kikristo katika mwaka wa 33 W.K., kundi lilikuwa tengenezo la kueneza evanjeli. Washiriki walo wa kwanza, yaani wanafunzi 120, hawakupoteza wakati bali walianza papo hapo kuwa wahubiri wa Ufalme. Historia ya kimungu ina maandishi yanayosema ‘wote walijazwa roho takatifu, wakaanza kusema.’ Tafadhali angalia kwamba yanasema wote, wala si wengine tu kati yao, walianza kusema “matendo makuu ya Mungu.” (Matendo 2:4, 11) Hapo ulionekana ushuhuda wa uwezo na hekima ya Mungu ikiwajaza waabudu hao wenye kuitikia majaliwa ya ajabu ya kutoa ushuhuda katika lugha wasizokuwa wamejifunza shuleni hapo kwanza. Mwujiza fulani ulilisimamisha kundi la Kikristo juu ya msingi wa kuzitangaza habari njema.
11. Petro alikaziaje kwamba ni lazima Wakristo wote wawe wahubiri?
11 Baadaye katika siku hiyo, Petro alitumia unabii wa Yoeli kulihusu hilo kundi la Kikristo lililoanzishwa karibuni: “Itakuwa siku za mwisho, asema Mungu, nitawamwagia watu wote [roho] yangu, na wana wenu na binti zenu watatabiri; na vijana wenu wataona maono; na wazee wenu wataota ndoto. Naam, na siku zile nitawamwagia watumishi wangu wanaume na wanawake [roho] yangu, nao watatabiri.” (Matendo 2:17, 18; Yoeli 2:28, 29) Ye yote wa Wakristo, au Wakristo wote tu, walipaswa kuwa waeneza-evanjeli. Wanaume, wanawake na hata vijana wangekuwa na ushiriki wa bidii katika kutoa unabii au kutangaza, kunena, kububujika kwa kutokwa vinywani na ujumbe wa Mungu wa habari njema.
Kueneza Evanjeli Kunatia Ndani Kutoa Onyo
12. Kwa sababu gani ujumbe wa Ufalme wa Mungu si habari njema kwa kila mtu?
12 Ujumbe wa Ufalme wa Mungu si habari njema kwa kila mtu, kwa maana una onyo la uharibifu. Ni lazima mfumo wa sasa ulio mpotovu uondoshewe mbali pamoja na wafuasi wao ndipo zile habari njema ziweze kuwa na faida ya kudumu. (Mithali 21:18) Waabudu wa Yehova wenye mioyo minyofu hawawezi kuigeuza dunia hii iwe paradiso ikiwa alama za uovu zinabaki kuutia madoa uzuri wayo. Yule Mdhamini wa habari njema hakutoa amri ya “kutangaza mwaka wa nia njema” tu bali pia kutangaza “siku ya kulipa kisasi kwa upande wa Mungu wetu.” (Isaya 61:2, NW) Vivyo hivyo, ujumbe wa mmoja wa malaika wanaotajwa katika Ufunuo una maneno haya: “Mcheni Mungu, na kumtukuza, kwa maana saa ya hukumu yake imekuja.”—Ufunuo 14:7.
13. (a) Wakristo wa kwanza walikuwa na nia gani kuelekea kazi ya kueneza evanjeli? (b) Kwa kutumia andiko, onyesha namna Wakristo wa kwanza walivyoona uhitaji wa kufanya haraka.
13 Wakristo wa karne ya kwanza waliona haraka ya wakati, wakazieneza habari njema upesi sana kama ilivyowezekana. Sehemu hiyo ya habari njema iliwatambulisha pia Wakristo wa kwanza kwa watu. “Tazamio la Wakristo juu ya wakati wa mwisho halikuwa tamaa nyingi tu ya kungojea kuja kwa Ufalme wa Mungu.” Badala ya hivyo, tazamio hilo “lilionyeshwa kwa hatua kubwa ajabu ya utendaji wa bidii na ongezeko la harakati za kuutayarisha ulimwengu kwa ajili ya kurudi kwa Kristo na kuja kwa Ufalme,” kinaeleza kitabu Encyclopaedia Britannica. Makundi yalihimizwa kwa ukawaida juu ya kukaribia kwa ule mwisho na uhitaji wayo wa kuwa tayari. Mitume walifahamu kwamba kueneza evanjeli kwa haraka kulikuwa sehemu ya lazima ya Ukristo ndipo iwezekane kuwafikia watu wote kabla ya kufika kwa siku ya Mungu ya kulipa kisasi. Basi, Ukristo ulivuvumka.—Warumi 10:13, 14; 1 Wathesalonike 5:2, 6; 2 Petro 3:11-14.
14, 15. Ni kwa njia gani jitihada ya kueneza evanjeli imekuwa na matokeo makubwa juu ya historia?
14 Ingawa usahihi wa ujumbe wa Ufalme ulififishwa na kupotoshwa baada ya karne ya kwanza, ule mwisho uliendelea kutazamiwa kwa uthabiti. Kwa mfano, kulingana na wanahistoria fulani, kwa kiasi fulani safari ya Columbus ya karne ya 15 kwenye nusu-duara ya magharibi ya dunia ilisababishwa na imani ya kwamba ilikuwa lazima Bara Hindi ifikishiwe habari njema kabla ya Kristo kurudi. Baadaye, maoni kama hayo ndiyo yaliyoharakisha makundi-makundi ya watu wengi wahamie sehemu mbalimbali. Mifano ni kuhama kwa Wapyurita karne ya 17, kuhamia Amerika kwa Wabaptisti, Watetemekaji (Quakers) na Wamethodisti katika karne ya 18, na kuhamia Urusi na Palestina kwa Wajeremani katika karne ya 18 na ya 19.
15 Basi, je! inaweza kusemwa kwamba kazi ya kueneza evanjeli iliyoanzwa na Yesu Kristo imekuwa na matokeo yenye kufika mbali na ya kudumu? Historia inajibu kwa kusema Ndivyo. Ingawa si sikuzote jitihada ya kueneza evanjeli ilipofanywa kama Kristo alivyoagiza, bado ilikuwa na matokeo makubwa juu ya ulimwengu. Kitabu Encyclopaedia Britannica kinamalizia kutoa muhtasari juu ya “Ukristo” kwa kusema hivi: “Ukristo ndiyo nguvu ya kiroho ambayo imeongoza historia ya kibinadamu kwa uthabiti zaidi na labda ukaibadili sana zaidi ya kitu kinginecho chote.”
Uenezaji wa Evanjeli wa Kisasa
16. (a) Maneno yanaweza kukatwa kwa kusema nini juu ya Wakristo wa karne ya kwanza? (b) Ni ulizo gani lingeweza kuulizwa juu ya utoaji wa ushuhuda wa kisasa?
16 Uchunguzi wa maandishi hayo ya historia ya kimungu na ya kilimwengu unafanya maneno yakatwe kwa njia moja ya maana: Kwamba Wakristo wote wa karne ya kwanza walikuwa waeneza-evanjeli. Ili mtu awe Mkristo na abaki akiwa hivyo, ilimpasa awe akihubiri kwa ukawaida. Basi, je! leo hiyo imekuwa njia ya ibada ya kishamba na isiyopendeza, isiyo na ladha ya kisasa ya kuvuta watu? Labda ndivyo ilivyo kwa mawazo wa mwanadamu, lakini sivyo kulingana na mawazo ya Mungu.—Mithali 16:25; Yeremia 8:9.
17. Mashahidi wa Yehova wameirudishaje ile alama ya kweli ya uenezaji wa evanjeli?
17 Historia ya kisasa ya Mashahidi wa Yehova inaonyesha kwamba wao wameurudisha kabisa ule usahihi wa kweli wa ujumbe wa habari njema za Ufalme. Kwa kutii amri ya Kristo wanajishughulisha sana katika kazi ya kueneza evanjeli kwa mapana na marefu, kwa jinsi isiyopata kuwa na kifani. Ni lazima ushuhuda utolewe duniani pote kabla ya mwisho wa mfumo huu. (Mathayo 24:14) Kwa muda wa miaka 100 iliyopita, hapo ndipo hasa Mashahidi wa Yehova wamekuwa wakikazia macho. Toleo la kwanza la Mnara wa Mlinzi, ambao wakati huo ulikuwa ukiitwa Mnara wa Mlinzi wa Sayuni na Mleta Habari za Kuwapo kwa Kristo (katika Kiingereza), lilitaja hivi kusudi la kuwapo kwa gazeti hilo:
“Hii ndiyo namba ya kwanza ya buku la kwanza la ‘Mnara wa Mlinzi wa Sayuni,’ na huenda lisiwe ni kosa kutaja lengo la kuchapishwa kwalo. Ni kwamba sisi tunaishi ‘siku za mwisho’ . . . nasi tunataka sana ‘watu wa nyumba ya imani’ waamke kabisa wauone uhakika uliopo.”—Julai 1879.
Baadaye, mwaka wa 1884, Mashahidi wa Yehova walijumlika pamoja wakiwa waeneza-evanjeli wakatengeneza shirika. Kusudi la shirika hilo lilionyeshwa katika makala ya pili ya mkataba walo kwa maneno haya:
“Kusudi ambalo limefanya shirika hili liundwe ni kueneza sana kweli za Biblia katika lugha mbalimbali kupitia uchapishaji wa trakti, vikaratasi, magazeti na hati nyingine za kidini, na kupitia njia nyinginezo zote zilizo halali kisheria.”
Je! vyombo hivyo vimekuwa vikitimiza kusudi lavyo lililotangazwa? Historia inajibu kwa kusema Ndivyo.
18. Kazi ya kueneza evanjeli ya watu wa Yehova imenasaje fikira za ulimwengu?
18 Kazi ya Mashahidi wa Yehova ya kueneza evanjeli imenasa fikira za ulimwengu. Imetambuliwa na habari zayo zikaandikwa katika magazeti na vitabu, katika mahakama zilizo kuu zaidi na katika vitabu vya historia. Tangu toleo la kwanza la Mnara wa Mlinzi katika lugha moja, ambapo nakala 6,000 zilichapwa mara moja kwa mwezi, mpaka toleo la sasa la nakala 10,050,000 zenye kuchapwa kwa lugha 102, mwenezo walo umekuwa mkubwa kuliko wa jarida lo lote la kidini. Ukuzi umekuwa wa kustaajabisha, ukazidi saa elfu chache zilizokuwa zikitumiwa kila mwaka katika kazi ya kueneza evanjeli karne ya 19. Mwaka wa 1982 saa zaidi ya milioni 384 zilitumiwa katika kazi ya kuhubiri, jumla ya vitabu, vijitabu na magazeti milioni 286 ikaangushwa, na jamaa zaidi ya milioni moja na nusu zikapokea mafundisho ya Biblia katika nchi na maeneo 205. Yote hayo yametimizwa na kikundi cha watu 2,477,608 mwaka wa 1982, na hiyo ni hesabu ndogo wanapolinganishwa na waliyofanya.
19. (a) Mashahidi wa Yehova wanamhesabia nani sifa kwa mafanikio ya kazi ya ulimwenguni pote ya kueneza evanjeli? (b) Ikiwa wewe ni mweneza-evanjeli, inakupasa ufanye nini, kulingana na Mathayo 10:7?
19 Je! Mashahidi wa Yehova wanajisifia ujuzi wao wa akili na nguvu zao kwa sababu ya matendo hayo ya kustaajabisha? Hapana. Sifa yote ni ya Mungu wetu mwenye hekima na uwezo, Yehova, yule Mweneza-Evanjeli wa kwanza. Kwa hiyo wewe utafanya nini? Ikiwa umepaona mahali panapoufaa uenezaji wa evanjeli katika ibada ya kweli na unataka kwa moyo mnyofu kumpendeza Yehova, basi eneza evanjeli kwa ukawaida, juma kwa juma, au kama alivyosema Yesu: KATIKA KUENENDA KWAKO, HUBIRI’!—Mathayo 10:7.
Je! Wewe Unaweza Kujibu Maulizo Haya—
□ Yehova amedhaminije utangazaji wa habari njema?
◻ Malaika wameshiriki daraka gani katika kuzitangaza habari njema?
◻ Yesu Kristo alijishughulisha sana kufanya kazi gani?
◻ Kwa sababu gani inaweza kusemwa kwamba ili mtu awe Mkristo wa kweli ni lazima awe mweneza-evanjeli?
◻ Ni tazamio gani lililobaki likiwa na nguvu kwa wenye kujiita wafuasi wa Kristo?
◻ Leo Mashahidi wa Yehova wanathibitikaje kuwa ni waeneza-evanjeli wa kweli?
[Picha katika ukurasa wa 11]
Waeneza-evanjeli wa kimbingu na kidunia wanashirikiana kwa umoja kuzihubiri habari njema