“Lichukieni Lililo Ovu”
Watu wa Mungu wanaishi katika siku mbovu, zinazolinganika na siku za Noa, wakati ‘[Yehova] aliona ya kuwa maovu ya mwanadamu ni makubwa duniani na kwa-mba kila kusudi analowaza moyoni mwake ni baya tu sikuzote’ (Mwanzo 6:5; Mathayo 24:37-39) Hizi ndizo siku zilizotajwa kwa njia ya unabii kwenye Ufunuo 12:12, unaosema: “Ole wa nchi . . . kwa maana yule Ibilisi ameshuka kwenu mwenye ghadhabu nyingi, akijua ya kuwa ana wakati mchache tu.” Ibilisi angependa kupangua kila jambo ambalo yule Mtengenezaji Mkuu, Yehova Mungu, ameipangia dunia hii. Hiyo ni kutia ndani mpango wa ndoa. Kwa sababu Shetani analeta mashambulizi makali sana juu ya maadili (tabia njema) na jamaa, nyakati nyingine inakuwa lazima kutaja mambo kwa kuyatoboa wazi kabisa yaeleweke vizuri katika ‘kuishindania imani.’—Yuda 3.
Ulimwengu wa Shetani umeshusha sana tabia ukaingia katika upotovu wa kuchukiza sana. Huu ndio ulimwengu mchafu sana wenye kuruhusu matendo maovu ambao wengi wa watu wa Yehova wanalazimika kuishi nao kila siku, sawasawa na vile Lutu mwenye kumwogopa Mungu alivyolazimika kushindana na ‘mwenendo wa ufisadi wa wahalifu’ waliokuwa katika mji wa kale wa Sodoma. (2 Petro 2:7) Katika hizi nyakati za hatari, gazeti Mnara wa Mlinzi linajiona likiwa na daraka la kukaza fikira za watu kwenye viwango ambavyo Wakristo wa kweli wanapaswa kuvitetea katika jamii ya watu wenye kutenda maovu mengi. Linapofanya hivyo, inakuwa lazima lionyeshe watu mengine ya mazoea ya ufisadi ambayo yamekuwa kawaida ya watu wengi katika ulimwengu huu wa kisasa. (Zaburi 92:7) Inaonekana kuwa inafaa kabisa mambo hayo yatobolewe wazi kabisa bila kuyaficha, na inaonekana inafaa wazazi pia wayazungumze na watoto wao kwa kutumia busara. (Katika ulimwengu huu mbovu, ni afadhali zaidi wazazi ndio watoe mwongozo wa kukomaa na wenye upendo juu ya mambo ya ngono, badala ya kuacha watoto wao wajiokotee habari hizo. Na ni wazi kwamba baadaye watoto watajiokotea habari hizo kwa vijana wenye maelekeo ya kuzungumza ngono shuleni, hata kama wazazi wao hawatayazungumza nao.)
Kwenye Waefeso 5:3 tunaambiwa hivi: “Lakini uasherati usitajwe kwenu kamwe, wala uchafu wo wote wala kutamani, kama iwastahilivyo watakatifu.” Sisi hatuyataji mambo hayo kwa njia chafu wala ya mchezo-mchezo inayotumiwa na walimwengu wa Shetani. Lakini wakati afya njema ya kiroho ya watu wa Mungu inapotiwa hatarini na ulimwengu wa watu wasiomcha Mungu wanaowazunguka, sisi tunajisikia tukiwa na lazima ya kutumia “uhuru mkubwa wa kusema” tunapozizungumza hatari zinazotuzunguka. (2 Wakorintho 3:12; 7:4; Waefeso 3:12, NW) Hivyo ndivyo makala inayofuata itakavyofanya.—Warumi 12:9.