Wewe Uko Upande Gani wa Lile Suala la Ufalme?
NENO “suala” lina maana gani hapa? Lina maana ya jambo linalofanyiwa ubishi kati ya watu wawili au watatu au vikundi vya watu. Jambo hilo ni jambo linalohitaji kujadiliwa na kukatiwa shauri kimamlaka au kwa njia yenye kusadikisha. Sasa suala linalohusika ni la ulimwenguni pote. Linahusiana na Ufalme wa Mungu kupitia mtawala aliyemweka, Yesu Kristo. Tangu mwaka wa 1919 ulioifuata vita, miaka 63 iliyopita, unabii uliotamkwa na huyo mtawala-mwekwa umetimizwa na Mashahidi wa Yehova katika nchi 205, yaani: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.”—Mathayo 24:14, NW.
Matokeo yamekuwa nini? Yamekuwa kwamba: Tawala zote za dunia zimelazimika kuelekeana na suala lenyewe, yawe yamekuwa yakilifurahia au hayakulifurahia. Kufikia sasa inaonekana wazi hawakulipenda. Sasa ni kama tunaishi katika machweo ya (kutokomea kwa) falme za dunia. Kutokana na vita vya ulimwengu viwili falme nyingi za kidunia zimepinduliwa na mahali pazo pakachukuliwa na tawala za namna nyingine. Pamechukuliwa na jamhuri au na tawala za kutumia nguvu za kiujamaa au namna nyinginezo za serikali za kimamlaka. Leo zingali zimebaki angaa falme 15, kama Mwungano wa Ufalme wa Uingereza na Irelandi ya Kaskazini, ufalme wa Yordani, ufalme wa Nepali katika Asia, ufalme wa Tonga katika Pasifiki ya Kusini na ufalme wa Swazilandi katika Afrika.
Kuondolewa kwa Falme za Kibinadamu
Falme zote za kibinadamu zinaelekeana na giza nene la maangamizi kamili, si kwa sababu tu falme za namna ya serikali ni chache, bali kwa sababu namna zote za serikali ya kibinadamu zinaelekea kuondolewa ziachie njia serikali ya ulimwenguni pote isiyo ya kibinadamu. Unabii wa Danieli 2:44 wa miaka zaidi ya 2,580 iliyopita unasema hivi: “Katika siku za wafalme hao Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele, wala watu wengine hawataachiwa enzi yake; bali utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.” Vita ya Ulimwengu ya Kwanza iliyoanza mwaka wa 1914 haikuwa utimizo wa unabii huo wa Danieli wenye kutia moyo, lakini ilionyesha kwamba Mungu wa mbingu alikuwa amemketisha Mfalme mchaguliwa wake juu ya kiti cha kimbingu akiwa na uwezo wa kuutimiza unabii huo duniani.
Leo serikali zote za kibinadamu zinaelekea uharibifu hata wenye kuletwa na hizo zenyewe, kwa sababu zina vifaa vya vita vya hali ya juu sana ya kisayansi. Waelezaji wenyewe wenye kujua mengi juu ya mambo ya ulimwengu ndio wanaotuonya sote juu ya msiba unaoelekea kutokea. Wanaona kwamba tunaishi katika ule unaoitwa na Biblia “wakati wa mwisho,” au “siku za mwisho.” (Danieli 12:4; 2 Timotheo 3:1, 2) Mataifa hayataki kabisa kuanza vita ya ulimwengu ya tatu, kwa sababu wanajua kitakachowapata wote—maangamizi kwa wote wenye kupigana. Wangependa kuleta mambo kwenye hali ambayo wanaweza kupaza sauti ya shangwe wakisema kwa uhakika, “Kuna amani na salama”! (1 Wathesalonike 5:3) Hivi karibuni watakapofanya tangazo la hadhara la namna hiyo, halitamaanisha amani pamoja na Mungu wa mbingu. La, sivyo, kwa maana tangu mwaka wa 1914 mataifa hayo yamekuwa yakipigana naye. Yanatenda kinyume cha kusudi jema lake kwa wanadamu. Kwa ruhusa ya Mungu yameonyesha muda wa maelfu yote ya miaka ya historia ya kibinadamu kwamba yameshindwa kusimamia dunia kwa njia yenye kuwapa wanadamu wote faida za milele, achia mbali kutawala tu kwa utukufu wa Mungu, Muumba wa mwanadamu.
Mungu Mwenye Nguvu Zote ana wakati wake mwenyewe wa kuukomesha mfumo wa mambo uliopo, kabisa kabisa. Katika wakati wake barabara atauondoa huu mfumo wa mambo ukatokomee mbali. Mashahidi wa Yehova wametumiwa kujulisha mataifa habari hiyo. Basi hayana kisababu cha kujitetea, yaje kusema hayakujua.
Utawala wa Mwanadamu au Utawala wa Mungu?
Mataifa, yaani, mamlaka zao za usimamizi, yameonyesha yako upande gani wa lile suala la ufalme wa Mungu kupitia Kristo. Yamependelea utawala wa mwanadamu uendelee na kupinga wa Mungu. Yameshikilia msimamo wa kuipinga serikali ya Yehova Mungu na Kristo wake. Msimamo wao unapendelea Shetani yule Ibilisi, yule “mkuu wa ulimwengu huu,” kulingana na vile Yesu Kristo alivyowaambia mitume wake: “Yuaja mkuu [“mwana-mfalme,” kulingana na Authorized Version] wa ulimwengu huu, wala hana kitu kwangu.”—Yohana 14:30; angalia pia Mathayo 4:8-11; 2 Wakorintho 4:4.
Kwa kuwa mataifa yamekwisha kufanya uamuzi wao na ndio wanaoushikilia, lazima kila mtu ajijibie mwenyewe swali hili la maana sana, Mimi niko upande gani wa lile suala la Ufalme? Hatuwezi kuepuka kufanya uamuzi juu ya suala hili kubwa linalohusu ulimwengu mzima. Hata tukilipuza, hiyo tu haitaepusha ye yote kati yetu asipatwe na matokeo mabaya yanayolihusu. Hakuna nafasi ya mtu kutokuwamo upande wo wote. Lazima tuwe ama upande wa Ufalme wa Mungu au tuwe tunaupinga.
Wengi sana kati ya watu walio hai leo huenda wakawa hawakuwa hai wakati wa ule mwaka wa 1914, vita ilipotokea. Kwa hiyo hawawezi kukumbuka mfululizo wa matukio yenye maana kubwa ya tangu wakati huo maana hawakuyaona kwa macho yao wenyewe. Hata hivyo, ile “ishara” inayoonyesha “umalizio wa mfumo mambo” iliyotabiriwa na Yesu Kristo imeonekana na ingali inaonekana itazamwe na mataifa na mbari zote za watu. Wote wanahisi matokeo ya “ishara” (NW) hiyo yakiwagusa. Ni jambo rahisi kuelewa. Tukisoma matabiri ya Yesu Kristo kulingana na maandishi yaliyo katika Mathayo, sura 24 na 25, Marko sura ya 13 na Luka sura ya 21, tutajua kwamba alitabiri vita, njaa kali, magonjwa ya kipuku, matetemeko ya ardhi, kuteswa kwa wafuasi wake, dhiki yenye kuzidi kukaza mataifa yenye fadhaa, na mahubiri ya ushujaa ya “habari njema” za Ufalme “katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote” moja kwa moja mpaka mwisho wa huu mfumo wa mambo wenye kuumiza watu kwa machungu mengi.
Bila shaka, wakati wa karne ya kwanza ya Wakati wa Kawaida wetu. Wakristo wa Kweli walihubiri sana katika Asia, Afrika na Ulaya habari njema za Ufalme unaokuja. Hiyo ni zamani kabla ya Wazungu kuvumbua bara za Amerika ya kaskazini na Kusini na Australia na visiwa vingi vya bahari kuu za Atlantiki na Pasifiki, tangu karne ya 15 na kuendelea. Wamisionari wa kidini walitumwa waende kwenye maeneo hayo yaliyokuwa yamevumbuliwa karibuni. Nyakati za karibuni zaidi sosaiti za Biblia zimeanzishwa zikaieneza Biblia kote kote kwa lugha nyingi. Lakini ule ujumbe wa Ufalme haukuwa ukihubiriwa na wamisionari na viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo, hapana. Hawakuhubiri kwamba Ufalme wa Yehova Mungu kupitia Yesu Kristo ungekuwa suala la ulimwenguni pote. Mahubiri yao hayakuwa ya namna inayofanya tangazo juu ya Ufalme liwe sehemu ya ile “ishara” iliyopasa kuonyesha “umalizio wa mfumo wa mambo.”