Sura 63
Mashauri Zaidi Yenye Kusahihisha
YESU na mitume wake wakiwa wangali katika ile nyumba katika Kapernaumu, jambo fulani zaidi ya yale mabishano ya mitume juu ya ni nani aliye mkubwa kuliko wote linazungumzwa. Hiki ni kisa ambacho huenda pia kikawa kilitukia waliporudi Kapernaumu, wakati Yesu alipokuwa hayupo binafsi. Mtume Yohana anaripoti hivi: “Sisi tuliona mwanamume fulani akifukuza roho waovu kwa kutumia jina lako nasi tukajaribu kumzuia, kwa sababu yeye hakuwa akiandamana nasi.”
Kwa uwazi Yohana anaona wale mitume kuwa ni kikoa cha waponyaji, chenye kushikilia cheo hicho, ambamo mtu mwingine yeyote hapaswi kuingia. Kwa hiyo yeye anahisi kwamba mwanamume huyo alikuwa akifanya kazi za nguvu nyingi kwa njia isiyofaa kwa sababu yeye hakuwa sehemu ya kikundi chao.
Hata hivyo, Yesu anashauri hivi: “Msijaribu kumzuia, kwa maana hakuna mtu ambaye anafanya kazi za nguvu juu ya msingi wa jina langu ambaye ataweza kunitukana vyepesi; kwa maana yeye ambaye hayupo dhidi yetu yuko kwa ajili yetu. Kwa maana yeyote ambaye anawapa nyinyi kikombe cha maji kunywa juu ya msingi wa kwamba nyinyi ni wa Kristo, mimi nawaambia kikweli, yeye hatapoteza thawabu yake kwa vyovyote.”
Haikuhitajiwa kabisa mwanamume huyo afuate Yesu kwa uhalisi ndipo awe upande wake. Kundi la Kikristo lilikuwa halijaanzishwa bado, kwa hiyo kutokuwa kwake sehemu ya kikundi chao hakukumanisha kwamba yeye alikuwa wa kikundi tofauti. Kwa kweli mwanamume yule alikuwa na imani katika jina la Yesu na hivyo alifaulu kufukuza roho waovu. Yeye alikuwa anafanya jambo fulani ambalo lililingana kwa kufaa na lile ambalo Yesu alisema lilistahili thawabu. Yesu aonyesha kwamba kwa kufanya hivyo, huyo hatapoteza thawabu yake.
Lakini namna gani ikiwa mwanamume yule alikwazwa na maneno na vitendo vya wale mitume? Jambo hilo lingekuwa zito sana! Yesu alionelea hivi: “Yeyote yule ambaye anakwaza mmoja wa wadogo hawa ambao wananiamini, ingekuwa vizuri zaidi kwake kama jiwe la kusagia kama lile linalozungushwa na punda lingewekwa kuzunguka shingo yake na kwa kweli yeye atupwe ndani ya bahari.”
Yesu anasema kwamba wafuasi wake wanapaswa kuondoa kutoka maisha zao kitu chchote kilicho kipendwa kwao kama mkono, mguu, au jicho ambacho huenda kikasababisha wakwazike. Ni vizuri zaidi kuwa bila kitu hicho chenye kuthaminiwa sana na kuingia katika Ufalme wa Mungu kuliko kukishikilia na kutupwa ndani ya Gehena (rundo la takataka zenye kuchomeka karibu na Yerusalemu), ambayo inafananisha uharibifu wa milele.
Pia Yesu aonya hivi: “Hakikisheni kwamba nyinyi wanaume hamdharau mmoja wa wadogo hawa; kwa maana mimi nawaambia nyinyi kwamba malaika zao mbinguni sikuzote wanaangalia uso wa Baba yangu ambaye yumo mbinguni.” Ndipo yeye anapotoa kielezi cha thamani kubwa ya “wadogo” kwa kueleza juu ya mwanamume mmoja ambaye ana kondoo mia moja lakini anampoteza mmoja. Mwanamume yule ataacha wale 99 akatafute yule mmoja aliyepotea, Yesu anaeleza, na anapompata atafurahi sana juu yake kuliko juu ya wale 99. “Vivyo hivyo,” Yesu anamalizia, “si jambo la kutamanika kwa Baba yangu ambaye yumo mbinguni kwa mmoja wa wadogo hawa apotee.”
Inawezekana ni kwa sababu ya kufikiria mabishano yaliyokuwa miongoni mwa mitume wake kwamba Yesu anahimiza hivi: “Mwe na chumvi ndani yenu wenyewe, na mwendeleze amani kati ya mmoja na mwingine.” Vyakula ambavyo havina ladha vinafanywa vipendeze katika kaakaa la kinywa kwa kutumia chumvi. Hivyo, chumvi ya mfano inafanya mambo ambayo mtu anasema yawe rahisi zaidi kukubalika. Kuwa na chumvi kama hiyo kutasaidia kuhifadhi amani.
Lakini kwa sababu ya kutokamilika kwa kibinadamu, nyakati nyingine magomvi mazito yatatukia. Yesu anaandaa pia miongozo ya kuyashughulikia. “Ikiwa ndugu yako anafanya dhambi,” Yesu anasema, “nenda ukafunue kosa lake kati yako naye peke yenu. Ikiwa anakusikiliza, umempata ndugu yako.” Ikiwa yeye hasikilizi, Yesu anashauri, “chukua pamoja nawe mtu mmoja au wawili zaidi, ili kwa kinywa cha mashahidi wawili au watatu kila shauri lipate kuthibitika.”
Kama hatua ya mwisho tu inayoweza kuchukuliwa, Yesu anasema, peleka shauri lile kwa “kundi,” yaani, kwa waangalizi wa kundi wenye madaraka ambao wanaweza kutoa uamuzi wa kihukumu. Ikiwa mtenda dhambi yule hatafuata uamuzi wao, Yesu anamalizia, “mwache awe kwako kama mtu wa mataifa na kama mtoza kodi.”
Katika kufanya uamuzi kama huo, waangalizi wanahitaji kufuata kwa ukaribu maagizo yaliyo katika Neno la Yehova. Hivyo, wakati wanapopata mtu akiwa na hatia na anastahili adhabu, hukumu ile tayari ‘itakuwa imefungwa mbinguni.’ Na wakati wao ‘wanapolegeza duniani,’ yaani, kupata mmoja akiwa bila hatia, hiyo tayari itakuwa ‘imelegezwa mbinguni.’ Katika mazungumzo kama hayo ya kuchunguza sana mambo ya hukumu, Yesu anasema, “mahali ambapo pana wawili au watatu ambao wamekusanyika pamoja kwa jina langu, hapo mimi nipo katikati yao.” Mathayo 18:6-20; Marko 9:38-50; Luka 9:49, 50, NW.
▪ Kwa nini haikuhitajiwa kabisa katika siku za Yesu kuandamana naye?
▪ Shauri la kukwaza mmoja aliye mdogo ni zito kadiri gani, na Yesu anatoaje kielezi cha umaana wa wadogo kama hao?
▪ Ni jambo gani ambalo labda lasukuma Yesu atoe kitia-moyo kwa mitume wawe na chumvi miongoni mwao wenyewe?
▪ Kuna umaana gani katika ‘kufunga’ na ‘kulegeza?’