Shamba Lenye Kuzaa Ngano na Magugu
“Tueleze mfano wa yale magugu katika lile shamba.”—Mt. 13:36, NW.
1, 2. (a) Kwa habari ya kupanda, kuna kanuni gani za hakika? (b) Ni mfano gani unaotegemea kanuni hizo mbili?
“KUPANDA na kuvuna” ni sehemu ya majira ambayo Yehova Mungu alisema moyoni mwake kwamba hayatakoma “siku zote za dunia.” (Mwa. 8:21, 22, ZSB) Kanuni ya msingi yenye kuhusiana na hiyo ilielezwa na mtume Paulo, alipoandika hivi: “Yo yote mutu anayopanda, ndiyo atakayovuna.”—Mwa. 6:7, ZSB.
2 Mkulima aliyekuwa amefanya kazi kwa bidii akipanda mbegu njema ya ngano wakati wa kupanda mbegu alikuwa na uhakika kwamba kwa wakati wake kungekuwako mavuno, kwa sababu ya mambo hayo ya hakika. Ni kawaida yake kwamba kuvuna kunafuata kupanda. Vivyo hivyo, wakati wafanya kazi wake wa shambani walipomwambia wakati fulani baadaye kwamba shamba lake lilikuwa linazaa si ngano tu bali pia namna fulani ya magugu, yeye alikuwa na uhakika kwamba tendo fulani la hila lilikuwa limefanywa. Yeye alikuwa anajua alichopanda: ngano, wala si magugu. Tukio hilo jipya lilihitaji kufanyiwa uamuzi. Wafanya kazi wake walipendekeza tendo la mara moja lichukuliwe. Walitaka kuyang’oa magugu hayo mara iyo hiyo, walakini mkulima huyo mwenye hekima alituliza tamaa yao nyingi. Akawaambia wangojee, kwa kuogopa kuumiza ngano wakati wa kuyang’oa magugu. Acheni zote zikue pamoja. Majira ya kuvuna yangekuwa wakati unaofaa wa kutenganisha ngano ya halisi na ya uongo.
3. Yesu alitoa mfano wa matukio gani ya maana yanayohusiana na Ufalme nayo kazi ya kutenganisha ingekuwa sehemu ya nini?
3 Mfano huo ulitumiwa na Yesu Kristo kuonyesha matukio fulani ambayo yangetokea katika kazi aliyokuwa ameanzisha duniani. Kazi hiyo ya kupanda ilikuwa imekusudiwa itokeze zao linalotakiwa la Wakristo wa kweli ambao wangeshirikishwa pamoja naye katika serikali ya kimbinguni inayojulikana kama “ufalme wa mbingu.” Kwa njia hiyo alitabiri kwamba upandaji wake mzuri ungeingiliwa na adui Shetani Ibilisi. Shamba hilo lingezaa mavuno yanayotakiwa ya mfano wa ngano, Wakristo wa kweli na pia zao la Wakristo wa bandia (udanganyifu) wenye mfano wa magugu. Wote wangeruhusiwa wakue pamoja mpaka wakati wa mavuno, wakati kazi ya kutenganisha ingefanywa. Pamoja na hayo, kazi hiyo ya kutenganisha ingekuwa ni sehemu zaidi ya “siku za mwisho,” “umalizio wa mfumo wa mambo.”—Mt. 13:24-30, 36-43, NW; linganisha Mathayo 24:3, NW; 2 Timotheo 3:1.
4. Sababu gani mfano huo utupendeze?
4 Je! ungependezwa kuona mfumo (system) huu mbovu ukifikia mwisho wake? Je! wewe binafsi utapatwa na matokeo ya kazi hii ya kuvuna? Na, wakati uo huo yaweza ikawa kwamba mfano wa Yesu unatoa ufahamu juu ya historia ya Ukristo wakati wa karne zote zilizopita? Acheni tuone.
MFANO WA NGANO NA MAGUGU
5, 6. (a) Kwa sababu gani usemi “ufalme wa mbingu” katika mfano huu hauwezi kuwa unahusu serikali ya kimbinguni ya Kristo? (b) Basi, mifano ya ufalme inahusu nini na inafananisha nini?
5 Kwenye fuo (kando) za Bahari ya Galilaya, karibu na nyumba alimokuwa akikaa, Yesu alieleza mfano huu kwa wanafunzi wake na umati mkubwa wa watu watafiti (wenye kutaka kujua), kwa kusema hivi: “Ufalme wa mbingu umekuwa kama mtu aliyepanda mbegu njema katika shamba lake. Watu walipokuwa wamelala usingizi, adui yake alikuja naye akarudia kupanda magugu katikati ya ile ngano, akaondoka. Jani lilipoota likazaa matunda nayo magugu yakatokea pia.”—Mt. 13:24-26, NW.
6 Tukiangalia haraka-haraka ile mifano mingine ya ufalme katika Mathayo sura ya 13 tunasaidiwa kujua kwamba usemi “ufalme wa mbingu” kama unavyotumiwa katika mifano hii hauwezi kuwa unahusu serikali au ufalme wa Kimasihi uliokamilishwa mbinguni. Je! mtu ye yote aweza kuwazia “magugu,” “uovu” wenye mfano wa chachu (mstari Mt 13:33; 1 Kor. 5:8) au watu wanaofananishwa na ‘samaki’ waovu, wasiofaa (mistari Mt 13:47-50) wakishirikishwa pamoja na Kristo katika ufalme wake wa kimbinguni? Sivyo kabisa! Kwa hiyo, lazima mifano hiyo iwe inahusu matukio mema na mabaya kuhusiana na kuchagua washiriki wa Kristo wa wakati ujao katika “ufalme wa mbingu.” Sana-sana, mfano wa ngano na magugu unaonyesha hali kati ya wale walioko duniani wanaodai kuwa wameitwa watawale pamoja na Kristo katika ufalme wake. Hali hiyo ingeruhusiwa kwa wakati fulani kabla ya kumalizwa kwenye “mavuno” ya mfano.
7, 8. (a) “Mwana wa mtu” ni nani? (b) Ni unabii gani mwingine unaotaja “mwana wa mtu” na wale wanaofananishwa na “mbegu njema”?
7 Baadaye Yesu mwenyewe alieleza maana ya mfano wa “mwenye nyumba,” au “mtu aliyepanda,” “katika shamba lake,’ “mbegu njema,” “adui yake” na “magugu.” Masimulizi hayo yanasema hivi: “Kisha baada ya kuruhusu umati wa watu uondoke alienda akaingia katika nyumba hiyo. Wanafunzi wake wakamjia na kusema: ‘Tueleze mfano wa yale magugu katika lile shamba.’ Katika kujibu akasema: ‘Mpanzi wa ile mbegu njema ni Mwana wa mtu; shamba hilo ni ulimwengu; kwa habari ya mbegu njema, hawa ndio wale wana wa ufalme; bali magugu ni wale wana wa yule mwovu, na adui aliyewapanda ni Ibilisi.’”—Mt. 13:36-39, NW.
8 Yesu alijitambulisha kuwa ndiye “Mwana wa mtu.” (Mt. 8:20, NW; Mt 25:31; 26:64) Kwa kupendeza, ilikuwa kuhusiana na Ufalme kwamba Yesu akaitwa kwa njia ya unabii “Mwana wa mtu” katika njozi aliyoipokea Danieli. Unabii huo unasema hivi: “[“Mwana wa mtu”] akapewa mamlaka, na utukufu, na ufalme, ili watu wote, mataifa yote, na lugha zote wamutumikie; mamlaka yake ni mamlaka ya milele, isiyopita kamwe, na ufalme wake ufalme usioweza kuangamizwa.” Ikionyesha kwamba Mwana wa mtu angekuwa na washiriki wenye kutawala pamoja naye, njozi hiyo ya kiunabii ilisema hivi pia: “Na ufalme na mamlaka, na ukubwa wa ufalme chini ya mbingu zote watapewa watu wa watakatifu wake Aliye juu: ufalme wake ni ufalme wa milele, na wote wenye mamlaka watamutumikia na kumutii.”—Dan. 7:13, 14, 27, ZSB.
KUPANDA “MBEGU NJEMA”
9. “Shamba” ni nini, na kwa sababu gani Yesu amepanda “mbegu njema” ndani yalo?
9 Yesu, “mwenye nyumba” wa mfano huo, anapanda “mbegu njema katika shamba lake,” akiwa na kusudi la kukusanya kutoka ulimwenguni hesabu inayotakiwa ya “watakatifu” hao, au wale “wana wa ufalme.” Tunaelezwa kwamba “shamba” hilo ni “ulimwengu [Kigiriki, koʹsmos],” ulimwengu wa wanadamu. Tangu wakati wa huduma ya kidunia ya Yesu kuendelea, wanadamu walipata kuwa “shamba linalolimwa,” shamba la kidini lenye kutoa nafasi ya kupanda na kulima ile “mbegu njema,” au wale “wana wa ufalme.” (1 Kor. 3:9, NW) Kwa juhudi Yesu alitayarisha sehemu ya “shamba” la Kiyahudi wakati wa ile miaka mitatu na nusu ya huduma yake ya kidunia. (Mt. 9:35-38) Halafu, kuanza Pentekoste ya mwaka 33 W.K. kuendelea, yeye alipanda “mbegu njema,” kwanza kati ya Wayahudi, na mwishowe katika ulimwengu mzima, au “shamba.”—Matendo 1:8, NW.
10. Kazi ya kupanda ilifanya maendeleo gani kati ya Wayahudi na waongofu?
10 Akieleza juu ya “mbegu njema,” Yesu alisema hivi: “Hawa ndio wale wana wa ufalme.” Wa kwanza wa “wale wana wa ufalme” waliozaliwa na kutiwa mafuta kwa roho walikuwa ni mitume waaminifu wa Yesu na wale wanafunzi wengine mia moja hivi, wanaume kwa wanawake, waliopokea zawadi ya roho takatifu katika Pentekoste mwaka 33 W.K. katika Yerusalemu. (Matendo 1:13-15; 2:1-4) Siku iyo hiyo, karibu wengine 3,000, Wayahudi kwa waongofu, waliongezwa kwenye kundi la Kikristo lililokuwa limeanzishwa karibuni. (Matendo 2:5-11, 41) Yehova aliibariki kazi hiyo ya kupanda kwa kuendelea kuwaongezea “wale waliokuwa wakiokolewa,” hata kwamba karibuni “hesabu ya watu waume [inaelekea wanawake hawakuhesabiwa] ikawa kama elfu tano.” Muda mfupi baadaye, masimulizi hayo yanaendelea kusema hivi: “Walioamini wakazidi kuongezeka kwa Bwana, wengi, wanaume na wanawake.” (Matendo 2:47; 4:4; 5:14) Kazi hiyo ya kupanda ilikuwa ikisonga mbele kwa haraka kati ya Wayahudi na waongofu.
11. Kupanda kulifanya maendeleo gani kati ya Wasamaria na watu wasio Wayahudi?
11 Baada ya kufanya mpango kwamba mbegu zipandwe kati ya Wasamaria (Matendo sura 8), Mpanzi Yesu, kupitia roho takatifu, aliipanua kazi hiyo ya kupanda ikawafikia watu wasiotahiriwa ambao si Wayahudi au Mataifa. (Matendo, sura 10; Mdo 13:1-5, 46, 47) Kwa miongo michache ya miaka (makumi machache ya miaka) makundi ya Kikristo yalianzishwa kutoka Afrika ya Kaskazini mpaka kwenye Bahari Nyeusi na kutoka Babilonia mpaka Italia, kama si kufika mbali zaidi kuelekea magharibi. (Matendo 2:5-11; 1 Pet. 5:14; Rum. 15:24; Kol. 1:5, 6, 23) Kwa sababu ya kupanda kwa juhudi, ‘jani liliota na kuzaa matunda.’—Mt. 13:26, NW.
KUPANDWA KWA MAGUGU BAADAYE
12, 13. “Adui” yule ni nani, naye alipandaje “magugu” “watu walipokuwa wamelala usingizi”?
12 Walakini kulikuwako dhara (umizo) lililokuwa likikusudiwa kufanywa. Mfano wa Yesu ulikuwa umekwisha kuonya juu ya jambo hilo: “Wakati watu walipokuwa wamelala usingizi, adui yake alikuja naye akarudia kupanda magugu katikati ya ile ngano, akaondoka. Jani lilipoota likazaa matunda, nayo magugu yakatokea pia.” (Mt. 13:25, 26, NW) Yesu alionyesha kwamba “adui yake” alikuwa ni “Ibilisi,” ambaye ndiye angefanya kazi yake ya kuharibu “wakati watu walipokuwa wamelala usingizi.” Katika Biblia “kulala” kwaweza kufananishwa na kifo au kusinzia kiroho. (Mt. 9:24; Rum. 13:11; 1 The. 5:6) Baada ya kuzungumza juu ya ‘kumaliza mwendo wake,’ Paulo aliwaambia wazee waliotoka kundi la Kikristo la Efeso hivi: “Najua mimi ya kuwa baada ya kuondoka kwangu mbwa-mwitu wakali wataingia kwenu, wasilihurumie kundi; tena katika ninyi wenyewe watainuka watu, wakisema mapotovu, wawavute hao wanafunzi wawaandamie wao. Kwa hiyo kesheni.”—Matendo 20:24-31.
13 Mambo ya hakika ya kweli yanaonyesha kwamba “watu walipokuwa wamelala usingizi” ndipo Shetani alipokuja “akarudia kupanda magugu katikati ya ile ngano.” Mara tu mitume, ambao wakiwa jamii walikuwa ‘kizuizi’ cha uasi-imani, walipoanza kulala usingizi katika kifo, ndipo wazee wengi Wakristo walipoacha ‘kukesha.’ (2 The. 2:3, 6-8) Kwa kusinzia kiroho, hawakulinda “wana wa ufalme” na “mbwa-mwitu wakali” walioanza kuingia katikati yao. Wao walikuwa ni yale “magugu” yaliyopandwa katikati ya ile “mbegu njema.” Akizungumza juu ya mwisho wenye kukaribia wa kipindi cha mitume, Yohana, mtume wa mwisho kufa, aliandika hivi: “Watoto, ni wakati wa mwisho; na kama vile mlivyosikia kwamba mpinga Kristo yuaja, hata sasa wapinga Kristo wengi wamekwisha kuwapo. Kwa sababu hiyo twajua ya kuwa ni wakati wa mwisho. Walitoka kwetu, lakini hawakuwa wa kwetu. Maana kama wangalikuwa wa kwetu, wangalikaa pamoja nasi. Lakini walitoka ili wafunuliwe kwamba si wote walio wa kwetu.”—1 Yohana 2:18, 19.
14. Tunapewa habari gani juu ya aina ya magugu yanayotajwa katika mfano wa Yesu?
14 Yesu alisema hivi: “Magugu ni wale wana wa yule mwovu.” (Mt. 13:38, NW) Katika kitabu chake Natural History of the Bible, H. B. Tristram anatoa maelezo juu ya namna ya magugu yanayotajwa katika mfano huu. Anaandika hivi: “Magugu (zizania) ni yale yale sawa na zawân, ya Kiarabu, ambayo ni kutoka hayo jina la Kigiriki linatoka, Lolium temulentum, Magugu Yenye Ndevu. . . . Ni namna fulani ya nyasi [za nafaka ya] rye, na kati ya aina za jamii ya nyasi hiyo peke yake ndiyo yenye mbegu zenye sumu Neno zawân, latokana na zân, ‘kutapika,’ matokeo ya kula magugu hayo yanakuwa ni kuchafuka moyo sana, kifafa, na kuhara, hatimaye kuleta kifo mara nyingi Mmea huo, ukiwa ni wenye jani pana zaidi ya nyasi nyingi za mwitu, unafanana kabisa na ngano mpaka suke linapotokea,’
15. (a) Je! “magugu” hayo ni “ngano” iliyoharibika (b) Kwa hiyo, “Mwana wa mtu” hana lawama ya nini?
15 Lazima iangaliwe kwamba “magugu” hayo si namna iliyoharibika ya ngano,; kama ambavyo wanachuo Wayahudi wa kitabu Talmud (kitabu cha sheria na pokeo ya Kiyahudi)a na wengine walivyoamini wakati mmoja. Mbegu za ngano hazijigeuzi kamwe zikawa magugu. Kufanya hivyo kungepingana na sheria ya Yehova isiyoweza kubadilishwa: “Dunia na ichipuze nyasi, mbegu zenye kuzaa majani, miti ya matunda yenye kuzaa matunda kulingana na jinsi zake.” (Mwa 1:11, 12, NW) Jambo hilo hakika la kisayansi linamwondolea lawama yo yote “Mwana wa mtu,” Kristo Yesu, ‘mpanzi wa mbegu njema,’ ya yale yaliyotokea “katika shamba lake.” “Mbegu njema” aliyoipanda haingeweza kamwe kuwa zao la magugu. Ingeweza kuzaa “ngano” peke yake, au “wana wa ufalme” wa kweli. Kilichositawi baadaye katika “shamba lake” yalikuwa ni matokeo ya moja kwa moja yaliyofanywa makusudi na yenye nia kudhuru (kuumiza) ya kupandwa kwa “magugu” baadaye, au wale “wana wa yule mwovu.”
16. Kwa sababu gani mfano huo wa “ngano” na “magugu” unapendeza kuhusiana na historia?
16 Kwa hiyo, mfano wa Yesu wa “ngano” na “magugu” unaeleza sana historia ya Ukristo wakati wa karne zote zilizopita. Mambo ya hakika ya kihistoria yanaonyesha kwamba baada ya kifo cha mitume Shetani alianzisha kati ya makundi ya Wakristo wa kweli “magugu,” “mbwa-mwitu wakali” na “wapinga Kristo,” kama vile Yesu, Paulo, Petro, Yohana na Yuda walivyokuwa wametabiri. (Matendo 20:29; 2 Pet. 2:1-3; 1 Yohana 2:18; Yuda 4) Imekuwa kama vile Yesu alivyosema: “Jani lilipoota likazaa matunda nayo magugu yakatokea pia.”—Mt. 13:26, NW.
17. “Magugu” hayo yalianza kuonekana waziwazi hasa wakati gani?
17 “Magugu” hayo yalipata kuonekana waziwazi hasa wakati wa karne ya pili na ya tatu, wakati ambapo mafundisho yasiyo ya kimaandiko kama vile kutokufa kwa nafsi, moto wa mateso na Utatu wa miungu yalipoanza kufundishwa na wale wenye kuitwa mababa wa kanisa. Wengi wa wanaume hao walikuwa wanafalsafa (wanafilosofia) zaidi ya kuwa waangalizi Wakristo wa kweli wenye kuwa waaminifu kwa mafundisho ya Biblia. Upeo ulifika mapema katika karne ya nne, wakati Mtawala Konstantino mpagani alipounganisha Ukristo huo ulioasi imani na dini ya kipagani ya Roma. Ukristo huo wa kubandia (kudanganya), ukiwa ndio Katoliki ya Roma, Orthodoksi ya Urusi, Orthodoksi ya Ugiriki na namna mbalimbali za Uprotestanti, umetokeza zao kubwa la “magugu” si katika karne zote zilizopita tu bali pia kufikia wakati huu wa sasa.
“ACHENI ZOTE ZIKUE PAMOJA”
18. Kulingana na mfano wa Yesu, kuna matukio gani mengine zaidi?
18 Hali hiyo isingeweza kukosa kuwahangaisha “watumwa” wa “Mwana wa mtu.” Mfano wa Yesu unaendelea kusema hivi: “Watumwa wa mwenye nyumba wakamjia wakamwambia, ‘Bwana, je! wewe hukupanda mbegu njema katika shamba lako? Basi, inakuwaje lina magugu?’ Yeye akawaambia, ‘Adui, mtu mmoja, alifanya hivyo.’ Wakamwambia, ‘Basi, unataka, twende tukayakusanye?’ Yeye akasema, ‘Hapana; ili kwa vyo vyote, mtakapokuwa mkikusanya magugu, msije mkang’oa ngano pamoja nayo. Acheni zote zikue pamoja mpaka mavuno; na katika kipindi cha mavuno nitawaambia wavunaji, Kwanza kusanyeni magugu myafunge katika matita ili myateketeze kwa moto, kisha mkusanye ngano katika ghala yangu.’ Mt. 13:27-30, NW.
19. Kwa sababu gani “watumwa wa mwenye nyumba” walikuwa na wasiwasi?
19 Kama “watumwa” (mstari 27) hao wenye kuhangaika ndio wale wale “wavunaji” (mstari 30) Yesu haelezi. Ikiwa ndivyo, hiyo ingemaanisha kwamba malaika walikuwa na wasiwasi kwa ajili ya ukuzi mwingi wa “magugu” katika shamba la Bwana yao. (Mt. 13:39, NW) “Watumwa” hao waliuliza kama wanaweza kung’oa mara moja magugu hayo yenye ndevu, yakifananisha “wale wana wa yule mwovu.” (Mt. 13:38, NW) Walikuwa wanaogopa kwamba Wakristo hao wa kubandia, au “magugu,” ambayo yalipandwa na “adui,” Ibilisi, kwa kusudi la kuumiza, yangesonga “ngano” ya kweli, “wale wana wa ufalme” wa kweli.
20. “Mwenye nyumba” aliwajibuje “watumwa” wake, nalo jambo hilo limeonekanaje katika historia?
20 Walakini “mwenye nyumba,” “Mwana wa mtu,” hakuwapa ruhusa “watumwa” wake waende wakakusanye “magugu” hayo, au Wakristo wa uongo, wakawatenganishe na “ngano” ambayo ndiyo Wakristo wa kweli. Yeye alisema hivi: “Acheni zote zikue pamoja mpaka mavuno.” Na kwa hiyo imekuwa kwamba Ukristo wa kweli na wa uongo umekua pamoja katika “shamba,” au “ulimwengu,” wa wanadamu. Hata hivyo, ilikuwa lazima “wakati wa mavuno” ufike. Ungefika lini? Nalo jambo hilo linakuhusuje wewe?
[Maelezo ya Chini]
a “Talmud ya Yerusalemu inataja maoni ya kwamba magugu yanaitwa zunim kwa sababu yanafanya ngano mezannot (‘[i]fanye uzinzi’), yaani, inabadili tabia zake na kugeuka kuwa magugu.”—Kitabu Encyclopædia Judaica, Volume 15, safu 810.
[Picha katika ukurasa wa 9]
Magugu yenye ndevu
Ngano ya kweli