Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w85 12/15 kur. 26-30
  • “Ninyi Ni Chumvi ya Dunia”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Ninyi Ni Chumvi ya Dunia”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • ‘Kukolezwa Chumvi’
  • “Mwe na Chumvi Ndani Yenu”
  • “Chumvi ya Dunia”
  • Chumvi Inahifadhi Kusiwe Kuharibika
  • Udumifu na Ushikamanifu
  • Chumvi Ni Bidhaa Muhimu
    Amkeni!—2002
  • “Imetokana na Wazazi Safi Zaidi”
    Amkeni!—2006
  • Kuzoa Chumvi Baharini kwa Kutumia Jua na Upepo
    Amkeni!—2003
  • Donge la Chumvi
    Amkeni!—2005
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
w85 12/15 kur. 26-30

“Ninyi Ni Chumvi ya Dunia”

“Ninyi ni chumvi ya dunia; lakini chumvi ikiwa imeharibika itatiwa nini hata ikolee?”​—MATHAYO 5:13

1. Chumvi ya kawaida ni nini?

CHUMVI ni kitu cha kustaajabisha. Ni mchanganyiko wa sodiamu, namna ya madini isiyo ya kawaida, na klorini, gesi yenye sumu. Uhakika wa kwamba sehemu hizo mbili hatari zinaweza kuungana zitengeneze kitu chenye faida ni uandalizi mzuri ajabu uliofanywa na Muumba ili kufaidi wanadamu.​—Zaburi 104:24.

2. Inaweza kuonyeshwaje kwamba chumvi inazuia kuoza na inaweza kuwa kitu cha kuhifadhia?

2 Jambo moja ni kwamba, chumvi ina nguvu nyingi za kuzuia kuoza. Kwa mfano: Mwanamume fulani aliweka ngozi mbili za kondoo waliochinjwa ndani ya mahali pa kuwekea mizigo pa motokaa, akafunga safari ndefu katika joto jingi la Afrika. Mwishowe alipofungua mahali pa kuwekea mizigo, palikuwa na harufu mbaya na ngozi hizo zilikuwa zimejawa na funza! Hata hivyo, ngozi hizo zenye manyoya zilisafishwa, na kusuguliwa kabisa kwa chumvi. Matokeo yalikuwa nini? Zikawa mazulia mororo ya kuwekwa kando ya vitanda yaliyotumiwa miaka mingi.

3. Ni nini kinachoweza kusemwa juu ya thamani ya chumvi na kupatikana kwayo?

3 Basi, ni wazi kwamba chumvi ni kitu chenye thamani cha kuhifadhia vitu. Pia ina faida nyingine. Kwa kweli, katika China ya kale ndiyo iliyokuwa ya pili kwa dhahabu katika thamani. Neno la Kilatini la “chumvi” ni sal, na katika siku za milki ya Roma, askari-jeshi walilipwa sehemu ya mshahara (salarium) kwa kupewa chumvi. Bila shaka, katika sehemu nyingi leo, chumvi ni kitu cha kawaida na haina bei kubwa. Bahari zina chumvi ambayo kiasi chayo ni maili milioni 4 1/2 za marefu sita​—chumvi ya kutosha kuweza kufunika United States yote kwa kina cha kilometa 1.6! Hata Yesu Kristo alipokuwa duniani, chumvi ilikuwako kwa wingi. Kwa mfano, maji ya Bahari ya Chumvi yalitoa chumvi nyingi, na kulikuwako vilima vyenye kutoa chumvi karibu na mahali ambako mke wa Lutu aligeuka akawa “nguzo ya chumvi.”​—Mwanzo 19:26.

4. Ni kwa sababu gani tunaweza kusema kwamba chumvi ina umaana kuhusiana na uhai?

4 Chumvi ni dawa pia. Miili yetu ina wakia nane za chumvi, ambazo kama zingekosekana tungekufa. Kwa hiyo chumvi ni ya lazima ili kuwa hai. Lakini kama inavyotumiwa katika Biblia, chumvi pia ina umaana wa mfano unaohusiana na maisha na utendaji wa Mkristo.

‘Kukolezwa Chumvi’

5. Kwa habari ya chakula, chumvi inatumikia kusudi gani?

5 Mpishi anaposahau kutumia chumvi anapopika chakula fulani, chakula hicho huenda kikakosa ladha hata watu wakakataa kukila. Ni kama Ayubu alivyosema: “Je! kitu kisicho na ladha humkini kulika pasipo chumvi?” (Ayubu 6:1, 6) Chumvi inaongeza mwonjo wa chakula. Faida hiyo ya chumvi na kufaa kwayo kama kitu cha kuhifadhia zinatumiwa katika Maandiko kwa njia ya mfano. Chumvi inatumiwa hasa katika kueleza aina inayofaa ya usemi.

6. Andiko la Wakolosai 4:6 linahusuje huduma ya Mashahidi wa Yehova?

6 Mtume Paulo aliandika hivi: “Maneno yenu yawe na neema sikuzote, yakikolea munyu [chumvi], mpate kujua jinsi iwapasavyo kumjibu kila mtu.” Tafsiri nyingine inasema: “Mazungumzo yenu yanapaswa kuwa daima mema na ya kuvutia, na mnapaswa kujua jinsi ya kumjibu vizuri kila mmoja.” (Wakolosai 4:6; Habari Njema kwa Watu Wote) Wakristo wa kweli wanatumia saa nyingi wakizungumza na watu juu ya Ufalme wa Mungu. Bila shaka, si Mashahidi wa Yehova wote ambao ni wafasaha wa kusema. Hata hivyo, wakithamini sana ujumbe na kusema kwa usadikishi na uchangamfu, wanaweza kugeuza mioyo ya watu wengi kwenye ukweli wa Neno la Mungu. Basi, ni jambo la maana sana usemi wa watumishi wa Yehova uwe wenye neema na wa kuvutia!

7. Maneno ya Mkristo ‘yaliyokolezwa chumvi’ yanaweza kuwa na matokeo gani mazuri?

7 Maneno ya Mkristo ‘yaliyokolezwa chumvi’ hayamsaidii msikiaji apate tu ladha nzuri ya ujumbe wa Biblia bali pia yanaelekea kuhifadhi uhai wa wale wanaousikiliza. Kwa hiyo, kama vile chumvi ilivyo ya lazima ili kuwa hai, ndivyo usemi wa watumishi wa Yehova unavyoweza kumaanisha uzima kwa wale wanaosikiliza kwa kuthamini yale ambayo wanasema juu ya kusudi la Mungu na Ufalme wake.​—Linganisha Yohana 6:63, 68.

8. Kwa sababu gani neema inapasa kuwa katika usemi wa wahudumu Wakristo?

8 Basi, neema yapasa kuwa sehemu ya usemi wa Wakristo wanaposema na watu wasioamini. Nyakati nyingine wasikiaji wa ujumbe wa Ufalme wanajibu kwa ukali au kwa ukaidi. Lakini watumishi wa Yehova hawapaswi kamwe kujibu kwa njia iyo hiyo. Badala yake, sikuzote wanapaswa kuwa wenye neema. Maana yake nini kuwa mwenye neema? Inamaanisha kuwa mfadhili, mwenye kupendeza, kufanya uungwana, na kuwa mwenye rehema. Njia ya Mkristo ya fadhili na subira katika kushughulika na maulizo, vipingamizi, malawama, au adabu mbaya mara nyingi inatokeza tofauti ya maana sana. Ni kama mithali moja inavyosema, “Jawabu la upole hugeuza hasira.” (Mithali 15:1) Neema, kufanya uungwana, na majibu ya busara katika huduma ya Kikristo ni mambo yanayoweza kufanya watu walio wagumu na wenye uchungu wawe wororo na wenye mioyo mizuri kweli kweli.​—Mithali 25:15.

9. Wakristo wanapaswa kupashanaje habari na waamini wenzao, na kwa sababu gani?

9 Basi, Wakristo wanapaswa kupashanaje habari na waamini wenzao? Bila neema? Hata! Kwa sababu gani? Kwa sababu watumishi hao wa Yehova walio wakfu ni sehemu ya “kundi la Mungu” pia, ambalo lapasa kutendewa kwa wororo.​—Linganisha 1 Petro 5:2-4; Matendo 20:29.

10. Andiko la Waefeso 4:29-32 linapasa kuhusuje lugha ambayo watumishi wa Yehova wanatumia?

10 Je! mtumishi wa Yehova anapaswa kutumia lugha mbaya anapozungumza na wafanyi kazi wenzake ambao huenda wakawa wamemuudhi? Je! ingefaa mnyapara Mkristo atumie usemi mchafu anapokasirishwa na wafanyi kazi? Waume na wake Wakristo wanapoudhika kidogo, je, wanapaswa kutukanana au kutukana watoto wao? Isiwe hivyo kamwe! Paulo aliandika: “Neno lo lote lililo ovu lisitoke vinywani mwenu . . . Uchungu wote na ghadhabu na hasira na kelele na matukano yaondoke kwenu, pamoja na kila namna ya ubaya; tena iweni wafadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma, mkasameheane kama na Mungu katika Kristo alivyowasamehe ninyi.”​—Waefeso 4:29-32.

“Mwe na Chumvi Ndani Yenu”

11, 12. Yesu alikuwa akisema juu ya “chumvi” ya aina gani katika Marko 9:50, na maneno hayo yangetaka kuwe na usemi na matendo ya aina gani?

11 Kwa kuwa sisi si wakamilifu, nyakati nyingine sote tunazungumza isivyompasa Mkristo. Ni kama mwanafunzi Yakobo alivyokubali waziwazi: “Maana twajikwaa sisi sote pia katika mambo mengi. Mtu asiyejikwaa katika kunena, huyo ni mtu mkamilifu, awezaye kuuzuia na mwili wake wote kama kwa lijamu.” (Yakobo 3:2, 8-10) Wanafunzi wa kwanza wa Yesu hawakuwa tofauti, na ilikuwa lazima wakaripiwe kwa kushindwa kusemezana kwa neema. Kwa mfano, katika pindi fulani wanafunzi walibishana vikali juu ya ni nani mkubwa zaidi kati yao. Yesu alikipa kikundi chote hicho mashauri mazuri dhidi ya kukwaza wengine na kwa kufanya hivyo ‘watiwe chumvi kwa moto,’ au kuharibiwa katika Gehena. Halafu alimalizia kwa maneno haya: “Mwe na chumvi ndani yenu, mkakae kwa amani ninyi kwa ninyi.”​—Marko 9:33-50.

12 Kwa wazi, kwa maneno hayo Yesu hakuwa akizungumza juu ya kiasi kidogo cha chumvi halisi kilichokuwa ndani ya miili ya wanafunzi wake. Badala yake, alikuwa akisema wawe wenye kufikiria wengine, wenye busara, timamu, na wenye kufanya amani kwa maneno na kwa mwenendo​—wawe wenye kutenda kwa njia yenye kuvutia wengine. Hilo ni jambo la maana sana ili Wakristo wa kweli wabaki wakiwa na amani wao kwa wao.

“Chumvi ya Dunia”

13. Yesu alimaanisha nini alipowaambia wafuasi wake hivi, “Ninyi ni chumvi ya dunia”?

13 Kuwahusu wafuasi wake, Yesu alisema pia: “Ninyi ni chumvi ya dunia.” (Mathayo 5:13) Kwa kusema hivyo, Yesu hakumaanisha kwamba kwa halisi wanafunzi wake walikuwa chumvi. Badala yake, chumvi ni kitu cha kuhifadhia, na ujumbe ambao wafuasi wa Yesu walikuwa wakiwapelekea watu ungehifadhi maisha za wengi. Kweli kweli, wanafunzi wake walikuwa na uvutano wa kuhifadhi wale waliosikiliza ujumbe wao, wakawazuia watu hao wasiharibike kiroho na kiadili. Hakukuwa shaka juu ya uhakika wa kwamba habari njema zilizotangazwa na wafuasi wa Yesu zingehifadhi maisha.​—Matendo 5:20; 13:46-48.

Chumvi Inahifadhi Kusiwe Kuharibika

14. Ili kujizuia kuharibiwa na ulimwengu, ni nini kinachohitajiwa?

14 Kwa maoni ya Yehova Mungu yaliyokwezwa na yaliyo safi, bila shaka mfumo wote huu mbovu wa mambo unaonekana kama ngozi za kondoo zilizotangulia kutajwa. Kabla ya kusafishwa na kupakwa chumvi, zilinuka na zilikuwa na wadudu wabaya. Kwa kadiri fulani, kila mtu anapatwa na matokeo ya hali za ulimwengu huu, na ili kuepuka kupatwa na uchafu unaoingia katika kila sehemu ya maisha, mtu anahitaji uhodari na ni lazima adumishe ukamilifu wake kwa Mungu. Ni kwa njia hiyo tu mtu anaweza kujihifadhi asiharibike kiadili. Anahitaji si neema ya usemi tu bali pia sifa ya kuhifadhi inayomwezesha akatae uchafu katika namna zake zote. Katika habari hii, kuna uhitaji wa haraka wa “chumvi.”​—1 Petro 4:1-3.

15. Ni mifano gani mizuri iliyowekwa na Yesu na Danieli?

15 Ni lazima mtumishi mwaminifu wa Yehova ajue jinsi ya kukataa mazoea mabaya na vishawishi. Kumbuka kwamba Yesu alikataa mara tatu aliposhawishwa na Shetani jangwani. (Mathayo 4:1-10) Na ufikirie mfano uliotolewa na nabii Danieli. Yeye alijifunza kukataa akiwa mchanga sana. Danieli alipokuwa mwanamume kijana katika ua wa kifalme wa Babuloni, yeye pamoja na wenzi wake walipewa “posho ya chakula cha mfalme.” Lakini Danieli na rafiki zake walikataa. Huko hakukuwa ni kukataa ukaribishaji. Badala yake, Waebrania hao vijana wanne walisisitiza kuwa wanataka chakula chenye mboga na maji tu kwa sababu walihangaikia kuepuka chakula kilichokatazwa na Sheria ya Yehova au kilichochafuliwa na sherehe za kipagani. Uhodari kweli kweli ulihitajiwa ili kuchukua mwendo huo. Matokeo yalikuwa yenye kuthawabisha, kwa maana mwishoni mwa kipindi kilichowekwa cha jaribu, sura yao ilikuwa nzuri zaidi ya wale waliokubali chakula cha kifalme. Na kwa njia ya kiroho Waebrania hao walifurahia haraka na kibali ya Yehova.​—Danieli 1:5-17.

16. Ni kwa sababu gani inaweza kusemwa kwamba Danieli alikuwa mtumishi wa Yehova ‘mwenye chumvi ya kutosha’?

16 Yehova Mungu alihakikisha kwamba Danieli na washiriki wenzake walihifadhiwa kwa sababu ‘wao wenyewe walikuwa na chumvi.’ Lakini tunaweza kujifunza zaidi kwa Danieli. Aliwekwa rasmi kwenye cheo cha juu katika serikali ya Kibabuloni. Akiwa katika hali hizo lazima awe alikataa mambo mara nyingi, kwa maana alikuwa amezungukwa na wapagani, na ua wa kifalme bila shaka ulikuwa umejawa na mwenendo usio wa adili, kusema uwongo, rushwa, hila za kisiasa, na mazoea mengine machafu. Danieli alikazwa sana nyakati nyingi. Lakini ingawa alikuwa katikati ya “ulimwengu” wa wakati huo, yeye hakuwa “sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 17:16, NW) Danieli alikuwa mtumishi mwaminifu wa Yehova, ‘mwenye chumvi ya kutosha.’ Maadui wa Danieli, labda kwa kuudhika kwa sababu ukamilifu na unyofu wa Danieli uliwaonyesha kuwa wabaya, hata walijaribu kumwangamiza! Hata hivyo, walilazimika kukubali kwamba yeye hakuwa na “kosa wala hatia ndani yake.” (Danieli 6:4, 5) Huo ni mfano mzuri kama nini!

17. Ni majaribu gani magumu yanayokabili vijana Wakristo leo?

17 Kama Danieli na rafiki zake, vijana Wakristo leo wanakabili majaribu magumu. Hasa shuleni, wanalazimika kukabiliana na dawa za kulevya, tumbaku, vileo, mazungumzo machafu, mwenendo usio wa adili, kudanganya, roho ya uasi, ibada ya uwongo, utukuzo wa taifa, mashirika mabaya, mafundisho ya uwongo kama vile mageuzi, na mavutano mengine yenye nguvu. Kijana Mkristo anahitajiwa awe ‘mwenye chumvi ya kutosha’ ili aweze kubaki akiwa mshika-ukamilifu aliye safi katika kukabili vishawishi vyote hivyo.

18. (a) Wazazi Wakristo wangefanya vema kufikiria maulizo gani? (b) Ni nini kinapendekezwa kwa wazazi wanaoona ugumu kusaidia watoto wao?

18 Kwa hiyo, wazazi Wakristo, fikirieni kwa uangalifu hali ya jamaa yenu. Je! washiriki wote wanafanya maendeleo ya kiroho? Je! mmezuia uchafu wa kilimwengu usiwachafue vijana wenu? Je! mnajua wanayofanya na wanayofikiri na kuhisi hasa juu ya ibada ya kweli? Je! wanachukia vitu vichafu vya ulimwengu huu au wamo katika hatari ya kuvutwa navyo? (Amosi 5:14, 15) Ikiwa, ninyi wazazi, hamna hali ya ukaribu na watoto wenu ili mwasaidie, au mkiona hilo ni jambo gumu, mbona msitoe sala ya bidii juu ya hilo kwa Yehova? Hakika anaweza kukusaidia ushinde kipingamizi hicho.​—1 Yohana 5:14.

19. Ni nini kati ya mambo ambayo wazazi Wakristo wanapaswa kukataa?

19 Ninyi mlio wazazi Wakristo, mnaweka mfano wa namna gani? Je! mnakataa kabisa mambo yenye madhara ya kula kupita kiasi na kunywa kupindukia, na pia namna nyingi za ukosefu wa adili na uchafu zinazozoewa katika sehemu zinazowazunguka? Je, mnakataa rushwa, mnakataa wivi mdogo-mdogo na mizaha ya maneno machafu na usemi wa watu wa kilimwengu? Kazini au katika mtaa wenu, je, ninyi mnajulikana kuwa watu safi, wanyofu, wasio na hila? Kukataa wakati unaofaa ni jambo la maana sana ili kuwa “chumvi ya dunia.”

Udumifu na Ushikamanifu

20. Chumvi ilitumiwaje kuhusiana na ibada ya Yehova katika Israeli wa kale?

20 Bila shaka kwa sababu chumvi ilifananisha hali ya kutoharibika, ilitumiwa katika ibada ya Yehova katika Israeli. Kwa mfano, sadaka zote kwenye madhabahu zilipasa kutiwa chumvi. Katika Torati iliyotolewa kupitia Musa, ilisemwa hivi: “Usiiache sadaka yako ya unga kupungukiwa na chumvi ya agano la Mungu wako; utatoa chumvi pamoja na matoleo yako yote.” Na ‘agano la chumvi’ lilionwa kuwa lenye kufungamanisha.​—Mambo ya Walawi 2:13; Hesabu 18:19; 2 Mambo ya Nyakati 13:4, 5.

21. Wakiwa ndio “chumvi ya dunia,” ni nini kinachotakwa kwa watumishi wa Yehova leo?

21 Watumishi wa Yehova, ambao ni mashahidi wake, ndio “chumvi ya dunia.” Jambo hilo linataka wawe wasioharibika, waaminifu, na washikamanifu. Ni lazima wawe na bidii katika kusitawisha matunda ya roho takatifu ya Mungu​—upendo, furaha, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, na kujiweza. (Wagalatia 5:22, 23, NW) Matunda ya roho ndicho chanzo cha sifa za kiroho, zenye mfano wa chumvi. Lakini uhakika tu wa kwamba wengine wamemtumikia Yehova kwa miaka mingi hautoi uhakikisho kwamba hawataanguka. (1 Wakorintho 10:12) Yesu mwenyewe alituonya juu ya hilo.

22. Ni nini umaana wa sehemu ya mwisho ya Mathayo 5:13?

22 Kumbuka kwamba baada tu ya Yesu kusema, “Ninyi ni chumvi ya dunia,” aliongeza hivi: “Lakini chumvi ikiwa imeharibika itatiwa nini hata ikolee? Haifai tena kabisa, ila kutupwa nje na kukanyagwa na watu.” (Mathayo 5:13) Nyingine ya chumvi iliyotumiwa wakati Yesu alipokuwa duniani ilikuwa imechanganywa na vitu vingine. Kwa hiyo kama chumvi yenyewe ingeondolewa na mvua au kwa njia nyingine yo yote, sehemu iliyobaki ilifaa kutupwa nje tu, labda itupwe juu ya vijia na kukanyagwa-kanyagwa na wenye kupita. Kama chumvi haingetunzwa katika hali inayofaa, ingeweza kwa urahisi kuwa bure tu.

23. Sisi Mashahidi wa Yehova tunapaswa kuyaonaje maneno ya Yesu, “Ninyi ni chumvi ya dunia”?

23 Basi, sisi watumishi washikamanifu wa Yehova na Mwanaye Yesu Kristo na tuwe waangalifu ‘tusiharibike’ kamwe, au tusipoteze sifa za mfano wa chumvi yenyewe. Badala yake, na tutie kila jitihada ili kusitawisha matunda ya roho ya Mungu. Sikuzote na tuwe wenye neema katika usemi, tukitangaza ujumbe wa Ufalme kwa bidii na kwa njia hiyo kusaidia kuhifadhi maisha za wengine. Na tusiharibiwe kamwe na ulimwengu huu mchafu, bali sikuzote na tukumbuke maana kubwa na pendeleo kubwa linalohusiana na maneno ya Yesu: “Ninyi ni chumvi ya dunia.”

[Picha katika ukurasa wa 29]

Akiwa kijana, Danieli alijifunza kukataa

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki