Maneno Yenye Fadhili Yaweza Kuwa na Matokeo Mazuri
Alipokuwa akitangaza “habari njema” nyumba kwa nyumba, mmoja wa Mashahidi wa Yehova katika El Salvador alizungumza na wasichana wawili wachanga kwa njia ya fadhili. Mama aliporudi nyumbani, binti zake walimwambia habari ya yule mgeni mwenye fadhili pamoja na yale aliyosema. Mama huyo alikuwa mfuasi wa dini ya Evangelical naye aliamini juu ya kuponya kwa imani, kwa kuwa alikuwa akidhani kwamba mwanawe alikuwa ameponywa kupitia kwa sala. Yeye hakuwa amepata kuwasikiliza Mashahidi, lakini aliazimia kwamba angefanya hivyo katika wakati ujao kwa sababu mmoja wao alikuwa amewatendea wasichana wake wachanga kwa fadhili.
Kwa hiyo wakati Shahidi mwingine alipomtembelea, mwanamke huyu alimkaribisha nyumbani kwake na kuuliza maulizo mengi. Hii iliongoza kwenye funzo la Biblia, na upesi baada ya hapo mwanamke huyo akawa akihudhuria mikutano ya Kikristo. Walakini aliendelea vilevile kwenda katika kanisa lake. Ndipo yule mwana wake akawa mgonjwa tena, naye akajiuliza: “Nimpeleke kanisani akaponywe tena, au namna gani?” Alipata kukutana na Shahidi barabarani na kumweleza juu ya tatizo lake. Shahidi huyo alimweleza kwamba haimpasi kuendelea ‘kusita-sita katikati ya mawazo mawili.’ (1 Fal. 18:21) Hakumpeleka mwanawe kanisani akaponywe, walakini alipona. Leo mwanamke huyo ni Mkristo aliyebatizwa. Kweli kweli, maneno yenye fadhili yasemwayo na mtangazaji wa Ufalme kwa watoto wachanga mwishowe yanaleta matokeo mazuri.