‘MWANA WA PEKEE’
(Funzo la Kitabu hs 2:23-39)
1. Kwa kuwa ‘Mwana Pekee’ wa Mungu, Yesu Kristo ana cheo gani kati ya viumbe vya Mungu?
YESU KRISTO alijitaja kuwa nani alipokuwa akiongea na mtawala Nikodemo Myahudi? Sikiliza: “Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Alipojitaja kuwa ‘Mwana wa pekee’ wa Mungu alikuwa akijitambulisha kuwa ‘mzaliwa wa kwanza’ wa Mungu. Kuumba vitu moja kwa moja bila kusaidiwa na mtu mwingine ye yote kulianza na kukaisha wakati huyu ‘mzaliwa wa kwanza,’ ‘Mwana wa Pekee’ alipoumbwa. Zaidi ya Yesu kujiita “mwanzo wa kuumba kwa Mungu,” mtume Paulo ampa jina linalofanana na hilo, akisema: “Naye ni mfano wa Mungu asiyeonekana, mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote.” (Kol. 1:15) Kwa hiyo, Mungu alipokwisha kumwumba “mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote,” vitu vyote vilivyofanywa baada ya hapo vilikuwa viumbe vingine. Mungu alimtumia “Mwanawe pekee” kuumba vitu hivyo vingine vyote.
2. Kulingana na Wakolosai 1:15, 16 na Yohana 1:1-3, Mungu aliumba vitu vingine vyote kwa kutumia nani?
2 Mtume Paulo aonyesha wazi hilo amtajapo kwanza “mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote” kisha aendelea kusema: “Kwa kuwa katika yeye vitu vyote viliumbwa, vilivyo mbinguni na vilivyo juu ya nchi, vinavyoonekana na visivyoonekana.” (Kol. 1:16) Sasa twaweza kufahamu maneno ya Yohana katika Yohana 1:1-3: “Hapo mwanzo kulikuwako Neno [Kigiriki, Logos], naye Neno [Logos] alikuwako kwa Mungu, naye Neno [Logos] alikuwa Mungu, Huyo mwanzo alikuwako kwa Mungu. Vyote vilifanyika kwa huyo; wala pasipo yeye hakikufanyika cho chote kilichofanyika.” Katika kitabu cha Mwisho cha Biblia, kilichoandikwa na Yohana pia, yeye atuambia kwamba Yesu Kristo aliyetukuzwa ana cheo “Neno la Mungu,” si Mungu Neno: “Na Jina lake aitwa, Neno [Logos] la Mungu.”—Ufu. 19:13.
3. Ni kwa sababu gani na kwa njia gani Logos alikuwa na “ukuu” kuliko wengine?
3 “Mwanzo wa kuumba kwa Mungu” alipewa heshima na haki za kuwa “mzaliwa wa kwanza,” alikuwa na ukuu kuliko wengine wote ambao wangekuwa ‘wana wa Mungu’ baadaye. (Kol. 1:18) Hiyo ilitia ndani kuombwa na Baba yake wa mbinguni ashirikiane naye kuumba vitu vingine vyote mbinguni na duniani.
4. Kwa sababu gani viumbe vya kiroho walioumbwa kupitia kwa Logos hawaitwi wanawe?
4 Wakati Neno au Logos alipotumiwa kuumba ‘Wana wa Mungu’ wote wasiohesabika, bila shaka roho takatifu ya Mungu Baba yake ilitenda kazi kwa nguvu nyingi juu yake na kupitia kwake. Ilikuwa pamoja naye na ilitenda kazi kwa ajili yake. Bila shaka ilitenda kazi wakati huo kama ilivyofanya baadaye alipopata kuwa mwanadamu asiye na makosa duniani akaponya watu kwa mwujiza. Kwa hiyo alisema alitoa mashetani kwa kutumia roho ya Mungu. (Luka 11:20; Mt. 12:28) Kwa kuwa roho ya Yehova Mungu ilitenda kazi pia kupitia kwa Logos huko juu mbinguni, hao ‘Wana wa Mungu’ walipoumbwa kupitia kwake hawamwoni yeye kuwa Muumba na Baba yao. Hawaitwi wana wa Logos. Wanaitwa “Wana wa Mungu” wa kweli.—Ayubu 1:6; 2:1; 38:7.
5. Wakati wa kuumbwa mwanadamu, ni nani aliyeambiwa na Mungu, “Na tufanye,” na kwa sababu gani Yeye ndiye aliyefaa kusema hayo?
5 Kwa hiyo sasa ni wazi kwamba siku ya sita ya kuumba wakati Mungu aliposema, “Na tufanye mtu kwa mfano wetu, kwa sura yetu,” alikuwa akisema na ‘mzaliwa wake wa kwanza’ “Mwanawe pekee.” (Mwa. 1:26-31) Pengine alimwambia mwana huyu “Na tufanye” alipofikiria kuumba malaika wa mbinguni pia, kutia na makerubi na maserafi. Yehova Mungu Aliye Juu Zaidi na Muumba wa vita vyote Ndiye aliyekuwa na haki ya kuamua kitakachoumbwa. Malaika walipaswa kuwa wana wake. Akitazamiwa kuwa Baba, alitumia mapenzi yake kuamua wakati atakapokuwa na wana zaidi wa kiroho wa mbinguni. Roho yake tu ndiyo nguvu ya utendaji ya pekee ambayo ingeweza kutumiwa kuumba vitu zaidi.
6. Adamu na Hawa walipofukuzwa waliona ‘wana gani wa Mungu’ katika mlango wa bustani, na ni nini kilichoendesha upanga ulioendelea kuzunguka-zunguka humo?
6 Baadaye ‘wana wa Mungu’ makerubi, walionekana katika mlango wa Bustani ya Edeni. Kwa sababu gani? Wanadamu wawili wa kwanza Adamu na Hawa, walimwasi Mungu wakafukuzwa katika makao yao ya Paradiso. Kwa hiyo makerubi waliwekwa katika mlango wa bustani kuwazuia watenda dhambi hao wawili wasirudi na kujaribu kujizuia wasife. (Mwa. 3:24) Adamu na Hawa waliona makerubi waliovaa miili ya kibinadamu. Bila shaka “upanga wa moto uliogeuka huko” katika mlango wa bustani uliendeshwa na roho takatifu ya Mungu, ili kuzuia wanadamu wachafu.
7. Isaya aliona wana wa Mungu wa namna gani katika njozi, na baadaye Ezekieli aliona wa namna gani?
7 Katika karne ya nane K.W.K. nabii Isaya aliona ‘wana wa Mungu’ maserafi, katika njozi. Maserafi hao walikuwa wakimtumikia Yehova Mungu katika hekalu lake. (Isa. 6:1-7) Katika karne iliyofuata, nabii Ezekieli katika Babeli alipewa njozi akaona ‘wana wa Mungu,’ makerubi.— Eze. 1:1-25; 9:3; 10:1-20; 11:22.
8, 9. Ni nini kinachoonyesha kwamba makerubi wanasafiri kasi (haraka) sana Mungu awatumapo, nao ni washiriki wa serikali gani?
8 Makerubi ambao ni “viumbe hai,” bila shaka husafiri kasi (haraka) sana Mungu awatumapo. Kwa hiyo, Mungu alipoombwa msaada, ‘alipanda juu ya kerubi akaruka, naam, aliruka upesi juu ya mabawa ya upepo [ya roho, NW]—.’—Zab. 18:10
9 Bila shaka katika makao ya kiroho miendo mikubwa sana humalizwa baada ya muda mfupi. Umbali haukuzuia Mfalme Hezekia wa Yerusalemu asisaidiwe haraka sana baada ya kwenda hekaluni wakati taifa lilipokabiliwa na hatari. Alisali akasema: “Ee [Yehova] wa majeshi, Mungu wa Israeli, ukaaye juu ya makerubi, wewe, naam, wewe peke yako, ndiwe Mungu wa falme zote za dunia.” (Isa. 37:14-37) Makerubi humtii Yehova Mungu, kama kwamba amewakalia; nao watahusiana na ufalme wake utakaoletea wanadamu wote faraja ya haraka sana wakiwa katika shida iliyo nyingi kupita zote. Maneno ya unabii ya Zaburi yanapatana na baraka hiyo: “[Yehova] ametamalaki, mataifa wanatetemeka; ameketi juu ya makerubi, nchi inatikisika.” (Zaburi 99:1; 80:1 pia.) Cheo bora cha Yehova akilinganishwa na makerubi kilionyeshwa katika sanduku la agano ambalo nabii Musa aliagizwa aunde.—Ebr. 9:5.
10. Cheo cha Yehova kuhusiana na makerubi kilionyeshwaje katika habari ya sanduku la dhahabu lililojengwa na Musa?
10 Sanduku hilo la dhahabu lilitumiwa kuwekea vitu vitakatifu. Lilikuwa na funiko lililopandwa na makerubi wawili wa dhahabu wenye mabawa yaliyotandazwa kufunika kiti cha rehema au upatanisho. Wakati sanduku hilo lilipowekwa katika Patakatifu Zaidi pa hema au hekalu, nuru ya mwujiza (nuru ya shekina) ilitokea juu ya mabawa ya makerubi. (Kut. 25:10-22; 2 Fal. 19:15) Hivyo Yehova alionyeshwa kama akiweka kiti chake cha enzi juu ya makerubi na kuwapa maagizo akiwa hapo. Musa alieleza aliyoona mwenyewe, aandikapo hivi: “Kisha, Musa alipoingia ndani ya hema ya kukutania ili kunena na Mungu ndipo alipoisikia sauti ikinena naye kutoka hapo juu ya kiti cha rehema, kilichokuwa juu ya sanduku la ushahidi, ikitoka kati ya yale makerubi mawili; naye akanena naye.”—Hes. 7:89.
MAHALI PASIPOONEKANA PA UTENDAJI
11. Kwa sababu gani bila shaka mbinguni ni mahali pa utendaji mwingi zaidi kuliko unaoendelea duniani mwote leo?
11 Mbingu si mahali pa kujikalia kitako kwa starehe tu, kama vile kuchukuliwa na wingu lenye kwenda polepole ukiwa umelikalia kwa kuning’iniza miguu yako kando yake. Mtu aliye mtendaji kupita wote katika makao yote ya vilivyo hai, aliye Chanzo kikuu cha nguvu zilizo nyingi sana, hukaa huko! Roho takatifu yake ambayo ni nguvu ya utendaji inaenea katika mbingu zote zisizoonekana. Utendaji wa wanaokaa katika makao hayo na kumtumikia Yehova unapita utendaji wote unoendeshwa katika dunia yetu yote leo. Inakuwa lazima wanaomtumikia Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wote, Yehova Mungu, wasafiri umbali mkubwa sana sana, kuliko kutoka duniani kwenda mwezini. Yako mambo yasiyohesabika yanayopaswa kufanywa, zaidi ya kutunza sayari yetu ndogo sana sana, Dunia. Tusijipofushe tukose kuona utendaji wa mbinguni ati kwa sababu macho yetu dhaifu hayawezi kuuona. Tuna sababu kamili ya kuona kwa jicho la imani.—Ebr. 11:1, 27.
12, 13. Mtunga zaburi Daudi alionyeshaje alitambua malaika wa mbinguni wana uwezo mwingi zaidi, nasi wanadamu twaweza kujifunza somo gani kwao?
12 Kupatana na kusudi la Bwana Mungu, wana wake wa mbinguni wana maisha yenye kazi nyingi sana. Wana uwezo wa kutimiza mambo mengi zaidi kuliko sisi wanadamu. Wao ni watu wa kimungu. Hatuwezi kupima uwezo wao. Kulingana na historia ya Biblia, wamewezeshwa na roho takatifu kufanya mambo ambayo Sayansi haiwezi kufahamu.
13 Daudi alitambua kwamba walikuwa na uwezo wa kimungu alipowafikiria akasema: “Mhimidini [Yehova], enyi malaika zake, ninyi mlio hodari, mtendao neno lake, mkiisikiliza sauti ya neno lake. Mhimidini [Yehova] enyi majeshi yake yote, ninyi watumishi wake mfanyao mapenzi yake.” (Zab. 103:20, 21) Wanapofanya mapenzi ya Yehova, majeshi hayo ya malaika wa mbinguni wanawekea wanadamu wa duniani kielelezo bora cha kufuata. Ikiwa viumbe hao wenye nguvu za kimungu hawajioni kuwa wamestahili sana kumtumikia Muumba wao, basi sisi wanadamu wanyonge, wenye maisha mafupi tuliopo hapa chini, hatupaswi kujiona wala kujivuna hata tumwasi Yehova Mungu, tukijisikia hatuna wajibu wo wote kwake. Ni afadhali zaidi tumhimidi.
14. Roho takatifu inaonekanaje katika mbingu zote, na kwa sababu gani umoja ulioko hautavunjwa?
14 Roho takatifu itokayo kwa Mungu inaonekana katika mbingu zote wakati mwanawe mzaliwa pekee, makerubi wake, maserafi wake na malaika wake wote wanapomtumikia kwa upendo, yeye aliye Mungu mmoja wa kweli aliye hai. Roho yake, inayotiwa ndani ya watakatifu wote hao, inatokeza kati yao ‘umoja wa roho katika kifungo cha amani’ kama Waefeso 4:3 isemavyo. Wote wanashirikiana wakiwa chini ya Mungu Aliye Juu Zaidi, Yehova. Kwa kutumikia kwa umoja katika kazi zao mbalimbali, wanamwabudu yeye hasa. Umoja huo wa kutumikia na kuabudu hautavunjwa kamwe, hata na mashetani.
15. Ni nani anayeongoza wengine mbinguni kumwabudu na kumtumikia Mungu, na katika njozi ya Yohana ya Ufunuo 5:11-14 ilionyeshaje kwamba hilo linathaminiwa?
15 “Mzaliwa wa kwanza” wa Yehova, “Mwanawe pekee,” ndiye anayewaongoza kutumikia Mungu na kumwabudu hivyo bila kuyumba-yumba. Wakati mmoja yeye alikuwa na nia ya kutumikia kama mwana-kondoo wa kutolewa dhabihu hapa duniani. Makundi ya mbinguni yenye uaminifu yanamthamini kwa kujitolea kuwa dhabihu, kama vile sisi Wakristo tunavyomthamini. Ili kuhakikisha hilo, mtume Yohana apewa njozi ya mbinguni inayotimizwa sasa katika karne yetu ya 20.—Ufu. 5:11-14.
16. Kulingana na njozi hiyo, sisi tuna uchaguzi gani wa kufanya, nasi tutapendelewa kupewa roho takatifu tukifanya nini?
16 Namna gani sisi tuliopo duniani sasa, naam, tulio juu ya uso wa dunia tusiofika bado makaburini “chini ya nchi”? Kuna uchaguzi tupaswao kufanya. Je! tutashiriki kuitimiza njozi hiyo ya unabii kwa kujiunga na maelfu ya maelfu ya malaika watakatifu na kumpa heshima astahiliyo Mwana wa Mungu aliye mfano wa Mwana-Kondoo na kumwabudu kwa uchangamfu yeye anayekalia kiti cha ufalme, Yehova Mungu? Tukichagua wenyewe kufanya hivyo, sisi kama makundi yenye utukufu ya mbinguni tutapendelewa kupewa roho takatifu na Mpaji wa kila zawadi bora, Yehova Mungu.—Yak. 1:17.