Maswali Kutoka Kwa Wasomaji
● Je! maneno ya Yesu katika Mathayo 18:18-20 yanapasa yafahamike yanamaanisha kwamba mbingu zimefungwa na wajibu wa lazima wa kufuata maamuzi yanayofanywa na wanadamu duniani?
Mistari hiyo inasema hivi (NW): “Kwa kweli mimi nasema kwenu ninyi wanaume, Mambo yawayo yote ambayo huenda ninyi mkafunga juu ya dunia yatakuwa mambo yaliyofungwa katika mbingu, na mambo yawayo yote ambayo huenda ninyi mkalegeza juu ya dunia yatakuwa mambo yaliyolegezwa katika mbingu. Tena mimi kwa kweli nasema kwenu ninyi, Ikiwa wawili wa ninyi juu ya dunia wanakubaliana kuhusu jambo lo lote la maana ambalo wanapaswa kuomba, litatukia kwa hao kwa sababu ya Baba yangu katika mbingu. Kwa maana mahali palipo wawili au watatu wamekusanyika pamoja katika jina langu, hapo mimi nipo katikati yao.”
Kama Tafsiri ya New World (iliyoonyeshwa hapa) na tafsiri nyingine zionyeshavyo, mambo ‘yanayofungwa’ au ‘kulegezwa’ juu ya dunia ni mambo ambayo tayari yamekwisha ‘kufungwa’ au ‘kulegezwa’ katika mbingu. Maneno ya Kigiriki yaliyotumiwa hapa yanamaanisha kwa uhalisi ‘kuwa imekwisha kufungwa’ au ‘kuwa imekwisha kulegezwa,’ nayo yanaonyesha hali ya tendo lililokwisha kutimizwa na mtu mwingine. Ndiyo kusema, hali ya wakati wenyewe inadokeza kwamba tendo lenyewe lilikuwa limekwisha kuamuliwa katika mbingu na kwamba sasa linaonekana tu katika uamuzi unaofanywa baadaye juu ya dunia na wale wanaotaka kuonyesha “hekima itokayo juu.” (Yak. 3:17, 18) ‘Kufungwa’ kungemaanisha kupatikana na hatia ya kuadhibiwa; ‘kulegezwa’ kungemaanisha kupatikana bila hatia.
Maneno hayo ya Yesu yanafuata mazungumzo yake juu ya utaratibu unaopasa kufuatwa ikiwa mtumishi wa Mungu ana “kosa” kubwa la kutatua pamoja na ndugu yake. (Mistari 15-17) Huenda jambo hilo likafikia hatua ya shtaka kushughulikiwa na “kanisa” (kundi) katika maana ya kwamba lingeletwa mbele ya ndugu wenye madaraka katika kundi walichunguze na kutoa uamuzi. Kama shtaka lenyewe lingehakikishwa kuwa kweli na zito kiasi cha kutosha, na mtu yule asionyeshe toba, mtu huyo angechukuliwa kuwa “mtu wa mataifa na mtoza ushuru.” (UV) Angetengwa na ushirika. Bila shaka, haya yote yangehitaji mazungumzo mengi yenye uchunguzi wa kutosha. Mazungumzo hayo ndiyo Yesu alikuwa akitaja katika mistari 18 mpaka 20.
Kwa kuwa roho takatifu ingewajia wanafunzi wa Yesu kupita kwa Yesu kuanzia na baada ya Pentekoste 33 W.K., ingeweza kusemwa kwamba “mahali palipo wawili au watatu wamekusanyika pamoja katika jina langu [Yesu], hapo mimi nipo katikati yao.” Wote waliokusanyika kulichunguza jambo hilo wangehitaji kuwa macho kuona wanavyoelekezwa na vielekezo vya roho ya Yehova. Hasa wangehitaji kupima mambo kwa uangalifu kwa msaada wa Neno lake, kutia na maagizo na mafundisho ya Yesu, waone akili ya Yehova ingeuonaje mwenendo unaosemwa ulifuatwa na hatua inayopasa kuchukuliwa ikiwa ushuhuda unahakikisha shtaka ni la kweli na mtu huyo hatubu. Bila shaka, wale wenye kupima mambo bila upendeleo huenda wakapata kwamba mshtakiwa hana ‘hatia, au huenda ushuhuda ukawa hautoshi.
Katika karne ya kwanza, Wakristo walikuwa na utendaji wa kimwujiza wa roho takatifu ya Yehova katika mambo fulani ya uamuzi, kama vile katika uamuzi wa Anania na Safira. (Matendo 5:1-11; 1 Kor. 12:4-11) Baada ya zawadi za kimwujiza kukoma mitume walipokufa, Wakristo hawajatazamia vionyesho vya kimwujiza moja kwa moja kutoka mbinguni kuwaonyesha jinsi jambo linavyopasa kuamuliwa. (1 Kor. 13:8-13) Hata hivyo, bado tuna habari ambazo Neno la Yehova linasema juu ya mwenendo unaofaa na jinsi mambo yanavyopasa kuamuliwa. Kwa sababu hiyo, tunaweza kujua yale ambayo tayari yamekwisha kuamuliwa katika mbingu juu ya jambo fulani. Tutakubali kwamba, kwa sababu ya makosa ya kutokamilika kwa kibinadamu, nyakati nyingine makosa hufanywa katika uamuzi, lakini jambo hilo linazidi tu kuukazia uhitaji wa kushikilia sana maagizo yaliyo katika Neno la Yehova wakati wa kushughulikia mambo ili tuwe na uhakikisho wa kwamba jambo linaloamuliwa ndilo lile ambalo tayari limekwisha kuamuliwa katika mbingu.