Je! Kristo Amerudi?
‘“YESU KRISTO’ ARUDI—KATIKA KITWE.” Ndivyo habari kuu ya ukurasa wa mbele wa gazeti Times of Zambia ilivyosema, la Machi 24, 1980. Makala hiyo iliendelea kusema hivi: “Mwanamume anayejitangaza kuwa ndiye Yesu Kristo atengeneza chama cha kidini. . . . Yeye amechagua wanaume 12 wawe wanafunzi wake . . . ‘Mimi ndiye Yesu Kristo wa kweli na watu wengi wamenikubali,’ ndivyo alivyosema.”
Ni wazi kutokana na ripoti za habari kwamba hicho sicho kisa pekee kilichotokea. Katika nchi nyingine madhehebu nzima,“Moonies,” imesitawi huko Sun Myung Moon, na inasimuliwa katika magazeti kwa majina kama “Bwana wa Kurudi kwa Pili,” “Adamu wa Tatu, Masihi Mpya.”
Kumngojea Kristo arudi si tukio kubwa la kisasa. Katika historia yote wanadamu wengi wamejisingizia kuwa Kristo aliyerudi. Mamilioni wengine wamengojea kuja kwa pili kwa Yesu. Kitabu Encyclopædia Britannica kikizungumza juu ya wale, “waaminifu wa kanisa [la Kikristo] la kwanza, kinatoa maelezo haya: “Wao waliamini kwamba ahadi za Agano la Kale juu ya mletaji wokovu aliyekuwa akija zilitimizwa katika Yesu Kristo, lakini utimizo huo haukuwa umekamilika kabisa. Kwa hiyo, wao walingojea Kuja kwa Pili kwa Kristo, ambako waliamini kulikuwa kumekaribia.”
Hata hivyo, wengi leo wanashuku zile ahadi za Biblia zinazozungumza juu ya kurudi kwa Kristo. Jambo hilo linaonyeshwa na maelezo ya mhariri wa kidini wa gazeti la kila siku la Amerika aliyeandika hivi: “Imesemekana kwamba ‘tunaweza kutaja mara mia tofauti-tofauti katika historia ambazo, kulingana na orodha ya mambo ya vita, matetemeko ya ardhi, njaa, Yesu angalipaswa kuwa amekwisha kurudi.’”
Hali hiyo yenye mvurugo inayohusu kurudi kwa Kristo inatulazimisha tukabili maulizo ya wazi, kama: Je’ kweli kweli Kristo anapaswa kurudi akiwa na mwili? Je! tutaweza kumwona? Kwa sababu kuna mabandia (wenye kujisingizia) wengi tutawezaje kumtambua? Makala inayofuata itajibu baadhi ya maulizo hayo.