Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w79 11/15 kur. 22-24
  • Aitwa “Mwana wa Mungu, Kwa Jinsi ya Roho”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Aitwa “Mwana wa Mungu, Kwa Jinsi ya Roho”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
w79 11/15 kur. 22-24

Aitwa “Mwana wa Mungu, Kwa Jinsi ya Roho”

(Funzo la Kitabu hs 5:39-50)

1. Tofauti na wazo la kawaida la Wayahudi, Maandiko yao ya Kiebrania yalikuwa yametangulia kutangaza nini juu ya mambo ambayo yangempata Masihi?

HUKO nyuma katika siku za Yesu kulikuwako maoni yenye makosa juu ya namna ya mtu ambaye Masihi angekuwa na mwendo uliokuwa umeonyeshwa kwamba angefuata. Wapinzani wa Yesu hawakuona kwamba iliandikwa katika Maandiko ya Kiebrania yao wenyewe kwamba Masihi alipaswa kutaabika kulingana na mapenzi ya Mungu, mpaka kufa. Akiwa ndiye mkuu wa “uzao” wa “mwanamke” wa Mungu, “kisigino” chake kilipaswa ‘kupondwa.’ (Mwa. 3:15) Baada ya unabii mbalimbali wa Kiebrania kutimizwa katika habari hii, mtume Petro alionyesha jambo hili kwa kundi la Wayahudi katika hekalu Yerusalemu: “Mambo yale aliyohubiri Mungu tangu zamani kwa kinywa cha manabii wake wote, ya kwamba Kristo wake atateswa, ameyatimiza hivyo.”​​—⁠Matendo 3:18.

2. Ni maneno gani aliyowaambia mitume wake yanayoonyesha kwamba Yesu alifahamu kwamba Masihi alipaswa kuteswa na kufa?

2 Kutokana na Maandiko ya Kiebrania Yesu alijua kwamba Masihi alipaswa kutaabika na kufa. Ingawa mitume wake walimtambua kuwa ndiye Masihi, aliwashangaza kwa kuwaambia angekufa kifo cha aibu. Wakati mtume Petro alipokataa wazo hilo, Yesu alimwambia: “Nenda nyuma yangu, Shetani; u kikwazo kwangu; maana huyawazi yaliyo ya Mungu, bali ya wanadamu.” Mtangulizi wa Yesu, Yohana Mbatizaji, alitendwa na adui zake mambo waliyotaka kumtenda, naye Yesu alisema, “vivyo hivyo Mwana wa Adamu naye yuaenda kuteswa kwao.”​​—⁠Mt. 16:21-23; 17:12, 13.

3. Kwa sababu ya njia ambayo katika hiyo Kristo alikufa, kundi la wanafunzi wake katika karne ya kwanza W.K. walionwaje?

3 Mwishowe Yesu aliuawa kama mkufuru wa Mungu na mfitini wa Milki ya Rumi. Hilo likawa kwazo kubwa kwa Wayahudi na Mataifa yasiyo ya Kiyahudi, wasikubali Yesu kuwa Masihi aliyeahidiwa. Zaidi ya miaka 25 baadaye, Wayahudi katika Rumi walionyesha nia yao juu ya kundi la wanafunzi wa Yesu kwa kumwambia mtume Paulo mfungwa hivi: “Kwa maana katika habari za madhehebu hiyo imejulikana kwetu kwamba inanenwa vibaya kila mahali.”​​—⁠Matendo 28:22.-

4. Kama inavyoonyeshwa kwa habari ya mtume Paulo, ilikuwa lazima Wakristo wathibitishe nini kutoka kwa Maandiko juu ya Masihi?

4 Kwa hiyo ikawa lazima Wakristo wahakikishe kwamba kufa kwa Yesu juu ya mti wa mateso nje ya Yerusalemu kulihakikisha kwamba alikuwa ndiye Masihi wa kweli, Kristo wa Mungu wa Maandiko Matakatifu. Kwa mfano, tuchukue kisa cha mtume Paulo katika sinagogi katika Thesalonike, Makedonia: “Na Paulo, kama ilivyokuwa desturi yake, akaingia mle walimo, akahojiana nao kwa maneno ya maandiko sabato tatu, akiyafunua na kuwaeleza ya kwamba ilimpasa Kristo kuteswa, na kufufuka katika wafu; na ya kwamba, Yesu huyu ninayewapasha ninyi habari zake ndiye Kristo.” (Matendo 17:1-3) Miaka mingi baadaye, mtume Paulo alisimama akiwa mfungwa mbele ya liwali Mrumi Festo na mfalme mwenye kuzuru Agripa aeleze habari yake. Alipofikia upeo wa kujitetea kwake alisema hivi:

“Basi kwa kuwa nimeupata msaada utokao kwa Mungu nimesimama hata leo hivi nikiwashuhudia wadogo kwa wakubwa, wala sisemi neno ila yale ambayo manabii na Musa waliyasema, kwamba yatakuwa; ya kwamba Kristo hana budi kuteswa na ya kwamba yeye kwanza kwa kufufuliwa katika wafu atatangaza habari za nuru kwa watu wake na kwa watu wa Mataifa.”​​—⁠Matendo 26:22, 23.

5. Paulo alishuhudia mwujiza gani uliofanywa na Mungu ulio mkubwa zaidi ya yote?

5 Paulo alikuwa amekuwa shahidi wa ufufuo huo, kama vile alivyotangaza kwa ujasiri mbele ya Festo na Agripa. (Matendo 26:12-18) Vilevile, katika 1 Wakorintho 15:3-8, Paulo anashuhudia kwamba, kabla ya kugeuka kwake, kulikuwako “ndugu zaidi ya mia tano” waliojionea kwa macho yao ukweli wa kwamba Yesu alikuwa amefufuliwa kutoka kwa wafu. Ufufuo huu wa Yesu Kristo kutoka kwa wafu katika siku ya tatu ya kifo chake ulikuwa ndio mwujiza mkubwa zaidi wa Mungu. Walakini Mungu alikuwa na uwezo mwingi ajabu wa kuufanya. Sababu gani ikawa hivyo? Mtume Petro anaonyesha sababu, anapoandika hivi: “Basi, hata Kristo alikufa mara moja tu kuhusu dhambi, mtu mwenye haki kwa wasio haki, ili apate kuongoza ninyi kwa Mungu, yeye akiuawa katika mwili, lakini akifanywa hai katika roho. Katika hali hii pia alikwenda zake na kuwahubiri roho kifungoni.”​​—⁠-1 Pet. 3:18, 19, NW.

6. Kulingana na maneno ya Petro, Yesu alifanywa kuwa hai akiwa nini?

6 Petro alikuwa na maana gani? Hii: Kwamba Mungu Mwenye Nguvu Zote hakumfufua Yesu kama mtu wa kibinadamu bali alimfufua kama mtu wa roho, mtu wa kiroho asiyepatwa na uharibifu, asiyepatwa na kifo au asiyeweza kufa.

7, 8. (a) Baada ya roho ya Mungu kushuka Juu yake katika Mto Yordani, Yesu alitangazwa kuwa nini? (b) Kwa kufufuliwa kutoka kwa wafu Yesu alitangazwa kuwa Mwana wa Mungu kulingana na nini?

7 Mwili wa Yesu wa nyama ulikuwa umepandwa katika kifo, kama dhabihu ili Mungu aukomeshe. Kwa hiyo Yesu alifufuliwa kwenye uzima wa kimbinguni akiwa na “mwili wa roho,” wenye utukufu, akiwa asiyeweza kupatwa na kifo, asipate kufa tena. (1 Kor. 15:42-54) Mapema, wakati wa siku ya kubatizwa kwake Yesu katika maji, Yehova Mungu alimzaa kupitia kwa roho Yake takatifu ili kuanzia wakati huo awe Mwana wa Mungu wa kiroho mwenye taraja la urithi wa kimbinguni. Akishuhudia kuzaliwa kwa Yesu, Mungu alizungumza kutoka mbinguni, akitangaza kwamba Yesu aliyetiwa mafuta alikuwa mpendwa Wake, Mwana wa kiroho aliyemkubali. (Mt. 3:13-17) Walakini wakati wa siku ya kufufuliwa kwake Yesu kutoka kwa wafu, Mungu alimtangaza kuwa Mwana wa Mungu aliyezaliwa kwa roho kabisa. Ndiyo sababu Paulo anaandika hivi:

8 “Injili ya Mungu; ambayo Mungu amekwisha kuiahidi kwa kinywa cha manabii wake katika maandiko matakatifu; yaani, habari za Mwanawe aliyezaliwa katika ukoo wa Daudi kwa jinsi ya mwili, na kudhihirishwa kwa uweza kuwa Mwana wa Mungu, kwa jinsi ya roho ya utakatifu [jinsi gani?] kwa ufufuo [kutoka kwa] wafu, Yesu Kristo Bwana wetu.”​​—⁠Rum. 1:1-4.

9. Katika Waefeso 1:19-21, Paulo anasema nini juu ya mwujiza wa ajabu wa Mungu katika kumfufua Yesu?

9 Akishuhudia ukuu wa mwujiza wa Yehova katika kumfufua Yesu Kristo kuwa roho asiyeweza kufa, mtume Paulo anaendelea kuandika hivi: “Kwa kadiri ya utendaji wa nguvu za uweza wake; aliotenda katika Kristo alipomfufua katika wafu, akamweka mkono wake wa kuume katika [makao ya kimbinguni]; juu sana kuliko ufalme wote, na mamlaka, na nguvu, na usultani, na kila jina litajwalo, wala si [katika taratibu hii ya mambo] tu, bali katika [i]le [i]jayo pia.” ​—⁠Efe. 1:19-21; Flp. 2:5-11; 1 Pet. 3:21, 22.

10. “Mwanamke” anayemaanishwa katika Mwanzo 3:15 ni nani, na kwa kumfufua Yesu, Mungu aliponya kidonda gani?

10 Kwa kufanya ufufuo huu wa ajabu wa Yesu Kristo, Daktari wa kimbinguni, Yehova, aliponya kidonda ambacho Joka Mkubwa, Shetani Ibilisi, alikuwa amejeruhi “kisigino” cha “uzao” wa “mwanamke” kupitia kwa tengenezo lake ovu la kidunia. (Mwa. 3:15) “Mwanamke” huyu katika siri hii ya Mungu, hakuwa mtenda dhambi Hawa au bikira Myahudi Mariamu, bali tengenezo la Mungu la kimbunguni lililo kama mke ambalo washiriki wake ni viumbe wa kiroho watakatifu. Tengenezo hilo lilimtoa Mwana mzaliwa pekee wa Mungu atumikie hapa duniani kama Masihi aliyeahidiwa.​​—⁠Linganisha Wagalatia 4:25, 26.

11, 12. Aliye Mkuu wa “uzao” wa “mwanamke” wa Mungu yuko katika hali ambayo katika hiyo aweza kufanya nini, nayo ni mambo gani tunayoshangilia ambayo yatakuja kupitia kwake?

11 Aliye Mkuu wa “uzao” wa “mwanamke” wa Mungu sasa yuko katika hali ya kuweza kumjeruhi Joka Mkubwa, Shetani Ibilisi kichwani na kumponda pamoja na “uzao” wake wote. Tuwe sisi ni Wayahudi au watu wa Mataifa, hatuhitaji kutazamia kuja kwa Masihi wa kweli katika mwili duniani yetu. Yeye alikuja na kutimiza sehemu yake duniani katika karne ya kwanza ya Wakati wa Kawaida wetu. (1 Yohana 4:2; 2 Yohana 7) Sasa amethawabishwa kwa utukufu mbinguni. Yeye ni Masihi au Kristo wa kiroho, awezaye kufanya zaidi sana ya Masihi au Kristo wa kidunia.

12 Utukufu wote na umwendee Yehova Mungu, aliyemtia mafuta Mwanawe Yesu ‘kwa roho takatifu na nguvu’ awe Masihi mpendwa! Wote wanashangilia baraka za ajabu za milele ambazo zimeahidiwa kuja kwa wanadamu wote kupitia kwa Masihi wa kiroho aliyetukuzwa, Kristo wa Mungu!​​—⁠Matendo 10:38; Mwa. 22:18.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki