Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w79 12/1 kur. 3-8
  • Ninyi Msienende Tena Kama Waenendavyo Mataifa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ninyi Msienende Tena Kama Waenendavyo Mataifa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MKAZO KUTOKA KWA ULIMWENGU
  • NAMNA MATAIFA WANAVYOENENDA
  • MIOYO ISIYOSIKIA
  • WAMEJITOA KATIKA UFISADI
  • MWUJIZA WA KIADILI
  • WATOTO WA NURU WANATENDA TOFAUTI
  • Jinsi ya Kuchagua Burudani Inayofaa
    “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu”
  • Jinsi ya Kuchagua Burudani
    Jinsi ya Kudumu Katika Upendo wa Mungu
  • Chagua Burudani Inayomfurahisha Yehova
    Furahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
  • Chagua Burudani kwa Hekima
    Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo—2019
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
w79 12/1 kur. 3-8

Ninyi Msienende Tena Kama Waenendavyo Mataifa

“Ninyi msienende tena kama waenendavyo mataifa pia . . . huku akili zao zikiwa zimetiwa giza.”​—⁠Efe. 4:17, 18; NW.

1. Kwa nini habari inayofuata ni ya maana?

Hali ya adili duniani pote inakuwa mbaya kwa haraka sana. Namna za tafrija ambazo, miaka michache iliyopita zingeonekana kuwa zenye kuchukiza sasa zinakubalika sana na watu walio wengi. Uvutano huo unahatarisha hata kundi la Kikristo. Ni jambo gani laweza kufanywa ili kupinga maelekeo hayo? Makala zinazofuata zitatoa majibu yenye maana.

2, 3. (a) Yesu na Paulo walifananisha mwenendo wa Wakristo na nini? (b) Kwa ujumla sifa ya Mashahidi wa Yehova ni nini,’ hata hivyo ni nini kimepata watu wengine mmoja mmoja?

2 “Ninyi ni nuru ya ulimwengu,” akasema Yesu Kristo. Mwenendo wa Mkristo unapaswa kuangaza sana katika ulimwengu wenye giza la kiadili. Paulo aliwaagiza wanafunzi wote “wanaoishi katika ulimwengu mbaya na uliopotoka” waendelee ‘kung’ara . . . kama nyota zinavyoliangaza anga.’ Hata wanafunzi hao wa kwanza, ingawa walishirikiana na Yesu na mitume, bado walikuwa wanadamu wasiokamilika. Iwapo hawakuwa waangalifu wangevutwa na mazingira ya kiadili ya ‘ulimwengu mbaya uliopotoka’ na katika wakati wa kushawishwa wangeacha adili zao za Kikristo. Kwa kweli, wengine walirudia kabisa matendo ya giza.​—⁠Mt. 5:14; Flp. 2:15, HNWW; Flp. 3:18, 19.

3 Vivyo hivyo, pia, wakati wetu mkazo upo wa kutufanya turudie giza la ulimwengu huu. Inasikitisha kwamba, Wakristo, wengine wameshindwa na mkazo huu. Ingawa Mashahidi wa Yehova wanajulikana ulimwenguni pote kwa ajili ya maisha yao manyofu na ya adili, wengine mmoja mmoja wameacha kuenenda kama “watoto wa nuru” na ikawa lazima waondolewe kundini. Mwenendo wao si mfano bora tena. Ni nini laweza kuwa jambo linalotokeza matukio haya yasiyopendeza?​—⁠1 Kor. 5:13; Efe. 5:8.

MKAZO KUTOKA KWA ULIMWENGU

4. Ni jambo gani limepata adili za ulimwengu, na namna za tafrija zenye kupendelewa na wengi zinathibitishaje hili?

4 Kwa wazi mazingira ya adili ulimwenguni pote yamekuwa mabaya zaidi. Wengi katika ulimwengu ‘wamekufa ganzi.’ (Efe. 4:19) Jambo hili ni wazi kutokana na tafrija zinazoenea pote leo. Sababu gani tutaje tafrija peke yake? Kwa sababu twaweza kujifunza mambo mengi juu ya maelekeo ya mtu kutokana na yale anayofanya mtu baada ya saa za kazi wakati ambapo aweza kufanya lo lote atakalo kufanya. Yale anayofanya mtu na wakati wake amalizapo kazi, yanaeleza mengi juu ya vile alivyo hasa. Tukiamua kutokana na namna mbaya za tafrija zenye sifa mbaya zinazopendwa na watu wengi sana leo, ubora wa adili za ulimwengu wa leo umeshuka sana. Lakini kushuka huko kunakuhusuje wewe?

5. Kwa nini ni wakati unaofaa kwetu kufikiria mashauri katika kitabu cha Waefeso?

5 Kumbuka kwamba, sisi si Wakristo wa kwanza kuishi wakati wa kipindi cha adili zilizoshushwa. Masimulizi ya watu ‘waliokufa ganzi’ yalihusu watu fulani walioishi katika mji wa Mashariki ya Kati wa Efeso wakati wa mwanzo-mwanzo wa Ukristo. Barua ya mtume Paulo kwa Wakristo wa Efeso inapaswa kuwa ya maana sana kwetu, kwa kuwa ndani yake anaeleza maana ya kutembea kama “watoto wa nuru.” Shauri lake lafaa kweli kweli katika hizi “siku za mwisho” zenye hatari wakati ambapo wengi wanaojidai kuwa Wakristo ni “wenye kupenda anasa.”​—⁠2 Tim. 3:1-7, 13.

NAMNA MATAIFA WANAVYOENENDA

6, 7. (a) Katika Waefeso 4:17, Wakristo wanasihiwa waache kufanya nini? (b) Watu wa mataifa walikuwa ‘wanaenendaje’ katika kame ya kwanza?

6 Katika Waefeso 4:17 Paulo aliwasihi Wakristo wenzake ‘wasienende tena kama vile mataifa waenendavyo pia katika ubatili wa akili zao.’ Wakati huo watu wa mataifa walikuwa ‘wakienendaje’? Shahidi wa karne ya kwanza aliyeshuhudia kwa macho yake alikubali hivi:

“Watu wanatafuta anasa kutoka kila chanzo. Hakuna uovu unaozuilika; . . Tumelemewa na usahaulifu wa yale yaliyo ya heshima. Mwanadamu . . . sasa anachinjwa kwa ajili ya ucheshi na michezo . . . ni tamasha yenye kuridhisha kuona mwanadamu akiuawa.”a

Pasipo mradi wa kweli katika maisha watu wengi walikazia kupita kiasi kujifurahisha, wakitafuta anasa kutoka chanzo cho chote.

7 Efeso wa kale ulikuwa mahali pazuri kuweza kutimiza tamaa za watu za tafrija. Ulikuwa na jumba kubwa sana la maonyesho lenye viti 25,000 na uwanja wa michezo au uwanja wa mbio za farasi ambao ungeweza kutoa tamasha za kufurahisha tamaa yo yote. Majengo haya yalijengwa na mamlaka ya ulimwengu iliyokuwapo, Rumi, ambayo juu yake mwana-historia mmoja alisema hivi: “Hakika, hali ya adili ya mamlaka hiyo ilikuwa, katika mojawapo ya mambo fulani ya masimulizi yenye kuchukiza sana yaliyopata kuandikwa yanayopatikana katika maandishi.”

MIOYO ISIYOSIKIA

8. (a) Waefeso 4:18 inavuta fikira kwa watu wenye mioyo ya namna gani, na neno la Kigiriki lilimaanisha nini hapo awali? (b) Je! hali hiyo ilitokea ghafula?

8 Paulo aliwasimulia watu hawa kuwa ‘akili zao zimetiwa giza, . . . kwa sababu ya kutosikia kwa mioyo yao.’ (Efe. 4:18; NW) Mioyo yao ilikuwa haiwezi kusikia cho chote. Neno la Kigiriki linalomaanisha “kutosikia” laweza kufuatiliwa mpaka kwenye masimulizi ya jiwe lililokuwa gumu kuliko marmar. Neno hilo lilitumiwa katika utabibu kuhusiana na jiwe la chokaa ambalo pole pole linaweza kufanyika katika viungo vya mwili mpaka vinalemaa visiweze kufanya tendo lo lote. Pole pole mioyo ya hao waliotiwa giza ilifanywa kuwa migumu, isiyosikia, migumu kama vile jiwe. Jambo hili halikutukia mara moja, walakini lilikuwa tendo la pole pole. Namna ya tafrija waliyochagua ilitokeza jambo hili. Namna gani hivyo?

9, 10. Katika karne ya kwanza ni nini iliyokuwa tafrija yenye kupendelewa na wengi, nayo ilikuwa na matokeo gani juu ya watazamaji?

9 Je! wewe wafahamu namna ya tafrija iliyopendelewa sana wakati huo? Michezo ya kupigana, ambayo mtu aliwekwa apigane na mtu au mnyama katika vita vya kupigana mpaka kufa. Wazia tamasha hiyo: Uwanja umejaa maelfu ya watazamaji, wengine wakiwa wameketi chini ya uvuli wa pazia la hariri lenye rangi zenye kuvutia. Muziki mtulivu pamoja na mnuko wa maji yenye manukato yakitiririka kupitia marefu ya uwanja na kutokeza hali nzuri kwa kufunika sauti na harufu za kifo. Kwa ghafula kundi lote la watu lasimama katika wazimu wa kupiga kelele: “Mwue! Mshambulie! Mtoe damu! Mbona anapiga kwa udhaifu sana namna hiyo?” Machinjo yote haya yalifanywa, kama vile mmoja aliyehudhuria michezo hii alivyosema, kwa ajili ya “kufurahisha, kuchesha, na kustarehesha.”

10 Watu ambao wanaweza kutazama mapambo yenye jeuri kama hayo, ambao macho yao yangetazama kwa furaha umwagaji wa damu, waliziona namna nyingine za tafrija kuwa zisizovutia na zisizochangamsha. Kama vile mwana-historia mmoja alivyosimulia kwa ufupi, “iliharibu maono ya kuwa na huruma kwa sababu ya kuteseka ambayo hutofautisha mwanadamu na wanyama.”

11. Kweli au uongo?​—⁠Kwa kuwa michezo ya kupigana kwa panga pamoja na wanyama haipo tena, tafrija za leo haziwezi kutokeza watu wenye ‘mioyo isiyosikia.’ Kwa nini wajibu hivyo?

11 Huenda ukasema, hiyo ni hali isiyoaminika. Walakini je! hali inayolingana na hiyo haipo leo? Ni kweli kwamba, mashindano ya kupigana na wanyama yamekwisha zamani, hata hivyo angalia jambo lililoonwa na mleta habari mmoja:

“Mwue! Mpige nyingine tena! Na ndivyo mwuaji huyo alivyofanya ‘akampiga nyingine.’ Alimpiga risasi. . . . Hao wenye kuamuru uuaji huo​—⁠watu watatu waliokaa nyuma yangu katika jumba la sinema walikuwa, kwa hali zote, waendaji wa sinema wa kawaida.”

Je! lilikuwa jambo lisilo la kawaida? Hata kidogo. Ukweli ni kwamba katika nchi nyingi sinema na vipindi vya television vyenye kupendwa sana na watu wengi mara nyingi ni zile zinazoonyesha jeuri. Tafrija za namna hiyo zimesaidia sana kutokeza watu wasio na huruma, ambao “wameacha kuona uchungu,” au kuchomwa ko kote na dhamiri.​—⁠Efe. 4:19, Tafsiri ya Kingdom Interlinear.

WAMEJITOA KATIKA UFISADI

12. (a) Waefeso 4:19 inatoa maelezo gani ya ziada juu ya namna watu wa mataifa walivyokuwa wakienenda? (b) “Mwenendo mpotovu” unamaanisha nini, na je! tafrija ya wakati huo iliuonyesha?

12 Mtume Paulo anaongeza kwamba watu wa mataifa si kwamba tu walikuwa ‘na mioyo migumu,’ bali pia “[walijitia] katika mambo ya ufisadi wapate kufanyiza kila namna ya’ uchafu kwa kutamani.” (Efe. 4:19) Vilevile alizungumza juu ya “uasherati” na mambo yaliyo ya “aibu hata kuyanena.” (Efe. 5:3, 12) Katika karne ya kwanza, tafrija ndiyo tena iliyotokeza mazoea haya, wakati huu ikiwa jukwaani au majumbani ya michezo. Ni mambo gani ambayo yangeweza kutazamwa?

‘Waliyoona waume waliodanganywa, uzinzi na mapenzi ya siri ndiyo yaliyokuwa mambo ya kawaida. Wema ulifanyiwa mzaha, . . . kila kitu kilichokuwa kitakatifu na kilichostahili kuheshimiwa kiliingizwa kwenye mambo hayo machafu. Katika uchafu, . . . katika mazungumzo na maonyesho mabaya yaliyohalifu hali ya kuona aibu, tamasha hizi zilizidi yote. Wacheza ngoma za kuigiza hadithi walivua mavazi yao na kucheza wakiwa nusu uchi, na hata wakiwa uchi kabisa, jukwaani. Ujuzi haukuonwa kuwa kitu, kila kitu kilikusudiwa kutosheleza tamaa za mwili.’​—⁠The Conflict of Christianity with Seathenism, cha Gerhard Uhlhorn, uku. 120.

Lo! namna inavyochukiza! Kwa ufupi huu ndio “mwenendo mpotovu,” kwa kuwa neno la awali la Kigiriki linatoa wazo la kuwa tayari kwa anasa yo yote. Ni kukosa kuona aibu pamoja na kutojali yale ambayo wengine wanasema au kufikiri.

13. Je! “mwenendo mpotovu” kama huo unaonekana waziwazi katika nyingine za tafrija za leo?

13 Je! kuna tofauti yo yote leo? Uasherati umejaa sana katika mambo yanayo tolewa na njia za mawasiliano za kutolea tafrija. Katika nchi fulani, sinema za uasherati wa kila namna zimeonyeshwa hata katika television, kwa njia hiyo zikafika mpaka katika nyumba. Je! wasikilizaji wanaitikia? Katika Italia, wakati sinema ya uasherati ilipokuwa ikionyeshwa katika television, “mji wote ulikaa kimya kabisa wakati maonyesho haya yalipokuwa yakiendelea.”

14, 15. (a) “Tamaa” (Efe. 4:19) inamaanisha nini, na je! namna za tafrija leo zinatokeza watu wa namna hiyo? (b) Je! Wakristo waliojiweka wakf wanaweza kupatwa na matokeo mabaya ya kutazama kama tafrija mambo yanayoonyesha uasherati?

14 Akieleza maana ya sinema nyingi na maoni ya watu, mwandikaji mmoja alisema hivi:

‘Katika nyingi za sinema mpya, tamasha za watu wakifanya ngono wakiwa uchi​—⁠ngono za waume na wake, za watu wa jamaa moja, au wanaume kwa wanaume au wanawake kwa wanawake​—⁠​ndizo nyingi, . . . ’ Yeye alimalizia hivi, ‘Kwa ufupi, tumefikia hali katika jamii yetu wakati ambapo jambo lo lote lakubalika, mahali ambapo yote yaruhusiwa, na mahali ambapo hakuna vizuizi vinavyowekwa juu ya tamaa za mtu mmoja mmoja, katika kutosheleza tamaa na mawazo yake.’

15 Watu hao, wako tu, kama vile mtume Paulo anavyowaeleza kuwa, watu ‘wanaofanya uchafu wa kila namna kwa kutamani.’ Ndiyo, “kutamani” (“kuwa na zaidi,” Tafsiri ya Kingdom Interlinear), kutamani sana kutosheleza tamaa ya mtu kwa mambo yasiyofaa na kutosheleza maono ya moyoni ya mtu hata ilete hasara ya adili namna gani. (Efe. 4:19) Je! kutazama mambo hayo maovu kusingekuwa na matokeo mabaya juu ya kufikiri kwa Mkristo? Mmoja ambaye alitazama sinema kadha za namna hii alikubali hivi:

‘Huwezi kusahau tamasha hizo, [zinazoonyesha uasherati] kadiri unavyozidi kuzifikiria ndivyo unavyojipata ukitaka kufanya yale uliyoona. . . . Sinema hizo, zinakufanya ufikiri kweli kweli kwamba unakosa jambo fulani.’ Mwingine aliongeza hivi: ‘Unaanza kuwaza na kutaka kujua namna ambavyo ingekuwa.’

Huenda kila mtu asione hivi, walakini hatari iko. Akili zetu zinaweza kuongozwa katika njia zenye hila.

MWUJIZA WA KIADILI

16. Kulingana na Waefeso 1:6-8, Wakristo walikuwa wamepata baraka nyingi gani, na hii ilikuwa na matokeo gani juu ya maisha yao?

16 Namna hiyo ilivyo tofauti na mwendo wa wale waliokuwa katika kame ya kwanza ambao walimfuata Kristo kweli kweli! Wakati mmoja hawa walikuwa wameenenda chini ya uongozi wa taratibu hiyo na “mtawala” wake, Shetani, na hali yao ilikuwa ya kufanya “mambo yale yaliyoipendeza miili.” Walakini walibadilika. Kweli za Kikristo zilizoinuliwa zilifungua maoni mapya juu ya maisha. Wazia hili, Mungu alikuwa na nia ya kumtoa dhabihu Mwana wake mwenyewe, “mpendwa” wake, ili kwamba waweze kusamehewa deni yao kubwa ya dhambi! Lo! namna ilivyokuwa bei kubwa! Lo! namna zilivyokuwa rehema na fadhili zisizostahilika! “Hizi [fadhili zisizostahilika] yeye [Mungu] alizifanya ziwe nyingi sana kwetu katika hekima na ufahamu mzuri wote,” kasema mtume Paulo. Kwa hiyo si kwamba tu walikuwa na maarifa ya kweli, bali vilevile walipewa “ufahamu mzuri” huo ili waweze kupambana kwa kufaulu na matatizo ya kila siku.​—⁠Efe. 1:6-8, NW; 2:1-5, HNWW.

17. (a) Kuna ushuhuda gani kwamba Ukristo ulikuwa dini yenye uwezo? (b) Nguvu zake za adili zilionyeshwaje?

17 Yao ilikuwa dini ya uwezo. Roho ya Mungu ilikuwa imemfufua Yesu kutoka kwa wafu akakwezwa kwenye cheo cha juu zaidi sana kuliko mamlaka zote za ulimwengu. Sasa ‘uwezo uu huu uko na waamini wale.’ (Efe. 1:19-21) Lo! namna ulivyotokeza matokeo katika maisha za waamini hao! Kwa kulifikiria jambo hili la adili twaweza kuthamini uwezo wa Wakristo wa karne ya kwanza. Ulimwengu wa kale uliona uasherati kuwa jambo la kawaida. Cicero, mwandikaji wa zamani wa Rumi, hata alisihi hivi:

“Iwapo kuna mtu ye yote ambaye anafikiri kwamba wanaume vijana wanapaswa kukatazwa kabisa mapenzi ya makahaba [malaya], hakika yeye ni mkali sana. . . . Kwa kweli ni wakati gani hili halikufanywa? Ni wakati gani mtu alipopata kosa lo lote katika jambo hili?”

Hata hivyo “watoto wa nuru” walijiondoa wakawa huru na wakaendelea kuwa huru kutokana na mazoea hayo. Kulikuwa hakuna cho chote katika historia yote cha kulinganishwa na mwujiza wa kiadili uliofanywa na Ukristo.

WATOTO WA NURU WANATENDA TOFAUTI

18. Wanafunzi wa kwanza wangeonyesha kuthamini kwao kwamba walikuwa “watu watakatifu” kwa kufuata mwendo gani?

18 Wanafunzi hawa walikuwa na kanuni ya juu ya kufikia. Hivyo, Paulo alishauri hivi: “Lakini uasherati usitajwe kwenu kamwe, wala uchafu wo wote . . . kama iwastahilivyo watakatifu.” (Efe. 5:3) Si kujizuia tu kutofanya mambo hayo, bali pia kuepuka kuyazungumza kwa sababu ya kupata furaha ya mwili. Lo! namna kufikiri kwake kulivyotofautiana sana na wengine leo ambao huona kwamba, ‘mradi hufanyi uasherati wenyewe, hakuna jambo lo lote baya kuutazama na kuuzungumza kama njia ya kupata tafrija.’!

19. Waandikaji Wakristo wa karne za pili na tatu walionaje juu ya (a) ‘kukosa adabu kwa jumba la michezo na matendo ya kinyama ya uwanja wa kupigania’? (b) Kuona “mtu akiuawa”? (c) Kile kinachoweza ‘kumwasha mtu kwa tamaa au nyege’? (d) Twaweza kujifunzaje kufanya mambo mabaya?

19 Wakristo hao wa kwanza walionaje juu ya michezo ya kupigana kwa panga au na wanyama mpaka kufa pamoja na jumba la michezo, ambavyo ndivyo vitu vilivyokuwapo kama namna ya tafrija? Ebu angalia maelezo haya ya waandikaji waliojidai kuwa Wakristo ambao waliishi wakati wa karne za pili na tatu:

“Sisi [Wakristo] hatujishughulishi, katika kusema, kuona au kusikia, na wazimu wa sarakasi, kukosa adabu kwa jumba la michezo, [matendo ya] kinyama ya uwanja wa mapigano . . . Sababu gani tuwaudhi, iwapo [twaona kwamba kuna] mapendezi mengine?”​—⁠Tertullian.

“Sisi, tukiwa na maoni kwamba kuona mtu akiuawa ni sawa kabisa na kumwua, tumekana kwa kiapo tamasha kama hizo [michezo ya kupigana na wanyama].”​—⁠Athenagoras.

“Uvutano wenye kuharibu wa jukwaani ungali unachafua sana. Kwa maana kichwa cha sinema za ucheshi ni kuvunjia heshima mabikira, au mapenzi ya malaya; . . . Vijana au mabikira wanaweza kufanya nini, wanapoona kwamba mambo haya yanafanywa bila haya, na kutazamwa na wote? Kwa wazi wanaonywa juu ya wanayopaswa kufanya, na wanawashwa na tamaa, ambayo hasa huamshwa kwa kuona.”​—⁠Lactantius. [Ni sisi tumelaza maneno,]

“Je! Mkristo mwaminifu anafanya nini katikati ya mambo haya, kwa kuwa huenda hata asifikiri juu ya uovu? Kwa nini anapata furaha katika maonyesho ya tamaa . . . ? Anajifunza kufanya, huku akizoea kutazama. . . . Upesi tunazoea yale tunayosikia na kuyaona.”​—⁠Cyprian.

20. (a) Ni kwa nini Wakristo wa kwanza waliepuka tafrija zilizoshushwa? (b) Ni kwa nini mwenendo wao ulionekana kuwa tofauti?

20 Ingawa watu hawa waliishi miaka fulani baada ya Wakristo wa karne ya kwanza, twaweza kuona namna walivyofahamu msimamo wa Mkristo katika mambo haya. Waliepuka mambo hayo ya kujifurahisha yaliyoshushwa. Waliweza kuona namna isivyopatana kwa wale waliokuwa wamekwezwa kutoka gizani, ambao walikuwa wameondoa usemi mchafu, jeuri na uasherati kutoka kwa maisha yao, kuketi makusudi na kutazama mambo hayo kama tafrija. Kwa sehemu kubwa Wakristo hao walitii shauri la Paulo ‘mwache kushirikiana nao katika matendo yasiyozaa ya giza, na hata kuwakaripia.’ Maisha yao ya kila siku yaliyo safi katikati ya ulimwengu uliopotoka yalikuwa ‘karipio’ wakati wote kwa watu wa mataifa. Si ajabu kwamba walisemekana na ulimwengu usiomcha Mungu kuwa “adui wa jamii ya kibinadamu.” Wanafunzi hao walionyesha kwa furaha kwamba walikuwa chini ya uongozi mzuri zaidi kuliko jirani zao wenye kufikiria mambo ya kimwili. Walionyesha kwamba walikuwa ‘wamefanywa wapya katika uwezo unaoongoza akili zao.’ Na namna ulivyokuwa ‘uwezo’ tofauti! Wengine wasingeweza kujizuia wasione hili. Je! sisi hatutaki kuwa watu wa namna hiyo? Hata dai letu liwe nini, ama tutaonyesha “tunda la nuru” au tutaenenda kama waenendavyo mataifa.​—⁠Efe. 4:23; 5:9, 11.

21. Ni kwa sababu gani sisi leo twapaswa kuwa na maoni ya kweli juu ya namna ya tafrija tunayochagua’

21 Namna gani basi, juu ya namna ya tafrija tunayochagua leo? Wakati sisi au watoto wetu tunapofungua television zetu au kwenda sinema, ni mambo gani tunayotazama? Je! kuna tofauti ya kweli kati ya yale tunayochagua kutazama na ‘kukosa adabu kwa jumba la michezo la Rumi na matendo ya kinyama ya uwanja wa kupigana’? Mambo ya hakika yanaeleza namna Wakristo wengine walivyokosa kuwa waangalifu na kunaswa na uasherati kwa sababu ya kuzoea kuutazama.

22. (a) Je! ilikuwa rahisi kwa Wakristo wa karne ya kwanza kuenenda kama watoto wa nuru, hata hivyo waliweza kufanya nini? (b) Ni maulizo gani zaidi yanayohitaji kujibiwa?

22 Tofauti na hayo, lo! namna Wakristo hao wa kwanza walivyoonyesha nguvu za adili! Ingawa walikuwa wakiishi katika ulimwengu ambao mioyo ya wanadamu ilikuwa imefanywa kuwa migumu wasitambue kwamba walikuwa wakifanya dhambi nako kuona haya ko kote na kuwa na adabu kulikuwa kumesahaulika, walifaulu kuweka akili zao zikiwa zimekazwa juu ya mambo yaliyokuwa ya ‘kweli, staha, haki, safi, kupendeza, sifa njema, wema na sifa nzuri.’ (Flp. 4:8) Waliendelezaje uwezo huo katikati ya mazingira yenye uasherati? Kumbuka, walikuwa watu wa nyama na damu kama sisi leo. Walikuwa na uhitaji mkubwa wa tafrija. ‘Anasa nyingine’ zao zilikuwa nini? Twawezaje kuiga sana sana mifano bora kama ya “watoto wa nuru”? Haya ni maulizo ya maana ya kuzungumza katika makala inayofuata.

[Maelezo ya Chini]

a Lucius Seneca (4 K.W.K.​—⁠65 W.K.) Barua ya 95, #33.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki